SEHEMU YA 34:
Ilipofika saa tatu bila kumuona mke wangu nilijaribu kupiga tena simu lakini bado haikuwa ikipatikana. Niliamua kwenda kwa wazazi wake kutaka kujua kuna kitu gani kimetokea kiasi cha mke wangu kuondoka haraka na simu yake kutokuwa hewani kipindi kirefu.
Niliamua kumfuata kwao, nilitoka na kuegesha mlango, sikutaka kuufunga kwa kuhofia kupishana naye.
Nilikwenda ukweni kumuulizia mke wangu, nilikodi gari mpaka kwa wakwe zangu. Bahati nzuri nilikuta bado hawajalala, baada ya kugonga hodi mama mkwe alinikaribisha kwa vile aliifahamu sauti yangu.
Karibu baba Zawadi.
Asante mama, shikamoo, niliamkia huku nikiingia ndani na kukaa kwenye kochi.
Marahaba, kwema utokako?
Namshukuru Mungu, sijui mwenzangu amefika huku?
Mmh! Kwa leo sijamuona, kauli ile ilinishtua sana lakini nilificha mshtuko wangu.
Sasa atakuwa amekwenda wapi? nilijikuta nikimuuliza swali mama mkwe lisilomhusu.
Nitajuaje baba, kwani alikuaga anakwenda wapi?
Mama, yaani nimerudi nyumbani nimekuta ufunguo kwa jirani bila maelezo yoyote.
Zawadi yupo wapi?
Ameondoka naye.
Mmh! Sasa atakuwa amekwenda wapi?
Hata mimi nashangaa tena nasikia kaondoka na ile gari ya yule mwanaume wake.
Mmh! Unasema kweli? mama mkwe alionesha kushtuka.
Kutokana na maelezo ya mtu aliyemuona.
Kwa hiyo hukumuona kwa macho yako?
Sijamuona mama nimeambiwa.
Basi usifikirie moja kwa moja kuwa ameondoka na mwanaume wake wa zamani, kwani ameondoka tangu saa ngapi?
Saa tano.
Saa tano, sasa atakuwa amekwenda wapi na mtoto, kwani hali hii imetokea mara ngapi?
Ni leo tu mama toka tumalize yale matatizo yetu.
Nakuomba rudi nyumbani ukapumzike, akirudi atakueleza alikuwa wapi kama maneno yake hayaeleweki mlete kwangu. Nimechoka na upumbavu wake, hawezi kutuchezea akili kiasi hiki, mama mkwe naye alionekana kukerwa na kitendo cha mke wangu kuondoka bila kuaga.
Sawa mama.
Nina imani hakufika mbali angekuwa amekwenda peke yake ningekuwa na wasiwasi, lakini kwa vile ameondoka na mtoto atawahi kurudi tu huenda mmepishana amesharudi nyumbani.
Nitashukuru mama.
Basi baba rudi nyumbani, nina imani mpaka muda huu atakuwa amerudi tu.
Sawa mama, nilikubaliana na mama mkwe na kugeuza kurudi nymbani nikiwa na matumaini ya kumkuta.