Riwaya: Saa za Giza Totoro

Riwaya: Saa za Giza Totoro

Vipi kwa sisi tusio mabaharia tunaofuatilia hii stori pia twaweza kuchangia hiyo 500 ya vocha tumalizane na stori yetu? 😅
 
SEHEMU YA 27



ILIPOISHIA:
Kweli ilionesha alikuwa na upweke wa hali ya juu ndani ya moyo wake, kwani alinipokea kwa bashasha za hali ya juu, nikaanza kufumua mashuti ya nguvu na kusababisha awe analalama kama mtu anayeonewa lakini wakati huohuo akinihimiza kuongeza kasi ya mchezo.
SASA ENDELEA...
Basi tulikukuruka pale kisawasawa, japokuwa nilikuwa mgeni katika dimba hilo la kikubwa, mazoezi makali ya viungo niliyokuwa nafanya, ukichanganya na zile bia nilizokunywa, kiwango changu kilikuwa kikubwa kwelikweli mpaka Kezia mwenyewe akasalimu amri.
Ngwe ya kwanza ilipoisha, kila mmoja alikuwa hoi, Kezia akageukia upande wa pili akiwa hajiwezi kwa uchovu, na mimi nikageukia upande wa pili.
“Samahani kama uliona nimekudharau muda ule wakati mnafika, kweli wewe ni kidume cha shoka,” alisema Kezia kichovu huku akinigeukia na kunibusu, nikaachia tabasamu pana na kumbusu kwenye paji lake la uso.
“Nataka uwe mume wangu, kuanzia leo utakuwa mume wangu, sawa? Ukizingua nakutwanga risasi,” alisema kimasihara, tukacheka na kukumbatiana.
“Ahsante sana Snox, nakupenda mwenzio,” aliniambia kwa sauti ya kunong’ona. Sikumjibu kitu zaidi ya kuguna tu kwa sababu kiukweli sikuwa najua kama nampenda au la, kimsingi nilichukulia uhusiano wetu kama mapenzi ya kawaida tu.
Basi michezo ya hapa na pale iliendelea, Kezia akionesha kuchanganyikiwa kabisa na mimi, wakati tukijiandaa kwa ngwe ya pili, mlango wangu uligongwa kwa nguvu. Yaani huyo aliyegonga ungeweza kudhani tuna ugomvi naye kwa sababu akigonga kwa nguvu na kuutingisha mlango kwa nguvu.
Tukakurupuka pale kitandani na Kezia akaokota gauni lake na kukimbilia maliwatoni. Nikaenda kufungua.
“Hujasikia kengele?” mwanaume mwenye mwili mkubwa, aliyekuwa amevaa koti refu, alisema kibabe huku mkononi akiwa ameshika ile mikanda inayovaliwa na wanajeshi viunoni. Nikawa najiumauma kwa sababu ni kweli nilisikia kengele ikigongwa mara moja tu lakini hata sikuwa najua maana yake ni nini.
“Wewe ni mgeni?”
“Ndiyo!”
“Bahati yako, vaa nguo zako haraka elekea Goligotha,” alisema kibabe kisha akatazama saa yake huku akitingishatingisha ule mkanda wake.
“Nakupa dakika mbili uwe umeshafika.”
“Goligotha ndiyo wapi?”
“Mwenyeji wako ni nani hapa?”
“Bonta.”
“Hakukupa maelekezo?” alihoji mwanaume huyo na kabla sijamjibu chochote, kwa bahati nzuri Bonta naye alitokeza akiwa na wenzake, wote wakiwa wamevaa makoti marefu meusi.
“Gamutu, huyo ni mgeni niachie mimi ntamuelekeza,” alisema Bonta, naye kwa sauti ya kibabe ambayo sijawahi kumsikia akiitoa, Suma akageuka na kumtazama Bonta, wakatazamana kwa sekunde kadhaa kisha mwanaume huyo akanigeukia na kushusha pumzi ndefu, akaelekea kwenye mlango uliokuwa unafuatia.
“Mdogo wangu, jiandae tunaenda mazoezini,” alisema huku akinirushia mfuko wa plastiki, nikaudaka na kumtazama Bonta.
“Badilika fastafasta nakusubiri hapa nje,” alisema, nikawa bado sijaelewa. Sikuona sababu ya yule jamaa mwenye mwili mkubwa kuwa mkali kwangu kiasi kile wakati sikuwa najua chochote. Niliingia ndani na kuufungua ule mfuko, ulikuwa na koti refu jeusi na mabuti kama yale wanayovaa wanajeshi.
“Kezia alikuwa amesimama kwenye mlango wa kuingilia maliwatoni, akionesha kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake.
“Muda wa kazi umefika! Sijui akifika chumbani kwangu na kunikosa atanifanya nini.”
“Nani?”
“Si huyo Gamutu! Jamaa nuksi huyo, angeweza kukutandika na mkanda wa jeshi mpaka ukome,” aliniambia Kezia, sikumjali sana, nikabadilisha nguo harakaharaka na kuvaa suruari yangu na fulana, juu nikavaa lile koti na kumalizia na mabuti.
“Wakikuuliza chochote kuhusu mimi waambie hujaniona, ukitoka usifunge mlango tutakutana hukohuko,” alisema, nikamsogelea na kumbusu kwenye paji la uso, akatabasamu. Nikatoka nje ambako Bonta alikuwa akinisubiri na wale wenzake, tukaanza kuelekea upande wa pili ambako wala sikuwa nakujua.
Tulikatiza kwenye kama shamba fulani hivi la miti, tukatokezea upande wa pili, nikashtuka kutokana na nilichokiona.
Watu wengi walikuwa wamesimama kwa kujipanga mstari, wote wakiwa wamevalia makoti meusi na wakiwa wamesimama kikakamavu, kwa harakaharaka idadi yao ilikuwa ni zaidi ya thelathini, wanaume wakiwa ndiyo wengi huku pia kukiwa na wanawake wachache.
Watu walizidi kuongezeka na hesabu za harakaharaka, mpaka Gamutu mwenyewe anafika, kulikuwa na watu kama hamsini hivi. Alipofika tu, nilimuona Kezia naye akiwasili kwa kujifichaficha, akajichanganya kama vile alikuwepo.
“Hii tabia ya kuwa tunafuatanafuatana vyumbani baada ya kengele leo ndiyo mwisho. Siku nyingine sitawafuata na mkanda, nitakuwa nakuja na bastola,” alisema kwa sauti iliyojaa vitisho. Basi kilichofuata baada ya hapo, alianza kutugawa kwa makundi, yakapatikana makundi matano.
Tukaanza mazoezi, yeye alikuwa amesimama mbele kwa hiyo akawa anatuelekeza kwa vitendo kisha tunaanza kufanya kama yeye alivyofanya huku akipita na kutukagua.
Nilishangaa kugundua kwamba hata akina Bonta nao walikuwa na mbabe wao maana pale yeye ndiyo alikuwa ‘top’, wengine wote wakawa wanafuata maelekezo yake, hakukuwa na Bonta wala Jombi, wote tulikuwa chini yake.
Tulianza kwa pushapu, yeye kazi yake ikawa ni kusema tu ‘chini, juu, chini...’ kisha anapita kukagua kama kuna aliyekuwa anafanya mzaha. Tofauti na kule Kazimzumbwi ambako wengi wetu tulikuwa tukibabaika, pale kila mtu alikuwa fiti, pushapu zilipigwa kwa muda wa kama saa nzima.
Ilifika mahali mimi mikono ikawa imekufa ganzi kabisa lakini nikawa najikaza. Baada ya hapo, tulianza zoezi la kurukaruka vichura, tukaruka kwa muda mrefu mpaka nikawa nahisi kama mwili wangu unapoteza ushirikiano.
Hakukuwa na mtu aliyekuwa ‘analialia’ kuchoka, akabadilisha zoezi na sasa tukawa tunafanya ‘squats’, kwa wale wanaofanya mazoezi mara kwa mara watakuwa wanalijua hili zoezi, unajishika mikono kichwani au kiunoni halafu unakuwa unashuka chini mpaka unachuchumaa kisha unasimama.
Tulifanya zoezi hili kwa muda mrefu mpaka uzalendo ukaanza kunishinda. Mara kwa mara Bonta alikuwa akinitazama kuhakikisha kama naenda sawa na wenzangu, akawa ananipa ishara za kunitia moyo ambazo kimsingi zilinisaidia sana.
Baada ya hapo, alituamrisha wote kuingia kwenye jengo kubwa kama bwalo hivi, mle ndani mlikuwa kama ‘gym’, kulikuwa na vyuma vingi vya kufanyia mazoezi na vifaa vingine vingi, tukanyanyua sana vyuma zamuzamu huku akipita kukagua kwa karibu kuona kama kila mtu anafanya kile alichoambiwa.
Zoezi la mwisho, lilikuwa ni la ‘ku-craw’, haya mazoezi huwa wanayafanya sana wanajeshi, mnalala chini na kuanza kujivuta kwa kutumia tumbo huku ukitumia viwiko vya mikono.
Alitupeleka kutambaa umbali mrefu sana, wakati mwingine tukipita kwenye mifereji, kwenye miba, kwenye kokoto mpaka mimi ikafika mahali nikawa nahisi tumbo na viwiko vya mikono vinavuja damu.
Mpaka tunamaliza, ilikuwa tayari ni alfajiri, kengele ikagongwa tena mara moja kama mwanzo, tukarudi na kwenda kujipanga palepale tulipoanzia, Gamutu akawa anatoa maelekezo.
“Usiku wa leo kuna kazi! Mtakaochaguliwa mtajulishwa mapema, ambao hamtachaguliwa kutakuwa na mazoezi ya kulenga shabaha, atakayeleta masihara tutamuweka yeye kama sehemu yakujifunzia shabaha, wale wenye mikono yote ya kushoto muanze mazoezi mapema,” alisema kibabe kisha akatoa ishara ya wote kutawanyika.
“Vipi mshkaji wangu, uko vizuri kinoma. Nilikuwa nakufuatilia,” Kezia aliniambia wakati nikitembea kichovu kurudi chumbani kwangu, tukacheka kichovu maana wote tulikuwa tumechafuka na kuchoka vibaya.
Hatukuwa na stori nyingi, tukaagana na kilammoja akaenda kwenye chumba chake. Nilielewa kwa nini Kezia muda niliofika aliniambia kwamba amechoshwa na maisha ya pale gerezani. Ilikuwa ni zaidi ya kambi ya jeshi, zaidi ya gereza.
Kwa mazoezi yale, nilielewa ni ugumu gani polisi wanakabiliana nao kwa sababu kwa mazoezi yale, mkienda kufanya tukio halafu mkakutana na polisi wachovu, mnaweza kuwafanyia kitu kibaya sana.
Yalikuwa ni mazoezi magumu na ya kuchosha sana ambayo hata kama ulikuwa na moyo mzuri kiasi gani, yanakubadilisha na kukufanya uwe na roho ya kikatili. Nilipoingia ndani kwangu, nilifikia bafuni, nguo zilikuwa hazitamaniki, ikabidi nianze kwanza kuzifua, kisha na mimi nikaoga na kujisafisha vizuri.
Mpaka narudi kitandani kupumzika, ilikuwa ni tayari saa kumi na moja alfajiri. Nilipojilaza tu, nilipitiwa na usingizi mzito, nilikuja kuzinduliwa na mtu aliyekuwa akigonga mlango.
Niliamka kichovu nakutoka, alikuwa ni yule mzee wa chakula, alikuwa ameleta kifungua kinywa. Kilikuwa ni kifungua kinywa cha nguvu, supu, chapati nne na vikorombwezo vingine kibao.
“Wewe ni mgeni? Sura yako ni ngeni kwangu,” aliniambia yule mzee, nikamjibu kwamba ni kweli mimi ni mgeni na ndiyo kwanza nilikuwa nimefika jana yake tu.
“Utapaweza kweli hapa? Maana shughuli ya hapa si ya kitoto,” aliniambia huku akitabasamu, sikumjibu zaidi ya kutabasamu kichovu maana alichokuwa anakisema tayari nilishaanza kukiona. Basi akaniachia kifungua kinywa na kuondoka zake.
Alipoondoka tu, Gamutu alikuja na kunigongea, nikapata bahati ya kumtazama vizuri. Hata sijui nimuelezee vipi, lakini kwa kifupi aliniambia kwamba na mimi nimepangwa kwenye kazi ya usiku kwa hiyo nijiandae.
Mapigo ya moyo yalinifyatuka paaah! Moyo ukaanza kunidunda, nikajua mwisho wangu umewadia.
Je, nini kitafuatia?



Sehemu ya 27 imeletwa kwa udhamini wa Pyaar
 
SEHEMU YA 28


ILIPOISHIA:
Alipoondoka tu, Gamutu alikuja na kunigongea, nikapata bahati ya kumtazama vizuri. Hata sijui nimuelezee vipi, lakini kwa kifupi aliniambia kwamba na mimi nimepangwa kwenye kazi ya usiku kwa hiyo nijiandae.
Mapigo ya moyo yalinifyatuka paaah! Moyo ukaanza kunidunda, nikajua mwisho wangu umewadia.
SASA ENDELEA...
Kumbukumbu za tukio la kwanza tulilolifanya kule Tandika, zilikuwa zikipita kwa kasi ndani ya kichwa changu, nikawa nasikia milio ya risasi, nikawa nawaona wale wenzangu wawili jinsi walivyochakazwa na risasi na kupoteza maisha, mmoja palepale eneo la tukio na mwingine ndani ya gari!
Japokuwa kulikuwa ni baridi, nilijihisi kijasho chembamba kikinitoka. Gamutu aliondoka na kuniacha nimesimama palepale mlangoni, mawazo mengi yakiendelea kupita ndani ya kichwa changu.
“Oya vipi mwanangu, mbona unambwelambwela hapo?” sauti ya Kezia ndiyo iliyonizindua kutoka kwenye lindi la mawazo, nikalilazimisha tabasamu kwenye uso wangu.
“Daah! Mwanangu jana bado kidogo nibambwe, lile dubwasha sijui lingenifanya nini maana huwa linanitongoza kila siku nalikimbia,” alisema Kezia kwa mbwembwe na kunifanya nishangae. Stori zake kidogo zilinisahaulisha jambo zito lililokuwa mbele yangu.
Tuliingia ndani, Kezia akaendelea kunipa michapo kuhusu yeye na Gamutu na jinsi anavyomfanyia visa baada ya kukataa kuwa naye kimapenzi.
“Ujue mimi hapa napata sana shida sema kwa sababu nimeshakuwa na roho ya korosho, najua namna ya kushughulika na mijitu kama gamutu,” alisema Kezia huku akicheka na kujitupa kitandani kwangu.
Nilishangaa sana kusikia Gamutu pamoja na ubabe wake wote, kumbe na yeye alikuwa akimtaka Kezia kimapenzi. Kama nilivyoeleza, Gamutu alikuwa na mwonekano wa kutisha kwelikweli, yaani ile taswira halisi ya jambazi ulikuwa unaweza kuipata kwa kumtazama. Alikuwa mrefu, mwenye mwili mkubwa halafu usoni ana makovu makubwamakubwa, midomo yake imebadilika rangi na kuwa myeusi, nadhani ni kwa sababu ya kunywa pombe kali na kuvuta sana sigara na macho yake yalikuwa mekundu sana nadhani ni kwa sababu ya kuvuta ‘mibange’.
“Lakini nampendea kwenye kazi, akiwaongoza kwenye ‘misheni’, anasimama mwenyewe mstari wa mbele na akishika chuma huwa hana masihara hata kidogo,” alisema Kezia na kunielezea jinsi ilivyokuwa kwenye matukio kadhaa aliyowaongoza.
“Nimeambiwa na mimi leo nitakuwa miongoni mwa watakaotoka usiku, yaani hapa nimechanganyikiwa kwelikweli,” nilimwambia Kezia, akacheka sana na kuniambia kwamba mwanzo mgumu, baadaye nitazoea na nitakuwa siogopi tena.
Maneno yake kidogo yalinifariji, tukaendelea kupiga stori za hapa na pale, tukikumbushiana tuliyoyafanya jana. Stori ziliendelea mpaka muda wa chakula cha mchana ambapo yule mzee aliponiletea cha kwangu, Kezia alimwambia na cha kwake pia amletee palepale kwangu, jambo ambalo alilikubali.
Tulikula chakula na Kezia, tukipiga stori nyingi na kucheka sana, tulipomaliza, Kezia alianza uchokozi wake tena, mwisho tukajikuta tukiwa kitandani. Alikuwa mwalimu mzuri sana kwangu na kadiri tulivyokuwa tukiendelea, ndivyo nilivyokuwa nikizidi kujifunza mambo mengi ambayo awali sikuwa nayajua.
Ukichanganya shibe na uchovu, tulijikuta tukipitiwa na usingizi palepale tukiwa tumelala kihasarahasara. Kilichokuja kunizindua, ni baada ya kusikia mlango ukigongwa kwa nguvu, nikakurupuka na kuanza kutafuta nguo zangu, Kezia akiwa bado ameuchapa usingizi.
Kibaya ni kwamba kumbe yule mzee alipoleta chakula, hatukukumbuka kufunga mlango, kwa hiyo aliyekuwa anagonga, alipoona kimya alijaribu kunyonga kitasa, kweli mlango ukafunguka.
Nilishtuka mno kugundua kwamba kumbe aliyekuwa akigonga alikuwa ni Gamutu, macho yangu na yake yakagongana, nikamuona akihamishia macho yake haraka kwa Kezia ambaye bado alikuwa amelala.
“Ahaaa! Kumbe ndiyo mchezo mnaoufanya huu,” alisema Gamutu huku akianza kuchomoa mkanda wa kijeshi kwenye suruali yake. Sauti yake ilimzindua Kezia kutoka usingizini, naye akakurupuka na kuanza kutafuta nguo zake.
“Tulia hivyohivyo,” alisema Gamutu huku akifunga mlango kwa ndani na kutusogelea. Kezia alikuwa ameshavaa skin tight yake, akakurupuka huku akiwa amejifunika shuka na kusimama mbele yangu huku akihema kwa nguvu.
“Gamutu please, naomba usifanye jambo lolote, mimi na wewe tutazungumza baadaye,” alisema Kezia kwa sauti ya kubembeleza, Gamutu akamtazama kwa sekunde kadhaa kwa macho ya ukali, nikamuona akifumba macho yake kidogo na kuyahamishia kwangu, akanitazama huku akihema kisha akashusha pumzi ndefu, Kezia akawa anaendelea kumsihi atulie watayazungumza.
Katika hali ambayo sikuitegemea, nilishangaa kumuona Gamutu akiurudishia mkanda wake kiunoni, kisha akageuka na kutaka kutoka nje, alipoufikia mlango akawa ni kama amekumbuka kitu.
“Jiandae tunaenda kwenye maandalizi ya mwisho sasa hivi, nakupa dakika mbili,” alisema kisha akafungua mlango na kutoka, akaubamiza kwa nguvu, mimi na Kezia tukawa tunatazamana.
“Nisamehe, mimi ndiyo mwenye makosa,” alisema Kezia na kwenda kufunga mlango kwa ndani, akaja na kunikumbatia kwa nguvu huku akinibusu sehemu mbalimbali za mwili wangu.
“Mkienda naye kwenye kazi kuwa makini, anaweza kukufanyia makusudi kulipa kisasi, nitajaribu kuzungumza naye kabla hamjaondoka, najua namna ya kumtuliza,” alisema, akaniachia na kuanza kuvaa nguo zake, na mimi nikavaa za kwangu na kuanza kujiandaa kama alivyoniambia.
Harakaharaka Kezia alinibusu tena na kwenda kufungua mlango, akatoka na kuniambia anataka kabla hatujaondoka tuonane, nikatingisha kichwa kumkubalia, moyoni nikaanza kuwa na hofu kwa sababu kweli Gamutu angeweza kunifanyizia.
Baada ya kumaliza kujiandaa, nilitoka na kuelekea kule kwenye uwanja wa mazoezi, nikawakuta baadhi ya watu wakiwa wameshafika, muda mfupi baadaye Gamutu akaja akiwa ameongozana na Bonta.
“Zungumza naye!” alisema Gamutu huku akimuonesha ishata Bonta eti azungumze na mimi, nilishajua kinachoendelea, basi nikawa mpole maana nilijua nikiendelea kuleta ujeuri, kinachoweza kunikuta ni kibaya sana.
“Vipi mdogo wangu,” alisema Bonta huku akinishika begani kirafiki kama kawaida yake, tukasogea pembeni ambapo aliniambia kwamba amepelekewa mashtaka na Gamutu kwamba namuingilia kwenye anga zake. Nilikubali kila kitu kwa sababu hata Bonta mwenyewe alikuwa anajua kinachoendelea na yeye ndiye aliyechomekea ishu ya ukaribu kati yangu na Kezia.
“Sikia mdogo wangu, huyu jamaa huwa ana visasi sana, we achana na yule msichana, kama unashindwa kumuacha basi fanyeni mambo yenu kwa siri, anaweza kukufanyia kitu kibaya maana siyo mtu mzuri,” alisema Bonta, basi nikawa natingisha kichwa kwa unyenyekevu kumuonesha kwamba nimemuelewa.
Kwa kuwa muda wa mazoezi ulishafika, tulianza kupewa maelekezo ya nini cha kufanya na aliyekuwa akitoa maelekezo hayo, alikuwa ni Gamutu, marakwa mara akawa ananikata jicho baya na mimi nikawa nainamisha kichwa chini kwa sababu sikutaka aone kama ‘namvimbia’.
Alitupa mchongo wa kazi nzima, ilikuwa ni kazi ya kwenda kuvamia nyumbani kwa mfanyabiashara mmoja mkubwa jijini Dar es Salaam aliyekuwa akiishi Kunduchi na kulikuwa na taarifa kwamba ameingiza nchini fedha kibao za kigeni lakini ameshindwa kuzipeleka benki akihofiwa kukamatwa kwa kesi ya utakatishaji wa fedha haramu.
“Bosi Mute anazitaka fedha zote leoleo na mimi nimeamuahidi kwamba zitapatikana, sasa asitokee kenge yeyote wa kufanya uzembe kutaka kutukwamisha,” alisema Gamutu huku safari hii akiwa amenikazia macho mimi, nikajua kazi imeanza.
Ilikuwa ni mapema mno kwangu mimi kuingia kwenye ‘mabifu’ ya kugombea wanawake na wakubwa zangu, moyoni nikajiapiza kwamba kama hilo likipita salama, sitaki tena kuwa karibu na Kezia.
Tulielekezwa kila kitu kinachotakiwa kufanyika, tukaoneshwa na ramani ya nyuma yenyewe na jinsi walinzi wanavyojipanga. Tulipewa vifaa muda huohuo, ikiwa ni pamoja na makoti mengine pamoja na silaha, Gamutu akasisitiza kwamba kila mmoja akatulie kwenye chumba chake kusubiri muda wa kazi.
Baada ya hapo, tulitawanyika na kila mmoja akaelekea kwenye chumba chake, wakati tukiondoka Bonta alinikonyeza na kunipa ishara fulani, nikamuona akimfuata Gamutu, wakaondoka pamoja.
Mle ndani kutembea na silaha halikuwa jambo la ajabu kwa hiyo na mimi nilibeba bunduki yangu na kwenda nayo ndani kwangu pamoja na vile vifaa vingine nilivyopewa. Nikaenda kujitupa kitandani nikiendelea kutafakari mambo mengi ndani ya kichwa changu.
Muda uliyoyoma nahatimaye kigiza kikaanza kuingia, Kezia jinsi asivyo muoga, mishale ya kama saa moja hivi, alikuja tena chumbani kwangu huku akiwa amechangamka kama kawaida yake. Akaniambia ameshazungumza na Gamutu ila amemwambia atampa majibu atakaporudi usiku.
“Wala usiwe na wasiwasi ila cha msingi ni kuwa naye makini tu mkiwa kwenye kazi,” alisema Kezia, akanibusu na kunitakia kila la heri kisha akaondoka zake. Chakula kilikuja, nikala harakaharaka na baadaye, nilisikia filimbi ikipulizwa, kama Gamutu alivyokuwa ametuelekeza, nilitoka harakaharaka nikiwa nimeshajikoki na kwenda mpaka kule kwenye lile jengo kubwa ambako tuliambiwa ndiyo sehemu ya kuondokea.
Nilipofika, nilikuta magari mawili, Toyota Noah yote ya rangi nyeusi yakiwa yameshapaki, wenzangu wakawa wanaingia na mimi nikajichanganya na kuingia. Tuliondoka watu kumi na mbili, sita kwenye kila gari na kati ya wote hao, ni mimi peke yangu ndiye niliyeonekana kuwa mdogo.
Hata kabla ya kuambiwa chochote, nilijua kwamba lazima kazi itakuwa ngumu na ndiyo maana wanaondoka wakongwe watupu, isipokuwa mimi tu. Nilifarijika sana kugundua kwamba Bonta naye ni miongoni mwa tunaoenda nao.
Kutoka Kibaha mpaka Kunduchi, tulitumia muda wa kama dakika arobaini tu, tukawa tumeshafika kwani madereva walikuwa wakiendesha kwa kasi utafikiri tupo kwenye mashindano.
Tulienda kupaki kwenye eneo moja la wazi lililopo ufukweni kabisa mwa bahari, upande wa kushoto kulikuwa na makaburi ambayo baadaye niliambiwa kwamba ni makaburi ya Wagiriki.
Tulipofika, wote tulishuka kwenye magari, gamutu akarudia tena kutupa maelekezo ya mwishomwisho, akasema inabidi tuvutevute muda kidogo maana ilikuwa bado mapema. Muda huo ilikuwa ni karibu saa tano za usiku.
Basi wengine walianza kuvuta ‘mibange’ pale ufukweni, wengine wakawa wanakunywa pombe kali lakini mimi sikutaka kutumia kilevi chochote, tishio la Gamutu lilinifanya nitamani muda wote kuwa timamu.
Tulivutavuta muda mpaka ilipofika saa saba, Gamutu akatoa ishara na wote tukaingia kwenye magari, tukatoka na safari hii magari yalikuwa yakienda mwendo wa taratibu, tukielekea kwenye makazi ya mfanyabiashara huyo ambaye baadaye nilikuja kugundua kwamba anaitwa Subash, ana asili ya India.
Tulipokaribia kwenye hekalu lake, tuliteremka kwenye magari, Gamutu akaanza kutupanga namna ya kuingia, cha ajabu eti alinipanga mimi na yeye tupite njia moja, hofu ikazidi kutanda kwenye moyo wangu.
Mle kwenye magari tuliwaacha madereva tu ambao nao walikuwa wameyawasha magari na kuyaweka ‘silensa’, kwa wanaojua kuendesha magari watakuwa wananielewa.
Tulitawanyika na kuanza kusonga mbele kwa tahadhari kubwa kuelekea kwenye jengo hilo, tukiwa tumelizunguka, wakati tunakaribia, niliamua kuikoki bunduki yangu ili kuzijaza risasi katika ‘chemba’, tayari kwa chochote.
Katika hali ambayo sikuitegemea, nilishangaa ikigoma kuikoki, nikahisi labda nilikuwa sijatoa ‘safety lock’, nikahakikisha lakini hakukuwa na tatizo, nikajaribu tena kuikoki lakini wapi. Kijasho kikaanza kunitoka, muda huohuo Gamutu alitoa amri ya kuanza kushambulia, milio ya risasi ikaanza kurindima lakini ya kwangu ilishindwa kabisa kutoa risasi hata moja.
Walinzi waliokuwa wamejipanga, nao wakiwa na silaha za moto, walianza kujibu mashambulizi, mimi nikawa bado nahangaika na bunduki yangu huku Gamutu akiwa ametangulia na kuniacha nyuma nikihangaika, akili ikanituma kuchomoa ‘magazini’ ili niichomeke vizuri.
Nilishtuka sana kugundua kwamba ‘magazini’ yangu ilikuwa tupu, haikuwa na risasi hata moja, nikajua lazima aliyenifanyia mchezo huo ni Gamutu kwa sababu yeye ndiye aliyekuwa akigawa bunduki.
Nilijiona mzembe sana kwa kushindwa kuikagua tangu tukiwa kule kambini, nikiwa bado sielewi nini cha kufanya, nilishtukia tukimulikwa na taa kali iliyokuwa kwenye mnara wa mbele wa lile jengo, kisha risasi zikaanza kumiminwa kwa kasi kuelekea pale tulipokuwepo, nikazidi kuchanganyikiwa huku nikiwa sijui nini cha kufanya.
Je, nini kitafuatia?



Sehemu yq 28 imeletwa kwa udhamini wa Pyaar
 
SEHEMU YA 29




ILIPOISHIA:
Nilijiona mzembe sana kwa kushindwa kuikagua tangu tukiwa kule kambini, nikiwa bado sielewi nini cha kufanya, nilishtukia tukimulikwa na taa kali iliyokuwa kwenye mnara wa mbele wa lile jengo, kisha risasi zikaanza kumiminwa kwa kasi kuelekea pale tulipokuwepo, nikazidi kuchanganyikiwa huku nikiwa sijui nini cha kufanya.
SASA ENDELEA...
Akili zilinituma kulala chini maana sikuwa na ujanja tena, bunduki haina risasi halafu tunashambuliwa. Basi nilibinuka kikomando na kuangukia pembeni ya maua, mahali ambapo nilijua hata wakipiga risasi vipi hawawezi kunipata.
Kwa kuwa wenzangu walikuwa wakisonga mbele, na mimi niliamua kusonga mbele lakini kwa mfumo tofauti, nilianza ku-craw kama tulivyojifunza kule kambini lakini nilijitahidi kuwa makini nisionekane, nikawa natambaa kufuata mstari wa maua.
Mvua ya risasi iliendelea kumiminika kwa kasi, Gamutu akawa anaendelea kupambana kwelikweli huku akisonga mbele. Alichokisema Kezia kweli nilijionea mwenyewe, Gamutu hakuwa na masihara kwenye kazi, alikuwa anatisha kama jinamizi.
Muda mfupi baadaye, wale walinzi waliacha kujibu mashambulizi, nadhani waliona hawawezi kupambana na moto wetu. Tayari tulikuwa tumeshafika kwenye lango la kuingilia na ile mbinu tuliyotumia ya kutokea pande tofauti, naona ilisaidia sana kuwachanganya wale walinzi.
Huku kila mmoja akihema, Gamutu alitugawa tena, akachagua wanaotakiwa kuingia ndani kisha mimi na wenzangu wawili, tulitakiwa kubaki pale nje. Hakukuwa na muda wa kupoteza, akafyatua risasi kwenye kitasa kisha geti likaachia na kufunguka, akageuka na kunitazama usoni.
Nilijua kwa nini amenitazama vile, pengine alitegemea mpaka muda huo ningekuwa nimeshaangushwa, na mimi nikamtazama kwa jicho kali, akaingiza mkono kwenye koti lake, akatoa ‘magazini’ ya ziada na kunirushia, nikaidaka na ndani ya sekunde chache, tayari nilishaipachika kwenye bunduki, nikaikoki na kweli ikakubali.
Mpaka hapo nilijua kwamba kumbe alifanya makusudi na pengine alikuwa anataka jambo baya linitokee mapema kabisa. Hakuna aliyeelewa nini kimetokea, basi wote wakaingia ndani na sisi watatu tukajipanga pale nje kuhakikisha tunawalinda.
Kwa kawaida, mnapoingia sehemu kufanya tukio, hasa kama sehemu yenyewe ni ndani, lazima baadhi mbaki nje ili hata kukitokea la kutokea, wawepo wa kuwasaidia wenzao. Tulijipanga kwa mfumo wa kugusanisha migongo huku kila mmoja akitazama upande wake, chuma kikiwa 'standby'.
Kule ndani tulisikia risasi zikiendelea kurindima, na sisi tukazidi kukiweka tayari kwa chochote. Wakati kazi ikiendelea ndani, tulishtukia gari likija kwa kasi kutoka barabara kuu huku likipiga ving'ora. Yale magari tuliyokuja nayo yalikuwa yamepaki pembeni kiasi kwamba ukipita haraka huwezi kuyaona, ukichanganya na rangi yake nyeusi ndiyo huwezi kushtukia kabisa.
Awali tulijua ni polisi, ikabidi tubadili mfumo wa kukaa kwa haraka, wote tukaelekeza silaha zetu kule lile gari lilikokuwa linatokea.
Kumbe lilikuwa ni gari la kampuni ya ulinzi, nadhani ndiyo waliokuwa wakilinda nyumba hiyo. Kiukweli miongoni mwa vitu ambavyo vinapaswa kufanyiwa kazi haraka na mamlaka zinazohusika, sijui ni jeshi la polisi au wizara ya mambo ya ndani, ni hizi kampuni za ulinzi.
Hebu fikiria, watu wanaona kabisa kwamba moto unawaka lakini wanakuja tu kichwakichwa na gari lao, walichoona cha maana kwao ilikuwa ni kuwasha ving'ora tu, hakika walikuwa wanacheza na moto na sijui kama hata huwa wanapitia mafunzo ya kijeshi, nadhani wengi huwa wanachukuliwa mitaani tu, na hata kama wamepitia mafunzo basi yanakuwa ni yale ya juujuu.
Basi tulikaa kuwasubiri, ‘walipojaa’ kwenye mstari tu, tulianza kuwafyatulia risasi na mimi nilimlenga dereva, ndani ya sekunde chache tu, gari lilishapoteza mwelekeo, nadhani ile risasi niliyomlenga dereva ilifika mahali pake, likayumbayumba na kwa sababu lilikuwa kwenye mwendo wa kasi, liliacha njia na kwenda kugonga mti kwa nguvu.
Hatukuwaacha, tuliendelea kushona risasi palepale lilipogonga mti na muda mfupi baadaye, kulikuwa kimya kabisa, kilichokuwa kinaonekana ni moshi na vumbi tu, tukaacha kufyatua risasi na kuinama, macho yote yakiwa pale ili akichomoza yeyote kati yao, tumalize kazi.
Hakuna aliyetoka, nadhani hawakutegemea kwa walichokutana nacho na sidhani kama kuna yeyote kati yao aliyesalimika, maana kama alisalimika risasi lazima ajali ilimtuliza. Ukimya uliendelea kule nje, ndani zikawa zinasikika risasi mojamoja na sauti ya Gamutu akitoa amri.
Muda mfupi baadaye, sisi tukiwa bado tumekaa mkao uleule wa kutazama eneo la tukio, Bonta alitoka akiwa amebeba bega, akafuatiwa na jamaa mwingine anaitwa Suma, kila mmoja akiwa na begi mkononi. Wakatoka mbio na kushtuka kuona hali waliyoikuta pale nje.
“Ni gari la walinzi, walikuwa wanakuja kwa kasi tukawatuliza,” alisema yule jamaa mwingine tuliyekuwa naye.
“Tunaondoka! Toeni back-up,” alisema Bonta, akimaanisha anataka tuwalinde mpaka watakapofika kwenye magari, tulifanya hivyo, nguvu zetu tukazielekeza zaidi pale kwenye lile gari maana hatukuwa na uhakika kama tumewamaliza wote au la!
Mbele walitangulia watu wawili wakiwa na silaha, wakafuatia Bonta na Suma ambao nao silaha zilikuwa mikononi huku wakiwa na yale mabegi ambayo nilijua lazima ndiyo yenye hizo fedha, nyuma yao wakafuatia wengine nao wakiwa na silaha na sisi kama tulivyoambiwa, wote watatu tulibaki kuweka ‘back-up’, na tulishafundishwa kwamba ukiambiwa uwe ‘back-up’, maana yake hata kuondoka au kuingia kwenye gari nyie ndiyo mnakuwa wa mwisho.
Watu wote walitoka kisha na sisi tukaanza kuwafuata kwa staili ileile ya kutengeneza kama duara dogo hivi kwa kupeana migongo halafu kila mtu anatazama upande wake kuhakikisha hakuna mtu yeyote anayeshambulia kutoka upande wowote, kwa hiyo hata mkitembea mnatembea kwa staili ya kuondoka kwa pamoja.
Tulitoka mpaka kwenye gari, kwanza wakaingia wakina Bonta na mizigo yao, dereva akaondoa gari kwa kasi kubwa. Ni hapo ndipo nilipogundua kwamba kuna mtu mmoja muhimu sana hakuwa ametoka pamoja na wenzake, Gamutu.
“Jamani Gamutu yuko wapi?”
“Mh! Hayupo kwenye lile gari la kwanza?”
“Hayupo, walioingia mle wote nimewaona na kwa kawaida Gamutu asingeweza kupanda kwenye gari la kwanza,” nilisema, mjadala ukaibuka pale. Wengine wakaniunga mkono kwamba Gamutu hakuwa ametoka.
“Tuondokeni! Hayo yatakuwa ni makosa yake,” alisema mmoja kati yetu, wazo ambalo sikuliunga mkono, ikabidi nishuke.
“Oyaa, tuondokeni! Tutakuacha na wewe,” alisema dereva na kabla hata hajamalizia kauli yake, tulisikia majibizano makali ya risasi yakianza upya kurindima kule ndani. Ni hapo ndipo kila mtu aliponiamini kwamba Gamutu hakuwa ametoka.
Sijui nilipata wapi ujasiri, nilianza kukimbia kwa kasi huku nikiwa nimeinama, nikienda kwa staili ya ‘zig-zag’, yaani unakimbia kwa kuhamahama kutoka upande mmoja kwenda mwingine huku ukisonga mbele.
Staili hii tulifundishwa kwamba hata kama kuna mtu anataka kukupiga risasi, hawezi kukulenga kwa urahisi mpaka awe mtaalamu wa shabaha kwelikweli. Niliikamata vizuri bunduki yangu na muda mfupi baadaye, tayari nilikuwa nimeshafika pale getini.
Kwa kuwa lango lilikuwa wazi, nilijibinua sarakasi na kuingia ndani nikiwa nabingirika.
Nilichokiona kilinishtua, Gamutu alikuwa amewekwa ‘mtu kati’, risasi zilikuwa zikipigwa kutoka ghorofa ya pili, nadhani walikuwa ni walinzi waliosalia, wakawa wanamlenga pale chini kiasi cha kumfanya ashindwe kusonga mbele, ikabidi awe anajibizana nao huku akijibanza kwenye kuta za viunga vya maua vya lile jumba la kifahari.
Katika mbinu tulizofundishwa, unaponaswa kwenye hali kama hii, huwezi kukimbia, lazima awepo mtu mwingine ambaye atakuwa anakupa sapoti, yaani mmoja anashambulia huku mwingine akiangalia njia ya kukimbia, akipata upenyo anakimbia na kujificha mbele, naye anaanza kushambulia na wewe ndiyo unapata nafasi ya kukimbia, basi mnaenda hivyo mpaka mnatoka.
Hicho ndicho kilichofanyika. Gamutu akiwa ameshapaniki, akijua amepatikana, alishtukia nikiibuka kwa kasi ya kimbunga na kuanza kupiga risasi mfululizo kule juu yalikokuwa yanatokea mashambulizi, akageuka haraka na kuniangalia, wala sikuwa na muda wa kumtazama.
“Mooove!” nilipaza sauti nikimuamrisha Gamutu ainuke pale alipokuwa amenasa wakati mimi nikiendelea kufyatua risasi mfululizo. Mbinu hili ilifanikiwa, Gamutu alifyatua risasi kadhaa kisha akainuka na kuanza kukimbia, mimi nikawa naendelea kuwazubaisha wale kule juu mpaka aliponifikia, tukageuka wote na kuanza kupiga risasi kwa pamoja huku tukirudi nyuma, tukafanikiwa kutoka getini na kuanza kukimbia kwa kupokezana.
Mimi nilikuwa nafyatua risasi huku yeye akikimbia, mbele kidogo na yeye akasimama na kuanza kufyatua, nikapata upenyo wa kukimbia, sekunde chache tu baadaye tukawa tumeshafika kwenye gari, tukarukia ndani kama mizigo.
Kugeuka nyuma, kulikuwa na walinzi kama wanne hivi wakiwa wameshafika getini, wakiendelea kufyatua risasi lakini tayari walishachelewa, dereva akaondoa gari kama tupo kwenye mashindano. Kijasho kilikuwa kikimtoka Gamutu kwelikweli, kwa mara ya kwanza nilimuona akiwa na hofu anavyokuwa.
Gari likiwa linaendelea kupasua lami kwa kasi, alishusha pumzi ndefu na kunitazama, nikajifanya sina taimu naye.
“Snox!” aliniita kwa sauti ambayo bado ilikuwa inatetemeka, nikamgeukia na kumtazama ‘kikauzu’, tukawa tunatazamana, watu wote walikuwa kimya ndani ya gari, wakitutazama.
“Bila wewe nilikuwa nakufa mdogo wangu! Sijui ulipata wapi akili za kunifuata kule ndani,” alisema kwa sauti ya kutetemeka, nikawa namtazama bila kusema chochote.
“Ahsante sana Snox, yaani hata siju...” alisema lakini kabla hajamalizia kauli yake, tulishtukia dereva akifunga breki za ghafla na kukata kona kali, wote tukatazama mbele ambapo tulishtuka kugundua kwamba kuna gari la polisi lilikuwa limepaki kwa namna ya kubloku barabara, mapigo ya moyo yakanilipuka kuliko kawaida.
Je, nini kitafuatia?



IMELETWA KWA UDHAMINI WA Pyaar
 
SEHEMU YA 30



ILIPOISHIA:
“Ahsante sana Snox, yaani hata siju...” alisema lakini kabla hajamalizia kauli yake, tulishtukia dereva akifunga breki za ghafla na kukata kona kali, wote tukatazama mbele ambapo tulishtuka kugundua kwamba kuna gari la polisi lilikuwa limepaki kwa namna ya kubloku barabara, mapigo ya moyo yakanilipuka kuliko kawaida.
SASA ENDELEA…
Tukiwa tumepigwa na butwaa, tulishtukia wale polisi wakianza kulishambulia gari letu kwa risasi, nikajua nisipokuwa makini yanaweza kutokea yaleyale ya Tandika, haraka sana nikajilaza chini kabisa ya siti, dereva naye akatumia uwezo wake binafsi wa kuligeuza gari na kuliondoa kwa kasi ya kimbunga.
Mbele kidogo aliiacha barabara ya lami na kuingia barabara ya vumbi, akaendelea kukanyaga mafuta kwa nguvu na ndani ya sekunde chache tu, tulikuwa tumeshawapoteza kabisa wale polisi.
Nilipohakikisha hakuna milio tena ya risasi inayosikika zaidi ya mvumo wa upepo mkali uliokuwa unaingia kwa kupitia kioo kimoja kilichokuwa kimevunjwa kwa risasi kuonesha kwamba gari lilikuwa kwenye kasi isiyo ya kawaida, niliinua kidogo kichwa, nikaona kumbe wenzangu wote nao walikuwa wamelala kama mimi.
Watu walipoona mimi nimeinuka, nao waliinuka na cha ajabu eti kila mtu alianza kucheka kwa nguvu huku wakimshangilia dereva. Nilikumbuka kwamba kumbe wote mle ndani walikuwa wamelewa isipokuwa mimi tu.
“Washenzi hawa, kwa akili zao lazima watakuwa wameshapigiana simu kutuzuia barabarani, sasa ni mwendo wa barabara ya vumbi mpaka tunafika,” alisema Gamutu huku akikaa vizuri pale kwenye kiti chake, dereva akawa anatingisha kichwa kuonesha kwamba amemuelewa.
Safari iliendelea kwa kasi kubwa huku Gamutu akiwa bado ananitazama, alionesha kuwa na shauku kubwa ya kuendelea kupiga stori na mimi ila niliamua kuendelea kumuoneshea uso wa mbuzi ili siku nyingine asije akarudia tena kunifanyia kile alichokifanya kwa sababu ni kama alikuwa amekusudia kunitoa sadaka.
“Mbona kama bado umenikunjia mdogo wangu, tusameheane, sisi wote wanaume bwana,” alisema Gamutu huku safari hii akinipigapiga begani kirafiki kama anavyofanyaga Bonta, nikashusha pumzi ndefu na kutazama pembeni.
“Mkuu leo bila dogo ulikuwa umeisha,” alisema dereva, watu wote mle ndani ya gari wakamuunga mkono na kila mtu akaanza kunisifia. Ilibidi tu niulainishe moyo wangu, Gamutu akakiri kwamba tangu aanze kazi hiyo, hakuna siku ambayo amewahi kuwekwa mtu kati kama siku hiyo, akarudia tena kunishukuru sana na kuomba yaishe.
“Kwani mlikuwa na bifu?”
“Hamna! Kawaida tu si unajua tena,” Gamutu alijibu harakaharaka na kukatisha swali lililokuwa limeulizwa na mmoja kati yetu mle ndani. Stori ziliendelea, nikamuona Gamutu akitoa simu na kubofya namba fulani, kisha akaiweka simu sikioni.
“Mmefika wapi?” aliuliza, sijui alijibiwa nini, akaendelea:
“Hakuna nzi maana huku walitaka kutuletea namna gani,” alisema Gamutu, sijui alijibiwa nini. Yaani mazungumzo yale, hata kama kungekuwa na mtu anasikiliza, asingeweza kuelewa chochote kwa sababu yalikuwa katika mfumo wa mafumbo matupu.
“Wanakaribia ngome! Suka changamsha,” alisema Gamutu, dereva akaongeza mwendo, nilipochungulia pale kwenye ‘dash board’, niliona mshale wa spidi ukigonga kwenye namba 160, kuonesha kwamba gari lilikuwa likikimbia kwa kasi ya kilometa 160 kwa saa.
Sikuwa mzoefu wa magari lakini hali halisi ilikuwa inajionesha kwamba mwendo ulikuwa mkubwa sana, moyoni nikawa naomba kusitokee chochote mbele yetu maana kama tungepata ajali kwenye mwendo ule, sidhani kama kuna mtu angetoka.
Baada ya muda, tulitokezea Barabara ya Morogoro, dereva akaendelea kulichochea gari na haukupita muda mrefu, tukawa tumeshafika Kibaha, akakata kona na kuingia upande wa kulia kwenye barabara ya vumbi iliyokuwa inaelekea ngome.
Safari iliendelea na hatimaye tuliwasili salama ngome, muda huo ilikuwa tayari ni saa tisa kama na nusu hivi, usiku wa giza totoro. Tulikuta tayari akina Bonta wameshawasili na kushusha mizigo yao, lile gari lao lilishaondolewa eneo hilo, tukateremka kwenye gari huku tukigongesheana mikono na kukumbatiana kama kupongezana kwa kazi, gari likaingizwa ndani kabisa.
“Kazi nzuri sana!” alisema Gamutu baada ya kuwa wote tumekusanyika, akanigeukia na kunitazama.
“Usiku wa leo naomba nizungumze kitu ambacho nimekishuhudia kwa macho yangu!” alisema Gamutu huku akinishika mkono, akaninyanyua mkono juu kama vile wanavyofanyaga marefa wa ndondi wanapomtangaza mshindi.
“Huyu ndiyo nyota wetu wa leo, ahsante sana Snox na nakukaribisha rasmi kambini,” alisema kisha akanikumbatia kwa nguvu, akaendelea:
“Ukimtazama unaweza kumdharau lakini huyu ndiye aliyeokoa maisha yangu leo, natangaza rasmi kumpandisha mpaka kikosi cha kwanza, naomba mumpe ushirikiano,” alisema Gamutu na kututaka wote tutawanyike, kila mtu akawa anakuja na kunikumbatia na kunipongeza.
“Imekuwaje mdogo wangu!” alisema Bonta huku akinikumbatia kwa furaha. Ilibidi nimueleze kila kitu, akacheka sana na kuniambia kwamba hakukosea kunichagua siku ile aliponiona nikipigana na konda wa daladala. Maneno yake yalinifanya nicheke sana, alikuwa amenikumbusha kitu kilichozirudisha nyuma kumbukumbu zangu.
“Mtu akikuona anaweza kukuchukulia poa lakini mimi nakuhakikishia wewe ni bonge la jembe,” alisema huku tukiendelea kucheka, akanisisitiza kuwa makini na ishu ya Kezia na pia akanitaka niongeze juhudi katika mazoezi.
“Muda mwingine kama huna kazi uwe unakuja kunishtua tunaenda kupasha wenyewe, nataka uwe moto wa kuotea mbali,” aliniambia Bonta, basi tukaagana na mimi nikaingia chumbani kwangu.
Nilijifungia na kuanza kutafakari kila kitu kilichotokea, kiukweli nilijihisi furaha sana ndani ya moyo wangu. Nilikuwa najua kwamba nafanya kitu kibaya sana kwa kutegemea mtutu wa bunduki kujipatia riziki, lakini nikawa naikumbuka kauli ya Bonta kwamba ‘wakati mwingine unatakiwa kuwa na roho mbaya ili uishi vizuri kwenye hii dunia iliyojaa watu wenye roho mbaya’.
Baadaye nilienda kuoga na kujilaza, haukupita muda mrefu nikapitiwa na usingizi mzito. Niliposhtuka, tayari ilikuwa ni saa mbili za asubuhi, nikaenda tena kuoga na kurudi kitandani, nikawasha runinga maana nilikuwa napenda sana kufuatilia nini kinachoendelea kila tunapofanya tukio.
Habari kubwa kwenye TV asubuhi hiyo, ilikuwa ni ujambazi wa kutisha uliotokea Kunduchi. Nilisikitika sana kugundua kwamba kumbe katika lile tukio, mfanyabiashara tuliyeenda kumvamia, alikuwa amepigwa risasi ya tumbo iliyomjeruhi vibaya sana.
Pia walinzi kumi na mbili walikuwa wamepoteza maisha huku wengine sita wakiwa na hali mbaya. Tukiwa eneo la tukio nililiona kama ni dogo lakini kumbe halikuwa dogo, lilikuwa kubwa na la kutisha na ukiona mpaka TV zinarusha tukio kama ‘breaking news’ saa nyingi baada ya kutokea, tena kutoka eneo la tukio, basi ujue siyo jambo dogo.
Tukio lilikuwa limetokea majira ya saa nane za usiku, lakini muda huo saa mbili za asubuhi, bado TV zilikuwa zikirusha kila kitu ‘live’, hiyo tu ilitosha kuonesha tukio lilikuwa kubwa kiasi gani.
“Ni jambo la kusikitisha kuona ujambazi unataka kurudi tena kwa kasi, nawaomba wananchi watulie na watuamini, tutahakikisha tunawatafuta wahusika kwa udi na uvumba na kuwafikisha mbele ya mkono wa sheria, na bahati nzuri ni kwamba eneo la tukio kulikuwa na kamera za CCTV kwa hiyo tunaendelea kufuatilia kwa karibu, naamini tutawapata wahusika wote,” kamanda wa polisi wa kanda maalum alionekana akiwa anazungumza moja kwa moja kutoka eneo la tukio.
Nilishtuka kusikia kwamba kumbe eneo la tukio kulikuwa na kamera za CCTV, nikahisi lazima wakifuatilia kwa makini wanaweza kutubaini na kuzijua sura zetu wote tuliohusika, hofu ikarudi upya kwenye moyo wangu.
Nilisimama huku nikitetemeka, nikafungua pazia na kutazama nje, niliwaona akina Bonta wakiwa wamekaa kwenye viti vya kulala kule kwenye bustani za miti na maua, wakiendelea kunywa na kuvuta ‘mibange’ yao.
Nilishaanza kulemaa kitu kimoja, kila nilipokuwa na hofu ndani ya moyo wangu, nilikuwa napenda kupoteza mawazo kwa kunywa pombe, harakaharaka nikaenda kwenye friji na kufungua, nikatoa chupa mbili za bia na kuzifungua kwa mpigo, nikaanza kugida huku nikiendelea kufikiria nini itakuwa hatma yetu endapo sura zetu zikionekana.
Dakika chache baadaye, nilikuwa nimeshamaliza, nikaenda kuchukua nyingine mbili na kuendelea kunywa. Haukupita muda mrefu, nikawa nimeshaanza kuchangamka, ile hofu niliyokuwa nayo ikawa inapungua kadiri pombe ilivyokuwa ikizidi kukolea kichwani.
Nilienda kufungua mlango na kutoka nje, nikakaa pale kibarazani kidogo kisha nikarudi ndani, nikavaa fulana na kwenda pale walipokuwa wamekaa akina Bonta.
“Nimesikia eti pale kumbe kulikuwa na CCTV Camera,” nilimwambia Bonta, akaniambia nisiwe na wasiwasi, hilo ni jambo dogo ambalo halitakiwi kunisumbua kichwa.
“Kwa sasa tunywe na kufurahi, Bosi Mute yuko njiani anakuja, najua tutafurahi zaidi akifika,” aliniambia kwa sauti ya kilevi, akasogezea msokoto na kunipa.
“Hapana!”
“Aaah! Unataka kuniudhi tena, hebu piga,” alisema, nikaona basi isiwe kesi, nikapokea na kupiga pafu moja. Kama kawaida yangu, nilianza kukohoa, watu wote wakawa wananitazama huku wakicheka.
“Utazoea tu wala usijali,” aliniambia Bonta, nikavuta tena na safari hii sikukohoa, nikamrudishia mwenyewe, chupa kadhaa za pombe kali zikasogezwa pale mezani. Kule ndani nilikuwa nimeanza kunywa bia lakini pale hapakuwa na bia, pombe zote zilikuwa ni zile kali, nikajua kazi ipo kwelikweli.
Muda mfupi baadaye, lililetwa sinia lililojaa nyama na bakuli kubwa lililokuwa na supu, kila mmoja akachukua kibakuli chake na tukaanza kujisevia, ikawa ni mwendo wa kula, kunywa na kuvuta. Ile hofu niliyokuwa nayo iliisha yote, nikawa mtu mwingine tofauti kabisa.
Siri moja ya ulevi, ukiwa umelewa, hasa pombe kali na misokoto kama tulivyokuwa tunafanya, unaweza kufanya tukio halafu kesho yake ukisimuliwa, ukakataa kwamba siyo wewe. Hata sijui Kezia alifika saa ngapi pale tulipokuwa tumekaa, nilishtukia tu akiwa amekaa pembeni yangu, naye akinywa huku muda mwingi akiwa ananitazama.
“Snox! Umelewa, twende ukapumzike,” aliniambia, hata sikumbuki nilimjibu nini lakini baadaye nilipokuja kuzinduka, nilijikuta nikiwa nimelala chumbani kwangu nikiwa hata sijielewi.
Mara nikasikia mlango ukigongwa, kabla hata sijainuka, mlango ulifunguliwa. Alikuwa ni Kezia, akaniambia Bosi Mute alikuwa amefika na anahitaji kuzungumza na mimi. Nilishtuka kwa sababu kiukweli bado nilikuwa nimelewa sana, nitazungumza naye nini nikiwa kwenye hali kama ile?
“Kajimwagie maji kwanza, nakusubiri,” alisema Kezia, nikasimama huku nikipepesuka na kuelekea bafuni, nikajimwagia maji kwa wingi lakini bado haikusaidia chochote, bado nilikuwa nimelewa kwelikweli.
“Sasa itakuwaje?” nilimuuliza Kezia kilevi, akaniambia twende itajulikana hukohuko tukifika, nikavaa vizuri na kutoka huku nikiwa napepesuka. Aliniongoza mpaka kwenye chumba cha mikutano, nilipoingia nilikuta watu wote wamekaa na kutulia, utafikiri walikuwa wananisubiri mimi tu.
Mbele kabisa alikuwa amekaa Bosi Mute huku akivuta ‘ciger’ kama kawaida yake. Huku nikipepesuka, Kezia akaniongoza mpaka sehemu niliyotakiwa kukaa, nikajibwaga kama mzigo huku kichwa kikiwa kinazunguka kwelikweli.
“Snox!” aliita Bosi Mute. Kwa kawaida, ukiitwa unatakiwa kusimama na kuinamisha kidogo kichwa kama ishara ya utii lakini kwa jinsi nilivyokuwa nimelewa, haikuwa kazi rahisi kusimama, watu wote wakawa wanacheka wakati nikijikakamua kusimama.
Je, nini kitafuatia?


IMEDHAMINIWA NA Pyaar
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom