Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

Sarafina - Mtunzi Nyemo Chilongani

SEHEMU YA 94...

Siku hizo zikakatika, hakumuona Sarafina wala mtoto wake. Akarudi hospitalini, akalia sana, akakata tamaa na kadiri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele ndivyo alivyokuwa akizidi kuumia kitandani pale.
“Daktari!” alimuita daktari aliyekuwa akiingia na kutoka ndani ya chumba alichokuwemo.
“Unasemaje?”

“Naomba kalamu na karatasi!” alisema David kwa sauti ndogo, daktari akaondoka, ba baada ya dakika chache akarudi na kalamu, karatasi mikononi mwake, David akaichukua, akainuka kitandani pale, kwa tabu sana akakaa na kuegemea mtu kwa nyuma.

Alisikia mauamivu makali, alivumilia, alitaka kuandika vitu kwa ajili ya Sarafina, aliamini kwamba kamwe asingeweza kumuona ila aliamini kwamba maandishi yalikuwa yakiishi na ingetokea siku moja yangeweza kumfikia mwanamke huyo.

Kabla ya kuandika maneno yoyote yale katika karatasi ile, akatulia, akaangalia juu, mawazo yake yakaanza kurudi nyuma kabisa, tangu siku ya kwanza kuonana na msichana huyo, alikuwa mrembo, alimpenda, lakini kwa ujinga wake, kwa tamaa zake mwisho wa siku akampa mimba na kumshinikiza kuitoa kitu ambacho msichana huyo alikataa.

Kila kitu alichokuwa akikiwaza wakati huo, kiliuchoma moyo wake. Aliendelea kukumbuka mambo mengi, kumbukumbu zilizomuumiza ambazo zilimfanya kujuta zaidi na zaidi. Baada ya kukumbuka kwa dakika chache, akaanza kuandika maneno hayo.
Mpenzi Wangu Sarafina.

Nakumbuka siku ya kwanza nilipokuona, hakika ulikuwa msichana mrembo ambaye sikuamini kama ningeweza kuwa pamoja nawe. Nilikupenda kupita kawaida na nilipokwambia, ulijitambua, uliutambua uzuri wako, ukanikatalia lakini mwisho wa siku ukanikubalia.
Mpenzi Wangu Sarafina.

Nilikupata, nikakupenda, sikuwa na akili, nilikuwa kijana mwenye mambo mengi. Mbali na wewe nilikuwa na wanawake wengine, nilikuchukulia kama nilivyowachukulia wengine, sikukujali sana, nilikuchukulia kuwa mwanamke wa kupita, sikukuthamini inavyotakiwa. Nisamehe sana Sarafina.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 95...

Mpenzi Wangu Sarafina.
Baadaye ukaniambia kwamba una mimba. Sikuwa tayari kuwa na mtoto, nilikuchukulia kama mwanamke wa starehe, niwe na mtoto ili iweje? Nikaamua kukwambia kwamba ulitakiwa kutoa, kama nilivyokwambia, ndivyo nilivyowaambia wengine. Nisamehe sana Sarafina.

Mpenzi Wangu Sarafina.
Niliendelea kutembea na wanawake wengine, kulala nao ndiyo ilikuwa sifa ya ujanani, niliwatambia wenzangu kwamba nilikuwa kiwembe, nilimchukua kila msichana niliyekuwa nikimtaka, sikujua kama muda unakwenda, sikujua kwamba kila ubaya unaoufanya una gharama zake, nisamee sana Sarafina, sikujua, wakati mwingine natamani sana kama muda ungerudi nyuma, nisafishe pale nilipokosea ila sitoweza tena.
Mpenzi Wangu Sarafina.

Najua ulijifungua, sikujua ulikuwa ukiishi vipi. Nilipokuona barabarani ukiwa na mtoto ambaye niliamini ni wangu kwa kuwa tulifanana sana, nilichukia. Niliona ukitaka kuniharibia uhusiano wangu kwa mke wangu, kwa kuwa sikukuhitaji, nikaondoka. Hicho ni kitu ambacho kinaniumiza mpaka leo hii. Kwa nini nimekufanyia yote hayo? Kwa nini sikukuonea huruma Sarafaina wangu? Hakika ninastahili kupata yote ninayopata kwani mauamivu ninayoyasikia moyoni, ni makubwa kuliko maumivu ya kidonda nilichokuwa nacho.
Mpenzi Wangu Sarafina.

Nilijiona mjanja, nilijiona mjuaji, baada ya kuhangaika sana na kuoa, hatimaye nikapata pesa, nikajiingiza kwenye matumizi ya madawa ya kulevya. Ninahisi kuna kitu hapa. Nilichukia madawa ya kulevya, ila kwa nini niliingia? Nahisi Mungu aliniingiza ili baadaye nipate kile kilichokusudiwa na kuutambua uovu wote niliokuwa nimekutendea maishani mwako.

