Riwaya: Scolastica Temu

Riwaya: Scolastica Temu

SEHEMU YA 14

TULIPOKOMEA.....

Kilichomtia kiburi zaidi Kibutu ni milioni kadhaa zilizokuwa bado ndani ya begi lake ambalo hakuling’atua begani hata alipokuwa kaketi. Milioni moja aliyoitenga sasa ilikwishapungua na kubaki laki kadhaa. Hata hivyo aliamini kuwa kwa Scolastica atalainika tu, atake, asitake. Atamwomba radhi na atampa laki kadhaa za kumpoza. Atakataa? Hawezi!

Kiburi cha Kibutu kilikuwa katika ubora wake!

****ENDELEA****

“Nilishindwa kuvumilia, Scola,” alizungumza mwishoni mwa risala yake. “Ningefanya nini wakati nilikuwa nikikuhitaji sana na wewe ukawa unanipa majibu ya kuudhi? Lakini hayo tuyaache, Scola. Yamepita. Nakuomba sana radhi kwa yaliyotokea. Na siyo tu kwamba nakuomba unisamehe, bali pia nakuomba upokee kitu kidogo nilichonacho katika kuthibitisha kuwa ninakupenda na nilichokifanya nakijutia.”

Scolastica aliuinua uso na kumtazama kwa macho makali. Kisha akamuuliza, “Unataka kunipa nini?”

Tazama ya Scolastica haikuwa na amani hata chembe. Kibutu alilibaini hilo, lakini hakubabaika. Bado alikuwa na ule ujasiri uliosababishwa na milioni mbili zilizohifadhiwa ndani ya begi na laki saba na ushei zilizokuwa ndani ya mfuko mmoja wa suruali.

Alichoamini yeye ni kwamba, Scolastica ni mwanamke tu, ambaye huenda anaishi kwa kutegemea mshahara wa mwezi, huenda labda na vijisenti vya kuhongwa na hawara. Hakujua kuwa alikuwa akifanya kazi, na wala hakuwa na haja ya kujua, ila tu alijenga imani hiyo. Kwa jinsi akili yake ilivyomtuma, alihisi huenda Scolastica analipwa mshahara usiozidi shilingi lake nne au tano kwa mwezi.

Kama atakuwa analipwa kiasi hicho cha pesa, atakuwa na uwezo wa kukataa fidia ya laki kadhaa atakazokabidhiwa usiku huo? Uwezo huo hana, Kibutu aliendelea kuamini hivyo. Hivyo, akiwa hatishwi na swali pamoja na huu utazamaji wa Scolastica, alimjibu, “Nataka kukufidia kidogo.”

Scolastica aliendelea kumtazama kwa makini. Alipoyamisha macho ni pale tu alipoishika chupa ya bia na kunywa funda mbili kubwa za bia kisha akairejesha mezani. Akamrudia Kibutu.

“Sijakuelewa, ujue?”

Kibutu aliamua kukisogeza zaidi kiti chake kwa Scola. Wakawa jirani zaidi na huenda hakutaka wanachoongea kinaswe na yeyote asiyehusika. Akilini mwake aliamini kuwa shilingi laki tano zingetosha kumlainisha Scolastica. Laki tano za mkupuo kama fidia kwa tukio la zaidi ya mwezi mzima uliopita, tukio ambalo huenda hata halimtii uchungu tena mtendewa, si zitakuwa kama pesa za bure?

Akiendelea kujiamini kwa kiasi kikubwa, akasema, “Nimeona nikufidie kwa kiasi kidogo cha pesa.”

“Fidia?” Scolastica aliendelea kumkazia macho.

“No,” Kibutu alijisahihisha. “Tuseme ni kama pole tu. Ni kiasi kidogo tu Scola. Haiwezi kuwa fidia, lakini naomba tu uipokee.”

Hii harufu kali ya jasho kutoka kwa Kibutu ilikuwa ni kero ambayo Scolastica alilazimika kuivumilia. Alijua hii ni kero ya muda, itapita tu. Kimoyomoyo akawa akicheka, pia akilia.
Kumbukumbu sahihi ya ile siku isiyosahaulika kule Komakoma, ilimjia na kumfanya awakumbuke wale wenzake Kibutu, ambao mmojawao alimtamkia maneno ya dharau na kumlazimisha aondoke huku pia akiwa ameshinikizwa azivunjevunje laini za simu yake!

Sasa aliamua kumsikiliza na kwenda naye sambamba huyu Kibutu, auone mwisho wa kilichomleta hapa mezani. “Hiyo pole yako ni kiasi gani?”

Kibutu aliingiza mkono mfukoni na kuchomoa bunda zito la noti. Akatenga mafungu saba ya shilingi laki moja, moja. Akamkabidhi Scolastica shilingi laki tano kwa namna ambayo hakutaka macho yasiyohusika yashuhudie. Laki mbili akazirejesha mfukoni. Kisha kwa sauti ya chini, yenye kijimkwaruzo kilekile cha kilevi, akanong’ona, “Ni laki tano.”

Ulikuwa ni mnong’ono ulioyafikia masikio ya Scolastica kwa usahihi. Akawaza, azichukue au aziache? Papohapo akajiambia kuwa utakuwa ni ujinga kuziacha laki tano za bure. Akilini mwake, alipata picha kuwa Kibutu anajiona kampa pesa nyingi sana za kuweza kumfanya ababaike na kumsujudia.

*****

NUSU saa baadaye, walikuwa kama wapenzi wa muda mrefu. Laki tano zilizokuwa ndani ya mkoba wa Scolastica zilimwongezea hasira na kujiamini zaidi. Oda ya nyamachoma ikatolewa. Vinywaji vikaendelea kutua mezani.

Scolastica hakujali pale Kibutu alipodiriki kumpapasa paja. Ya nini kujali ilhali alikuwa hapo kwa malengo maalum? Hakujali kupapaswa, alichojali ni kutouruhusu ulevi kichwani mwake na kujali muda.

Kwa upande wa Kibutu, akilini mwake aliamini kwa kuwa tayari laki tano zilishaingia kibindoni mwa Scolastica, basi hakuna litakaloshindikana. Fedha ni uchawi wa kipekee, aliwaza. Hatoki mtu hapa mpaka kieleweke, alijiapiza.

Wakati akijiapiza hivyo, hakujua mwenzake alikuwa akiwaza nini. Akiwa ni mwanamke aliyejiamini kwa kiwango cha juu, Scolastica akitumia akili za darasani, akachanganya na za kuzaliwa, alikuwa mtulivu na makini katika kufuatilia kila kilichofanya na kusema na Kibutu.

Pamoja na hoja hii na ile kuzungumzwa, hata hivyo Scolastica hakuwa mbumbumbu, alijua Kibutu anakoelekea, hivyo hakushangaa alipomsikia akipendekeza kuhusu kuwa wote usiku huo hadi kunakucha.

Lilikuwa ni pendekezo lililokaribia kumchekesha Scolastica, kicheko cha wazi, lakini hakuwa, mjinga kiasi hicho. Aliendelea kucheka na kulia kimoyomoyo. Kwa kufuata zile ambazo zilishachukuliwa kama kanuni, Scolastica alipingana na pendekezo hilo. Mwananke hapaswi kukubali papohapo atongozwapo na mwanaume, vinginevyo ataonekana ni malaya.

Scolastica naye aliifuata imani au kanuni hiyo, lsakini Kibutu hakukubali; alisimama kidete. Mwanaume akabembeleza na kubembeleza, kiwangocha pombe aliyokunywa kikizidi kumwongezea morali ya kutaka kile alichokikusudia. Hatimaye, akiataka kuhakiiiksha hakosi anachokitaka, akaitupa laki moja mapajani kwa Scolastica.

Scolastica akamtazama Kibutu kwa huruma, hiyo lakini nayo ikiingia mkobani. Siachi kitu, alijisemea moyoni. Dakika chache baadaye mzizi wa fitina ukakatwa. Scolastica akatoa tamko. Kibutu akakaribia kuwehuka kwa furaha!

Wakati Kibutu akifurahia kupewa kibali kwa burudani ya usiku huo, Scolastica alikuwa akilichekea moyoni pato lake.
Laki sita kiimchezomchezo tu!

Saa nne kasoro dakika chache, Kibutu alipendekeza waondoke. Kwa jumla hakuwa na shida tena ya kuwa ndani ya hiyo baa. Alikunywa bia na pombe kali za kutosha, alichohitaji sasa ni kupata burudani na mrembo Scolastica.

Alishajiwekea utaratibu wa kutokwenda baa na teksi yake usiku. Alihofia kuzidiwa na kilevi na kushindwa kuendesha kwa ufanisi. Hivyo, hata alipokuwa hapo Mood Bar siku hiyo, alikuwa amekwishaegesha gari sehemu fulani anakolipia egesho. Alipotupa macho kule kaunta akawaona wale vijana bado wapo. Akamwita mhudumu mmoja na kumtaka akamwitie mmoja wa vijana wale.

Dakika mbili, tatu baadaye kijana mmoja alikuwa mbele yake.
“Hamidu, niko na shem wako,” alimwambia kimadaraka. “Please, kanitafutie usafiri hapo nje. Siyo bodaboda au bajaji. Tafuta teksi, tena ya maana siyo lingalangala linaloweza kufia njiani.”

Kijana yule alipoondoka, Scolastica aligugumia bia yake na kuirejesha chupa chini. Kisha akamwambia Kibutu, “Kama tunaondoka kwa nini tusichukue na bia mbilmbili za kumalizia huko kwako?”

Kibutu hakupinga, hakuwa mtu wa kupinga pendekezo lolote la Scolastica, ilimradi kishamkubalia kuumaliza usiku wakiwa pamoja! Nani kama yeye? Kwa nini asiione siku hiyo kuwa ni ya kipekee?

Wakati wakiifuata teksi nje, mfuko wenye bia nne, mbili za Scolastica na mbili za Kibutu ulikuwa umeshikwa na mkono wa kulia wa Scolastica.

Safari ya Komakoma!

***ITAENDELEA KWA HISANI YA Madame S ***
 
SEHEMU YA 15


TULIPOKOMEA.....

Kibutu hakupinga, hakuwa mtu wa kupinga pendekezo lolote la Scolastica, ilimradi kishamkubalia kuumaliza usiku wakiwa pamoja! Nani kama yeye? Kwa nini asiione siku hiyo kuwa ni ya kipekee?
Wakati wakiifuata teksi nje, mfuko wenye bia nne, mbili za Scolastica na mbili za Kibutu ulikuwa umeshikwa na mkono wa kulia wa Scolastica.
Safari ya Komakoma!

****ENDELEA*****

YALIKUWA ni mazingira yaleyale ambayo Scolastica hakuweza kuyasahau. Ilikuwa ni nyumba ileile ambayo haikupotea katika kumbukumbu zake. Ndiyo, ni hapahapa ambako kiasi cha mwezi mzima na zaidi kidogo, aliletwa kimsobemsobe na kutendwa kile ambacho nacho kamwe hawezi kukisahau.

Wakati teksi ilipoegeshwa kando ya nyumba hii, Kibutu alimwambia Scolastica, “Baby, tumefika.”

Eneo hilo lilikuwa kimya na huenda ni kwa kuwa tayari ilishatimu saa nne na dakika zake. Scolastica alikuwa makini. Akaiangalia nyumba iliyokuwa kulia mwa hii waliyoteremkia. Akaitazama na ya kushoto. Kote kulikuwa tulivu, taswira iliyoonesha kuwa huenda wakazi wake wameshalala au hawapo. Pikipiki mbili zikiwa na abiria wawili, wawili waliopakiwa kimishkaki, zlimpa picha kuwa suala la kupata usafiri hapo siyo tatizo atakapohitaji kuondoka.

Suala ni kwamba, ataondoka usiku huohuo au kesho asubuhi? Haikumwingia akilini kuwa aumalize usiku akiwa ndani ya nyumba hiyo anayoingia kwa mara ya pili, baada ya ile siku yenye adha isiyosahaulika. Hakuwa tayari kufanya hivyo, lakini hata hivyo, pia hakuwa na uhakika wa usalama wake. Je, wale watu ambao walishirikia na huyu Kibutu siku ile, wanaishi humohumo ndani au wana makazi yao kwingine?

\Ndani kulikuwa giza, ikionesha pia kama nyumba za jirani, huenda hamna mtu au kama kuna mtu au watu basi wameshalala.

Wakati Kibutu akishughulika kumlipa dereva, Scolastica hakutaka dereva huyo amwone kwa usahihi. Kwa jumla hakutaka macho ya mtu yeyote asiyehusika kwa muda huo, amwone kwa zaidi ya sekunde mbili. Huu ulikuwa ni muda muhimu sana kwake, muda aliouhitaji, labda zaidi ya vipindi vilivyopita kwa siku hiyo.

Hivyo, alipoteremka tu alikwenda kuegemea boneti la gari kwa nyuma na kubaki akiangaza macho walikotoka. Kibutu na dereva walipomalizana, kisha gari likaondoka, papohapo Scolastica alimvaa Kibutu. “Sikia Kibutu. Sitaki matangazo. Kama humo ndani kwako mko wengi na wenzio ni watu wa macho juu, juu, siingii. Hapo utanisamehe.”

Walikuwa kwenye kiambaza kilichozingirwa na kijigiza. Isingekuwa rahisi kwa yeyote kuweza kuwatambua kuwa huyu ni nani na huyu ni nani.

“Hapa hakuna matangazo, baby,” Kibutu alisema kwa sauti yake ileile ya kilevi, huku akimkumbatia Scolastica na kumpapasa makalio.

“Kweli?” Scolastica alimuuliza, huku naye sasa akimpapasa kidevu huku mkono mwingine ukimpapasa tumboni na kushuka chini zaidi, ambako ulifanya kile kilichosababisha Kibutu atoe mguno hafifu.

“Sikudanganyi, baby,” Kibutu aliipata sauti yake kwa tabu.

“Unaishi na nani?”

“Niko alone, nakuapia! Yaani mimi kama mimi, niko peke yangu. Ila kuna wapangaji wengine watatu ambao ni kama hawapo. Mmoja ni msela tu, dogo wa mishentauni. Huyo ana wiki hayupo, wakati mwingine anakaa kwa ndugu zake huko Mwananyamala Kwa Mama Zakaria. Mwingine ni baamedi; rudi yake ni kati ya saa saba au nane, na huenda pia akarudi asubuhi. Na kuna mdada mmoja, mlokole, nasikiaga eti aliachika kwa mumewe nd’o akaja kupanga hapa; akaokoka na kuokoka daaaadek! Eti sasa anasali huko kwenye makanisa ya kilokole….”

Scolastica alichoshwa na mwendelezo wa ‘mashairi’ hayo. Alifurahishwa na hicho alichohitaji kukijua. Kwamba Kibutu yuko peke yake kwa muda huo. Papohapo akamkata kauli: “Ok, twende basi. Sitaki mashilawadu wanikute hapa. Hujui mi’ ni mchumba wa mtu?”

Kibutu aliingiza mkono mfukoni na kujipapasa kwa muda kisha akatoa rundo la funguo. Akaupachika ufunguo mmoja kwenye kitasa na kuufungua mlango. Varadna kubwa iliwalaki baada ya Kibutu kupapasa ukuta na kuwasha taa. Haraka Scolastica akaingia na kuangaza macho kwa makini, wakati Kibutu akifungua tena mlango kwa funguo.

Kisha mwenyeji akatangulia, mgeni akamfiuata. Ni mlango wa mwisho, kulia ndiko kulikokuwa na chumba cha Kibutu. Akaufungua mlango huo na kuwasha taa. Sasa wote walikuwa ndani ya chumba cha Kibutu, na Scolastica aliendelea kumshukuru Mungu kwa kutoonwa au kuonana na mtu yeyote humo ndani.

Ilikuwa ni nyumba ya kawaida, kama zilivyo nyumba nyingi za uswahilini. Ilimpa picha Scolastica kuwa hakukuwa na chumba ambacho kilikuwa na huduma za bafu na choo ndani. Kwa vyovyote, huduma hizo zilipatikana eneo la uwani, ambako aliuona mlango wa kutokea ukiwa jirani na chumba hiki cha Kibutu.

Sasa Scolastica aliyahamishia macho ndani ya chumba hiki. Akakiangalia kitanda kipana kilichokuwa shaghalabaghala, kitanda ambacho kiasi cha mwezi mmoja uliopita, kilikuwa shahidi wa lile tukio lisilosahaulika. Kama ilivyokuwa siku ile, usiku huu pia kitanda hiki hakikuwa katika mvuto wowote.

Akaiangalia shuka ya rangi ya kijivu, iliyokuwa haijatandikwa, ikiwa pembezoni mwa kitanda hicho. Usela! Aliwaza. Taswira iliyojidhihirisha ni kwamba, siku hiyo, kama siyo siku zote, Kibutu alipokurupuka kitandani hakuwa na muda wa kukitazama mara ya pili, zaidi, huenda alitwaa mswaki na kwenda kusafisha meno, akaoga, akavaa kisha huyooo, kwenye mihangaiko yake.

Hata hivyo, kutokuwa safi kwa chumba hicho halikuwa suala ambalo mwanamke huyo aliona kuwa linamhusu hata chembe. Alichofanya ni kujitupa sofani na kuendelea kuukumbatia huu mkoba wake. Ule mfuko wenye chupa za bia aliuweka sakafuni kwa kuwa hakupaona pengine pa kuuweka. Hakukuwa na stuli wala meza. Hakushangaa, alijua kuwa kina ‘chapombe’ wengi wanaishi maisha ya aina hiyo. Mtu anaweza kuhonga pesa mpaka milioni ilhali anaishi kwenye chumba kisichokuwa na hadhi.

Akabaki akimtazama Kibutu ambaye sasa alionekana kuwa huru zaidi. Ndiyo, Kibutu alijiona yu huru kupindukia. Sasa akalivua shati na kulirusha kwenye begi kubwa lililokuwa kando ya kitanda. Kisha akaivua suruali na kubaki na boksa pekee. Akaja kuketi sofani kando ya Scolastica.

“Baby….baby Scola ujue kuwa nakupenda sana,” sauti yake isiyotofautiana na mkoromo wa jibwa linalokaribia kukata roho ilimfikia Scolastica katika namna iliyozidi kumtia faraja na matumaini zaidi.

“Hata mimi nakupenda, Kibu,” likamtoka Scolastica huku kajilaza kifuani pake na kuvumilia harufu kali ya mchanganyiko wa jasho na pombe.

“Asante mtoto mzuri,” Kibutu alibwabwaja na kuyatupia macho kwenye ule mfuko wa chupa za bia. Kisha: “Kwa hiyo inakuwaje, tumalizie kwanza bia zetu au?”

“Hapo umesema la maana sana, mpenzi.”

“Us’konde.” Tayari Kibutu alishanyanyuka na kuelekea dirishani. Akafunua pazia na kuchukua kifaa cha kufungulia chupa, kisha akarejea sofani.

Hakukaa, aliinama na kufungua chupa, ile kisha akakirudisha kifaa kile alikokitoa. Aliporejea sofani, alifikia kuitwaa chupa na kupiga funda moja la kinywaji kabla hajairejesha chini.

Scolastica alikuwa mbali kiidogo kimawazo. Wala hakuharakisha kunywa bia yake. Alimtazama Kibutu na kumwambia, “Lakini baby, nadhani ungejimwagia kwanza maji nd’o ukaja tufaidi awamu hii ya mwisho. Unajua wewe ulikuwa kwenye mihangaiko yako ya maisha. Mimi nilipokuja pale baa nd’o kwanza nilikuwa nimetoka home. Niko fresh kabisa yaaan. Kaoge upone, utajisika fresh sana, ujue.”

Pamoja na kiwango cha pombe kukitawala kichwa cha Kibutu, hata hivyo hakuwa mwehu. Haya maneno ya Scolastica yalikuwa na maana kubwa na akaamini kuwa akilifanyia kazi pendekezo lake, atajisikia vizuri zaidi na ataweza kuwajibika ipasavyo pale kitanda kitakapowalaki.

“Point!” alibwata huku akinyanyuka. Akaufuata mlango na kuufungua. Lakini kabla hajatoka, akamgeukia Scolastica na kumwambia, “Ten minutes, baby.”

Akatoka akimwacha Scolastica akichekea moyoni kwa kuona sasa Mswahili anaihama lugha yake. Pombe hizi! alijisemea kimoyomoyo.

Lakini mara akazinduka. Hakutaka kuwa mpumbavu. Alipaswa kupajua huko Kibutu anakokwenda kuoga. Huu haukuwa muda wa kumwamini yeyote. Haraka akajitoa sofani na kuufungua mlango. Akamkuta Kibutu ndiyo kwanza amefungua mlango wa uani, akiwa na ndoo tupu mkononi akienda nje.

Muda mfupi baadaye kwa kutumia upenyo mdogo wa mlango huo wa uani, akamshuhudia akichota maji bombani. Kisha kwa kutumia upenyo huo mdogo wa uwazi mlangoni, alimshuhudia akipanda ngazi kadhaa kabla hajafika juu, katika choo ambacho huenda pia kilitumika kama bafu. Choo cha uswahilini.

Scolastica alirudi ndani haraka ambako sasa alichukua chupa yake ya bia na kunywa funda mbili kubwa kisha akaiweka chini. Akaufungua mkoba wake na kutoa kijibahasha kilichohifadhi tembe tatu za Olanzapin. Akatwaa tembe moja na kuiweka kwenye kifuniko cha moja ya bia zilizofunguliwa. Kisha akapekua tena ndani ya mkoba wake na kufanikiwa kupata sarafu ya shilingi mia moja. Akaitwaa. Akaanza kuisaga ile tembe kwa uangalifu huku akisikilizia huko nje kama Kibutu anarejea.

Ndani ya dakika moja alikuwa amekwishaisaga tembe hiyo na unga wake kisha akaumimina kwa uangalifu ndani ya chupa ya bia ya Kibutu. Akashusha pumzi ndefu na kukisukumia kifuniko kile uvunguni mwa kitanda. Akavisugua vidole kwa nguvu kwenye sofa lile akihofia, asije akawa amebaki na chembechembe za unga wa tembe ile!



***ITAENDELEA***
 
SEHEMU YA 16


TULIPOKOMEA....

Ndani ya dakika moja alikuwa amekwishaisaga tembe hiyo na unga wake kisha akaumimina kwa uangalifu ndani ya chupa ya bia ya Kibutu. Akashusha pumzi ndefu na kukisukumia kifuniko kile uvunguni mwa kitanda. Akavisugua vidole kwa nguvu kwenye sofa lile akihofia, asije akawa amebaki na chembechembe za unga wa tembe ile!

****ENDELEA****

KUDHAMIRIA kutekeleza azma ni jambo moja. Kufanikiwa kutekeleza azma hiyo ni jambo lingine. Katika dhamira ya utekelezaji wa tendo la ngono, umakini, utulivu kisaikolojia sanjari na pumzi ya kutosha, ni vigezo ambavyo huweza kumfanya mwanamume yeyote ailinde heshima yake mbele ya mwanamke.

Wakati Kibutu alipokuwa akinyanyua kopo la mwisho maji na kujimwagia mwilini, tayari alikwishajihisi yuko tofauti na wakati alipokuwa amekuja hapo nyumbani. Ule utawala mkubwa wa pombe kichwani, japo haukumalizika, lakini kwa kiasi kikubwa alijiona ana nafuu. Alijisikia mwepesi kiasi.

Laki sita zilizokuwa katika himaya ya Scolastica, sasa mwanamume hakutaka ziende bure. Alipaswa kuzilipia bila ya kujua. Hivyo, kwa usiku huo, ndani ya chumba chake, katika kitanda kilekile, Kibutu alitaka afanye kila kitu!

Kila kitu!

Alipokwishaiweka ndoo kando ya mlango ule wa uani, akafunga mlango vizuri kwa komeo, kisha akaelekea chumbani kwa maringo, aliliwazia jukumu lililo mbele yake.

Alimkuta Scolastica akiwa ametulia sofani huku akiperuzi mitandao kwenye simu. Kibutu alifunga mlango kwa funguo kisha akajitupa sofani, kando ya Scolastica huku akiachia tabasamu kubwa. “Sasa niko fresh kama ulivyonishauri…"

Hakumalizia kuzungumza, mara simu yake ikaita. Ilikuwa ndani ya mmoja wa mifuko ya suruali yake aliyokuwa akaitupia kwenye begi kando ya kitanda. Akashtuka na kuinyanyuka haraka. Akaifuata na kuitoa. Akabonyeza sehemu fulani na kutegea sikioni. Akaaanza kwa sauti ya majidai, “Vipi, Kisengo, mbona leo ulipotea jumla?”

Scolastica alishtuka kulisikia jina hilo. Alikumbuka siku ile alipotekwa, zaidi ya kulijua jina la Kibutu, pia aliwasikia wenzie wakizungumza na kuitana majina hasa wakati wamemaliza kutimiza dhamira zao. Walipomshinikiza kuzivunja laini za simu yake, walikuwa wakizungumza kwa kutajana majina. Ambacho hakuwa na hakika kwa usiku huu ni kuweza kuzikumbuka zile sura na kuzitofautisha kwa majina.

Ni kwamba, kama watu wale wangetokea hapo kwa pamoja, angewakumbuka vizuri, lakini asingeweza kusema kuwa huyu ni Kisengo na huyu ni Machemba. Majina alikuwa nayo kichwani na sura zilikuwa kichwani, kazi ilikuwa ni kuoanisha majina na watu.

Zilimchukua dakika kama mbili Kibutu akiongea kwenye simu hiyo. Hatimaye kwa sauti ileile ya maringo, akasikika akisema, “Aisee, niko na shemeji yako, tutaongea kesho. Muhimu we ni kujali muda tu. Na kama hupajui hapo Maseru, we fika tu hapo Mkwajuni jirani na kituo cha mabasi ya mwendokasi. Ukiuliza yeyote pale atakuonyesha. Kuanzia saa kumi huwa kunachangamka. Utasikia makelele ya muziki na wakati mwingine pia kelele za runinga kama kuna mechi zinaonyeshwa….”

Alipokata simu, alisonya na kuamua kuizima kabisa. Kisha akamgeukia Scolastica. “Watu wengine wasumbufu,” alisema huku akijitupa tena sofani. “Niko zangu na mtoto mzuri, halafu mtu anaanza kupigapiga simu, eti hapajui hapo tulipokubaliana kukutana.”

“Si ni msh’kaji wako?”

“Ni kweli. Lakini si angepiga asubuhi! Usiku wote huu kwani nd’o tunataka kukutana hapo baa?”

Scolastica alitwaa chupa yake na kuipeleka mdomoni. Akanywa funda moja na kuirejesha chini. Akili yake ilikuwa kwa Kibutu, amshuhudie akishusha funda la kinywaji chake.

Naam, Kibutu naye akaitwaa chupa yak e na kunywa funda zito, akatulia kidogo na kunywa funda lingine. Alionesha kuwa hahitaji kuendelea kunywa zaidi, bali kustarehe na mrembo aliye kando yake. Funda la tatu liliposhuka kooni, akaitua chupa chini. Sasa akamgeukia Scolastica. Akamtazama kwa macho yaliyoanza kurembukia kwa kasi.

“Baby…baby…” yalimtoka maneno hayo kwa sauti dhaifu huku akimwegemea Scola stica. “Baby….tuachane na bia….tukalale kwa….kwanzaaaa….”

Ulimi ulianza kuwa mzito kutamka, macho yakazidi kuwa mazito kuona. Miguu ilikosa nguvu ya kuubeba mwili, lakini alipoilazimisha kuwa mhimili, ikamtii kwa sekunde ya kwanza, sekunde ya pili ikaghairi; akaenda mzima mbele na kuanguka kifudifudi kama gunia. Akajitahidi kugeuka na kutaka kutamka maneno. Mdomo ukawa ukifunguka kwa taabu na kutamka maneno ambayo Scolastica hakuyasikia.

Ndiyo, maneno aliyoyatamka, hayakuyafikia masikio ya Scolastica na kwa jumla Scolastica hakuhitaji kuyasikia wala kuyaelewa. Katika kuiweka ratiba yake kwa kwenda na muda, aliufungua mkoba wake na kutoa kitambaa kizito ambacho alijifunga madhubuti eneo zima la puani na mdomoni. Kisha, alimtazama tena Kibutu na kumwona akiwa ametopea usingizini, akivuta na kuzishusha pumzi kwa nguvu.

Hakuwa na wasiwasi kwa kuwa alishayatambua mazingira ya nyumba hiyo. Aliiangalia saa na kukuta ni saa tano na dakika ishirini. Akaingiza mkono ndani ya mkoba na kuitoa chupa ndogo ya PAK. Akaifungua na kumsogelea KIbutu taratibu. Akamwinamia na kuigusisha kwenye tundu moja la pua. Kibutu alipovuta pumzi kwa nguvu mara mbili, Scolastica aliitoa chupa hiyo na kuifunga kama mwanzo, kwa umakini vilevile.

Ilitosha.

Dakika iliyofuata, alikuwa amekwishajiweka sawa, mkoba begani. Akajiandaa kutoka, lakini akasita. Aliikumbuka simu ya Kibutu. Akaifuata sofani na kuitwaa. Aliamini kuwa itakuwa msaada mwingine muhimu kwake. Akaipachika mkobani kisha akaufungua mlango. Akatoka baada ya kufunga kwa funguo na kuondoka nazo.

Kwa mbali alihisi kiroho kikimdunda. Wasiwasi ulikuwa ukimwingia kila alipokumbuka jinsi alivyotekeleza moja ya ratiba zake. Alipita koridoni hapo taratibu hadi akaufikia mlango wa mbele. Akaziangalia tena funguo hizi nane ambazo aliziona wakati Kibutu akizichambua na kuutumia mmoja kufungulia mlango huo.

Huku kwa mbali akihisi vidole vikimtetemeka, akaanza kujaribu kufungua bila ya kujua ufunguo halisi ni upi.

Ufunguo wa kwanza, ukagoma.

Wa pili, ukamkatalia.

Wa tatu, ukamringia.

Wa nne, ukamtii.

Taratibu, akakishika kitasa na kukizungusha. Bado alihisi woga. Nyumba nzima ilikuwa kimya na taa ya hapo varandani ilitoa nuru kali. Hakuipenda hali hiyo. Akaifuata swichi na kuizima. Hakuyajua mazingira yatakayomlaki huko nje. Kuna yeyote atakayemwona wakati akitoka? Je, atakutana na mmoja wa wakazi wengine wa hapo akiwa ndiyo amerejea?

Aliomba Mungu yote hayo yasitokee. Huku bado akivuta pumzi kwa wasiwasi, akakizungusha tena kitasa, taratibu na kuufungua mlango, taratibu vilevile.

*****ITAENDELEA KESHO****

***
 
SEHEMU YA 17


TULIPOKOMEA....


Taratibu, akakishika kitasa na kukizungusha. Bado alihisi woga. Nyumba nzima ilikuwa kimya na taa ya hapo varandani ilitoa nuru kali. Hakuipenda hali hiyo. Akaifuata swichi na kuizima. Hakuyajua mazingira yatakayomlaki huko nje. Kuna yeyote atakayemwona wakati akitoka? Je, atakutana na mmoja wa wakazi wengine wa hapo akiwa ndiyo amerejea?
Aliomba Mungu yote hayo yasitokee. Huku bado akivuta pumzi kwa wasiwasi, akakizungusha tena kitasa, taratibu na kuufungua mlango, taratibu vilevile.

***ENDELEA***


NJE kulikuwa vilevile, ksaama wakati walipoingia. Utulivu mkubwa. Wakati akiurudisha mlango, pikipiki moja ikapita. Alitaka kuisimamisha lakini akasita. Hakutaka kuchukua usafiri wowote akitokea hapo. Akaufunga mlango ule kwa funguo kisha akaondoka taratibu.

Sasa kumbukumbu ya siku ile, alipooneshwa njia ya kupita ikamjia. Akaifuata njia hiyo, akijua fika kuwa atakwenda kutokea kituo cha daladala cha Komakoma. Lakini siku hii hakutaka kutembea mpaka huko kituoni. Alipokwishajiona kuwa yuko mbali na ile nyumba alimokuwa, akawa akitegea pikipiki yoyote itakayokuja aipungie mkono. Mara akaiona moja ikimjia kwa mbele. Alipoifanyia ishara, dereva akakanyaga breki.
“Mkwajuni,” alimwambia wakati akipanda.

Pikipiki ikaondoka. Sasa kwa kiasi fulani alijiona yu salama. Ule wasiwasi uliokuwa umemwingia wakati akiondoka ndani ya ile nyumba, sasa ulimtoka. Walipofika Mkwajuni, Scolastica aliteremka na kuifuata Barabara ya Katumba. Hakufika mbali, alikata kushoto na kuifuata barabara finyu akiwa hana sababu yoyote wala hakuwa anakwenda popote. Ilikuwa ni katika kuhakikisha tu yule dereva asijue kwa hakika anakoelekea.

Alijua kama kutafanyika uchunguzi na ikabainika kuwa dereva fulani alimbeba mwanamke mwenye mwonekano fulani, basi huenda dereva huyo akahusika kwenye mahojiano. Na hapo ndipo atakaposema kuwa abiria wake alimpeleka wapi.
Hapo inaweza kuwa ni bahati mbaya kwake kwani, kwa jinsi alivyojua askari wa upelelezi wanavyofanya uchunguzi wao kwa umakini, kama wakiamua kulivalia njuga tukio fulani, wanaweza kuja kumdaka kwa urahisi sana. Ni hisia hizo zilizomfanya badala ya kwenda Biafra moja kwa moja, aje kwanza huku Mkwajuni na kumpoteza boya yule bodaboda.
Alitembea taratibu na kuingia ndani ya Baa ya Maseru kwa kupitia mlango wa uchochoroni, akakatisha humo ndani na kuja tena kutokea barabara kubwa. Kule juu akazikuta pikipiki nyingine zikiwa zimeegeshwa Akapanda moja na kumwamuriu dereva ampeleke Pazi Social Club. Dakika chache baadaye alikuwa anateremka nje ya baa hiyo, eneo la Biafra.

Aliingia ndani na kuzungukia upande wa pili, akatoka na kuendelea na safari yake. Sasa hakuchukua usafiri wowote. Taratibu tu, kama mtu aliyetoka matembezi ya kawaida hapo jirani, alitembea na kuukuta Mtaa wa Kairuki mbele kidogo, ambao aliufuata hadi akafika kwake. Baada ya kuoga, hakutaka kufanya chochote kingine. Alikuwa akiwaza ni taswira gani itakayojitokeza baadaye huko Komakoma pale itakapobainika kuwa maiti ya Kibutu imeanza kuoza. Na alipanga asubuhi ya siku inayofuata, ndipo aanze ‘kucheza’ na hii simu aliyoichukua huko Komakoma.

Usingizi uliochangiwa na pombe na uchovu wa mihangaiko ya siku hiyo, ulimchukua akiwa hapohapo sofani, nusu kaka, nusu kalala.
*****
KUTIMIZA miadi kwa wakati, ni jambo ambalo Kisengo alilizingatia sana. Mara kwa mara alikuwa akikorofishana na baadhi ya watu katika mipango yao, kwa kutotimiza miadi kwa wakati. Usiku wa jana alikubaliana na Kibutu kuwa wakutane eneo la Mkwajuni saa kumi na mbili jioni kwa ajili ya kuzungumzia mpango fulani.
Saa kumi na moja jioni, alikuwa akitoka nyumbani kwake, Magomeni Mikumi akitembea taratibu akiamini kuwa hajachelewa katika miadi hiyo. Akapanda daladala lililomfikisha kituo cha Mkwajuni baada ya dakika chache.
Alipoteremka, alimfuata kijana mmoja aliyeonekana alikuwa akivizia kupata tenda ya kubeba mizigo. Akamuulizia ilipo Baa ya Maseru.

“Ile pale, mjomba,” kijana huyo alimwonesha kwa kidole upande wa pili wa barabara. Kisengo akavuta hatua na kuifikia baa hiyo baada ya muda mfupi. Ni kweli kulikuwa kumeshaanza kuchangamka. Eneo moja kulikuwa na kundi la watu waliojikusanya vitini wakiangalia mecho fulani ya soka na eneo lililobaki kukiwa na wateja wa vinywaji vya aina mbalimbali.

Akachagua meza iliyokuwa na wahudumu wawili wa kike. Akavuta kiti na kuketi.
“Karibu kaka,” mhudumu mmoj alimwambia huku akiwa amesimama.
Kisengo aliangalia saa kukuta ndiyo kwanza imefika kumi na moja kasorobo. Akaagiza bia. Akiwa naye ni mgonjwa kwa wanawake, mmoja wahaudumu hawa, hasa yule aliyebaki alimvutia na akaanza maongezi naye japo ya kawaida, lakini akidhamiria mwisho wa maongezi yake na Kibutu, lazima aondoke naye.

Maongezi kati yao yalishamiri japo mara kawa mara pia mhudumu huyo alikuwa akilazimika kwenda kuhudumia wateja wengine. Ni muunganiko wao huu wa vipindi vifupivifupi ndio ulimfanya hata Kisengo akasahau kuwa alikuwa na miadi na Kibutu. Kutahamaki, saa kumi na mbili kasoro dakika tano, bia tatu zikiwa zimekwishapenya tumboni!
Alishtuka hivyo wakati alipokuwa amebaki peke yake na hivyo kuamua kuangalia tena saa. Akasonya huku akimlaumu Kibutu kimoyomoyo. Akakumbuka kuwa ni yeye aliyemsisitizia kujali muda. Sasa mbona hadi hii saa kumi na mbili hajatokea?

Akaamua kumpigia. Hata hivyo mara mbili mfululizo alizopiga akaambulia kuwa namba haipatikani eti ajaribu baadaye. Akamtumia ujumbe wa maandishi. Nao ukaonekana unaelea tu, haujaingia.
“Atakapojisikia atanipigia,” alinong’ona kwa hasira.
Saa nne usiku ilimkuta hapohapo Maseru Bar, na zaidi ya mara nne alizompigia tena Kibutu bado hakuambulia kitu. Ndipo alipoamua kumtumia ujumbe: ‘umenikalisha hapa na kunifanya nipate hasara kwa kunywa bia. Utairejesha gharama niliyotumia.

Sasa kesho nitakuja saa kumi na mbili, kama hutaweza tena kuja, basi dili life.
Alijua kuwa atakapoiwasha simu atausoma ujumbe huo.

***ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom