Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

SEHEMU YA 80...

Wakarudi barabarani, wakasimisha gari na kumwambia Ibrahim ateremke na Malaika huku mvua kubwa ikipiga nje. Ibrahim hakuwa na jinsi, akamchukua Malaika wake, akamshusha kutoka garini na kumuweka kwenye lami.

“Bro! Mbona mnataka kutuacha! Mbona mnanichia majanga?” aliuliza Ibrahim huku akilia, kila alipomwangalia mpenzi wake, Malaika moyo ulimuuma mno.
“Baki naye, utaomba msaada! Msaada pekee tuliowapa ni kuwaacheni hai!” alisema Jumanne na Fredi kuliondoa gari mahali hapo ambapo baadaye akampigia simu David na kumwambia kwamba tayari waliwaua watu hao kwa kuamini kwamba wasingeonana tena katika maisha yao.
Ibrahim akabaki na Malaika wake, aliangalia kila upande, hakukuwa na magari mengi yaliyokuwa yakipita na hata yale machache yaliyokuwa yakipita mahali hapo hayakuwa yakisimama hata kidogo.

Alishindwa kujua afanye nini, kila alipomwangalia Malaika, moyo wake ulimwambia kwamba hiyo ndiyo ilikuwa siku ya mwisho za uhai wa msichana huyo mdogo ambaye tangu kuzaliwa kwake, alikuwa mtu wa kuteseka tu.
“Malaika usiniache! Usiniache Malaika subiri niendelee kusimamisha magari,” alisema Ibrahim huku akiwa amemuinamia msichana huyo na mvua kali ikiendelea kunyesha.

Ibrahim hakutaka kuacha, bado alihitaji msaada mkubwa kutoka kwenye gari lolote lile, alimwangalia msichana Malaika, alionyesha kabisa kwamba alikuwa akienda kufa kwani kwa jinsi mwili wake ulivyokuwa, alionekana kutokuwa na muda mwingi wa kuendelea kuishi.

Magari hayakusimama, yaliendelea kuwapita. Uamuzi wa mwisho kabisa alioufanya Ibrahim ni kumbeba Malaika na kumuweka katikati ya barabara na kusimama karibu yake, alitaka kuona gari lolote ambalo lingepita alisimamishe.
Wala hazikupita dakika nyingi, gari ndogo aina ya Spacio likaonekana mbele yake. Ibrahim akapunga mikono juu kama kulisimamisha gari hilo.

Alikuwa akipiga kelele ili aonekane kwani kama asingelisimamisha na gari hilo kupita, ilimaanisha lingemgonga yeye na msichana Malaika aliyelala chini.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 81...

Ilikuwa ni kama bahati, dereva wa gari hilo akamuona, akafunga breki kwa nguvu na gari kusimama kama mita tatu kutoka pale aliposimama Ibrahim. Hakutaka kusikia lolote, akambeba Malaika na kulifuata gari hilo ambapo dereva akafungua kioo.

“Vipi?” aliuliza dereva huyo.
“Naomba mtusaidie! Malaika anakufa,” alisema Ibrahim, hapokuwa alikuwa na moyo wa kushujaa lakini alishindwa kujizuia, akaanza kulia, machozi yake hayakuonekana kutokana na mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha.

Dereva huyo mwanaume akamwangalia Malaika, kwa jinsi alivyoonekana, alikuwa kama mfu. Alitaka kumwambia Ibrahim asijisumbue sana kwa kuwa rafiki yake alikuwa amekufa lakini hakutaka kumuumiza.

Akamfungulia mlango na kuingia ndani, akabaki akimshangaa Malaika, alionekana kuwa binti mdogo lakini hali aliyokuwa nayo ilimtisha mno. “Imekuwaje?” aliuliza dereva huyo.
“Naomba utupeleke hospitali! Malaika wangu atakufa,” alisema Ibrahim huku akilia kama mtoto.

Kwa hali aliyokuwanayo Malaika hakukuwa na la kupoteza mahali hapo, kwa haraka sana akapiga moto na kuondoka mahali hapo kwa kasi. Alikuwa na jukumu la kuyaokoa maisha ya msichana huyo mdogo, mvua kubwa iliendelea kunyesha lakini hilo halikumfanya kupunguza mwendo, aliendelea kusonga mbele kwa mwendo wa kasi.

Akafika Kibamba katika Hospitali ya Dk. Faroukh, akaliingiza gari ndani ya hospitali hiyo ambapo machela ikaletwa haraka sana na msichana huyo kuwekwa juu yake na kusukumwa kuelekea ndani ya jengo la hospitali hiyo.

“Mmh! Jamani! Kuna nini tena?” aliuliza nesi mmoja, alivyokuwa akimwangalia Malaika katika machela ile, aliogopa kwani kwa jinsi alivyokuwa, alionekana kama tayari alikuwa mfu.
“Hali ni mbaya! Naomba muokoe afya ya binti huyu,” alisema dereva.

Malaika akapelekwa mpaka katika chumba cha upasuaji na kuingizwa humo. Hawakuangalia pesa, kitu cha kwanza kabisa walichokijali kwa wakati huo ni hali ya msichana huyo mdogo.

Alipofikishwa ndani, madaktari wawili wakaingia, waliguswa kumuhudumia msichana huyo mdogo ambaye alionekana kuhitaji msaada hasa. Ibrahim na dereva yule hawakutakiwa kuingia ndani, wakabaki nje kwenye benchi huku wakisikilizia ni kitu gani kingeendelea huko.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 82...

Ibrahim alikuwa akilia mno, kwake, kila alipoangalia hakuona kabisa kama kulikuwa na dalili za mpenzi wake kupona. Alikata tamaa na aliona kabisa huo ndiyo ulikuwa mwisho wa msichana huyo mrembo.

“Mungu naomba umsaidie! Naomba umponye Malaika wangu,” alisema Ibrahim huku akiwa amejiinamia.
Muda ulizidi kwenda mbele, dakika zikakatika na mlango wa chumba kile haukufunguliwa. Kila mmoja akahisi kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa msichana yule ila baada ya saa moja, ukafunguliwa na daktari kutoka.
Uso wake tu ukaonyesha kile kilichokuwa kimeendelea ndani ya chumba kile hakikuwa kizuri, alionekana kukata tamaa, alionekana kama mtu ambaye alijitolea sana lakini mwisho wa siku hakufanikiwa kwa kile alichokuwa amekikusudia.

Akawaangalia Ibrahim na dereva waliokuwa nje ya chumba kile kwenye benchi na kuwaomba kumfuata. Wakamfuata mpaka taika ofisi yake ambapo huko hakutaka kuwaficha, aliwaambia ukweli kwamba Malaika alikuwa kwenye hali mbaya, alikuwa akiumwa ugonjwa ambao kama angevuka salama miaka kumi na nane, angepona kabisa kwani asilimia tisini na tano walikuwa wakifa kabla ya kuvuka umri huo.

“Anaumwa nini?” aliuliza dereva.
“Sickle cell!”
“Sickle cell?”
“Ndiyo!”
Dereva akashusha pumzi nzito, akamwangalia Ibrahim ambaye hata ugonjwa huo hakuwa akiufahamu, na mbaya zaidi hakuwahi hata kuusikia. Hakujua ulikuwa ugonjwa wa nini, hakujua ni kwa jinsi gani ugonjwa huo ulikuwa ukiathiri mwili wa mgonjwa.

Sickle Cell ulikuwa ni miongoni mwa magonjwa mabaya yaliyokuwa yakiua watu wengi duniani hasa watoto. Mtu aliyekuwa na ugonjwa huu, mara nyingi ilikuwa ni lazima afe kama tu hatofikisha umri wa miaka kumi na nane na kuvuka salama.

Ugonjwa huu ambao husababisha damu kupungua kwa kiwango kikubwa, tena mara kwa mara mwilini mwa mgonjwa, ulikuwa gumzo nchini Tanzania kipindi hicho. Ugonjwa huo unapokomaa, mwili wa mgonjwa hudhoofika na kusikia maumivu makali.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 83...

Ni ugonjwa unaohitaji damu nyingi kwani mgonjwa anaweza kuwa na damu ya kutosha leo hii asubuhi na jioni akaonekana kutokuwa na damu ya kutosha kutokana na seli hai nyekundu kuzishambulia seli ambazo hupeleka damu katika mifupa. “Atapona?” lilikuwa swali la kwanza alilouliza Ibrahim.
“Kupona atapona ila….”
“Ila nini daktari!”

“Sijajua kama atafikisha umri wa miaka kumi na nane. Kwa kifupi, katika kipindi hiki cha maisha yake kitakuwa ni kipindi chenye mateso sana. Atahitajika kula sana vyakula vya kuongeza damu lakini pia vilevile atatakiwa kwenda hospitali kuongeza damu mara kwa mara, hata kwa wiki mara kumi, vinginevyo, atakufa,” alisema daktari huyo ambaye hakutaka kuficha chochote kile.
“Hivyo tu halafu atapona moja kwa moja.”

“Kama atavuka miaka kumi na nane akiwa hai, ugonjwa utapona na ataishi ila kama hatovuka basi atakufa kwani ugonjwa huu huwa haumruhusu mtu kuvuka miaka hiyo, kwa bahati akivuka, na ugonjwa unapona moja kwa moja,” alisema daktari huyo maneno yaliyomfanya Ibrahim kushusha pumzi nzito.
*
*

Malaika alikuwa kitandani, mwili wake haukuwa na nguvu, kwa juu, dripu ya damu ilikuwa ikining’inia. Aliyafumba macho yake, wakati mwingine aliyafumbua na kuangalia huku na kule.
Alikuwa kwenye maumivu makali mno, pale kitandani alipokuwa, hakuacha kulia, aliumia na alihisi maumivu makali katika mifupa yake. Ugonjwa huo ulikuwa ukimtesa kupita kawaida, alionekana kukata tamaa na kila alipoangalia maisha yake ya mbele, alihisi kabisa kwamba alikuwa akiend kufa.

Ibrahim ambaye alikuwa akiingia ndani ya wodi ile, alipokuwa akimwangalia msichana wake, moyo wake ulichoma kupita kawaida. Hakuamini kama hizo ndizo zilikuwa hatua za mwisho za msichana huyo.

Wakati mwingine alikataa kabisa kukaa karibu naye kwani kwa jinsi msichana huyo alivyokuwa akilalamikia maumivu makali ya mifupa ilimfanya kutamani kulia, ili kupusha uchungu mkubwa moyoni mwake, wakati mwingine alikuwa akiondoka kabisa.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 84...

Kipindi hicho kilikuwa ni cha mateso makali, aliendelea kukaa hospitalini hapo kwa siku mbili ndipo akaruhusiwa huku akiwa amekwishawekewa damu ya kutosha. Kitu kimoja alichokuwa akihitaji kukifahamu sana ni sababu iliyowafanya kutokuuawa na watu wale.

Hakukumbuka kitu chochote ambacho kilitokea msituni. Alichokikumbuka ni kwamba walikuwa ndani ya gari, wanaume wale walisema kwamba walikuwa wakienda kuwaua ila cha ajabu kabisa mpaka muda huo wote walikuwa hai.
“Nini kilitokea?” aliuliza Malaika.
“Walituacha baada ya kuona upo hoi,” alijibu Ibrahim huku akimwangalia Malaika.
“Kweli?”

“Ndiyo! Unajisikiaje lakini?” aliuliza Ibrahim.
“Kidogo nafuu! Ila wakati mwingine mifupa inauma mno,” alisema Malaika.
Ibrahim aliumia, muda mwingi maneno ya daktari yalikuwa yakimjia kichwani mwake, akakosa amani, akakosa furaha na kujua kwamba mpenzi wake huyo kuna siku angekufa, na hata kwa jinsi walivyokuwa wakifurahia maisha, kuna siku msichana huyo asingekuwa mikononi mwake.

Hakutaka kumwambia, alijua ni kwa namna gani msichana huyo angeumia kama tu angemwambia ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea. Hakuishi kwa furaha tena, hata msichana huyo alipokuwa akimwambia maneno mazuri ya matumaini lakini bado kumbukumbu zake zilikuwa palepale kwamba ilikuwa ni lazima msichana huyo afariki dunia.
Hawakuwa na maisha ya kitajiri, zile pesa alizokuwa ameziiba Ibrahim ndizo ambazo ziliyaendesha maisha yao. Alikuwa na akili ya biashara, alijua kabisa kwamba kwa kiasi alichokuwa nacho ingekuwa kazi nyepesi kabisa kama angeanzisha biashara na kufanikiwa.

Hakuwa na umri mkubwa, wakati Malaika akiwa na miaka saba, yeye alikuwa na miaka kumi na saba hivyo kidogo akili yake ilikuwa imepanuka vya kutosha. Akafungua genge la kuuza mbogamboga za majani, hakuishia hapo, akaamua kununua toroli na madumu na kuanza kuuza maji.

Aliamini kwamba kupitia biashara hizo zingeweza kumsaidia. Ndani alibakiza kiasi cha milioni tano na alitaka kuona kiasi hicho kikiendelea kukua na si kupungua kwani kama kuyahatarisha maisha yake kwa ajili ya pesa hizo aliyahatarisha hivyo hakuona kama kulikuwa na sababu ya kuzitumbua pesa hizo.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 85...

“Ibrahim, naomba uniambie kitu kimoja,” alisema Malaika huku akimwangalia Ibrahim.
“Kitu gani?”
“Kwa nini huna furaha siku hizi?” aliuliza Malaika.
“Nani? Mimi?”
“Kwani kuna nani mwingine hapa?”
“Malaika! Nafikiria zaidi maisha, ni kwa jinsi gani maisha yetu yataendelea kwenda mbele. Hivi huoni jinsi tunavyoishi kwa shida kidogo? Tuna pesa, nafikiria ni kwa jinsi gani nitaweza kufungua biashara nyingi,” alisema Ibrahim, alitoa maelezo mengi ambayo hayakuwa na maana.

“Bado hujanipa jibu ninalolitaka,” alisema Malaika.
Moyoni mwake alianza kuhisi kitu, akajua kwamba kulikuwa na kitu ambacho mwanaume huyo hakutaka kumwambia. Aliyahofia maisha yake, alijua kwamba kulikuwa na uwezekano wa kufa na ndiyo maana mwanaume huyo hakutaka kumwambia ukweli.

Ibrahim alijikaza kiume, wakati ameulizwa swali hilo, hakutaka kuonyesha majonzi yoyote yale japokuwa bado kumbukumbu za maneno aliyoyasema daktari zilikuwa zikijirudia kichwani mwake.
Hali ya Malaika haikubadilika, katika kipindi cha mvua ambacho kilikuwa na baridi kali alikuwa akilalamika maumivu ya mifupa hasa katika uti wa mgongo, alihisi kabisa pingili za uti wa mgongo zilikuwa zikiachia.

Yalikuwa ni maumivu makubwa, akawa akipelekwa hospitalini ambapo huko, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuongezewa damu kwani ilikuwa ikipungua kwa kasi kubwa mno.
Hayo yalikuwa ni maisha ya mateso, ugonjwa wa sickle cell uliendelea kuyatesa maisha yake kiasi kwamba kuna wakati aliomba kufa kwani mauamivu aliyokuwa akiyasikia hayakuwa yakielezeka.

“Hizi Folic Acid zitaweza kumsaidia, cha msingi awe anakunywa kidonge kimoja kwa siku,” alisema daktari, alikuwa akimwambia Ibrahim.
Folic Acid zilikuwa moja ya dawa zenye nguvu ambazo alitakiwa kunywa mgonjwa aliyekuwa akiumwa ugonjwa huo. Wakati seli hai nyekundu za damu zinapokuwa zikipambana kuhakikisha damu haipungui, dawa hiyo ndiyo inayozisaidia seli hizo katika mapambano hayo.

Ilikuwa kazi kubwa, mwili ulikiwa kuwa na damu ya kutosha. Kila siku kazi ya Malaika ilikuwa ni kunywa vidonge hivyo ambavyo viliuzwa kwa bei ya juu lakini kwa kuwa Ibrahim alikuwa na pesa, hilo halikuonekana kuwa tatizo.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 86...

“Kuna siku utapona tu!” alisema Ibrahim huku akimwangalia Malaika aliyeonekana kukata tamaa kabisa.
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Ila nimesikia huu ugonjwa mbaya sana!”
“Hakuna. Si ugonjwa mbaya! Ni ugonjwa wa kawaida ambao unaweza kupona kabisa,” alisema Ibrahim huku akimwangalia Malaika.

Hiyo ndiyo ilikuwa kazi kubwa aliyokuwa nayo. Kila siku ilikuwa ni lazima amtie moyo kwani pasipo kufanya hivyo ilimaanisha kwamba binti huyo angekufa kwa kuwa tu angekata tamaa mbele yake alingeona giza.

Kidogo Malaika akafarijika, kwake, kitu kilichompa tumaini la kuishi kwa kipindi kirefu kilikuwa ni maneno ya mwanaume huyo. Alimpenda kutoka moyoni mwake, na kila siku alimwambia kwamba hakuogopa kufa bali kitu pekee alichokuwa akikiogopa moyoni mwake ni kumpoteza tu.

“Kweli?”
“Ndiyo! Siogopi kufa tena! Kitu pekee ninachokiogopa ni kukupoteza mpenzi,” alisema Malaika huku akimwangalia mpenzi wake huyo aliyeonekana kuwa kwenye mapenzi ya dhati.
*
*

Maisha ya David yalikuwa ni kula bata tu, kila siku alikuwa mtu wa kusafiri kusafirisha madawa ya kulevya. Aliingiza kiasi kikubwa cha pesa na Bwana Mpobela alikuwa akimtegemea kwani mbali na kusafirisha huko, David alikuwa mjanja, viwanja vya ndege kulipoonekana kuna noma, alitumia kila ujanja hata kusafirisha kwa meli ya mizigo lakini mwisho wa siku mzigo ufike salama.
Mpaka katika kipindi hicho, mke wake, Gloria hakujua kitu chochote kile, alidanganywa vya kutosha na kuona kwamba mume wake huyo alikuwa mfanyabiashara ambaye alikuwa akisafiri safiri.

Biashara ilikuwa, watumiaji wa madawa ya kulevya wakaongezeka. David akatanua utajiri wake, akaanza kuvuma jijini Dar es Salaam kwamba alikuwa bilionea aliyekuwa akichipukia.
Baada ya miaka miwili kufanya biashara hiyo, David akaanza kuvutika na utumiaji wa madawa ya kulevya. Alikuwa akishangaa, vijana wengi walikuwa wakitumia madawa hayo na kuyasifia, mzigo mkubwa aliokuwa akiupeleka Tanzania ulikuwa ukimalizika kwa kipindi kifupi sana hali iliyomfanya kugundua kwamba kulikuwa na watumiaji wengi waliokuwa wameongezeka.

iTAENDELEA.
 
SEHEMU YA 87...

Alitaka kujua kuhusu madawa hayo, kama kuna wengi walikuwa wakivuta na kuendelea kuishi, kwa nini na yeye asijaribu kufanya hivyo? Hapo ndipo alipoanza kujiingiza katika utumiaji wa madawa hayo.

Hakutaka kumwambia mkewe, alifanya kificho, siku za kwanza zilionekana kuwa za mateso lakini baada ya wiki moja ya kutumia, akavutiwa mno na madawa hayo. Kila alipokuwa akivuta, akili yake ilihama, alijiona kuwa na nguvu kubwa, alijiamini na alihisi kuwa na uwezo wa kufanya jambo lolote lile.

Hiyo ilikuwa ndiyo stimu yenyewe. Alipokuwa akivuta, alijifungia hotelini na kuanza kubwia unga mdogomdogo kitu kilichomfanya kujisikia hali ya tofauti kuliko kipindi cha nyuma.

Taratibu akawa anaingia katika mkumbo wa matumizi ya madawa hayo, wakati mwingine hakuwa akifanya kazi nyingine zaidi ya kujifungia hotelini na kuanza kuvuta madawa hayo ambayo kwake yalionekana kuwa kitu bora na muhimu kuliko vyote katika dunia hii.

“Nilichelewa sana kujua hiki kitu! Kwa nini sikuambiwa mapema?” alijiuliza kila alipokuwa akitumia. Wakati mwingine alijihisi akiwa Marekani akizungumza na bilionea Bill Gates kuhusu kuinua hali ya uchumi wa Tanzania na wakati ukweli ni kwamba alikuwa nchini Tanzania, katika hoteli moja jijini Dar es Salaam. *
*
*

Alianza taratibu sana lakini mwisho wa siku David akaanza kuzoea, akawa mtumiaji mzuri wa madawa hayo, alifanya kwa siri, hakutaka Gloria ajue kilichokuwa kikiendelea. Kila alipokuwa akielekea kazini, alijifungia ofisini na kuanza kutumia madawa hayo.

Mzee Mpobela ambaye alikuwa karibu naye akashtukia kilichokuwa kikiendelea, kila alipomwangalia David aligundua kwamba mwanaume huyo alianza kutumia madawa ya kulevya. Ilimuumiza sana, japokuwa alikuwa akiwauzia watu wengine lakini alijua madhara ya kutumia madawa hayo.

Hakupenda kumuona David akitumia, akamuita kwa lengo la kuzungumza naye, alimwambia kwamba alikuwa akitumia madawa ya kulevya kitu ambacho hakikuwa kizuri lakini David akakataa na kumwambia kwamba hakuwa akitumia madawa hayo.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 88...

Kwa kumwangalia ilikuwa vigumu kuamini kwani dalili zote alikuwa akizionyesha. Mzee Mpobela aliendelea kumsisitizia kwamba madawa ya kulevya hayakuwa mazuri, alitakiwa kuachana nayo lakini kwa Davidi ilikuwa vigumu sana kumkubalia.

Siku ziliendelea kukatika, baada ya mwaka mmoja wa kutumia kisiri hatimaye mkewe, Gloria akaanza kugundua kwamba mumewe hakuwa sawa, hakuwa imara kama kipindi cha nyuma na mbaya zaidi sauti yake ikaanza kubadilika na kusikika kama ya mtu anayetumia madawa ya kulevya.

“Mume wangu!” aliita Gloria.
“Unasemaje mke wangu!”
“Kuna nini kinaendelea?”
“Wapi?”
“Sauti yako inabadilika kila siku, kuna nini?” aliuliza Gloria huku akimwangalia mumewe huyo.

“Hakuna kitu!” alijibu David.
Alijaribu kumdanganya mke wake, hakutaka kabisa mwanamke huyo agundue kile kilichokuwa kikiendelea, kila siku alijificha, alitumia kisiri na aliporudi nyumbani alionekana kuwa sawa lakini baadaye kila kitu kikawa hadharani.

Gloria hakutaka kukubali, alijua kabisa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea kwa mume wake, alimtilia shaka kwamba alikuwa akitumia madawa hayo na hivyo kwenda ofisini kwake.

Hakutaka kumpa taarifa, kama mumewe alikuwa akirudi nyumbani salama, hakuwa akifanya kitu sasa madawa hayo alikuwa akivutia wapi zaidi ya kazini kwake?

Gloria akaenda huko, alipofika sehemu ya mapokezi, hakutaka mumewe kupigiwa simu kwani alijua kwamba endapo angejua kwamba amekuja basi angeficha kila kitu.

“Karibu!” alimkaribisha sekretari.
“Ahsante! Yupo huyu?” aliuliza Gloria.
Hata kabla msichana huyo hajajibu kitu chochote kile Gloria akaanza kupiga hatua kuelekea ofisini kwa mumewe. Akaufungua mlango na kuingia ndani.

David alipomuona, akashtuka, haraka sana akainuka kwenye kiti na kumfuata kwa lengo la kumkumbatia na kumbusu kama kawaida yake, Gloria akamsukumia pembeni na kuifuata meza yake.

Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kufungua droo za meza ile, kile ambacho alikitarajia ndicho alichokutana nacho humo. Macho yake yakatua katika mfuko wa nailoni, alipouchukua na kuufungua akakutana na madawa ya kulevya pamoja na bomba la sindano.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 89...

“Let me explain,” (acha nikuelezee) alisema David.
“What do want to tell me?” (unataka kuniambia nini?) aliuliza mwanamke huyo kwa hasira.
“I’m not what you think I’m,” (mimi sipo kama unavyonifikiria) alisema David.

“Who are you?” (wewe nani?) aliuliza Gloria huku akionekana kubadilika, japokuwa mara kwa mara alikuwa akikasirika lakini siku hiyo alionekana kuwa tofauti na siku nyingine kiasi kwamba David mwenyewe alianza kuogopa.

Hakuwa na cha kujitetea, alikamatwa akiwa na madawa ya kulevya, Gloria hakutaka kusikia chochote kile, akatoka na kurudi nyumbani kwake. Njiani alikuwa akilia, hakuamini kile alichokutana nacho kwa mumewe, wakati mwingine alihisi kama alikuwa ndotoni ambapo baada ya muda fulani angeamka kutoka katika usingizi mzito.

Alimfahamu mumewe, alikuwa na sifa za kuitwa mume bora kutokana na jinsi alivyokuwa. Hakujua ni nini kingetokea kama angemwambia baba yake, hakujua kama kila kitu alichokuwa nacho David kuhusu madawa yalitoka kwa mzee huyo.
Gloria akabadilisha mawazo, hakutaka kurudi tena nyumbani, ilikuwa ni lazima kuwasiliana na baba yake kwa lengo la kuonana na kuzungumza naye.

Hilo halikuwa tatizo, Mzee Mpobela akamwambia amfuate ofisini kwake ambapo huko wakaanza kuzungumza.
Hakushangaa, aliligundua hilo tangu kitambo na alijaribu kumwambia David kuachana nayo lakini mwanaume huyo hakutaka kusikia. Walimwaga maji na ilikuwa vigumu kuyazoa.

Akampigia simu David na kuomba kuonana naye baada ya kurudi nyumbani. Hilo halikuwa tatizo, wakaonana na kuweka kikao cha watu wanne tu, wazazi wa Gloria, Gloria mwenyewe na David.

David hakukataa, alikiri kutumia madawa hayo na aliahidi kuacha lakini hakukuwa na mtu aliyedhani kama mwanaume huyo angeacha kutumia madawa hayo kwani watumiaji wengi waliokuwa wakitumia, ilihitajika nguvu nyingi sana kuacha.

Kama walivyofikiria ndivyo ilivyotokea, madawa ya kulevya yakamchukua David, akaanza kupoteza nguvu, mwili wake ukaanza kuchoka japokuwa alijitahidi sana kula. Alibwia madawa ambayo hayakuwa yakimpenda hivyo kuanza kudhoofika mwili wake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 90...

Yalikuwa ni maumivu makali kwa Gloria, kilichokuwa kikitokea hakuwa akikiamini, kitendo cha kumuona mumewe akianza kupotea kilimtia uchungu mkubwa moyoni mwake.
Mwaka mwingine uliofuata, David akachakaa, hakuwa yule wa kipindi cha nyuma, maisha yake yaliendeshwa kwa kutumia madawa ya kulevya na kila alipokuwa akikosa kutumia kwa saa kumi na mbili mwili mzima ulikuwa ukiwasha kana kwamba alipakwa upupu.

“Baba msaidie mume wangu! Anapotea,” alisema Gloria huku akilia.
“Nimemsaidia sana lakini sidhani kama itawezekana tena,” alisema Mzee Mpobela.
Alijitahidi kumpeleka katika vituo vya watumiaji wa madawa ya kulevya (soba) lakini kila hali yake iliporudi na kuwa nzuri, aliporudi nyumbani aliendelea kubiwa madawa ya kulevya.

Yalimuumiza, yaliichafua damu yake, mishipa yake ilitobolewa sana kwani alipokuwa akiikosa mikononi alikuwa akiifuata ya shingoni mwake. Aliumia lakini hakuwa na jinsi, alikuwa akiitafuta stimu ambayo ingemfanya kujisikia furaha kila wakati.

Akawa anakutana na wenzake na kuanza kutumia huko, tena wakati mwingine akitoroka nyumbani na kwenda kuishi mbali kabisa. Gloria na baba yake walimtafuta sana, kila walipompata, alitoroka tena na alikuwa akirudi nyumbani pale alipokuwa akiishiwa tu, alipopata pesa, alitoroka tena.

“David mume wangu unanitesa,” alisema Gloria huku akimwangalia mume wake huyo.
“Mimi?”
“Ndiyo! Unanitesa sana! Kwa nini lakini?” aliuliza Gloria.

Mwenyewe alijiona kuwa sawa, hakuacha, kila siku alikuwa mtu wa kutumia madawa hayo. Watu wengi walimuonea huruma, waliona jinsi alivyokuwa akipotea, jinsi alivyokuwa akiyahatarisha maisha yake, kila mmoja alihuzunika lakini hawakujua ni kwa namna gani wangeweza kumsaidia kuepuka na madawa hayo.

Baada ya mwaka mwingine kuingia, mishipa yake ikaanza kupata matatizo, utumbo wake uliokuwa ukipeleka chakula ukaanza kuhadhiriwa, figo zikachoka na hatimaye akapata kidonda kidogo ubavuni, kidonda kilichokuwa kikitoka usaha kila siku.

Mzee Mpobela hakutaka kukubali, bado alimpenda sana David, alichokifanya ni kuanza kumsaidia, alimpeleka katika Hospitali ya Muhimbili, akatibiwa, hakikupona, akarudishwa nyumbani.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 91...

Alikuwa akitia huruma, japokuwa alikuwa mgonjwa lakini hakutaka kuacha madawa ya kulevya. Kidonda kile kiliendelea kumtesa, wakati mwingine alikuwa akilia usiku lakini asubuhi kama kawaida aliendelea kubiwa madawa hayo.

Kidonda kile kidogo kikaanza kuongezeka taratibu na baada ya miezi miwili akapelekwa tena hospitalini ambapo daktari aliamua kuwaambia ukweli kwamba kidonda kile kisingeweza kupona maisha yake yote kwani madawa ya kulevya aliyokuwa akitumia yalimsababisha kansa ya damu iliyoanza kumtafuna.

“Unasemaje?” aliuliza Gloria huku akiwa haamini.
“Mumeo ana kansa ya damu,” alisema daktari kwa huruma huku uso wake ukiwa kwenye huruma nzito. Gloria akaanza kulia kwani aliamini mwisho wa kansa ile ndiyo ungekuwa mwanzo wa kifo cha mume wake kitu ambacho hakutaka kuona kikitokea.

**** Yalikuwa ni majibu mabaya kwa Gloria, hakuamini kile alichokisikia kwamba mume wake mpendwa, David alikuwa na kansa ya damu iliyokuwa ikimtafuna ambayo kitaalamu ilijulikana kama Leukemia.

Alilia usiku na mchana, kila alipokuwa akimwangalia mume wake kitandani pale, moyo wake ulimuuma na kumchoma. Hakuona kama mume wake huyo angeweza kupona kwani kila siku kile kidonda kilichokuwa ubavuni mwake kilizidi kutoa usaha na mbaya zaidi kiliendelea kuchimbika kwenda ndani.

David aliumia, alilia kitandani pale, hakujua kama ugonjwa huo ulikuwa ni laana kutokana na yote aliyokuwa ameyafanya. Alitembea na wanawake wengi, aliwapa mimba na kuwalazimisha kutoa. Hakuona thamani ya wanawake wale, hakujua kama mwisho wake huo ulitengenezwa na wanawake wale ambao kila siku walilia kwa ajili yake.

Machozi ya uchungu waliyokuwa wameyatoa kwa ajili yake leo hii yalikuwa yakilipwa kwa maumivu makali mwilini mwake. Aliendelea kuteseka, kila siku Gloria alikuwa akishinda hospitalini hapo, kila alipokuwa akimwangalia mume wake, alibadilika, hakuwa kama yule aliyekuwa kipindi cha nyuma.

Mwili wake ulikongoroka, madawa yale yalimuumiza mno, wakati mwingine, alikuwa akitetemek, mwili wake ulizoea madawa hayo, alipokuwa akiyakosa, alikuwa akiteseka kupita kawaida.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 92...

Mzee Mpobela akamnunulia dawa za kuondoa usongo wa kutumia madawa ya kulevya, dawa za Methadone, David alianza kuzitumia hizo lakini hazikusaidia, bado alikuwa na usongo mkubwa wa kutumia madawa hayo.

Walitaka aachane kabisa na utumiaji wa madawa hayo, wakaamua kumsafirisha na kumpeleka nchini Malaysia, huko alitakiwa kukaa katika kituo kimoja cha watu waliokuwa wanatumia madawa ya kulevya lakini wakawa wanapatiwa tiba.
Akawekwa huko, kidogo ilimsaidia, hamu ya kutumia madawa hayo ikaanza kuondoka, mwili ukaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ila ni kitu kimoja tu ndiyo kilichokuwa kikimtesa, nacho kilikuwa ni kidonda alichokuwa nacho ubavuni.

Hakikupata nafuu, kila siku kilitoa usaha, wakati mwingine kilikuwa kikinuka sana hali iliyomfanya kutengwa na watu mbalimbali. Kwa kuwa alikuwa kero katika kituo hicho, uongozi ukamwambia kwamba alitakiwa kurudi nchini Tanzania.
Akarudishwa, Gloria akabaki naye akiendelea kumuuguza mume wake. Hakupata nafuu, kila siku alikuwa mtu wa kulia tu, aliteseka, aliumia lakini hakukuwa na nafuu yoyote ile aliyokuwa akiipata.

Kidonda kikachimba na kuchimba, mbavu zikaanza kuonekana, mbali na kuchimbika kwa kidonda hicho, kansa ikaongezeka kwani hata dawa alizokuwa akizitumia hazikumsaidia hata kidogo.

Macho yakaanza kuwa mekundu, kila alipokuwa akikaa, alihisi mwili wake kuwasha kupita kawaida. Akaanza kuviona viungo vyake kuwa vizito, akashindwa kutembea, alihisi damu zikiwa zimejaa miguuni, akahisi moyo wake kuwa mzito, aliteseka na kuteseka lakini hakupata nafuu hata mara moja.

“Sarafina ananiua…” alijikuta akisema mbele ya mkewe.
Gloria alishindwa kuelewa ni kitu gani kilitokea, alimwangalia mume wake kwa macho yaliyomtaka kurudia tena kile alichokisema. David hakunyamaza, alimwambia mke wake kwamba kulikuwa na mtu aliyekuwa akisababisha yeye kuwa katika hali hiyo.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 93...

Aliwachezea wanawake wengi, aliwaambia wanawake hao watoe mimba lakini wote hakuwakumbuka, mtu aliyemkumbuka zaidi alikuwa Sarafina. Picha aliyokutana naye barabarani ikamjia, hakuwa Sarafina yule wa kipindi cha nyuma, alikuwa mwingine kabisa, aliyechoka, ambaye alihitaji msaada mkubwa ila kwa kuwa alikuwa jeuri, akaondoa gari lake pasipo kumsikiliza kwa chochote kile.
Picha hiyo ilimuumiza kupita kawaida.

Alibaki kitandani pale akilia kwa uchungu. Ulikuwa ni muda wa kutubu dhambi zake, alijua kwamba alikuwa katika hatua ya mwisho ya kuvuta pumzi ya dunia hii, alitubu, Mungu amsamehe kwa yote aliyokuwa ameyatenda.

“Mtafute Sarafina umuombe msamaha!” aliisikia sauti ikizungumza moyoni mwake.
Hakujua mwanamke huyo alikuwa wapi, hakujua kama bado alikuwa akiendelea kukaa mitaani au wapi. Alimshirikisha mke wake juu ya jambo hilo, hakutaka kumficha, alimwambia ukweli juu ya kila kitu.

Ilipita miaka mingi nyuma lakini Gloria alikumbuka kila kitu. Moyo wake uliumia, haukuumia kwa sababu ya mwanamke mwingine bali uliumia kwa kuwa mwanamke mwenzake alifanyiwa jambo kama hilo, hakika alijiona kama yeye ndiye aliyefanyiwa.

“Namkumbuka. Ni miaka mingi imepita,” alisema Gloria.
“Ninaamini yeye ndiye chanzo cha kila kitu kilichotokea mke wangu! Nahitaji kumtafuta mwanamke huyu nimuombe msamaha,” alisema David huku akimwangalia mke wake.

Alidhamiria kwa moyo mmoja, siku iliyofuata, hakutaka kukaa hospitalini, wakaomba ruhusa kutoka, wakapewa na kuanza kumtafuta Sarafina. Kila alipokuwa akitembea, david hakutembea vizuri, alikuwa akichechemea na muda mwingi alihitaji kupumzika.

Kidonda kilimtafuta, kilimtesa, kilitoa usaha, kilinuka lakini hakutaka kuona akibaki hospitali, alitaka kumtafuta mwanamke huyo, amuone mtoto wake na kumlea lakini si kuona akifa pasipo kumuona mwanamke huyo.

Alimtafuta Sarafina kwa siku ishirini, alitembea sehemu kubwa na mkewe, mitaani lakini kote huku hakufanikiwa kumuona mwanamke huyo. Moyo wake uliuma, ulichoma, alijutia maisha yake, ni kweli alikuwa na pesa lakini amani ya moyo ilikuwa ni zaidi ya pesa alizokuwa nazo.

Itaendeea.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom