RIWAYA: MSAKO WA MWEHU
MTUNZI: Badi .M. Bao
MAWASILIANO. 0625920847, ( whatsap )
E- mail:
badi.bao11@gmail.com
Dar es Salaam
SEHEMU YA TANO
️[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji737]
Jumamosi nyeusi iliyotanda huzuni
Kulipokucha kila kona ya nchi katika siku hiyo ya Jumamosi gumzo lilikuwa ni tukio la mlipuko wa jana yake kwenye jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani. Magazeti yote yalitoa taarifa ya tukio hilo kwa ufasaha kabisa. Televisheni zote za ndani ya nchi zilisitisha vipindi vya burudani na michezo wakawa wanaripoti juu ya tukio hilo la kishenzi na kinyama mfululizo.
Mpaka kufikia saa sita mchana wa siku hiyo ya Jumamosi ilithibitika watu 50 walifariki dunia huku zaidi ya 100 wakilazwa hospitalini Muhimbili kama wahanga wa kisanga hiko cha kigaidi. Miongoni mwa waliofariki dunia walikuwa ni Mabalozi wote wawili wa Marekani na Canada, pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani. Pia Wabunge 10 nao walipoteza maisha yao, hivyo ilikuwa ni misiba iliyogusa Tanzania nzima. Kama hukufiwa na Mbunge wako, basi utakuwa umepoteza Mjomba, Shangazi, Rafiki, Baba, au Mama ili mradi kila mtu aliguswa kwa namna moja au ingine.
Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Nchi alizungumza mubashara na wananchi kupitia vyombo vya habari vya redio, televisheni na mitandao ya kijamii. Alitangaza maombolezo ya kitaifa ya wiki moja na bendera ya taifa itapepea nusu mlingoti. Pia aliwataka wananchi kuwa watulivu wakati vyombo vya usalama vinawasaka wahusika ili wafikishwe mahakama. Akawahakikishia kuwa serikali yao ipo makini kuhakikisha inavitumia vyombo vyake vya ulinzi na usalama na wananchi kukabiliana na tishio la makundi ya kigaidi dhidi ya Tanzania.
Ikapangwa Ijumaa ijayo kuwa ni ya mazishi ya kitaifa. Ambapo Wabunge waliofariki watapelekwa Dodoma Bungeni kuagwa kwa heshima zote kisha maiti zao zitapelekwa Majimboni kwao kwenda kuzikwa. Miili ya Mabalozi wa Marekani Na Canada ilisafirishwa kwenda nchini kwao kuzikwa. Pia serikali ya Marekani ikawataka raia wake wote waliopo Tanzania warejee nyumbani mara moja mpaka tishio la kigaidi dhidi yao litakapokoma. Wingu jeusi lilitanda katika nchi ya Tanzania kwa upande wa kidiplomasia. Ilishachafuka kimataifa sifa yake ya kuwa kisiwa cha amani na usalama, ikapotea na kuanza kuonekana kuwa sio sehemu salama tena bali ni kisiwa cha mauti na machafuko.
Vyombo vya usalama vilikuwa sasa vinaanza mkesha wa usiku na mchana kwa ajili ya kuwasaka wahusika wa tukio hilo la kigaidi.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji737]
SURA YA NNE
"Magaidi wajianika dhahiri shahiri"
Vyombo vya Dola vilichanganyikiwa havikufahamu lengo la magaidi kufanya shambulio hilo kwa nchi ya Tanzania. Mashushushu wakatawanywa kila mtaa wanahaha na kunusanusa kutafuta penyenye za watu waliokula njama za kulipua mabomu kwenye Jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani, Ijumaa iliyopita.
Ilipofika siku ya Jumapili asubuhi fumbo la makusudio ya shambulio hilo likateguka, likawa hadharani kweupe. Vipeperushi viliokotwa vimesambazwa mitaani maeneo yote ya Jijini kuanzia Posta Mpya mpaka Kariakoo. Mbagala kuu mpaka Bunju, hakuna kichochoro, wala kinjia ambacho vipeperushi hivyo havikufika. Kipeperushi hicho kilisomeka kama ifuatavyo :
"TUNATAKA NCHI YA TANZANIA IKATE MAHUSIANO YA KIDIPLOMASIA NA MAADUI ZETU NCHI YA KENYA MARA MOJA. TUNATOA MUDA WA SIKU TATU TU BALOZI WA TANZANIA AWE AMERUDISHWA TANZANIA, MWISHO JUMATANO IJAYO, VINGINEVYO KISHINDO KINGINE KIKUBWA KINAKUJA MJIANDAE KUCHIMBA MAKABURI MENGI ZAIDI"
احب الحور العين
Ujumbe huo ulioishia na chata ya maandishi ya lugha ya kiarabu ulizusha kizaa upya na kupandikiza hofu mpya miongoni mwa wananchi. Hapo kila mtu akawa anajiuliza "hao walioandaa kipeperushi ni watu gani, mbona hawajajitaja!". Wale watu waoga wenzangu na mimi wakaanza wakakacha kwenda Mjini tena, na wengine wakarudi Mikoani kwao kabisa kupisha upepo mbaya upite.
Magaidi walishafanikisha walichokikusudia, nacho ni kupandikiza hofu na taharuki miongoni mwa wananchi na kudhoofisha uchumi wa nchi. Pia watalii wakaanza kuogopa kuitembelea Tanzania. Kwa watu wa usalama kwao haikuwa shida kutambua kuwa hivyo ni vitisho toka kundi la kigaidi la "Al-shabaab", walihitaji muda tu kuthibitisha dhana yao hiyo. Adui aliyetangaza vita ya hadharani na nchi ya Kenya ni kundi la kigaidi la "Al-shabaab". Kundi hilo lilikuwa linaendesha mapambano ya ulipizaji kisasi dhidi ya Jeshi la Kenya ambalo katika miaka michache iliyopita lilijiunga na "Vikosi vya Umoja wa Afrika" (AMISON) kwa lengo la kuwaondoa wapiganaji wa kundi hilo katika Miji mikubwa na midogo nchini Somalia. Hivyo vipeperushi hivyo sasa vilionyesha "Al-shabaab" wanakusudia kuifanya Kenya ni kisiwa, iwe nchi iliyotengwa na majirani zake wa Afrika Mashariki. Mipango ambayo walijua fika kama itafanikiwa itadhoofisha Umoja wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla. Hivyo kuzima ndoto za viongozi waasisi wa Afrika akina Kwame Nkurumah wa Ghana na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania. Ndoto yao ya kutamani uwepo wa Umoja wa Afrika wenye nguvu ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kila nyanja ya kimaendeleo. Magaidi tayari walileta kishindo cha mtego kilichowanasa wakazi wa Tanzania.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
[emoji3586]Vibaraka wa Al-shabaab wakabidhiwa mikononi mwa Kachero Manu[emoji3586]
Ofisi za Usalama wa Taifa kitengo maalumu cha Ujasusi, zilikuwa zipo katika jengo la "Benjamin William Mkapa Pension Tower" roshani ya tano katika mtaa wa Azikwe. Zamani jengo hili lilikuwa linaitwa "Mafuta House". Zilikuwa ni ofisi za siri ambazo mtu wa kawaida huwezi kujua kazi wanazofanya watu hao. Ilikuwa ni Ofisi yenye Makachero bobezi wasiozidi watano, pamoja na Mkuu wao wa kazi mpya Bwana Omega Mtanika na Katibu Muhtasi wao dada Kokunawa.
Siku hiyo ya Jumatatu asubuhi Makachero wawili 'Manuel Yosepu maarufu kama "Kachero Manu" na Kachero wa kike Yasmine Abeid walikuwa wameitwa ofisini kwa Mudiru wao wa kazi Bwana Omega Mtanika ili wapewe jukumu jipya la kikazi.
Kachero Manu alikuwa ndio kwanza bado mpya mpya hajamaliza hata fungate lake la ndoa aliyoifunga hivi karibuni na mpenzi wake wa siku nyingi, tokea akiwa Chuo Kikuu, Bi Faith Magayane. Alipigiwa simu jana yake Jumapili saa sita mchana, akiwa yupo "Hotel Verde", Zanzibari na Katibu Muhtasi wa Mudiru wake kuwa anatakiwa arudi ofisini mara moja.
Mara baada ya vipeperushi vya magaidi wa "Al-shabaab" kusambazwa kwenye kila kona ya Jiji. Idara ya Usalama wa Taifa ikaona kuna haja ya Jeshi la Polisi kupigwa jeki na Kachero Manu, ambaye ametabahari katika fani ya Ukachero. Maji yalishazidi unga kwa Jeshi la Polisi, mapambano dhidi ya magaidi walio na uthubutu wa kufanya shambulio katika Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Ndani yalikuwa ni mapambano kabambe. Ilikuwa ni patashika ya nguo kuchanika, mtoto hatumwi dukani, ngoma inogile mpaka kieleweke.
Kachero Manu kumuelewesha mkewe kuwa anavunja fungate kwa sababu ameitwa ghafla kazini, ilikuwa ni kazi nzito kueleweka. "Kama kazi yenyewe hiyo ambayo inakukosesha hata muda wa kutulia na mke wako katika kipindi muhimu kama hiki cha fungate bora uache kazi tu. Huu ndio muda adhimu tuliotakiwa kama wanandoa wapya kujenga mustakabali wetu mpya wa namna ya kuendesha maisha yetu" yalikuwa ni maneno makali yaliyoropokwa na mke wa Kachero Manu akiwa amefungwa na joto la hasira kooni mwake.
"Sasa mke wangu nikiacha kazi hii nitafanya kazi gani? " aliuliza Kachero Manu swali la mtego kwa sauti ya kubembeleza huku amemkazia macho mkewe. "Utajiajiri tu, utafute shamba Bagamoyo unalima mbogamboga na matunda na huku unafuga ng'ombe na kuku maisha yatajipa tu" aliweka msisitizo kwa sauti ambayo inaonyesha anamaanisha kile anachokizungumza hatanii japo chembe.
"Mke wangu, uhondo wa ngoma ingia uicheze, usizuzuke na ile michanganuo ya kilimo sijui cha matikiti au ufugaji wa kuku inayokufikia mezani kwako pale benki kwenye idara yako ya mikopo ukajua basi kilimo na ufugaji kinalipa sana.
Michanganuo mingi inakolezwa matokeo kuliko uhalisia ulivyo, mie imani yangu naamini kila Mtanzania mkubwa kwa mtoto ana Diploma ya Usanii hata kama hajasomea sanaa kule chuo cha TASUBA, Bagamoyo. Utaletewa mchanganuo wa kilimo cha matikiti uelezwe ekari moja itakuzalishia milioni sita, lakini ukienda kukifanya hicho kilimo au kuangalia hali halisi ya uchumi wa wakulima hao wa matikiti hauendani na michanganuo yao uliyoisoma. Kilimo na ufugaji Tanzania bado kuna changamoto kubwa ya masoko, bei duni, pembejeo feki, na zinginezo kibao. Labda serikali yetu siku za mbele ije na sera ya kulinda bei ya wakulima wa mbogamboga na matunda na bidhaa za mifugo kama mayai, maziwa na nyama. Vinginevyo bado haujanishawishi mke wangu kucheza pata potea na ya kuacha kibarua changu kinachonipa jeuri Jijini" alimalizia maelezo yake Kachero Manu bila kupindisha maneno kwa mkewe ili kumuweka sawa.
"Mhhh....haya bana ngoja tukomae na ajira za mkoloni za maofisini, ambazo zinatubana mpaka tunashindwa kufurahia maisha ya kifamilia, muda wote tunatenganishwa na majukumu ya kikazi tu" alijisemesha kwa manung'uniko mke wake huku akionekana ameshakubaliana na maelezo ya mumewe kwa shingo upande.
"Magaidi wamelipua Wizara ya Mambo ya Ndani na kusababisha vifo vya viongozi kadhaa, hivyo hamna mtu anaweza kuwafunza adabu magaidi kama mimi serikali ndio imeona hivyo, ngoja nikatoe jasho na damu yangu kwa ajili ya nchi yangu. Nchi ikichezewa na magaidi wakafanya wanavyotaka wao watakuja kutupangia mpaka muda wa kulala na kuamka" aliendelea kukizalendo kwa mkewe ili kumjenga kuwa ameolewa na mpambanaji katika medani za kivita, ambaye anaweza hata kuiacha familia yake miaka miwili mtawalia anaipigania nchi. Alitaka atambue kabisa kuwa hajaolewa na mwanamuziki ambaye anabembeleza mpenziwe kwa nyimbo, vilio na chakula cha nyuki, zawadi ya mauaridi.
Kachero Yasmine Abeid nae alijumuishwa kwenye jukumu hili kutokana na sababu mbili kubwa. Kwanza yeye ndio aliyefanikiwa kuzima mashambulio ya mabomu yenye viashiria vya ugaidi yaliyokuwa yanarindima Zanzibar kila kukicha katika miaka ile ya 2012-2013. Pia alikuwa ni fasaha sana katika bahari ya lugha za Kiarabu na Kisomali, hivyo huenda kuna nyaraka zinaweza kupatikana za siri yeye ndio atakuwa mtarujumani wa lugha kwa Kachero Manu. Alihamishiwa kikazi kuja bara kutokea Zanzibar yapata mwaka na nusu sasa.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji737]