SEHEMU YA 41
Siku ya Jumamosi ilipofika, nilikodi pikipiki kwa ajili ya kuzunguka makanisa yote ya mjini. Kanisa kubwa lilikuwa katikati ya mji pia madogo yalikuwa pembeni kidogo na mji hayakupungua manne.
Niliamini hata kama ningezunguka kutwa nzima nitaweza kufika toka kanisa moja kwenda lingine kwa wakati bila kuchelewa.
Dereva wa pikipiki aliniuliza swali baada ya kuzunguka zaidi ya mara mbili makanisa yote ambayo hayakuonesha dalili zozote za kufungwa ndoa.
“Sikiliza ndugu yangu, tutamaliza mafuta bure, kwa nini tusiende kwenye ofisi za kanisa ili tujue kuna ndoa au hakuna na kama ipo itafungwa saa ngapi? Hiyo itatusaidia kuja kwa wakati kuliko kuzunguka na kukufanya upoteze fedha nyingi.”
Wazo lile nilikubaliana nalo na kuamua kwenda kwenye ofisi za kanisa kuulizia kama kuna ndoa ilikuwa ikifungwa siku ile. Makanisa yote manne yalinieleza kuwa siku ile hakukuwa na ndoa yoyote ila Jumapili kulikuwa na ndoa nne ambazo zote zingefungwa kwenye kanisa kuu tu.
Niliamini katika ndoa zile nne lazima moja itakuwa ya mke wangu kipenzi Suzana, mama Zawadi.
Nilimshukuru dereva wa pikipiki ambaye kwa sasa angeitwa bodaboda. Nilikubaliana naye kunifuata nyumbani siku inayofuata na kunipeleka kanisani ili nikaweke pingamizi ndoa ya mke wangu.
Baada ya kurudi nyumbani nilikuwa na mawazo mengi kuhusiana na hiyo kesho na kujiuliza nitakapotoa pingamizi litakubaliwa au ndiyo nitaabika hasa kutokana na ndoa yetu kufungiwa Bomani.
Upande mwingine niliamini nitakuwa na nguvu ya kuvunja ndoa ya mke wangu kwa vile ilikuwa ikitambuilika kiserikali na vyeti nilikuwa navyo.
Nilipanga kesho nikienda kuweka pingamizi niende na vyeti vya ndoa ili kutia uzito pale mke wangu atakaponikana.
Siri ile sikutaka kumshirikisha Simon kwa kuhofia kunipa ushauri mbaya ambao ungeharibu mipango yangu yote. Ushauri wa Simon mwanzo niliuamini lakini baada ya ushauri wake kusababisha mke wangu kukimbia, sikumuamini tena na kuona ndiye chanzo cha matatizo yangu.
Siku ya pili, baada ya kufuatwa na dereva wa pikipiki niliwasili kanisani saa tatu asubuhi japokuwa ndoa ilikuwa ikifungwa saa saba mchana.
Nilikaa pale mpaka saa nne na nusu ndipo magari ya maharusi na ndugu na jamaa walipoanza kuingia. Muda mfupi kanisani pakawa na watu wengi na magari kutokana na harusi nne kufungwa, nilisubiri kwa hamu nimuone mke wangu akitaka kufunga ndoa na kuweka pingamizi.
Nami nilikuwa mmoja wa watu niliowahi ndani viti vya mbele kanisani kusubiri ibada ya ndoa. Kanisa lilijaa watu wengi sana pamoja na maharusi wote. Kwa vile mabibi harusi walikuwa wameziba nyuso zao, iliniwia vigumu kumtambua mke wangu ni nani kati ya wale wanne.
Baada ya taratibu zote kufanyika ndoa zilianza kufungwa moja moja huku nikisubiri kwa hamu kuiona sura ya mke wangu. Ajabu ndoa zote zilifungwa bila kuiona sura ya mke wangu. Nilijikuta napagawa na kujiuliza nilielezwa ndoa nne au tano?
Baada ya ndoa zote kufungwa bila kushuhudia sura ya mke wangu, watu wote walitoka kanisani na kubakia peke yangu. Nilijiuliza mke wangu atakuwa amekwenda kufunga ndoa wapi.
Nikiwa nado nimesimama kama sanamu nikiwa bado na matumaini huenda kuna ndoa nyingine ingekuja kufungwa, nilishtuliwa na mhudumu wa kanisa.
“Ndugu vipi mbona huondoki na wenzako?”
“Samahani kaka kuna ndoa nyingine zaidi ya hizi?”
“Hakuna, leo kulikuwa na ndoa nne tu hakuna zaidi ya hizi.”
“Mmh! Sijui watakuwa wamekwenda kufunga ndoa wapi?” nilijikuta nikizungumza peke yangu kwa sauti.
“Kina nani?” mhudumu wa kanisa aliniuliza.
“Ooh! Samahani,” nilijikuta nikijibu na kuondoka bila kuaga mpaka nje ya kanisa.
Nje ya kanisa watu walikuwa ndiyo wanamalizikia kuondoka, nilijikuta nimerudi nyumbani kwa miguu na kumsahau dereva wa pikipiki aliyenipeleka. Kwa kweli nilikuwa nimechanganyikiwa na kuamini kama maneno aliyonieleza mke wangu yana ukweli basi atakuwa amefunga ndoa siku ile.
Usiku ulikuwa mrefu kwangu, usingizi ulinikimbia kabisa. Mawazo yote yalikuwa kwa mke wangu na kuona kama kweli ameolewa basi atakuwa amenifanyia ukatili mkubwa sana. Siku ya pili ilikuwa Jumatatu, sikuweza kwenda kazini, nilikuwa kama mtu niliyefiwa, hata chakula kilinishinda.
Jioni Simon alikuja kunitazama na mmoja wa wafanyakazi wenzangu na kunikuta nimejilaza sebuleni mikono kichwani huku pembeni ya macho yangu yakiweka michirizi na kulowesha kwenye mito ya kochi. Simon alinishangaa sana na kuniuliza:
“Kazala una matatizo gani?”
“Simon wewe si wakuniuliza swali kama hilo, unajua vizuri matatizo yangu,” nilimjibu bila kumuangalia.
“Kazala umetoka nyumbani kufuata mapenzi au kazi?”
“Nimefuata kazi.”
“Unaacha kwenda kazini kwa ajili ya mwanamke, nilikueleza toka zamani kuwa huyu mwanamke si chaguo sahihi kwako, lakini ukaona labda nakuchokonoa majibu sasa umeyaona.”
“Simon usiseme hivyo wewe ndiyo sababu ya mke wangu kunikimbia.”
“Mimi?” Kauli yangu ilimshtua Simon.
“Ndiyo.”
“Mimi nimefanya nini?” alionesha kushangaa.
“Ushauri wako ndiyo sababu ya mke wangu kukimbia.”
“Kweli aliyekuroga amekufa, kitendo cha kumfumania mkeo ni mimi? Si ulitaka kufa kwa mawazo nimekusaidia bado huoni msaada wangu?”
“Msaada gani wakati mke wangu kanikimbia.”
“Mkeo yule sawa na kuku aliyelala nje, si kuku tena ni kwale.”
“Lakini umeona lawama zote zinatokana na ninyi watu wa pembeni kuingilia ndoa yangu.”
“Hao watu wa pembeni unaowalaumu ndiyo waliomponya mwanao aliyekuwa fundi majiko.”
“Pamoja na hayo, lakini ninyi ndiyo chanzo cha mke wangu kukimbia.”
“Kwani shemeji kaenda wapi?” Shedu, mfanyakazi mwenzangu aliyeongozana na Simon aliniuliza.
“Hata najua yule mwanamke kaamua kuniua ningali hai,” nilizungumza kwa sauti ya kukata tamaa.
“Kazala wanawake wamekwisha mpaka uchanganyikiwe kiasi hiki?” Shedu aliniuliza.
“Kwani huyo aliyemchukua mke wangu hakuona wanawake wengine mpaka kamchukua mke wangu? Kibaya zaidi jana kamuoa kabisa.”
“Utani huo! Atamuoaje mke wa mtu?” Shedu alishtuka.
“Mpaka kamtoa kwangu atashindwa vipi kumuoa kabisa?”
“Kwa hiyo Kazala bado unampenda mkeo?” Shedu aliniuliza akinikazia macho.
“Tena sana.”
“Na akirudi utakuwa tayari kumsamehe?”
“Ndiyo, najua si akili yake ni ushawishi wa watu wenye fedha wanaoona maskini kama sisi hatuna haki ya kuwa na wanawake wazuri.”
“Mtu mwenyewe unamjua?”
“Kwa sura namjua ila sijui anakaa wapi?”
“Upo tayari kumeza mfupa?”
“Una maana gani?”
“Najua huna uwezo wa kushindana na yule bwana kwa nguvu na fedha, lakini lipo kimbilio la wanyonge nakwambia mkeo atarudi mwenyewe.”
“Kimbilio la wanyonge! Kimbilio gani?” nilishtuka kusikia vile na kutaka kulijua hilo kimbilio la wanyonge.
“Kwa babu.”
“Kwa babu una maana gani?”
“Kwa mganga wa kienyeji.”
“Kweli ataweza?” nilimuuliza kutaka uhakika.
“Bwana wee tena hawa wanaopenda wake za watu kazi yake ndogo sana, nakwambia ndani ya siku mbili mkeo atarudi, ikivuka haifiki wiki.”
“Kweli?”
“Kweli kabisa, unajua taarifa zako nimezisikia toka kwa swahiba wangu hapa, roho iliniuma na kuona umefanyiwa ukatili, kibaya nasikia jamaa ana mke yaani asiridhike na mkewe aje amchukue wako? Tena nitakupeleka mguu kwa mguu hadi kwa mzee wangu, nakuapia mkeo atarudi,” Shedu alinihakikishia kunirejeshea furaha.
“Kama kamuoa?” niliuliza swali ambalo kwangu lilikuwa tata.
“Nimekueleza mkeo atarudi, si mkeo wa ndoa?”
“Ndiyo.”
“Basi atarudi huyo, tukifika kwa babu kazi imekwisha.”
“Gharama zake?”
“Si kubwa sana, utamudu tu.”
“Huyo babu yupo wapi?”
“Tanga katika Wilaya ya Lushoto Kijiji cha Mlalo kisha unaingia ndani zaidi kuna sehemu inaitwa Tewe, hapo temea mate chini kuna kufuru za ajabu, watu wanaweza hata kumfufua maiti akatembea.”
“Nauli yake si kubwa?”
“Ya kawaida utaimudu.”
“Mmh! Nipo tayari hata kesho.”
“Itabidi muombe ruhusa ya siku mbili ili mwende na kurudi,” Simon aliyekuwa kimya muda wote alichangia.
“Lakini Shedu usemacho ni kweli?” pamoja na Simon kuchangia bado sikumuamini Shedu.
“Kwa nini tuandikie mate na wino upo? We twende halafu uniulize swali hilo baada ya kutoka kwa babu.”
Tulikubaliana kesho nikaombe ruhusa kazini ili twende Mkoa wa Tanga kwa mtaalam.