Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

SEHEMU YA 108...

Akampigia simu, kitu cha kwanza kabisa alichokutana nacho ni malalamiko kutoka kwa mzee huyo kwamba hakumpata mtoto, pale walipokubaliana kwamba mtoto angekuwepo, hakumkuta.
“Unasemaje?” aliuliza nesi huku akishtuka.

“Hakuna mtoto! Yupo wapi?”
“Si nilikwambia kwenye lile pipa nililokuonyeshea jana!” “Sikumkuta!”
“YoU must be kidding me,” (unanitakia) alisema nesi huku akionekana kuchanganyikiwa.
Hakutaka kubaki ndani ya hospitali, akatoka huku akiwa na presha kubwa, hakutegemea kusikia kile alichokisikia kwamba mtoto hakuwepo katika pipa lile na wakati alimuweka na kurudi ndani.
Alipotoka nje, akaelekea katika pipa lile, hakumkuta mtoto kitu kilichomchanganya. Hakuridhika kuangalia juu ya pipa tu bali akaanza kuangalia kila kona, hakikubadilika kitu, kila kona hakuona mtoto kitu kilichomfanya kuwa na hofu kubwa.

“Ila alikuwa hapa,” alisema nesi.
“Yupo wapi sasa?”
“Nilimuweka hapa,” alisema nesi na kuondoka mahali hapo, akaenda kwa walinzi getini, alijua fika kwamba kama mtoto alichukuliwa mahali pale ilikuwa ni lazima mtu huyo apite pale getini, akaenda mpaka kule, alipouliza akaambiwa kwamba kulikuwa na mwanaume aliyepita dakika chache zilizopita akiwa na mtoto.

“Mbona hamkumzuia?” aliuliza nesi huku akichanganyikiwa.
“Sisi tulijua ndiyo mtu wa mipango ndiyo maana tukaachana naye!” alijibu mlinzi mmoja.
“Mungu wangu! Tumekwisha!”
Nesi akarudi ndani huku akikimbia, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, hakumjua mtu aliyemuiba mtoto huyo, alitetemeka kwa hofu kubwa, akawafuata wenzake, akawaambia kila kitu kilichotokea kwamba mtoto hakuwepo.

Kila mmoja alichanganyikiwa, wengine wakahisi kwamba kama wanataniwa kwani kila wapokuwa wakifanya dili la kuiba watoto walikuwa wakipelekwa huko na hakukuwa na mtu aliyekuwa akiwachukua, sasa ilikuwaje huyo achukuliwe?
Hospitalini kulikuwa ni kizaazaa, kitendo cha kutumia bastola humo kiliwafanya polisi kumkamata na kumpeleka kituoni ambapo huko akaelezea kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Itaendelea
 
SEHEMU YA 109...

Kwanza polisi hawakujua kama mtu huyo ndiye alikuwa yule Richard bilionea aliyekuwa akivuma kwa utajiri lakini baada ya kujielezea kidogo polisi wote wakaonyesha heshima kwani mtu aliyesimama mbele yao hakuwa wa mchezomchezo, mbaya zaidi mpaka namba ya rais alikuwa nayo kwenye simu yake.

Aliwaambia kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba mkewe alikuwa na ujauzito wa watoto mapacha na si mtoto mmoja kama ilivyojionyesha. Akatakiwa kupeleka ushahidi hilo halikuwa tatizo, kwa sababu karatasi ngumu za Ultra sound alikuwa nazo, akazipeleka na kuwaonyeshea, hakuishia hapo, mpaka madaktari ambao walimpima katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili wakaripoti kituoni na kuthibitisha kwamba kweli Bianca alikuwa na mimba ya watoto mapacha.

“Kwanza manesi na madaktari wote waliokuwa ndani ya chumba kile wanatakiwa kufikishwa polisi,” alisema mkuu wa kituo.
Hilo likafanyika, haraka sana polisi wakaelekea hospitali na kuwakamata madaktari na manesi waliokuwa katika chumba cha leba na kuelekea polisi. Kila mmoja hakuona kama wangenusurika katika kesi hiyo, walikuwa wakimuomba Mungu kuwaokoa kwani Richard alikuwa tofauti na watu wengine kabisa.

“Nyie hamnijui! Mimi nawafunga jela maisha,” alisema Richard huku akiwaangalia wauguzi hao waliokuwa wakiingia ndani.
Wote wakafikishwa selo na kutakiwa kutulia huko. Kila mmoja alijuta kushiriki mchezo huo mchafu na maneno ya Richard aliyokuwa akisema kwamba angewafunga maisha yaliwatisha zaidi.
Huko wakaambiwa kwamba yule Richard bilionea waliyekuwa wakimsikia sana ndiye huyo, kila mmoja akashtuka, hofu waliyokuwa nayo ikaongezeka zaidi kitu kilichowafanya wote kuona kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao.

**** Gloria alisimama mbele ya kitanda alichokuwa mume wake, mashavu yake yalilowanishwa na machozi yaliyokuwa yakimtoka, aliumia, hakuamini kama huo ndiyo ungekuwa mwisho wa mume wake aliyekuwa akimpenda.

Moyo wake ulichoma, japokuwa mwanaume huyo alikuwa mtumiaji wa madawa ya kulevya lakini kwake hakujali, alikuwa mume bora, aliyemfanya kuwa mwanamke bora ambaye kamwe hakutaka kumuona akiondoka mikononi mwake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 110...

Alisimama huku akimwangalia, hakuwa mume wake, hakuwa akihema, alibadilika na kuwa marehemu. Madaktari wakfika katika kitanda hicho, walipogundua kwamba alikuwa amefariki wakamfunika kwa shuka la kijani na kuanza kumuondoa mahali hapo.

Wakati wakimtoa ndipo ile barua aliyoiandika David ikaanguka chini. Gloria akaichukua na kuanza kuisoma. Ilikuwa ni barua yenye kuchoma, iliyomtoa machozi mno moyoni mwake.

Alimkumbuka Sarafina, alimkumbuka yule mtoto aliyekuwa amebebwa, moyo wake uliumia mno na hakuamini kama kungekuwa na mwanaume ambaye angekuwa na moyo kama wa mume wake.

Alimsikitikia mwanamke yule, alijua kwamba Sarafina aliacha chuo kwa kuwa alikuwa na mimba, mimba ile aliitunza miezi yote na kujifungua, kwa kuwa hakuwa na maisha mazuri ndipo akaamua kuishi mitaani.

Alitakiwa kumlaumu mume wake lakini kutokana na mapenzi ya dhati aliyokuwa nayo moyoni, hakumlaumu zaidi ya kumuachia Mungu. Alilia, alihuzunika, macho yake yakawa mekundu mno kwa ajili ya kulia sana.

“Why did you do this?” (kwa nini ulifanya hivi?) aliuliza huku akiwa na barua ile mikononi mwake.
Huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kila kitu, mume wake alifariki dunia na baada ya siku tatu wakamzika David katika makaburi ya Kinondoni jini Dar es Salaam.

**** “Juma…Juma fungua mlango!” alisema Ibrahim huku akiwa amesimama mlangoni, hakuonekana kujiamini, alikuwa akiangalia huku na kule kuona kama kulikuwa na watu waliokuwa wakimfuatilia.

Mlango ukafunguliwa na mwanaume mmoja, alivalia pensi nyekundu na juu hakuwa na nguo yoyote ile. Alibaki akimshangaa Ibrahim, hakumuelewa kutokana na mazingira yaliyokuwepo, mikononi mwake alikuwa na mtoto mdogo aliyekuwa akilia sana.

“Imekuwaje? Mbona mtoto? Kwani shemeji alikuwa na mimba?” aliuliza Juma huku akimshangaa Ibrahim.
“Subiri niingie ndani kwanza!” alisema Ibrahim na kuingia.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 111

Juma hakuwa na majibu, kila alipomwangalia Ibrahim, alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka mwanaume huyo kuja na mtoto. Alijua kabisa kwamba Malaika hakuwa na mimba, mbaya zaidi Ibrahim hakuwa na msichana mwingine kiasi cha kusema kwamba aliachiwa mtoto, sasa yule mtoto alitoka wapi?

“Imekuwaje na mtoto?” aliuliza Juma.
Hapo ndipo Ibrahim alipoanza kumwambia Juma kila kitu kilichotokea hospitalini, jinsi alivyomuona mtoto yule na kwenda kumchukua. Alimsimulia kila kitu na wote kugundua kwamba inawezekana manesi walikuwa wamepanga njama za kumuuza mtoto huyo kama hospitali nyingine zilivyofanya.

“Inabidi uwe na uhakika na hili! Rudi hospitalini!” alisema Juma.
“Hivihivi?”
“Badilisha nguo halafu vaa kofia!” alishauri Juma.
Hilo ndilo alilolifanya, alitaka kujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea. Akabadilisha nguo na kuanza kurudi huko. Akasahau kuhusu mpenzi wake, Malaika, kitu kilichokuwa kichwani mwake ni mtoto yule aliyekuwa amempata.

Alipofika getini, walinzi hawakumgundua, akaingia mpaka ndani ambapo kule akakuta watu wakiwa wamekusanyana, wengine walikuwa wakijadili ishu ya mtoto iliyomfanya Ibrahim kusogea karibu ili apate ukweli juu ya kila kitu kilichokuwa kimetokea.

“Basi ndiyo hivyo! Jamaa kavimba ile kinoma. Hawa manesi siyo kabisa, wameiba mtoto bhana,” alisema jamaa mmoja.
“Kweli kabisa. Yaani unawezaje kuiba mtoto! Mtu anakuja ana mimba, mnamuhudumia, kapata mapacha halafu mnaiba mtoto mmoja, kweli haki hii?” alihoji jamaa mwingine.
“Siyo haki kabisa.”

“Kwa hiyo jamaa yupo wapi?” aliingilia Ibrahim.
“Kakamatwa! Kapelekwa polisi. Kapiga risasi kama kumi hivi,” alisema jamaa mwingine na kuongezea chumvi na wakati risasi iliyopigwa ilikuwa moja tu.
“Duuh! Yupo kituo gani?”
“Hapo Osterbay!”

Ibrahim hakutaka kubaki mahali hapo, akaondoka na kuelekea katika kituo hicho. Hakuchukua muda mrefu akafika huko, stori iliyokuwa ikibamba kituoni hapo ni juu ya mtoto aliyekuwa ameibwa.
Polisi wanawake walionekana kuchukia zaidi, walijua uchungu wa mwana, walipokuwa wakiwaona madaktari na manesi ambao walihusika katika wizi ule waliwaonyeshea chuki kubwa.
“Samahani bro!” alisema Ibrahim huku akiwa amemsogelea Richard.
 
SEHEMU YA 113...

“Naomba baadaye! Waandishi naomba mnihoji baadaye!” alisema Richard, kwa jinsi Ibrahim alivyoonekana, jinsi alivyovaa shati lake na kuchomekea kinadhifu, akahisi kwamba alikuwa mwandishi wa habari.
“Ila bro!”

“Naomba uniache!” alisema Richard kwa hasira, tena kwa sauti ya juu, hakuonekana kuwa sawa, akaelekea kaunta, baada ya dakika chache akatoka nje, akaingia ndani ya gari lake, akaliwasha na kuondoka kurudi hospitalini.

**** Hali ya Malaika ilikuwa mbaya kitandani, ugonjwa wa Sickle Cell uliendelea kumtesa, alikuwa akilia, muda wote ule aliona dhahiri kwamba alikuwa akienda kufa.

Madaktari walikuwa wakihangaika kuyaokoa maisha yake, hawakutaka kumpoteza binti huyo aliyekuwa na sura ya kipole, kwao, hakukuwa na kitu ambacho kingewauma kama kuona msichana huyo akifariki dunia.
Madaktari walikuwa wakiingia kwa zamu, walimuwekea dripu za damu kwani alikuwa amepoteza damu kwa kiwango kikubwa sana. Alitia huruma pale kitandani alipokuwa na kwa jinsi alivyokuwa akisikia maumivu, alimuona malaika mtoa roho akiwa ameingia wodini kwa ajili yake.

Alibaki akimuomba Mungu, alimshukuru kwa kila kitu, alijua dhahiri kwamba alikuwa akienda kufa lakini alitaka Mungu ampe nafasi ya kufanya mambo yaliyo mema, pale alipokosea, arekebishe na kufariki kwa amani kabisa.
Hakuwahi kuwa na maisha mazuri, siku zote maisha yake yalitawaliwa na umasikini mkubwa. Hakuwa na pesa lakini alimuomba Mungu amponye ili aweze kuwasaidia watu wengine, wale waliokuwa na matatizo, awasaidie watoke kwenye matatizo hayo waliyokuwa nayo.

Alimuomba Mungu kwa dakika kadhaa, machozi yalikuwa yakimtoka, moyo wake ulimuuma mno, ilikuwa ni kama Mungu alisikia kilio chake kwani baada ya kusema Amen, akahisi mwili wake ukianza kurudi katika hali ya kawaida, maumivu aliyokuwa nayo katika mifupa yake yakaanza kupotea.

Moyo wake ukawa na furaha kubwa, hakuamini kile kilichokuwa kikitokea, alilia sana, wakati mwingine alikuwa na hisia kwamba kulikuwa na mtu aliyekuja kitandani pale, alikuwa akimshika kuanzia miguuni mpaka kichwani, alitamani kuzungumza kitu lakini akauona mdomo wake kuwa mzito.

itaendelea.
 
SEHEMU YA 114...

Alitaka kuuliza mtu huyo alikuwa nani lakini alishindwa kufanya hivyo. Mifupa ikaacha kuuma, alibaki akishangaa, ulikuwa ni muujiza ambao hakuwa ameutegemea maishani mwake kwani kwa kawaida mifupa yake ilivyokuwa ikiuma, mpaka kupata nafuu ilikuwa ikichukua muda mrefu.

“Ugonjwa huu ni kusudio langu ili upate kile nilichomuahidi mama yako siku moja,” alisikia sauti hiyo ikizungumza, ilikuwa ni kama pembeni yake kulikuwa na mtu aliyekuwa akimwambia maneno hayo.
Haraka sana akageuka upande wa kulia ambapo alihisi kulikuwa na mtu akiwa amesimama na kumwambia maneno hayo, hakukuwa na mtu na hakujua alikuwa nani.

Aliposikia sauti hiyo, ghafla maumivu ya mifupa yakaanza kurudi tena, kwa kasi mara mbili zaidi ya ile aliyokuwa nayo kipindi cha nyuma. Alilia kwa sauti, maumivu yalizidi, alihangaika pale kitandani, alirusha miguu yake huku na kule kiasi kwamba kila mtu aliyekuwa ndani ya wodi ile alihisi kwamba hiyo ndiyo ilikuwa dakika za mwisho za kuvuta pumzi ya dunia hii.

“Lete dripu nyingine, lete dripu nyingine,” alisema daktari aliyekuwa akimhudumia, haraka sana nesi mmoja akachomoka mahali hapo na kwenda katika benki ya damu ambapo baada ya sekunde hamsini akarudi akiwa na dripu nyingine ya damu.

Wakamuwekea harakaharaka, walikuwa wakijaribu kuyaokoa maisha yake, hawakujua sababu ya hali yake kubadilika ghafla kitandani pale alipokuwa. Baada ya kuwekewa dripu ile ya damu, kidogo akarudi katika hali yake ya kawaida, machozi yalikuwa yakimtoka huku akiwa ameyafumba macho yake.

Alitia huruma pale alipokuwa. Daktari yule na nesi hawakuondoka, walibaki mahali hapo wakiangalia kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo. “Is she going to die?” (atakufa?) aliuliza nesi huku akionekana kuwa na hofu kubwa.

“No! I guess God is going to do something!” (hapana! Nafikiri Mungu anakwenda kufanya jambo) alisema daktari huyo huku akimwangalia Malaika aliyekuwa kimya kitandani pale.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 115...

Wala hazikupita dakika nyingi, Ibrahim akaingia ndani ya wodi hiyo, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutaka kujua hali ya mpenzi wake. Madaktari hawakumwambia kitu, walijua fika kwamba wangemshtua hivyo kumwambia kwamba alikuwa akiendelea vizuri na angeweza kuruhusiwa baada ya siku kadhaa.

“Alikuwa analia?” aliuliza Ibrahim.
“Ndiyo! Alikuwa akihitaji kukuona wewe!” alidanganya daktari.
“Na damu imepungua kwa kiasi kikubwa mpaka kuwekewa dripu ya pili?’ aliuliza Ibrahim huku akimwangalia Malaika.
“Ndiyo! Ila ni mzima!”
“Mmh!”
“Nini?”

Ibrahim alikuwa akimwangalia Malaika kitandani pale, kwa jinsi alivyoonekana ilikuwa ni vigumu kugundua kama msichana huyo alikuwa mzima. Alikuwa akipumulia mashine ya gesi, alionekana kuzidiwa na hata mapigo yake ya moyo yalivyokuwa yakidunda alionekana kama mtu ambaye alikuwa katika hatua za mwisho kuvuta pumzi ya dunia hii.

“Malaika! Ongea nami, Malaika usiniache peke yangu,” alisema Ibrahim huku akimwangalia msichana huyo kitandani pale.
“Usilie Ibrahim,” Ibrahim aliisikia sauti ya Malaika ikimwambia hivyo, ilikuwa ni sauti ya chini kabisa, ya kunong’oneza ambayo ilimshtua sana Ibrahim, akayainua macho yake na kumwangalia msichana huyo.

“Malaika…Malaika…” aliita.
“Usilie! Mungu anataka kufanya muujiza juu ya afya yangu,” alisema Malaika kwa sauti ya chini sana na kisha kutoa tabasamu pana, tabasamu lililowashtua hata madaktari wenyewe kwani lilikuwa tabasamu lililojaa matumaini makubwa kwamba ni kweli Mungu angekwenda kufanya muujiza juu ya afya yake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 116...

Ilikuwa ni kesi kubwa, Richard hakutaka kukubali, moyo wake ulikuwa na hasira kubwa kutokana na kile kilichokuwa kimetokea. Alikuwa akilalamika na muda wote aliwaambia madaktari kwamba ilikuwa ni lazima kufanya jambo baya ambalo lingebaki na kuwa historia mahali hapo.

Kila mtu aliona jinsi mwanaume huyo alivyokuwa akimaanisha, sura yake ilionyesha msimamo mkali juu ya kile alichokuwa akikizungumza, watu wote waliokuwa wakimsikia alivyokuwa akiongea, wakahisi kwamba mwanaume huyo angekwenda kuichoma moto hospitali hiyo.

Alisimama mbele ya mke wake, wote walikuwa wakilia. Bianca hakuamini kile kilichokuwa kimetokea, kilimuumiza mno, hakutegemea kumuona mtoto mmoja, aliambiwa kwamba alikuwa na watoto wawili na hata walivyokuwa wakichezacheza tumboni alihisi kabisa kulikuwa na watoto wawili.

Kujifungua kwake kulileta maumivu makubwa, alitegemea kwamba angepata furaha baada ya kupata mtoto lakini matokeo yake moyo wake ulikuwa na majonzi tele.

Manesi na madaktari waliohusika katika mchezo huo walikamatwa na kufikishwa polisi, kila mmoja alikuwa na hofu, walitamani kumrudishia mwanaume huyo mtoto wake lakini kitu cha ajabu kabisa, mtoto hakuonekana pale alipokuwa ameweka, kulikuwa na mtu aliyemfuata na kuondoka naye.

Hospitali hiyo ikaingia kwenye kashfa kubwa, watu wakazungumza mambo mengi kuhusu tukio lile lililokuwa limetokea. Tabia hiyo ya kuiba watoto ikawafanya watu wote kuikacha hospitali hiyo kwa kuona kwamba hata kama wao wangekwenda kujifungua hapo kulikuwa na uwezekano wa watoto wao kuibwa.

“Tena hii tabia imekuwa kubwa sana. Juzikati kuna mwanamke aliibiwa mtoto hivyohivyo katika hospitali hiyohiyo. Kumbe ndiyo mchezo wao,” alisema mwanamke mmoja, alikuwa akimwambia mwandishi wa habari.

“Tena ndugu mwandishi! Kuna dokta Zabroni, huyo ndiyo noma kwa kucheza michezo hiyo, anajenga majumba ya kifahari kwa kuwauza watoto wa wenzake,” alisema mwanamke mwingine, dokta Zabroni ndiye aliyesuka mipango yote.

Itaendelea.
 
SEHEMU 117...

Zilipita siku mbili wauguzi hao wakafikishwa mahakamani, wakakiri kuhusika kwa tukio hilo na hivyo kuhukumiwa kifungo cha miaka kumi na tano gerezani. Hilo halikumpa furaha Richard, alicheza mchezo mzima wa watu hao kufungwa gerezani kama kisasi kwa kile walichokuwa wamemfanyia.
Pamoja na hayo yaliyotokea, kuwafunga wauguzi hao, bado kulikuwa na swali moja tu kichwani mwake; mtoto wake alikuwa wapi?
*
*
*

Juma alibaki na mtoto chumbani kwake, kichwa chake hakikuwa sawa, alichanganyikiwa kwani kila alipomwangalia mtoto yule hakujua ni kitu gani alitakiwa kumfanyia.
Hakuwa na uji ndani ya chumban chake, hakuwa na kitu chochote kile zaidi ya maji na wali wa jana uliokuwa umebaki. Moyo wake ulikuwa na hofu, mtoto alikuwa akilia sana ishara iliyoonyesha kwamba alikuwa akisikia njaa kali.
Hakutaka kubaki ndani ya chumba hicho, alichokifanya ni kutoka na kwenda dukani ambapo akanunua maziwa na kurudi chumbani pale na kuanza kumnywesha mtoto yule ambaye akawa anakunywa huku akiachia tabasamu pana.

Moyo wake ukaridhika, akachukua simu yake na kumpigia Ibrahim kwa lengo la kwenda nyumbani na kumchukua mtoto huyo lakini hakuwa akipatikana.
Akawa na wasiwasi kwamba inawezekana Ibrahim alikwenda pale kumtelekeza mtoto yule na kuondoka zake. Akaanza kumsubiri huku muda wote macho yakiwa kwa mtoto yule.

Maneno aliyoambiwa kwamba mtoto yule alikuwa ameibwa hayakuingia akilini mwake, hakuamini kama kungekuwa na hospitali ambayo ingethubutu kufanya kitu cha kijinga kama hicho, alichohisi ni kwamba Ibrahim aliamua kutumia uongo huo ili akubaliane naye na kukaa na mtoto huyo.

Alikaa mpaka baada ya saa kadhaa ndipo Ibrahim akarudi chumbani hapo na kuanza kuzungumza naye. Hakuonekana kuwa sawa, alikuwa amechanganyikiwa, hali aliyokuwa nayo mpenzi wake hospitalini ilimchanganya kupita kawaida.
Picha ya mpenzi wake alipokuwa kitandani ilipomjia kichwani mwake moyo wake ulimuuma kupita kawaida.

Hakuamini kama kitendo cha kuwa na Malaika kingemfanya kuishi maisha ya machungu, yenye maumivu makali kama aliyokuwa akiishi.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 118...

Alimwambia Juma kilichokuwa kikiendelea hospitalini, Malaika hakuonyesha dalili zozote za kupona, kila alipokuwa akizungumza, ilionekana kabisa alikuwa akienda kufa japokuwa yeye mwenyewe alisema kwamba Mungu angemponya ugonjwa ule, kuumwa kwake kusingekuwa mwisho wa maisha yake.
“Kwa hiyo vipi kuhusu huyu mtoto?” aliuliza Juma.

“Sijajua! Ninataka akae hapa kidogo kabla ya kwenda kumwambia baba yake,” alisema Ibrahim huku akimchukua mtoto yule.
“Akae hapa?”
“Ndiyo! Kwa siku kama mbili hivi!”
Juma alikataa katakata kubaki na mtoto huyo. Alikuwa msumbufu, kwa saa kadhaa alizokuwa naye tu ilikuwa balaa, alikuwa akilia muda wote kiasi kwamba mpaka mwenyewe akaona kero.

Ibrahim hakuwa na jinsi, ilipofika usiku, akamchukua mtoto huyo na kwenda naye nyumbani kwake. Huko, akamnunulia maziwa, akamnunulia pempasi na kuanza kumuhudumia kwa kila kitu.

Moyo wake ulimuuma mno, hakuamini kama mtoto mzuri kama alivyokuwa huyo alikuwa akiuzwa kwa mtu mwingine. Hakutaka kuona hilo likitokea na ndiyo maana aliamua kumchukua na kuondoka naye.

Usiku hakulala kwa raha, muda mwingi mtoto huyo alikuwa akiamka na kuanza kulia. Alichokuwa akikifanya Ibrahim ni kumpa maziwa pasipo kujua kama alikuwa akisikia njaa au kulikuwa na kitu kingine.
Ni kama alikesha, ilipofika asubuhi, akamuita mpangaji mwenzake, mama Issa na kumwambia kuhusu suala la kumuacha mtoto huyo kwake mpaka pale atakaporudi na kumchukua tena.

“Ni mtoto wa nani?”
“We acha tu!”
“Niambie ukweli kwanza!” alisema mama Issa.
“Ukweli ni kwamba kuna msichana nilizaa naye ndiyo kaja kumtelekeza kwangu,” alisema Ibrahim, hakutaka kumwambia ukweli kwani kama angethubutu kufanya hivyo basi stori zingeenea na hatimaye kuanza kutafutwa yeye.

Mama Issa alimwangalia Ibrahim, alimshangaa, angewezaje kutembea na msichana mwingine na wakati ndani alikuwa na Malaika. Moyo wake ulimuuma mno, aliyaamini maneno yote aliyoambiwa na Ibrahim, ila hakuwa na jinsi, kishingo upande akamchukua.

“Ila Malaika akirudi siyo unihusishe katika mambo yako,” alisema mama Issa.
“Wala usijali! Sitomwambia chochote kuhusu wewe.”

Itaendelea.
 
SEHEMU 119...

Akaondoka na kwenda hospitalini. Njiani alikuwa na mawazo tele, alitaka kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja. Hakuacha kumuomba Mungu amponye msichana wake aliyekuwa hoi hospitalini.
Hakuchukua dakika nyingi akafika hospitalini hapo na moja kwa moja kuelekea katika chumba alichokuwemo Malaika.

Kama alivyokuwa jana ndivyo alivyokuwa siku hiyo, alikuwa hoi na alionekana kama mfu kitandani pale.
Dripu za damu zilikuwa zikipishana tu, ilipotoka hii, ilitundikwa hii. Madaktari walikata tamaa, walijua kabisa kwamba msichana huyo alikuwa akienda kufa ndani ya siku chache zijazo lakini hawakutaka kumwambia Ibrahim kwa kujua kwamba angeumia sana.

Siku hiyo alizungumza naye kwa shida, msichana huyo alizidi kumwambia kwamba asiwe na hofu juu ya afya yake kwani aliamini kwamba Mungu wa Mbinguni angeweza kumponya ugonjwa aliokuwa akiumwa.
“Nitapona tu! Sitokufa mpenzi! Nitapona tu,” alisema Malaika huku akimwangalia mpenzi wake.

Ibrahim akaondoka hospitalini hapo, hakutaka kumwambia kitu chochote kuhusu mtoto aliyekuwa amemuiba hospitalini hapo. Alipofika nyumbani, akamchukua mtoto yule na kukaa naye chumbani kwake. Hayo ndiyo yakawa maisha yake ya kila siku, mpaka wiki inakatika bado alikuwa na mtoto huyo kitu kilichompa wakati mgumu.

“Ni lazima niwatafute wazazi wake, siwezi kuwa na huyu mtoto kila siku,” alisema Ibrahim, watu wa kwanza kabisa kuwasiliana nao walikuwa polisi, kile kituo ambacho Richard alikwenda kwa ajili ya kutoa taarifa.

Hakutaka kuchelewa, siku hiyohiyo akaondoka mpaka katika Kituo cha Polisi cha Osterbay, alipofika, akawaambia polisi kwamba alitaka kumfahamu mwanaume yule aliyekwenda pale wiki mbili zilizopita kuhusu kuibiwa mtoto hospitalini.

“Wewe wa nini?” aliuliza polisi mmoja.
“Ninataka kuzungumza naye!”
“Unaye mtoto?”
“Hapana! Ila ninataka kumsaidia!”
“Kumsaidiaje?”

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 120...

“Mimi ni mganga wa kienyeji kutoka Sumbawanga. Nilisoma kwenye gazeti kuhusu tukio hilo. Ninataka nimfanyie dawa na ndani ya wiki moja tu atafanikiwa kumpata mtoto wake,” alidanganya Ibrahim, polisi wale wakamwangalia kijana huyo, kwa jinsi alivyokuwa akionekana, hata aliposema kwamba alikuwa mganga, hakukuwa na aliyebisha kwani hakuwa msafi sana, fukara ambaye alihitaji msaada.

“Mmh!”
“Mkuu! Najua unaweza ukawa huamini kabisa kuhusu uwezo wangu, ila unaweza kuniruhusu nikakufuata usiku twende sehemu ili uniamini. Ikifika asubuhi tu utakubaliana na mimi,” alisema Ibrahim huku akimwangalia polisi huyo.
“Unichukue mimi?”

“Ndiyo! Nikupeleke baharini uone mambo yanayotokea huko usiku,” alijibu Ibrahim.
“Wewe kijana acha masihara. Hebu kaa hapo niwasiliane naye,” alisema polisi huyo, Ibrahim akakaa kwenye benchi, polisi yule akapekua faili ambapo baada ya kuona jina la Richard, akampigia simu kwa lengo la kuzungumza naye kuhusu ‘mganga’ yule aliyefika kituoni hapo.

**** Moyo wa Richard uliuma, alihuzunika usiku na mchana, japokuwa kwa kutumia pesa zake aliwafunga wauguzi wale lakini hakuridhika hata kidogo. Kuwa na mtoto mmoja haikuwa mipango ya Mungu, yeye alipanga wawe na watoto wawili lakini kutokana na ukatili wa binadamu, wakajikuta wakiwa na mtoto mmoja.

Aliogopa hata kumwangalia mkewe, muda wote Bianca alikuwa mtu wa kulia na kuhuzunika, hakuwa na furaha hata kidogo na muda mwingi alikuwa akijifungia chumbani na mtoto wake akilia.

Siku zikaendelea kukatika, moyo wake uliendelea kuumia zaidi, kila siku alikuwa mtu wa mawazo na wakati mwingine hata kwenda kazini alishindwa kabisa kwani alihitaji kubaki nyumbani na kumfariji mke wake.

“Mtoto wetu hayupo mikononi mwetu, yupo sehemu anaishi! Kwa nini Mungu ameamua kutuadhibu namna hii?” aliuliza Bianca huku akilia.

“Usilie mke wangu! Kuna siku mtoto wetu atapatikana tu!” alisema Richard huku akimwangalia mke wake aliyembeba pacha wake mmoja.
“Ni wiki sasa imepita!”

Itaendelea.
 
Yep alinishangaza alipo sema upo na hapo tulipo swahiba zako wote walikwepo.

Nakupongeza kwa kujitoa kwa ajili yetu.
Aliniambia aliniita notification za tag huwa sipati mm kabisa
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom