Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,400
Reaction score
465,165
01

“Jamani leo natangaza rasmi….” alisikika jamaa mmoja akiwaambia wenzake.
“Tangaza…” wenzake walisema huku wakicheka.

“Kuanzia leo kwa hapa chuo, hakuna demu mkali kama yule Msukuma…” alisema jamaa huyo.
“Msukuma gani?” aliuliza jamaa mmoja huku akimwangalia mwenzake huyo aliyeamua kutangaza.
“Sarafina Butati! Yaani hakunaga!”
“Hahaha!” watu wote wakajikuta wakicheka.

“Jamani yule mtoto mkali! Jamani yule mtoto anaita! Jamani yule mtoto ana figa! Jamani! Jamani! Jamani! Nasema hivi! Kwa hapa chuo hakuna demu mkali kama Sarafina,” alisema jamaa huyo.
“Anamshinda Manka wa Kichaga?” aliuliza jamaa mwingine.

“Manka! Hivi yule demu anaingia kwa Sarafina? Hivi ushawahi kuvuta picha kichwani mwako ukamuona Sarafina akiwa mtupu? Yule mtoto jamani ni mkali sana, kuna kila haki ya sisi marijali kumpigia misele,” alisema jamaa huyo na wote kuanza kucheka.

Huyo ndiye msichana aliyekuwa gumzo katika Chuo cha Amazon kilichokuwa Temeke jijini Dar es Salaam. Kila mwanaume aliyekuwa katika chuo hicho cha ufundi alivutiwa na msichana huyo, uzuri wake uliwapagawisha wanaume wengi kiasi kwamba kila mmoja alimtolea macho.

Sarafina alikuwa msichana mrefu, mwenye mwendo wa maringo, alikuwa na hipsi pana ambazo kwa watoto wa mjini walipenda kuziita pisto, alikuwa na miguu iliyojazia kidogo huku akiwa na mapaja manene kiasi kwamba kila alipoyaruhusu yaonekane, kila mwanaume aliyamezea mate.

Usoni hakuwa wa kawaida, alikuwa na sura nyembamba, mdomo wake ulikuwa na lipsi pana, hata kama macho yake alikuwa akiyakaza, bado yalionekana kusinzia kwa mbali mithili ya mwanamke aliyekula kungu.

Mashavuni mwake alikuwa na vishimo viwili ambavyo viliufanya uzuri wake kuonekana kila alipokuwa akicheka hata kutabasamu. Hakuwa msichana wa kusuka, muda mwingi nywele zake alikuwa akizikata huku sura yake hiyo akiipendezesha na miwani meusi.
Sarafina hakujua kutembea kwa kasi, kila alipokuwa akitembea, alitembea kwa mwendo wa maringo kana kwamba hakuwa akikanyaga ardhi hiihii.

Aliwadatisha wanaume wote waliokuwa chuoni hapo, kila mmoja alimpenda, kila mmoja alitamani hata siku moja msichana huyo mrembo awe mpenzi wake.

Itaendelea
 
Sehemu ya 02

Sauti yake ilikuwa nyororo, kipindi cha kwanza wanaume wengi walihisi kwamba msichana huyo alikuwa akifanya kusudi lakini baada ya kumzoea wakagundua kwamba hiyo ilikuwa ndiyo sauti yake ya kila siku, sauti ya kumtoa nyoka pangoni, sauti iliyowadatisha hata wanaume waliokuwa mbali waisikiapo kutaka kumuona msichana huyo aliyeitoa sauti hiyo.

Sarafina alikuwa na sifa ya kuwa msichana mrembo, hakuonekana kuwa na kasoro, kila alipopita, alikuwa gumzo, wanaume walimsifia kwa kuwa alikuwa na mvuto wa ajabu.

Japokuwa alikuwa mzuri na wa kuvutia sana lakini Sarafina hakuwa mtu wa maringo, alipenda kuzungumza na kila mtu, wanaume wengi wakatumia nafasi hiyohiyo kumtongoza lakini msichana huyo hakuwa mwepesi kuingilika kama wasichana wengine, hakuwa msichana mwepesi hata kidogo.

Wanaume waliteseka, walihangaika, ikafika kipindi wakahisi kwamba inawezekana msichana huyo alipenda mwanaume aliyekuwa na gari, waliokuwa na magari wakamfuata kwa lengo la kumuingiza katika mitego yao lakini hawakufanikiwa.

Wengine wakahisi kwamba msichana huyo alihitaji pesa, wanaume wakajipanga vilivyo, wakamfuata huku mifuko ikiwa imejaa lakini msichana huyo hakuingilika, hakuwakubalia, kwake, hakujali pesa wala magari.

Wanaume hawakuchoka, kila mmoja alikuwa na uhakika wa kumpata msichana huyo kama tu wangeweza kuweka nguvu zao katika ufuatiliaji.

Kitu walichokifanya ni kuanza kumtumia zawadi mbalimbali msichana huyo.
Hilo halikutosha, halikubadilisha moyo wake, aliendelea kuwa na msimamo uleule kwamba hakutaka kuingia kwenye uhusiano na mwanaume yeyote yule, kitu alichokuwa akikitaka ni kusoma na kufikia malengo yake.

Alikwenda Dar es Salaam kwa ajili ya kusoma chuo. Hakuzaliwa katika familia yenye uwezo mkubwa sana jijini Mwanza, ilikuwa familia ya kawaida iliyokuwa na maisha ya kawaida sana ambayo ilikuwa ikiishi katika mtaa wa kimasikini, mtaa choka mbaya wa Mabatini hapohapo Mwanza.

Alipomaliza kusoma katika Shule ya Sekondari ya Mwanza, wazazi wake wakakopa pesa katika kikoba cha Saccos moja kwa ajili ya Sarafina na kuelekea jijini Dar es Salaam kusoma, walipopewa, wakamlipia ada ya mwaka mzima na kumpa fedha nyingine kwa ajili ya maisha yake huko.
 
Sehemu ya 03

Sarafina alipofika chuoni, alionekana kuwa msichana wa kawaida, hakuonekana kama alikuwa na mvuto lakini baada ya kukaa kwa miezi sita, wanaume wakaona utofauti, uzuri wake wa asili ukaanza kuonekana.

Mpaka kipindi hicho, Sarafina hakuwahi kumjua mwanaume, alikuwa msichana bikira ambaye alijiapiza kwamba mwanaume wa kwanza ambaye angempa nafasi ya kuutoa usichana wake ndiye ambaye angekuwa mume wake.

Alijitunza, kila siku aliwakatalia wanaume, japokuwa alifuatwa sana lakini hakuchoka kuwakataa wanaume, kwake, bado ndoto yake ya kuolewa akiwa bikira iliendelea kuishi moyoni mwake, hakuwapenda wanaume wenye magari, hakuwapenda wanaume wenye pesa, alichokuwa akikihitaji ni kumpata mwanaume mwenye uwezo wa kawaida ambaye angemuonyeshea mapenzi ya dhati, mwanaume ambaye angemwambia ‘Nakupenda’ kila siku asubuhi na usiku.

“Sara! Unajua wewe ni mzuri sana!” alisema mwanaume mmoja, aliamua kumfuata Sarafina kama walivyokuwa wenzake.
“Umekwishaniambia sana Jumanne!”
“Nimetokea kukupenda bure!”
“Kwani wote wanaonipenda wananipenda na hela?” aliuliza Sarafina huku akitoa tabasamu lililompa matumaini mengi Jumanne.

“Hahah! Sarafina! U mzuri sana, hebu angalia jinsi unavyotabasamu, dimpozi zako zinaniua kishenzi, hakika nimeona wanawake wengi warembo lakini kwako! Haki ya Mungu hakuna kama wewe,” alisema Jumanne huku akitoa tabasamu ambalo aliamini kwamba lingemchanya msichana huyo.

“Nashukuru! Naomba niondoke.”
“Kwa hiyo?”
“Kuhusu nini? Si umeniita, nimekuja, umenisifia, nimekubali!”
“Ila sijamaliza.”
“Basi malizia!”
“Nakupenda.”

“Nashukuru! Kingine?”
“Ningependa uwe mpenzi wangu!”
“Haiwezekani Jumanne.”
“Sarafina, pamoja na tabasamu lako lote bado unanikataa?”

“Kwani tabasamu ndiyo kupendwa? Si kila tabasamu ni la furaha Jumanne. Mwingine anatabasamu lakini moyo wake unawaka moto. Naomba unielewe, sihitaji kuwa na mwanaume yeyote yule,” alisema Sarafina, tayari alisimama pale alipokuwa, hakutaka kuongea tena, huyo akaondoka zake.
 
Sehemu ya 4

Jumanne alibaki akiwa amekaa kitini, hakuamini kama kweli alimkataa, alikwishajigamba kwa wenzake kwamba angempata Sarafina kwa gharama zozote zile, waliwekeana dau lakini mwisho wa siku msichana huyo alimkataa huku akimtolea tabasamu pana.

Moyo wake uliuma, ulichoma mno, hakutaka kukubali, aliendelea kumfuatilia msichana huyo lakini hakukuwa na kilichobadilika, kama ulivyokuwa msimamo wake kipindi cha nyuma ndiyo ukawa uleule kwamba hakutaka kuwa na mwanaume yeyote yule.

“Nitaendelea kuwa bikira mpaka nitakapoolewa. Mwanaume wangu wa kwanza kumvulia nguo atakuwa mume wangu,” alisema Sarafina huku akiwa kitandani. Usingizi ukampitia.
**** Miongoni mwa wanaume waliokuwa wakimpenda Sarafina alikuwa kijana Richard Lema. Huyu hakumpenda msichana huyo kipindi hicho tangu siku ya kwanza alipokanyaga katika chuo hicho alitokea kumpenda kwani kila alipomwangalia, aliuona uzuri wa msichana huyo japokuwa hakuwa amelizoea jiji.

Richard alikuwa miongoni mwa watoto wa matajiri wakubwa jijini Dar es Salaam, alikwenda kusoma katika chuo hicho kwa sababu tu hakutaka kuishi maisha ya kifahari, siku zote alijihesabia kuwa mtu wa kawaida, kijana aliyetoka katika familia nyingine ya kimasikini.

Hakukuwa na mtu aliyejua maisha halisi yake, kila siku chuoni hapo alikuwa akienda kwa daladala, alikuwa na gari la kifahari nyumbani kwao lakini hakutaka mtu yeyote afahamu kama alikuwa mtoto wa kitajiri na hata marafiki zake walipotaka kumtembelea, aliwaita katika chumba alichopanga uswahilini Tandale.
Kila siku alipokuwa akimwangalia
Sarafina, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda mno, alimpenda msichana huyo, alitamani sana kumfuata na kumwambia ukweli kwamba alikuwa akimpenda kwa moyo wote lakini aliogopa, hakujiamini, hakuwahi kuzungumza na msichana yeyote yule.

Hata uzuri wa msichana huyo ulipoanza kuonekana, bado alikuwa kwenye mapenzi ya dhati, alimpenda sana lakini kumfuata na kumwambia ukweli wa moyo wake lilikuwa jambo gumu sana kufanyika, aliendelea kuumia kila siku, aliendelea kuteseka lakini kufumbua mdomo wake na kumwambia msichana huyo ukweli, hakuthubutu kabisa.
 
Sehemu ya 5

“Nitamwambia tu! Lakini lini? Mbona nateseka tu kila siku?” alijiuliza lakini akakosa jibu kabisa.
Siku zikaendelea kukatika, idadi ya wanaume waliokuwa wakimpenda msichana huyo ikaongezeka, Richard alichukia, aliumia, alitamani kuwasimamisha wanaume wote kwa kuwaambia wasimfuate msichana huyo lakini ilishindikana, kila siku idadi ya wanaume hao iliendelea kuongezeka zaidi
.
Baada ya kukaa kwa mwaka mzima chuoni ndipo alipoamua kujipanga, akatafuta siku maalumu ya kumwambia msichana huyo ukweli, hakutaka kuvumilia, kama kulikuwa na watu wanakataliwa, basi hata naye alitakiwa kujaribu bahati yake na kama ingetokea kukataliwa, isingekuwa mara ya kwanza.

“Ila ninaogopa! Mungu! Naomba unitie ujasiri,” alisema Richard, siku hiyo ilipofika, akaamua kumfuata msichana huyo.

*** Richard hakutaka kuvumilia, hakuwa radhi kuuona moyo wake ukiteseka na wakati mtu ambaye angempa pumziko alikuwepo katika dunia hii. Hakutaka kusubiri, aliogopa kuchoka na hivyo akapanga siku ya kumfuata Sarafina kwa ajili ya kumwambia ukweli jinsi moyo wake ulivyojisikia.

Alijipanga sana, muda wa kutoka darasani, akaanza kujivutavuta kwa ajili ya kuzungumza na Sarafina. Hakuwa na nafasi, wakati yeye akitaka kumsogelea msichana huyo mrembo na kumwambia ukweli, tayari wanaume wawili walimuwahi na kuanza kuzungumza na msichana huyo.

Moyo wake uliumia mno, siku hiyo aliitenga kwa ajili ya msichana huyo, hakuamini kama ingeshindikana kabisa kuzungumza naye. Akavumilia, akasubiri wale wamalize kuongea naye lakini cha ajabu wanaume hao walimng’ang’ania kama ruba.

Mpaka inafika saa kumi na moja alipokuwa akiondoka, wanaume hao wakaondoka naye. Alikasirika sana lakini hakuwa na jinsi, akaondoka mpaka nyumbani kwao, akaingia chumbani na kuwa na kujilaza kitandani.

Alikuwa mtoto wa bilionea mkubwa ambaye alitokea kumpenda msichana Sarafina. Utajiri mkubwa aliokuwa nao baba yake ulionyesha dhahiri kwamba hakuwa na hadhi ya kuwa na msichana kama Sarafina, alitakiwa kuwa na msichana aliyekuwa na hadhi kubwa, msichana ambaye kwenda Marekani, Italia ilikuwa ni sawa na kwenda Kariakoo.
 
SEHEMU YA 6:....

Hakutaka kujali hilo, alipomfuata, utajiri wake aliuweka pembeni, aliyatanguliza mapenzi kwani aliamini kwamba pesa zisingeweza kununua mapenzi, hata kama angekuwa na pesa kiasi gani angeishia kununua ngono na si upendo.

“Kwa nini inakuwa hivi? Wale ni wakina nani? Kwa nini wanamng’ang’ania sana?” alijiuliza Richard pasipo kupata jibu.
Wivu mkali ukaukamata moyo wake, huo haukuwa mwisho, ulikuwa ni kama mwanzo wa harakati zake, aliendelea kumfuatilia lakini wanaume walewale hawakutaka kumuacha, kila siku walikuwa naye, walizungumza naye sana mpaka akawa anakasirika.

“Hawa ni wakina nani?” alijiuliza.
Hapo ndipo alipoanza kufuatilia, alitaka kuwajua wanaume wale walikuwa wakina nani na walihitaji nini kwa Sarafina. Kwenye kufuatilia kwake akagundua kwamba wanaume hao walikuwa marafiki wakubwa, mmoja aliitwa David Kimario, mwanaume aliyekuwa akitingisha kwa kuzifunua sketi za wanawake na mwingine alikuwa Paschal Malengo ambaye huyo alikuwa muonganishaji mkubwa aliyekuwa akitumiwa na David.

Japokuwa David alikuwa bingwa wa kutembea na wasichana wengi lakini kwa Sarafina alifua dafu, alijitahidi sana kumtongoza lakini alimkatalia kumtumia Paschal ambaye alijua sana kucheza na akili za wasichana.

Kitendo cha kuwa na Sarafina kila siku, Paschal alijitahidi kumuweka sawa, alijitahidi kuulainisha moyo wa msichana huyo ukubaliane na David ambaye alikufa na kuoza moyoni mwake.
“Kumbe! Kwa staili hii sitoweza kuongea naye, ngoja nitafute namba yake ya simu,” aliwaza.

Hilo ndilo alilolifanya, akaitafuta namba ya msichana huyo. Kuipata haikuwa kazi kubwa, watu wengi walikuwa nayo, alipoipata tu, akatafuta siku na kumpigia simu kwa lengo la kuonana naye.
“Wewe nani?” aliuliza Sarafina.
“Richard!”
“Okey! Nikusaidie nini Rich?” aliuliza Sarafina.
“Ningependa nionane na wewe!”
“Ili?”
“Nizungumze na wewe!”
“Kuhusu?”
“Stori tu!”
“Samahani! Sina muda kaka yangu!”
“Saraf….”

“Naomba unielewe! Sina muda!” alisema Sarafina na kisha kukata simu.
Moyo wa Richard ukauma vilivyo, akanyong’onyea, akajilaza kitandani na kuanza kumfikiria msichana huyo.
Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 7....

Moyo wa Richard ukauma vilivyo, akanyong’onyea, akajilaza kitandani na kuanza kumfikiria msichana huyo. Alijua kwamba alikuwa na muda wa kutosha wa kuonana naye lakini hakutaka kwa kuwa hakumfahamu, hakujua ni kwa jinsi gani alikuwa akimpenda.

Hakutaka kukubali, kwa kuwa alimpigia simu, alichokifanya ni kumtumia meseji. Ilikuwa vigumu sana kujibiwa, alipofikisha meseji ya ishirini ndipo akatumiwa meseji fupi tu iliyosomeka ‘Nalala’.

“Uwe na usiku mwema!” alimalizia kwa kumtumia na msichana huyo hakujibu kitu chochote kile.
Kwa jinsi mapenzi yalivyouendesha moyo wake, usiku mzima alibaki akiiangalia meseji ile ya ‘Nalala’ aliyoandikiwa na msichana yule. Moyo wake ulifarijika, hakuumia kwa kumtumia meseji ishirini na zote hazikujibiwa, kitendo cha kuambiwa meseji moja iliyomaanisha kwamba hakutakiwa kutuma meseji yoyote, moyoni mwake akaridhika.

Hakukoma, hata siku iliyofuata aliendelea kumtumia meseji lakini hakuwa akijibu mpaka alipotumiwa meseji nyingi mno. Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake na baada ya wiki mbili, ili kuepuka usumbufu, Sarafina akakubaliana na Richard na kuonana naye.

“Tuonane wapi?” aliuliza Sarafina.
“Nakusikiliza wewe tu! Ila mimi naishi Tandale, sasa unaweza kuangalia sehemu rahisi ya mimi na wewe kuonana,” alisema Richard.

“Kule Tandale kwa vibaka?”
“Ndiyo hukohuko, mabonde kuinama kulipojaa roba za mbao!” alijibu Richard.
“Mmh!”
“Ungependa tuonane wapi?”
“Serena hotel”
“Mmh!”
“Mbona unaguna!”

“Nitaweza kugharamia jamani! Kule maji si yatakuwa shilingi elfu kumi! Nitaweza kweli?” aliuliza Richard, wakati huo walikuwa wakizungumza.
“Sasa wewe unamfuata msichana mzuri halafu huna hela?”

“Basi sawa. Sipendi kuacha kuonana na wewe! Nitajitahidi nifike huko,” alisema Richard na hivyo kupanga kuonana siku hiyo saa kumi na moja jioni.

Saa tisa na nusu tayari Richard alikuwa mahali hapo, alivalia simpo, kama kawaida yake hakutaka kwenda na gari lake la kifahari, alichukua daladala ambayo ilimshusha Akiba na kuchukua Bajaj iliyompeleka mpaka katika Hoteli ya Serena na kuingia ndani, sehemu ya mgahawa na kuagiza soda.
“Nimekwishafika!” alisema Richard.
 
SEHEMU YA 8...

“Nimekwishafika!” alisema Richard.
“Sawa. Niandalie chakula. Mbuzi wa kuchoma, chipsi na soseji nne!” alisikika Sarafina.
“Mmh!”
“Mbona unaguna! Au niahirishe?”
“Hapana! Wewe njoo!”

Kwa kipindi kichache tu Sarafina alivyoanza kuzoeana na kina David alibadilika. Maneno matamu aliyokuwa akiambiwa na Paschal kuhusu David yalimteka. Moyo wake ukabadilika, matumizi makubwa waliyokuwa wakitumia wanaume hao pamoja naye akaona kwamba kila mwanaume aliyekuwa akija mbele yake ilimbidi kuwa na fedha za kutosha.

Alikumbuka kwamba alitoka kwenye familia iliyokuwa na umasikini mkubwa, kitendo cha David kuwa radhi kutoa kiasi chochote cha fedha kuhakikisha anampata kikamlevya Sarafina na kugundua kwamba pesa ilikuwa kila kitu katika maisha yake.

Hakuwahi kumuona Richard, hakuwa akimpenda ila alichokuwa akikitaka ni kutumia pesa zake tu. Alijua kwamba hakuwa na fedha kwa sababu hata mtaa aliokuwa akiishi ulikuwa ni walala hoi hivyo alimwambia vitu ambavyo aliamini kwamba asingeweza kuvitimiza hata mara moja.

Baada ya dakika kadhaa, Sarafina akafika mahali hapo. Richard alipomuona akiingia, hakutaka kubaki kitini, kwa heshima akasimama na kumkaribisha msichana huyo ambaye akatulia kitini. Kabla ya kufanya kitu chochote kile, Richard akamuita dada wa chakula na kumwambia kuhusu ile oda aliyokuwa ameiweka, mwenyewe alikuwa amefika.
“Karibuni sana,” alisema dada wa chakula huku akiweka chakula mezani.

“Ahsante sana,” alisema Richard huku akiwa na maji tu, akajifanya kutokuwa na fedha kabisa.
Richard alibaki akimwangalia Sarafina. Kwa jinsi alivyokuwa akionekana siku hiyo, alionekana kuwa tofauti na Sarafina aliyekuwa akimfahamu. Alibadilika, muonekano wake ulikuwa ni wa tofauti sana.

Kichwani alikuwa na mtindo mpya wa nywele, alizinyoa nywele zake kwa mtindo wa kiduku kwa mbali huku akiwa amezipaka blichi iliyomfanya kuonekana tofauti kabisa huku puani akiwa na kipini kilichosindikizwa na tattoo iliyokuwa kifuani mwake, pembeni kidogo ya titi lake. Japokuwa alikuwa na mabadiliko makubwa mwilini mwake lakini Richard hakuacha kumpenda msichana huyo, kwake, bado aliendelea kuwa namba moja moyoni mwake.
“Sarafina!” alimuita.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 9...

“Niambie! Umesema unaitwa nani vile?”
“Richard!”
“Ooh! Okey! Niambie Richard!”
Richard akavuta pumzi ndefu, akamwangalia msichana huyo, akashusha pumzi, kilichomuuma ni kwamba Sarafina hakulifahamu jina lake, alijiona kupuuzwa sana, alijiona kutokujaliwa na msichana huyo na ndiyo maana alisahauliwa jina lake japokuwa alikuwa akiwasiliana naye sana tu.

Richard hakutaka kujificha, aliteseka kwa kipindi kirefu moyoni mwake hivyo kumwambia jinsi alivyokuwa akimpenda. Sarafina alibaki kimya, alikuwa akimwangalia Richard na kumsikiliza kila neno alilokuwa akizungumza.

Kwa muonekano wake, mwanaume huyo alionekana kumpenda sana lakini kitu kilichompa wakati mgumu Sarafina ni kwamba hakuwa mwanaume wa ndoto yake, alitoka kwenye familia ya kimasikini, alitakiwa kuitoa familia yake kutoka pale ilipokuwa, kitendo cha kuwa na mwanaume masikini kama Richard kilimaanisha kwamba angeyafanya maisha yake kuwa vilevile.

“Unanipenda mimi?” aliuliza Sarafina.
“Ndiyo! Ninakupenda sana kutoka moyoni mwangu!” alijibu Richard huku akimwangalia kwa jicho lililomaanisha upendo mkubwa aliokuwa nao moyoni mwake.

“Daah!”
“Kuna nini tena?”
“Umechelewa!”
“Najua kwamba msichana mrembo kama wewe huwezi kuwa singo! Ila naomba unifikirie! Sarafina, ninakupenda, wewe ni msichana unayeufanya moyo wangu kutetemeka, ni msichana ambaye naamini nikiwa na wewe nitakuwa na furaha, amani moyoni mwangu,” alisema Richard huku akimwangalia Sarafina.

“Siwezi kuwa na wewe!”
“Kwa nini?”
“Richard! Mimi si hadhi yako! Samahani! Sikudharau ila ni bora nikwambie ukweli, halafu mbali na hilo, nina mpenzi!” aljibu Sarafina.
“Una mpenzi?”
“Ndiyo! Anaitwa David! Yule mwanaume ninayekuwa naye sana chuoni,” alisema Sarafina.

Hakukuwa na kitu kilichowahi kuuchoma moyo wake kama kuyasikia maneno hayo. Alihisi kitu kama msumari wa moto ukiuchoma moyo wake vilivyo. Akayafumba macho yake, akakiinamisha kichwa chake chini, alipokiinua, machozi yakaanza kujikusanya machoni mwake.
“Sarafina! Ninakupenda kupita kawaida, ninaomba niwe nawe. Nimepoteza muda wangu kwa ajili yako, nimekuwa nikikufikiria sana.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 10....

“Sarafina! Ninakupenda kupita kawaida, ninaomba niwe nawe. Nimepoteza muda wangu kwa ajili yako, nimekuwa nikikufikiria sana. Sarafina, ninakupenda, ninakupenda zaidi ya unavyofikiria, ninakupenda zaidi ya David anavyokupenda, ninakupenda kuliko mwanamke yeyote chini ya jua,” alisema Richard huku kwa mbali machozi yakianza kutoka.

“Haiwezekani Richard. Ahsante sana kwa chakula,” alisema Sarafina, hakutaka kubaki mahali hapo, akasimama na kuanza kuondoka huku akiwa hajui ni kwa jinsi gani mwanaume huyo alikuwa akimpenda moyoni mwake.

Alipoondoka, Sarafina hakuangalia nyuma, Richard alibaki mezani pale huku akiwa amechoka na kuumia vilivyo. Alimwangalia Sarafina alivyokuwa akiondoka, hata kuondoka mahali hapo akashindwa na hivyo kuchukua chumba katika hoteli hiyo na kulala siku hiyo.
Usingizi ulikuwa mzito, kichwa chake kilivurugika, alichanganyikiwa kupita kawaida. Kila alipofumba macho, taswira ya msichana huyo ilimjia kichwani mwake kitu kilichomfanya kuwa kwenye hali mbaya kupita kawaida. “Sarafina!

Nitakupata tu! Siwezi kuacha kukwambia kwamba nakupenda. Nitakupata tu,” alisema Richard na kutulia katikati ya kitanda, usingizi haukuja, usiku mzima alikesha kama popo akimfikiria Sarafina.
**** Sarafina hakuwa na habari na Richard, kwake, mwanaume huyo alionekana kuwa mtu wa kawaida, asiyejiweza ambaye hakuwa na uhakika kama angeweza kumnunulia hata wigi la Kibrazil. Hakutaka kuwa naye, umasikini wa nyumbani kwao ulikitesa kichwa chake na hakukuwa na kitu kingine alichokifikiria kama kupata pesa za kuweza kufanya kila kitu.

Alihitaji nguo, vipodozi na vitu vingine vingi kwa ajili ya maisha yake hivyo hakuona kama kulikuwa na sababu ya kuwa na mwanaume ambaye hakuwa na pesa.

Aliendelea kutanua, david hakuwa na hiyana, alimpa Sarafina kila kitu alichokuwa akikihitaji lakini pia naye alipata kila kitu alichokuwa akikihitaji kwa msichana huyo. Mapenzi yakamchanganya Sarafina, hakumfikiri mwanaume yeyote yule, kwake, David alikuwa zaidi ya mtu yeyote yule, kwake, hakukuwa na mwanaume ambaye alikuwa na thamani kubwa kama David.

Je, nini kitaendelea?
 
Uyo nyemo chilongani hizo hadithi za abunuasi zilimfanya akafeligi form 4 haha alitaga afu alikuaga mnoko huyo yani kiherehere ila kwenye judgment day akaishia kutaga nadhani alipata 4 ile ya zero....
Saivi nani ana muda wa kusoma hadithi za abunuasi
 
SEHEMU YA 11...

Chuoni wakajua, watu wengi wakashangaa, sarafina hakutakiwa kuwa na mtu kama David, mwanaume huyo alikuwa mtu wa wanawake, aliwafunua wanawake wengi chuoni hapo, aliwafanya alivyotaka, wanawake wengi walilia kwa ajili yake, wengi walitoa mimba kwa kuwa alikuwa akizikataa, kitendo cha Sarafina kuwa na mwanaume huyo ilionekana kuwa kama marudio ya maisha ya wasichana wengine kwamba naye angepatwa na balaa kama yaliyowapata wanawake wengine.

“Sarafina! Ninakupenda, ninakupenda sana,” alisema David huku akimwangalia msichana huyo machoni.
“Nakupenda pia!”
“Ungependa twende wapi?”
“Maisha Basement! Nimesikia kuna wasanii, Diamond na Ali Kiba watapanda jukwaani kwa pamoja kutambulisha ngoma yao mpya. Jamani! Nawapenda wale mpaka naumwa!” alisema Sarafina huku akimwangalia David.
“Hakuna shida!”

Maisha ya starehe yakamteka msichana huyo, alikwenda huku na kule akila raha, kwake, kila kitu kilionekana kuwa chepesi kwa kuwa tu alikutana na mwanaume aliyekuwa tayari kumpa kiasi kingi cha fedha kwa ajili ya kufanyia mambo yake.
Hakutaka kumfikiria Richard, kila alipokuwa akimuona chuoni hapo, alimuonea huruma, alionekana kuwa mwanaume mwenye maisha duni, mwanaume ambaye alitakiwa kupata zali la mentali kumpata mwanamke mwenye pesa ili ayaendeleze maisha yake, kwake, kwa jinsi alivyomwangalia Richard, alionekana kuwa naye mbalimbali kama mbingu na nchi.

Maisha yaliendelea, kila siku walikuwa watu wa kula raha. Sarafina alibadilika kwa asilimia mia moja, hakuwa yule Sarafina wa zamani, yule mshamba mshamba ambaye hata kufika Mlimani City aliogopa.

Alikuwa na bwana mwenye pesa kidogo ambaye aliyafanya maisha yake kuwa na mteremko. Hakuwa akiingia sana darasani kama kawaida, muda mwingi alikuwa akilala kwani kwa nyakati za usiku alikuwa akitoka sana na kwenda klabu.

Baada ya miezi miwili ya starehe Sarafina akaanza kuona mabadiliko, yale mapenzi aliyokuwa akiyaonyesha David yalionekana kupungua. Hakuwa mtu wa kumpigia simu kama ilivyokuwa zamani, hakuwa mtu wa kumtumia meseji kama kipindi kilichopita.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 12...

Yeye ndiye alikuwa mtumaji wa meseji na mpigaji simu. Hilo lilimuumiza kwa kuwa alikuwa akimpenda mwanaume huyo, hakutaka kumuacha, mabadiliko hayo yaliufanya moyo wake kusikia maumivu makubwa mno.

Akatafuta muda wa kukaa na David kwa lengo la kuzungumza naye lakini kila walipokutana, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa kufanya ngono. Maisha hayo yakamtawala, akawa mtumwa wa ngono kwa David kiasi kwamba hakupata muda wa kumuuliza kuhusu uhusiano wao kuanza kuyumba.

“Tatizo nini David?” aliuliza Sarafina.
“Kuhusu nini?”
“Umebadilika!”
“Nimekuwaje mpenzi? Mbona nipo kawaida. Halafu leo umetokelezea kweli! Kwa hicho kinguo ulichokivaa! Urembo wako wa asili unaonekana vilivyo,” alisema David, akamtoa Sarafina katika lengo lake. Akabaki anatabaamu.

“Huna tofauti na Jeniffer Lopez aliyokuwa kwenye ubora wake. Hebu njoo kitandani kwanza,” alisema David, hapohapo akamuinua Sarafika kutoka kwenye kochi lililokuwa chumbani kwake na kumuweka kitandani, kilichofuata ni kushikana hapa na pale, kuvuana nguo na ndani ya dakika kumi, kitanda kikaanza kulalamika.

Miezi mingine miwili baadaye, Sarafina akaanza kujihisi tofauti mwilini mwake, akaanza kusikia uchovu huku muda mwingi akitamani kulala. Hakujua ni kitu gani kiliendelea lakini hali aliyokuwa nayo alipowaambia marafiki zake, hawakumficha, wakamwambia kwamba inawezekana ikawa mimba.

Akashtuka, hakutegemea kusikia kitu kama hicho, aliogopa, japokuwa alikuwa akilala sana na David lakini hakutarajia kama ingetokea siku moja angepata mimba, aliogopa, kila alipowakumbuka wazazi wake, jinsi walivyohangaika kutafuta pesa ili asome, akaona kungekuwa na tatizo kubwa.

Hakutaka kusubiri, haraka sana akaelekea hospitalini kwenda kupima. Njiani alikuwa akitetemeka, aliogopa, kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka. Hapo ndipo alipojuta kuwa na David, alijuta kuwa katika uhusiano na mwanaume huyo.

Alipofika hospitalini akakaa kwenye foleni na zamuu yake ilipofika akaingia ndani ambapo akaambiwa apeleke mkojo wake na kufanya hivyo, ulivyopimwa, akagundulika kuwa na mimba ya wiki mbili.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 11...

Chuoni wakajua, watu wengi wakashangaa, sarafina hakutakiwa kuwa na mtu kama David, mwanaume huyo alikuwa mtu wa wanawake, aliwafunua wanawake wengi chuoni hapo, aliwafanya alivyotaka, wanawake wengi walilia kwa ajili yake, wengi walitoa mimba kwa kuwa alikuwa akizikataa, kitendo cha Sarafina kuwa na mwanaume huyo ilionekana kuwa kama marudio ya maisha ya wasichana wengine kwamba naye angepatwa na balaa kama yaliyowapata wanawake wengine.

“Sarafina! Ninakupenda, ninakupenda sana,” alisema David huku akimwangalia msichana huyo machoni.
“Nakupenda pia!”
“Ungependa twende wapi?”
“Maisha Basement! Nimesikia kuna wasanii, Diamond na Ali Kiba watapanda jukwaani kwa pamoja kutambulisha ngoma yao mpya. Jamani! Nawapenda wale mpaka naumwa!” alisema Sarafina huku akimwangalia David.
“Hakuna shida!”

Maisha ya starehe yakamteka msichana huyo, alikwenda huku na kule akila raha, kwake, kila kitu kilionekana kuwa chepesi kwa kuwa tu alikutana na mwanaume aliyekuwa tayari kumpa kiasi kingi cha fedha kwa ajili ya kufanyia mambo yake.
Hakutaka kumfikiria Richard, kila alipokuwa akimuona chuoni hapo, alimuonea huruma, alionekana kuwa mwanaume mwenye maisha duni, mwanaume ambaye alitakiwa kupata zali la mentali kumpata mwanamke mwenye pesa ili ayaendeleze maisha yake, kwake, kwa jinsi alivyomwangalia Richard, alionekana kuwa naye mbalimbali kama mbingu na nchi.

Maisha yaliendelea, kila siku walikuwa watu wa kula raha. Sarafina alibadilika kwa asilimia mia moja, hakuwa yule Sarafina wa zamani, yule mshamba mshamba ambaye hata kufika Mlimani City aliogopa.

Alikuwa na bwana mwenye pesa kidogo ambaye aliyafanya maisha yake kuwa na mteremko. Hakuwa akiingia sana darasani kama kawaida, muda mwingi alikuwa akilala kwani kwa nyakati za usiku alikuwa akitoka sana na kwenda klabu.

Baada ya miezi miwili ya starehe Sarafina akaanza kuona mabadiliko, yale mapenzi aliyokuwa akiyaonyesha David yalionekana kupungua. Hakuwa mtu wa kumpigia simu kama ilivyokuwa zamani, hakuwa mtu wa kumtumia meseji kama kipindi kilichopita.

Je, nini kitaendelea?
Nasubiri kitachoendelea
 
13...

Alipofika hospitalini akakaa kwenye foleni na zamuu yake ilipofika akaingia ndani ambapo akaambiwa apeleke mkojo wake na kufanya hivyo, ulivyopimwa, akagundulika kuwa na mimba ya wiki mbili.

Alilia sana, alihuzunika kupita kawaida. Mbele yake maisha yakaanza kuonekana kuwa na ukungu mkubwa, hakuamini kama mwisho wa kila kitu ungekuwa namna ile.
Hakutaka kukaa kimya, akampigia simu David, mwanaume huyo alipoiona simu hiyo, hakuipokea, alitulia huku akiiiangalia tu. Mapenzi yalitoka moyoni mwake, hakumpenda Sarafina kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma, alikuwa msichana wa starehe, alimuhitaji kipindi ambacho alikuwa na mhemko, kipindi ambacho wasichana wake wote walikuwa bize, ndipo alipopigiwa simu na kumfuata David ambapo huko, akavua nguo zake, akajilaza kitandani na kupanua miguu yake.

“Unasemaje?” lilisikika swali kutoka kwa David mara baada ya kupokea simu.
“Nataka nikuone mpenzi!”
“Kuna ishu gani?”
“Kuna kitu nataka tuzungumze!”
“Kuhusu nini?”
“Tuonane kwanza!”
“Sasa hicho kitu hakina hata intro? Niambie kwanza!” alisema David.
“Nimetoka hospitali!”

“Unaumwa?” Hapo ndipo Sarafina akaanza kumuelezea David kila kitu kilichotokea, jinsi alivyokuwa akijisikia uchovu na kwenda hospitalini na kupima na kugundulika kwamba alikuwa na ujauzito.

“Mimba ya nani sasa?” aliuliza David.
“Yako!”
“Yangu? Eti mimba yangu! Unasema kabisa bila hofu, huogopi kudanganya mtoto wa kike, unajiamini na kusema mimba yangu,” alisema David, hakutaka kuongea sana, hapohapo akakata simu.
“Halo! Halo! Halo mpenzi!” aliita Sarafina lakini upande wa pili hakukusikika sauti tena.

Aliumia moyoni mwake, akalia kupita kawaida, hakuamini kile kilichotokea kwamba David, mwanaume aliyempenda kwa moyo wa dhati alimgeuka baada ya kumwambia kwamba alikuwa mjauzito.
Hapo ndipo alipoiona dunia chungu, hapo ndipo maneno ya wazazi wake walipomwambia kwamba alitakiwa kusoma ndipo yalipoanza kurudi kichwani mwake. Alijuta, kile kilichokuwa kimetokea kwake kilionekana kuwa kama ndoto ambapo baada ya muda angeshtuka na kujikuta akiwa kitandani.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 14...

Alijuta, kile kilichokuwa kimetokea kwake kilionekana kuwa kama ndoto ambapo baada ya muda angeshtuka na kujikuta akiwa kitandani.
Alimpenda David, alimwamini sana na muda mwingi walikuwa wakizungumza juu ya kutengeneza familia pamoja lakini kitu cha ajabu kabisa, alipopata mimba, mwanaume huyo akamwambia kwamba haikuwa yake.

Hakutaka kukubali, akampigia simu David kwa lengo la kumsisitizia kile alichomwambia kwamba kilikuwa ni ukweli lakini simu ya mwanaume huyo haikuwa ikipatikana na alipokuwa akipiga zaidi na zaidi, simu ikaacha kupatikana, kwa maana hiyo ikawa imezimwa.
“David….nini kimetokea? Mbona umebadilika?” aliuliza Sarafina na kuanza kulia.

Hiyo ndiyo siku iliyobadilisha maisha yake yote, huzuni kubwa ikamjaa moyoni mwake, akakosa furaha, akakosa amani, hakujua ni kitu gani alitakiwa kuwaambia wazazi wake kama tu wangegundua kuwa alikuwa na mimba.

“Sarafina! Kuna nini?” aliuliza rafiki yake aliyeitwa Catherine.
“Nina mimba!” alijibu Sarafina.
“Una mimba?”
“Ndiyo!”
“Ya nani? Ya David?”
“Ndiyo!”

“Imekuwaje? Imepitaje tena?” aliuliza Catherine kana kwamba hakujua mimba ilikuwa inapitaje.

Sarafina hakujibu swali hilo, akajilaza kitandani, akajifunika shuka na kuendelea kulia. Moyo wake ulichoma na kuchoma, aliumia lakini ukweli haukubadilika, bado uliendelea kubaki vilevile kwamba David alikataa mimba.
“Nitafanya nini? Ni lazima nimtafute!” alisema Sarafina.

Hakutaka kuchelewa, akaanza kumtafuta mwanaume huyo kwa lengo la kuzungumza naye. Hata walipokutana, hakubadilika, aliendelea kumwambia kwamba mimba haikuwa yake.

Hilo lilimuuma mno, David yuleyule aliyekuwa akimsiia ndiye aliyekuwa akimwambia maneno hayo ambayo moyoni mwake yalifanana na msumari wa moto.
Hakuwa na la kufanya zaidi ya kukubaliana na ukweli kwamba alikuwa na mimba na mhusika alikataa kwa kusema kuwa haikuwa yake.

“Kaitoe,” alisema rafiki yake, Catherine.
“Bora nifanye hivyo! Siwezi kuwa na mimba, nitawaambia nini wazazi wangu! Cathy! Siwezi kuwa na mimba, sipo tayari kuzaa, ni bora niitoe,” alisema Catherine.
“Basi mwambie David!”

“Nimwambie nini?”
“Kwamba unatoa mimba!”
“Atakubali?”
“Akikataa sawa. Ila ninachotaka akupe pesa ya kutolea,” alisema Catherine.
“Sawa.”
 
SEHEMU ya 15...

Hilo ndilo alilolifanya Sarafina, hakutaka kuchelewa, akampigia simu David na kumwambia lengo lake la kutaka kutoa mimba hiyo hivyo alihitaji kiasi fulani cha pesa. David hakutaka kuchelewa, hapohapo, tena kwa haraka sana akamtumia kiasi cha shilingi laki mbili.
“Kaitoe haraka sana,” aliandika ujumbe mfupi.

“Sawa mpenzi!” aliitikia Sarafina na kumpanga Catherine kwamba siku inayofuata ilikuwa ni ya kwenda kwenye zahanati ya uchochoroni kwa ajili ya kutoa mimba.
**** Moyo wa Richard haukuwa na nafuu, ulitawaliwa na majonzi tele, alikosa furaha ambayo alitegemea kwamba angeipata. Alihuzunika mno kwa sababu alikataliwa na msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote.

Hakuacha kumfikiria, kila alipolala usiku, taswira ya msichana huyo ilimjia ndotoni. Wakati mwingine alitamani kumwambia kwamba alikuwa mtoto wa bilionea mkubwa lakini aliogopa kufanya hivyo.
Kila siku ilikuwa ni ya mateso tele, alipokwenda chuo na kumuona Sarafina akiwa na wakina David, moyo wake ulimuuma kupita kawaida. Alitamani kuwafuata wanaume hao na kuwaambia wamuachie msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wa dhati lakini hilo halikuwezekana kabisa.

Siku ziliendelea kukatika, baada ya miezi kadhaa, akamuona Sarafina akianza kubadilika. Hakuonekana kuwa na furaha kama kipindi cha nyuma, hakuonekana kuwa na ukaribu na David kama ilivyokuwa.

Hilo halikumsumbua, aligundua kwamba mwanaume huyo alimchezea msichana huyo na hivyo kuamua kuachana naye. Hiyo ilionekana kuwa nafasi yake na kumfuata lakini alihofia. Kama Sarafina alimkataa kipindi cha nyuma, alikuwa amebadilika nini? Ilikuwa ni lazima kumkataa kwa mara nyingine tena.
Akaachana naye, akaendelea na mambo yake lakini kila alipomuona, moyo wake haukuacha kuuma kwani alitamani kumuona akiwa na furaha siku zote, furaha isiyomuhusisha mwanaume yeyote yule zaidi yake.

Baada ya kupita miezi mitatu, akashtuka kumuona msichana huyo akiwa amenenepa na kugundua kwamba alikuwa na mimba. Huo ndiyo ulikuwa msumari mkubwa kuliko yote moyoni mwake. Aliumia kwani kwa jinsi alivyompenda Sarafina hakutegemea kumuona akiwa na mimba ya mwanaume mwingine.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 16...

Uongozi wa chuo ulipogundua hilo, haukutaka kumuacha, ukamfukuza. Richard aliumia zaidi, alitamani kumfuata Sarafina na kumwambia kwamba alikuwa tayari kumlea hata mtoto wake lakini mwisho wa siku awe naye lakini hilo lilishindikana kabisa.
Alikaa siku mbili, akaamua kumtafuta Sarafina, ili akimpata aweze kuzungumza naye lakini kitu kilichomchosha ni baada ya kuambiwa kwamba msichana huyo alirudi nyumbani kwao Mwanza.

“Lakini nasikia kwao ni masikini! Itakuwaje?” alijiuliza lakini hakupata jibu.
Hakutaka kuishia hapo, alichokifanya ni kumpigia simu, haikuwa ikipatikana, marafiki wa msichana huyo wakamwambia kwamba aliachana na matumizi ya simu kwani kila alipokuwa akiliona jina la David moyo wake ulimuuma mno.

“Na atarudi lini?” aliuliza Richard.
“Labda akijifungua!”
“Daah! Nitakwenda Mwanza kumtafuta. Anaishi wapi vile?” aliuliza Richard.
“Mabatini!”
“Mmh! Napafahamu! Nitakwenda huko!” alisema Richard.

Alipafahamu Mabatini, ulikuwa ni mmoja wa mitaa masikini jijini Mwanza. Moyo wake ulikuwa na hamu kubwa ya kumsaidia, ni kweli alimkataa, ni kweli hakumtaka lakini bado ndani ya moyo wake alisikia mapenzi mazito juu ya msichana huyo.

Alimpenda sana, hakutaka kubaki Dar es Salaam, siku iliyofuatia akapanda ndege na kuelekea Mwanza huku lengo lake likiwa ni kuonana na msichana huyo na kumwambia kwamba alikuwa tayari kumlea mtoto wake ambaye angemzaa.
**** Sarafina na Catherine wakafika katika zahanati moja uswahilini kwa ajili ya kutoa mimba. Msichana huyo alionekana kuogopa, katika maisha yake alisikia sana juu ya madhara ya kutoa mimba, alijua kabisa kwamba kizazi kingeweza kuharibika au yeye kufa lakini hayo hayakumtoa dhamira yake aliyotaka kuifanya.

Alikaa kwenye benchi na Catherine, japokuwa walikuwa wakiongea lakini Sarafina hakuonekana kuwa sawa kabisa, alikuwa kimya, kichwa alikiinamisha na muda mwingi machozi yalikuwa yakimtoka.

Kichwa chake kilisumbuliwa na fikira kuhusu David, bado hakuamini kama mwanaume huyo alimtenda kiasi chote hicho. Yaani pamoja na mapenzi aliyompa, pamoja na kumthamini sana lakini mwisho wa siku mwanaume huyo akaondoka mikononi mwake.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 17....

Baada ya dakika ishirini, daktari akatokea mahali hapo na kuwaita. Akawauliza tatizo walilokuwa nalo na wao kumwambia ukweli kile kilichowapeleka kuwa ndani ya zahanati hiyo.
“Kama ni ya wiki mbili, gharama ni elfu sitini,” alisema daktari huyo.
“Hakuna tatizo!”

Wakaambiwa wasubiri kwenye benchi, muda wote Sarafina hakuonekana kuwa na raha, mapigo ya moyo yalikuwa yakidunda huku mbele yake akikiona kifo. Hakuhitaji mtoto kipindi hicho, bado alihitaji sana kusoma na ndiyo maana alikuwa mahali hapo.

“Naogopa sana Cathy!” alisema Sarafina huku akimwangalia rafiki yake.
“Unaogopa nini? Wala huwezi kufa, ni kitendo cha dakika kadhaa tu, hata maumivu husikii tena,” alisema Catherine.
“Kweli?”
“Ndiyo!”

Alimwamini sana, wakaendelea kusubiri na baada ya dakika kadhaa, daktari akamuita Sarafina ambaye aliingia ndani ya chumba kile na kumtaka kulala kitandani. Akafanya hivyo.

Mapigo yake ya moyo yaliendelea kudunda zaidi, aliogopa, moyo wake ukajawa na hofu huku kijasho chembamba kikianza kumtoka. Alipoiona mikasi na visu juu ya meza, alizidi kuogoa zaidi.

“Mbona unatetemeka binti?’ aliuliza daktari.
“Hapana! Hapana dokta! Siwezi!” alisema Sarafina huku akijitoa katika kitanda alichokuwa amelala.
Akatoka ndani ya chumba kile, daktari akabaki akimshangaa. Hakusimama kuzungumza na Catherine aliyekuwa akimsubiri kwenye benchi, aliunganisha na kutoka nje kabisa. Rafiki yake huyo alibaki akishangaa, hakuamini kama kazi ile ilifanyika kwa dakika chache namna ile.

Alipomfikia, akamuuliza kama daktari alimaliza lakini Sarafina alimwambia kwamba aliahirisha, hakutaka kuitoa mimba hiyo, alikuwa radhi kuzaa lakini si kuua kiumbe kisicho na hatia.
“Unasemaje?” aliuliza Catherine huku akionekana kutokuamini.
“Acha nizae. Naweza kumzaa Lady Jay D au Nyerere. Sipo tayari kutoa mimba,” alisema Sarafina.

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom