SEHEMU YA 35
Wakati bia mbili, mbili za awali zikipotelea matumboni mwao, huku karanga za kukaangwa zikitafunwa, walikuwa wakiongea hoja hii na ile, hoja za kawaida tu. Ni pale mzunguko wa tatu ulipoingia, ndipo Ndonya alipoikita hoja yake.
Nina suala moja, muhimu ambalo nimependa kuwashirikisha,” alisema huku akiipapasa glasi iliyojaa kinywaji chake. Akawatazama kwa zamu, uso ukiwa unaonesha umakini wa hilo analotaka kulisema. Akaongeza, “Nitahitaji mawazo yenu na ushauti wenu vilevile. Nahisi tutakuwa na mjadala kwa kuwa hamkulitarajia hili ninalotaka kuwaambia.”
***SASA ENDELEA***
Ukimya wa muda mfupi ukatawala, wakitazamana. Kisha Ndonya akaitwaa chupa ya kinywaji na kuipeleka mdomoni. Akanywa funda kubwa na kuirudisha chupa hiyo mezani. Akilini mwake alikuwa akiliwazia hilo analotaka kuwaambia hao wenzake. Aliamini kuwa hataeleweka wala kuaminika. Zaidi, watamchukulia kuwa anawaletea masihara au amechanganyikiwa kutokana na kifo cha kaka yake.
Lakini aliamua kuwa iwe, isiwe, alishapanga kuwa hilo analowashirikisha, kamwe hatalitengua. Wakimhisi kuwa anaanza kuwa chizi ni juu yao. Hajali. Akakohoa kidogo na kujiweka sawa kitini.
“”Kama mnavyojua, msh’kaji wenu sina mke, japo ajira yangu inaniingizia posho ya maana. Tuko pamoja?”
“Tuko pamoja,” Kipini alijibu kwa sauti ilhali Kapamba alitikisa tu kichwa akionesha ishara.
“Wewe Kipini una mtoto, ingawa huna demu mmoja,” Ndonya aliendelea. “Kapamba unaishi na demu, ingawa ni kwa siku moja, moja kama unavyoniambiaga. Mimi sina demu wa kudumu wala sina mtoto. Napaswa kuondokana na hali hii, nijijengee heshima. Tumeelewana hapo?”
“Hiyo ni kweli,” Kapamb aliafiki.
“Huo nd’o ukubwa, kaka,” Kipini naye alisema.
Ndonya alishusha pumzi ndefu na kuwatazama wenzake kwa zamu. Wakati huo alikuwa akipanga namna ya kuiweka hoja yake hadharani. Alitambua fika kuwa wenzake wangehitaji kumjua huyo mke mtarajiwa. Ni hapo ndipo aliamini kungezuka mjadala. Mjadala mkubwa. Wangetaka kujua ni kwa nini kamchagua huyo mke mtarajiwa. Angewatajia bayana sababu ya kumchagua huyo mke mtarajiwa. Ndiyo, angewatajia, lakini ikiwa ni sababu ya kinywani tu, si ya kutoka moyoni.
“Nimewaambia hivyo kwa sababau tayari nimeshayasumbua sana macho na nimeihangaisha akili kumsaka yule ambaye moyo utaridhia kumuoa,” alisema huku akiendelea kuwaangalia kwa zamu, akionesha umakini. Akaendelea, “Nimempata, lakini sijaongea naye chochote. Kama akinikubali, basi sitachukua siku nyingi kabla ya kuwaambia kuwa siku fulani, tarehe fulani, mwezi fulani, mwaka huu, nitakuwa na sherehe ndogo nyumbani kwangu, sherehe ya kumpata mwenza.”
Kipini na Kapamba walitazamana kidogo kisha wote wakamrudia Ndonya.
“Nadhani ni vizuri ukitutajia walao jina na wasifu wake huyo mke mtarajiwa,” Kipini alisema.
“Hilo halina shida,” Ndonyab alisema huku akiitwaa tena chupa ya bia na kuipeleka kinywani. Funda lingine kubwa likapenya kooni. Akasema, “Mtu mwenyewe mnamfahamu sana tu na huenda mkashangaa kusikia nimemchagua yeye.”
“Tunamfahamu?” Kipini alimuuliza huku akimtazama kwa makini.
“Nd’o maana’ake. Mnamfahamu vizuri.”
“Ni nani?” Kapamba alidakia.
“Ni Scola.”
“Scola?” Kipini na Kapamba kwa pamoja wakalitaja jina hilo, macho yao yakiwa yamemganda Ndonya.
“Ndiyo, ni Scolastica Temu,” macho ya Ndonya ni kama yalikuwa yakitoa nuru fulani isiyoelezeka kwa urahisi, akiwatazama wenzake kwa zamu kama anayeyasoma mawazo yao.
Kimya kifupi kikatawala huku Kipini na Kapamba wakimtumbulia macho, wasiiamini kauli yake.
Hatimaye Kipini alikivunja kimya hicho. “Tufafanulie, please. Ni Scolastica Temu gani unayemzungumzia?”
“Wewe unamfahamu yupi au unawafahamu wangapi?”
“Yule malaya,” Kipini alijibu papohapo.
“Malaya?” Ndonya alimkzia macho. “Malaya gani unayemsema wewe?”
“Yule malaya aliyewaua ndugu zetu.”
Ndonya alishusha pumzi ndefu. “Nimekuelewa,” alisema kwa utulivu, macho akiwa ameyagandisha mezani. Kisha akayainua tena na kumwangalia Kipini sawia. “Sikulaumu. Labda una haki ya kumwita hivyo na kumpa sifa hiyo ya umalaya. Lakini pia huenda hastahili kupewa sifa hiyo…”
“Ni malaya tu!” Kapamba naye alidakia. “Kamuua kaka’ako, Machemba. Kawaua na wanaume wengine wawili. Yote hiyo kwa nguvu ya umalaya wake tu!”
“Lakini…” Ndonya alisema.
“Hakuna cha lakini, Ndonya!” Kipini alimkata kauli huku akimtazama sawia, uso kaukunja. “Yule ni malaya tu! Tena malaya mbwa! Yaani kwa hilo mi’ sikuelewi kabisa!”
“Hata mimi sikuelewi msh’kaji!” Kapamba naye alidakia.
Kwa mbali tabasamu likachanua usoni pa Ndonya. “Nilitarajia hoja hii ingegota hapo,” hatimaye alisema huku bado akiachia tabasamu lake dhaifu. “Ninachopenda kuwaambia tu ni kwamba, najisikia kumpenda sana mwanamke yule.”
Ukimya mwingine ulitawala katika meza hiyo. Kisha Kapamba akamwita mhudumu aliyekuwa akitoa huduma kwenye meza nyingine. Mhudumu huyo alipofika aliagizwa pakiti ya sigara na alipoletwa, kitu cha kwanza alichofanya Kapamba ni kuchoma moja na kuiwasha. Pakiti akaiweka mezani.
Kipini naye alikuwa mshirika. Akatwaa moja na kuwasha. Ndonya alikuwa akiperuzi kwenye simu yake. Ukimya huu ulichukua muda mrefu kuliko wakati mwingine tangu wafike hapo.
Mara Kapamba akajitoa kitini. “Mniwie radhi, ngoja nipate akili kidogo,” alisema huku akisogea pembeni na kuvuta sigara kwa mikupuo ya mfululizo, akihakikisha moshi haurejei upande wenye wateja wengine akiwamo Ndonya. Kipini naye alikuwa amejitoa na kwenda upande mwingine.
Dakika kama tatu hivi walirejea mezani huku kila mmoja akimalizia kwa kuupuliza moshi angani.
“Nadhani akili yangu haiko sawa, siamini ninachokisikia toka
kwako,” hatimaye Kapamba alisema huku akiimalizia bia na kusogeza chupa pembeni.
“Ongeza,” Ndonya alimwambia.
“Hapana, labda nipate kitu kikali, kinichangamshe akili,” Kapamba alisema.
“Agiza tu,” aliambiwa.
Muda mfupi baadaye chupa ndogo ya pombe kali ilikuwa imelala mezani hapo baada ya kufunguliwa. Kapamaba alikuwa ameshapiga kiwango kikubwa kidogo cha kinywaji hicho. Akashusha pumzi kwa nguvu. Vitone vya jasho vikajitokeza kwa mbali katik paji lake. Akatwaa leso na kujifuta. Kisha kwa mara nyingine akamimina kinywaji hicho, safari kiwango kidogo tu.
Akairejesha glasi mezani bila ya kunywa tena. Akakiegemea kiti. Akamtazama Ndonya kwa macho makali. Kisha: “ Hivi uko serious, Ndonya?”
“Sina masihara, mjue,” sauti ya Ndonya ilimtoka kwa utulivu na kujiamini.
“Inakuwaje unampenda mtu aliyemuua kaka’ako,” Kapamba sasa alikuwa alikuwa na ujasiri wa kuhoji.
“Unataka kuniambia nilipaswa kumchukia?” uso wa Ndonya, uso ulionawiri kiukwasi, ulikuwa katika mtazamo wa utulivu vilevile, macho yakiendelea kuwatazama rafiki zake kwa zamu.
Kapamba alimtazama Ndonya na kumwona akiwa kawaida, akionekana kutoichukulia taarifa yake kama mzaha. “Sijakuelewa,” alisema huku akiendelea kumtazama.
“Sina sababu ya kumchukia,” Ndonya alisema. “Lakini kama ni wewe ndiye ungekuwa umefanyiwa vile alivyofanyiwa Scola, ungelichukulia poa tu?”
Si Kipini wala Kapamba aliyejibu. Zaidi, waliendelea kumtazama kwa macho yasiyoamini akisemacho.
Ndonya akaendelea, “Uamuzi aliouchukua Scola, unatokana na uchungu wa ukatili aliotendewa. Amedhalilishwa utu wake! Yeyote anayefanyiwa kitendo kile, anaweza kuchukua uamuzi wowote bila ya kujali madhara yake. Na kwa upande mwingine, msinichukulie kuwa nafurahia kuuawa kwa kaka yangu, Machemba. Hapana. Kifo chake kinaniuma sana. Machemba kanilipia karo ya masomo yangu ya uhasibu. Leo napata pesa
kutokana na mkono wake….”
“Huna uchungu wowote, Ndonya!” Kapamba alisema kwa msisitizo, japo sauti yake ilikuwa ya chini. “Nakwambia Ndonya, huna majonzi ya kufiwa na kaka’ako! Labda useme tu unalingine la kutuambia! Zungumza kitu halisi ulichotuitia hapa!”
“Sina lingine la kuwaambia,” Ndonya alijibu haraka kwa msisitizo. “Lingine litoke tena wapi wash’kaji?”
“Una maana umetuita hapa kwa mzaha huo usio na maana?” Kipini alimuuliza.
“Unaweza kuuita mzaha au vyovyote vile,” Ndonya alijibu kwa upole. Hakuonekana kubabaishwa kwa maneno ya wenzake. “Na ninajua itakuwa ni vigumu kwenu kuniamini. Lakini ukweli wangu nd’o huo. Nahitaji kuoa, na mtu pekee ambaye moyo wangu u radhi kwake s’o mwingine zaidi ya Scolastica! Ni huyo tu! Ni yeye pekee!”
Kipini na Kapamba waliguna, wakatazamana kidogo kisha wakamrudia Ndonya.
“Na mimi nakuuliza, uko serious?” Kipini naye akauliza.
“Nd’o maana’ke.”
Kwa mara nyingine Kipini aliguna. Kisha: “Lakini si unajua kuwa Scolastica ana kesi ngumu sana? Na si unajua kuwa huenda mwisho wa kesi ya ukawa mbaya?”
“Hilo pia nalijua vizuri sana.”
“Sasa kama unajua hivyo, kwa nini unatuletea hadithi za kitoto hapa msh’kaji wetu?” kwa mara nyingine Kapamba alizuka tena. “Kwa vyovyote vile mwanamke yule hatanusurika. Huo nd’o ukweli wenyewe. Ni mawili; ama ahukumiwe kifungo cha maisha au atahukumiwa kifo! Unataka kumuoa mwanamke wa kifungwa? Unataka kumuoa mtu anayesubiri hukumu ya kifo?”
Ndonya aliachia tabasamu la mbali huku akitwaa chupa ya bia na kunywa funda moja na kuirudisha mezani. Kisha: Mbona unageuka kuwa jaji mapema hivi, Kapamba? Yaani tayari umemhukumu motto wa watu! Unasahau kuwa yeye sio mhalifu bali ni mtuhumiwa wa uhalifu?”
***ITAENDELEA ***
Sent using
Jamii Forums mobile app