RIWAYA: SCOLASTICA TEMU (13)
MTUNZI/ MWANDISHI: INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)
MWAKA 2002 GAZETI LA LETE RAHA
MAREKEBISHO: MWAKA 2016
TULIPOKOMEA...
KIBUTU alikwishaigeuza sheria badala ya kawaida, ile tabia yakwenda Mood Bar kunywa bia kila siku. Jioni ya siku hii, kama jana na juzi, akiwa na kiburi cha kulipwa shilingi milioni tatu kutokana na zabuni hewa aliyopewa na kampuni iliyokuwa ikitumia teksi yake kwa kutoa huduma, alijisikia kuwa katika sayari nyingine. Nani kama yeye?
***ENDELEA***
Juzi jioni aliingia hapo Mood Bar akiwa na shilingi laki tano, akaondoka na elfu hamsini! Hakujali. Jana kaondoka na laki moja japo aliingia na laki tatu. Alimnunulia yeyote kinywaji au kitafunwa. Jioni hii, alikuja na vijana wawili, marafiki zake, ambao walikuwa ni ndugu wa mwenye nyumba wake. Kibutu alielewana sana na vijana hao na katika kuonesha kuwa anawajali, ndipo alipowapigia simu ili waje hapo Mood Bar saa kumi na moja jioni.
Hadi kufikia hii saa tatu kasoro usiku, tayari Kibutu alikuwa na bia tano kichwani na wale vijana nao kila mmoja akiwa ameshusha bia kadhaa. Walizungumza hoja hii na ile lakini zaidi, hoja iliyozikamata ndimi zao ni kuhusu soka la Ulaya, wakizungumzia usajili wa timu mbalimbali maarufu za huko.
Pia, kilifika kipindi, vijana hao ambao kiumri walikuwa wadogo kwa Kibutu, walianza kumshawishi ajiingize katika mchezo wa bahati nasibu, maarufu ‘kubeti’ kufuatia matokeo mabalimbali ya mechi mbalimbali za soka duniani.
Wakati wakiendelea kuongea, wakicheka na kutaniana, sauti zao zikiwa za juu, mara macho ya Kibutu yaliganda kwa mwanamke aliyepita jirani, nao akielekea msalani. Macho hayo yakazidi kumganda mwanamke huyo, yakiwa yametua kwenye lile robota la kiuno, ambalo ni kama lilikuwa limeamua kuwadhihaki na kuwanyanyasa kusudi wote waliolikodolea macho.
Ugonjwa wa Kibutu ni wanawake wenye maumbile ya aina hiyo. Bia tano zilizokuwa zimekwishaichangamsha damu yake, zilimvuta awasahau kwa muda hawa vijana. Na kwa jumla pia, pamoja na kwamba kwa kiasi fulani uchangamfu kutokana na bia hizo, ulikuwa umeongezeka, hata hivyo haukumpotezea ule ugonjwa wa kuhitaji warembo.
Akaguna wakati akimshuhudia yule mwanamke akitokomea msalani. Alipoyarejesha macho kwa vijana hawa, akakuta nao wakimtazama huku tabasamu zikichanua nyusoni pao. Mmojawao akamchokonoa, “Kaka, kama kawaida yako, viumbe wa aina hiyo hawakupiti! U’shasahau hata tulichokuwa tukiongea!”
Wote wakacheka.
“Acheni tu wadogo zangu,” hatimaye Kibutu aliipata sauti yake. Akaitwaa glasi ya bia na kuipeleka mdomoni. “Unajua wadogo zangu, wanawake wengine ni kama hawakuzaliwa duniani; walishushwa toka mawinguni maja kwa moja daaaadek! Mana’ake dah!”
Vijana wale wakacheka na kumuunga mkono, kila mmoja akionekana kumsifia huyo mwanamke aliyekuwa kaingia msalani. Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo aliporejea, Kibutu na vijana hao walijifanya kama hawana mpango naye. Lakini kisirisiri, walimtupia macho, kila mmoja kimoyomoyo akivutiwa na tembea yake na umbo lake. Kibutu alijiepusha kumwangalia moja kwa moja usoni, ila alipowapita, kama awali aliunyanyua uso na kumtazama tena.
Alipoyarejesha macho kwa vijana hawa ambao sasa walikuwa wamezirejea bia zao, nao wakamtazama sawia.
“Kaka vipi? Umeuona mzigo huo?” mmojawao alimuuliza.
“Siuachii!” Kibutu alijibu kwa sauti ya kujiamini, macho yake mekundu yaliyoshiba kilevi, yakiwatazama kwa zamu.
Vijana wakacheka.
“Siwatanii!” Kibutu alisisitiza huku akiangalia mwanamke yule anakoishia. Alipomwona kaketi, naye akairejea bia yake.
“Mnasikia wadogo zangu,” alisema, “kuna wakati ukiwa katika rika la ujana, inabidi uutumie ujana wake ipasavyo. Mambo mengine, usipoyafanya ujanani, utajikuta unayakurupukia uzeeni. Hapo ndipo utalkapoonekana chizi na limbukeni wa kutupwa! Changamkeni katika miaka hii. Mimi sifanyagi uzembe. Kama mfukoni kuna mkwanja kidogo kwa nini usiyafaudi maisha?
“Kuna maisha gani zaidi hapa duniani kama haya? Ni kunywa na kuwafaidi mademu wazuri. Kesho Mungu akikwambia njoo, unaenda ukiwa umeyatekeleza majukumu yako yote!” Vijana wale walitikisa vichwa wakionesha kuafikiana naye, labda kinafiki kwa kuwa kawanunulia bia. Kuna ule usemi kuwa ‘anayekupa ofa ya bia, akizungumza uongo au hata akizungumza jambo aambalo huwezi kuafikiana naye, usimpinge; kubaliana naye.’ Watoto hawa wa mwenye nyumba wake waliifuata sera hiyo.
Wakaendelea kuzungumzia soka la Ulaya huku akili ya Kibutu ikiwa zaidi kwa yule mwanamke mzuri aliyeikamata akili yake. Kitu kimoja kilichomsumbua kidogo, ni kwamba, kanywa bia lakini hizi bia ni kama zimelijaza zaidi tumbo kuliko kuiweka akili katika ujasiri aliouhitaji. Alihitaji kuwa jasiri na kujiamini hasa atakapokuwa anaongea na yule mwanamke mzuri. Akaamua kuagiza toti tano za pombe kali. Alipoletewa, alizinywa kama maji ya kawaida na kumrejeshea mhudumu glasi. Akakunja uso kidogo na kushusha pumzi ndefu. Sasa akajihisi yu katika hali aliyoihitaji.
Akaagiza bili yake. Alipoletewa, alilipa kisha akawaagizia vijana wale bia mojamoja na kuwaambia, “Wadogo zangu, ngoja nikabeti kwa yule mrembo.”
SCOLASTICA TEMU alishangaa kumwona Kibutu akiisogelea meza hii huku akiwa na glasi ya bia mkononi. Alitembea huku mkono wa kushoto ukiwa ndani ya mfuko wa suruali na alionekana kuwa na maringo fulani, labda kutokana na pesa alizozimiliki jioni hiyo.
Wakati huo yule dada aliyekuwa kaagiza mlo alikuwa kishaondoka. Kibutu alipoifikia meza hiyo, aliitua glasi mezani kisha kwa sauti yenye kijimkwaruzo cha kilevi, akamuuliza Scolastica, “Mama mdogo, naweza kuketi, au kuna wenyewe?”
Sema yake ya majidai, sauti yake ya kilevi, harufu kali ya jasho la pombe kwenye mavazi yake, vilimfanya Scolastica amcheke kimoyomoyo huku akimdharau kwa kiwango cha juu. Akajifanya kama hajamsikia, akaendelea kuyagandisha macho kwenye simu yake, akichati ‘kimagumashi.’
“Shangazi, naruhusiwa kukaa?” swali lingine.
“Kaa tu,” Scolastica alijibu huku akiendelea kuyaepuka macho yake.
Kibutu akaketi. Papohapo mhudumu alikuwa mbele yake. “Lete bia na mwongeze shangazi hapa kinywaji,” alisema kwa sauti yake ileile ya kilevi. Mhudumu alipoondoka ndipo sasa, kwa nguvu ya mchanganyiko wa bia na zile toti kadhaa za pombe kali, ujasiri ukamzidia Kibutu. Hakujali wa kuogopa chochote. Alimhitaji huyu mwanamke mrembo aliyeyateka macho ya wengi humo ukumbini.
Lakini mara akashtuka alipomtazam kwa makini usoni. Haikuwa sura ngeni machoni mwake. Japo alikuwa na bia kadhaa kichwani, akachanganya na toti kadhaa za pombe kali kiasi cha kuunda ulevi wa kiasi fulani ubongoni, hata hivyo hakuwa mwehu. Nani kasema kuwa mtu akilewa anakuwa mwehu? Mwehu ni mwehu na mlevi ni mlevi! Mbona mtu anakunywa bia kumi au mizinga kadhaa ya pombe kali na anafika nyumbani kwake?
Imani hiyo ilikuwa kichwani mwa Kibutu na alijiamini kuwa hata kama kanywa kiasi gani, lakini hawezi kusema kuwa jana alimtukana mtu kutokana na kuzidiwa na kilevi na kwamba hakuwa na kumbukumbu.
Hivyo, mshtuko alioupata hapa, aliamini kuwa haoti wala hajajichanganya. Hapana. Hii siyo sura ngerni. Ni yule Scolastica ambaye mara kadhaa alikuwa akimchukua kwa teksi pale Kinondoni Kwa Manyanya, kwenye kituo cha daladala na kumpeleka kwake, eneo la Biafra.
Kwa hili hakutaka kujidanganya. Ni mwenyewe. Swali likanjia, na yeye anamkumbuka? Hii inama yake ni ya kweli au anazuga? Huyu anazuga, alijisemea moyoni. Hata hivyo akaamua kuwa makini zaidi. Akamtupia salamu huku akimtazama kama asiyemtambua. Scolastica aliunyanyua uso na kumtazama. Macho yakakutana. Akaipokea salamu yake, kistaarabu bila ya mwonekano wowote wenye taswira ya chuki au dharau. Hata bia ya ofa ilipoletwa, Scolastica alikubali ifunguliwe na akainywa. Dakika kumi baadaye walikuwa mbali kimaongezi.
Alianza Kibutu, kwa kuwa alikwishaamua kumvalia njuga iwe, isiwe, akatema cheche. Akashusha risala ya kuomba radhi, Scolastica akimsikiliza kwa utulivu, mara chache akimtazama usoni na kuyarejesha macho kwenye simu yake.
Kilichomtia kiburi zaidi Kibutu ni milioni kadhaa zilizokuwa bado ndani ya begi lake ambalo hakuling’atua begani hata alipokuwa kaketi. Milioni moja aliyoitenga sasa ilikwishapungua na kubaki laki kadhaa. Hata hivyo aliamini kuwa kwa Scolastica atalainika tu, atake, asitake. Atamwomba radhi na atampa laki kadhaa za kumpoza. Atakataa? Hana ubavu huo!
Kiburi cha Kibutu kilikuwa katika ubora wake!
**ITAENDELEA***