Sarafina! Mimi ni mkosaji, nimekukosea sana, nimekuumiza sana, ila pamoja na yote hayo, naomba unisamehe, nisamehe kwa yote niliyokutendea, ni ujinga, ni upumbavu, hakika ninastahili haya ninayoyapata. Hakika nimejifunza mambo mengi, na kupitia maisha yangu natumaini wanaume wengi watajifunza.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 96...

Mpenzi Wangu Sarafina.
Nina hamu ya kumuona tena mtoto wangu. Ninaumia ninapokufa nikiwa na mtoto mmoja tu. Nilijiona mjanja kumpa muda mke wangu kwamba hatutakiwi kuwa na mtoto kwa sasa mpaka baadaye. Ni upumbavu pia kwani kuwa na mtoto ni jambo jema mno. Sarafina, nina hamu ya kumuona tena mtoto wangu, sijui nitamuona vipi, ila ninamkumbuka mno.
Mpenzi Wangu Sarafina.

Ninaomba msamaha! Nisamehe kwa yo…..
Aliandika maneno mengi, kwa sana alihitaji msamaha kwa yote aliyokuwa ameyafanya. Hakumaliza kuandika tena, vidole vyake vikalegea, kalamu ikaanguka, macho yakawa mazito na hatimaye kufumba milele.

David akafariki kitandani pale kwa maumivu makali. Kansa ya damu ilimtafuta kwa kiasi kikubwa mno. Kilichokuwa kimemuuma mno si kansa bali moyo wake uliokuwa ukijuta kwa kila kitu alichokuwa amemfanyia msichana ambaye kila siku alimwambia kwamba alikuwa akimpenda kwa moyo wote.
*
*
*

Richard alishindwa kuubadilisha ukweli, ukabaki palepale kwamba mtoto wake alikuwa amefariki alipokuwa akizaliwa. Alilia sana, alimwangalia mke wake pale kitandani alipokuwa, moyo wake ulimuuma na kuna wakati alimlaumu Mungu kwa kumsababishia maumivu makali kiasi hicho.

Alisimama mbele ya kitanda alicholalia mke wake, alimwangalia huku moyo wake ukiwa kwenye maumivu makali. Alikumbuka namna Bianca alivyokuwa na hamu ya kumuona mtoto wake, alikumbuka jinsi mwanamke huyo alivyokuwa makini katika kuitunza mimba yake, hakujua ni kitu gani kingetokea baada ya kufumbua macho na kugundua kwamba mtoto wake alikuwa amefariki dunia.

Machozi yalimbubujika, alikuwa kwenye kipindi kigumu, kilichojaa maumivu makali kuliko vipindi vyote. Alisimama palepale, hakutaka kuondoka, alimwangalia mke wake machoni mwake, hakuona kama kungekuwa na mtu ambaye alikuwa na uwezo wa kumpa faraja zaidi ya mtoto wake ambaye alikufariki katika kipindi alichokuwa akizaliwa.

Baada ya saa moja, wazazi wa pande zote wakafika hospitalini hapo. Walipomuona Richard kila mmoja alimuonea huruma, alikuwa mnyonge, mwenye mawazo na hata walipoyaangalia macho yake waligundua kabisa kwamba mwanaume huyo alikuwa na maumivu makali moyoni mwake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 97...

“Pole sana Richard,” alisema baba yake huku akimpigapiga mgongoni.
“Nashukuru sana! Naamini kila kitu kinachotokea kipo katika makusudi yake,” alisema Richard huku akikiinamisha kichwa chake.
Baada ya saa nne kupita ndipo Bianca akafumbua macho kitandani pale. Mtu wa kwanza kabisa kumuona alikuwa mume wake na swali la kwanza kuuliza lilikuwa ni juu ya mtoto wake.

Alitaka kumuona, alikumbuka kwamba kabla ya kupoteza fahamu alikuwa katika chumba cha uzazi kwa ajili ya kujifungua na hata alipoyafumbua macho yake, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kutaka kumuona mtoto wake huyo.
Aliangalia huku na kule, hakukuwa na mtoto, aliwaona wazazi wake na mume wake huyo ambaye uso wake ulikuwa kwenye majonzi tele. Akahisi kulikuwa na kitu kimetokea kwani ilikuwa ni vigumu watu hao kuwa kwenye nyuso hizo na wakati alikuwa amejifungua.

“Mtoto wangu yupo wapi?’ aliuliza Bianca huku akimwangalia mume wake.
“Mke wangu! Subiri kwanza! Unaendeleaje?’ aliuliza Richard huku akimwangalia Bianca.
“Niambie kwanza mtoto wangu yupo wapi!”
“Bianca! Pumzika kwanza!”
Moyo wa Richard ukauma zaidi. Bianca hakutaka kunyamaza, alitaka kusikia mahali alipokuwa mtoto wake. Hakujua kama alikuwa amefariki, alichokijua ni kwamba alijifungua salama na mtoto huyo kuhifadhiwa mahali fulani.

Richard alijitahidi kumtuliza mkewe kitandani pale lakini moyo wake ulikuwa ukiuma mno. Alijizuia kwa nguvu zote asionyeshe majonzi yoyote yale au hata kumwaga machozi kwa mkewe lakini kikafika kipindi akashindwa kabisa kwani kwa jinsi Bianca alivyokuwa akimuulizia mtoto na moyo wake kujua kwamba alifariki ila hakutaka kumwambia ukweli,
Bianca alielewa kilichokuwa kikiendelea, kitendo cha mume wake kunyamaza kumwambia kilichokuwa kimetokea ilimaanisha kwamba mtoto wake alikuwa amefariki dunia kitu kilichomuuma mno.
Akaanza kulia kwa sauti huku akimtaja mtoto wake.

Richard aliyekuwa mbele yake akashindwa kuvumilia, haraka sana akatoka na kwenda ukutani ambapo huko akaanza kulia kwa uchungu mkubwa.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 98...

Moyo wake ulimuuma zaidi, alijitahidi mno kumficha mkewe lakini hakufanikiwa na mwisho wa siku kugundua kwamba mtoto wake mpendwa alikuwa amefariuki dunia.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli. Mioyo yao iliumia mno, mpaka siku ambayo Bianca aliporuhusiwa kurudi nyumbani, alionekana mnyonge kupita kawaida na muda mwingi alikuwa akilia kwa kilio cha kwikwi.

Richard hakutaka kwenda kazini, kwa siku hizo akaamua kukaa nyumbani kuomboleza kwani kama kuumia, aliumia mno na mbaya zaidi, mkewe ambaye ndiye alikuwa faraja yake pekee naye pia akawa ameumia.
Siku zikakatika, wakaendelea kukaa kwenye majonzi mazito. Baada ya mwezi mmoja kupita, wakakubaliana kukubaliana na hali iliyotokea kwamba kama mtoto wao kufariki, alifariki na hivyo walitakiwa kufanya mambo yao kama kawaida.

Walichokifanya ni kuendelea na maisha ya kawaida huku wakimuomba Mungu awape mtoto mwingine. Kila mmoja alionekana kuwa siriazi kwa kipindi hicho, katika siku zote za hatari za kushika mimba ndizo ambazo walikuwa wakifanya mapenzi kwa nguvu zote.

Walichokuwa wakikihitaji kilikuwa ni mtoto. Mungu aliwapa kila kitu maishani mwao, ili furaha yako ikamilike ilikuwa ni lazima kupata mtoto. Walijitahidi kupita kawaida lakini matokeo yakawa bila kwa bila.

Hawakujua tatizo lilikuwa nini. Miezi sita ya majaribio ikapita lakini Bianca hakushika mimba. Wakawa na hofu, wakahisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea, wakati mwingine Richard alihisi kwamba mke wake alishindwa kuzihesabu siku zake za kuingia kwa mwezi hivyo kuanza kuhesabu kwa pamoja.

Walifuata kalenda lakini bado Bianca hakujisikia hakuchafuka na mbaya zaidi hata kujisikia kichefuchefu hakujisikia. Hawakukata tamaa, waliendelea zaidi, mwaka ukakatika, hali ilikuwa hivyohivyo, Bianca hakuwa amepata mimba kitu kilichowafanya kwenda hospitalini.

“Kwa muda gani?” aliuliza daktari.
“Mwaka mzima! Hakuna kitu,” alijibu Richard huku akionekana kukata tamaa, muda wote huo Bianca alikuwa kimya, hakuwa na la kuongea, kama kumuomba Mungu, alimuomba sana lakini hakukuwa na kitu chochote kile.

“Itabidi tumfanyie uchunguzi mke wako,” alisema daktari kitu ambacho kwa Richard hakukuwa na tatizo lolote lile.
 
SEHEMU YA 99...

Hilo ndilo walilolifanya madaktari hao, wakampima Bianca na kugundua kwamba alikuwa na tatizo kubwa katika mfumo wake wa uzazi. Ukuta wake wa uterasi ulikuwa umechanika hivyo kuwa vigumu kwa kushika mimba.
“Unasemaje?” aliuliza Richard huku akionekana kushtuka.

“Kwa hapa! Ni vigumu sana kushika mimba. Kama unasema mimba yake iliharibika, basi tatizo lilianzia hapo,” alisema daktari huku akimwangalia Richard.
Wote wakabaki kimya, wakainamisha vichwa vyao chini, maneno aliyozungumza daktari huyo yaliwaumiza kupita kawaida. Hawakuamini kama huo ndiyo ungekuwa mwisho wa mwanamke huyo kushika mimba.

“Inamaana hatoweza kushika mimba?” aliuliza Richard huku akishtuka.
“Ndiyo! Ila kama atafuata maelekezo ya kidaktari basi atashika baada ya miaka mitatu,” alijibu daktari huyo, jibu lililowafanya wote kunyong’onyea kwani hawakutegemea kusikia kitu kama hicho!
“Miaka mitatu au miezi mitatu?” aliuliza Bianca huku akimwangalia daktari huyo.
“Miaka mitatu! Siku 1095,” alijibu daktari huyo kitu kilichomfanya Bianca kuanza kuangua kilio mahali hapo.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 100...

Mawingu mazito yakaanza kujikusanya katika anga lote la Dar es Salaam, watu wote waliokuwa njiani kuelekea majumbani mwao wakaanza kufanya haraka kwani dalili zilionyesha kwamba mvua kubwa ingenyesha muda mfupi ujao.

Wale waliokuwa ndani kwa lengo la kutoka, wakavaa makoti yao huku wengine wakichukua miamvuli kwani hali iliyokuwa ikionekana ilimtia hofu kila mmoja na kuhisi kwamba mvua kubwa ambayo haikuwahi kutokea kwa mwaka huo ingeweza kunyesha dakika chache tu zijazo.

Kwa watu waliokuwa wakiishi mabondeni hawakuwa na amani. Waliichukia mvua, kila ilipokuwa ikinyesha, walikuwa wakiweka ndoo katika sehemu ambazo zilipitisha maji huku wengine wakichukua vifaa vya umeme na kuviweka juu ya kitanda kwa kuhofia mafuriko.

Wakati huohuo Malaika alikuwa ndani ya chumba alichokuwa akiishi na Ibrahim. Alikuwa na hofu kubwa, alikuwa na ugonjwa wa Sickle Cell, kila baridi lilipokuwa likipiga alikuwa akihisi maumivu makali katika mifupa yake kitu kilichomnyima raha kabisa na kuhisi kwamba muda wowote ule angeweza kufariki dunia.

Alijikunyata kitandani, alikosa amani, dalili za mvua kubwa iliyotaka kunyesha ikamfanya kukosa raha kabisa. Nyumba ilikuwa sehemu nzuri na waliishi hapo kwa miaka nane lakini bado moyo wake ulikuwa na hofu kubwa.

Moyo wa Ibrahim ulikuwa kwenye maumivu makali, alimfahamu Malaika, alikuwa msichana aliyekuwa kwenye mateso makali hasa katika kipindi cha baridi. Aliumia kila alipokuwa akimuona akilia, wakati mwingine alimlaumu Mungu, kama alikuwa na uwezo wa kufanya uponyaji, kwa nini hakumponya Malaika ili naye awe mzima kama watu wengine?
“Malaika mpenzi!” alimuita mpenzi wake.
“Abee!”

“Ngoja nikuletee shuka jingine!” alisema Ibrahim, akafungua kabati na kutoa shuka moja na kumfunika Malaika kitandani pale.

Msichana huyo akajikunyata, Ibrahim alikuwa pembeni kwenye kiti, hakutoka nje, alibaki akimwangalia mpenzi wake namna alivyojikunyata kitandani pale. Wakati akisikia maumivu makali moyoni mwake kwa kile kilichokuwa kikiendelea, mvua hiyo kubwa ikaanza kunyesha.

Je, nini kitaendelea? Tukutane kesho
 
SEHEMU YA 101...

Hali ya hewa ikabadilika ghafla, joto likamezwa na baridi kali kuanza kupiga. Ingawa Smalaika alijifunika shuka kitandani pale lakini yalishindwa kuzuia baridi kumpiga na kumsababishia maumivu katika mifupa yake.

Akaanza kulia kama mtoto, alisikia maumivu makali mno, maimivu ambayo alikuwa akiyasikia kila siku alipokuwa akihisi baridi kali au ugonjwa huo ulipokuwa ukimkumba ghafla.

Ibrahim akasimama kutoka pale kitini na kumfuata Malaika kitandani pale, alipomfikia, akavua nguo zake na kisha kumfunika msichana huyo. Kwa jinsi alivyokuwa akilalamikia maumivu makali moyo wake ulimuuma, siku zote alitamani kumuona msichana huyo akipona na kuwa mzima kabisa lakini kila alipomuomba Mungu kwa ajili ya kufanya muujiza huo, ilishindikana kabisa.

“Nakufa Ibrahim!” alisema Malaika huku akilia kwa maumivu makali.
“Huwezi kufa! Huwezi kufa mpenzi!” alisema Ibrahim huku akimlalia juu yake kwenye zile nguo kama njia mojawapo ya kumpa joto.

Hakuacha kulia, kadiri muda ulivyokuwa ukizidi kwenda mbele ndivyo ambavyo alihisi maumivu makali. Ibrahim aliogopa, siku hiyo hali ilionekana kuwa tofauti kabisa, msichana huyo alikuwa kwenye maumivu makali kuliko siku nyingine.
Nje kulikuwa na mvua lakini hakutaka kukubali, ilikuwa ni lazima kumtoa msichana huyo na kumpeleka hospitalini. Akamnyanyua kitandani pale, akatoka nje, Malaika aliendelea kulia, kwa jinsi baridi lilivyokuwa likimpiga ndivyo alivyozidi kulia zaidi.

Wakatafuta Bajaj na kumpandisha. Kila neno aliloongea Malaika mahali hapo, alisema kwamba alikuwa akifariki dunia kwani maumivu aliyokuwa nayo kipindi hicho yalikuwa makubwa kiasi kwamba asingeweza kuvumilia hata mara moja.
Bajaj haikuchukua muda mrefu ikafika katika Hospitali ya Mwananyamala na kuanza kutibiwa. Alikuwa kwenye hali mbaya, tatizo alilokuwa nalo lisingeweza kutibika mahali hapo, akatakiwa kuhamishwa na kupelekwa katika Hospitali kubwa ya Moscow Medical iliyokuwa Posta jijini Dar Es Salaam.
“Kwa nini Moscow?” aliuliza Ibrahim.
“Kwa huu ugonjwa ulipofikia, apelekwe huko! Sisi hatuna dawa za kumpa,” alisema daktari huku akimwangalia Ibrahim.

“Ila ile hospitali ni gharama kubwa! Tutaweza kuzimudu?” aliuliza Ibrahim.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 102...

“Nyie nendeni huko tu! Lolote litakalotokea sawa tu! Sidhani kama watakataa kumtibu mtu mwenye hali mbaya kama huyu,” alisema daktari.
Hawakuwa na jinsi, Ibrahim akamchukua Malaika wake na kuondoka hospitalini hapo.

Japokuwa hakukuwa mbali lakini kwa Malaika ilikuwa ni sawa na kutoka Dar mpaka Arusha, aliona kama wanachelewa kufika kwani maumivu aliyokuwa akiyasikia katika mifupa yake hayakuweza kuelezeka.

“Mungu! Kwa nini usiniue! Niue tu nikapumzike! Niue tu kama ulivyomuua mama yako kuliko kunitesa hivi,” alisema Malaika huku akiwa ndani ya Bajaj kuelekea hospitalini.

Hawakuchukua muda mrefu wakafika hospitalini hapo ambapo moja kwa moja Malaika akapeleka katika chumba cha matibabu na kuanza kutibiwa. Muda wote Ibrahim alikuwa nje ya chumba kile, kichwa chake kilikuwa na mawazo mno.

Pale alipokuwa alishindwa kuendelea kukaa kwani muda wote alikuwa akisikia sauti ya kilio kutoka kwa Malaika aliyekuwa ndani ya chumba kile.
Akasimama na kuondoka kwani alizidi kuumia na kuhisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa msichana wake ambaye kila siku kwake alikuwa ni wa thamani kuliko mtu yeyote yule.

Akatoka nje ya hospitali hiyo, akakaa sehemu na kujiinamia, machozi yalikuwa yakimtoka kama mtoto mdogo, pale alipokaa peke yake, akaanza kusikia vishindo vya mtu akija kule alipokuwa.

Akayainua macho yake, akamuona dada mmoja, nesi akitembea kwa mwendo wa harakahara kuelekea sehemu huku akiwa amebeba mtoto. Hakujua nini kilitokea lakini kwa jinsi nesi yule alivyoonekana, alikuwa na hofu, hakujiamini na hata alipokutanisha naye macho, hakuonekana kuwa sawa.

Hakutaka kupuuzia, alipopita, naye akasimama na kuelekea kule alipokwenda nesi yule kwa mwendo wa kunyata. Alitaka kujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mahali hapo.

Akamuona nesi yule akisogea mpaka sehemu fulani iliyokuwa na pipa safi na zuri kisha kumuweka mtoto yule kwa juu huku akiwa amemfunika vizuri. Hapohapo nesi yule akahukua simu, akapiga sehemu na kuanza kuongea na mtu fulani.

Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 103...

“Huku nyuma…ndiyo…kwenye pipa…sawa….usisahau kuniwekea kwenye akaunti ya simu ya namba hii…sawa…tupo wanne…haina shida,” alisema maneno hayo na kisha kukata simu, harakaharaka akaondoka na kumuacha mtoto yule.

Huku akiwa na maswali mengi, akaliona gari moja la kifahari likisimama umbali kama wa mita hamsini, mwanaume mmoja akateremka na kuanza kuelekea kule alipokuwa.

Akagundua kilichokuwa kikiendelea, ilionyesha kwamba mtoto alikuwa ameibwa ndani ya hospitali hiyo na mwanamke huyo ndiyo alikuwa akija kumchukua.

Kwa haraka sana akasimama na kuelekea kule kulipokuwa na mtoto yule, hakutaka kujiuliza maswali, akamchukua na kuanza kukimbia naye kwa machale pasipo kuonekana. Akapita salama getini, tena akisalimiana na walinzi kisha kutokomea zake.
*
*

Hicho kilikuwa kipindi cha huzuni kuliko vyote. Richard na mke wake walibaki wakimwangalia daktari, hawakuamini kile walichoambiwa kwamba walitakiwa kusubiri kwa mwaka mzima ndipo Bianca angepata mimba na kujifungua salama.
Wakaondoka hospitalini hapo wakiwa na huzuni tele, hawakuwa na jinsi, hawakupingana na daktari huyo, kama walivyoambiwa ndivyo walivyotakiw akufanya na hivyo kusubiri.

Siku ziliendelea kukatika, hakukuwa na mtu aliyekuwa na furaha ndani ya nyumba, kila mmoja alionekana kuwa mnyonge, tena katika kipindi kama hicho ambapo ukuta wa kizazi chake ulikuwa umechanika, Richard hakutakiwa kuingiza mbegu ndani ya Bianca kwa kuepuka kumsababisha matatizo makubwa, hivyoo alitakiwa kusubiri.

Siku zilikatika, miezi ikakatika na hatimaye mwaka kukatika. Wakarudi tena kwa daktari yuleyule wa magonjwa ya kinamama na kuzungumza naye, akampima Bianca, ule ukuta wa kizazi uliokuwa umechanika ukarudi katika hali yake ya kawaida na kuambiwa kwamba sasa walitakiwa kutafuta mtoto.

Hiyo ndiyo kazi iliyobaki. Wakajituma usiku na mchana, wala hawakuchukua wiki nyingi, Bianca akaanza kukosa siku zake za mwezi, akampa taarifa mumewe na walipokwenda kupima, akaonekana kuwa mjauzito.

Hicho ndicho walichokuwa wakikihitaji kwa kipindi kirefu, Richard akaanza matunzo mapya, akajitoa mara tatu ya vile alivyojitoa kipindi cha nyuma.
 
SEHEMU YA 104...

Muda huo kila mmoja alikuwa makini, hawakutaka kuona wakimpoteza mtoto kama ilivyokuwa kipindi cha nyuma.
Walitaka kujua jinsi mapema kabisa, baada ya miezi kadhaa wakaenda kupima na kipimo cha Ultra Sound na kuambiwa kwamba Bianca alikuwa na watoto mapacha wa kiume kitu kilichomfanya kila mtu kuwa na furaha.

“Mapacha?” aliuliza Richard.
“Ndiyo! “ alijibu daktari.
“Mungu wangu! Siamini! Mke wangu una watoto mapacha! Mke wangu una watoto mapacha!” alisema Richard, machozi yakaanza kumtoka kwa furaha, alirukaruka kama kichaa, kila alipomwangalia mkewe, alisikia furaha kubwa ambayo hakuwahi kuipata kabla.

Wakaondoka na kurudi nyumbani, waliendelea kufurahia, wakafanya shopping, tena mjini Dubai! Walizunguka sehemu nyingi, mpaka nchini Ufaransa kwa ajili ya kuwanunulia vitu watoto wao.
Bianca alipofikisha miezi nane akapelekwa katika Hospitali ya Moscow Medical Center kwa ajili ya kusubiri hukohuko kwa mwezi mzima, hata akishika uchungu, aushike akiwa hukohuko na si kuanza kukimbizana.

Kila siku Richard akawa na kazi ya kwenda hospitalini hapo kumjulia hali mke wake, alifurahi kila alipokuwa akimwangalia. Aliporudi nyumbani, mawazo yake yalikuwa kwa mkewe lakini zaidi yalikuwa kwa watoto wake mapacha ambao hakuwaona ila aliwasubiri kwa hamu.

“Umezungumza nao?” alisikika daktari mmoja akiuliza.
“Ndiyo! Wamesema wanatoa milioni kumi!”
“Haina shida. Wapange kabisa na walinzi ili mwanaume huyo akitoka na mtoto asiulizwe maswali yoyote yale,” alisema daktari.

“Sawa haina shida!”
Nesi akafanya kama alivyoambiwa, ilikuwa ni lazima waibe mtoto na kumpa bilionea mmoja aliyetafuta mtoto katika maisha yake bila mafanikio. Walinzi wakapangwa na kuahidiwa kupewa pesa, hakukuwa na tatizo lolote lile, na mtoto aliyetakiwa kuibwa alikuwa mmoja kati ya wale wawili ambao alitakiwa kujifungua Bianca.

Mchezo ukaenda kama ulivyotakiwa, Bianca akajifungua huku akiwa hoi, na bila kupima mara ya kwanza asingeweza kujua kama alijifungua mapacha. Akalala kitandani hoi, nesi mmoja akamchukua mtoto mmoja, akatoka naye mlango wa nyuma wakati Bianca akiwa hoi, akaenda naye mpaka nje,
 
SEHEMU YA 105...

Pale alipomuweka kwa ajili ya mwanaume mmoja kuja kumchukua, akamchukua Ibrahim na kuondoka naye, hata alipofika getini, walinzi wakaonekana kutokuwa na hofu, waliambiwa kuhusu mwanaume huyo, hivyo hata walipomuona Ibrahim wakahisi ndiye mwenyewe, wakamsalimia na kutokomea na mtoto huyo.

**** Moyo wa Richard ulikuwa na presha kubwa, pale alipokaa alikuwa akitetemeka kwa furaha, aliikutanisha mikono yake huku akimuomba Mungu, wazazi wake walikuwa pembeni huku wakimtia moyo kwa kumwambia kwamba mkewe angejifungua salama.

Hakutulia kwenye benchi alilokuwa amekaa, wakati mwingine alikuwa akismama na kuzunguka huku na kule, alitaka kusikia sauti ya watoto wake mapacha ambao aliamini kwamba Mungu aliwabariki.

Wala hazikupita dakika nyingi, akasikia sauti ya mtoto ikilia ndani ya chumba kile, akaruka kwa furaha, hatimaye ndoto yake ya kuwa na mtoto akaiona ikiwa imetimia.

Akawakumbatia wazazi wake, alikuwa akilia kwa furaha, hazikupita dakika nyingi mkewe akatolewa ndani ya chumba kile, alikuwa hoi, akapelekwa katika chumba cha mapumziko na kutakiwa kutulia huko.

Richard alibaki akimwangalia mkewe aliyekuwa amelazwa katika machela iliyokuwa ikisukumwa kuelekea katika chumba cha mapumziko. Kwa mbali, japokuwa hakuonekana kuwa na nguvu sana Bianca alikuwa akitabasamu kwa furaha, hakuamini kama alikuwa amejifungua salama kabisa.

Kumuona mkewe haikutosha, akamwambia daktari kwamba alitaka kuwaona watoto wake wa kiume kwani ndicho kitu ambacho alikisubiri kwa miaka mingi sana. Hapohapo daktari akamwambia asubiri katika chumba alicholazwa mkewe huku mtoto alikiandaliwa kwa ajili ya kupelekwa katika chumba cha mama yake.

Hilo halikuwa tatizo, yeye na wazazi wake na wakwe zake wakaondoka na kuelekea katika chumba kile, kila mmoja alionekana kuwa na furaha tele, hawakuamini kama mwisho wa siku walifanikiwa kupata wajukuu.

“Hongera sana mke wangu!” alisema Richard huku akimwangalia mkewe, Bianca aliyekuwa kitandani.
“Nashukuru!” alisema Bianca kwa sauti ndogo.
 
SEHEMU YA 106...

“Nashukuru!” alisema Bianca kwa sauti ndogo.
Wala hazikupita dakika nyingi, mlango ukafunguliwa, nesi mmoja akaingia huku akiwa na mtoto mikononi mwake, alipofika, akamgawia Bianca ambaye akampokea huku akiwa na furaha tele, hakuamini kama mwisho wa siku angekuwa mama.

“Mwingine yupo wapi?” aliuliza Richard huku akiwa na hamu ya kubeba mtoto.
“Mwingine nani?” aliuliza nesi.
“Mtoto!”
“Mbona alijifungua mtoto mmoja,” alisema nesi huyo huku akimwangalia Richard.
“Mtoto mmoja? Kivipi na wakati alikuwa na ujauzito wa mimba ya mapacha?” aliuliza Richard, alishtuka, si yeye tu bali hata wazazi wake walishtuka baada ya kuambiwa kwamba Bianca alijifungua mtoto mmoja.

Richard akahisi kulikuwa na kitu kimetokea, hakuamini kile alichoambiwa, vipimo vyote vya ultra sound alivyokuwa amepiga mke wake vilionyesha kwamba alikuwa na watoto wawili tumboni, sasa ilikuwaje aambiwe kwamba alijifungua mtoto mmoja.

Kwa jicho alilokuwa akimwangalia nesi huyo, akaogopa, akatoka ndani ya chumba hicho kwa lengo la kwenda kumuita daktari mkuu. Richard hakubaki ndani, akatoka huku akiwa na hasira kali, alijua kulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea, alijua dhahiri kwamba madaktari na manesi walicheza mchezo wa kumuibia mtoto mmoja.

“Dokta…” aliita nesi huku akiingia ofisini kwa daktari.
“Kuna nini?” aliuliza daktari.
Richard akaingia ndani ya ofisi hiyo, alikuwa akitetemeka kwa hasira, alimwangalia daktari huku akitaka kujua ukweli juu ya kilichokuwa kikiendelea, alitaka kufahamu mahali mtoto wake mwingine alipokuwa.

Akamwambia daktari kila kitu kwamba alikuwa na uhakika kuwa mkewe alijifungua watoto mapacha kwani vipimo vyote vya ultra sound vilionyesha kwamba alikuwa na ujauzito wa watoto mapacha, sasa iweje aambiwe kwamba alikuwa amejifungua mtoto mmoja.

“Dokta! Ninamtaka mtoto wangu!” alisema Richard, alibadilika, alikuwa na muonekano uliomaanisha kwamba muda wowote ule angeweza kufanya jambo lolote.
“Hebu subiri kwanza!”

“Dokta! Unaniambia nisubiri! Nisubiri nini?” aliuliza Richard, alipoona hiyo haitoshi, akaufunga mlango kwa ufunguo na kisha kuuweka mfukoni, humo ndani walikuwa watatu tu, hapohapo akachomoa bastola yake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 107...

“Nawapeni dakika mbili tu za kujua mahali alipo mtoto wangu mwingine! Vinginevyo nawamaliza wote humu ndani,” alisema Richard huku akiwa ameishika bastola yake.

Alidhamiria kuua, alikwishawahi kusikia namna watoto walivyokuwa wakiibwa hospitalini, hakutaka kuona hilo likimtokea na ndiyo maana alikuwa radhi kufanya jambo lolote lile.

Dokta mkuu hakuwa akijua lolote, alimwangalia Richard, aliogopa kwa kuhisi kwamba kweli mwanaume huyo angeweza kuwapiga risasi mahali hapo. Dokta akamtaka Richard atulie na amsikilize nesi kile alichotaka kukizungumza.

Nesi huyo hakutaka kuzungumza ukweli, alidanganya kwamba Bianc alijifungua mtoto mmoja na si wawili kama alivyosema Richard. Maneno hayo yakamtia hasira zaidi na ili kumuonyeshea kwamba alikasirika, akamnyooshea bastola, pasipo kuvutwa mkono na daktari risasi iliyotoka ingempiga kichwani.

“Paaa!” ulisikika mlio wa risasi ndani ya chumba cha daktari huyo.
“Nawaua wote wawili! Yaani mnanifanyia uhuni na hamjui nilisubiri kwa kipindi gani! Nawaua wote humu ndani,” alisema Richard huku akiikoki bastola yake.
Mlio ule wa risasi ukawashtua watu wengine waliokuwa nje ya chumba kile, haraka sana wanaume wawili wakavunja mlango, wakaingia ndani, wakamkuta Richard akiwa na bastola yake mkononi, alidhamiria kuua kwani kwa uhuni aliokuwa amefanyiwa asingeweza kuuvumilia hata mara moja.

Watu hao wakamuwahi na kumtuliza, kwa hasira alizokuwa nazo akabaki akilia huku akitetemeka, nesi yule akakimbia kwenda kutoa taarifa kwa wenzake kwamba picha ilikuwa imeungua kwani kabla ya kwenda hospitalini hapo tayari mwanaume alijua kwamba mkewe alikuwa na watoto mapacha tumboni.

“Una uhakika?” aliuliza Dk. Massawe ambaye naye alihusika katika wizi wa mtoto huyo kwa lengo la kupata pesa.
“Ndiyo!”
“Hebu wasiliana na Mzee Ngamanywa umwambie kuhusu mtoto,” alisema Dk. Massawe huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Tumwambieje?”

“Amrudishe, tutamtafutia mtoto mwingine,” alisema Dk. Massawe.
Nesi yule akachukua simu yake kwa lengo la kumpigia mzee huyo, kitu cha kwanza kabisa alichokutana nacho ni missed calls zaidi ya kumi kutoka kwa huyo mzee, alichofikiri zilikuwa simu za kumtaka kumshukuru kwa kile alichokuwa amemfanyia.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom