SEHEMU YA 27….
“Acha ujinga, mwenye amri kwenye nyumba ni mwanaume, umeona sababu ya kupangiwa kurudi nyumbani? Ilikuwa ili ajiandae usimfumanie. Umerudi mara moja na kukuta yale, hebu jiulize tangu mhamie hapo ni mara ngapi yule mwanaume anakuja kama kwake na kufanya uchafu wake?”
“Nashangaa sasa hivi sijui amekuwaje, lakini siku zote mke wangu alikuwa mtu mwenye heshima, hata sijui kabadilika vipi?” bado niliendelea kumtetea mke wangu.
“Kazala mkeo si mtulivu tangu mwanzo, sema ulikuwa hujui kwa vile jambo usilolijua ni sawa na usiku wa giza. Lakini hafai kuwa mke wa mtu. ”
“Kwa hiyo unanishauri nini kwa hili?”
“Hapa hakuna chochote cha kufanya, kama umeyajua yote mabaya ya mkeo na mengine kushuhudia kwa macho yako unasubiri nini, unataka akuue?”
“Unanishauri nifanye nini?”
“Yule mwanamke hakufai, achana naye ujipange upya bila hivyo atakuua kwa kihoro. Hebu jiangalie, umeshuhudia uchafu wa mkeo mara moja tu, umekuwa hivi kama mgonjwa wa kifua kikuu. Ameshakujua wewe nyoka wa plastiki huumi, ipo siku atakuteremsha kitandani ili alale na mwanaume wake.”
“Wee atawahi?” nilijikakamua mwanaume.
“Utafanya nini?”
“Nitaua mtu.”
“Hukuua mtu ulipofumania watu wapo kitandani hawana nguo mwilini, utaweza kusema kitu mbele ya mwanaume mwenzako aliyewapangia nyumba?”
“Lakini nilimsikia akisema hata yeye hapendi kuja pale nyumbani ila mke wangu ndiye anayemlazimisha,” najua majibu yangu yatakufanya unicheke na kuniona zuzu, nioneeni huruma mwenzenu kweli nilikamatika, kupenda kubaya, nilikuwa zuzu kwisha kazi.
“Kazala majibu gani hayo? Mbona kupenda kumekugeuza zuzu, au umeinamishwa?”
“Sijainamishwa,” nilikataa katakata neno la kuinamishwa na mke wangu zaidi ya kumpenda tu.
“Basi ndugu yangu kwa usalama wako muache yule mwanamke kabla hajakuacha, la sivyo muda si mrefu utakufa au kuwa nwendawazimu.”
“Kwa kweli kuachana na mke wangu siwezi labda unipe njia nyingine ya kumtuliza.”
“Utamtuliza vipi?”
“Kwa vyovyote vile hata kwenda kumueleza yule jamaa aachane na mke wangu.”
“Mimi siwezi kufanya hiyo kazi, labda ukamueleze mwenyewe kwani mbaya wako si unamjua?”
“Basi nakuomba kitu kimoja.”
“Kitu gani,” kauli ile ilinifanya nikae vizuri kumsikiliza.