Riwaya: Saa za Giza Totoro

Riwaya: Saa za Giza Totoro

SEHEMU YA 31




ILIPOISHIA:
“Snox!” aliita Bosi Mute. Kwa kawaida, ukiitwa unatakiwa kusimama na kuinamisha kidogo kichwa kama ishara ya utii lakini kwa jinsi nilivyokuwa nimelewa, haikuwa kazi rahisi kusimama, watu wote wakawa wanacheka wakati nikijikakamua kusimama.
SASA ENDELEA...
“Mnamuona huyu kijana? Wangapi wanamjua?” alisema Bosi Mute, baadhi ya watu wakanyoosha mikono na wengine wakawa wanaendelea kucheka kwa sababu kwa jinsi nilivyokuwa ‘nimeutwika’, na ukizingatia kwamba sikuwa nimezizoea pombe, nilionekana kituko.
“Nakumbuka siku ya kwanza kuonana naye, aliletwa kwangu na Bonta! Sikumuamini, na naomba nikiri hapa waziwazi, sikudhani kama anaweza kuwa mtu muhimu kwetu kama ilivyo sasa.
“Nilimuona kama bado mdogo na asiyeweza kuendana na kasi yetu, lakini niliamua kumpa nafasi ili akue akiwa mikononi mwangu. Ndani ya kipindi kifupi tu tangu aungane nasi, ameonesha uwezo wa ajabu sana.
“Kwa heshima na taadhima, naomba wote tumpigie makofi,” alisema Bosi Mute, watu wote wakawa wanapiga makofi na kushangilia. Nilijisikia furaha isiyo na kifani ndani ya moyo wangu.
“Kwa mliokuwa naye usiku mtakuwa mnajua kilichotokea na ndiyo maana pengine amelewa sana leo! Kama motisha, natoa huu mzigo kwa ajili yake,” alisema Bosi Mute huku akitoa maburungutu mawili ya noti za shilingi elfu kumikumi mpya, yaliyokuwa yamefungwa vizuri, akatoka pale alipokuwa amekaa na kuja mpaka pale nilipokuwa, akanikabidhi yakiwa kwenye mfuko wa plastiki kisha akanikumbatia kwa furaha kisha akarudi sehemu yake.
Watu waliendelea kushangilia, Bosi Mute akaendelea kunimwagia ‘misifa’ mpaka nikahisi kama dunia yote naimiliki, alitoa maagizo kwa Gamutu na mwenyeji wangu Bonta kuhakikisha wanaendelea ‘kunipika’ zaidi kwa sababu eti mimi ni mtu muhimu sana.
Baada ya hapo, mgao wa pili ulipita kwa sababu kila tulipokuwa tukienda kufanya kazi, kuna mgao ulikuwa ukitolewa kwa watu wote, huku walioenda kwenye kazi wakipewa mgao wa juu zaidi ya wale wengine.
Likaongezwa burungutu jingine na kuufanya ule mfuko wa plastiki ukaribie kukatika sehemu ya kushikia, kama umewahi kubeba mzigo mzito kwenye mfuko wa rambo utakuwa unajua, nilipata fedha nyingi sana siku hiyo.
Japokuwa nilikuwa nimelewa, nilikuwa makini sana na fedha zangu, baada ya kikao kuisha, makreti ya bia, pombe kali, nyama choma na ‘mazagazaga’ mengine yaliletwa, watu wakaendelea kunywa na kufurahi lakini mimi sikuwa na uwezo wa kuendelea.
“Twende ukapumzike,” alisema Kezia huku akinishika mkono, kiukweli alinisaidia sana maana nilishapoteza mwelekeo, watu wengi wakawa wanakuja na kunipongeza, nikawa nachekacheka tu huku pombe zikizidi kukolea kichwani.
Kezia alinipeleka mpaka chumbani kwangu, akahakikisha ameniwekeza fedha zangu vizuri, akarudi na kuchukua pombe, naye akaja mlemle ndani na kufunga mlango kwa ndani.
Nilikuja kuzinduka wakati giza likiwa limeshaingia, nikamkuta Kezia akiwa amelala pembeni yangu, akiwa anachezea simu yake na kuendelea kunywa, nadhani mwenzangu alikuwa mzoefu na pombe.
Nilienda kuoga tena, nikarudi na kuanza kufakamia nyama choma alizokuwa ameniletea Kezia na kunywa maji mengi, kidogo nikawa najisikia vizuri. Kezia alinikumbusha kila kilichokuwa kimetokea, sikuwa nimesahau ila kumbukumbu hazikuwa zimekaa vizuri.
Usiku huo nililala na Kezia mpaka asubuhi kama mke wangu na hata ile hofu ya Gamutu sikuwa nayo tena japo Bonta alikuwa amenisisitiza sana kuwa makini na Kezia. Kesho yake niliamka nikiwa mchovu, kama ujuavyo tena masuala ya pombe, kama ukilewa sana basi ukiamka asubuhi lazima uwe na ‘hang-over’ ya nguvu.
Kezia alinifundisha kwamba njia nzuri ni ‘kuzimua’, tukanywa tena bia kadhaa asubuhi hiyo na kuendelea kupumzika. Kwa sababu ilikuwa wikiendi, siku hiyo tulishinda ndani tu na Kezia, tukawa tunapiga stori, tunaleteana michezo ya kimapenzi na kufurahi, ilionesha kwamba Kezia alikuwa ameanza kunipenda kiukweli kutoka ndani ya moyo wake kwani kuna wakati nilimsikia akizungumzia kuhusu maisha yetu ya baadaye.
“Mimi siwazi kuhusu maisha ya baadaye Kezia, nina matatizo makubwa sana nyumbani kwetu kama nilivyokwambia, inabidi niyatatue kwanza ndiyo akiliyangu itakapokaa sawa.”
“Nakuelewa Snox, lakini unafikiri tutafanya hii kazi mpaka lini? Kwa nini tusipange maisha yetu ya baadaye?” alisema Kezia kwa hisia za ndani kabisa za mapenzi. Kiukweli sikuwa nawaza kama yeye, nilikuwa naona ni mapema sana kuanza kufikiria kuishi na mtu wakati nilikuwa na ndoto nyingi kichwani mwangu, ikiwa ni pamoja na kurudi shule.
Hata hivyo sikutaka kumuonesha wazi kwamba sikuwa na malengo naye, basi nikawa namkatisha kijanja na kumwambia kwamba tunahitaji muda zaidi wa kuandaa mkakati wa namna ya kujitoa kwenye kazi hiyo.
Siku hiyo nayo ilipita, nikapata wazo kwamba natakiwa kuomba ruhusa ili niende nyumbani kumjulia hali baba kwa sababu mara ya mwisho nilipoondoka, hali yake wala haikuwa nzuri na japokuwa nilikuwa nimewaachia fedha za kutosha kwa ajili ya matumizi na dawa za baba, nilikuwa nahitaji kwenda kujionea mwenyewe maendeleo yake.
Nilipomwambia Kezia, aliniambia kwamba anataka kwenda na mimi na akanihakikishia kwamba nikimuomba Gamutu ruhusa ataniruhusu japo kwa masharti. Akanifundisha mbinu kwamba nianze mimi kuomba ruhusa, kisha na yeye ataomba ruhusa kivyake, ila inabidi tukakutanie Dar es Salaam kisha ndiyo tuendelee na ratiba nyingine.
Nilikubaliana naye lakini kama kawaida yangu, nilitaka pia kwenda kuzungumza na Bonta. Nilipomweleza ishu ya mimi kwenda nyumbani, alinikatalia na kuniambia kwamba natakiwa kusubiri hali ya hewa itulie kwanza, akaniambia kwamba kwa tukio tulilofanya, lazima polisi watakuwa wanaendelea na msako wa nguvu kila kona, kwa hiyo naweza kujikuta nikiangukia kwenye mikono yao.
“Lakini baba anaumwa na wewe unajua hali tuliyomwacha nayo.”
“Watumie tu hela! Unafikiri ukikamatwa itakuwaje? Kwanza utasababisha matatizo makubwa zaidi kwa sababu huna uwezo wa kuvumilia maumivu, wakikutesa lazima utaeleza ukweli na kutuchoma, watumie hela,” Bonta alinisihi sana na japokuwa kwa nje nilikubaliana naye, ile hulka yangu ya nikiamua jambo lazima nilifanye, ilinisukuma kufanya kila kinachowezekana ili nirudi nyumbani.
Nilipoenda kumwambia Kezia alichoniambia Bonta, naye alinishauri kwamba tusubiri kidogo mpaka hali itakapotulia kwa sababu alichokisema Bonta kilikuwa cha msingi sana. Naye sikutaka kuonesha kumbishia lakini moyoni nilishakuwa na maamuzi yangu na ilikuwa ni lazima niyatekeleze.
Basi ratiba za kawaida ziliendelea pale kambini, baada ya mapumziko ya siku mbili, tuliendelea na mazoezi kama kawaida, ikawa kila saa sita usiku tunaamshwa na kwenda kufanya mazoezi mpaka alfajiri, tunapumzika kisha ikifika saa kumi jioni tunaingia kwenye mafunzo ya mengine ya matumizi ya silaha, ikiwemo kulenga shabaha.
Nilijumuika na wenzangu kwa siku tatu, siku ya nne nikaanza kujipanga kutoroka. Kwa hesabu zangu nilipanga kwamba ile alfajiri tukitoka kwenye mazoezi, mi natafuta upenyo na kuruka ukuta maana isingewezekana kuondoka kwa kupitia mageti kwani yalikuwa na ulinzi saa ishirini na nne.
Nilipanga kwamba nitafanya kila kinachowezekana, ikifika saa kumi jioni niwe nimesharudi, kwa mfumo huo nilijua hakuna anayeweza kujua kwamba niliondoka. Basi nilijipanga kwa kila kitu na hatimaye siku ya nne alfajiri, niliruka ukuta nikiwa na kiasi kikubwa cha fedha nilizopewa kama zawadi na zile nyingine nilizopewa kama ujira wa kazi tuliyofanya.
Zilikuwa ni fedha nyingi sana kutembea nazo mfukoni lakini kwa kuwa nilikuwa nimechukua bastola ya Kezia bila mwenyewe kujua, sikuwana hofu hata kidogo, nikaanza kukatiza maporini mpaka nilipofika kwenye mashamba, nikawa natafuta uelekea wa barabarani.
Mpaka inafika saa kumi na moja alfajiri, tayari nilikuwa nimefika Kibaha Maili Moja, nikajichanganya na abiria wengine stendi huku nikijitahidi kutoonesha chochote kinachoweza kuwapa watu wengine wasiwasi. Muda mfupi baadaye, niliingia kwenye Coaster iliyokuwa inaelekea Dar es Salaam.
Bado kulikuwa na kigiza kile cha alfajiri na abiria wengi walikuwa wamelala, nadhani walikuwa wanatoka safari ya mbali. Sikuzungumza na mtu yeyote na nilijitahidi sana kuwa mtulivu, safari ikaanza huku nikiwa makini kuwachunguza abiria wote waliokuwa ndani ya lile gari, mmoja baada ya mwingine.
Mbele kidogo, gari lilisimamishwa na askari waliokuwa wameweka kizuizi barabarani, wengine wakazunguka upande wa dereva na wengine wakaja kwenye mlango wa abiria na kumwamuru konda afungue.
“Habari zenu abiria?” aliuliza askari mmoja kwa sauti ya juu iliyosababisha hata abiria waliokuwa wamelala washtuke, wachache wakamjibu.
“Hebu washa taa zote za ndani dereva,” alisema yule askari, dereva akatii, askari wengine watatu wakaingia, jumla wakawa wanne, wakawa wanapita na kuwatazama abiria vizuri, mmoja baada ya mwingine. Mapigo ya moyo yalianza kunienda mbio kuliko kawaida wakati yule askari mmoja akisogea upande niliokuwa nimekaa huku akiwa amenikazia macho.
Je, nini kitafuatia?
 
SEHEMU YA 32



ILIPOISHIA:
“Hebu washa taa zote za ndani dereva,” alisema yule askari, dereva akatii, askari wengine watatu wakaingia, jumla wakawa wanne, wakawa wanapita na kuwatazama abiria vizuri, mmoja baada ya mwingine. Mapigo ya moyo yalianza kunienda mbio kuliko kawaida wakati yule askari mmoja akisogea upande niliokuwa nimekaa huku akiwa amenikazia macho.
SASA ENDELEA...
“Habari yako!”
“Nzuri afande, shika..mooo!” nilimjibu yule askari ambaye sasa alikuwa amenisogelea pale nilipokuwa nimekaa.
“Unatoka wapi?”
“Natoka nyumbani naenda kazini.”
“Unafanya kazi wapi?”
“Mjini.”
“Unafanya kazi gani?”
“Aaa eeh! Naha...ngaika tu afa..nde! Niko gereji!” nilijibu kwa kubabaika, nadhani tayari yule askari alishahisi kwamba kuna kitu hakipo sawa kwa sababu nilipoteza kabisa utulivu.
Hata angekuwa mtu mwingine yeyote katika nafasi yangu, lazima angechanganyikiwa kwa sababu kwanza kiunoni nilikuwa na bastola na kwenye mfuko wa koti, nilikuwa na magazini iliyojaa risasi, achana na zile zilizomo kwenye bastola. Kama hiyo haitoshi, nilikuwa na kiasi kikubwa sana cha fedha nilizokuwa nimezisunda kwenye suruali na kwenye lile koti nililokuwa nimevaa.
“Kitambulisho chako tafadhali,” alisema yule askari, mapigo ya moyo yakawa yanazidi kunienda mbio kuliko kawaida kwa sababu ukweli ni kwamba sikuwa na kitambulisho chochote na kwa kawaida askari akitaka kukutia hatiani, hata kama huna kosa, anakimbilia kukuuliza kitambulisho.
“Afande John, hebu njoo mara moja kuna tatizo huku,” sauti ya askari mwingine ilisikika kutokea kule mbele ya gari, akageuka kuwatazama wenzake. Nadhani yeye ndiye aliyekuwa akiitwa Afande John.
“Nimekwambia toa kitambulisho,” alinisisitiza huku akigeuka na kunipa mgongo, nikajifanya kama najipapasa mwilini kutafuta kitambulisho wakati ukweli ni kwamba sikuwa na kitambulisho chochote, akasogea kule mbele alikoitwa na wenzake. Kule nako kulikuwa na zogo lingine, kumbe kulikuwa na abiria aliyekuwa akisafirisha gunia la mirungi na alikuwa amelichomeka katikati ya siti!
Kwa jinsi yule askari alivyokuwa amenikomalia, nilijua nisipofanya kitu, kweli naweza kujikuta nikiishia pabaya. Nilichokifanya, kwa kasi ya mshali nilivuta kioo na kukisogeza nyuma, kikaachia upenyo ambao naweza kuruka.
Kufumbana kufumbua nilijipindua na kuruka dirishani, huku mkono mmoja ukiwa tayari umeshaichomoa bastola na kuishika, niliamua liwalo na liwe, siwezi kukamatwa kizembe namna hiyo. Kelele walizopiga abiria niliokuwa nimekaa nao kwa mshtuko, ziliwashtua wale askari ambao wote walikuwa wamemzingira yule jamaa aliyekuwa amebeba mirungi.
Kwa kasi ya kimbunga nilikimbia na kuyavuka magari mengine ambayo nayo yalikuwa yamesimamishwa yakiendelea kukaguliwa, nikatokea upande wa pili wa barabara na kuanza kutimua mbio kwa kasi kubwa huku nikihema kwa nguvu. Nilijua kitu pekee kinachoweza kuniokoa kwa wakati huo, ni mbio tu, hakuna kingine.
Kila kitu kilifanyika kwa haraka mno kiasi kwamba mpaka askari wale walipokuja kushtukia ni nini kilichotokea mpaka abiria wengine wakashtuka kiasi kile, tayari nilikuwa nimeshazamia kwenye vichaka vilivyokuwa pembeni ya barabara upande wa pili.
Nikasikia vishindo vikija kwa kasi upande ule niliokimbilia huku askari wakijaribu kumulika kwa tochi zao kali. Ili kuwapunguza kasi, nilifyatua risasi mbili hewani, hali ikachafuka eneo hilo.
Kwa mafunzo niliyokuwa nimeyapata kule kambini, nilikuwa najua kwamba askari wanaposikia mlio wa bunduki, hata kama walikuwa wanakimbia, kwa kawaida ni lazima kwanza walale chini au watafute sehemu ya kujikinga kwanza ili kuepuka kupigwa risasi kizembe na kuangalia ni wapi risasi zinakotokea, kwa hiyo kitendo cha mimi kufyatua risasi ghafla, kiliwachanganya na kuwazubaisha kwa muda, huo ukawa upenyo mzuri kwangu kuzidi kukimbia.
Kwa bahati nzuri, kule nilikokimbilia kulikuwa kama na bonde hivi, kwa hiyo nikawa naporomoka kwa kasi kushuka chini na muda mfupi baadaye, tayari nilikuwa nimetokezea upande wa pili, kutazama nyuma nikaona mwanga wa tochi ukifuata kule nilikokuwa nakimbilia, nikafyatua risasi nyingine mbili na kulenga pale zile tochi zilipokuwa.
Nilijua kwa kitendo kile, hawawezi kuendelea kunifuatilia kwa sababu sasa mimi ndiye niliyekuwa tishio kwao. Niliendelea kukimbia na kiukweli mazoezi magumu ya gamutu yalinisaidia sana kuwa na pumzi, dakika chache baadaye nikawa nimeshawapoteza.
Nilijiona kuwa na mkosi sana kwa sababu kama nisingetumia mbinu hiyo, nilikuwa naenda kunaswa kizembe sana na sijui Bosi Mute angesikia kama nimekamatwa angechukua hatua gani, nikawa nazikumbuka zile sifa alizokuwa ananimwagia wakati akinitambulisha rasmi kwa wenzangu na kunipongeza kwa kazi nzuri niliyoifanya.
Nilichoamua ilikuwa ni kurudi kambini haraka iwezekanavyo kabla hakujapambazuka vizuri kwa sababu tayari ile ilikuwa ni hatari kubwa kwangu. Nilikimbia kwa muda mrefu, nikikatiza kwenye vichaka na mashamba ya korosho na minazi.
Ili kuficha utambulisho wangu kwamba kama wamenimaki kwa mavazi niliyovaa isiwe rahisi kunitambua, nilivua lile koti na shati, nikazifunga fedha zangu vizuri na kuendelea kukimbia nikiwa kifua wazi, mkono mmoja nikiwa nimeshika zile fedha nilizokuwa nimezingirisha kwenye nguo na mkono mwingine nikiwa nimeshika bastola.
Baada ya dakika kadhaa, tayari nilikuwa nimeshafika kwenye barabara inayoelekea Hospitali ya Tumbi, nikaivuka na kuendelea kukimbia kwa kasi utafikiri nashiriki kwenye mashindano ya mita mia moja.
Nilipofika umbali wa kama mita mia mbili hivi, nilisikia muungurumo wa gari likipita kwa kasi kuelekea Hospitali ya Tumbi, ilibidi nijibanze kwenye mti wa mbuyu na kulitazama, lilikuwa ni gari la polisi.
Nadhani walikuwa wameamua kunifukuza kwa gari na kwa mahesabu yao, waliamini kwamba kwa kipindi hicho lazima nitakuwa bado sijavuka barabara kwa sababu walikuwa wakimulika na tochi zao kali upande wa pili wa barabara, mbio zangu zilikuwa zimesaidia kuwazidi akili kwa sababu kama nisingekazana, pengine wangenikuta nikiwa bado sijavuka barabara na kwa jinsi tochi zao zilivyokuwa na mwanga mkali, wangeweza kuniona.
Nilijutia sana uamuzi wangu wa kutosikiliza ushauri, hata wa Bonta aliponiambia kwamba huko mtaani bado hali siyo shwari kwa hiyo nisiende nyumbani badala yake niwatumie hela kwa njia ya simu. Lile gari lilipopita, niliendelea kukimbia, safari hii nikiwa nimeongeza kasi zaidi ya awali, kweli asiyesikia la mkuu huvunjika guu.
Muda mfupi baadaye, nilitokezea sehemu iliyokuwa na makazi ya watu, ikabidi ile bastola niifiche na kuvaa fulana, lile koti nikabaki nimelishika vilevile, nikatokezea kwenye Barabara ya Morogoro na bila kupoteza muda, nilimsimamisha dereva wa bodaboda aliyekuwa akipita, akasimama mita chache mbele.
“Nipeleke machinjioni.”
“Dah! Braza kule siwezi kwenda muda huu, wanatupora sana pikipiki zetu,” alisema huku akipangua gia na kutaka kuondoka, ikabidi nitumie ushawishi wa fedha.
“Nitakupa shilingi elfu thelathini, kuna ng’ombe wetu wameibwa usiku nahisi watakuwa wanachinjwa muda huu, nataka niwahi,” nilimdanganya, kweli akaingia kwenye laini. Nilipanda, harakaharaka akaiondoa pikipiki na tukawa tunaelekea upande wa Mlandizi, kilometa chache mbele akakata kona mkono wa kulia na kuingia kwenye barabara ya vumbi.
Nilimwambia machinjioni kwa sababu kambi yetu ilikuwa upande huo ingawa kulikuwa na umbali mrefu kutoka hapo machinjioni mpaka kufika kambini kwetu, kwa wenyeji wa Kibaha watakuwa wanaelewa machinjio ya zamani ilipo, ni umbali wa kilometa kadhaa kutoka barabara kuu na upande huo hauna shughuli nyingi za kibinadamu na hata nyumba zake zimejengwa mojamoja sana.
Njiani nilikuwa namhimiza aongeze mwendo, wakati mwingine tukawa tunaserereka kwenye mchanga na kunusurika kuanguka, uzuri ni kwamba ilionesha na yeye alikuwa na uzoefu wa kutosha wa kuendesha pikipiki.
Tulipokaribia machinjioni, nilimuelekeza kwamba anishushe, nikamlipa fedha zake na harakaharaka akageuza pikipiki yake na kuondoka, nadhani alihofia kwamba pengine nina lengo la kumkaba na kumnyang’anya pikipiki yake, nikajifanya kama naelekea machinjioni na nilipogeuka na kujiridhisha kwamba yule bodaboda ameshapotea, nilikata kushoto na kuingiakwenye mashamba ya watu, nikaendelea kukimbia kufuata uelekea wa ile barabara inayoelekea kambini.
Mpaka kunapambazuka, bado nilikuwa nikiendelea kukimbia, yaani kama ni adhabu ya ukaidi, nilikuwa nimejipa adhabu kali kwelikweli. Baada ya kukimbia kwa zaidi ya dakika hamsini, hatimaye nilianza kuuona ukuta wa ngome, nikawa najiuliza nitaingiaje na nikionwa itasemaje kwa sababu sasa kulishapambazuka kabisa, moyoni nikajiambia potelea mbali.
Nilikimbia mpaka mwisho kabisa wa ukuta huo, upande wa nyuma, nikaenda mpaka kwenye mti mkubwa wa mkorosho uliokuwa upande wa nyuma, nikapanda na kuanza kuchungulia kwa ndani. Hakukuwa na pilikapilika zozote, nikashuka harakaharaka na kuanza kuhangaika kuruka ukuta.
Ukuta wa nyuma ulikuwa mrefu sana na kwa juu kulikuwa na nyaya za senyenge ambazo ukipita kizembezembe lazima zikunase. Nilitumia akili ya ziada, pembeni kulikuwa na gogo refu la mnazi, nikalisimamisha na kuliegamiza ukutani, kisha nikalitumia kupanda mpaka juu ya ukuta, nikajipenyeza kwa umakini kwenye zile senyenge kisha nikaligeua lile gogo, likadondokea upande wa nje kisha na mimi nikajirusha na kudondokea upande wa ndani.
Kwa bahati mbaya, wakati nikianza kujirusha, suruali ilinasa kwenye zile nyaya, hali iliyosababisha nipoteze ‘taimingi’ ya kuruka, nikajichana mguuni palepale kwenye senyenge na hata nilipotua chini, niliangukia mkono mmoja, nikasikia umelia ‘nkaa!’ kisha ukawa ni kama umekufa ganzi.
“Haya yote ni kwa sababu ya kutomsikiliza Bonta,” nilisema huku nikijikakamua na kuinuka, damu nyingi zikawa zinanitoka pale nilipojichuna na senyenge huku mkono nao ukianza kuniuma kwelikweli, eneo la kiwiko. Narudia tena, kama ni adhabu, nilikuwa nimepata adhabu ya kutosha kwa ukaidi wangu. Japokuwa nilikuwa nasikia maumivu makali, nilijikongoja na kupita nyumanyuma kuelekea kwenye chumba changu.
Wakati mwenyewe nikiamini kwamba hakuna aliyeniona, kumbe kule nilikokuwa napita, damu zilikuwa zikichuruzika na kuweka alama bila mimi mwenyewe kushtukia.
Nilipoingia ndani, nilikimbilia bafuni kwanza, nikavua nguo zote na kuzitupa koridoni, nikaanza kujimwagia maji huku nikiendelea kuugulia maumivu makali ya mkono na lile jeraha la mguuni, ilifika hatua nikawa siwezi tena kuvumilia maumivu, machozi yakawa yananitoka huku nikijilaumu sana kwa uzembe nilioufanya.
Nilikaa bafuni kwa zaidi ya dakika kumi na tano mpaka nilipohakikisha jeraha limeacha kutoa damu, nilipotoka ndiyo nikashtuka kuona kuna alama za damu kuanzia mlangoni mpaka bafuni, nikiwa bado nimepigwa na butwaa, nilisikiamlango wangu ukigongwa kwa nguvu.
“Fungua!” nilisikia sauti nzito ambayo sikugundua haraka ni ya nani kwa sababu kama ni Gamutu, tayari sauti yake nilikuwa naijua.
“Ngo! Ngo! Ngo!” mlango uligongwa tena kwa nguvu zaidi ya mara ya kwanza, nikazidi kuchanganyikiwa, nikiwa hata sijui nifanye nini.
Je, nini kitafuatia?
 
Duh! Boss atamuelewa kweli, si ndo atahisi anataka kusaliti kambi.
 
SEHEMU YA 33


ILIPOISHIA:
“Fungua!” nilisikia sauti nzito ambayo sikugundua haraka ni ya nani kwa sababu kama ni Gamutu, tayari sauti yake nilikuwa naijua.
“Ngo! Ngo! Ngo!” mlango uligongwa tena kwa nguvu zaidi ya mara ya kwanza, nikazidi kuchanganyikiwa, nikiwa hata sijui nifanye nini.
SASA ENDELEA...
Nilipiga moyo konde na kuamua liwalo na liwe, sikuwa na wasiwasi kwamba wanaweza kuwa ni watu kutoka nje kwa sababu mle ndani kulikuwa na ulinzi mkali sana, isingekuwa rahisi kwa mtu yeyote wa nje kufika mpaka kwenye mlango wa chumba changu.
“Habari yako,” mwanaume mmoja kati ya watatu waliokuwa pale mlangoni kwangu, wakiwa na silaha mikononi, kila mmoja akiwa amevalia sare maalum alinisalimu. Walikuwa ni walinzi waliokuwa wakilinda lile eneo lote la kambi yetu.
“Salama!”
“Toka nje tafadhali!” alisema, nikatoka nje kuwasikiliza.
“Bila shaka wewe ndiyo Snox.”
“Ndiyo!”
“Na bila shaka ukiona sare hizi utakuwa umeshatujua sisi ni akina nani.”
“Ndiyo! Si makamanda wetu mnaotulinda?”
“Ndiyo! Sasa kuna tatizo limetokea na inaonekana wewe ndiye mhusika,” alisema huku akinitazama.
“Unaweza kutueleza kwamba alfajiri ya leo ulikuwa wapi?”
“Nilikuwepo, vipi kwani?”
“Unaweza kueleza hizi damu zilizochuruzika kutoka kule kwenye ukuta mpaka ndani ya chumba chako zimetoka wapi?” alisema huku akinionesha michirizi ya damu iliyokuwa imejichora chini. Nilijiona mzembe sana kwa sababu ni kweli nilipoinghia ndani niligundua kwamba nilikuwa nikiacha michirizi ya damu, lakini sijui kwa nini sikupata akili ya kutoka na kufuta pale kwenye korido kwa sababu bado ilikuwepo na ilionesha kwamba imeingia ndani kwangu.
Nilishindwa kueleza chochote, wakaniuliza kama ndani ya chumba changu kulikuwa na mtu mwingine yeyote, wale walinzi wakalazimika kuingia ndani kwangu na kupekua ili kuhakikisha kama kweli hakuna mtu mwingine.
“Inabidi tuondoke na wewe, utatusamehe lakini kama ambavyo nyie mpo kazini, na sisi pia tupo kazini. Bosi akigundua kwamba kuna tukio kama hili halafu sisi hatujachukua hatua yoyote, inaweza kua tatizo,” alisema yule kiongozi wao, nikaona sasa imeshakuwa balaa.
“Naombeni tuyazungumze ndugu zangu, unajua kama mlivyosema hii ni kazi mnaweza kuniharibia hata mimi.”
“Tatizo lako hutaki kusema ukweli, tutakusaidia vipi wakati hatujui kilichotokea?”
Nilishusha pumzi ndefu na kuwatazama mmoja baada ya mwingine, nilichoamua ilikuwa ni kuwaeleza tu ukweli, kwamba alfajiri nilitoroka bila ruhusa lakini wakati narudi, niliruka ukuta ndiyo nikaumia mguuni na mkononi, kwa hiyo hizo damu zilikuwa ni za kwangu na hakuna tatizo lingine lolote.
“Tutajuaje kama unachokisema ni kweli?” yule kiongozi wao aliendelea kunikomalia, akili zikanicheza haraka, nikaingia ndani na kuhesabu noti kadhaa za shilingi elfu kumikumi, nikazitenga kwenye makundi matatu kisha nikatoka, nikawakabidhi kila mmoja mzigo wake, kwa hesabu za harakaharaka ilikuwa ni kama shilingi elfu hamsini kwa kila mmoja.
“Hebu tuelekeze ulipitia wapi, siku nyingine usirudie, ni hatari sana! Wewe kama unashida njoo tuzungumze lakini siyo kuruka ukuta,” alisema yule kiongozi wao, safari hii kwa lugha ya urafiki zaidi. Ama kweli pesa mwanaharamu, niliwaonesha kwa ishara tu, eti wao ndiyo sasa wakawa na kazi ya kupoteza ushahidi.
Walifukia alama zote za michirizi ya damu, na baadaye kumbe walitoka mpaka kule nje na kulitoa kabisa lile gogo la mnazi pale nilipoliangushia, kwa hiyo ushahidi kwamba nilitoka ukawa umefutika, tatizo likabakia kwenye majeraha yangu, mkono bado ulikuwa unauma sana kwenye kiwiko na lile jeraha sasa nilikuwa nalisikia jinsi ‘linavyopwita’.
Baada ya kumalizana nao, nilirudi ndani na kwenda kujilaza, haukupita muda mrefu Kezia akaja, kumbe naye aligundua kwamba asubuhi sikuwepo kwa sababu aliniambia kwamba alikuja na kunikosa. Aliniambia pia kwamba Bonta naye anajua kwamba alfajiri hiyo niliondoka, nikajiona mjinga sana, kumbe nilikuwa naleta usanii kwenye jumba la sanaa!
“Yaani hapa usidhani unaweza kufanya jambo halafu likawa siri yako! Najua huko nyumbani kwenu hujafika kwa sababu isingewezekana muda huu ukawa hapa, hebu niambie ulikuwa wapi,” alisema Kezia na kutaka kunikumbatia lakini nilimtoa kwa nguvu mwilini kwani alinigusa ule mkono nilioumia.
Akiwa anashangaa kwa nini nimemsukuma, macho yake yalitua kwenye jeraha langu la mguuni, akawa ananitazama machoni.
“Umepatwa na nini?” aliniuliza lakini kabla sijamjibu chochote, simu yangu ilianza kuita. Haikuwa kawaida yangu kupigiwa simu kwa sababu hata namba yangu nadhani watu waliokuwa wanaifahamu, hata watatu hawakuzidi kwa sababu ndiyo kwanza nilikuwa nimeanza kutumia simu maishani mwangu.
Kutazama namba ya mtu aliyekuwa anapiga, nilishtuka kugundua kwamba ni mama, harakaharaka nikaipokea.
“Kennedy mwanangu!” alisema mama huku akilia, mapigo ya moyo yakanilipuka na kuanza kunienda mbio kuliko kawaida, nilisikia sauti za watu wengine pia wakilia na kuomboleza, nikajua tayari mambo yameharibika.
“Mama! Mamaaa! Kumetokea nini?”
“Baba yako...” alisema mama lakini alishindwa kumalizia, akawa analia kwa huzuni kisha simu ikakatwa.
Nilibaki nimesimama nikiwa ni kama siamini nilichokisikia, nilihisi mwili wote ukifa ganzi, hata sijui nini kilitokea lakini nilishtukia tu machozi yakinichuruzika kwa wingi.
“Kumetokea nini?” Kezia aliniuliza kwa upole huku akinisogelea, lakini safari hii akiwa makini ili asinitoneshe tena kama awali.
“Baba amefariki,” nilisema huku machozi yakiendelea kunibubujika, japokuwa mama hakumalizia kauli yake lakini nilishaelewa kilichotokea.
“Mungu wangu, maskini pole,” alisema Kezia kwa upole, nikabaki nimeganda palepale kama sanamu machozi yakiendelea kunitoka, Kezia alitamani kunikumbatia lakini akawa hata hajui anishike wapi, nililitambua hilo nikamkumbatia kwa mkono mmoja, ule ambao ulikuwa mzima.
“Kaa kwanza utulie, sawa baba,” aliniambia kwa upole huku akinifuta machozi, nilijilaza pale kitandani, nikawa naendelea kuliakwa uchungu. Nililia sana siku hiyo na kilichoniliza zaidi ni kwamba japokuwa baba alikuwa amefariki, nisingeweza kwenda msibani kwa wakati.
Hali ya kilichokuwa kinaendelea huko nje, sasa nilikuwa naijua mwenyewe bila hata kusimuliza, nilijua uwezekano wa kusafiri salama mpaka kijijini Msanga bila kuangukia kwenye mikono ya polisi ni mdogo sana, hasa baada ya lile tukio lililotokea asubuhi hiyo.
Habari zilisambaa haraka, nadhani ndugu zangu walimpigia pia simu Bonta maana siku ile tulipoenda naye nyumbani niliwaona wakibadilishana namba za simu, muda mfupi naye akaja chumbani kwangu na kunikuta nikiwa na Kezia, nikiw ana majonzi makubwa.
“Hebu njoo kwanza pembeni tuzungumze,” Bonta alisema, tukatoka nje na kumuacha Kezia ndani.
“Umepata habari za kilichotokea nyumbani?” Bonta aliniuliza, nikatingisha kichwa kumkubalia huku machozi yakiendelea kububujika kwa wingi.
“Pole sana, hebu kwanza niambie kilichotokea asubuhi.”
Kwa jinsi nilivyokuwa namuamini, nilimsimulia Bonta kila kitu kilichotokea, akawa anatingisha tu kichwa kwa masikitiko.
“Siku nyingine nikikwambia jambo naomba uwe unanisikiliza, wewe ni kama mdogo wangu na kukulinda ni jukumu langu, unafikiri ukipatwa na matatizo kizembe itakuwaje?” Bonta alisema.
“Nisaidie niende msibani kwa baba, nakuomba kaka,” nilimwambia Bonta huku nikiwa naendelea kulia, akashusha pumzi ndefu na kuinua uso wake juu, akiwa ni kama anatafakari juu ya nini cha kufanya, nadhani alikuwa anaujua ugumu uliopo mbele yetu.
“Ngoja niwasiliane na bosi kwanza, nenda ndani kapumzike na usifanye chochote mpaka nitakapokwambia,” alisema Bonta kwa msisitizo na kuirudia kauli hiyo zaidi ya mara tatu, nadhani sasa alishakosa imani na mimi akahisi naweza tena kurudia makosa niliyoyafanya asubuhi.
Kabla hajaondoka, aliingia ndani na kumwambia Kezia anisaidie kuninyoosha mkono na kulitibu jeraha la mguuni, akamuitikia kwa heshima kisha akanielekeza kukaa kitandani.
“Jikaze baba, mimi niko na wewe katika kila unachopitia,” alisema Kezia huku akinibusu kwenye paji la uso, sijui aliushika vipi ule mkono wangu ulioteguka, nilishtukia tu ameunyonga kwa nguvu, nikasikia umelia ‘nkaa’ kwenye kiwiko. Nilishindwa kujizuia na kupiga yowe la nguvu kutokana na maumivu niliyoyasikia lakini cha ajabu, haukupita muda maumivu yakaanza kupungua.
“Umesharudi sehemu yake huo, maumivu yataisha tu,” alisema Kezia kwa upole, japokuwa alikuwa mrembo na sistaduu, Kezia alikuwa na roho ngumu sana, hata hivyo namshukuru alinisaidia kwani kweli mkono ulirudi kwenye hali yake, japo bado ulikuwa na maumivu.
Dakika kadhaa baadaye Bonta alirudi na kuniambia kwamba ameshawasiliana na bosi kwa hiyo nijiandae, nikapigwa na mshangao huku nikimtazama Bonta usoni.
“Jiandae, unashangaa nini?”
Je, nini kitafuatia?
 
SEHEMU YA 34





ILIPOISHIA:
Dakika kadhaa baadaye Bonta alirudi na kuniambia kwamba ameshawasiliana na bosi kwa hiyo nijiandae, nikapigwa na mshangao huku nikimtazama Bonta usoni.
“Jiandae, unashangaa nini?”
SASA ENDELEA...
“Sihitaji kujiandaa, nipo tayari!” nilisema kwa kujiamini huku macho yakiwa yamebadilika rangi na kuwa mekundu sana kwa sababu ya huzuni niliyokuwa nayo.
“Unatakiwa kuvaa kikawaida ili mtu yeyote asikushtukie, kama inawezekana inabidi utoke kisharobaro!”
“Tutapita wapi?”
“Wewe hilo halikuhusu, utaona mbele ya safari,” alisema Bonta, nikashusha pumzi ndefu na kujiinamia, nilikuwa nikijitahidi sana kupoteza mawazo machungu yaliyokuwa ndani ya kichwa changu kuhusu kifo cha baba lakini sikuweza kupambana na hisia za ndani! Ukweli ambao siwezi kuuficha ni kwamba nilikuwa nimeumia sana ndani ya moyo wangu.
Tulivutavuta muda huku Kezia akiendelea kunigangaganga na kunibembeleza mpaka kigiza kilipoanza kuingia. Bonta alinifuata na kuniambia muda wa kuondoka umefika kwa hiyo nijiandae.
Niliongeza kiwango cha fedha zaidi ya kile nilichokuwa nimekipanga awali kwa sababu sasa kulikuwa na jukumu kubwa la kugharamia mazishi kule nyumbani na nilikuwa najua kwamba mimi ndiye tegemeo kwa hiyo lazima nijiandae kwa namna yoyote kuubeba mzigo huo.
Baada ya kumaliza kujiandaa, safari hii nikiwa nimevaa mavazi ya kawaida kabisa kama Bonta alivyonielekeza, tulitoka mpaka kule kwenye ‘parking’, Bonta akawasha pikipiki kubwa ambayo ilikuwa ikifanana kidogo na ile nyingine ambayo huwa anaitumia siku zote.
Alivaa kofia ngumu kichwani, akanipa na mimi, nikavaa na muda mfupi baadaye, tuliianza safari ya kutoka huku nikiwa nimeushikilia vizuri mfuko uliokuwa na fedha. Kezia alikuwa akitusindikiza kwa macho huku akionesha kuguswa sana na hali niliyokuwa nayo.
Ujue mtu anapokupenda kwa dhati kutoka ndani ya moyo wake, unapofurahi naye atafurahi tu, hata kama hakuna kinachomfurahisha kwa wakati huo na inapotokea ukawa na huzuni, lazima na yeye ahuzunike.
Hicho ndicho kilichokuwa kinatokea kwa Kezia na ndiyo maana nimewahi kueleza kwamba nilishagundua kwamba licha ya ‘ugumu’ wake na mambo yake ya ‘kisela’, Kezia alikuwa na mapenzi ya dhati kwangu.
Bahati mbaya mimi wala sikuwa namchukulia kwa uzito huo, pengine labda ni kwa sababu bado sikuwa najua mambo mengi kuhusu hisia za mapenzi. Basi tulitoka mpaka getini, wale walinzi waliokuja kunigongea asubuhi wakatazamana kisha wakanitazama na wakawa ni kama wananipa ‘signal’ kwamba nisiwe na wasiwasi hakuna mtu yeyote anayejua kuhusu kilichotokea alfajiri.
“Wanapenda sana rushwa hawa washenzi, najua lazima umewahonga ili wakufichie siri zako!” alisema Bonta, kauli ambayo ilinifanya nicheke. Bonta alikuwa na uwezo mkubwa sana wa kusoma alama za nyakati na mazingira yanayomzunguka, ingekuwa mtu mwingine yeyote asingeweza kugundua chochote kama pale getini kuna ishara tumepeana.
Basi tuliendelea na safari lakini tofauti na nilivyotegemea kwamba tutaelekea ule upande wa Kibaha Mjini, ambao kimsingi huwa ni upande wa kulia ukitoka kambini, tulielekea upande wa kushoto ambao kimsingi sikuwa najua tunaenda kutokea wapi.
Kama kawaida yake, Bonta alianza kuendesha pikipiki kwa fujo, akawa anaichochea na kusababisha iwe inakimbia kwa kasi kubwa ingawa hii haikuwa na sauti kubwa kama ile anayoitumia akiwa jijini Dar es Salaam.
Tulipita kwenye mashamba mengi, tuakatiza kijiji kwa kijiji na mwisho, tukaenda kutokezea kwenye barabara ya lami inayotokea Msata. Kwa wanaoijua vizuri barabara hii, kuna mahali inaenda kuungana na ile barabara inayoelekea Arusha kutokea Chalinze kwa upande mmoja na upande wa pili, inaungana na Barabara ya Bagamoyo inayoenda mpaka jijini Dar es Salaam.
Sikuelewa ile ramani aliyoitumia Bonta mpaka tukafika kwenye barabara hiyo ambayo baadaye ilikuja kugeuka na kuwa njia muhimu sana kwetu (nitakuja kuielezea kwa kirefu siku nyingine), safari ikaendelea kwa kasi kubwa na kwa sababu sasa tulishakuwa tumeingia kwenye barabara ya lami, Bonta alikuwa huru kucheza na pikipiki yake kwa kadiri mwenyewe alivyokuwa anataka.
Alikuwa akiyapita magari ya abiria, yale yanayotoka Makumbusho au Mwenge jijini Dar es Salaam mpaka Bagamoyo kama yamesimama vile.
Kuna wakati pia alikuwa akiyapita mabasi makubwa, yale yanayotokea mikoa ya Kaskazini kama Arusha na Tanga kuelekea Dar es Salaam, ambayo baadhi huwa yanapita kwenye barabara hiyo kukwepa foleni kwenye Barabara ya Morogoro.
Wapita njia, wanedesha bodaboda na wapiga debe na makondakta wakati mwingine wakawa wanashindwa kujizuia na kupiga ‘mbinja’ kwa nguvu, wakimshangilia jinsi Bonta alivyokuwa anacheza na ile pikipiki.
Basi haukupita muda mrefu, tukawa tumeshawasili Mwenge jijini Dar es Salaam, yaani hata mimi kuna wakati nilikuwa nahisi kwamba haiwezi kuwa kweli kwamba tumeshafika mjini, muda huo tayari ilikuwa ni kama saa mbili za usiku.
Hatukusimama sehemu yoyote, tukakata kona na kuingia Barabara ya Sam Nujoma na sasa tukawa tunaelekea Ubungo. Bonta aliendelea na mbwembwe zake, tulipofika karibu na Daraja la Ubungo, niligundua kwamba kuna pikipiki mbili ambazo zinafahamika zaidi kama ‘tigo’ zilikuwa zinatufuatilia.
Kwa ambao hawajui ‘tigo’ ni nini, ni wale askari wanaokuwa kwenye pikipiki na kawaida huwa wanapakizana wawiliwawili wakiwa wamevaa unifomu na wakiwa pia na bunduki. Kazi yao kubwa huwa sijui ni ipi lakini mara kwa mara huwa nawaona wakisumbuana na madereva wa bodaboda.
“Kuna askari wanatufuatilia nyuma, wapo kwenye pikipiki mbili,” nilimwambia Bonta, nikamuona akitazama vizuri ‘side mirrors’, kwa sababu tayari ilikuwa usiku, nadhani hakuweza kuwaona vizuri.
“Wako wangapi?”
“Wanne!”
“Achana nao, hawawezi kutuzidi nguvu,” alisema huku akijaribu kuongeza mwendo lakini alikwama kutokana na taa za barabarani za Ubungo kuzuia magari yaliyokuwa yakitokea upande wetu.
Akiwa bado anatafuta upenyo wa kusogea mbele, tulishtukia pikipiki moja kati ya zile mbili, ikipita kwa kasi pembeni yetu, yaani dereva ni kama alikusudia kutaka kutusababishia ajali kwani kama Bonta asingetumia akili, ilikuwa tuvaane nao kiubavu-ubavu, dereva akasimamisha mbele kwa staili ya kutu-block, kisha yule mmoja aliyekuwa amepakizwa nyuma, akateremka na kutusogelea.
“Kwa nini unaendesha hovyo barabarani? Leseni yako iko wapi?” alisema yule askari huku akiwa amemsogelea Bonta. Ongea yake ilikuwa ya kisharishari na ilishaonesha ni kama amedhamiria kufanya kitu fulani.
Bonta aliingiza mkono mfukoni na kutoa leseni, yule askari akaiangalia kwa sekunde kadhaa akitumia tochi aliyokuwa ameishika kumulika, kisha akawa anamtazama Bonta usoni na eti alipoona hamuoni vizuri aliamua kummulika na tochi, kisha akawa anaifananisha sura yakena ile iliyokuwa kwenye leseni.
“Afande ee! Tuheshimiane basi, kwa nini unanimulika usoni? Wewe ukimulikwa usoni utafurahi?” Bonta alikoroma kwa jazba, kiukweli hata mimi niliona kabisa kwamba katika mazingira yale, wale askari ndiyo waliokuja wakiwa tayari wamepania kufanya jambo fulani kwa sababu sikuwa nimeona kosa lolote tulilolifanya.
Kitendo cha Bonta kumpandishia yule askari, kilisababisha askari mwingine atoke kwa nyuma kwa spidi na kuja kumkwida Bonta kwa nyuma huku mkono mmoja akiwa ameshika bunduki. Kumbe ile pikipiki nyingine ilikuwa ‘imetu-block’ kwa nyuma na mmoja kati ya askari wake, ndiyo yule aliyekuwa amemkwida Bonta.
“Shuka! Shuka!” alisema yule askari aliyetokea kwa nyuma, akanisukuma mimi kisha wakawa wanaendelea kushindana na Bonta.
Nadhani wao kwa kunitazama, waliona kama mimi sina madhara yoyote kwa hiyo nguvu zao zote walizielekeza kwa Bonta ambapo sasa hata wale wengine wawili waliokuwa kwenye pikipiki, walikuwa wameteremka, wakawa wanaendelea kumvutavuta Bonta.
“Usinikunje! We vipi wewe? Au mnamchukulia kila mtu boya,” alisema Bonta kwa sauti iliyoonesha kutokuwa na masihara hata kidogo, mimi nikawa natetemeka kwelikweli maana nilijua chochote kinaweza kutokea wakati wowote na nilikuwa nimesimama pembeni nikishuhudia kila kilichokuwa kinaendelea.
Wakati purukushani hiyo ikiendelea, mara taa za barabarani ziliruhusu magari yaanze kwenda, ukizingatia kwamba pikipiki yetu ilikuwa barabarani na zile za wale askari zilikuwa barabarani, madereva walianza kupiga honi kwa nguvu, kila mmoja akitaka apishwe ili awahi kuvuka kwenye taa, wengine walipoona kwamba ni askari wakawa wanatulia wenyewe huku wengine wakichungulia kutaka kuona ni kitu gani kinaendelea.
“Unajibu jeuri, unajibu jeuri si ndiyo?” alisema askari mwingine huku akimvuta Bonta kwenye helmet aliyokuwa amevaa, akaichomoa kwa nguvu kisha akamgonga Bonta na kitako cha bunduki kichwani.
Kitendo kile kiliniumiza sana moyo wangu, nilichogundua ni kwamba askari wengi wana kasumba ya kupenda kuwaonea raia pasipokuwa na sababu ya msingi. Kwa mwonekano wetu jinsi tulivyokuwa tumevaa, hasa Bonta, walihisi tunaweza kuwa ni masharobaro wa mjini tu ambao hatuna mbele wala nyuma, kwa hiyo wakataka kutumia nafasi zao kutunyanyasa.
Kitu ambacho walikuwa hawakijui ni kwamba jioni hiyo walikuwa wakicheza na watu hatari kwelikweli! Watu ambao kwanza tulikuwa tukitafutwa na jeshi la polisi kutokana na matukio makubwa ya kutisha tuliyoyasababisha.
Nikisema watu hatari namaanisha kweli hatari kwa sababu nilikuwa namfahamu vizuri Bonta, hakuwa mtu ambaye anakubali kuchezewa kirahisi, na alikuwa akiwachukia sana askari.
“Kosa langu nini mpaka unanipiga!” alisema Bonta kwa sauti ya kibabe huku safari hii akishuka kwenye pikipiki na kumsogelea mwilini yule askari aliyekuwa amempiga na kitako cha bunduki kichwani.
Nilikuwa najua kwamba pale alipo, Bonta alikuwa na bastola ambayo kwa jinsi alivyokuwa ameichomeka, isingekuwa rahisi kwa wale askari kuiona labda mpaka waamue kumsachi, lakini mimi pia nilikuwa na bastola ya Kezia, mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kwelikweli kwa sababu tayari harufu ya damu ilishaanza kusikika.
“Unanipiga na kitako cha bunduki kwa sababu ya nini? Mmetaka leseni si nimewapa? Kwa nini mnapenda kuwaonea raia wasiokuwa na hatia,” alisema Bonta huku sauti yake ikizidi kuongezeka na kuonesha kwamba alikuwa anakaribia kufanya tukio, huwa naijua sauti yake akikasirika inavyokuwa.
Katika hali ambayo ilimshangaza kila mmoja aliyekuwa anashuhudia tukio hilo, Bonta alimkunja yule askari aliyekuwa amempiga na kitako cha bunduki kichwani, sijawahi kuona mtu anayeweza kuwa na ujasiri wa kumkwida mtu aliyeshika bunduki mkononi, nadhani ujasiri huo uliwatisha hata wale askari wenyewe, purukushani kubwa ikatokea.
Je, nini kitafuatia?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom