Riwaya: Scolastica Temu

Riwaya: Scolastica Temu

SEHEMU YA 36



ILIPOKOMEA JANA
.“Sasa kama unajua hivyo, kwa nini unatuletea hadithi za kitoto hapa msh’kaji wetu?” kwa mara nyingine Kapamba alizuka tena. “Kwa vyovyote vile mwanamke yule hatanusurika. Huo nd’o ukweli wenyewe. Ni mawili; ama ahukumiwe kifungo cha maisha au atahukumiwa kifo! Unataka kumuoa mwanamke wa kifungwa? Unataka kumuoa mtu anayesubiri hukumu ya kifo?”
Ndonya aliachia tabasamu la mbali huku akitwaa chupa ya bia na kunywa funda moja na kuirudisha mezani. Kisha: Mbona unageuka kuwa jaji mapema hivi, Kapamba? Yaani tayari umemhukumu motto wa watu! Unasahau kuwa yeye sio mhalifu bali ni mtuhumiwa wa uhalifu?”
***SASA ENDELEA***
"Lakini si ameua?” Kapamba alikazia. “Alikamatwa na askari akiwa na chupa ya sumu kali ya PAK. Na hata marehemu Machemba alipopimwa ilithibitika kifo chake kilisababishwa na kuvuta hewa ya yenye sumu kali sana. Huoni mpaka hapo huyo mkeo mtarajiwa kesi imekalia vibaya? Atapona hapo?”
“Sijakataa kuwa alimuua kaka’angu,” Ndonya alijitetea. “Najua ni yeye aliyemuua. Lakini nilichotarajia kutoka kwenu siyo shutuma kwa uamuzi wangu wa kumuoa mtuhumiwa wa kesi nzito ya mauaji wakati siijui hatima ya kesi yenyewe.”
“Ok, tupe stori,” Kipini alisema.
Ndonya aliachia tabasamu huku akikimalizia kinywaji chake na kuisogeza chupa kando. Akatupa macho kwenye meza nyingine iliyokuwa imefikiwa na wateja wawili muda huo. Mhudumu alikuwa akiwasikiliza wateja hao na alipoanza kuondoka alitupa macho kwenye hii meza ya kina Ndonya na walipokutanisha macho, Ndonya akamwashiria kwa mkono aende.
“Ongeza,” Ndonya alimwambia alipowafikia.
“Moja tu?” mhudumu alimuuliza huku akiwa ameishika chupa tupu aliyokuwa Ndonya amemalizia kinywaji chake.
“Tatu kama mwanzo. Wenzangu wanamiksi.”
Mhudumu aliondoka kwa tembea ya kujitupatupa na kuyavuta macho ya Ndonya kwa muda mfupi. Kisha akawarudia wenzake. “Najua ni ka’vile ndoto ya mwendawazimu kutamka kuwa ninataka kumuoa mtuhumiwa wa kesi kubwa ya mauaji,” alisema. “Halafu hata sijaongea naye. Tena mtuhumiwa mwenyewe yuko rumande na dhamana imefungwa. Kwa kweli taswira halisi iliyopo hapo ni kwamba, hilo ni jambo lisilowezekana. Lakini nawaaambia, jambo hilo kwangu linawezekana.”
Kipini na Kapamba waliguna huku sasa kila mmoja akijimiminia kinywaji kile kikali na kunywa kwa mkupuo. Kisha Kapamba akamuuliza, “Litawezekana kivipi?”
“Kwa kumpata mtu atakayechukua nafasi ya Scolastica.”
“Mi’ sijakusoma, ujue,” Kipini alisema.
“Nina maana kuwa,” Ndonya alisisitiza, akiwatazama kwa makini, “italazimu kumpata mtu mwingine atakayechukua nafasi ya Scolastica badala ya huyu tunayemzungumzia.”
Lilikuwa ni tamko ambalo Kipini na Kapamba walilichukulia kama mzaha mwingine wa kitoto. Ukazuka ubishi, Kapamba akimtaka Ndonya aachane na wazo hilo ambalo yeye alilichukulia kuwa ni wazo la kipuuzi. Naye Kipini akadai kuwa hata kama Ndonya hakuwa na masihara katika hiyo hoja yake, hata hivyo utekelezaji wake ulikuwa ni jambo lisilowezekana.
Bado Ndonya alikuwa ngangari. Akasema, “Tatizo lenu nyie mko katika karne ya kumi na tisa. Hii ni karne ya ishirini na moja wash’kaji. Wanadamu wa sasa hawako kizani. Wanadamu wa leo akili zinachemka vilivyo. Kwa sasa hakuna jambo lisilowezekana. Si ajabu baada ya siku utasikia maghorofa yanajengwa huko kwenye sayari ya Mars. Tambueni hivyo.
“Ninaposema hilo ni jambo linalowezekana, mjue nimeshaliwazia na kulitafakari kwa kina kabla sijawashirikisha. Sijakurupuka. Mnachopaswa kujua ni kwamba kila jambo linawezekana kama tu pesa ipo. Mimi ninaamini hivyo. Mipango madhubuti na kutokuwapo kwa uhaba wa fedha ni nyenzo sahihi ya kufanikisha mpango mzito.”
Ukimya ukazuka baada ya mhudumu kuwaletea vinywaji. Alipoondoka, Ndonya akaendelea, “Nimelitoa wazo hilo nikitambua fika kuwa msipolitafakari kwa kina, lazima mtatoa pingamizi kubwa. Lakini tambueni kuwa sikuwa fala tu kuwaambia hivyo. Kama ni pesa, hilo siyo tatizo. Nimeshaweka bajeti ya kukamilisha ishu hiyo. Na mbele ya pesa kwa Tanzania ya leo, Tanzania hii ya karne ya ishirini na moja, lolote linawezekana. Hapa sasa ninachohitaji kwenu ni msaada usiowagharimu mifuko yenu. Hilo tu.”
Akatulia tena, akiwatazama kwa zamu na kubaini kuwa walitekwa na maneno yake. Macho ya Kapamba na Kipini yalikuwa katika mshangao na udadisi. Hilo likampa matumaini kuwa kila alilosema kwa wakati huo lilipenya kwa usahihi vichwani mwao.
“Kuna uwezekano wa kumpata Scolastica Temu bandia?” hatimaye aliwauliza.
Kimya kifupi kikapita, Kipini na Kapamba wakitupiana macho. Kisha Kipini akajibu, “Hilo linawezekana. Lakini ni lazima mtu huyo awe ameshayachoka maisha huru au awe ni mpenzi wa kuishi jela.”
Kapamba aliafiki kwa kutikisa kichwa. Kisha naye akachangia, “Na pia lazima kuwe na makubaliano halisi kati yake, sisi na watu wa gereza la Keko. Hapo ndipo pesa itakapotumika. Na siyo pesa ya kitoto.”
Ndonya hakuoneshwa kushangazwa na kauli ya Kapamba. Alionekana kujiamini kwa kiasi kikubwa. Akagongagonga kidole mezani huku akimtazama Kipini. “Kwa kauli yako unaweza kuifanya kazi hiyo na ukafanikisha?” hatimaye alimuuliza.
“Ipi kati ya hizo mbili?”
“Ya kumpata Scolastica bandia.”
“Inawezekana,” Kipini alijibu kwa kujiamini. “Lakini ni lazima ujipapase mifuko. Nakwenda kuonana naye na anipe hesabu yake kama tutaafikiana.”
“Najua,” Ndonya alikenua meno kidogo, akiachia tabasamu ambalo halikujiweka bayana. “Cha muhimu ni kumpata huyo atakayejitoa mhanga kuchukua nafasi ya Scolastica wangu tangu kukaa rumande hadi kusimama kizimbani. Na ni lazima atambue kuwa lolote linaweza kumkuta mwisho wa kesi hiyo. Huenda mahakama ikamwachia huru, huenda ikamhukumu miaka michache, huenda ikamhukumu kifungo cha maisha na huenda pia ikamhukumu kifo. Atapaswa kutambua hivyo. Huo ndio ukweli!”
“Tunajua hivyo,” Kipini alisema kwa utulivu. “Na ndiyo maana nasema itakupasa ujikamue mifuko kikamilifu. Ubahili weka kando.”
“Mimi sio bahili,” Ndonya alisema akikunja uso kwa mbali. “Ningekuwa bahili nisingewaita na kuwashirikisha ishu hii. Najua fika masuala ya aina hii, hufanikiwa kwa pesa kumwagwa. Kama nilivyowaambia awali, Tanzania ya leo siyo Tanzania ya karne ya kumi na tisa wala karne ya ishirini. Hii ni Tanzania yenye Watanzania wengi ambao wana mipango ya maendeleo yao binafsi. Hao hawajui kutoa huduma kwa wananchi bali kila kitu ni kwa pesa.”
Ukimya mfupi ukatawala mezani hapo. Ni wazi Kipini na Kapamba walikuwa wakimsikiliza zaidi aliyewaalika.
Ndonya akaendelea, “Nimewaita nyie rafiki zangiu wa karibu ili nipate uhakika wa kufanikisha au kutofanikisha suala hilo. Vinginevyo…”
“Ni suala dogo, Ndonya,” Kipini alimkata kauli. “Ni suala ambalo haliwezi kutuchukua hata siku mbili kulikamilisha.”
“Nakuuliza tena, nikikupa kazi hiyo utaiweza?” kwa mara nyingine Ndonya alimuuliza Kipini.
“Kwa nini inishinde? Pesa yako tu.”
“Pesa siyo tatizo,” Ndonya alitamba.
Baada kimya kingine kifupi, Ndonya alimgeukia Kapamba. “Kwa maoni yako una hakika tukiwasiliana na watu wa magereza mambo yatakwenda vizuri?”
Kapamba aliachia kicheko dhaifu, kicheko cha kujiamini. “Kama unavyojua, mimi ni mtoto wa town, kaka,” hatimaye alisema. “Siwezi kushindwa na jambo dogo kama hilo. Lakini kaa ukijua kuwa kuonana na wahusika wa gereza la Keko kwa suala hilo, siyo jambo la kulichukulia kwa uzito mdogo….”
“Hilo pia nalijua,” Ndonya alimkata kauli. “Nauchukulia uzito wa jukumu lako sawa na uzito wa jukumu la Kipini. Kwa kifupi naomba mnifanyie kazi hiyo huku mkijua haki yenu ipo.”
Akayagandisha macho kwa Kipini na kumwambia kwa sauti yenye msisitizo kiasi, “Kipini, fanya kazi ya kumpoata mtu ninayemhitaji. Mtu atakayekuwa Scolastica Temu halisi mbele ya askari polisi na hata jaji. Asiwe na dosari yoyote itakayowafanya watu wa dola wamshtukie na kushuku kuwa wana mtuhumiwa bandia.”
Akatulia kidogo na kumgeukia Kapamba. “Wewe itakubidi usubiri matokeo ya jukumu la Kipini. Sawa?”
“Poa, tu,” Kapamba alijibu.
***ITAENDELEA***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 37




TULIPOKOMEA


Akayagandisha macho kwa Kipini na kumwambia kwa sauti yenye msisitizo kiasi, “Kipini, fanya kazi ya kumpoata mtu ninayemhitaji. Mtu atakayekuwa Scolastica Temu halisi mbele ya askari polisi na hata jaji. Asiwe na dosari yoyote itakayowafanya watu wa dola wamshtukie na kushuku kuwa wana mtuhumiwa bandia.”
Akatulia kidogo na kumgeukia Kapamba. “Wewe itakubidi usubiri matokeo ya jukumu la Kipini. Sawa?”
“Poa, tu,” Kapamba alijibu.
*****SASA ENDELEA*****
SAA tisa alasiri, siku ya pili baada ya kikao kati ya Kapamba, Kipini na Ndonya, Kipini alikuwa njiani akienda nyumbani kwa Latifah. Kwa jumla baada ya kuulizwa swali lile na Ndonya, kuhusu upatikanaji wa mtu atakayetwaa nafasi ya Scolastica, akili ya Kipini ilihamia kwa mtu mmoja tu papohapo, na aliiamini akili yake. Hakutarajia kushindwa. Mtu mwenyewe ndiye huyo Latifah.
Hakufahamiana na Latifah jana au juzi tu, wala hakuwa akifahaamiana naye kijuujuu. Hapana. Walikuwa na mazoea ya zaidi ya miezi sita.
Kwa mara ya kwanza walikutana usiku mmoja kwenye
makutano ya barabara za Kinondoni na Tunisia, jirani na makaburi ya Kinondoni. Utaratibu wa kuzungukia maeneo wanakojiuza wanawake ulishageuka kawaida kwa Kipini. Kwa usiku huo, alipofika hapo, alikuta wanawake sita wakiwa pamoja. Watano kati yao walimfahamu na kumjua Kipini. Lakini kwa siku hiyo, yeye alivutiwa na huyo mwanamke mwenye sura iliyovutia na umbolililotamanisha. Ilikuwa ni sura ngeni machoni mwake, lakini mradi yuko hapo, ilitosha kutoa taswira kuwa naye yu tayari kwa yeyote, huenda hata kwa lolote.
Waliondoka pamoja na hawakuachana hadi kunakucha. Kuanzia siku hiyo, Kipini akanogewa, Mawasiliano yao yakapanua wigo. Ikawa kila inapotokea Kipini amechelewa kupata pesa hadi usiku ukaingia ndipo akapata, basi atampigia simu ajue yuko ‘viwanja’ na anamfuata hukohuko kwa gari kisha wanakwenda kujichimbia ama chmbani kwa Latifah au gesti.
Kitu ambacho Kipini alimpendea Latifah ni kwamba, pamoja na sura nzuri, umbo lililojengeka katika ubora unaostahili kuyavuta macho ya rijali, pia alikuwa akijua kila kitu pale walipochojoa mavazi yao. Alijua kila kitu! Kila kitu!
Hata hivyo, kumpenda huko hakukuingiza fikra za Kipini katika suala la kumtaka waishi kama mke na mume na siku moja wafunge ndoa. Hilo halikuwamo kabisa akilini mwa Kipini. Alimchukulia kuwa ni malaya. Kamkuta kwenye kundi la malaya wenzake, na alijua siku moja atamwacha aendelee na umalaya wake.
Kwa hoja ya kikao cha jana, alipowaza, aliona kuwa ni huyu mwanamke anayeweza kutwaa nafasi ya Scolastica kule gerezani. Huyu ana urefu kama Scolastica, mzuri kama Scolastica japo hawafanani sura na, ameumbika kama Scolastica kwa asilimia tisini na tano. Na aliamini kuwa mbele ya pesa, Latifah hatakataa.
Hakukisumbua kichwa kumfikiria mwanamke mwingine. Ndipo alasiri hiyo alikuwa kwenye bodaboda akielekea Kinondoni Moscow kwa Latifah. Alipofika alikuta ukimya katika nyumba hiyo chakavu yenye vyumba sita, vinne vya ndani na viwili vya uani. Nyumba iliyokuwa katika msongamano wa nyumba ambazo hazikupangika wala kuwa hata na mitaa ya kueleweka. Latifah aliishi chumba cha uani.
Mlango mkubwa wa mbele ulikuwa wazi, lakini kulikuwa kimya sana. Kama kawaida yake, kabla ya kuingia huko, kwa kuwa hawakuwa na miadi, Kipini aliamua kumpigia kwanza simu. Ikaita kwa muda mfupi na kupokewa.
“Upo nyumbani?” Kipini alimuuliza bila hata kumsabahi.
”Ndiyo.”
“Una mtu?”
“Hamna. Nilikuwa nimelala, nd’o naamka.”
“Ok, nakuja. Niko nje?”
Alikata simu kisha akapita kwenye korido ya nyumba hiyo na kutokea uani ambako alikwenda moja kwa moja hadi kwenye mlango wa chumba cha Latifah. Akagonga mara mbili.
“Ingia.”
Kipini akaingia. Mbele yake macho yakakutana na Latifah akiwa ameuvisha mwili wake kanga moja tu. Wakatazamana na Latifah akaachia lile tabasamu lake lililomwongezea uzuri, huku macho yake yanayotazama zaidi ya utazamaji wa kawaida, yakimpa taswira Kipini kuwa mwanamke huyo anachoamini ni kwamba, ratiba yao ni ileile.
Kipini naye akajikakamua kutabasamu, huku akiurudisha mlango taratibu. Akalifuata sofa kuukuu la karne ya kumi na tisa lililotosha kubeba watu wawili. Akaketi na kushusha pumzi. Akawa akingaza macho huku na kule kama vile ni mgeni wa siku ya kwanza.
Kilikuwa ni chumba kidogo na kisichokuwa na mvuto wa aina yoyote. Kilijua kulitunza joto kali la Dar, kiasi cha kumfanya hata Latifah mwenyewe, akiwa humo havai zaidi ya kanga pekee mwilini, bila hata ya vazi lingine huko ndani.
Kitanda kidogo kilichochoka, nacho kikiwa kimebeba godoro chakavu, lililotandikwa shuka nyeupe ambayo nayo ilikwishaupoteza ung’aavu wake, ni miongoni mwa samani zake zilizomsukumia maisha ndani ya jiji hilo la Dar, tangu alipotoka huko kwao mkoa fulani wa katikati ya nchi.
Sufuria mbili zlizokwishachakazwa na moto wa jiko la ‘mchina’ kwa muda mrefu, vikombe vitatu vya plastiki na glasi moja iliyokuwa jirani na chupa tupu ya bia, vilijumuisha uhalisia wa uduni wa mwanamke huyo mzuri, katika maisha ya kisasa.
Kipini hakushangazwa na hali hiyo. Aliwajua wanawake wengi, warembo wa jijini Dar es Salaam, ambao mitaani huonekana kama malaika kwa jinsi walivyojiremba ilhali vyumbani mwao pakiwa hapatofautiani na dampo. Latifah ni mmojawao. Latifah, ambaye sura yake ilitosha kumfanya mwanamume mwenye mke aitelekeze familia yake. Latifah, ambaye umbo lake liliwafanya baadhi ya madereva wapate ajali, baadhi wakinusurika kutokana tu na kumkodolea macho.
Alipoyahamisha macho kutoka katika ukaguzi wa chumba na kuyapeleka kwa Latifah, akamwona akitandua shuka kitandani, akaitundika kwenye kamba. Kisha akatwaa shuka nyingine kuukuuu zaidi, iliyokuwa ndani ya begi, akaitandika. Alipoona amekamilisha alivyotaka, akaketi kitandani hapo na kubaki akimtazama Kipini. Ni dhahiri alikuwa akimsubiri!
Kwa jinsi alivyoketi hapo kitandani kihasarahasara, akiiachia wazi sehemu kubwa ya mapaja yake manene, na kwa jinsi alivyoyaunda macho kiasi cha kumtia ashiki, hawaa na hanjamu rijali yeyote, angekuwa ni mtu mwingine aliye chumbani humo, angeutumia mwanya huo kwa kutaka kufanya naye mapenzi. Ndiyo, angekuwa mtu mwingine, siye Kipini ambaye si tu kwamba aliifahamu fika tabia ya Latifah, bali pia alishakuwa mteja wake wa kudumu hadi alasiri hii. Alimjua, walijuana!
Latifah hakuwa mtu wa kuambiwa ‘nakupenda.’ Alishajua kupenda, alishajua kupendwa. Raha na karaha za kupenda na kupendwa alizijua fika. Kadiri alivyozidi kukua kiumri na kukomaa kiakili, ndivyo pia mawazo ya kupenda pesa yalivyozidi kuutawala ubongo wake, tofauti kabisa na mapenzi. Matokeo ya kutawaliwa na mawazo hayo, ikawa ni kuishi na mwanamume mmoja kwa kipindi kifupi tu kisha anamtema.
Hatimaye maisha hayo nayo yalimchosha. Usumbufu wa wanaume aliowatema, ambao walijitahidi kumbembeleza kila kukicha, kila kukichwa, ulimfanya achukue uamuzi wa kuzisaka pesa kwa namna isiyomletea lawama wala usumbufu kutoka kwa mwanamume yeyote.
Sasa akawa ni mtu wa kukikimbia chumba chake kila jua lichwapo. Kwake, usiku ukawa ni mchana. Mapato yake yakaongezeka. Ikawa alhamdulilahi, kila aliporejea asubuhi, mkoba wake ulikuwa umesheheni pesa. Na kwa kuwa alijali zaidi pesa, labda kuliko kitu chochote kingine, hakuwa na muda wa kuisumbua akili yake kuhusu usalama wa mwili wake.
Mwanamume aliyehitaji huduma nyeti, zaidi ya huduma ya kawaida, alipaswa kutoa kiwango kikubwa zaidi cha malipo. Kipini alikuwa miongoni mwa wateja waliomkatia dau kubwa kwa minajili ya kupewa huduyma hiyo. Hivyo, alasiri hii, mwanamke alijua tayari pesa imeingia.
“Tia komeo mlangoni,” Kipini aliambiwa.
Labda angeipinga kauli hiyo, lakini akiamini kuwa mambo mazuri hayataki haraka, aliamua kutii. Alipokwishafunga, aligeuka na kumkuta Latifah kishaitupa ile kanga juu ya sofa. Akabaki mtupu kama alivyozaliwa.
Tofauti na wakati alipokuwa akimfuata na kumtangulizia dau nene, jioni hii Kipini hakuonesha kuwa na haraka. Huyu hakuwa Kipini ambaye kwa umbo hilo lililo mbele yake, tayari angekuwa amekwishavikata vifungoi vya shati na kuichana zipu ya suruali yake. Hapana. Huyu alikuwa Kipini mwingine, Kipini ambaye naye alikwishaujua utamu wa pesa na kuipenda ladha yake. Na humo chumbani alikuwa akiziwaza pesa atakazolipwa na Ndonya, baada ya kuitekeleza kazi aliyotumwa. Japo hakuwa akikijua kiasi atakachopata, hata hivyo kwa makadirio ya kichwani aliamini kuwa hakosi chini ya milioni mbili au tatu.
Latifa hakuchelewa kugundua kuwa Kipini alikuwa pale kimwili tu. Akamtazama jinsi alivyoduwaa. Lakini hakupenda kumuuliza chochote, alimfuata na kumkumbatia. “Vua basi,” alimnong’oneza huku akianza kufungua vifungo vya shati.
“Hapana, subiri,” Kipini alimzuia. “Leo nimekuja kivingine, ni zaidi ya yale mambo yetu. Ni suala zito lakini lenye faida kwako. Faida kubwa sana. Sidhani kama utaiacha tenda hiyo nono iliyokujia kama nyota ya jaha.”
Latifah alishtuka, akaitoa mikono shingoni kwa Kipni. Akamtazama kwa mshangao zaidi, huku sasa kaikita mikono kwenye shanga zilizokizingira kiuno chake. “Una maana gani?” hatimaye alimuuliza.
***KIPINI KAJA KUTEKELEZA AGIZO LA NDONYA. ANAKUMBANA NA MTIHANI. JE, ATAUSHINDA MTIHANI HUO?***
***ITAENDELEA KESHO***

Nawatakia sikukuu njema ya Krismasi

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA38



ILIPOKOMEA JANA....
“Hapana, subiri,” Kipini alimzuia. “Leo nimekuja kivingine, ni zaidi ya yale mambo yetu. Ni suala zito lakini lenye faida kwako. Faida kubwa sana. Sidhani kama utaiacha tenda hiyo nono iliyokujia kama nyota ya jaha.”
Latifah alishtuka, akaitoa mikono shingoni kwa Kipni. Akamtazama kwa mshangao zaidi, huku sasa kaikita mikono kwenye shanga zilizokizingira kiuno chake. “Una maana gani?” hatimaye alimuuliza.
***SASA ENDELEA***
Kipini alitabasamu kwa mbali huku akimtazama Latifah usoni. “Unaonaje kama tungeketi tukazungumza kidogo? Nadhani dakika kumi au kumi na tano zitatosha. Haziwezi kuzidi.”
Latifah alionesha kumshangaa Kipini, lakini hakutia neno. Akarudi kitandani na kuketi vilevile mtupu. Kipini naye akaketi kando yake na kuanza kuzungumza lililompeleka hapo. Jambo lililomtatiza kwa wakati huo ni kutojua afanye nini kuhusu kiwango cha malipo yanayostahili kutolewa kwa Latifah. Hakukubaliana rasmi na Ndonya kuwa ni kiasi gani cha fedha atakachopewa Latifah kwa kujitolea mhanga kubeba kesi isiyomhusu.
Hata hivyo, akilini mwa Kipini, aliutambua uzito wa suala hilo. Alimjua Latifah kuwa ni Malaya, lakini pamoja na umalaya wake, si kwamba ni mwendawazimu au taahira. Ni mwanamke mwenye akili zake timamu. Anaijua fedha. Kwa suala kama hilo, ambalo linahusu ama kifungo cha maisha au miaka thelathini au hukumu ya kifo, kwa Latifah hatalichukulia kwa uzito wa kawaida.
Ni hapo ndipo alipoamua mwenyewe kujipangia kiasi cha kumwambia na ampime yeye atasimamamia wapi. Alimweleza kinagaubaga ili asije baadaye kuona kama ameuzwa. Na kwa hakika Latifah alimwelewa vizuri. “Unasemaje?” alimuuliza baada ya kuhitimisha maelezo yake.
Ulikuwa ni mtihani akilini mwa Latifah. Ni kweli alipenda pesa na kiwango alichotajiwa na Kipini kilikuwa kikubwa kikilinganishwa na kile alichopata kutokana na kazi ya kumchojolea mwanamume huyu na yule. Kule alikokesha usiku aliambulia kurudi nyumbani na pesa zisizofikia kiwango hiki alichotajiwa na Kipini.
Mara nyingi alikuwa akitrudi na shilingi laki moja na nusu au chini ya hapo, lakini hazikupungua elfu hamsini.
Kiwango hiki cha Kipini, cha kupewa kwa mara moja kilikuwa ni kikubwa lakini alitambua fika kuwa lazima ajitoe mhanga; akubali kuingia rumande gerezani akiwa ni mtuhumiwa wa kesi ya mauaji.
Hakuwa mbumbumbu, mara kadhaa, akiwa katika msako wa pesa usiku katika barabara za Kinondoni, Oysterbay, Shekilango maeneo ya Corner Bar na kwingineko, aliwahi kutiwa mbaroni na askari wa doria, kisha akafikishwa mahakamani ambako alikosa dhamana. Akatupwa rumande.
Akiwa rumande alikumbana na watuhumiwa kadhaa wa kesi za mauaji, ambao aligundua walikuwa na miaka zaidi ya mitano na kesi zao hazijaisha. Alitambua kuwa mtuhumiwa anaweza kusota rumande kwa takriban miaka kumi kabla ya mahakama haijatoa tamko lolote. Na si ajabu mtuhumiwa kujikuta akihukumiwa kifungo cha maisha kama siyo hukumu ya kifo.
Ni hilo lililomfanya Latifah autafakari uamuzi wa kukubaliana na Kipini. Alitulia akiwaza kwa takriban dakika nzima, kisha akayainua macho na kumtazama Kipini sawia. “Umejipanga vipi kwa ajili ya mimi kujitoa mhanga?” alimuuliza akionekana kuwa makini.
“Kuna milioni zako tano taslimu,” Kipini alijibu, akiwa amekadiria kiwango ambacho hakujua kama Kipini atakubaliana naye na kama Latifah ataafiki.
Hapo ndipo Latifah alipoamua kupiga jiwe. Kwake, milioni tano aliona si lolote si chochote. Kama aliweza kuingiza laki kwa usiku mmoja, ina maana milioni tano ndani ya mwezi mzima alikuwa na uwezo wa kuzipata. Kwa suala hili alikuwa radhi kujitoa mhanga, lakini si kwa kiwango hicho cha pesa.
“Milioni tano?” hatimaye alimuuliza Kipini huku kamkazia macho.
“Ndiyo,” Kipini naye alikazia. “Siyo za mafungu. Unapewa taslimu, kama utakuwa na mtu wa kumwamini unamwachia. Unaweza kuwaachia hata wazazi wako.”
“Lakini si unaujua uzito wa kesi yenyewe?”
“Naujua, nd’o maana nimekutajia kiwango hicho.”
Latifah alibibitua midomo na kusonya. “Siyo kwa pesa hiyo,” hatimaye alisema kwa dharau. “Nakwambia kweli. Hapo unielewe. Chini ya milioni ishirini dili linakufa! Kujitoa mhanga s’o suala la mchezo. Wanaojitoa mhanga kuua halaiki ya watu kwa kujilipua huwa hawalipwagi vihela mbuzi kama hivyo vya nauli ya bodaboda.
“Mimi najitoa mhanga. Huenda kesi ikaniishia kwa kuhukumiwa kifo, hivyo ni bora hata wazazi wangu nisiwaache na maisha duni huku wanajua kabisa nimejitolea kwa ajili yao. Ikibainika kuwa nimehukumiwa kifo baada ya kujitolea kubeba kesi ya malaya mwenzangu, tena kwa senti chache kama hizo, kila mmoja ataicheka maiti yangu! Walahi nakuapia!”
Kipini alikuna kichwa akitafakari. Kwa kiasi fulani aliliona jukumu alilobeba ni zito kuliko lilivyo. Bado akawaza, kiwango hicho Ndonya atakikubali? Na bado yeye Kipini alikuwa akimwona huyu Latifah ndiye aliyestahili kuchukua nafasi ile kutokana na mwonekana wake. Akawaza, ampigie simu Ndonya na kumwambia mhusika amesimamia kiwango gani au aende na jibu moja tu watakapokutana ana kwa ana? Suala la kupiga simu akaliweka pembeni kwanza. Akaamua kuendelea kupambana kuhusu kiwango cha malipo.
“Huna haja ya kukuna kichwa, kukunja uso wala kufikiri sana,” Latifa alikuwa na msimamo. “Huo nd’o ukweli wangu. Kama kweli uko serious na suala hilo, ishirini ziweke mbele, niachane na mambo ya kwenda viwanja. Unajua, Kipini, mimi kwa siku kule viwanja sikosi laki hata laki na nusu. Sura yangu inalipa, umbo langu linalipa. Piga hesabu napata shilingi ngapi. Sasa kama unataka kunipa milioni tano eti nikajitose kwenye kesi yenu, si nitakuwa bwege wa kutupa?”
“Siki’za Latifah,” Kipini alijikakamua. “Usichukulie kuwa kujitosa kwa kesi isiyo yako nd’o umejitupa motoni. Hapana, s’o hivyo! Unaweza kushinda kesi…”
“Weweee!” Latifah alimkata kauli kwa nyodo. “Usiniletee hadithi zako za ‘sungura akasema’ hapa! Mimi ni mtu mzima na nina akili timamu! Siwezi kucheza patapotea kwa suala kama hilo. Umenielewa?”
“Tangu hapo ni’shakuelewa, Latifah,” Kipini alikuwa mpole. “Kama nilivyokwambia awali, suala hili lina mhusika mkuu. Mimi ni mjumbe tu. Aliyenituma kumtafuta mtu wa kujitolea kubeba kesi hiyo ndiye aliyepanga kiwango hicho…”
“Hizo milioni tano?”
“Ndiyo.”
“Upuuzi!” Latifah alitamka kwa dharau, akibibitua tena midomo, akakunja na kuvikunjua vidole vya mkono wa kulia. Mara akajitoa kitandani na kuitwaa kanga, akalisitiri umbo lake ambalo lilikuwa bado tupu. Kisha akamgeukia Kipini na kumwambia, “Sikia, mpigie sasa hivi, umwambie msimamo wangu. Tena weka loud speaker, nisikie kila mnachoongea. Mwambie kabisa, siwezi kuchukua milioni tano kwa kuuza uhai au uhuru wangu wa kuishi kwa vihela mbuzi hivyo. Bila milioni ishirini katafute mwingine na sijui utampata nani labda mbwia unga, teja la kufa mtu lisilojali chochote katika maisha yake.”
Kipini aliwaza kama ampigie Ndonya hapohapo au asubiri wakutane? Bado akaamua kutompigia. Akili yake haikumtuma kuwa kashindwa kumshawishi Latifah. Alihisi mambo yanachelewa tu lakini atatoka hapo ameshinda. Na hakujua kama akimpigia Ndonya hapo na kuanza kuzungumzia suala hilo, wataelewana. Kuna watu hawapendi kuzungumza masuala nyeti kwenye simu. Teknolojia ya udukuzi imeshawazindua.
“Usiwe mkali, Latifah…hili ni suala la maelewano tu…”
“Hapana,” Latifa alimkata kauli. Kisha akiwa bado amesimama, akaendelea, “Samahani, nilitarajia unakuja kama unavyokuja siku zote; badala yake leo unaniletea stori zisizo na kichwa wala miguu. Kama kweli huna masihara, basi na mimi msimamo wangu nd’o huo. Sawa? Zaidi ya hapo, mlango ulioingilia ni huo,” akanyoosha mkono kuelekea mlangoni, “unaweza kufungua komeo na ukatokea hapohapo.”
Kipini aliusoma uso wa Latifah na kugundua kuwa hakuwa mtu wa kupoteza muda. Hakuwa mtu mwenye kuvunmilia mazungumzo ya muda mrefu. Alipenda vitendo, si mazungumzo au mijadala ya muda mrefu. Lakini naye akijiona kuwa ni mwanamume kamili, mwanamume asiyekubali kushindwa, akaamua kutumia kile kiitwacho ‘plan B.’
Akiwa yeye bado kaketi pale kitandani, kwa sauti ya upole, akasema, “Basi tuyaache hayo kwa muda huu. Akachomoa noti moja ya shilingi elfu kumi na nyingine ya elfu kumi na tano, akamnyooshea kumpatia huku akiongeza, “Njoo kwa yale mambo yetu. Au nd’o u’shakasirika?”
Kwa mbali tabasamu likamtoka huku akipokea noti zile. “Haya nd’o mambo,” alisema huku kwa mara ya pili akifungua fundo la kanga na kuitupa sofani.
Muda mfupi baadaye walikuwa katika hatua nyingine, miili yao ikitota jasho, ndani ya chumba hicho kidogo chenye dirisha finyu. Dakika kumi zilipokatika, kila mmoja alikuwa kando akijifuta jasho. Leso ya Kipini ililowa jasho ilhali kanga ya Latifah nayo ilitota. Sasa kila mmoja alikuwa ameshika kipande cha gazeti akijipepea huku akihema kwa nguvu.
Hatimaye wakatazamana kidogo, kabla ya Kipini hajairudia hoja yake. “Kwa hiyo umefikia wapi?”
“Kuhusu?”
“Ishu iliyonileta.”
Latifah alishtuka. Akamtazama Kipini kama atazamaye chochote cha kustaajabisha. Kisha: We’ vipi kwani? Si tayari ni’shakujibu? Kwani hujanielwa tu au unajifanya hamnazo?”
“Nadhani sijakuelewa,” Kipini alisema kwa upole. “Nakupa dakika mbili ufikiri vizuri.”
Latifah aliachia cheko la dhihaka, kisha akasema, “Acha dakika mbili, situmii hata dakika sifuri kufikiri chochote. Huo muda unaopoteza, ungeutumia kwa kuvaa nguo kisha uutazame mlango na kusepa zako.”
Kipini aliona yuko maji ya shingo. Akaamua liwalo na liwe, ampigie simu Ndonya muda huohuo, wajadiliane na kufikia mwafaka ili kama kweli Ndonya hatakubali basi mpango huu kwa Latifah uwe umekwisha. Atafutwe mtu mwingine.
Akaitwaa simu na kulisaka jina la Ndonya. Alipolipata akampigia.
***ITAENDELEA***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 39




ILIPOKOMEA JANA....
Latifah aliachia cheko la dhihaka, kisha akasema, “Acha dakika mbili, situmii hata dakika sifuri kufikiri chochote. Huo muda unaopoteza, ungeutumia kwa kuvaa nguo kisha uutazame mlango na kusepa zako.”
Kipini aliona yuko maji ya shingo. Akaamua liwalo na liwe, ampigie simu Ndonya muda huohuo, wajadiliane na kufikia mwafaka ili kama kweli Ndonya hatakubali basi mpango huu kwa Latifah uwe umekwisha. Atafutwe mtu mwingine.
Akaitwaa simu na kulisaka jina la Ndonya. Alipolipata akampigia.
*****SASA ENDELEA*****
NDONYA alitambua fika kuwa kumshawishi mtu kubeba kesi ya mtu mwingine, iwe ni kesi kubwa au ndogo, siyo jambo rahisi. Ni vigumu kwa mtu mwenye akili timamu kukubali kutwaa mzigo mzito kama huo bila ya makubaliano maalum yenye manufaa kwake.
Ni lazima kutakuwa na makubaliano yanayohusu pesa. Mtu huyo atataka pesa tena siyo pesa kidogo, ni nyingi. Hapo alitambua fika kuwa atapaswa kutokwa na pesa zisizo haba. Suala ni kwamba, je, Kipini atafanikiwa kumpata mlengwa?
Hilo ni moja. La pili lilihusu ushawishi unaoweza kuwafanya askari jela wakubali kumpokea kisirisiri mtuhumiwa bandia na kumwachia mtuhumiwa halisi. Hakutaka kujidanganya kuwa hatua hiyo itamgharimu pesa zaidi. Hakujua ni askari wangapi watakaohusishwa na jambo hilo, lakini aliamini tu kuwa ni lazima pesa atakazotoa huenda zikazidi atakazompa yule atakayejitoa mhanga kuchukua nafasi ya Scolastica Temu.
Hii ikiwa ni siku ya pili baada ya kuzungumza na Kipini na Kapamba kuhusu mpango huo, akiwa nyumbani kwake akiangalia runinga, mara simu yake ikaita. Alipoiangalia kwenye kioo akakuta jina la Kipini likitawala. “Kimejibu?” alijikuta akinong’ona huku akiipokea.
“Haloo,” alisema kwa sauti ya chini.
“Yap, kaka nimefikia hatua nzuri, ila sasa inabidi nikupe taarifa inayobidi unipe jibu,” Kipini alisema.
“Kwanza uko wapi?” Ndonya alimuuliza.
“Niko nyumbani kwa mhusika.”
“Nakusikiliza.”
“Ni kwamba zinatakiwa ishirini.”
“Ishirini… nini? Mkwanja”
“Nd’o mana’ake. Tunaongelea milioni hapo.”
"Dah! Zote hizo?”
“Kaka, ni ishu kubwa ilie. Na nilikwambia kabisa ujipange. Mtu anaweza kuhukumiwa kifo ujue!”
Ukimya ukapita kidogo Ndonya akitafakari. Kisha akaibuka, “Uko naye hapo?”
“Ndiyo. Yupo hapa.”
“Naweza kuongea naye?”
Ukimya ukapita kidogo kisha Kipini akasema, “Huyu hapa.”
Mara sauti ya kike ikapenya sikioni mwa Ndonya, “N’ambie.”
“Dada yangu mbona uko juu sana, punguza kidogo basi.”
“Ni’shamwambia huyu mjumbe wako kuwa haipungui hata shing’ moja,” sauti hiyo ilikuwa ya msisitizo uliomfanya Ndonya auone ugumu wa kuendelea kushawishi.
Kwa mbali Ndonya akaamua kuwa liwalo na liwe. Akasema, “Ok, dada’angu, us’jali. Utakuwa tayari lini?”
“Nyie tu. Mimi hata leo mkinipa mkwanja wangu mambo yanakwenda mnavyotaka.”
“Ok, basi nikiwa tayari jamaa atakutaarifu. Ila jipange ndani ya saa sabini na mbili tunamaliza mchezo. Sawa?”
“Nyie tu, nawaambieni.”
*****
SIKU hiyohiyo, saa mbili usiku, Kapamba alikuwa eneo la Tabata Relini ambako alimfuata askari magereza wa kike aliyeitwa Maisara. Uhusiano kati ya Maisara na Kapamba ulizaliwa katika kipindi ambacho Mwanahamisi, shoga yake Maisara, alikuwa ni hawara wa Kapamba. Ulikuwa ni uhusiano wa kawaida, mtu na shemeji yake. Hata hivyo, baadaye liliibuka penzi la siri baina yao, penzi lililodumu kwa miezi minne tu na kuyeyuka baada ya Maisara kubaini kuwa zaidi ya Mwanahamisi, pia Kapamba kumbe alikuwa na wanawake wengine.
Kuvunjika kwa penzi lao la siri, haikuwa sababu ya kuibua chuki baina yao. Waliendelea kuwasiliana kama kawaida, mara chache Kapamba akimtembelea na kuzungumza naye mazungumzo ya kawaida. Kwa hali hiyo, usiku huu mchanga Kapamba hakuona tabu kufika hapo na kuzungumza naye chochote, japo mazungumzo ya siku hii yalikuwa na umuhimu wake tofauti na siku zingine.
Alimkuta na akamweleza kinagaubaga madhumuni ya huo ujio wake. Naye kama Kipini, alijitahidi kupanga maneno na kuongea kistaarabu zaidi na kwa umakini wa hali ya juu, ili kuhakikisha ushawishi wake unakubalika kichwani mwa Maisara.
Ilikuwa ni hoja nzito sana kwa Maisara. Haikumwingia akilini kuwa suala lililozungumzwa na Kapamba linawezekana kwa namna yoyote ile. Akamtazama Kapamba kwa jicho kali kisha akamwambia, “Ni suala lisilotekelezeka.”
“Kwa nini unasema hivyo, Maisara?” Kapamba alimuuliza. “Kwa dunia ya leo, kwa Tanzania ya leo, kuna jambo lislowezekana mbele ya pesa?”
Maisara akaguna. “Kipi kinakufanya uamini kuwa ni jambo linalowezekana?”
“Kwa kuwa ninazungumza na Maisara, mwanamke wa shoka, mwanamke mwenye akili iliyojitosheleza, asiye mwoga na anayejitambua. Siamini kuwa bhiyo ni kazi inayoweza kukushinda. Natambua jinsi ulivyo makini.”
Ukimya ukatawala kwa muda. Yale maneno ya kapamba aliyotamka muda mfgupi uliopita kuwa ‘kwa Tanzania ya leo kuna jambo lisilowezekana mbele ya pesa?’ yakajirudia akilini mwake. Akajua kuwa mpango huu ulioletwa na kapamba una mkono wa rushwa. Ni kwamba hata huyo aliyemtuma kapamba anautambua uzito wa suala hilo naugumu wake kiutekelezaji.
Ni kwamba mchakato huyo unaweza kukamilika lakini pia unaweza kutoa matokeo yatakayomwathiri yeye aliye mwajiriwa wa Jeshi la Magewreza. Anaweza kukamatwa na kufunguliwa kesi au kufukuzwa kazi. Lakini wazo lingine lilimwingia kuwa, kama mchakato utakwisha vizuri na isibainike kuwa yeye kahusika kwa namna yoyote na wala isibainike kuwa kuna hujuma iliyofanyika, basi maisha yake yanaweza kuwa mazuri kulingana na pato atakalokuwa ameliingiza kutokana na kazi hiyo.
Na shilingi zitakazoingia katika himaya yake, hilo hakulijua na kwa wakati huo. Alikuwa na mambo mawili kichwani. Kwanza, alitambua fika kuwa ili Scolastica Temu halisi atoroshwe na badala yake aingie Scolastica Temu bandia, akili, mbinu na ujanja vilihitajika katika ukamilifu wake. Hakupenda kumhusisha askari mwingine yeyote kwa kuwa halikuwa suala lililopaswa kukiamini kichwa cha pili. Alihofia kuwa kukihusisha kichwa kingine litakuwa ni kosa ambalo angelijutia baadaye pale mpango huo utakapokuja kuwa hadharani wakati utekelezaji umeshafanyika. Hapo ndipo atatiwa pingu, kesi nzito ikimkaabili.
La pili, ambalo lilimfanya autilie shaka mpango huo, ni kwa kuhisi kama siku moja Scolastica bandia atapandwa na mzuka utakaomfanya atoe siri kwa askari yeyote mwingine, basi hapo mambo yatakuwa mabaya zaidi.
Kwa kulifikiria suala hili pili, akaamua kurusha swali, “Kwa nini huyu mtuhumiwa asitoroshwe bila ya kuingia mwingine badala yake?”
“Inawezekana,” Kapamba alijibu. “Lakini tatizo ni moja. Huyu aliyeko rumande atatoroshwa ili aende kuishi na huyo anayehangaikia mpango huu. Mtu huyo anataka akaishi naye kama mkewe. Kwa hali hiyo, kama mtuhumiwa pekee atatoweka rumande, kwa vyovyote vile lazima kutakuwa na msako mkali. Najua mna kumbukumbu zenu za wathumiwa wote. Sasa siku mtuhumiwa atakapotakiwa kwenda mahakamni mtafanya nini itakapobainika kuwa hayupo?
“Naamini lazima msako mkali utafanyika na hasa kwa kuzingatia kuwa mtuhumiwa mwenyewe ni wa kesi ya mauaji. Huwezi kujua, anaweza kuzuka shambenga mmoja akawabonyeza polisi na mambo yakawa si mambo. Cha ajabu ni kipi kama mwizi wa mamilioni benki huweza kukamatwa hata baada ya miaka miwili? Itawashinda askari kwa mwanamke mmoja aitwaye Scolastica Temu ambaye huenda miezi mitatu au minne tu baadaye, atakuwa kishajisahau kwa kujiona ni mama halali wa nyumbani?”
Maisara alionekana kuzama mawazoni. Ukimya mfupi ukatala kisha akaika tena na swali: “Kwani akishatoka rumande ataenda kuishi wapi na huyo jamaa yake?”
“Hapahapa Dar.”
“Hapa?!”
“Yeah, ni hapahapa.”
“Kwa nini? Anajiamini vipi?”
Kapamba alitabasamu kidogo. “Kuishi hapa siyo tatizo kama tayari kutakuwa na mtu anayesimama kizimbani kwa jina la SCOLASTICA TEMU akiwa ni mtuhumiwa wa kesi ya mauaji. Wala hilo lisikutie wasiwasi. Hakuna kitakachoharibika kama uko tayari kutekeleza mpango huu.”
“Lazima niwe na mashaka,” Maisara alikunja uso kidogo na kuonesha umakini. “Mimi ni mwajiriwa wa Jeshi la Magereza. Sina mume. Unadhani mambo yakiharibika maisha yangu yatakuwaje?”
“Ni kama yataharibika…”
“Tuchukulie kuwa yataharibika!” Maisara alimaka.
“Hilo haliwezi kuwa tatizo lisilotatulika.”
“Ki-vipi?”
“Maisara, elewa kuwa unazungumza na mtu asiyekuwa mbabaishaji,” Kapamba alisema huku akimtazama kwa macho makali. “Mimi siye yule Kapamba uliyekuwa ukimjua. Kapamba aliyekuwa akiishi kwa mfumo wa patapotea…”
Aliongea kwa kirefu, akijitahidi kumpa imani Maisara kuwa ni mtu anayejitambua. Hata hivyo, Maisara alishaujua na kuuzoea ulaghai wa wanaume. Haya ‘mashairi’ ya Kapamba yaliingia kichwani mwake na kukumbana na uhariri na uhakiki wa nguvu. Akayatafakari kwa kina huku akimtazama kwa makini, akizivuta akilini kumbukumbu za baadhi ya matukio yaliyomfanya asimwamini hata kwa asilimia sabini.
*****ITAENDELEA ***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 40




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
....
ALIONGEA kwa kirefu, akijitahidi kumpa imani Maisara kuwa ni mtu anayejitambua. Hata hivyo, Maisara alishaujua na kuuzoea ulaghai wa wanaume. Haya ‘mashairi’ ya Kapamba yaliingia kichwani mwake na kukumbana na uhariri na uhakiki wa nguvu. Akayatafakari kwa kina huku akimtazama kwa makini, akizivuta akilini kumbukumbu za baadhi ya matukio yaliyomfanya asimwamni hata kwa asilimia sabini.
*****SASA ENDELEA******
Kapamba alikuwa ni mtu wa kuishi jijini Dar es Salaam kwa mbinu hii na ile. Baadhi ya wafanyabiashara wa mitaa ya Sokoine, Ohio, Samora, Milambo, Maktaba, Azikiwe na minigineyo katikati ya jiji, walimfahamu na walizijua mbinu alizotumia katika kujipatia riziki.
Kila siku alikuwa mtanashati, akiwa ndani ya suti ya gharama kubwa, tai shingoni, viatu vilivyong’ara miguuni. Ndevu zilizochongwa na kuunda umbo la ‘O’ zilimwongezea mvuto na kumjengea heshima machoni mwa wengi na hivyo kumrahisishia namna ya kujipatia pesa kwa hila.
Si tu kwamba Maisara aliwasikia watu wakizungumzia mfumo wa maisha ya Kapamba bali pia, labda kwa bahati mbaya, siku moja akiwa ndani ya teksi Mtaa wa Ohio, saa sita mchana, alishuhudia Kapamba akikwidwa tai na mzungu mmoja.
Mzungu huyo aliyekuwa na umbo la kikakamavu, alikwishabadilika rangi na kuwa mwekundu mithili ya nyanya. Maisara, kama watu wengine wachache waliokuwa wamekusanyika katika eneo hilo, naye alivutwa kushuhudia kilichojiri. Lakini alipomwambia dereva teksi, akaambulia kauli ya kushangaza.
“Shangazi achana na mambo hayo. Huyo aliyetiwa loba ni mzoefu wa kuwatapeli wazungu na wageni wengine wa Dar. Nani asiyemjua?”
Maisara ambaye katika kipindi hicho alikuwa akianguka kitandani na Kapamba bila ya shoga yake, Mwanahamisi kujua, hayakumwingia akilini maneno haya ya dereva teksi. Kapamba aliwaambia kuwa yeye ni dereva wa malori ya mizigo yaendayo Rwanda, Zambia na Malawi, uongo ambao vichwani mwao ulikuwa ni ukweli halisi na hasa kutokana na jinsi alivyokuwa akimwaga pesa kwa Mwanahamisi na kumnunulia samani za kisasa.
Yeye mwenyewe, Maisara alitanguliziwa kitita cha shilingi laki tatu, ili wakaistareheshe miili yao katika hoteli moja katika kitongoji cha Kariakoo.
Maisara aliwajua baadhi ya madereva wa magari makubwa ya mizigo ambao pesa kwao huwa si kati ya matatizo yaliyowazunguka. Hivyo, hata Kapamba alipowadanganya kuwa ni dereva wa magari hayo, huku akitangaza ukwasi mbele yao kivitendo, walitokea kumwamni. Imani hiyo ilidumu kichwani mwa Maisara hadi siku hii alipomwona akikwidwa na Muitaliano.
“Simama!” alimfokea dereva huyo. “Acha tabia ya kufananisha watu ovyo! Unamjua yule kaka wewe?”
Dereva hakukanyaga breki, zaidi alitabasamu kidogo kisha akasema, “Anti ni nani asiyemjua huyo jamaa? Anaitwa Kapamba. Mimi namjua vizuri tu Ei-Tu-Zedi. Lakini hapa hajulikani sana kwa jina hilo. Wanamwitaga tu, Kipara. Kazi yake ni kuwadanganya Wazungu kuwa anaweza kuwabadilishia dola na kuwapa pesa ya hapa Tanzania. Lakini pesa anazowapa mara nyingi huwa ni feki. Au anaweza kuwadangaya kuwa anaingia ndani ya jengo lolote analolijua vizuri akidai kuwa anakwenda kuwachukulia pesa hizo za kibongo, kumbe anatokea mlango wa pili na kupotea.
“Akishafanya tukio hilo anaweza kupotea maeneo haya hata kwa miezi miwili ndipo akazuka tena. Sasa leo hapo kakutana na mjanja zaidi yake daaaadek! Umenisoma hapo shangazi?”
Maisara aliduwaa kwa muda akimtazama dereva huyo. Kisha akashusha pumzi ndefu na kutikisa kichwa kwa masikitiko. Sasa hakuhitaji kuhoji lolote. Yaliyosemwa na dereva teksi huyo yakawa yamempa picha halisi ya maisha ya Kapamba.
Hivyo hata kwa usiku huu, alijali kuwa makini na ujio huo wa Kapamba. Akaamua kukata mzizi. Akamwambia, “Suala lako linawezekana. Litawezekana kama utanipa mkwanja wa maana.”
“Hapo nd’o penye hoja sasa, “ Kapamba alisema. “Nipe hesabu yako kamili.”
“Milioni hamsini!”
Kapamba alishtuka. Hakatarajia kutajiwa kiwango hicho. Ndiyo, ni kweli alijua kuwa pesa atakayohitaji Maisara haitakuwa haba lakini hakufikia kuwaza zinaweza kuwa zaidi ya shilingi milioni kumi. “Dah! Mai mbona uko juu hivyo?”
“Hata suala lenyewe si la kitoto,” Maisara alijibu huku kamkazia macho. “Elewa kuwa nakiweka rehani kibarua changu. Lolote linaweza kutokea na kunifanya ama nikamatwe na kufunbguliiwa kesi au nipoteze ajira kwa kitakachochukuliwa kuwa ni uzembe. Kama nina pesa hiyo, naweza kuishi bila shida.”
Ukimya ukatawala kwa muda, Kapamba akiwa ameinamisha uso. Kisha akaunyanyua tena na kumwambia, “Nimekuelewa lakini shusha kidogo.”
“Kwani wewe nd’o mtoa hela au?”
“Mimi ni mjumbe tu, lakini nahisi kuwa mwenyewe atashindwa kufika huko unakotaka.”
“Mbona unamsemea? Wewe fikisha ujumbe huo. Sawa? Na mkielewana , nitakupa namba ya akaunti ya benki mzitume hukohuko.”
Kapamba aliwaza na kuwazua. Aakaona ili hatima ya maongezi haya ifikie mwisho, hakuwa na budi kuwasiliana na Ndonya wakati huohuo. Akaitwaa simu na kupiga. Maongezi yao yakaziteka dakika kadhaa, Ndonya akionekana kupingana na kiwango hicho, akihisi kuwa huenda Kapamba naye akaongeza ‘cha juu.’
Hatimaye Ndonya akaweka msimamo kuwa hana zaidi ya milioni thelathini. Vinginevyo Maisara aachwe na watafute njia nyingine. Ujumbe ulipomfikia Maisara, baada ya maongezi kati ya Kapamba na Ndonya, akautafakari na kuamua kukubaliana nao.
“Mzigo usiniletee hapa. Pesa za Kibongo siziamini; kuna za kweli na feki. Pelekeni benki. Nikupe ‘account number’ ya benki?”
“Nipe.”
Muda mfupi baadaye Kapamba aliondoka huku wakiwa wamekubaliana kukutana tena siku inayofuata na kupanaga kikamilifu mpango wao. “Muda wowote kesho mzigo unaweza kuingia kwenye akaunti yako,” alimwambia.
*****
ASUBUHI ya siku iliyofuata, Ndonya, Kipini na Kapamba a walikutana tena nyumbani kwa Ndonya na wakazungumza kwa kina kuhusu mpango wao. Moyoni Ndonya aliona kuwa pesa zinazohitajika katika mpango huo ni nyingi tofauti na alivyotarajia.
Mrithi wa Scolastica Temu anabeba milioni ishirini, huyu askari magereza milioni thelathini. Zilimuuma lakini hakujali. Akapga moyo konde na kuamua liwalo na liwe, hakuna kusitisha mchakato huo. Kilichomfariji ni akaunti zake mbili katika benki mbili tofauti. Akaunti hizo zilikuwa na jumla ya shilingi milioni mia moja na kumi.
Namna alivyozipata pesa hizo hakuna aliyejua, lakini ukweli ni
kwamba alikuwa amefanya hujuma fulani ndani ya kampuni akitumia cheo chake cha Uhasibu na akafanikiwa kujizolea pesa kwa wingi kwa awamu tofauti. Sasa alitambua kuwa milioni hamsini zitakwenda kwa hao watekelezaji wa mpango huo na bado alitambua fika kuwa anapaswa kuwalipa hawa marafiki zake, pesa ya maana.
Kama ameweza kutoa milioni hamsini kwa watu wawili, ni dhahiri hata hawa waliomfanyia mpango wa kuwapata wahusika nao watataka pesa ya kueleweka. Katika mazungumzo yao asubuhi hiyo ndipo wakaafikiana kuwa kila mmoja apate milioni kumi baada ya mpango kukamilika, yaani baada ya Scolastica kutoka jela na Latifah kuingia gerezani.
Hatimaye Ndonya akamgeukia Kapamba. “Unajua, Kapamba, suala hili linapaswa kukamilika kesho kama itawezekana. Sitaki kuchukua muda. Na ofisini nimedanganya kuwa nina msiba wa ndugu yangu huko Kibaha, kwa hiyo leo na kesho sitakuwapo. Katika siku hizi mbili yaani leo na kesho tukamilishe ishu. Sawa?”
“Hakuna shida, muhimu ni wewe pia kukamilisha ishu ya yule askari,” Kapamba alimwambia.
“Hilo sio tatizo. Nipe ile namba ya akaunti yake ya benki, halafu baada ya nusu sasa nitakuwa benki kukamilisha kila kitu. Nikishakamilisha, nitakutaarifu umwambie mzigo tayari ili kama ana mfumo wa kucheki muamala wa benki kwa kutumia simu aangalie hukuhuko aliko.”
Kapamba akampatia namba ya akaunti ya Maisara.
****ITAENDELEA SIKU YOYOTE...***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 41




ILIPOKOMEA TOLEO LILILOPITA...
“Hakuna shida, muhimu ni wewe pia kukamilisha ishu ya yule askari,” Kapamba alimwambia.
“Hilo sio tatizo. Nipe ile namba ya akaunti yake ya benki, halafu baada ya nusu sasa nitakuwa benki kukamilisha kila kitu. Nikishakamilisha, nitakutaarifu umwambie mzigo tayari ili kama ana mfumo wa kucheki muamala wa benki kwa kutumia simu aangalie hukuhuko aliko.”
Kapamba akampatia namba ya akaunti ya Maisara.
***SASA ENDELEA KULISONGESHA...
Saa tano na nusu, wakati Kapamba akiwa nyumbani kwake
akijishughulisha na hili na lile, mara simu yake ikaita. Alipoangalia kioo akakuta ni Ndonya. Haraka akaipokea.
“Kapamba,” sauti ya Ndonya ilipenya sikioni mwake sawia.
“Yap,” Kapamba aliitika.
“Nimeshatumbukiza mzigo. Anaweza kuangalia ila nadhani akitaka kudroo labda ni kesho, siyo leo.”
“Poa, ngoja nimwarifu.”
Dakika chache baadaye, Maisara alikuwa ameshazungumza
na Kapamba na kupewa taarifa ya kuingiziwa pesa katika akaunti yake benki.
“Hapo sawa, sasa uje nikupe maagizo mengine muhimu,” Maisara alimwambia wakati wakihitimisha maongezi.
“Sasa hivi?”
“Yeah, ikiwezekana fanya muda huu. Leo niko off. Nipo tu home.”
“Ok. Nipe nusu saa.”
*****
“UNASiKIA, kesho nitakuwa kazini,” Maisara alimwambia Kapamba mara tu walipokutana nyumbani kwa Maisara mchana huo. “Ningeshauri mje keshokutwa mchana saa tisa hivi.”
“Saa tisa?”
“Ndiyo, saa tisa alasiri,” Maisara alijibu. “Nina sababu ya kuchagua muda huo. Kitakuwa ni kipindi cha watuhumiwa kufanya kazi za nje. Ni wakati mwafaka kwa dili kuchezwa.”
"Kwa nini isiwe kesho?”
“Hapana, tusiwe na pupa wala haraka bila sababu ya msingi,” Maisara alijibu. “Mpango huu ni mzito, hatupaswi kuharibu hatua yoyote tunayofikia.”
“Tutawasilianaje?”
“Nitakupigia saa tatu au nne asubuhi kuthibitisha kama hakuna mabadiliko yoyote ya ratiba, maana tunaweza kuwa tumepanga hivi kumbe mabosi wangu wakanipangia majukumu mengine labda ya kutoka kabisa eneo la gerezani.”
Kapamba akatikisa kichwa akiashiria kukubaliana naye.
“Halafu, nimesahau jambo moja muhimu,” Maisara alisema huku akinyanyuka na kulifuata kabati. Akalifungua na kutoa gauni refu, jekundu.
“Huyo mtu wenu anapaswa kuwa na gauni kama hili. Na kama kweli mnaamini kuwa anafanana sana na mtuhumiwa basi hakikisheni gauni la aina hii atakalovaa liwe limemtaiti mapajani. Kwani hana hipsi kama huyu mtuhumiwa?”
“Amefunga hipsi za ukweli,” Kapamba alijibu haraka “Yaani tofauti yao ni ndogo sana.”
“Basi hakikisheni mnamshonea au sijui mnamnunulia gauni kama hili. Atakapokuja awe amelivaa.”
Kapamba alilishika gauni hilo na kuliangalia kwa muda kisha akasema, “Unaonaje, tulipige picha, niende nayo.”
“Poa tu, lilaze pale kitandani, uchukue picha."
Kapamba alitwaa simu yake kubwa mfukoni na kuchukua picha ya gauni hilo. Dakika chache baadaye alikuwa ameagana na Maisara na akaita bodaboda pale nje, akarudi kwake.
*****
NDONYA hakushangaa wala kufikiri sana alipoambiwa kuwa lilihitajika gauni fulani, gauni atakalopaswa kuvaa mtu atakayechukua nafasi ya Scolastica Temu gerezani. Aliitazama kwa makini picha aliyooneshwa na Kapamba kisha akatabasamu na kusema kwa sauti ndogo, "Ni kazi ndogo tu. Kufikia kesho jioni gauni hili litakuwa tayari. Kuna mtaalamu wangu asiyebahatisha katika taaluma ya ushonaji."
Ratiba ya siku iliyofuata, ilikuwa ni ya mambo kwenda haraka na kutopoteza muda. Kipini alipigiwa simu akitakiwa amlete Latifah hapo kwa Ndonya ili apimwe hilo gauni lililopaswa kushonwa. Vipimo vilipokwishafanyika, Ndonya aliingia garini na kukanyaga mafuta akielekea Kariakoo. Huko akakitafuta kitambaa cha gauni hilo na alipokipata akarudi haraka hadi kwa fundi aliyempima Latifah.
“Usiniwekee usiku msh’kaji wangu,” alimwambia fundi huyo. “Kama huna hakika ya kuimaliza kazi hiyo leo n’ambie kabisa.”
Fundi akacheka kidogo Kisha: “Ndonya siku hizi huniamini?”
“Sina maana hiyo, ila isije kuwa naondoka hapa na wewe unaliweka pembeni na kuendelea na kazi nyingine za watu.”
Fundi alikunja uso kidogo na kubakia akitazama mlangoni. Alikuwa akiwaza, ni kwa nini asijifungie na kukamilisha hii kazi ya Ndonya, kazi aliyolipwa pesa nyingi? Aliamini kuwa kama mlango utakuwa wazi kuonesha dhahiri kuwa ofisi inaendelea na majukumu, watakuja wateja wake ambao kuna nguo zao hapo ambazo hajazimaliza na baadhi aliwaahidi leo.
Atawajibu kwa Kiswahili gani pale watakapomkuta anapambana na hili gauni alilolipwa maelfu ya pesa ili likamilike leo? Kwa vyovyote, alijua lawama atakazoshushiwa hazitakuwa na mfano. Ndipo akaamua kuweka wazi kwa Ndonya.
“Itakuwa hivi,” alisema kwa upole huku akamtazama Ndonya sawia. “Nitajifungia mchana kutwa. Hadi saa kumi na mbili gauni lako litakuwa tayari. Tupo pamoja?”
“Pamoja sana.”
“Poa, tambaa. Nipigie saa kumi na moja, nikwambie nimefikia hatua gani.”
Alikuwa ni fundi mahiri sana katika fani hiyo. Na alikuwa ni mwaminfu. Hakupenda kuitia dosari kazi yake. Hivyo walipoachana tu na Ndonya, alijifungia ndani, akawasha feni na kuianza kazi hiyo.
Saa kumi na moja na nusu, Ndonya akiwa hajampigia simu, yeye alikuwa ameshahitimisha kazi yake. Akampigia simu Ndonya na kumtaarifu kuwa aufuate mzigo wake.
"Tayari?" Ndonya aliuliza kwa mshangao. "Au msh’kaji umelipua?"
Kicheko kikamtoka yule fundi. "Sasa msh’kaji wangu unanivunjia heshima ujue. Wewe njoo uchukue na kukagua. Kama nimelipua utaniambia, lakini uthibitisho kuwa nimelipua utajulikana mwenye kuivaa atakapojipima."
"Poa nakuja sasa hivi."
*****
"NAHISI kuwa hujalipua," Ndonya alimwambia fundi cherehani wakati alipoingia ndani ya chumba cha ushonaji na kukabidhiwa gauni lile. Alilitazama kwa muda na akajisikia kuridhika.
Ndonya, akiwa njiani alimpigia simu Kipini na kumwambia ahakikishe Latifah anakuja usiku kujipima gauni hilo.
"Hana noma nimeshaongea naye," Kipini alisema. "Yupo tayari, nitakuja naye muda huo.”
Saa mbili usiku, wanaume wale watatu wakiwa na Latifah, walikuwa sebuleni kwa Ndonya. “Shemeji yangu, gauni lako ndilo hili,” Ndonya alimwambia Latifah huku akilitoa gauni hilo ndani ya mfuko na kumkabidhi.
Latifah alilipokea na kuliangalia, akiligeuzageuza katika kulikagua.
“Ingia chumba hicho ujipime kwa kulivaa kabisa,” Ndonya akamwelekeza.
Latifah akasimama na kuelekea chumbani. Dakika kama kumi hivi baadaye akatoka akiwa amelivaa gauni hilo.
“Waoooo…” Kapamba akabwata. “Toto liko vizuri daaaah…. Kipini mpaka nakuonea wivu yani!”
Vicheko vikatawala kwa kila mmoja. Naam, gauni hilo lilimkaa vizuri Latifah, likiwa limembana eneo la mapajani kama lile alilovaa Scolastica.
“Yeah, limemkaa inavyostahili,” Kipini alisema.
"Ni ka’vile namwona Scola wa Keko," Kapamba aliongezea.
“Sasa nimekubali,” Ndonya alisema huku akiwatazama wenzake kwa zamu. “Nadhani huu ni mwanzo mzuri wa mafanikio ya mpango wetu.”
Kisha akamgeukia Latifah. Akamtazama kwa makini toka juu hadi chini, akionesha kuridhishwa na mwonekano wake. “Kesho nd’o siku ya utekelezaji? Uko tayari au kuna tatizo lolote?”
Wakati huo akilini mwa Ndonya kulikuwa kumejiwa na wazo lenye wasiwasi wa kuzidiwa ujanja. Huyu mwanamke kishapewa malipo yake. Je, hawezi kuondoka hapa na kutokomea jumla na wasimwone tena? Ni kipi kitamfanya ashindwe kukitelekeza chumba chake na kukodi gari usiku huo na kutokomea kusikojulikana?
Wasiwasi huo ulimtawala kwa muda mfupi na akajikuta akifanya maombi ya kimyakimya moyoni kuwa Mungu amsaidie Latifah asitokomee na pesa atakazompa.
“Hakuna tatizo lolote,” Latifah alijibu kwa utulivu.
“Ok, utakwenda nalo gauni umelivaa au utabadili na ulivae kesho wakati wa kutimiza majukumu yetu?”
“Ngoja nikabadili.” Akarudi chumbani na kurejea yale mavazi aliyokuja akiwa ameyavaa.
Hakukaa tena, alibakia kasimama huku mkoba wake ukining’inia begani. Macho yake yaliyokosa aibu wala woga, yalikuwa yamemganda Ndonya na mara Kipini. Kisha: “Nawasubiri sasa. Ili kila kitu kiende sawa, ni kuondoka hapae nikiwa kamili.”
“Yaani na mzigo wako, eti?’
Nd’o maana’ake."
Ndonya alinyanyuka. Akaenda chumbani ambako alitumia takriban dakika tano kisha akatoka na kijimfuko kilichotuna. "Mzigo wako," alisema huku akimkabidhi Latifah. Kisha akaongeza, "Ni vizuri kama utatulia uhesabu ili tusije kulaumiana baadaye."
Wakati Latifah akihesabu, Kapamba na Ndonya walimshuhudia vidole vyake vikitetemeka kwa mbali. Hawakushangaa. Kama mtu haujawahi kushika milioni moja kwa mkupuo, kwa nini milioni kumi au zaidi zisikupagawishe?
Wanaume hao wakawa wakiendelea na mazungumzo mengine ya kawaida. Robo saa baadaye ndipo Latifah alipohitimisha kazi ya kuzihesabu pesa zile. Akaunyanyua uso na kumwangalia Ndonya kisha akamwambia, “Ziko sawa.”
“Ok, nadhani utakuwa mwaminifu,” Ndonya alimwonya huku kakunja uso, akimwangalia kwa makini. “Sisi tunakuamini, na wewe ujiamini. Usitugeuke! Sisi siyo watu wa kuzidiwa akili. Naomba ulijue hilo.”
“Vipi kwani? Kama hamniamini, tuvunje dili!” Latifah alitamka kwa ukali, sauti yake ikiwa ya chini lakini akiwatazama kwa macho makali.
“Hapana, usipaniki,” Ndonya alimpoza. “Ni katika kuwekana sawa tu. Kumradhi kama nimekukwaza.”
Kipini na Kapamba walikuwa kimya wakiwatazama kwa zamu.
“Kwa hiyo kinachoendelea?” Latifah aliuliza huku akiuingiza ule mfuko wenye pesa ndani ya mkoba wake.
“Kesho saa tatu asubuhi uwe hapa,” Ndonya alimwambia. “Utakaa hapa mpaka muda wa kwenda Keko utakapowadia. Inawezekana ukashindwa kupakumbuka?”
“Kama sitakuwa na mwenyeji, siwezi kupakumbuka.”
“Us’konde,” Ndonya alicheka. “Kipini si yupo? Sidhani kama kwa leo itakuwa vibaya mkiumaliza usiku kwa kuagana rasmi.”
“Yeye tu,” Latifah alisema kwa majidai na uso wa kujiamini. “Kama atakuwa tayari kukesha itakuwa poa zaidi…pumzi kwangu si tatizo.”
Kapamba na Ndonya wakacheka huku wakimtazama Kipini. Kisha Ndonya akamtazama Kipini na kumwambia, “Kaka, kazi kwako. Unalo hilo. Lakini hakikisheni kesho mnawahi kukanyaga hapa; sawa?”
Tabasamu la mbali likamtoka Kipini.
***ITAENDELEA ***

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom