SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Nipo ndugu yangu, aniteke nani na mie mikono mivululu kama donnie yen[emoji23] [emoji23]

Pilika pilika tu, najikuta sipati muda wa kutksha kutokea mtaa wetu uleee a.k.a mtaa pendwa, almaarufu mtaa wa 7.
[emoji23][emoji23][emoji23][emoji23][emoji23] ukuje bana mtaa wa 7 kwetu ata kupita tumekumiss mnoooo
 
Wao shunny hongera. Baada ya kuwa msomaji Wa kila hadithi.leo umeamua kutuletea.naisubiria.ila mambo ya arosto unayajua.fanya bampa to bampa.thanks in advance. Kabla ya vitu kuanza
Ahahahha nayajua mamy arosto hakuna hapa kabisa
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 001

*Simulizi za series*


Jua lilinyanyuka na kuangaza ardhi ya Goshen: mojawapo ya tawala kubwa iliyopata kutokea mashariki ya mbali katika karne ya kumi baada ya kuzaliwa kwa kristo.

Ndege wake wakubwa wenye rangi za kuvutia waliamka wakaruka huku na kule wakitandaza sauti zao nyembamba. Sauti hizo marigoli zikawasili masikioni mwa malkia Sandarus na kumwamsha. Alikuwa amevalia nguo nyepesi za kulalia zilizokuwa zinaangaza kuonyesha mwili wake mchanga wa miaka ishirini na tano.

Kichwa chake chenye hekima kilikuwa kimefunikwa na nywele nyingi rangi ya kahawia. Miguu yake mirefu ila yenye nyama ilisimika ardhini na kusimamisha mwili wake mrefu mwembamba. Alah! Alikuwa mzuri haswa. Macho yake yalikuwa makubwa yaliyolegea. Mdomo wake ulikuwa mdogo ila hakika ukichanua kwa tabasamu ungekufanya uache shughuli yako na kumtazama.

Nyonga zake zilijiachanua na kukikimbia kiuno. Vidole vyake vilikuwa vyembamba virefu vyenye kucha bawabu. Tumbo lake flati na mapaja mekundu. Amini nakuambia siwezi kumaliza kuongelea uzuri wake kwani nikifanya hivyo tutajaza kitabu hiki.

Alipiga mihayo akanyoosha viungo vyake. Aliendea dirisha akafungua na kuangaza kutazama nje ya jengo lake kubwa la kifalme. Huko akaona makazi ya wananchi na wananachi wake wakiamka, wakikatiza na hata wakishughulika.

Alitabasamu akarejea kitandani kabla tu ya punde kijakazi wake kuingia akiwa kavalia gauni refu la kaki na kiremba kizito. Aliinama kumsalimu malkia kisha akamtazama na tabasamu.

“Malkia wangu, nimewasili. Nini wataka?”

“Hakuna ninachohitaji Zura.” Alisema Malkia Sandarus kwa sauti yake nyembamba ila yenye amri ndani yake.

Zura, kijakazi wa malkia, alikuwa ni mwanamama mzee wa miaka arobaini na tano. Si tu kwamba alikuwa ni kijakazi, bali pia alikuwa kama mama kwa Malkia huyo aliyempoteza mama yake punde tu alipozaliwa. Na kwa mujibu wa taratibu za kipindi hiko, Sandarus alipata mwanaume akiwa mdogo kabisa wa umri wa miaka mitano.

Alichukuliwa na mfalme wa Goshen, kwa jina Loop, kwa mujibu wa kumlelea ili aje kumuoa. Na kwa wakati wote huo, Sandarus akamjua Zura kama mama. Ni pale tu alipokuwa ndipo akapata kuujua kweli hizi chungu: hana mama, hampendi mwanaume aliyeozwa naye, baba yake hayupo tena hai, hana kaka wala dada, lakini pia pale alipo si nyumbani, nyumbani kwao ni kusini ya mbali kwenye utawala wa Maam.

Baba yake alikuwa mtu mkubwa kwenye hiyo tawala na kama mojawapo ya njia ya kuunganisha tawala hizi mbili: Goshen na Maam, babaye akamtoa akaolewe huko.

Tokea akiwa mtoto, Zura alimlea kama mwanaye. Lakini zaidi ya hapo alifanikiwa kumuandalia mazingira mazuri malkia huyo kuwa karibu sana na wananchi wake. Akiwa mtoto, alienda kuchota maji na hata kucheza na wanachi wa kawaida.

Hakuwa na majivuno wala malezi ya kunanga, matokeo yake watu wengi ndani ya tawala hiyo wakampenda na kufurahishwa naye.

“Ungependelea chakula gani mama?” Zura alimuuliza malkia akiwa ameinamisha uso wake chini. Malkia Sandarus alitabasamu akamjongea karibu na kumshika mabega.

“Unajua nini napendelea, mama.”
“Naitwa Zura, malkia.”
“Najua.”
“Ukiniita mama, nitashitakiwa. Nimeonywa sana juu ya hilo. Sina hadhi ya kuwa mama wa malkia.”
“Tafadhali. Siwezi kuacha kukuita mama. Na kama kuna yeyote atakayekufanya kitu basi atashughulika na mimi.”

Zura hakusema tena kitu. Amekuwa akisema hilo jambo la kuitwa mama kila siku na inaonekana anaongea na sikio la kufa. Aliufunga mdomo wake akafuata chakula akipendacho malkia wake: Aliporejea na kuhakikisha malkia wake anakula, aligeuza aondoke ila akaitwa pale tu alipofika mlangoni.

“Mfalme anaendeleaje?” Aliuliza Malkia Sandarus akila.
“Unamaanisha mumeo?” Zura aliuliza.
“Namaanisha mfalme.” Malkia Sandarus akajibu. Zura aliguna kwanza kisha akachukua hatua chache zilizomfikisha kitandani alipoketi na malkia wake.
“Malkia, inabidi ifikie mahali ukubali ya kwamba mfalme ni mumeo. Hakuna kitakachobadili hilo kamwe.”
“Sitaki kuongelea hayo mambo, mama.”

Hilo ndilo lilikuwa jibu la Malkia Sandarus kila alipoongea na Zura kumhusu mumewe – Mfalme Loop. Hakumpenda mwanaume huyo.

Matendo yake ya kumbaka kila siku kwanguvu lakini pia kumpiga mara kwa mara kulimfanya Malkia Sandarus amchukie mwanaume huyo zaidi. Ni kwakuwa tu aliwapenda watu wa Goshen ndiyo mana alikuwepo pale, ni kwakuwa tu watu wa Goshen walimpenda ndio mana alikuwa pale la sivyo angekuwa tayari ameshatoroka, kama kila siku anavyosema.

Baada ya kumaliza kula na kujiandaa kwa mavazi maridadi Malkia Sandarus aliongozana na Zura wakaenda kwenye kingo ya mto wa Boa wakiongozana na walinzi watano waliojibebelea kwenye farasi.

Huko walinzi walikaa kando kidogo kuwapisha wanawake hao kuteta na kutembea. Walisogea mbali zaidi na walinzi, Zura akamshika mkono Sandarus na kuhakikisha kwanza kama wapo mwenyewe. Ni kweli walikuwa wenyewe. Sasa akamnong’oneza:
“Kuna kitu nataka nikuambie.”

Malkia Sandarus aliogopa. Hakuwahi kumuona Zura katika hali hiyo na bila shaka sasa alitegemea kuna kitu makini anataka kuambiwa. Zura alitazama tena kushoto na kulia akarudia:
“Kuna kitu nataka nikuambie.”

“Sema.” Malkia Sandarus alisema kwa pupa. Sauti yake ililowa hofu. Alikuwa anaishiwa staha ya kungoja sasa. Zura alishusha pumzi ndefu, akasema:
“Kuna kitu niliambiwa nikupatie.”

“Kitu gani?”

“Mkufu. Baba yako kabla hajafariki alinihasa nikupatie mkufu huo. Lakini kwa siri sana, na haitakiwi yoyote aone wala kuuvaa kabisa.”

Malkia alikunja sura. Kuna kitu alihisi akipo sawa. Alijua baba yake amefariki tena kabla hata hajapata uwezo wa kumkumbuka kwa undani. Kwanini leo hii anapewa hiko kitu?

Na kwanini mkufu na si kingineko? Maswali hayo yalikuja upesi mno kichwani kwake. Aliyauliza Zura akamjibu kwa utulivu:
“Nimeshindwa kabisa kuendelea kutunza jambo hilo kifuani mwangu. Ila ujue kwamba wakati baba yako anafariki aliniita faragha akanipatia mkufu huo kwasababu aliniamini. Aliniambia hata mfalme asijue hilo. Aliniambia na kunielekeza mengi juu ya huo mkufu, lakini pia …” Hakumalizia. “Lakini nini?” Malkia aliwahi kuuliza.

Zura alitazama chini asiseme kitu. Alitazama tu maji ya mto yakitiririka. Kifuani mwake kuna jambo alikuwa anataka sema ila alikuwa anaogopa. Haikuwa na mantiki sasa kulificha jambo hilo ilhali ameshagusia jambo la mkufu, moyo wake ulimwambia.

Wakati akiyafikiria hayo Malkia alikuwa anamtazama kwa matamanio ya kutaka kusikia.

“Unatakiwa uvae mkufu huo baada tu ya mfalme kufa.” Alisema Zura.
“Kwanini?” Malkia Sandarus akauliza.
“Sijajua kwanini ila ndivyo baba yako alivyoniambia.”

Haikuleta maana kwanini mkufu huo una masharti hivyo. Hakuna aliyejua, hata Zura mwenyewe aliyekabidhiwa alikuwa ana ufahamu finyu juu ya hilo.

Waliondoka huko mtoni wakaelekea mpaka nyumbani kwa Zura, huko mkufu ukachopolewa toka kwenye kiboksi kidogo cheusi cha mbao, akakabidhiwa Malkia Sandarus. Mkufu huo ulipoketi kwenye kiganja cha mwanamke huyo, uling’aa kisha ukazima ghafla.

“Ndio huo!” Zura alisema.

Ghafla mlango ulifunguliwa akaingia mwanaume mnene mwenye ndevu na nywele nyingi. Alikuwa ni mume wa Zura. Mkufu ulifichwa haraka asipate kuuona. Alipomuona Malkia alipiga magoti akasalimu.

“Naweza nikaenda?” Malkia aliuliza akimtazama Zura.

“Ndio waweza kwenda, malkia wangu.”

Kabla hajaenda, akasema:
“Nitahitaji kukuona muda si mrefu.”

Aliondoka akaenda kuketi mwenyewe chumbani kwake. Alitazama mkufu ule aliopatiwa akiupekuapekua na maswali mengi yasiyo na majibu yakigonga kichwani. Mwishowe aliutia ndani ya kiboksi na kukiweka chini ya uvungu mwa kitanda.

Baada ya siku mbili, mfalme Loop alifariki dunia. Msiba wake ulivuma na wakuu wa tawala kadha wa kadha wakahudhuria. Alifariki akiwa na miaka mia moja kamili.

Msiba wake ulidumu kwa juma moja kisha baraza la wazee wa tawala la Goshen likaketi kwa ajili ya kuzungumza na kupanga juu ya nani ataendeleza utawala tangu mfalme akiwa hai hakufanikiwa kupata hata mtoto mmoja toka kwa wake zake wote wanne.

Kwenye majadiliano ya baraza hilo akateuliwa Mzee Fursa kusimamia tawala ya Goshen kwa muda wa takribani mwezi mmoja wakati mchakato wa kumpata mrithi ukifanyika kwa kukusanya maoni toka kwa wajumbe na pia wananchi.

Ndani ya muda huo wa mwezi, siku moja ikiwa ni katikati ya usiku mnene, Malkia Sandarus aliamka toka usingizini baada ya kusikia sauti ya kitu kikigonga mbao.

Alifungua macho yake akastaajabu kukuta chumba chake kikubwa chenye kila aina ya samani za ghali na za kupendeza kikiwa na mwanga mwekundu hafifu. Alifuatilia mwanga huo akagundua unatoka chini ya uvungu wake wa kitanda.


Alitaka kuita mlinzi aliyekuwa amesimama nje ya mlango, ila akasita. Alijibandua toka kitandani akachungulia chini ya kitanda, akaona mwanga huo watoka ndani ya kisanduku kile cheusi alichokabidhiwa na Zura.

Ilikuwa ni mkufu? Alijiuliza na nafsiye.

Alivuta kisanduku hicho akakifunua na kutazama. Kweli ilikuwa ni mkufu! Ulikuwa unawaka kama vile ulivyowaka kwa mara ya kwanza ulipotiwa mkononi mwake. Alibakia akiutazama mkufu huo na kujiuliza maswali kadhaa: kwanini unawaka? Kwanini alikabidhiwa tena kwa masharti?

Akiwa anaupekuapekua kwa kuugeuzageuza, pasipo kujua mwanga wa mkufu huo ukapenya chini ya mlango na kutua kwenye kiatu kikubwa cha mlinzi aliyekuwa amesimama huko nje.

Mlinzi alipata wasi akagonga mlango kuulizia usalama. Ila ajabu, mwanga wa mkufu ulijifinya na kupotea ghafla.

Malkia Sandarus aliurudisha mkufu huo ndani ya kisanduku kisha akajilaza. Usingizi haukumjia haraka kwasababu ya mawazo yaliyokuwa yamemtinda. Alitamani pakuche ili apate fursa ya kuulizana hilo jambo na Zura maana ndiye mtu pekee anayeweza kujadili naye juu ya mkufu huo.

Palikucha na alipoamka tu, alikutana na uso kwa uso na Zura. Alikuwa tayari ameshafika kwa ajili ya kufanya usafi na kusikiliza haja za malkia wake. Malkia alimueleza yale yote aliyopata kuyaona usiku, Zura akamkumbusha:
“Malkia wangu, uliambiwa uvae mkufu huo punde tu mfalme atakapokufa.”

“Na je nikiulizwa ni wapi nilipoutoa, nitasemaje?”

“Utalaghai mfalme alikuletea kama zawadi toka tawala za mbali.”

Malkia Sandarus alivaa mkufu huo, punde ukawaka na kuzima kama vile ulivyofanya kipindi cha kwanza kabisa. Hapo zikapita siku kadhaa na kukaribia kabisa siku ya kuwasilishwa maoni na mapendekezo ya wajumbe na wananchi juu ya nani atachukua utawala wa Goshen. .
.
.
.
.*** .
.
.
.
Katikati ya usiku mnene wa kuamkia siku ya mapendekezo na maoni, Malkia Sandarus alihisi joto kali kwenye kifua chake. Aliamka upesi kutazama akakuta kidani cha mkufu wake chawaka na kumetameta.

Alidhani ni kama siku zile, ila baada ya muda kidogo akagundua haikuwa kama siku zile kwani siku ile mkufu huo hakumuunguza na wala haukuwa wa moto kama siku hiyo. Haraka alivua akauweka mkononi. Ilimchukua muda mfupi tu akagundua kwamba kuna kitu.

Ndio.

Ukiachana na mwanga uliokuwa unamulika, kulikuwa kuna kitu ndani ya mwanga huo. Alitazama ukutani akaona picha ya mtu ndani ya huo mwanga. Alikuwa ni mwanaume mnene, mrefu mweusi.

Alitazama vema akagundua mwanaume huyo alikuwa ni mzee Fursa. Alikuwa anaongea na wazee watatu wa baraza na kandokando mwao walikuwepo wanajeshi watatu.

“Hatuwezi tukakubaliana na hili.” Sauti ya Fursa ilisikika toka mkufuni. Malkia Sandarus alisogeza masikio yake kwenye mkufu huku macho yake yakiangaza ukutani. “Mwanamke atatuongozaje?

Siwezi kabisa nikaheshimu maoni haya. Na hii ni kwa ajili ya Goshen. Endapo tukiruhusu akashika madaraka, basi lazima tutayumba na hakika Jayit muuaji atatuvamia na kuifanya hii tawala kuwa simulizi.”


Jayit ni mtawala wa Devonship. Tawala hiyo ipo upande wa magharibi ya mbali na tangu iundwe haijawahi kupatana na tawala ya Goshen hata kidogo. Chanzo cha chuki na uhasama wao ni vita iliyotokea huko miaka ya nyuma kwasababu ya kugombania ardhi ya makaburi.

Mtawala huyo wa Devonship alitaka ardhi hiyo kwa madai babu yake alizikwa hapo. Anahitaji ardhi hiyo hata kama kwa muda huo hakuwa tena mkazi wa Goshen. Hakuna aliyejua mpaka sasa kwanini anataka makaburi hayo, ila ndani ya roho yake alikuwa na kazi nayo kubwa na muhimu mno.

Kazi hiyo kwa miaka nenda rudi haijapata kutimia kwasababu tu ya kuhofia utawala wa Goshen chini ya familia ya Loop.

Ila kwa sasa familia hiyo imeenda baada ya mazishi, na haijaacha hata mtu wa kuendeleza utawala huo uliokuwa na mahusiano makubwa na tawala za karibu. Sasa Jayit anaona hiyo ni fursa marigoli kupata anachokitimiza. Hiyo ndio fursa adhimu ya kutimiza haja zake:

Kupata ardhi ya makaburi!

Malkia Sandarus alishika mdomo wake kwa mshangao akitazama ukutani. Hakuamini alichokuwa anakiona. Hakuamini kama mzee Fursa anaweza akapanga tukio kama lile la kupuuza mapendekezo na maoni ya wananchi. Na si tu kwamba ameishia hapo ila sasa alikuwa ameagiza wanajeshi wale watatu waje kummaliza!

Kwa muda kidogo Malkia hakuamini kile alichokuwa anakiona. Kwa namna moja ama nyingine alihisi analaghaiwa na ule mkufu ambao umepanga kumkosanisha na watu wake. Ila baada ya muda mfupi alijikuta ananza kusadiki.

Alisikia sauti ya mwanajeshi ikilalamika kwa maumivu mlangoni kisha akasikia kishindo cha mtu akidondoka. Ghafla mwanga wa mkufu ulizima na kukawa giza. Na sasa mlango wake ukawa unapigwa kwanguvu ukilengwa kuvunjwa! Moyo wake ulitatuka. Ni haraka akajikuta anapata joto kali mwilini la kutosha kabisa kumvujisha jasho.
.
.
.
***
 
MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN --- 002

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Alisikia sauti ya mwanajeshi ikilalamika kwa maumivu mlangoni kisha akasikia kishindo cha mtu akidondoka.

Ghafla mwanga wa mkufu ulizima na kukawa giza. Na sasa mlango wake ukawa unapigwa kwanguvu ukilengwa kuvunjwa! Moyo wake ukatatuka.

Ni haraka akajikuta anapata joto kali mwilini la kutosha kabisa kumvujisha jasho.

ENDELEA

Afanye nini? Akili yake ilijiuliza na kuanza kuchambua upesi. Kama angeendelea kukaa mule ndani ya dakika moja basi angekuwa mikononi mwa wale wanaokuja kuuchukua uhai wake kama vile walivyoagizwa na Fursa.

Alisimama upesi akaendea dirisha la chumba chake. Alitazama chini akapaona mbali, je angojee wanaokuja? Hapana! Alijitupia huko nje akafikia kwa kudondoka kama mzigo.

Akaumia mno, ila hakutaka kukaa hapo akanyanyuka na kuanza kukimbia. Wanaume wale waliokuwa wamemfuata walimtazama kwa kupitia dirishani na kumnyooshea kidole kabla hawajatoka hapo upesi kwenda kumfuata.

Ajabu Malkia alikuwa anakimbia kama chizi. Alikuwa anajificha kama mwivi akijibanza na kutokozea kule. Hakutaka kukutana na mlinzi yeyote hivyo alikuwa makini mno kutazama na kuhakikisha kabla hajachomoza na kupiga kwata.

Aliendea banda la farasi huko akapiga mluzi na haraka farasi wake rangi nyeupe akajiri toka gizani. Alimkwea wakaondoka upesi toka eneo lile.

Ilikuwa ni usiku mkali na kulikuwa tulivu mno. Watu waliopo nje walikuwa kwenye vibaa vidogo wakinywa mivinyo na kucheza, nao pia walikuwa wachache mno.

Makelele ya farasi wa Malkia akikimbia huko nje ndiyo yalisikika kwanguvu. Mwezi ulikuwa unafifia na kufunikwa na mawingu mara kwa mara. Hali ya hewa ilikuwa baridi, mbwa waliokuwa wamelala nje walikuwa wamejikunja kujipa angalau joto.

Farasi wa Malkia alisimama mbele ya nyumba ya Zura, Malkia akashuka na kugonga mlango hapo mara tatu huku akimuita Zura kwa jina. Zura aliyegundua kwamba hiyo ni sauti ya malkia wake aliamka haraka akaufungua mlango.

Alistaajabu kumuona Malkia yupo hapo kwa muda ule wa usiku mzito tena akiwa peke yake. Kabla hajauliza nini kilitukia, Malkia alimtaka apande farasi waondoke upesi.


“Tunaenda wapi malkia wangu?”

“Nakuamuru panda farasi!” Alifoka Malkia Sandarus. Zura hakubisha tena akakwea farasi huyo na haraka wakaondoka eneo hilo.

Ilichukua muda mfupi sana farasi watano waliowabebelea wanaume wenye miili mikubwa ndani ya sare za walinzi wakafika mbele ya nyumba ya Zura. Wanaume wawili walishuka upesi toka kwenye farasi wao wakauvunja mlango.

Waliwasaka Malkia Sandarus na Zura nyumba nzima lakini hawakuona kitu. Walimkwida mume wa Zura na kumtoa ndani ya nyumba wakamrushia nje kana kwamba mbwa.

“Wapo wapi?” Aliuliza mlinzi mmoja mrefu zaidi ya wote.

“Sijui walipo. Naapia kwa Mungu!” Alijibu mume wa Zura akiwa anatetemeka. Uso wake ulitia huruma mno. Mlinzi alisonya kwa kupuuzia kisha akamwambia kwa kufoka:
“Utasema tu!”

Alimnyanyua juu kisha akamtupa tena chini. Mume wa Zura alipiga kelele kali za maumivu. Kiuno chake kiliteguka na mkono wake wa kulia ulivunjika. Alisikia maumivu makali lakini wanaume wale hawakujali juu ya hilo.

“Wapo wapi?” Swali lilirudiwa. Jibu lilikuwa ni lile lile toka kwa mume wa Zura. Walimtesa mpaka pale walipohakikisha mwanaume huyo hayupo hai tena.

Walimuingiza ndani kwake wakatimka. Walitafuta ndani ya mji mzima, hawakumpata Malkia. Walirudi kwa bwana Fursa wakamfikishia hizo taarifa.

“Kamtafuteni mpaka nje ya mji!” Fursa alibweka. “Ni lazima apatikane kwa gharama yoyote ile. Ni lazima apatikane kabla hakujakucha!”

Wanaume wale waliondoka upesi kwenda kumtafuta Malkia Sandarus kwa mara ya pili. Mara hii waliongozana na mbwa watatu. Walizunguka mji mzima lakini hawakumpata.

Walitoka sasa nje ya mji wakirandaranda maporini lakini napo huko hawakufanikiwa mpaka wanafika mpakani mwa tawala yao. Walikuwa wamechoka pasi mafanikio.

“Atakuwa ameelekea nje ya Goshen.” Mmoja alisema.

“Basi hakuna haja ya kuendelea kumfuatilia. Huko lazima atauwawa.”

Waliridhia juu ya hilo kabla hawajarejea kwa Fursa na kumueleza. Japokuwa hawakumpata Malkia ila taarifa hiyo ya kutokuwepo ndani ya himaya ya Goshen ilimpatia ahueni.

“Huko nje ya Goshen hawezi akadumu.” Alisema Fursa akitabasamu. “Ni wazi wachawi wa Tanashe watamfanya kitoweo.”

Usiku huo wote aliumaliza kwa kunywa mvinyo pamoja na wazee wenzake watatu wa baraza. Walikuwa wanfurahia hatimaye kuiweka Goshen mikononi mwao.

“Hakutakuwa tena na mwingine wa kuchukua utawala huu zaidi yangu.” Alijigamba Fursa. “Mtu pekee aliyekuwa ana kura zaidi yangu haonekani. Wananchi watajua amekimbia himaya yake!”

Walicheka wakaendelea kunywa na kunywa.

Wakati usiku huo ukiwa ni murua kwao, kwa Malkia Sandarus na Zura ilikuwa ni kinyume: walikuwa porini wakipigwa baridi kali, lakini pia walikuwa nje ya himaya ya Goshen. Ilibidi wafanye hivyo kwa usalama wao kwani ndani ya himaya yao hakukuwa salama tena.

“Sasa tutafanyaje malkia wangu?” Zura aliuliza baada ya Malkia kumueleza kila kitu.

“Sijajua bado.” Akajibu Malkia Sandarus. Alikuwa anatembea kigoigoi akimvuta farasi wake.

“Basi tupumzike, malkia wangu. Kadiri tunavyokwenda huko tunasogelea hatari. Tunazidi kuiacha Goshen!” Alishauri Zura. Malkia aliona wazo hilo ni jema akamfungia farasi wake mtini wakaketi chini.

Walijikunyata kwa baridi. Walikumbatiana wapashane moto. Kutokana na usiku kuwa mwingi na pia uchovu, hawakudumu macho wakalala.

Baada ya lisaa limoja, bado ikiwa ni usiku katikati ya msitu huo uliokuwa kwenye himaya ndogo ya Tanashe, vishindo vya watu wakitembea na sauti zao zikiteta ndani ya lugha isiyoeleweka vilisikika kwa mbali.

Vishindo na sauti hizo zilikoma baada ya muda mfupi na watu hao waliokuwa wanaongea na kutembea wakaonekana: wabibi watatu wakiwa wamevalia mashuka meusi. Bibi mmoja alikuwa hana macho kabisa, mwingine alikuwa ana jicho moja na wa mwisho alikuwa na macho yote mawili.

Yule mwenye macho mawili alikuwa wa kwanza kuwaona Malkia Sandarus na Zura mtini. Yeye ndiye aliwasimamisha wenzake akawaonyeshea kwa kidole.

Waliteta ndani ya lugha yao isiyoeleweka kisha wakaanza kuwafuata binadamu hao wakiwa na nyuso zenye hamu ya kujua. Kabla hawajafika, Malkia alishituka toka usingizini. Haraka pia akamuamsha na Zura.

“Nyie binadamu mnafanya nini Tanashe?” Aliuliza mwanamke mwenye macho yote mawili. Yule ambaye hakuwa na macho kabisa alinyofoa jicho moja la mwenzake huyo kisha akalipachika usoni kwake apate kuona. Sasa kila mmoja akawa na jicho moja.

“Tumepotea!” Alisema Malkia. Bibi wale wakacheka kwanguvu.

“Hakuna anayepotea ndani ya Tanashe.” Alisema mmojawao. “Kama ukija huku basi inakuwa imepangwa!”

“Basi inakuwa imepangwa!” Akaitikia bibi mwingine kwa furaha.

“Basi inakuwa imepangwa!” Akamalizia bibi mwingine kwa furaha.

“Tafadhali, msitudhuru.” Alisema Zura. “Naomba mtupe hifadhi. Nasi tutakuja kuwarejeshea mara mbili ya fadhila zenu.”

Bibi wale walitazamana kisha wakaangua vicheko. Nyuso zao zenye jicho moja moja zilikuwa zinatisha kwa makunyanzi. Midomo yao ilikuwa na meno machache yakiwa yamekaa mbali mbali.

“Hakuna atakayewadhuru.” Alisema bibi mmoja. “Mtakuwa salama pasipo shaka lolote.”

“Pasipo shaka lolote!” Akaitikia bibi mwingine kwa furaha.

“Pasipo shaka lolote!” Akamalizia bibi mwingine kwa furaha.

Malkia alitazama na Zura pasipo kusema kitu. Mioyo yao ilikuwa na shaka, ndio. Ilikuwa ni ngumu kuwaamini bibi wale wageni machoni mwao kama kweli wanachosema ndicho wanamaanisha.

Lakini sasa watafanya nini? Ilionekana wazi hawakuwa na machaguzi mengi, hivyo japokuwa walikuwa na hofu wakaamua kuridhia kwenda na bibi wale.

Walitembea kwa mwendo wa dakika kama tatu wakafika kwenye nyumba moja kubwa mno. Nyumba hiyo ilikuwa kimya isisikike chochote, pia ilikuwa giza.

Ilizingirwa na miti mirefu kila pande, kwa giza la usiku ule kama usingeliambiwa kama pale kuna nyuma basi usingelitambua.

Mlango ulifunguliwa na wale wabibi wakatangulia kuingia ndani. Waliwasha maginga machache ya moto na kukawa kuna nuru japo si yenye nguvu. Malkia Sandarus na Zura waliketi kwenye viti walivyoelekezwa kisha wakaletewa mabakuli mawili ya supu.

Harufu yake ilikuwa kama mizoga. Hakika kama ungelipata kunusa ungekaribia ama ungelitapika kabisa. Malkia na Zura walishindwa kupeleka mabakuli hayo kinywani wakayatua mezani.

Hapo ndio Malkia akaona wabibi wale watatu wakiteta huku wakimtazama. Alipata shaka. Aliimshirikisha jambo hilo Zura, Zura akamtaka awe na subira lakini pia wawe makini.

Bibi wale waliokuwa wamekaa mbali kidogo walisogea karibu wakamtamzama Malkia.

“Wewe ni Malkia wa Goshen?” Aliuliza mmojawao. Kabla Malkia hajajibu, akamtazama kwanza Zura.

“Ndio. Mimi ni Malkia.”

“Na huo ni mkufu wako shingoni?” Swali hilo lilimshitua Malkia Sandarus. Moyo wake ulipasuka na kuzizima. Alijiuliza mara tatu kwanini ameulizwa swali lile. Je bibi hao watakuwa tayari wamegundua nguvu yake? Mdomo ulikuwa mzito kufunguka.

“Ndio ni wa kwake.” Akajibu Zura. Bibi wale walitazamana na kuteta kwa lugha isiyoeleweka, kisha tena wakarudisha nyuso zao kwa Malkia.

“Tunaweza kuuona?”

Zura na Malkia wakatazamana. “Nadhani umekwisha uona.” Zura alijibu.

“Namaanisha tunaweza tukaushika?” Alipendekeza bibi mmoja, wenzake wakatikisa kichwa kuonyesha wanaunga mkono hoja. Zura wakatazamana tena na Malkia.

Macho yao yalikuwa yana hofu na maswali ya mashaka ndaniye. Ila mwishowe Malkia aliuvua mkufu wake akawapatia. Kila bibi alinyoosha mkono wake ili autwae mkufu huo. Mwenye mkono mrefu aliupata akiwa wa kwanza, ila punde mkufu huo ulipofika kiganjani mwa bibi huyo ukawaka na kuwa wa moto.

Uliunguza mkono wa bibi aliyeupokea, bibi akaudondosha chini! Haraka bibi wote walisogea mbali na mkufu huo uliokuwa unawaka na kutoa nuru kubwa ndani ya nyumba.

Wakati wakifanya hivyo walikuwa wanateta na lugha yao isiyoeleweka. Malkia alichutama akautwaa na kuuvaa mkufuwe.

“Umetoa wapi hiki kitu?” Aliuliza bibi mmoja akimtazama Malkia.

“Nimeutoa kwa baba yangu.” Malkia alijibu.

“Baba yako anakaa wapi?”

“Alikuwa anakaa Maam. Amefariki kwa sasa!”

Wale bibi wakatazamana na kuteta kwa muda wa kama dakika tano kisha wakarudisha tena nyuso zao kwa Malkia.

“Unaweza ukatupeleka kwenye kaburi lake?”

“Mkafanye nini?”

“Kuna mambo machache tunataka kuongea naye.”

“Mtaongeaje na mtu ameshakufa.”

“Tunaweza kuongea na wafu. Tafadhali tupeleke.”

Malkia Sandarus alitazamana na Zura kisha akarudisha uso wake kwa bibi wale waliokuwa wanamtazama kwa uso wa ukame na hamu ya majibu.

“Nikiwapeleka mtanipa nini kama mrejesho?”

“Tumekupa hifadhi!”

“Hapana, hifadhi pekee haitoshi. Bila shaka kuna jambo kubwa mnataka kuling’amua.”

Bibi wale walitazamana wakateta kwa lugha yao ya kipekee kwa dakika moja kisha wakamrudia tena Malkia.

“Tutakueleza matumizi yote ya mkufu huo.”

“Malkia wangu, ni hatari kufuata hayo wanayoyataka.” Alinong’oneza Zura. “Huwezi jua wana lengo gani.”

“Usijali, nitalitilia hilo maanani.” Malkia alinong’oneza kumwambia Zura. Alikubaliana na bibi wale kuwapeleka huko makaburini, wale bibi wakafurahi mno.

Waliwataka Zura na Malkia Sandarus wawafuate kuelekea uani kwani kuna njia ya haraka kufika huko Maam ndani ya muda mfupi. Zura na Malkia wakatii.

Walielekea huko wakakuta chungu kikubwa cheusi kilichokuwa kinafuka moshi wa kijani. Wabibi wale walikizingira chungu hiko na kusema maneno kadhaa kabla hawajatia majani fulani humo chunguni na kuwaamuru Malkia na Zura waingie.

Ili kuwapa imani na kuwaondoa hofu, bibi wawili walitangulia kuingia humo chunguni. Walizama wasionekane wapi walipoelekea. Zura na Malkia walifuatia nao wakazamia, wakafuatiwa na bibi mmoja aliyebakia.

Yani kufumba na kufumbua tu wakajikuta ndani ya himaya ya Maam! Kwa Malkia na Zura likawa la kushangaza sana hilo. “Ueleko upi yapo hayo makaburi?” Aliuliza bibi mmoja upesi.

Malkia akawawelekeza na punde wakaanza kuelekea huko. Walipofika bibi wale walizingira lile kaburi la baba yake Malkia na punde likafunguka!

Alitoka humo mtu mithili ya zombie. Akiwa kama mtu anayejua alichoitiwa alielekea moja kwa moja kwa wale bibi, akaongeleshwa na lugha isiyoeleweka. Alitikisa kichwa mara mbili kuitikia. Alipotikisa kichwa mara ya tatu alimgeukia Malkia Sandarus na Zura.

Macho yake yalikuwa yanang’aa kwa wekundu. Uso wake japokuwa haukuwa na nyama lakini ulionekana kughafirika. Alipiga hatua ndefu kuwafuata Malkia na Zura na mkono wake wa kuume ulikuwa unanyooshea kifuani palipokuwa na mkufu!

Hapo Malkia akaamka toka usingizini. Kumbe ilikuwa ni ndoto! Akiwa anahema kwa pupa na macho yake yakiwa yamemtoka, alitazama kushoto kwake. Huko akawaona wale bibi wakiwa wamesimama.

Walikuwa vilevile kama alivyowaona ndotoni. Alimuamasha Zura upesi, bibi mwenye macho mawili akawauliza:

“Nyie binadamu mnafanya nini Tanashe?”

Malkia akatahamaki zaidi kwani lilikuwa ni swali lilelile aliloulizwa akiwa ndotoni.

Na sasa hapo ndipo akajua ya kwamba yale aliyoyaona ndotoni yalikuwa ni yale yatakayotukia mbele yake.

Sasa afanyaje?
.
.
.
.
****
.
.
.
Lako jicho.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom