Riwaya: Scolastica Temu

SEHEMU YA 42




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
“Yeye tu,” Latifah alisema kwa majidai na uso wa kujiamini. “Kama atakuwa tayari kukesha itakuwa poa zaidi…pumzi kwangu si tatizo.”
Kapamba na Ndonya wakacheka huku wakimtazama Kipini. Kisha Ndonya akamtazama Kipini na kumwambia, “Kaka, kazi kwako. Unalo hilo. Lakini hakikisheni kesho mnawahi kukanyaga hapa; sawa?”
Tabasamu la mbali likamtoka Kipini.
*****SASA ENDELEA****
SAA tatu asubuhi ya siku iliyofuata, siku ya Jumatano, Ndonya, Kipini, Kapamba na Latifah walikuwa wameketi sebuleni nyumbani kwa Ndonya. Ilikuwa ni siku rasmi ambayo Ndonya alidhamiria kutotimiza azma ya kumwona Scolastica akiwa nje ya Gereza la Keko.
“Naamini kila kitu kiko sawa,” Ndonya alisema huku akiwatazama kwa zamu mmoja baada ya mwingine.
“Tunaweza kudai hivyo,” Kapamba alisema. “Uhakika ni pale huyu Latifah atakapokuwa ameingia Keko na Scola ametoka.”
“Kwani tatizo liko wapi?” Ndonya alikunja uso.
“Mpaka sasa hakuna tatizo lolote,” Kapamba alijibu. “Kumbuka tunapaswa kuwasiliana na yule anti wa gerezani, tupange vya kupangika visivyoweza kupanguka. Tutakapokutana tena hapa, saa sita au saba hivi, tutajua hatua muhimu tuliyofikia.”
Wakati wakiendelea kuongea, mara simu ya Kapamba ikaita. Haraka akaitoa mfukoni na kuitazama. Jina la Maisara lilikuwa likielea kwenye kioo. “Samahani kidogo,” aliwaambia wenzake na kutoka.
Akiwa nje ndipo akabonyeza kitufe cha kupokelea. “Haloo Mai,” alisema kwa sauti ya chini.
"Mambo ni shwari hapa," Maisara alisema kwa utulivu.
"Uko job?"
"Yeah. Na hakuna jipya kwa hiyo ni kama tulivyozungumza."«
"Saa tisa?"
"Ndiyo."
"Poa."
Kapamba akarudi ndani na kuwataarifu wenzake kuhusu makubaliano yake na Maisara. “Kwa hiyo twende na muda. Kwa sasa ngoja nifike home mara moja. Halafu saa nane tukutane hapa.”
*****
KICHWA cha Maisara hakikutulia asubuhi hii. Zile pesa, shilingi milioni thelathini alizowekewa kwenye akaunti yake, benki, hazikuwa za ushindi wa bahati nasibu. Zilikuwa za kumfanya akiuke sheria na kanuni za kazi yake, akiwa ni mwajiriwa wa Jeshi la Magereza. Na katika kuhakikisha hakuna kitakachoharibika katika mpango huo, alijihimu kuripoti ofisini mapema tofauti na siku nyingine.
Baada ya kutekeleza majukumu yake na kukutana na wakuu wake, hakupewa majukumu mengine ya kumfanya atoke nje ya gereza. Ndipo alipoamua kuzungumza na Scolastica kwanza kabla ya kuzungumza na Kapamba. Alitaka ajue ni kwa namna gani Scolastica ataupokea ujumbe huo. Je, atakubali au atakataa?
Alimwita kando na kumwambia, “Sikia Scola, japo siku ulipoingia ulinionesha kiburi, kwa kujifanya chizi, hata hivyo mimi sina kinyongo na wewe. Nimekuita kwa suala moja muhimu na zito. Ni suala linalohusu kesi yako.”
“Kuna nini tena?” Scolastica alimuuliza huku akimkazia macho.
“Usishtuke,” Maisara alimtuliza. “Siyo jambo baya. Ni zuri kwa upande wako japo sijui mwisho wake utakuwaje.”
Ukimya ukachukua nafasi, wakitazamana.
“Maisara, acha kuniweka roho juu,” Scolastica alisema huku akionekana kujawa na tashwishwi. “Ni vizuri ukiwa wazi na kunyoosha maneno yako. N’ambie kuna nini?”
Maisara alishusha pumzi. Akageuka kulia na kushoto, kisha akamrudia Scolastica. “Kuna mpango unaopaswa kutekelezwa leo. Leo hii!”
“Mpango gani?”
“Unatakiwa kuwa huru,” Maisara alishusha zaidi sauti. “Uwe huru leo hii! Umenielewa?”
“Nimekusikia, sijakuelewa,” Scolastica alisema huku kakunja uso, umakini ukiwa umezingatiwa. Alimtazama Maisara bila ya kupepesa.
“Wewe ni msomi, Scola,” Maisara alimwambia huku akiwa amemkazia macho. “Na ni mtuhumiwa wa kesi nzito ya mauaji! Kwa bahati mbaya, ulipobambwa na askari, ulikutwa na chupa ya sumu kali ya PAK mkobani mwako. Sumu ile imepigwa marufuku na serikali. Wewe kwa nini ulikuwa nayo? Na taarifa ya daktari ilithibitisha kuwa marehemu alikufa kwa kuvuta hewa yenye sumu kali.”
Akatulia kidogo kisha akaendelea, “Ile taarifa ya daktari siyo ya kuichukulia kwa uzito wa unyoya. Kaa ukijua hivyo! Pamoja na kwamba umesomea Sheria, na una shahada ya taaluma hiyo, hata hivyo, siioni sababu ya wewe kulichukulia suala hili kama vile kumsukma mlevi aliyechuchumaa. Ni suala zito kuliko unavyoweza kulichukulia. Tambua kuwa kuna wanasheria kama wewe, wenye shahada kama wewe na wengine wanakuzidi. Umenisoma?”
Kama Maisara alitarajia jibu lolote kutoka kinywani mwa Scolastica, haikuwa hivyo. Alichoambulia ni tabasamu la mbali tu, tabasamu ambalo hakubaini kuwa kama lilitoka moyoni au lilikuwa bandia tu.
Akaendelea: "Huwezi kujua, huenda kuna mawakili wengine wanaohangaika kuhakikisha unachukua hukumu ya kifo. Huwezi kujua! Kwa vyovyote, amini usiamini, ndugu wa marehemu, yule uliyekutwa naye chumbani, hawatalichukulia suala hili kama la kawaida. Kwa vyovyote watalivalia njuga! Hata kwa gharama yoyote! Kaa ukijua hivyo Scola!"
Kufikia hapo akatulia tena. Akameza funda la mate huku akitazama pande zote za dunia. Kisha kwa sauti ya chini zaidi, akimtazama Scolastica kwa makini zaidi, akasema, "Leo, leo hii unatakiwa kutoka!"
"Kutoka?"
"Ndiyo! Unaachana na Gereza la Keko! Pia usiwe mtu wa kuhitajika kusimama kizimbani kwa tuhuma yoyote ile, hususan hii ya mauaji. Kwa kifupi unatakiwa kuwa huru. Huru kabisa! Sasa umenielewa?"
"Kwa kiasi fulani nimekuelewa," Scolastica alimjibu. “Lakini nahitaji ufafanuzi zaidi.”
“Ni hivi,” Maisara alisema. "Kuna mtu…kuna mtu amejitolea kwa hali na mali kuhakikisha wewe huendelei kusota rumande. Na siyo kusota rumande tu bali pia kusimama kizimbani. Kwa maana nzuri zaidi, ni kwamba mtu huyo hataki tuhuma dhidi yako ziendelee kuwapo."
Scolastica alishangaa. Hakutarajia kuwa kuna mtu anayeweza kuwa na uchungu kiasi hicho kwa tuhuma zilizomkabili. Alizaliwa peke yake. Hana dada wala kaka. Mama alikwishafariki dunia. Baba hajulikani aliko. Mjomba wake aliyemsomesha, mwaka juzi naye aliaga dunia. Ni nani huyo ambaye hana nasaba naye, akatokea kuubeba huu mzigo mzito? Na ni kwa kigezo gani atakachotumia mtu huyo, kama yupo, cha kumwokoa mtuhumiwa mwenye kesi kubwa kiasi hicho?
Aliamini kuwa uzito wa kesi iliyomkabili, ulihitaji mtu wa karibu, mtu ambaye ama ni shangazi, mjomba, kaka, dada, babu, bibi na kadhalika. Katu haikumwingia akilini kuwa jamaa fulani, wa nyumba ya jirani, au mtu yeyote mwingine, anaweza kuubeba mzigo kama huo.
Ndipo aliporusha swali, “Huyo mtu ni nani?”
“Ni msamaria mwema.”
“Msamaria mwema?! Hana jina?”
“Analo. Lakini si vizuri muda huu kujadili jina au chochote kimhusucho yeyote katika mpango huu. Nitakupa picha kwa kifupi. Ni mwanamume aliyetokea kukupenda sana kwa kiwango kisichokadirika.”
“Ni nani?” Scolastica alionekana kukasirika, akamtazama Maisara kwa namna ya kukerwa na mzunguko wa maneno yake.
“Tulia. Utamjua tu. Yupo mahali fulani, akikusubiri utoke, akakufiche mahali fulani, serikali isitambue kinachoendelea. Unachopaswa kufanya ni kuamua moja; uko tayari kuiacha Keko? Au utaivalia njuga kesi yako, wewe peke yako?”
Scolastica aliwaza kabla ya kutamka chochote. Aliyatambua fika maisha ya kusota rumande. Japo kabla ya mkasa huu hakuwahi kuingia rumande kwa tuhuma yoyote ile, lakini alishawaona watu waliowahi kuchukua siku kadhaa katika maisha ya rumande. Katika kila watu kumi, saba walikuwa wameathiriwa sana na maisha ya huko. Afya zao zilionesha dhahiri kutetereka. Ni kwa rekodi alizonazo, ndiyo maana alipachukulia mahali hapo kama jehanamu.
Ndiyo, alipachukulia kama jehanamu, na kwa maneno haya ya Maisara, hakupenda kuingiza ubishi au udadisi wowote ukerao. Alitambua fika kuwa katika kipindi hiki anachosota rumande, Jeshi la Polisi litakuwa likiendelea na upelelezi wa kina, upelelezi ambao kama utakamilika na ukatoa matokeo ya kumtia hatiani, basi kitakachofuata ni kuongezewa tuhuma nyingine dhidi ya watu wawili; Kibutu na Kisengo. Na itakapothibitika mahakamani kuwa ni yeye aliyezing’oa roho za hao watatu, kitakachofuata ni hukumu nzito, hukumu ya kutisha, hukumu itakayoweza kuung’oa uhai wake kabla hata ya utekelezaji wa hukumu yenyewe.
*****ITAENDELEA JUMATATU.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 43





ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
Ndiyo, alipachukulia kama jehanamu, na kwa maneno haya ya Maisara, hakupenda kuingiza ubishi au udadisi wowote ukerao. Alitambua fika kuwa katika kipindi hiki anachosota rumande, Jeshi la Polisi litakuwa likiendelea na upelelezi wa kina, upelelezi ambao kama utakamilika na ukatoa matokeo ya kumtia hatiani, basi kitakachofuata ni kuongezewa tuhuma nyingine dhidi ya watu wawili; Kibutu na Kisengo. Na itakapothibitika mahakamani kuwa ni yeye aliyezing’oa roho za hao watatu, kitakachofuata ni hukumu nzito, hukumu ya kutisha, hukumu itakayoweza kuung’oa uhai wake kabla hata ya utekelezaji wa hukumu yenyewe.
*****SASA ENDELEA***
Ni hisia hizo zilizomfanya ajikute kwa unyonge akitamka, "Niko radhi kutoka. "Ok, leo mtakapokuwa kwenye kazi za nje, mimi nd’o nitakuwa msimamizi wa kundi utakalokuwamo. Yatakayotokea ndiyo yatakayokupa tiketi ya kuiacha Keko. Umenielewa?"
"Nimekuelewa."
*****
SAA saba mchana, Maisara bado kiroho kikimdunda kwa mbali, alitwaa simu na kumpigia tena Kapamba. Ilipopokelewa akamuuliza, "Kapamaba mko vizuri?"
“Yeah,” Kapmba alijibu kwa kujiamini. Wakati huo ndiyo alikuwa akienda kwa Ndonya. Akaongeza, “Tumejipanga vizuri wala usihofu.”
“Sasa sikia,” Maisara alisema, “Saa tisa hiyo mimi nitakuwa kwenye kundi atakalokuwamo mtu wenu, nikilisimamia. Ukifika utaniona tu. Nadhani ni vizuri mngefika kabla ya saa tisa kwa kuwa mimi nitakuwa pale kuanzia saa nane. Kuwahi ni vizuri
zaidi.”
“Us’jali.”
“Na vipi, mmepata nguo kama ileile kwa asilimia mia moja?”
“Yuko kama alivyo huyo mtu wetu yaani!” Kapamba alijibu kwa kujiamini.
“Ok, hapo sawa.”
Muda ulikwenda, hatimaye kikafikia kipindi kile ambacho moyo wa Maisara ulikosa utulivu. Ilikuwa ni saa nane na dakika kadhaa. Ni wakati huo alipouona ujumbe wa maandishi kwenye simu yake: ‘Tuko njiani tunakuja.’ Ulikuwa ni ujumbe kutoka kwa Kapamba.
Jua kali lililoshusha miali yake ardhini na kuzua joto la kuchusha, lilisababisha Maisara ajikute akijifuta jasho kila baada ya muda mfupi. Jasho hilo lilichanganywa na ukali wa jua, sanjari na mapigo mazito ya moyo, yaliyoambatana na fikra kuhusu mpango uliokuwa ukipaswa kufanyika dakika kadhaa baadaye. Kila baada ya muda mfupi alikuwa akitupa macho kwenye lango kuu la uzio wa gereza.
Ndipo kikafikia kipindi ambacho alikisubri. Moyo ukazidi kumdunda kwa wasiwasi. Akashindwa kuamini kuwa mpango huu utafanikishwa au la. Alimwona Kapamba akiingia ndani ya uzio huo huku akiandamana na mwanamke mrembo aliyevalia gauni jekundu lililomshika mwilini.
Walikuwa wakitembea taratibu, wakionekana kujiamini kwa kiasi kikubwa hali iliyomwondolea wasiwasi Maisara. Sasa naye akashusha pumzi ndefu na kujiwa na hali ya kujiamini.
Akaamini kuwa hakuna litakaloharibika. Akacheka kimoyomoyo kwa furaha. Kicheko cha ushindi. Sasa akawa na imani kuwa zile pesa, shilingi milioni thelathini, zilizotulia ndani ya akaunti yake benki, ni halali yake na anaweza kuzitumia apendavyo.
Kwa kiasi kikubwa, Maisara, katika fikra zake kwa muda huo, alimchukulia Kapamba kama mwanamume asiyekuwa wa kawaida katika utekelezaji wa mipango mikubwa. Kumpata mwanamke mwenye umbo, sura, hata rangi sawa na mtuhumiwa Scolastica Temu, halikuwa jambo ambalo alilitarajia. Huyu mwanamke alifanana na Scolastica Temu kwa asilimia tisini. Hata vazi alilouvika mwili wake, lilikuwa sawa na lile alilovaa Scolastica.
Mara akawaona wamesimama kama wanaosubiri jambo fulani. Walikuwa mithili ya wapenzi fulani walioshibana na hasa ukimtazama na Kapamba aliyetinga suti nyeusi, maridadi iliyompendeza.
Akayahamishia macho yake kwa Scolastica, ambaye wakati huo alikuwa akiendelea kufanya usafi, akiwa hajui kinachoendelea akilini mwa Maisara. Alichokifanya Maisara ni kumwita kando na kumnong’oneza, “Mambo yameiva. Ondoka taratibu hadi kwa wale watu; yule bwana mwenye suti nyeusi na yule mwanamke aliyevaa gauni kama hili lako.” Wakati akisema hivyo, hakutumia ishara yoyote ya mkono, bali macho yalikuwa yamewaganda Latifah na Kapamba ambao nao walikuwa wakimtazama sawia.
Akaendelea, “Usihofu. Tupa fagio hilo hapa chini. Nenda hadi pale. Salimiana nao. Mimi nitakuwa nyuma yako, hatua chache tu, kwa kuwa hatutaki kuvuruga mpangilio. Nitakapofika, nitaondoka na yule mwanamke na wewe utaondoka na yule mkaka. Umenisoma?"
Scolastica aliitika kwa kutikisa kichwa. Kwa jumla akili yake haikuwa imetulia. Mapigo ya moyo wake yaliongeza kasi. Bado aliona hicho ni kama kiinimacho. Lakini akapiga moyo konde na kuanza utekelezaji wa maelekezo ya Maisara. Akavuta hatua taratibu, akimwacha Maisara pamoja na watuhumiwa wenzake ambao hawakujua kinachoendelea.
Kisha tena akasita. Alihisi jasho likimtoka mwili mzima. Akageuka kumtazama Maisara. Akakumbana na macho makali ambayo ni kama yalikuwa yakisema, ‘nenda…unasita nini?’ Kichwani mwake aliona kuwa huu ni mchezo wa kuigiza, mchezo ambao hauwezi kuyabadili maisha yake kuanzia siku hiyo.
Akiwa bado ameduwaa, Maisara alimfuata haraka na kumgusa begani. “Mbona unaduwaa tena?” alimuuliza kwa sauti ya chini. “Jikakamue. Nenda. Na ninakutakia maisha mema. Lakini tusikose kuwasiliana." Akatoa kadi ya simu na kumpatia. "Utakapotulia unipigie kwa namba zilizoko humu. Sawa?"
"Sawa," Scolastica alijibu kwa sauti ya chini, kitetemeshi kikijitokeza kwa mbali. Akageuka tena na kuendelea na safari ya kuwafuata Kapamba na Latifah, safari ambayo bado aliona kuwa ni miongoni mwa viinimacho visivyopendeza.
*****
"SHEM Latifah," Kapamba alimgusa Latifah bega la kushoto. Sasa tuko ukingoni mwa kazi yetu. Huyo dada anayetujia ndiye utakayechukua nafasi yake."
Latifah alishusha pumzi ndefu, akimtazama Scolastica Temu aliyekuwa akiwajia. Akamtazama kwa makini zaidi. Kisha akainamisha uso akiutafakari mfumo mpya wa maisha mapya aliotarajia kuuanza siku hiyo, mfumo uliokuwa hatua chache sana mbele yake.
Alikuwa ni mtu aliyekwishazoea kulala muda aliopenda na kuamka wakati aliotaka. Isitoshe, hakuwa na kawaida ya kula chakula kisichoiridhish
a nafsi yake; kama hakula viazi mbatata kwa nusu kuku, basi alilijaza tumbo kwa biriani iliyotengenezwa kwa ubora wa hali ya juu.
Vinywaji vyake pia vilikuwa ni vile tu vilivyothibitis
hwa ubora na Shirika la Viwango, soda baridi au maziwa ya pakiti huku akitafuna keki au yai la kuchemshwa. Si hayo tu, Latifah, mwanamke mrembo, alishajenga mazoea ya kukumbatiwa na mwanamume yeyote, aliye tayari kutoa chochote ili apate penzi, na hakujali rangi, umri, utaifa wala kabila la mwanamume huyo.
Hayo ndiyo maisha yaliyokwishauteka ubongo wake. Lakini sasa aliyaona kuwa maisha hayoyalimpatia pato dogo la kumfanya aishi kama mwanadamu mwingine yeyote, aishiye maisha ya kati, si zaidi ya hapo.
Shilingi milioni ishirini alizokabidhiwa na Kipini juzi, hazikuwa chache. Katika kazi yake ya kukesha kwenye hoteli kubwakubwa na wakati mwingine kando ya barabara maarufu, akisaka wateja, alifanikiwa kupata pesa, ndiyo. Lakini aliamini kuwa kama angekuwa anarudi nyumbani asubuhi na kitu kama shilingi laki tatu au nne, hapo angenufaika kwa kazi aliyokuwa akiifanya. Hazikufikia kiwango hicho. Leo ana milioni ishirini!
Kipi bora, kukesha ukisaka wanaume na kupata laki moja au chini ya hapo au kubeba kesi isiyo yake, kesi ambayo kuna kufa au kupona? Kichwani mwake aliona kuwa ni bora kubeba kesi. Milioni ishirini zilimtia kiburi. Hakuyajali maisha yatakayomkabili wakati atakapokuwa akiisotea kesi isiyo yake!
Wala hakukisumbua kichwa kwa kufikiria mateso atakayokabiliana nayo endapo jaji atamhukumu kifungo cha maisha. Isitoshe, hakujali kuwa zile milioni ishirini hatazifaidi kama atahukumiwa kifo!
Alikuwa na wazazi na ndugu zake. Wazazi wake waliishi Mbagala Kizuiani. Asubuhi ya siku hii, mara tu alipotoka kwa Ndonya, alikodi teksi hadi huko kwa wazazi wake. Akaonana na mama yake na kumweleza kwa kina kuhusu suala hilo.
Mama yake alishtuka, akashangaa, kisha akapinga. Alimpenda sana Latifah, ingawa alikuwa na watoto wengine wanne wa kiume, waliokuwa wadogo zake Latifah. Huyu Latifah alikuwa tegemeo lake kuu. Alikuwa ni mtoto aliyewajali sana. Hazikuzidi siku tatu bila ya Latifah kufika na kuwapatia pesa za matumizi zisizo haba!
*****ITAENDELEA *****

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 44




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
Mama yake alishtuka, akashangaa, kisha akapinga. Alimpenda sana Latifah, ingawa alikuwa na watoto wengine wanne wa kiume, waliokuwa wadogo zake Latifah. Huyu Latifah alikuwa tegemeo lake kuu. Alikuwa ni mtoto aliyewajali sana. Hazikuzidi siku tatu bila ya Latifah kufika na kuwapatia pesa za matumizi zisizo haba!
***SASA ENDELEA***
Kwa jumla maisha yao yalitegemea mfumo wa maisha ya Latifah. Wadogo zake Latifah kina Mkatamaji, Kiburugwa, Muumini na Lambalamba walikwishatekwa na maisha ya mitaani. Kiburugwa na Mkatamaji walijikita katika uporaji kwenye vichochoro vyenye giza totoro. Muumini na Lambalamba, wao walikuwa wasemaji wakuu katika vijiwe vya kahawa na kubobea katika sekta ya uvutaji bangi.
Hivyo, wazazi wake Latifah walijikuta hawapokei taarifa zozote nzuri kutoka vinywani mwa watu baki kuhusu watoto wao. Wengi waliwajia kwa malalamiko. Mtu mmoja alidai kuwa Lambalamba aliwakera kwa kuvuta bangi nyuma ya nyumba yake. Mwingine alisema kuwa Lambalamba huyohuyo aliapa kutolipa deni la pesa alizodaiwa baada ya kuchukua misokoto kadhaa ya bangi.
Muuza kahawa yeye alimshutumu Muumini kwa kutolipa deni la kahawa aliyowaagizia ‘washkaji’ zake kwa siku tano mfululizo; shilingi elfu tano na mia nane. Mwingine ambaye alikuwa ni Mwenyekiti wa Mtaa, alipeleka malalamiko kwa baba yake Muumini akidai kuwa Muumini kamkashifu kuwa hana ubavu wa kuwamiliki wake zake wawili wa ndoa.
Kulikuwa na idadi kubwa ya watu iliyomlalamikia kuwa wanawe, Kiburugwa na Mkatamaji, ama wamewapora pesa vichochoroni au wamekunywa pombe ya mnazi na kuondoka bila kulipa.
Tabia hizo ziliwafanya wazazi wakate tamaa kwa kiasi fulani. Hawakuwa na matumaini tena ya kusaidiwa na vijana hao. Walimtegemea Latifah pekee, ambaye aliwaletea pesa mara kwa mara.
Wazazi hao hawakujali kuwa binti yao alipata pesa kwa mfumo upi, wao walijali kupata pesa. Siyo kwamba walikuwa gizani kuhusu mfumo wa maisha ya Latifah. La. Walijua kila kitu, lakini hawakujali. Ndiyo maana mama yake hakukubaliana na taarifa hii ya Latifah.
“Tutaishije mwanangu?” aliuliza kwa masikitiko. “Huoni jinsi umri unavyotusogeza kaburini? Wewe ndiye Mungu wetu hapa duniani. Kama utakwenda huko Keko, nani atatulisha hadi mola atakapozitwaa roho zetu?”
Yalikuwa ni maneno yaliyomchoma sana Latifah. Lakini akapiga moyo konde na kusema, "Usihofu, mama. Sitafia huko na wala sitakaa zaidi ya miezi mitatu. Hata hivyo," akasita na kufungua mkoba aliokuja nao. Akatoa mafurushi kadhaa ya noti.
Akamkabidhi mama yake huku akisema, "Hizi zitawasaidia kwa kipindi ambacho sitakuwapo. Naomba mzitumie vizuri kwa sababu kiwango fulani katika hizo nitakitumia kwa kunitoa huko gerezani. Na itabidi mzifiche vizuri mama, hao kaka zangu wasijue kabisa!"
Mama yake aliyapokea mafurushi yale huku mikono ikimtetemeka. Hakuwahi kushika kiasi kikubwa vile cha pesa! Na kwa sauti ileile ya kutetemeka, akasema, "Mwanangu mbona sikuelewi? Hizi pesa zote za nini? Na ni shi’ngapi?"
"Ni shilingi milioni ishirini,"Latifah alijibu. "Hapa nina laki yangu ya kunilinda. Usihofu mama yangu kipenzi. Na hii iwe ni siri yako zaidi mama. Nakuamini zaidi wewe kuliko hata baba. Tunza siri hii. Nitatoka tu, ila hizo pesa zitunze sana. Nadhani hata ikiwezekana baba asijue kuwa unazo.
"Ukiweza zichimbie hata ardhini huko chumbani. Nina hofu baba akijua kuwa una pesa nyingi hivyo ataendekeza kunywa pombe. Nitakupa maagizo mengine ukija kuniona huko rumande. Ila kabla ya kuzichimbia , toa kiasi cha kutosha kwa ajili ya mahitaji yenu. Msishinde njaa eti mnanitunzia pesa zangu. Sawa mama?”
“Nimekusikia, mwanangu.”
*****
“SHEM Scola vipi, huamini kuwa sasa uko huru?” Kapamba alimuuliza Scolastica huku akimgusa begani. Wakati huo teksi ilikuwa katika mwendo wa wastani, zaidi ya mita mia tano kutoka Gereza la Keko. Walikuwa wameketi siti ya nyuma na wakati Kapamba akimuuliza hivyo, alitumia sauti ya chini sana, sauti ambayo haikuyafikia masikio ya dereva.
Scolastica aliguna, akamtazama kidogo kisha akayarejesha macho chini.
“Huamini?”
Sasa macho yao yakagongana. Kapamba akauona mrundikano wa maswali ndani mboni za macho ya Scolastica. Ndani ya maswali hayo yaliyojidhihiri
sha usoni, pia kulikuwa na taswira ya wasiwasi. Scolastica alionesha dhahiri kutoamini kilichotokea wala kumwamini huyu aliye kando yake.
“Usihofu kitu, shemeji,” Kapamba aliendelea. “Najua huelewi kitendawili hiki kilivyoteguliwa. Us’jali, tutakapoteremka nitakusimulia kwa kina.”
Alichokifanya Scolastica ni kukubali kwa kutikisa kichwa tu. Safari ikaendelea huku Kapmaba akiwa ameshazua mazungumzo mengine akimhusisha dereva moja kwa moja.
Safari yao ilikomea Kinondoni, Mtaa wa Kazima, hatua chache kutoka alipoishi Ndonya. Dakika chache baadaye walikuwa sebuleni, ndani ya eneo ambalo Ndonya aliishi kwa mkataba baina yake na mwenye nyumba.
Akiwa sofani, Scolastica Temu hakuchelewa kubaini kuwa
maisha ya mwenyeji wao siyo ya kubahatisha. Picha halisi ilijionesha. Ilikuwa ni sebuleni pana, iliyosheheni samani za kisasa. Wakati akiendelea kuangalia huku na kule, mara akawaona watu wawili wakiingia. Ni Ndonya na Kipini. Hawakuwa ni watu ambao Scolastica aliwafahamu, japo alihisi kuwa sura ya Ndonya haikuwa ngeni sana machoni pake. Ni wapi alipata kumwona? Au anamfananisha na nani? Alijiuliza na akakosa jibu.
Ndonya naye alipomtia machoni Scolastica, moyo ukapiga paa! Mshtuko ambao hata hivyo alijitahidi na akafanikiwa kuuhifadhi moyoni kiasi cha kutobainika kwa yeyote mwingine.
Baada ya kusalimiana, Ndonya akamtazama Kapamba na kisha akaserma, “Kapamba unastahili pongezi kaka. Safi sana.”
Kapamba aliona fahari kuambiwa hivyo. Naye kwa sauti ya majigambo, akasema, “Ni kweli haikuwa kazi ndogo. Lakini ni’shakwambia, kitakachonishin
da hapa Dar ni kuhamisha jengo la ghorofa thelathini na kulisogeza hata umbali wa mita mbili.
Lakini ukiniambia kesho unahitaji kuingia ikulu kuzungumza na rais, n’takuomba uahirishe hadi keshokutwa. Kesho hiyo mimi n’tatengeneza kila kitu na keshokutwa utapita lango kuu la ikulu huku walinzi wa pale wakikupa ‘shikamoo mzee’ kama vile wewe ni mfalme wa nchi moja tajiri duniani uliyekuja katika ziara kwa nchi changa.”
Kipini na Ndonya walicheka, lakini Scolastica hakucheka wala hata kuachia tabasamu la mbali; aliinamisha uso.
“Samahani shem,” Kapamba alisema huku akimgusa bega Scolastica. “Tunajua kuwa bado hujaelewa ni kipi kinachoendelea hadi sasa. Lakini ondoa hofu, ondoa mashaka moyoni mwako…”
Aliizungumza dhamira ya Ndonya. Akaweka bayana kuwa Ndonya katumia zaidi ya milioni sitini katika kuhakikisha suala hilo linakamilika bila ya shida yoyote. Ndiyo, alijitahidi kuzungumza katika namna ya kumtoa wasiwasi Scolastica na kwa kiasi fulani alifanikiwa, lakini hakufanikiwa kuuondoa udadisi uliokuwa moyoni mwake.
Scolastica alikuwa na kitu akilini mwake, kitu kilichomfanya ajikute akijiuliza maswali yalikosa majibu na udadisi aliosita kuuweka bayana kwa watu hao, kwa kile alichoamaini kuwa subira ilihitajika na umakini ulipaswa kuzingatiwa.
Alichofanya sasa baada ya kuyasikiliza haya ‘mashairi’ ya Kapamba, ni kuachia tabasamu la mbali, akiunyanyua uso na kuwatazama kwa zamu bila ya kuonesha woga wala chochote cha kutia taswira tata usoni pake. Kisha akasema, “Sijui niwashukuru vipi. Sidhani kama shukurani zangu zinaweza kutosha. Ningekuwa tajiri labda ningewapa pesa au magari. Lakini bahati mbaya mimi ni mwanamke hohehahe, nisiye na mbele wala nyuma…”
“Us’jali shem,” Kapamba alimdaka. “Ndugu yetu hahitaji chochote kutoka kwako. Anakuhitaji wewe. Anahitaji upendo kutoka kwako.” Kisha akamgeukia Ndonya. “Ndugu yetu nadhani sasa tumeutua mzigo. Nadhani ni muda mwafaka wa wewe na sisi tuwasiliane kisha tuachane kwa muda. Unaonaje?”
Ndonya alimwelewa. Hakupenda kupoteza muda. Akaingia chumbani ambako alichukua dakika kama kumi kisha akatoka na fungu la pesa kwenye mfuko. Akaketi na kuliweka mezani. “Hakuna siri baina yetu,” alisema. “Mzigo ni huo hapo. Fanyeni hesabu, mgawane.”
Zilikuwa ni shilingi milioni kumi.
Dakika kama ishirini baadaye, Kapamba na Kipini walikuwa wamenyanyuka vitini wakieleka mlangoni. Lakini kabla hawajatoka, Kapamba aligeuka na kumpungia mkono Scolastica huku akisema, “Shemeji, baadaye.”
*****
‘Shemeji!’ Scolastica aliwaza kwa hasira. Yamekuja vipi haya ya kuitwa ‘shemeji?’ Huyo Ndonya, hii ndiyo mara yake ya kwanza kumtia machoni. Alishangaa. Hata hivyo hakusema chochote. Akatulia aone kipi kitakachoendelea.
Sasa walikuwa wawili tu; yeye na Ndonya. Kimya kifupi kikatawala kati yao, kimya kilichovunjwa na Ndonya aliposema, “Pole sana Scola. Pole kwa matatizo yaliyokupata.”
“Asante,” Scolastica aliitika kwa sauti dhaifu akiyaepuka macho ya Ndonya.
Kilichofuata ni Ndonya kurejea yale yaliyosemwa na Kapamba, safari hii akiongezea viungo kadhaa katika kuhakikisha Scolastica anamwamini kwa asilimia mia moja. Lakini katika maneno yake, hakudiriki kumtamkia kuwa ana nia ya kufunga naye ndoa!
Kwa Scolastica yalikuwa ni maelezo yaliyomshangaza. Ni vipi mtu ahangaike kumtoa rumande mwanamke mwenye kesi kubwa kiasi hicho, eti kwa ajili ya mapenzi? Na kwa nini afanye hivyo pasi na hakika ya kupendwa na mwanamke huyo? Yawezekana mwanamume akahangaika, akitumia kiasi kikubwa cha pesa, lakini mwanamke akaja kumkana dakika ya mwisho, tena akiwa huru, uraiani! Atamfanya nini?
****ITAENDELEA****

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 45




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
Kwa Scolastica yalikuwa ni maelezo yaliyomshangaza. Ni vipi mtu ahangaike kumtoa rumande mwanamke mwenye kesi kubwa kiasi hicho, eti kwa ajili ya mapenzi? Na kwa nini afanye hivyo pasi na hakika ya kupendwa na mwanamke huyo? Yawezekana mwanamume akahangaika, akitumia kiasi kikubwa cha pesa, lakini mwanamke akaja kumkana dakika ya mwisho, tena akiwa huru, uraiani! Atamfanya nini?
***SASA ENDELEA***
Aliyawaza hayo huku akiwa ameshaiweka soni pembeni. Akawa akimtazama Ndonya usoni sawia. “Ndonya, hivi ni lini uliniona kwa mara ya kwanza?” hatimaye alimuuliza.
“Kwa nini?”
“Basi tu.”
“Kwa mara ya kwanza ilikuwa mwaka jana.”
“Wapi?”
“Hapahapa Dar.”
“Sehemu gani?”
“Kwani vipi?” Ndonya alishangaa. “Mbona maswali ka’ mahakamani?”
Kwa mara ya pili tangu afike hapo, Scolastica alitabasamu. “Napenda tufahamiane vizuri. Kwa bahati mbaya mimi sijawahi kukuona kabla ya leo. Kwa hiyo nadhani n’na haki ya kukuuliza kwa sababu, kufuatia maelezo yako unahitaji tuwe na uhusiano. Si ndo maana’ake?”
“Yeah. Kwa kweli nimetokea kukupenda sana. Hilo si utani.”
Scolastica bado alihisi kuna jambo ambalo liko gizani. Akaendelea kudadisi. “Sasa kama unanipenda, na unadai kuwa uliniona kwa mara ya kwanza mwaka jana, na unasema uliniona hapahapa Dar, sioni kwa nini ushangae kwa kukuuliza ni sehemu ipi uliyoniona. Dar es Salaam ni kubwa. Hapa tuko Kinondoni. Kuna tegeta, Bunju, Mbagala, Mbezi-Kimara, Mbezi Beach, Kigamboni na kwingineko. Tuko pamoja?”
“Tuko pamoja,” Ndonya alijibu kwa unyonge huku akikisumbua kichwa kufikiria harakaharaka jibu la kumridhisha Scolastica. Hakuwa na uongo wa kuutunga. “Nilikuona hapahapa Kinondoni,” hatimaye alijibu.
Lilikuwa ni jibu lisilokuwa na ukweli hata chembe ndani yake. Si kweli kuwa aliwahi kumwona mahali popote kabla ya tukio la kuuawa kaka yake, Machemba. Alimwona kwa mara ya kwanza siku aliposimamishwa kizimbani, Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu, akikabiliwa na tuhuma ya mauaji.
“Kinondoni pia ni kubwa, Ndonya,” Scolastica alimbana. “Kuna Kinondoni Shamba, Kinondoni Moscow, Biafra, Kwa Manyanya, Mkwajuni na kadhalika. Kinondoni ipi unayosema wewe?”
Ndonya alihisi kukosa pumzi. Alimwona Scolasrica akitumia taaluma yake ya sheria kwa kumbana. Maswali yake yalikuwa ni kero kwa kiasi fulani. Hata hivyo, alitambua fika kuwa hakupaswa kuyaepuka maswali hayo, bali alipaswa kumpa majibu. Na si majibu mradi ni majibu tu, hapana. Yalitakiwa majibu yaliyotulia, majibu yatakayokubalika akilini mwa Scolastica.
“Kinondoni hii pale Kinondoni ‘A’ kwenye kituo cha daladala.,” alijibu huku naye akimtazama Scolastica kwa namna ya kujiamini.
Ulikuwa ni uongo kinywani mwa Ndonya huku ukiwa ni ukweli masikioni na akilini mwa Scolastica. Ni kweli tangu alipoanza kazi serikalini na hatimye kuacha na kuingia kampuni binafsi ya uwakili, usafiri wake ulikuwa ni wa daladala, akipandia na kushukia hapo Kinondoni ‘A’.
“Kumbe?” hatimaye alitamka kwa upole huku akiyaepuka macho ya Ndonya. “Ni kweli. Kile nd’o kituo changu cha kuendea kazini.”
Kicheko cha moyoni kikamtoka Ndonya. Akaona kuwa kaicheza karata yake vizuri. Ujasiri ukamrudia kwa nguvu kubwa. Akaropoka, “Basi tangu nilipokuona siku fulani hivi, nikawa n’na hamu nikuone kila siku. Moyo wangu haukutulia. Nikawa ka’ chizi vile. Asubuhi pwee! Nipo kituoni, mradi tu nikuone.”
Scolastica akainamisha uso kwa soni. Akaachia tabasamu la mbali huku akifinyafinya vidole vya mikononi. Kisha, kwa sauti ya chini, akasema, “Ni kawaida yenu wanaume. Wanaume mna utamaduni wa kutumia lugha laini sana, na kujitia wanyonge sana wakati mnapotafuta kile mnachokihitaji kwa wanawake. Lakini mkishafanikiwa tu, zile sura za kondoo huvuliwa na kunaki na sura halisi, sura za chui au mnyama yeyote hatari.”
Akasita na kuunyanyua uso. Sasa akamtazama Ndonya usoni sawia. Tazama yake ilikuwa ya kujiamini zaidi. Akaendelea, “Kwa jinsi ninavyowajua wanaume, na kwa jinsi ninavyowachukulia, najisikia kutokuwa hata na wazo la kuolewa. Yaliyonikuta ni makubwa na kamwe sitayasahau. Nadhani mwenyewe unayajua, eti?”
Ndonya alitikisa kichwa akiashiria kukataa.
“Hujajua yaliyonikuta kabla sijakamatwa?” Scolastica alimtazama kwa macho makali.
“Kwa kweli sijui,” Ndonya alijibu kwa upole.
“Basi kama hujui, ni kwamba…” akamweleza jinsi alivyotekwa na kubakwa. Lakini hakukiri kuwa vifo vya waliombaka vilimhusu. Akahitimisha maelezo yake kwa kumuuliza, “Kama wewe nd’o ungekuwa mwanamke aliyefanyiwa vile ungewachukulia vipi wanaume nafsini mwako?”
Kichwani mwa Ndonya, swali hilo halikuwa la kujibiwa haraka bila ya kutafakari kwa kina. Scolastica alibakwa, ndio. Kitendo cha ubakaji kinalaaniwa dunia nzima. Jibu ambalo lilistahili hapo ni ‘NINGEWAONA WANAUME WOTE NI MAKATILI NA WAUAJI.’ Angejibu hivyo, lakini hakujibu hivyo. Badala yake jibu lililomtoka ni: “Baadhi yao ningewalaani.”
“Na baadhi yao?”
“Ningewachukulia kama wanaume wenye staha.”
Scolastica akaachia cheko dogo, cheko ambalo halikuwa hata na chembe ya furaha. “Kwa bahati mbaya, mimi na wewe kila mmoja ana moyo wake. Mimi najisikia kumwona kila mwanaume ni mamba mla watu. Ndiyo, kila mwanaume, isipokuwa wewe. Naona wewe uko tofauti na wengi. Labda kati ya wanaume mia moja, wa aina yako hawazidi watano. Huo ni wastani mbaya sana. Umenielewa?”
“Mpaka hapo nimekuelewa,” Ndonya alijibu. Na ninakushukuru sana kwa kutonihusisha na wanaume mafisadi, wakware na mabaradhuli. Kwa mkasa uliokupata, kwa mtu yeyote, tuseme kwa mwanamke yeyote atajisikia vibaya sana kisaikolojia. Pole sana. Na sasa naona nibadili mada. Ndiyo kwanza umetoka Keko. Unaonaje kama utajimwagia maji?”
“S’o mbaya,” Scolastica alijibu. “Lakini nadhani ni vyema kwanza ningefika kwangu. Nina zaidi ya wiki tangu nikamatwe. Sijui hali ya huko. Isitoshe, nguo za kubadili ziko huko.”
“Unataka kwenda kwako?” Ndonya alimshangaa. “Unajiamini vipi kiasi cha kujisikia kwenda kwako mapema hivi? Umesahau kuwa wewe bado ni mtuhumiwa wa kesi ya mauaji?”
“Najua hivyo.”
“Basi, tulia. Tunapaswa kuwa makini Scola.”
“Wasiwasi wako ni kwamba huenda kutakuwa na watu wamekuja kunisaka kwangu?”
“Hilo ni mojawapo.”
“Kwa hiyo ni kwa nini umenitoa Keko na kunileta kwenye maisha
yaliyojaa wasiwasi zaidi?”
“Siyo maisha ya wasiwasi, Scola,” Ndonya alisema kwa sauti ya
kusihi. Kisha akamtazama kwa makini zaidi na kuendelea, “Scola tambua kuwa nimetumia mamilioni ya pesa ili kuhakikisha unatoka kule ‘Jehanamu.’ Sikujali thamani ya pesa, nilijali mapenzi yangu, kwako.
“Na kaa ukijua Tanzania hii ina askari wengi sana. Wengi sana! Kuna wanaovaa magwanda rasmi pale wawapo kazini. Na kuna wale ambao kwa saa ishirini hawavaagi magwanda. Wote hao ni waajiriwa wa Jeshi la Polisi. Pia wapo askari wa kujitolea; wale ambao Jeshi la Polisi huwaita ni RAIA WEMA au Polisi Jamii. Hao huwa macho juu, juu, umbeya umewajaa vinywani mwao. ‘Askari’ hao watakapokuona ukiingia nyumbani kwako, tayari watakuja kama marafiki wema. Watakuuliza vipi kesi imekwisha fasta? Watakuuliza huku wakijua fika kuwa kesi ya mauaji na kama hiyo inayokukabili wewe ni nzito sana. Iweje ukaachiwa ndani ya siku saba tu?
“Watakusumbua kwa vijiswali hivi na vile. Wewe ni binadamu kama binadamu wengine wenye nyama na mifupa. Unaweza kujikuta unatamka chochote kile kinachoweza kuwapatia mwanga fulani. Hicho utakachokosea na kukitamka, huenda ndicho kitawapeleka wambeya hao katika kituo chochote cha polisi na kitakachofuata ni askari kujaa kwako huku wakiwa na kila nyenzo ya kukuzuia kuwatoroka. Fikiria vizuri Scola.”
Scolastica alimwelewa. Akaafiki.
*****
SIKU ya tatu baada ya Scolastica kutoka gerezani Keko, tayari alishayazoea haya makazi mapya. Alishakizoea kitanda na alishamjua Ndonya kimwili. Alichozingatia ni kutoonekana sana hadharani ingawa haikuwezekana kutoonekana kabisa.
Baadhi ya wapangaji wenzake Ndonya, wa kiume, waliobahatika kumwona Scolastica, walidiriki kumtamkia bayana kuwa kachagua mwanamke wa ukweli, mzuri mwenye mvuto mkali.
Kwa wanawake, wao walizua vineno kila walipokuwa wameketi nje wakiongea.
“Anajisikia sana…”
“Anarinia urefu wake…”
“Kalio lake linamtia kiburi…”
“Anajiona kafika…”
Walisema mengi ambayo hakuyafikia masikio ya Scolastica. Yangemfikia vipi ilhali hakuwa na tabia ya kuketi kibarazani na kujumuika nao? Yeye alikuwa na utaratibu wake kila Ndonya alipoondoka asubuhi.
Kwanza ni usafi wa ndani, kisha anaoga na kupata stafutahi. Baada ya hapo anaketi sebuleni kuangalia runinga. Kama ikitokea akawa na jukumu linalomlazimu kutoka nje ya eneo hilo, basi ni pale tu atakapokwenda kwenye duka lililo jirani au kwenye genge la vyakula kuhemea. Na kutokana na risala ya Ndonya, alilazimka kuchukua hadhari kwa kujitanda kanga kichwani, miwani mieusi usoni.
***ITAENDELEA***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 46




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA..
“Anajisikia sana…”
“Anarinia urefu wake…”
“Kalio lake linamtia kiburi…”
“Anajiona kafika…”
Walisema mengi ambayo hakuyafikia masikio ya Scolastica. Yangemfikia vipi ilhali hakuwa na tabia ya kuketi kibarazani na kujumuika nao? Yeye alikuwa na utaratibu wake kila Ndonya alipoondoka asubuhi.
Kwanza ni usafi wa ndani, kisha anaoga na kupata stafutahi. Baada ya hapo anaketi sebuleni kuangalia runinga. Kama ikitokea akawa na jukumu linalomlazimu kutoka nje ya eneo hilo, basi ni pale tu atakapokwenda kwenye duka lililo jirani au kwenye genge la vyakula kuhemea. Na kutokana na risala ya Ndonya, alilazimka kuchukua hadhari kwa kujitanda kanga kichwani, miwani mieusi usoni.
***SASA ENDELEA***
Kwa jumla katika siku hizo tatu hakupata matatizo makubwa. Kwa kuwa Ndonya alikuwa akimwachia pesa za kutosha kila aondokapo asubuhi, ilikuwa ni juu yake kuamua anywe nini na kula nini. Pia alikwishanunuliwa doti tatu za kanga na madera mawili.
Ni huduma hizo zilizofanya ichukuliwe kuwa hakuwa na matatizo makubwa. Hivyo ni dhahiri kuwa kama hakuwa na matatizo makubwa basi matatizo madogo yalikuwapo. Na hayo aliyapata nyakati za usiku na alfajiri. Kwa kuwa alilala hapo kwa mfadhili wake, chumba kimoja, kitanda kimoja, kila usiku na kila alfajiri alilazimika kuuachia mwili wake kufanywa chochote japo moyo haukuridhia.
Hilo lilikuwa ni tatizo ambalo kwa kiasi kikubwa lilimsononesha. Kuparamiwa kifuani kila alfajiri na kushinikizwa kulala kifudifudi kila kuchwapo, kwake ilikuwa ni adha, zaidi ya adha za rumande ya Keko gerezani.
Afanye nini? Aliamua kuvuta subira, akiyavumilia mateso hayo
huku akitafuta njia mwafaka wa kupata ufumbuzi. Hakupenda kutumia pupa. Alitambua fika kuwa pupa ya aina yoyote, itatoa matokeo mabaya, matokeo atakayoyajutia mbeleni.
*****
ASUBUHI hii, Ndonya akiwa ofisini mwake, hakujishughulisha hata kufanya chochote cha kikazi baada ya kuwasha kompyuta
yake. Zaidi, alijikuta akicheza gemu huku mawazo yakiwa mbali. Akili ilikuwa nyumbani kwake, akimfikiria Scolastica na vituko vyake vya chumbani.
‘Ni mwanamke wa ajabu!’ aliwaza. Hakumbuki ni mwanamke gani aliyewahi kufikia kiwango cha vituko vya faragha kama
alivyo Scolastica Temu. Akajenga hisia kuwa yawezekana huko Chuo Kikuu cha Makerere hakutoka na shahada ya sheria pekee, bali pia alitunukiwa shahada ya mapenzi. Hakuwa ni mwanamke wa kumfanya mwanamume rijali auone usiku unachelewa kutokomea au kumfikiria mwanamke mwingine, huku wakiwa kwenye kilele cha starehe.
Huyu alikuwa ni mwanamke mwenye ziada ya yale wayafanyayo wanawake wengine. Kama ataolewa, na siku moja mumewe akamfumania na mwanamume mwingine kitandani, bado itamwia vigumu mume kuchukua uamuzi wa kumtaliki.
Mara kwa mara, kwa siku zilizopita, Ndonya alikuwa akiwasikia wanaume kadhaa wakidai kuwa mwanamke mrembo sana hadharani ni mbumbumbu wa kutisha kitandani. Baadhi ya wanawake waliodaiwa kuwa na mvuto wa mapenzi machoni mwa wanaume ni weupe wa wastani, warefu, macho malegevu, matiti ya wastani, makalio makubwa na miguu iliyonona.
Wengi wa marafiki wa Ndonya waliwapa nafasi za juu kwa ubora wanawake wa aina hiyo. Lakini pia walionesha kutokuwa na imani kuhusu uwezo wao katika nyanja ya mapenzi kivitendo. Mara kwa mara, mwanamke wa aina hiyo atakapopita mbele yao wataropoka, "Hamna kitu pale… "
Ndonya alifikia hatua ya kuziafiki kauli hizo siku alipokumbana na Salma, mwanamke mnene, mrefu na mwenye makalio makubwa. Kila Salma alipopita kwenye kundi la vijana wa kiume au wakware ambao hawakutofautiana rika na baba yake mzazi, masikio yake yalinasa miguno na miluzi ya wazi kutoka vinywani mwao.
Ikatokea siku ambayo Ndonya alimtia machoni mwake. Udenda ukamtoka! Hakumwachia, alimfuatilia hadi akafanikiwa kuzungumza naye katika eneo ambalo lilikuwa uchochoroni. Wakafikia makubaliano.
Usiku wakawa pamoja katika gesti fulani ya uchochoroni. Na ni usiku huohuo ndipo alipoanza kuyaamini yaliyosemwa na rafiki zake. Salma hakuwa na chochote cha ziada kitandani, zaidi ya kutapatapa katika namna iliyozidi kumpunguzia msisimko Ndonya. Kipindi kirefu cha usiku huo, Ndonya alikitumia kwa kukoroma usingizini.
Huyo alikuwa ni Salma, siyo Scolastica Temu. Japo Scolastica aliumbika vizuri, kama walivyo wanawake wengi wenye asili ya Kitutsi, akiwa na sifa zile zilizozungumzwa kuwa ni za wanawake mbumbumbu chumbani, huyu hakuwa hivyo. Utundu wake faraghani uliwaacha mbali wanawake wengine wenye mvuto hadharani.
Kwa Ndonya, usiku wa jana kilifikia kipindi ambacho alikaribia
kumhoji ni wapi alikojifunzia utundu huo. Ni aibu za kiume tu zilizomfanya asite kuhoji.
Hata hivyo, pamoja na kuvutiwa na vituko hivyo, pia kulikuwa na jambo lingine lililomsumbua kichwa. Hakuzisahau milioni zake zilizoteketea katika mkakati wa kumtoa mrembo huyo kule rumande. Hakuzisahau na asingeweza kuzisahau!
Alikumbuka kuwa aliwaahidi rafikize, Kipini na Kapamba kuwa pale Scolastica Temu atakapokuwa katika himaya yake, siku fulani, tarehe fulani, mwezi fulani, mwaka huu, atakuwa na sherehe ndogo nyumbani kwake, sherehe ya kumpata mwenza. Na ili azma hiyo itimie, atalazimka kutumia kiasi kingine cha pesa.
Hii ilikuwa ni siku ya tatu. Je, afanye kama alivyowaahidi? Swali hilo lilimjia kichwani na kupata jibu la papohapo; HAPANA. Ndiyo, aliwaahidi, lakini ahadi hiyo haikuwa sheria. Hata serikali huahidi kutekeleza jambo fulani kwa muda fulani au kufanya jambo fulani mwaka fulani, lakini mwaka huo utafika na kupita bila hata ya sehemu ndogo ya ahadi kutimizwa.
Na atakapozuka mbunge mwenye ‘mdomo mrefu’ kuhoji kuhusu hilo, utaisikia serikali kupitia kwa waziri wa wizara husika ikidai kuwa bado ina mpango kuitimiza ahadi hiyo na kwamba, kutokana na sababu zisizozuilika, utekelezaji uliopaswa kufanyika katika muda uliopangwa awali, uliahirishwa.
Huenda utekelezaji huo ukafanyika baada ya muda fulani, au huenda usifanyike kabisa. Lakini ni mtu gani wa kawaida, atakayebaini kuwa ahadi hiyo ni hewa? Kitabaki ni kitendawili ambacho si lazima kiteguliwe.
Naye Ndonya hakutofautiana na serikali ya nchi yoyote, inayotumia mfumo huo. Akaamua kutowataarifu Kipini na Kapamba kuhusu ahadi yake. Na alikuwa na sababu ya kuchukua uamuzi huo.
Kwanza, alitambua fika kuwa tayari kishatumia gharama kubwa katika operesheni ya kumtoa Scolastica rumande. Pili, si kweli kwamba kitendo cha kuitumia gharama kubwa kiasi kile ilikuwa ni njia ya kuelekea kufanikisha kumuoa. Yeye ni wa kuoa leo? Aoe mapema kiasi hiki na kuwaacha warembo waliotapakaa jijini Dar? Hapana, hakuwa tayari kufanya hivyo.
Alikuwa ni mtu mwenye maradhi ya kupenda wanawake. Scolastica ni miongoni mwa wanawake waliomvutia. Alimpenda na kumtamani. Lakini hakuwa na dhamira ya kumuoa bali kustarehe naye tu!
Hivyo, takriban kila usiku, tangu siku ya kwanza, mwanamume alimkosesha mwanamke usingizi akiwa kama aliyedhamiria kumkomoa. Na huenda alidhamiria kumkomoa, kwa kuwa tayari kichwani alikuwa na lake jambo.
*****
KIFO ni tukio ambalo kila binadamu anapaswa kutambua kuwa litamtokea. Kama ulizaliwa basi kaa ukijua kuwa kuna siku ambayo utakufa. Inadaiwa kuwa tikiti ya kifo cha mtu yeyote hukatwa siku anapotoka tumboni mwa mama yake. Unaweza kufa kwa maradhi yoyote, unaweza kufa kwa ajali safarini, unaweza kufa kwa kipigo ukituhumiwa kutenda uhalifu fulani.
Pia, unaweza kufa kistaaarbu tu, bila ya kusumbua watu; unalala kitandani usiku, usingizi unakupitia, lakini huo unakuwa ni usingizi usio na kikomo.
Hivyo vyote ni vifo. Kiwe ni kifo kilichotokea kwa njia moja au nyingine, bado kitabaki kuwa ni kifo tu. Ndonya alitambua hivyo lakini akilini mwake aliamini kuwa kuna vifo vinavyowapata baadhi ya watu kabla ya siku zao.
***ITAENDELEA***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 47



ILIPOKOMEA...
KIFO ni tukio ambalo kila binadamu anapaswa kutambua kuwa litamtokea. Kama ulizaliwa basi kaa ukijua kuwa kuna siku ambayo utakufa. Inadaiwa kuwa tikiti ya kifo cha mtu yeyote hukatwa siku anapotoka tumboni mwa mama yake. Unaweza kufa kwa maradhi yoyote, unaweza kufa kwa ajali safarini, unaweza kufa kwa kipigo ukituhumiwa kutenda uhalifu fulani.
Pia, unaweza kufa kistaaarbu tu, bila ya kusumbua watu; unalala kitandani usiku, usingizi unakupitia, lakini huo unakuwa ni usingizi usio na kikomo.
Hivyo vyote ni vifo. Kiwe ni kifo kilichotokea kwa njia moja au nyingine, bado kitabaki kuwa ni kifo tu. Ndonya alitambua hivyo lakini akilini mwake aliamini kuwa kuna vifo vinavyowapata baadhi ya watu kabla ya siku zao.
SASA ENDELEA...
KIFO cha kaka yake wa tumbo moja; baba mmoja, mama mmoja, Machemba, hakukichukulia Kama tukio la kawaida, eti kwamba ni kifo kilichomkuta katika siku iliyopangwa na Mungu. Hapana.
Aliamini kuwa Mungu hakuhusika hata chembe na kifo hicho, bali yalitokea makosa fulani kwa watendaji wake, malaika, makosa yaliyosababisha binadamu mmoja wa kike atumike katika kung’oa roho ya Machemba duniani.
Aliamini hivyo, na ni imani hiyo iliyomfanya ajikute akishindwa kufanya kazi zilizomkabili mezani pake asubuhi hii. Badala yake akawa ni mwenye kutafakari hili na kupanga lile, yote hiyo ikiwa ni katika kuhakikisha kuwa anaitekeleza azma yake ambayo sasa ilibaki hatua moja tu, hatua muhimu zaidi iliyopaswa kufanywa kwa umakini wa hali ya juu.
Alikuwa na kitu fulani moyoni, kitu kilichomsukuma asiahirishe au kuvuta subira yoyote katika hatua hii ya mwisho iliyo mbele yake. Na ni kitu hicho kilichomfanya awe ameishaiva mitaa ya Uhindini katikati ya jiji, akipita duka hili na lile, akisaka akitakacho. Robo saa baada ya kuwa katika mchakato huo, akahisi alikuwa akicheza patapotea.
Sasa akaamua kuelekea Hosptali ya Hindu Mandal. Huko akafanikiwa kumwona daktari baada ya kusubiri kwa takriban dakika ishirini katika foleni.
“Dokta, nataka utambue kuwa ujio wangu kwako si kwamba naumwa chochote wala kuhitaji kupima afya,” alimwambia daktari huku akimtazama kwa makini.
“Huna tatizo lolote la kiafya?” Daktari Shivji Singh mwenye asili ya Kiasia alimshangaa.
“Ndiyo, siumwi! Nimekuja kwako kwa suala moja muhimu.”
“Suala gani?”
“Kwa kweli ni suala dogo kulingana na uwezo ulionao katika taaluma yako,” Ndonya alimjenga. “Na kwa upeo wako mkubwa, sidhani kama litakuwa ni suala litakalotuchukulia zaidi ya dakika tano. Sidhani.”
Daktari alimtazama Ndonya kwa makini zaidi, akizidi kumshangaa. Kisha: “Ni kuhusu nini?”
“PAK.”
“PAK?!” Daktari Shivji alimkazia macho.
“Yeah, PAK!” Ndonya alisisitiza.
Daktari aliguna huku akiwa bado amemkazia macho Ndonya. “PAK! Una maana PAK ipi?” hatimaye alimuuliza.
“Sumu!”
“Haa!”daktari alivua miwani na kumtazama Ndonya kwa macho makali zaidi. “PAK! PAK! Ya nini? Unaitaka kweli PAK au unatania?”
“Dokta, sikuja kuleta masihara hapa,” Ndonya alijibu kwa sauti ya chini, lakini ikiwa katika uthabiti uleule.
“Ok, hebu nifahamishe vizuri,” daktari alisema kwa utulivu.
Ndonya hakutishwa wala kubabaishwa na tazama ya daktari huyo. Alichofanya ni kutabasamu kidogo tu kisha akasema, “Kwa kifupi ni kwamba, naihitaji, na n’naitaka sana. Ikiwezekana kama ipo hapa, niondoke nayo.”
Sasa ilikuwa ni zamu Daktari Shivji kutabasamu. Lakini tabasamu lake nalo halikudumu zaidi ya sekunde tano. Kicheko hafifu kikamtoka. “Kwa kweli nisikudanganye,” hatimaye alisema. “Tangu niianze kazi hii rasmi kwa cheti cha udokta nilichokipata Humburg, Ujerumani, sijawahi kukutana na mtu wa aina yako.”
“Una maana gani dokta,” Ndonya alimkunjia uso. “Yaani unanichukulia kama punguani, si nd’o maana’ake?”
“Hapana, sina maana hiyo,” daktari alisema kwa upole.
“Una maana gani?”
Kwa mara nyingine, Daktari Shivji Singh, ambaye huu ulikuwa ni mwaka wake wa arobaini na tatu tangu azaliwe, tabasamu changa lilichanua usoni pake. Wakati huo alikuwa akimtazama Ndonya kwa utazamaji wa kawaida ilhali akilini akiona kama anatazama mzimu.
“Kwa kweli sijapata mgeni hapa ofisini, na mgeni huyo akawa akihitaji kitu hatari ka’ hicho,” hatimaye alisema. “Kwani unaifahamu vizuri hiyo PAK unayoitaka?”
“Kwa kiasi tu.”
“Niambie kiwango cha ufahamu wako kuhusu PAK.”
“Ndonya alikohoa kidogo, kikohozi cha kutafuta. “Naijua PAK kama sumu kali kwa kiumbe yeyote.”
“Je, matumizi yake?”
“Hayo siyajui, ndo maana nimekuja kwako dokta.”
Daktari aliangua kicheko kikali na kukikata ghafla. Kisha akasema, “PAK ni sumu, ndiyo. Lakini ukali wa sumu hiyo, siyo ambao wewe unaukadiria. PAK inatisha! Inaua ndani ya sekunde mbili, tatu tu! Siyo sumu ya kutia ndani ya chakula au kinywaji chochote ili iweze kuzua madhara. Hii ni sumu ya kipekee. Ni kiasi cha kuifungua tu chupa, kisha ukasogeza pua na kunusa. Sikufichi, hutavuta pumzi mara tatu!"
Yalikuwa ni maelezo yaliyomwingia Ndonya kwa usahihi. Kwa sekunde chache, wakawa kimya, wakitazamana. Kisha ukimya huo ukavunjwa na Shivji. “Ni kwa nini unaihitaji PAK?” alimuuliza huku akimtazama kwa macho yaliyohoji maswali mengi na hisia tofauti.
“Hilo liko nje ya mipaka yako, ukiwa ni daktari wa hosptali ya ‘private.’ Muhimu kwako ni kunipatia sumu hiyo. Siyo kwamba naomba msaada. Hapana. Pesa ninayo. Sema inauzwa shi’ngapi, tumalize biashara.”
Kimya kingine kilipita, wakitazamana. Hatimaye Shivji akasema, “Ninachojua mimi ni kwamba, PAK ilikuwa ikiuzwa kati ya shilingi elfa hamsini mpaka sitini. Hiyo ni wakati ilipokuwa ikiuzwa kwenye maduka ya dawa kwa uhalali tu kama vile Panadol. Lakini tangu serikali ipige marufuku uingizwaji na uuzwaji wake nchini, kutokana na mauaji yaliyotokea siku za hivi karibuni, sidhani kama sumu hiyo ipo katika duka lolote hapa Tanzania. Na kama ipo, basi itakuwa ikiuzwa kwa uficho mkubwa sana. Si ajabu ukakuta chupa moja inauzwa zaidi la shilingi laki mbili.”
" Kwa hiyo dokta katika hospitali hii hakuna sumu hiyo wala hamjawahi kuwa nayo?"
"Ya nini?" daktari alimaka. "Kazi yetu ni kutoa dawa ya kuponya, siyo sumu ya kuua!"
Ndonya alikunja uso, akihisi kukumbana na kikwazo kisichokwamuka. Kwa hospitali kubwa na maarufu kama hii, hakutarajia kuikosa sumu hiyo. Akawaza, aende wapi. Aende Aga Khan? Aende TMJ? Aende Muhimbili? Au aiache Dar na kuzivamia hospitali za mikoa mingine ? Je, aende KCMC- Moshi? Bugando-Mwanza? Kagondo mkoani Kagera au Nymasovu-Kigoma? Na je, kote huko anakokufikiria, kama atadiriki kwenda, atafanikiwa kuipata PAK?
Jibu lililomjia ni kwamba, atakuwa anacheza bahati nasibu. Japo aliamini kuwa kila penye kuuzwa dawa za kutibu ndipo pia zinapopatikana sumu za kuua, hata hivyo hakuwa radhi kwenda hapa na pale, bila ya kuwa na hakika walao kwa asilimia tisini kuwa atafanikiwa. Hivyo, wazo la ‘kuzitembelea’ hospitali hizo, alilifuta papohapo.
Akamrudia daktari. "Ni maduka gani ambayo kwa hapa Dar yalikuwa yakiuza PAK?"
"Ni mengi tu. Lakini ni yale maduka makubwa tu."
"Ni hayo ninayoyahitaji."
Shivji alicheka kidogo. Kichwani mwake alishajiwa na hisia kuwa huenda huyu ni mmoja wa mashushushu wa serikali. Pamoja na kuwa aliyajua baadhi ya maduka hayo, hata hivyo aliona kuwa kumtajia huyu mgeni wake itakuwa ni kumrahisishia kazi. ‘Kama katumwa, basi asumbuke kidogo ili alipwe mshahara unaomstahili,’ alijisemea kimoyomoyo.
Kwa sauti alisema, "Nilivyokwambia kuwa PAK ilikuwa ikiuzwa katika maduka makubwa, makubwa tu, sikuwa na maana kuwa nayajua maduka hayo. Namaanisha kuwa thamani ya PAK siyo ndogo. Ni vigumu kwa mtu mwenye kijiduka chake cha dawa kule Manzese, kuweka PAK akitarajia kuiuza ndani ya miezi sita."
***ITAENDELEA WIKI IJAYO***

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom