Riwaya: Scolastica Temu

Riwaya: Scolastica Temu

SEHEMU YA 18

TULIPOKOMEA....


Saa nne usiku ilimkuta hapohapo Maseru Bar, na zaidi ya mara nne alizompigia tena Kibutu bado hakuambulia kitu. Ndipo alipoamua kumtumia ujumbe: ‘umenikalisha hapa na kunifanya nipate hasara kwa kunywa bia. Utairejesha gharama niliyotumia. Sasa kesho nitakuja saa kumi na mbili, kama hutaweza tena kuja, basi dili life.
Alijua kuwa atakapoiwasha simu atausoma ujumbe huo.

***ENDELEA***


AKIWA amekerwa na kutokutana na Kibutu kama walivyokubaliana, aliondoka hapo saa tano akiwa pia ameghairi kuondoka na yule mhudumu ambaye saa nzima iliyopita walikuwa wameshakubaliana kuondoka wote.
Saa mbili asubuhi, aliangalia kama ujumbe wake utakuwa umeingia katika simu ya Kibutu. Akashangaa kukutana na maandishi ‘waiting for delivery details.’ Tangu jana mpaka saa hizi hajaiwasha simu! Au kaibiwa? Au imeharibika? Alijiuliza maswali mengi lakini hakuambulia jibu lolote.

Saa nne bado hakukuwa na ujumbe ambao ulionesha kuwa umesomwa. Alipojaribu kupiga akakumbana na jibu kama la jana kuwa namba anayopiga haipatikani. Bado hakujali sana. Alijua kuwa labda simu itakuwa na matatizo ndiyo maana haipatikani. Akaondoka na kwenda kwenye mihangaiko yake.

KWA Scolastica Temu, haukuwa usiku wenye burudani halisi ya usingizi. Hapana. Alizinduka saa tisa na kujikuta aking’aa macho hadi kunakucha. Angeupataje usingizi mzuri ilhali alitambua fika kuwa saa kadhaa zilizopita alikuwa na mtu ambaye alikuwa ni kero kubwa katika historia ya maisha yake tangu azaliwe?
Angeupata vipi usingizi halisi ilhali alitambua fika kuwa saa kadhaa zilizopita alimruhusu mtu huyo ampapase maungoni japo alimchukia zaidi ya alivyomchukia shetani?

Angeupata vipi usingizi uliostahili, wakati alitambua fika kuwa kwa mara ya kwanza amechukua uamuzi mgumu kutokana na tendo la kubakwa zadi ya mwezi mmoja uliopita? Alipozinduka usingizini alikuwa ametoka kuota ndoto isiyoeleweka vizuri. Kwamba, anakimbizwa na mtu asiyemjua na wakati akijitahidi kukimbia mara mbele yake akaona korongo kubwa lenye kiza kinene chini. Kwa kasi aliyokuwa nayo hakuwa na uwezo wa kusimama papohapo. Alijikuta yuko hewani na kuanza kutumbukia ndani ya shimo hilo pana na lenye kina kisichojulikana.

Alipiga kelele kubwa wakati akiwa hewani na ndipo ndoto hiyo ilipokatika ghafla! Alikurupuka na kukuta jasho likimtoka, taa bado ikiwaka. Kalala sebuleni! Akahema kwa nguvu huku akiangaza huku na kule na kushindwa kuelewa kwa nini kaota ndoto ya aina ile. Jambo moja lilimjia wakati huo, kwamba jana aliua! Hilo lilikuwa dhahiri akilini mwake! Nafsini mwake alikuwa na huruma, kiasi hata hakuwa radhi kuchinja kuku au kuua panya! Jana, akitumia tembe moja ya Olanzapin, kwa kudhamiria, aliisaga na kuumimina unga wake ndani ya bia ya Kibutu. Alifanya hivyo akitambua fika kuwa tembe ile itampa usingizi wa zaidi ya saa kumi!

Kama vile haitoshi, kwa kudhamiria tena vilevile, aliifungua chupa ya sumu kali ya PAK na kumvutisha Kibutu wakati akikoroma kwa nguvu ya tembe ya Olanzapin. Aliijua nguvuy ya PAK, kwamba itamchukua mtu sekunde zisizozidi thelathini tu za kuwa hai! Kaua! Hilo alilitambua fika. Damu ya mtu iko kichwani mwake! Kwamba baada ya kuondoka kule chumbani labda Kibutu atafufuka, hilo halikumwingia akilini asilani. Suala ni muda gani itabainika kuwa mtu kafia ndani kwake?

Aliamini kuwa matukio hayo huenda ndiyo yamemsababishia ndoto hiyo ya kutisha. Akaitazama simu yake kwa mara ya pili. Tisa na dakika ishirini. Sasa hakujisikia hata kuingia chumbani kulala. Kwa jumla hakujisikia tena kulala. Lakini ataenda wapi muda huo? Kungekuwa na klabu yoyote ya usiku angekwenda kuumaliza usiku huo. Haikuwapo.
Akautwaa mkoba na kuungalia ndani akivichunguza vitu vyake. Kila kitu kilikuwamo na zaidi ile simu aliyoichukua kwa Kibutu pia ilikuwamo. Alichofanya ni kuitwaa, akaizima kabisa. Kisha aliufunga tena mkoba na kuuweka ndani ya kabati, sehemu ya mafichoni.

Mara akakumbuka kuwa majuzi alipokuwa akirudi kutoka Kawe alikokwenda kunywa bia, alichukua bia mbili pale Pazi Social Club. Hakuzinywa, aliziweka ndani ya jokofu. Mpaka leo zilikuwapo. Sasa akaamua zimsindikize kuumaliza usiku huo kuelekea alfajiri. Saa kumi na mbili asubuhi, nje kukiwa kumepambazuka, mtoto wa kike alikuwa akimalizia chupa ya pili huku akiwa ameamua kuwa siku hiyo asitoke zaidi ya mita mia mbili kutoka humo ndani mwake. Aliamua aipumzishe akili. Lakini ataweza kutawa? Alijiuliza swali hilo na kushindwa kupata jibu sahihi. Akamwomba Mungu ampangie cha kufanya.

Saa moja alikuwa akitoka bafuni kuoga kisha akaenda tena palepale Pazi ambako alikunywa supu kisha akarudi ndani, akajifungia. Nusu saa baadaye alikuwa ametopea usingizini. Huu ukiwa ni usingizi halisi, shibe nzito ya supu ikiwa imeshika hatamu ya umiliki wa fahamu zake.

Kama aliyekuwa amepuliziwa dawa ya nusu kaputi, alijikuta akizinduka saa saba mchana. Akajishangaa. Saa mbili kasoro mpaka saa sita na nusu! Hata hivyo hakujali sana baada ya kuikumbuka ratiba ya jana na kutoupata usingizi wa haki usiku, ulioambatana na ndoto ya kutisha iliyomwondolea utulivu akilini kwa muda. Kwa mara nyingine akaingia bafuni na kujimwagia maji kwa muda mrefu. Alipotoka alijisikia yuko timamu. Akili ilikuwa imetulia. Hakuwa hata na dalili yoyote ya uchovu.

Akawasha runinga na kuangalia vipindi mbalimbali. Hivyo navyo vikamkinai. Akaamua kutoka. Saa yake ilisoma kumi kasoro. Njaa ilimsakama kwa mbali. Alihitaji kula, lakini hakuwa tayari kupika. Hakujisikia tu. Akawaza aende hapo Pazi kula, lakini wazo hilo likaota mbawa. Mazingira ya pale kwake hayakuwa ni rafiki. Kwa jumla hakupenda kujiweka hadharani sana katika kipindi hiki ambacho bosi wake na ofisi yake kwa jumla walijua kuwa yuko Kigoma.

Hivyo, wazo la kwenda tena Kawe likamrudia na akaliona kuwa ni sahihi. Alivaa nguo za kawaida ambazo hata wapangaji wenzake hawajawahi kushuhudia akizivaa, wala wafanyakazi wenzake; dera, kofia la pama kichwani na miwani mieusi machoni. Alionakana kama mwanamke wa taifa lolote la kigeni, na kwa jumla alipendeza. Hakutaka kubeba mkoba wake ule wenye vifaa muhimu. Alijichukulia kijimkoba kidogop tu cha kawaida na kisichokuwa na chochote cha maana zaidi ya pesa.

Alitembea hadi kando ya Barabara ya Kawawa ambako alikodi bajaji iliyompeleka Kawe kwenye baa ileile aliyokuwa akienda siku zote zilizotangulia. Alitoka huko saa mbili usiku, sasa akijisikia kurudi moja kwa moja kulala. Na alifanya hivyo. Aidha, hakutaka kukisumbua kichwa chake kwa lolote kwa usiku huo hasa kuhusu kuipekua simu ya Kibutu. Alipanga kufanya hivyo kesho yake asubuhi.

ALIAMKA mapema, saa moja kasoro. Usiku uliopita ulikuwa tulivu kwake. Hakupata ndoto yoyote iliyomtisha. Kwa jumla hakuota ndoto yoyote. Asubuhi hii akijisikia kuwa timamu zaidi kimwili alishughulikia usafi wa ndani, kisha akaoga na kama jana, alitoka na kwenda baa ambako aliagiza supu. Saa mbili alikuwa yuko vizuri tumboni. Sasa akaamua kuifanya ile kazi ya kuipekua simu ya marehemu Kibutu.

Akiwa amejitanda kanga pekee mwilini, alihakikisha kuwa kafunga milango na geti kwa funguo. Akaitwaa simu ya aliyekuwa Kibutu. Akaiwasha. Sekunde chache baadaye ujumbe tofauti ukaingia. Akatulia akisubiri ujumbe wote uingie. Kisha akajaribu kufungua. Akashukuru Mungu kukuta kumbe Kibutu hakuwa ameweka neno la siri la kuingilia.

Akauona ujumbe wa kwanza ukiwa ni wa kutoka kwa mtu aliysajiliwa kwa jina la Martha, akimuuliza kama atampatia pesa alizomwomba au hampi. Ujumbe wa pili ulitoka kwa mwanamke mwingine aliyekuwa akiomba wakutane leo. Ujumbe wa tatu na wa nne ulikuwa ukitoka kwenye kampuni za bahati nasibu, zikimshawishi kucheza kamari.
Ndipo alipouona ujumbe wa mtu aliyejazwa humo kwa jina la Kisengo. Akashtuka na kutulia. Akausoma ujumbe huo kwa makini. Tabasamu la mbali likamtoka, tabasamu lisilokuwa hata na chembe ya furaha.

***ITAENDELEA

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YQ 19

TULIPOKOMEA....


Akauona ujumbe wa kwanza ukiwa ni wa kutoka kwa mtu aliysajiliwa kwa jina la Martha, akimuuliza kama atampatia pesa alizomwomba au hampi. Ujumbe wa pili ulitoka kwa mwanamke mwingine aliyekuwa akiomba wakutane leo. Ujumbe wa tatu na wa nne ulikuwa ukitoka kwenye kampuni za bahati nasibu, zikimshawishi kucheza kamari.
Ndipo alipouona ujumbe wa mtu aliyejazwa humo kwa jina la Kisengo. Akashtuka na kutulia. Akausoma ujumbe huo kwa makini. Tabasamu la mbali likamtoka, tabasamu lisilokuwa hata na chembe ya furaha.

****ENDELEA****

Ujumbe huo ulitumwa jana. “Ina maana jana walikuwa na miadi ya kukutana hapo Maseru Bar, na leo anasema atakuja tena hapo Maseru, saa kumi,” alijikuta akinong’ona huku akirudia kuusoma ujumbe huo zaidi ya mara mbili.
Aliijua hiyo Maseru Bar hivyo, aliamua kuwa jioni hiyo ajaribu kucheza kamari yake kwa mara nyingine. Lazima aende. Wakati akiendelea kupekuapekua humo simuni, akakuta picha nyingi ambazo Kibutu alikuwa amepiga. Baadhi alikuwa na wanawake tofauti wakiwa kama walivyozaliwa, chumbani. Nyingine alikuwa baa akinywa bia. Picha mbili zilimvutia zaidi. Moja alikuwa na Kisengo na Machemba, wakiwa baa wakinywa bia. Nyingine, pia walikuwa pamoja lakini hii wakiwa wamesimama, wameliegemea gari dogo jeupe. Haikujulikana kama walikuwa baa au wapi, lakini kila mmoja alikuwa na chupa ya bia mkononi, Kibutu sigara mkononi.

Alichukua muda akiangalia hiki na kile ndani ya simu hiyo, akisoma ujumbe huu na ule. Hatimaye aliizima na kuiweka pembeni Akaendelea na kazi nyingine. Alijiona ana muda mrefu kabla ya jioni. Hivyo, alitoa nguo zilizokuwa chafu na kuanza kufua.

Alipomaliza kufua ilikuwa imeshafika saa saba mchana. Akawa anaona hana la kufanya zaidi. Akatulia sofani akiangalia runinga. Nusu saa ikapita akiwa macho kwenye runinga. Hatimaye akakumbuka kuwa alikuwa hajala. Zaidi ya supu ya kawaida asubuhi, hakuwa ametia kitu kingine tumboni hadi mchana huo.

Lakini bado alitambua kuwa alipaswa kuchukua hadhari kwa mambo mawili. Ofisini kwake walijua kuwa yuko Kigoma. Kwa hilo, alitambua kuwa alipaswa kujichunga sana. Kutoka humo ndani mchana, mchana na kwenda eneo la hadharani sana kama kule Barabara ya Kawawa ambako watu wengi walipita kwa miguu na wengine kwenye daladala, magari ya kawaida na hata mabasi ya mwendokasi, ilikuwa ni kama kujitangaza.

Isitoshe, tukio alilolifanya juzi halikuwa la kawaida. Ni yeye aliyeondoka Mood Bar akiwa na Kibutu. Waliondoka kwa teksi. Macho ya watu yaliwafuata. Zaidi, alitambua kuwa kuna wale vijana waili ambao hakujua walikuwa na nasaba gani na Kibutu, lakini ilionekana bayana wanafahamiana kwa ukaribu sana.

Pale itakapobainika kuwa Kibutu kafa, uchunguzi utakapoanza huenda wale vijana wakazungumzia kuhusu yeye kuondoka naye usiku wa siku ya tukio. Alitambua kuwa hawamjui na hawajui anakoishi. Lakini kama kuna yeyote mwingine aliyekuwa akimfahamu Kibutu, na siku ile naye alikuwa katika baa hiyo, huenda akawa msaada mkubwa kwa vyombo vya upelelezi.

Si karibu kila mtu mle baa alikuwa akimkodolea macho? Si ajabu kukuta wengine, wale wasio na staha, wakadiriki kumpiga picha, hasa alipokuwa akielekea na kutoka msalani, tukio ambalo huenda hata yeye hakuling’amua.
Kitendo cha kujitokeza ovyoovyo barabarani, hususan barabara kubwa kama ile ya Kawawa, kinaweza kumfanya mmoja wa abiria mwenye macho yasiyotulia, amwone. Kuonwa na mtu huyo, huenda kukawa ni jambo litakalomweka katika wakati mgumu kama mtu huyo mwenye macho yasiyotulia, ataamua kuteremka na kuja kumfuatilia.

Yote kwa yote, alipaswa kuchukua hadhari kabla ya jioni atakapoichukua hatua ya pili ya ratiba zake muhimu. Kwa hali hiyo, alitoka na kujaribu kugonga mlango kwa wapangaji wenzake. Zinduna alikuwapo, akafungua, wakasalimiana huku Zinduna akionekana kushangaa.
“Vipi, kumbe upo? Mwenzetu hatuonani!”
“Nipo tu mdogo wangu. Najisikia kuumwa.”
“Nini zaidi?”
“Ni kama malaria,” Scolastica alijibu huku akiangaza macho juu akiyakwepa haya macho ya Zinduna. Alihisi kuwa huenda anatambua anadanganya.
“Pole, mwenzangu. Sasa si ungepima?”
“Natarajia kufanya hivyo baadaye. Nitakwenda pale kwa Mvungi jioni.”
“Itakuwa vizuri. Ujue kama ni malaria kweli au labda tu ni mtikisiko wa kawaida wa mwili…”
“Sasa Zinduna,” Scolastica alimkata kauli. Alishachoshwa na maneno mengi. Na alimjua alivyokuwa kasuku. Si ajabu akazungumza maneno elfu mbili, wewe unasikiliza tu.
“Ndiyo, dada yangu.”
Scolastica akampa noti ya shilingi elfu kumi. “Naomba msaada wako.”
Zinduna aliipokea ilie noti huku akimtazama, akionekana kusubiri agizo.
“Na Janeth yupo?”
“Hayupo. Tangu ameenda kwenye misele yake jana, hajarudi. Kanipigia simu kuwa tukutane jioni sehemu fulani.”
“Sasa kwani umepika?”
“Bado, nilikuwa na mpango wa kuchukua chipsi kavu hapo mtaa wa pili.”
“Basi katika hela hivo kaniletee chipsi na nusu-kuku huko mtaa wa pili kwa Mpemba. Kachumbari hapana, ila pilipili kwa wingi na hiyo pilipili akufungie pembeni. Hela inayobaki agiza vya kwako.”
Tabasamu lkachanua usoni kwa Zinduna. “Asante dada’angu,” alisema huku akivaa kandambili na kuanza kutoka.
Scolastica akamzuia. “Subiri nikupe hotpot. Za kwangu wakuwekee humo, siyo waje kukufungia kwenye migazeti yao isiyoeleweka kama ni misafi. Si unajua siku hizi ile mifuko ya plastiki hakuna?”

WAKATI Kisengo alipokuwa akisubiri kuhudumiwa na mamalishe kwenye moja ya vibanda vilivyoko eneo la Magomeni Mikumi, saa sabab mchana, alikuwa na zaidi ya saa nzima akiwa hana umiliki wa simu yake.

Katika eneo alikoishi, Mtaa wa Manda, hakukuwa na umeme mtaa wote. Hivyo alilazimika kwenda umbali mfupi ambako alikuta umeme upo na akamwomba kijana mmoja muuzaduka amuwekee simu yake kwenye chaja.

Baada ya hapo alitembea huku na kule, akivuta muda na ilipofika saa saba wakati akisubiri mlo, ndipo aliona ulikuwa muda mwafaka hata wa kuichukua simu yake. Saa nne mpaka saa saba aliamini kuwa itakuwa imejaa.
Hapakuwa mbali kutoka hapo kwa mamalishe, akaenda na kuichukua kisha papohapo akaiwasha. Dakika moja baadaye akashuhudia ujumbe wa ‘massage delivered.’ Akachunguza kwa makini na kubaini kuwa kila alichomwandikia Kibutu sasa kimesomwa.

‘Ina maana sasa nd’o kaiwasha simu bwege huyu? Malaya gani kamkamata kiasi hiki?’ alijiuliza huku akirudi kule kwa mamalishe. Mara akaamua kupiga, lakini kama jana, mchana huu pia akaambulia jibu la kwamba namba haipatikani. Kwa hasira akasonya na kuiweka simu mfukoni. Hakuhangaika tena na suala hilo. Baada ya kula aliendelea na ratiba nyingine za kutafuta pesa, akiwa mbali na hapo Magomeni.

Saa kumi na moja ndipo alipoamua tena kwenda kule Maseru Bar, Kinondoni Mkwajuni kama alivyomtumia ujumbe Kibutu. Lakini kabla ya kupanda bodaboda na kwenda huko, alijaribu tena kumtafuta kwenye simu. Alipopiga simu safari hii iliita. Iliita kwa muda mrefu mpaka ikakatika. Akapiga tena ikatoa taarifa ya kuwa inatumika, ajaribu baadaye.
Akafarijika hata kwa kusikia ikiwa hewani. Lakini kwa nini hapokei? Yuko kwenye matatizo? Alijiuliza maswali hayo huku kwa mbali akijiwa nawasiwasi. Haikuwa kawaida ya Kibutu kumfanyia hivi. Mara akasikia mlio wa ujumbe wa maandishi ukiingia katika simu yake.

Haraka akaufungua na kuusoma. ‘Usijali, sorry, simu ilikuwa na matatizo. Nitakukuta mida hiyo uliyosema. Kuna tatizo kwenye spika, hatuwezi ongea.’ Taarifa hiyo ikamtia faraja. Sasa akapanda bodaboda na kuelekea Maseru Bar. Mfukoni akiwa pesa, shilingi laki mbili alizozipata kutokana na mpango fulani wa kimjimjini, hakukiona cha kumfanya asitangulie kufika huko baa na kuanza kushusha moja, moja huku pia akikutana na yule mhudumu wa jana, aliyepanga kuondoka naye kabla hajaghairi dakika za mwisho.

****ITAENDELEA PANAPO MAJAALIWA***


Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 20

TULIPOKOMEA....


Taarifa hiyo ikamtia faraja. Sasa akapanda bodaboda na kuelekea Maseru Bar. Mfukoni akiwa pesa, shilingi laki mbili alizozipata kutokana na mpango fulani wa kimjimjini, hakukiona cha kumfanya asitangulie kufika huko baa na kuanza kushusha moja, moja huku pia akikutana na yule mhudumu wa jana, aliyepanga kuondoka naye kabla hajaghairi dakika za mwisho.

***ENDELEA***
SAA kumi na moja na dakika chache alikuwa akiteremka eneo la Mkwajuni. Na kabla hajaenda huko Maseru Bar, akaingia ndani ya duka moja la dawa na kuagiza tembe moja maalum kwa matumizi aliyoyajua mwenyewe. Ilikuwa ni tembe aliyoamini kuwa itamlindia heshima ya uwanaume wake kama jioni hiyo atakutana tena na yule mhudumu na wakaondoka pamoja. Aliondoka dukani humo huku akiitafuna tembe hiyo, akimwacha muuzaduka akishangaa.
Muda mfupi baadaye aliingia ndani ya ukumbi wa baa hiyo. Kulikuwa na watu wachache. Mara tu alipokuwa akikifuata kiti, yule mhudumu wa jana, ambaye walikuwa wamekubaliana kuondoka, alimjia.

“Ilikuwaje jana?” lilikuwa ni swali la mhudumu huyo baada Kisengo kuketi na kusalimiana. Kicheko cha mbali kilitoka Kisengo, kisha: “Si unajua pombe tena. Maji yalizidi. Nimekuja shtuka niko ndani ya bajaji.”
“Huna lolote,” mhudumu yule alisema huku akibibitua midomo na kuondoka kwa madaha, akilitingisha umbo lake kusudi.
Kisengo alimtazama tu na kuishia kutabasamu. Kwa jumla, alijua kuwa hata huyo mhudumu mwenyewe, hakuwa na dhamira ya kwenda kustarehe, starehe halisi; alizihitaji pesa. Alijua kuwa asubuhi angemka katika hali njema kiuchumi.

Mbona jana alimwambia kuwa, kama angetaka waondoke muda wowote mapema, Kisengo angelazimika kulipia gharama kiasi fulani kwa meneja na papohapo mhudumu angekuwa huru? Kwa hali hiyo, akizingatia na uzoefu wake katika kuzuru baa mbalimbali, Kisengo hakubabaika. Alijua hata baadaye atakapomhitaji tena, hakutakuwa na kikwazo. Pesa tu. Aliamini kuwa shilingi elfu ishirini zingetosha kumlainisha. Lakini kwanza alihitaji kukutana na Kibutu, wazungumze kuhusu mpango ambao Kibutu alimdokeza. Mengineyo baadaye. Alikuwa peke yake katika meza hiyo, yenye viti vingine vitatu kando yake.

Hakujali kuwa peke yake, alijali kuhakikisha anaonana na Kibutu, wazungumze kitakachowakutanisha. Bia ya kwanza ilipoletw a na mhudumu kuondoka, Kisengo akawa ‘bize’ na simu yake, akiperuzi mitandaoni. Simu hiyo ilikuwa ni kama mtu wa pili kwake; ilimwondolea upweke. Nusu saa ikakatika akiwa na bia ya pili na wakati huo akiendelea kuyagandisha macho mitandaoni.

Ilipotimu saa kumi na mbili alishangaa kuona kimya. Ndiyo, Kibutu alimwahidi kuja muda huo, lakini hajafika. Mbona hata hatumi ujumbe wowote wa kusema yuko wapi na kwa nini anachelewa? Bia ya tatu ilipoletwa, kabla hajaianza, akaamua kumpigia tena simu Kibutu. Akabonyeza vitufe vinavyostahili, kisha akaitega sikioni. ‘Namba unayopiga kwa sasa haipatikani, tafadhali jaribu tena baadaye.’ Ndio ujumbe uliomjia sikioni.

“Kha!” alibwata kwa hasira. Hakutegemea kukuta simu ya Kibutu haiko hewani. Alijua utamaduni wa Kibutu ni kuhakikisha simu yake haizimwi. Sasa kama kamtumia ujumbe kuwa spika ina matatizo, mbona muda huu inaonesha dhahiri kuwa imezimwa?

‘Leo akiniletea ujinga ka’ jana nakata mawasiliano! Mtu anakuwa bwege wa kutekwa na wanawake kama nini sijui’ aliwaza kwa hasira. Alimjua kuwa ni mtu awapendaye sana wanawake. Japo alikiri wote walikuwa na ugonjwa huo, lakini yeye, kama yeye, alikuwa makini hasa kwa mambo ya utafutaji wa pesa. Hakuwa bwege wa kuendekeza ngono. Aliamini yuko hivyo, japo pia alijijua kuwa kama ana pesa za kutosha mfukoni, hakuwa tayari kumwachia mwanamke mzuri, mwenye kustahili kutamkiwa matamshi yanayomstahili.

Mbona siku ile alishiriki ngono ya kuchangia kule Komakoma kwa mtu aliyemhusu Kibutu? Ni kwa kuwa yule mwanamke alikuwa mzuri kupindukia. Kama mwanamke yule angekuwa wa kawaida tu, kama wanawake wengine wa kawaida, katu asingediriki kuchangia upuuzi ule. Yule mwanamke aliyeletwa na Kibutu alikuwa amekamilika kila idara! Ndivyo Kisengo alivyoamini.

Kwa kiasi fulani alijisikia kumpata tena, lakini atamwona wapi? Alikuwa ni mwanamke mwenye mvuto mkali, laiti kama kitendo kile kingefanywa na mwanamume mmoja, na mwanamke akiwa ameridhia, huenda ungepatikana ushirikiano halisi kiasi cha mwanamume kuridhika kwa kiasi kikubwa katika tendo lile. ‘Kama mimi ningekuwa Kibutu, nisingemfanyia vile, ningetumia mbinu zote za kiume, mpaka angelainika tu. Na siku ambayo angeingia kwenye sita kwa sita, pasingetosha daaadek!’ alijisemewa kimoyomoyo.

Alihisi Kibutu kuwa ni dhaifu katika utongozaji. Hajui kujieleza na huenda pia hajui kutumia pesa. Pia, alihisi huenda wanawake hawamkubali kutokana na ufupi wake na mwonekano wa sura yake isiyo na mvuto wa kiume. “Ndiyo maana akimpata mwanamke anakuwa zoba,” alijikuta akinong’ona huku akiipeleka chupa ya bia kinywani na kupiga funda zito.
Kwa hasira tena, akaamua kutuma ujumbe, ‘Vipi uko wapi? Saa moja kamili nasepa zangu.’ Alipoutuma ujumbe huo, akagundua kuwa haujaingia. Akaifungua simu yake kwenye mtandao wa fasebook na kwenda moja kwenye akaunti ya Kibutu ili aone kama labda alikuwa hewani muda mfupi uliopita au yuko hewani wakati huo. Huko nako akakuta hayuko hewani. Hata hivyo, pia akaamua kumtumia ujumbe kama huo wa awali.
Saa kumi na mbili u nusu!
Moja kasoro!

LABDA ni ile kawaida kwa asilimia kubwa ya wanawake kutokwenda na muda. Hadi saa saa kumi na moja na dakika nyingi, bado Scolastica hakuwa ameanza kujiandaa kwa lolote katika kuendeleza ile ratiba aliyojipangia. Baada ya kuletewa chipsi na nusu-kuku, akalijaza tumbo kisha akashushia na juisi baridi ya nanasi, alijilaza sofani akiwa na nguo pekee ya ndani, laini, akijisikia kuwa huru kwa kuwa alikuwa kajifungia na hakutaraijia kupigiwa hodi.

Alirudia kupekua simu ya Kibutu, na kuzibaini picha zaidi, nyingi zikiwa za video za ngono, zilizochezwa na watu weusi, ngoma za baikoko, ngoma za jadi za Jamaica zilizohusishsa ngono kwa aslimia mia moja, na moja, ni ya Kibutu mwenyewe akiwa na mwanamke aliyekuwa akimbusu, kumtomasa na kumnyonya sehemu mbalimbali mwilini.
Alipochoka kuipekeua simu hiyo, akaitwaa ya kwake na kuanza kuangalia taarifa mbalimbali za ulimwenguni kutoka katika mashirika ya habari tofauti, makubwa duniani. Alikuja kuachana na simu saa kumi na mbili kasoro. Akaingia bafuni kuoga kisha akaanza kuchagua nguo ya kuvaa kwa jioni hiyo maaalum.

Hakutaka kufanya kosa. Alihitaji kuwa katika mwonekano uleule wenye mvuto mkali mbele ya mwanamume yeyote mkamilifu kimwili na kisaikolojia. Hivyo, alichagua gauni refu la kitambaa laini, jekundu, mikanda ikiwa imezunguka mgongoni na kuliacha wazi eneo kubwa la mgongo wake, mabega nje, huku nywele ndefu na nyeusi tii zikiwa zimemwagika kwa nyuma. Aliona kuwa sasa kakamilika. Kavutia. Akaliachia tabasamu la mbali huku akiyarembua macho kidogo.

“Niko vizuri mtoto wa kike,” alijitapa kwa mnong’ono huku akiendelea kujikagua. Gauni hili lililomshika vilivyo eneo la mapajani, lilimuweka katika ule mwonekano uvutiao, kama siku alipokuwa Mood Bar, macho ya wanaume waroho yakimfuata wakati akielekea msalani.

Ni mwanamume gani ambaye hatavutiwa na haya macho yaliyolegea ya mtu anayeonekana kazidiwa na ashiki? Ni mwanamume gani mkamilifu, ambaye hataduwaa kwa muda pale atakaposhuhudia umbo zuri, lililotanuka mapajani kwa namna isisimuayo lilipita mbele yake? Ni mwanamume gani rijali ambaye hatayagandisha macho kwenye robota la kiuno ambalo litakuwa likijitupa huku na huku kama lililodhamiria kuwadhihaki wanaolitazama?

Akaachia kicheko cha chinichini baada ya kuridhika kuwa sasa alipaswa kuendelea na hatua nyingine. Alitwaa manukato yake yale ya bei ghali, akajipulizia, kisha akautwaa ule mkoba wake maalum kwa safari maalum.
Akaufungua na kuangalia kama kila kilichopaswa kuwamo, kimo. Kilikuwamo. Akaiangalia saa, na kukuta ni moja kasoro dakika kumi. Akaichukua simu ya Kibutu na kuiwasha. Mara akauona ujumbe ukiingia; ‘Vipi uko wapi? Saa moja kamili nasepa zangu.’

Akashtuka na kuharakisha kuondoka. Hakuyashangaa macho ya wapitanjia wenzake aliokutana nao, ambao hawakusita kumzungumzia pale alipopishananao.
“Kuna watu hawakuzaliwa…wameshushwa tu na mola,,."
“Duuu….Mungu anaumba…"
“Nikimpata huyu ataomba poo….”
Yalisemwa mengi, akayasikia na kuyaacha kama yalivyopenya masikioni mwake. Dakika chache baadaye alikuwa ndani ya bajaji akienda Maseru Bar, Kinondoni Mkwajuni.

****ITAENDELEA KESHO


Sent using Jamii Forums mobile app
 
mzee baba Baharia Wa Buza tupia kama vipande vitano hv viwe vinansaidia kupoteza muda... npo hapa magogoni kwenye interview sa naona muda hauendi kabisa... tupia vi5 vinsukume mpaka zamu yangu ifike
 
SEHEMU YA 21

“Kuna watu hawakuzaliwa…wameshushwa tu na mola,,,
“Duuu….Mungu anaumba…
“Nikimpata huyu ataomba poo….”
Yalisemwa mengi, akayasikia na kuyaacha kama yalivyopenya masikioni mwake. Dakik chache baadaye alikuwa ndani ya bajaji akienda Maseru Bar, Kinondoni Mkwajuni.

***ENDELEA***


Wakati akivuka kituo cha mwendokasi cha Mwanamboka, akaitwaa ile simu ya Kibutu na kuiwasha. Kisha akmtumia ujumbe Kisengo. ‘Niko njiani. Dakika tano tu nitakuwa hapo.’ Ilionesha dhahiri kuwa ujumbe huo umeingia. Hakuhitaji kujibiwa. Papohapo akaizima simu hiyo na kuirudisha mkobani.

Bajaji ile ilisimama jirani na Barabara ya Katumba. Scolastica akateremka na kurejea nyuma. Alipofika nje ya baa hiyo, akasikia mchanganyiko wa kile alichoona yeye kuwa ni kelele. Kulikuwa na kishindo cha muziki wa Kikongo kutoka katika spika zenye nguvu huku upande mwingine, sauti za mabishano ya watu waliokuwa wakiangalia mechi ya soka na spika zilizokuwa zikitangaza mechi hiyo nazo zikisikika kwa nguvu.

Akilini mwake hakupaona hapo kama palimstahili mstaarabu yeyote apendaye utulivu wakati akijipatia kinywaji. Lakini yeye hakuhitaji utulivu au vurugu. Alimhitaji Kisengo. Alihitaji kukamilisha lililomleta hapo. Sura ya Kisengo ilikuwa kichwani na hasa ikichangiwa na picha za kwenye ile simu na pia kumbukumbu ya siku ile ya kuudhi kule Komakoma.
Jioni hii hakutaka kubahatisha wala kuchelewa. Alitaka kuwa na hakika kuwa Kisengo yumo humo baa na kama kweli yumo, akimwona, ajilengeshe bila ya kuchelewa. Alipokuwa akiingia, alifurahi kubaini kuwa kwa siku hii, labda kutokana na hali ya hewa ya manyunyu, hakukuwa na wateja wengi. Baadhi ya meza zilikuwa tupu.

Angeweza kukaa hata hapa mwanzo kabisa alipoingilia, lakini hakufanya hivyo, alitaka kuhakikisha kuwa kwanza anayaona mawindo yake. Akavuta hatua fupi fupi akielekea kaunta. Kama kawaida, hii tembea yake ya kujidai iliyavuta macho ya watu na hasa wale wanaume wenye akili zisizotulia.

Kama kawaida hakuyajali hayo macho. Alivuta kiti kirefu cha pale kaunta na kuketi. Akaagiza bia. Bado alikuwa makini, macho yake yakitambaa kwa chati ukumbini humo na sasa alianza kuhofia kuwa kama ule ujumbe aliotuma Kisengo kuwa saa moja anaondoka, utafanyiwa kazi, basi huenda kweli muda huo ama akawa ameondoka au anajiandaa kuondoka.

“Dada niangalizie bia yangu,” alikurupuka kuisogeza bia ndani ya kidirisha cha kaunta.
“Vipi tena,” mhudumu wa kaunta alimuuliza huku akiisogeza ndani zaidi hiyo bia.
“Nafika toilet,” Scolastica alijibu huku akishuka kwenye hicho kiti kirefu.
Mhudumu alimwelewa. Scolastica alitembea taratibu akifuata uelekeo wa vyoo. Bado macho yake hayakuwa yametulia lakini haikuwa rahisi kwa yeyote mwenye macho ya kawaida atazamaye kwa upeo wa kawaida ambay e angeweza kumshtukia.

Alikuwa hata hajakifikia choo cha kike, alipotupa macho kulia, ukutani, akamwona Kisengo! Macho yao yakagongana, lakini yeye akayaepusha yake katika hali ya kawaida, akionekana kutojali wala kuhofia chochote, zaidi tabasamu la mbali likachanua na alitaka Kisengo alione.

Hakukuwa na chochote kilichompeleka huko msalani, lakini alilazimika kukaa dakika nzima kisha akatoka. Safari hii, kwa kudhamiria kabisa, akamtazama tena Kisengo na macho yao kwa mara nyingine yakagongana. Kama awali, mwanamke alipoyaepusha macho yake ni kama vile alikuwa na soni na kama kuna jambo alilolihitaji kwa Kisengo lakini anaona aibu kulitamka. Akaendelea kutembea taratibu akirudi kaunta, akiyaacha macho ya wengi yakimfuata.
*****
UJUMBE ulioingia kwenye simu ya Kisengo ulimkuta saa moja na dakika tano, muda ukiwa umeshapita kama alivyomuahidi Kibutu. Hata hivyo, hakujali, alizijua tabia za waswahili. Akikuahidi kukutana saa mbili, atakuja saa tatu. Usijali, ndivyo tulivyo.

Alichofanya ni kuagiza bia nyingine, akiendelea kusubiri. Ni wakati huo ndipo macho yake yalipomwona mwanamke mrembo akitokea kaunta akienda msalani. Akavutiwa na umbo lake, tembea yake na macho yake. Lakini pamoja na hayo, alihisi kuwa anamwona mwanamke mrembo ambaye si mgeni sana machoni mwake. Alimwona wapi na lini? Swali hilo likaelea hewani na kabla hajapata jibu, macho yao yakagongana, na mwanamke alipoyaepusha yake, alikuwa kama anayetamka jambo fulani au kama anayemfahamu.

Wapi nimeliona toto zuri hili? Kisengo alijiuliza tena wakati akiendelea kumtazama mgongoni na kukiri kuwa ni mwanamke mzuri, huenda zaidi ya wazuri aliowahi kuwaona. Robo saa tangu ule ujumbe umjie kuwa ndani ya dakika tano Kibutu angekuwa hapo, bado hakukuwa na hata mzimu wa Kibutu. Tayari bia aliyoagiza kama kuvutia muda akimsubiri ilikwisha. Akaamua kuachana naye na sasa damu ikiwa inamchemka, hakumfikiria tena yule mhudumu bali, alitaka kuicheza karata kwa huyu mwanamke mzuri, aliyeingia dakika kadhaa zilizopita.

Akajitoa pale kitini na kuelekea kaunta ambako kulikuwa na viti vingine viwili virefu vilivyokuwa tupu. Akaketi kiti kilichokuwa jirani na alipoketi Scolastica. Akaanza kwa kumtupia salamu, kisha dakika kumi baadaye wakawa wamezama katika maongezi ya kawaida na hata majina wakiwa wameshatambulishana, Kisengo akijitambulisha jina halisi ilhali, Scolastica akijiita Flora.

Maongezi yao ya kawaida, yaliwapeleka hadi saa tatu, Kibutu akiwa hajatokea na sasa Kisengo akaomba heri asitokee tena. Alimhitaji huyu mwanamke mzuri ambaye japo kichwa chake kilikuwa kimeshabeba bia tano, hata hivyo alihisi kuwa aliwahi kumwona mahala. Dukuduku hilo lilmfanya ajikute anamuuliza, “HIvi, Flora unasema unaishi Ubungo?”
“Ndiyo.”
“Kwa hiyo, hapa umekuja ukitokea Ubgngo?”
“Nd’o maanake.”
“Hujawahi kuishi hukoiu?”
Scolastica alitikisa kichwa akikataa. “Hii Kinondoni siijui kabisa yani. Na hapa nimekuja nikiwa na apointoimenyti na mdada flani lakoini naona nleo ndo basi tena. Saa nne narudi zangu home.”
“Basi naona nimekufananisha.”
“Na?”
“Na sister mmoja alikuwa akiishi huko Kinondoni ‘B’ kama
sikosei.”
“Yeah, huenda kweli umenifananisha. Huku sipajui kabisa.”
“Kwe;li duniani, wawili-wawili.”
Akilini mwa Scolastica, hakushangazwa na upotezaji wa kumbukumbu wa Kisengo. Siku ile alipobakwa, huyu Kisengo alikuwa na chupa ya pombe kali akinywa taratibu na alionesha dhahiri kuwa alikolewa na kilevi hicho. Matokeo yake ndiyo haya ya kuishia kufananisha.

Kimoyomoyo Scolastica alimcheka huku akijisemea, ‘leo ni mimi na wewe.’ Aliyagundua macho ya Kisengo yakimtazama zaidi ya utazamaji wa kawaida, yakidhihirisha njaa aliyonayo. Ni hilo alilolihitaji Scolastica, na hivyo akawa naye akiliachia lile tabasamu lake la kunyanyasa, tabasamu ambalo huwaroga wanaume wengi marijali.

Uchawi wa bia ukizidi kujidhihirisha katika akili ya Kisengo, aibu zikawa zimejitenga naye kwa umbali wa kilometa kumi kutoka hapo kaunta. Sasa akarusha ndoana kwa kujiamini. Mtiririko wa fasihi ukawa bayana katika ncha ya ulimi wake, macho yasiyopepesa ovyoovyo, yakiwa hayabanduki usoni mwa mwanamke huyo.

Zile laki mbili na ushei zilizokuwa zimepungua kidogo, zilikuwa nyenzo ya kumfanya ajiamini zaidi. Isitoshe, bia hii ya sita iliyokuwa nusu, nao ilimwongezea uchu wa kutaka usiku huo aumalize akiwa na Scolastica katika gesti yoyote.
Akamshawishi asirudi Ubungo usiku huo, ushawishi uliopata upinzani mdogo, upinzani bandia. Hatimye ukawa ni ushawishi ulioshinda. Saa tano ikawakuta wakimalizia bia zao lakini Scolastica akashauri waondoke na bia mbili, mbili.

“Hakuna shida,” Kisengo alisema kwa kiburi. Ndiyo, alijisikia kuwa mshindi kwa ombi lake kukubaliwa na Scolastica na hata alipoombwa kuchukua bia za ziada hakuona kuwa kuna tatizo lolote. Bado alikuwa hajalewa. Kwake, bia kilikuwa ni kinywaji laini, cha kawaida ambacho ili kifanye kazi njema kichwani mwake, alipaswa kunywa bia nane na kuendelea.
“Au tatu, tatu,” alimuuliza Scolastica huku akimpigapiga pajani.
“Mbili tu zinatosha. Hata kesho ni siku. Tunaweza kunywa hiyo kesho.”
Mpaka kufikia makubaliano yao, Kisengo alikuwa ameshawaza ampeleke wapi mwanamke mzuri kama huyu? Ni mwanamke aliyeonekana kuwa ana maisha mazuri. Hastahili kupelekwa kwenye gesti za kawaida hapo Kinondoni Moscow. Alipaswa kupelekwa kwenye hoteli yenye hadhi, kiyoyozi ukutani, runinga bapa ukutani, kisengeretua kikiwa kando yake.

Aliwaza na kuwazua hatimaye akaikumbuka Madina Guest House. Hiyo gesti ilikuwa Barabara ya Mwinjuma. Ilikuwa mpya na yenye hadhi iliyostahili kwa mtu wa aina ya Scolastica kulala.
Kisengo aliamini hivyo. Saa tano u nusu walikuwa ndani ya bajaji wakielekea huko Madina, mfuko wa bia nne ukiwa umekumbatiwa na Kisengo ilhali Scolastica akiwa na mkoba wake.

***ITAENDELEA


Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 22


TULIPOKOMEA....


Aliwaza na kuwazua hatimaye akaikumbuka Madina Guest House. Hiyo gesti ilikuwa Barabara ya Mwinjuma. Ilikuwa mpya na yenye hadhi iliyostahili kwa mtu wa aina ya Scolastica kulala. Kisengo aliamini hivyo.
Saa tano u nusu walikuwa ndani ya bajaji wakielekea huko Madina, mfuko wa bia nne ukiwa umekumbatiwa na Kisengo ilhali Scolastica akiwa na mkoba wake.

***ENDELEA***

Bajaji iliposimama nje ya gesti hiyo, Scolastica alikerwa na mazingira ya hapo nje. Kulikuwa na taa mbili zenye nuru kali kiasi cha mtu kuweza kuokota hata sindano ndogo chini. Taswira hiyo ilimfanya aamini kuwa kama mtu yeyote aliye umbali hata wa mita zaidi ya hamsini, anaweza kumtambua kama atamwona hapo nje. Hivyo, wakati Kisengo anasubiri dereva ampe chenji yake, Scolastica aliteremka haraka na kuvuta hatua ndefu akiingia ndani ya gesti hiyo.

Si dereva wa bajaji wala Kisengo, aliyeijua sababu halisi ya Scolastica kuwahi kuingia ndani ya gesti hiyo kabla ya aliyempeleka. Walijua tu kuwa ni ile dhana ya mwanamke kutopenda kuonekana akiingia gesti.
Alimkuta kijana wa mapokezi akiwa ametulia akiangalia runinga bapa iliyokuwa ukutani ikionesha tamthiliya ya nchi moja ya ughaibuni.

“Karibu dada,” kijana huyo aliyaondoa macho kwenye runinga, akamtazama sawia.
“Poa,” Scolastica alijibu huku akilifuata sofa lililokuwa kando ya mlango na kuketi.
Muda mfupi baadaye, Kisengo naye akaingia. Yeye akaenda moja kwa moja kaunta na kuzungumza na kijana huyo wa mapokezi. Kisha akatoa kiasi fulani cha pesa na kumpatia. Wakaendelea kuzungumza kwa sauti ya chini, maneno ambayo hayakuweza kuyafikia masikio ya Scolastica.

Kisha kijana huyo akajitoa kitini na kutangulia, akiifuata korido ndefu yenye vyumba vitano kulia na vitano kushoto. Kisengo alimfuata huku akimwashiria Scolastica amfuate. Korido hiyo ilikata kulia ambako kulikuwa na vyumba vingine vitano, vitano pande zote mbili. Hatimaye kijana huyo alisimama mbele ya chumba namba 7. Akachambua funguo alizoshika mkononi. Akaupachika mmoja ndani ya kitasa. “Karibuni,” alisema huku akitangulia kuingia.
Kilikuwa ni chumba kipana na kilichovutia. Kitanda kipana, chenye godoro nene na shuka nyeupe, kilikuwa mbele yao, chini ya dirisha pana, lililofunikwa na pazia zito jekundu.

Upande mmoja wa chumba hicho, ukutani, kulikuwa na runinga bapa kubwa iliyokuwa ikiendelea kuonesha muziki katika chaneli moja ya nje ya Tanzania. Kisengeretua cha kumsaidia mpangaji kubadili chaneli kwa jinsi atakavyo, kilikuwa juu ya kimeza kidogo, kando ya kitanda. Kiyoyozi cha kisasa kilichoonesha dhahiri kuwa bado ni kipya, kilikuwa upande mwingine ukutani kwa juu zaidi. Kwa jumla chumba hicho kilikuwa kikivutia kwa kiwango kikubwa. Kisengo alipitisha macho huku na kule akiwa amesimama na kutikisa kichwa akionesha kukubaliana nacho.

Hatimaye alimgeukia yule kijana wa mapokezi na kumwambia, “Ni chumba kizuri. Kwa jinsi kilivyo, kilistahili pia kuwa na choo, bafu humuhumu. Mengine yote mmejitahidi.”
Kijana yule aliachia tabasamu la mbali kisha akasema, “Ni kweli, lakini naona bosi hapo nd’o uwezo wake ulipoishia na hata niliwahi kumsikia akisema kuwa alipenda iwe hivyo unavyosema lakini akahofia kuwa hatapata wapangaji wa kutosha kutokana na gharama yake kuwa tofauti na hivi vilivyo. Na eneo lenyewe hili la huku, alihofia kupata hasara.”
“Labda alikuwa sahihi, lakini pia ni kwa kuwa hakujiamini tu.”

Wakati huo wote Scolastica alikuwa kimya, naye akikitupia macho chumba hicho ilhali akilini mwake akiwa na mambo mengine kabisa. Kwake, usafi wa chumba hicho na hewa nzuri, halikuwa jambo la kumwingia akilini. Alichohitaji ni wasaa wa kukamilisha ratiba yake, basi! Hata kama humu kungekuwa hakuna hata kitanda asingejali; hata kama kungekuwa pachafu kupindukia, isingekuwa kero kwake; hata kama kungekuwa kunatumia mwangaza wa kibatari, asingeumia moyo; alijali kuwa na mwanamume wake, Kisengo, wastarehe.

“Kwa hiyo toilet nd’o wapi?” Kisengo alimuuliza kijana huyo.
“Twende nikakuonyeshe.”
Walitoka wao tu, Scolastica hata hakunyanyuka. Alichofanya ni kuchukua chupa moja ya bia na kuifungua kwa meno kisha akaanza kunywa. Alitaka huyo Kisengo akitoka huko kuoneshwa choo, asifikie kumkumbatiakumbatia na labda akihitaji mapema zaidi; alitaka akija na yeyey aifungue bia yake, anywe.
Haukupita muda mara Kisengo akarejea. Na kama Scolastica alivyohisi, ni kweli baada ya kurudisha mlango, alimfuata na kuketi kando yake kisha akambusu shavuni, busu ambalo halikuwa chochote wala lolote katika hisia za Scolastica.
“Kunywa bia yako,” Scolastica alimwambia. “Hatukuzibeba kwa ajili ya kuja kuzihifadhi gesti. Hapana. Tunywe kwanza, ndipo mengine yaendelee.”
Kisengo aliachia cheko dogo huku akimtomasa Scolastica titi la kulia. “Nimekuelewa babe.” Akaitoa chupa moja na kuiweka kwenye kijimeza kilichokuwa mbele yao. Kisha ghafla akamgeukia Scolastica na kumuuliza, “Umeifunguaje bia yako? Una ‘opena’ au…”
“Au nini?” Scolastica alimdaka.
“Au umefungulia meno?”
Scolastica akaachia tabasamu kubwa huku tena akishusha funda la kinywaji kooni. “Ungetegemea nifungulie nini?”
Kisengo akaachia cheko dogo. “Dah mrembo utajing’oa jino bure! Ngoja niende kaunta nimuulize dogo kama ana ‘opena’ maana nimeona kama kuna kreti ya chupa za soda na bia pale chini.”
“Na ukija unafungua na kuwarudishia,” Scolastica ni kama alitoa amri. “Siyo baadaye tunakuja kugongewa mlango wakati tuko kwenye mambo yetu…”
“Yeah, ni kufungua chupa zote na kurudisha ‘opena’ yao.”
Kisengo alipoondoka tu kwenda mapokezi, Scolastica alitikisa kichwa huku akiachia tabasamu la mbali. Hazikutimu dakika tatu, Kisengo alirejea, na kifaa cha kufungulia chupa hizo. Akazifungua kimadaha, zikitoa mlio kama zinazolipuka, akijiona kuwa ni mkongwe wa kufungua vinywaji.

Kisha akambusu tena Scolastica shavu la kulia na kushoto na alipojaribu kumpenyezea ulimi, Scolastica aliuepusha mdomo wake huku kwa sauti ya deko la kike, akisema, “Bwanaaaa….haraka nini? Tupo wote mpaka kunakucha…hebu rudisha kwanza hilo dubwasha lao. Halafu…”
Neno la mwisho likamshtua kidogo Kisengo. Akasita kuondoka na kumtazama Scolastica kwa makini. “Halafu…?” alimuuliza.

“Nahitaji vocha, itakuwaje?”
Kisengo aliguna. “Vocha ya nini saa hizi? Kwani kuna dharura gani?”
“N’tapata au sipati? Mi’ naihitaji tu kwa ajili ya mawasiliano yangu mitandaoni.”
Kisengo alitikisa kichwa akijua wanawake ni wadau wakubwa wa kuperuzi mitandaoni. Lakini kuna umuhimu wa kuperuzi mitandaoni usiku huu ilhali kilichowaleta hapo ni kitu kingine kabisa? Hakumwelewa, lakini hakutaka kumkwaza. Akasema, “Hapo nje kuna baa moja ni kama night club na ni inakesha kwa kuwaendekeza machangu wanaozagaa hapo. Huwa pia kuna vocha. Ngoja nikakchukulie. Mtandao gani??”
Akatajiwa.
“Ya sh’ngapi?”
Pia akatajiwa.
Akatoka.

SI kweli kuwa Scolastica alihitaji vocha , alihitaji nafasi ya kutosha kukamilisha kila alichokikusudia. Mara tu Kisengo alipoondoka, yeye akatikisa kichwa kama anayesikitika. Lakini mara tabasamu la mb ali likamtoka huku akitwaa chupa na kunywa funda zito la bia yake ya chupa hiyo ndogo.

Alijua kuwa Kisengo hatawahi kurudi, ni lazima zitamchukua takriban dakika tano hadi kuingia tena ndani humo. Hivyo alichofanya baada ya kuirudisha chupa mezani, ni kuufungua mkoba wake na kuitoa tembe moja ya Olanzapin kati ya mbili zilizokuwamo. Haraka akaiweka tembe hiyo mezani na kutwaa chupa ya bia ya Kisengo. Akaikandamizia kwenye tembe hiyo kwa nguvu. Akahakikisha kuwa anaisaga vizuri kisha akapekua tena ndani ya mkoba wake na kutoa kijikaratasi kidogo ambacho aliwahi kulipia umeme kwa wakala siku nyingi zilizopita.

Akakitwaa kifuniko cha bia moja kati ya mbili za Kisengo, akakitega jirani na kingo ya meza. Kisha akaanza kuuvuta ule unga wa ile tembe taratibu kwa kutumia kile kijikaratasi. Alikuwa makini lakini pia akihakikisha kuwa hachelewi kulimaliza hilo alilolifanya.

Ndani ya dakika moja alikuwa amewishaumimina unga ule wa tembe ndani ya kile kifuniko cha bia. Na sasa, aliumimina kwa umakini ndani ya chupa moja ambayo pia aliiweka mbele zaidi na ikawa karibu na hii aliyokuwa akinywa yeye.
Wakati ungaunga huo ukitengeneza atomi ndani ya kinywaji, Scolastica alishuhudia kwa usahihi, na akaamini kuwa amekamilisha hatua muhimu iliyomleta humo chumbani. Akatwaa kitambaa ambacho kilikuwa juu ya mto mmoja kitandani na akapangusa pale mezani alipokuwa amesagia ile tembe. Kitambaa hicho hakikurudishwa pale kwenye mto, alikitupa uvunguni mwa kitanda.

Kisha alinyanyuka na kuelekea huko maliwatoni. Akakumbuka kuwa wakati Kisengo akipelekwa kuoneshawa, yeye alibaki, hivyo hakupajua. Akaamua kwenda mapokezi haraka kumwona yule kijana. Alimkuta akiendelea kuikodolea macho ile tamthiliya kwenye runinga. Akamuuliza na akaelekezwa. Muda mfupi baadaye alikuwa akitoka huko maliwatoni huku akiwa amenawa mikono vizuri kwa sabuni. Na sasa alijiamini kuwa yuko salama zaidi.
Alipokuwa akirudi chumbani, alikutana na Kisengo naye akiingia.

***ITAENDELEA****

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom