Riwaya: Saa za Giza Totoro

Riwaya: Saa za Giza Totoro

SEHEMUB YA 22


ILIPOISHIA:
Tukiwa tunalikimbilia kwa tahadhari kubwa huku tukifyatua ovyo risasi, tulishtukia magari mengine mawili ya polisi yakiingia kwa kasi ya kimbunga, askari wengi wakaruka kabla hata hayajasimama na kuanza kutufyatulia risasi kama mvua.
SASA ENDELEA...
Kilichotokea siku hiyo, kilikuja kubadilisha kabisa maisha yangu na naweza kusema kwamba hata ile roho ya ukatili na unyama niliyokuja kuwa nayo, ilisababishwa kwa kiasi kikubwa na kitu kilichotokea siku hiyo.
Hali ilichafuka, risasi zikawa zinamiminwa kama mvua, zote zikielekezwa kwetu. Kumbuka mpaka wakati huo, kundi la kwanza ambalo ndiyo lenye watu wazoefu, akiwemo Bonta, Jombi na wengine, lilishaondoka na tuliobakia, naweza kusema wote tulikuwa wanafunzi.
Tulijaribu kupambana, ikawa na sisi tunafyatua risasi kwa kasi lakini kwa sababu wale askari walikuwa wengi na walikuwa na mafunzo kuliko sisi, walituelemea. Nilijitahidi kadiri ya uwezo wangu kutumia mafunzo yote tuliyopewa na Mamba, ikiwemo staili ya kukimbia kwa kubingirika huku nikiendelea kufyatua risasi.
Pale chini palikuwa pamepigwa ‘pavings’,vile vigae vidogo vinavyowekwa kwenye barabara za nje kwa hiyo kujirusha hakukuwa jambo jepesi lakini ilikuwa ni bora kuvumilia maumivu ya kujirusha kuliko kupigwa risasi.
Sijisifii lakini naweza kusema kwamba kati ya wale tuliobaki, mimi ndiyo nilikuwa shapu kidogo na nilikuwa najua kinachotakiwa kufanyika ni nini.
Mamba aliwahi kutufundisha kule porini kwamba inapotokea mnashambulia, mnatakiwa kusonga mbele lakini mkiwa mnashambuliwa, mnatakiwa kurudi nyuma kwa kasi na alikuwa anatumia zaidi neno la Kiingereza la ‘retreat’, yaani kurudi nyuma kwa lengo la kukimbia au kujipanga upya.
Mimi nilishaona kwamba hali imechafuka na badala ya sisi kuwa washambuliaji, sasa tulikuwa tukishambuliwa, kwa hiyo nikaitumia vizuri ile dhana ya ‘retreat’ lakini wenzangu walionesha kwamba hawajaiva.
Nasema hivyo kwa sababu yule mmoja tuliyekuwa naye kwenye lile gari lililotuacha, yeye alikuwa akikimbia kwa staili ya kuwapa mgongo wale askari, yaani akili zake zilikuwa ni kuwahi kufika kwenye gari tu bila kujua hatari iliyopo.
Wala hakukumbuka hata kutumia ile mbinu niliyokuwa naitumia mimi, ya kujirusha kama unapiga ‘samasoti’, ukitua chini unageuka na kushambulia kisha unaruka tena! Yeye alikuwa anakimbia mzimamzima bila kujua kwamba kitendo cha kugeuka na kuwapa mgongo watu wenye silaha, kinatosha kumaliza kazi kwa sababu watakulenga bila kizuizi chochote.
Nikiwa namshuhudia kwa macho yangu, alishonwa risasi kibao mgongoni, akapiga yowe moja tu, akadondoka kama mzigo huku damu zikianza kuvuja mithili ya bomba lililopasuka. Sijawahi kushuhudia mtu akikata roho kwa kupigwa risasi, hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza.
Moyo wangu ulikufa ganzi, nikajua anayefuatia ni mimi na kamwe hakuna atakayeweza kutoka salama!
Nilimtazama pale chini alipodondoka, nikaingiwa na ujasiri wa ajabu, niliinuka na kuikamata vizuri bunduki, nikaanza kufyatua risasi kwa staili ambayo Mamba alituambia kwamba inaitwa ‘sweeping’, yaani unafagia kutoka kushoto kwenda kulia kisha unarudi tena kushoto.
Kitendo kile kilisaidia kuwapunguza kasi wale askari kwani niliona wengine wakianguka na wengine wakijirusha kukwepa risasi, nikatumia mwanya huo kujirusha mpaka kwenye gari.
Japokuwa mimi ndiye niliyekuwa mbali, niliwatangulia wale wenzangu kuingia kwenye gari, dereva naye alishakanyaga mafuta na gari likawa linatoa moshi, yule mwingine alifanikiwa kupanda lakini mwenzake alipojaribu kuingia kwenye gari, naye alishonwa risasi kibao za mgongoni, akadondoka kama mzigo huku damu zikivuja mithili ya bomba.
Dereva aliondoa gari kwa kasi kubwa, tukajua tumesalimika! Kufumba na kufumbua tukashtukia vioo vya lile gari vikimwagika kuonesha kwamba wale askari bado walikuwa wakiendelea kutufyatulia risasi.
Akili ya haraka ilinituka kulala chini kabisa ya siti, tukamuachia derava afanye kazi yake ambapo alikuwa akiendesha gari kama kichaa, honi kali, breki za ghafla, kona za ajabuajabu na kelele za watu waliokuwa wakikoswakoswa na gari letu zilishereheshwa na milio ya risasi zilizokuwa zikiendelea kufyatuliwa kuelekezwa kwenye lile gari.
Nilijikausha pale chini huku nikishikilia vyuma vinavyoziunganisha siti za gari na ‘chasis’, dereva akaendelea kufanya yake na kiukweli nikiri kwamba maisha yetu kwa wakati huo, yalikuwa yakimtegemea yeye.
Hata sijui alifanikiwa vipi kuwaacha wale askari ambao nao walipoona tumekimbia, waliingia kwenye magari na kuanza kulifukuzia gari letu huku wakifyatua risasi kama mvua.
Dakika kadhaa baadaye, gari likiwa linakwenda kwa mwendo ambao huwezi kuuelezea kwa urahisi, milio ya risasi iliacha kusikika, nikajikaza kiume na kuinua kichwa changu kutazama kule nyuma, sikuweza kuona chochote kutokana na jinsi gari lilivyokuwa linatimua vumbi, nilichoamini ni kwamba tayari tumeshawaacha wale askari.
Bado moyo wangu ulikuwa ukienda mbio kuliko kawaida, kitendo cha kushuhudia wenzetu wawili wakipigwa risasi mbele ya macho yetu, kilinifanya niwe ni kama nimechanganyikiwa.
Niliikamata vizuri bunduki yangu, nikachomoa ‘magazine’ ambayo ilikuwa imeshaisha risasi, nikachukua nyingine kwenye koti langu na kuipachika, nikaikoki bunduki huku nikitetemeka kuliko kawaida. Niliielekezea kule nyuma kwa ajili ya kujihami, huku moyo wangu ukipiga kwa nguvu na kusababisha mwili wote ulowe kwa jasho.
Kioo cha nyuma na vile vya pembeni vilikuwa vimevunjwavunjwa kwa risasi na kama unavyojua, kioo cha gari kikikutana na kishindo cha kutosha, hakiishii tu kutoboka bali kinamwagika chote! Ndivyo ilivyotokea.
Kwa muda wote huo, sikuwa nimemtazama yule mwenzangu mmoja tuliyefanikiwa kuingia naye kwenye gari, kwa sababu nilimuona akiingia akiwa mzima, niliamini amejibanza chini ya siti kama nilivyokuwa nimefanya mimi lakini nilipogeuka na kumtazama, nilishtuka kupita kawaida.
Macho yake alikuwa ameyakodoa mpaka mwisho, tena yakitazama upande wa juu! Damu nyingi zilikuwa zimetapakaa pale alipolala, ni hapo ndipo nilipogundua kwamba kumbe naye alikuwa amepigwa risasi.
Niliiinama haraka na kujaribu kumtingisha, lakini hakutisikika! Nilijaribu kusikiliza mapigo ya moyo wake, nikagundua kwamba hayakuwa yakipiga. Ulikuwa ni mshtuko mkubwa mno kwangu, kwa tafsiri nyepesi, katika lile kundi la watu wanne kutoka kikosi B, ni mimi peke yangu ambaye nilikuwa hai mpaka muda huo na hata sikuwa na uhakika kama nitafika kambini nikiwa hai.
Nilishindwa kujizuia, machozi yakawa yananitoka huku nikiwa bado siamini, kila kitu kilitokea kwa kasi kubwa sana kiasi kwamba kuna wakati nilikuwa najihisi kama nipo kwenye ndoto. Hata sikuelewa dereva amepita njia gani, akili zilipokuja kunikaa sawa, nilishtukia tukiwa getini, walinzi wakafungua geti haraka na gari likaingizwa ndani kwa kasi kubwa.
Halikupaki pale ninapofahamu kwamba magari huwa yanapaki, nilishangaa geti jingine likifunguka kutokea chini ya ardhi na kutengeneza kama ngazi fulani ya kuingilia chini, gari likaingia kisha lile geti likafungwa.
Harakaharaka niliruka kupitia vioo vilivyovunjwa, nikasimama huku nikitetemeka kuliko kawaida, bunduki ikiwa mkononi. Dereva naye aliteremka na kunifuata, naye akionesha kuchanganyikiwa sana.
“Safi sana braza!” aliniambia huku akinikumbatia na kunipigapiga mgongoni!”
“Wenzetu wote wamekufa!”
“Vitani hatuhesabu waliokufa! Tunahesabu tuliorudi salama,” alisema huku na yeye akitetemeka! Sekunde chache baadaye, tulikuwa tumezungukwa na akina Bonta, Jombi na wenzake.
“Mmerudi wangapi?” aliuliza Jombi huku akisogea kibabe, mdomoni akitoa moshi mwingi wa kile kilichoonekana kuwa ni bangi kutokana na harufu yake! Hakuna aliyemjibu. Macho yangu yalicheza kwa haraka, nikamuona Bonta na wale wengine tuliokuwa nao eneo la tukio wakiwa wameshawasili.
Walikuwepo wengine kadhaa ambao nikiri kwamba sijawahi kuwaona, Jombi akazidi kutusogelea, akasimama jirani na yule dereva tuliyekuja naye, akamkumbatia huku akimpigapiga mgongoni.
“Kazi nzuri sana! Safi sana,” alisema kisha akanifuata na mimi.
“Umewezaje kurudi salama! Umenishangaza sana,” alisema huku akinikumbatia kwa nguvu, akaninyanyua juujuu na kupiga kelele kwa nguvu!
“Mmemuona mwanaume mwenzetu?” alisema huku akiwa bado ameninyanyua, akicheka kicheko ambacho hata sijui nikiiteje! Wenzake wote wakawa wanapiga makofi. Bado machozi yalikuwa yananitoka, akanishusha na kunikumbatia tena!
Wenzake nao walisogea, kila mmoja akawa ananipongeza kwa kazi nzuri na wa mwisho alikuwa ni Bonta ambaye yeye hakusema maneno mengi zaidi ya kunipa mkono kisha akatoa ishara kama ananipigia saluti.
“Sikukosea kukuchagua,” alisema kisha akageuka na kunipa mgongo, akarudi kule kwa wenzake, harakaharaka niliwaona wanaume wengine wawili ambao sikuwahi kuwaona kabla, wakaja pale kwenye gari wakiwa na machela, wakautoa mwili wa yule mwenzetu na kutoka naye.
Hata sijui walielekea wapi lakini nadhani walimpeleka kwenye vyumba vingine kulekule chini. Kitu ambacho nilikuwa sikijui, kumbe kwenye ile kambi kulikuwa na sehemu nyingine ya chini ya ardhi ambako nako kulikuwa na watu kibao kama kule juu, nikabaki nimepigwa na butwaa.
Bado nilikuwa siamini kama hatimaye nipo salama, nikawa hata sijui nijipongeze au niendelee kulia. Bonta alinipa ishara kwamba nimfuate, basi lile kundi lote likawa linaelekea upande wa pili kulikokuwa na lile gari jingine ambalo nalo lilikwenda eneo la tukio.
Lile sanduku tuliloliiba kule benki, lilikuwa limeshateremshwa, wanaume wenye nguvu wakawa wanasaidiana kulibeba na tulitokezea kwenye chumba kilichokuwa kama karakana fulani hivi. Bosi Mute alikuwa amekaa juu ya meza, naye akivuta sigara na kutoa moshi mwingi.
Alipotuona tukiingia tu, alisimama na kuanza kupiga makofi, basi tuligawanyika makundi mawili, wale ambao sijawahi kuwaona walikaa upande wao na sisi tuliokuwa eneo la tukio tulisimama upande wetu, Bosi Mute akatusogelea na kuanza kutukumbatia, mmoja baada ya mwingine.
“Chalii umerudi salama! Aisee,” alisema huku akinikumbatia na kama ilivyokuwa kwa Jombi, naye aliniinua juujuu kwa furaha, akanipongeza sana. Nilijiuliza maswali mengi sana kwamba kauli zao zilikuwa zinamaanisha nini.
Kwa lugha nyepesi, hakuna aliyetegemea kwamba nitarudi salama, kwa hiyo walitutoa wakijua kwamba wote kutoka Kikosi B tunaenda kufa? Nilishindwa kupata majibu. Harakaharaka lile sanduku lilisogezwa kwenye mashine kama za kukatia vyuma, wanaume wanne wakawa wanasaidiana kuliweka vizuri kisha mashine ikawashwa, likaanza kukatwa pale kwenye kitasa.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 23




ILIPOISHIA:
Kwa lugha nyepesi, hakuna aliyetegemea kwamba nitarudi salama, kwa hiyo walitutoa wakijua kwamba wote kutoka Kikosi B tunaenda kufa? Nilishindwa kupata majibu. Harakaharaka lile sanduku lilisogezwa kwenye mashine kama za kukatia vyuma, wanaume wanne wakawa wanasaidiana kuliweka vizuri kisha mashine ikawashwa, likaanza kukatwa pale kwenye kitasa.
SASA ENDELEA...
Baada ya dakika chache za kuhangaika na lile sanduku, hatimaye walifanikiwa kukata kitasa na kufungua mlango, ndani kulikuwa kumesheheni noti mpyampya, za shilingi elfu kumikumi na shilingi elfu tano.
Bosi Mute ndiye aliyekuwa wa kwanza kutia mkono, akatoka na kibunda kimoja kilichokuwa kimefungwa kwa staili ya tofauti kidogo, kama umewahi kwenda benki na kuona jinsi noti mpya zinavyofungwa na kutengeneza kama ‘kiboksi’ hivi, basi ndivyo hela hizo zilivyokuwa zimefungwa.
Alikifungua kile kiboksi na kurusha maburungutu hewani, watu wote wakawa wanashangilia kwa furaha.
“Mmefanya kazi nzuri sana!” alisema Bosi Mute huku akielekeza zile fedha zote zitolewe kwenye lile sanduku na kuwekwa mezani. Japokuwa sanduku kilikuwa dogo, kwa jinsi zile fedha zilivyokuwa zimepangwa, ilionesha zilikuwa nyingi kwelikweli kwani zilipowekwa pale mezani, zilitengeneza kama kamlima fulani.
“Nawaruhusu mkapumzike ila kila mmoja anatakiwa kuwa makini sana,” alisema Bosi Mute huku akimpa kila mmoja kibunda cha fedha. Alipofika kwangu, alinipa vibunda viwili kwa furaha na akaniambia nimemfurahisha sana.
Baada ya hapo, kila mmoja akiwa na fedha zake, tulitoka na kupanda mpaka kwenye kile chumba cha mikutano, tukabadilisha nguo na kukabidhi vifaa vyote tulivyoondoka navyo, tukatoka kila mmoja na njia yake.
Kiukweli bado nilikuwa na hofu kubwa mno ndani ya moyo wangu, kumbukumbu za tukio lililotokea zilikuwa zikiendelea kujirudia kwenye kichwa changu, ikafika mahali kichwa kikawa ni kama kinataka kuchanganyikiwa.
“Vipi mdogo wangu, hebu twende huku,” alisema Bonta baada ya kuniona nasuasua pale juu nikiwa hata sielewi nini cha kufanya.
“Piga msumari kwanza mambo mengine yote yatakaa freshi,” alisema huku akitoa msokoto wa bangi, akauwasha na kuvuta mafunda kadhaa, akanipa. Nilishindwa kukataa, kimsingi sikuwa nimewahi kuvuta bangi hata siku moja lakini kwa hali niliyokuwa nayo kwa wakati huo, niliona labda inaweza kunisaidia.
Nilivuta funda la kwanza, Bonta akawa ananitazama usoni, akanielekeza jinsi ya kumeza moshi. Nilipojaribu, moshi ulinipalia na kusababisha nikohoe sana, watu wote wakawa wanacheka kwa nguvu.
Nilipotulia, nilijaribu tena, nikavuta na kumeza kiasi kikubwa cha moshi, sikukohoa tena! Nikarudia tena na tena, nikaanza kuhisi kama kichwa chote kimekufa ganzi.
Bonta alikuwa akinisemesha lakini nilikuwa nikimsikia kwa mbali sana, ile hofu iliyokuwa imetanda kwenye kichwa changu ikayeyuka na nikaanza kujihisi kama raha fulani hivi ambayo ilinifanya nitamani kucheka.
Basi nilijiinamia palepale huku nikiwa natabasamu mwenyewe, Bonta akawa anacheka sana na kunipigapiga mgongoni.
“Shushia na hii,” alisema huku akichukua ule msokoto mkononi mwangu maana niliikuwa nimeushika tu ukiendelea kuisha, akanipa kichupa kilichokuwa na pombe kali, nikafungua kifuniko na kupiga funda moja.
Kila kitu kilibadilika, sikukumbuka tena chochote kilichotokea, nikawa najihisi nina raha kubwa sana ndani ya moyo wangu. Hata sijui tuliondokaje pale baadaye nilishtukia tu tukiwa ndani ya teksi na Bonta huku nikijihisi usingizi mzito sana.
Alinipeleka mpaka Sinza, akahakikisha naingia ndani na kufunga milango yote kisha akaniambia sitakiwi kutoka kwenda mbali biola kumpa taarifa. Kwa jinsi nilivyokuwa najisikia, nilienda kujitupa kwenye kochi, nikawasha redio na kufungulia sauti ya juu, usingizi mzito ukanipitia.
Nilipokuja kuzinduka, ilikuwa ni majira ya kama saa nne hivi za usiku, kichwa kilikuwa kinanigonga kwelikweli, nikaamka na kwenda kupunguza sauti ya redio, nikaingia bafuni kwenda kuoga kwani tangu nimerudi, sikupata hata muda wa kujimwagia maji.
Nilioga na kurudi kwenye friji, nikachukua chupa kubwa ya maji na kunywa kwa wingi maan animewahi kusikia kwamba maji ni dawa nzuri ya kichwa.
Baada ya kumaliza kunywa maji, nilianza kuhisi njaa kali sana, nikarudi chumbani na kubadilisha nguo, nikachukua noti mbili za shilingi elfu kumikumi na kabla sijatoka, nilichukua ile suruali niliyokuwa nimeivaa wakati natoka kazini, maburungutu yangu mawili ya noti mpyampya yalikuwepo.
Niliyatoa na kuyahifadhi chini ya godoro nilikokuwa nimeweka zile hela zangu nyingine, hata sikutaka kuhesabu kwa muda huo, nikavaa vizuri na kutoka kwa lengo la kwenda kununua chakula. Nilipakumbuka pale Cheers nilipopelekwa na Bonta, nikaamua kwenda kwa sababu nilikipenda chakula chake.
Nilipofika tu, wale wahudumu walinikumbuka, basi wakaja kunisalimu kwa bashasha huku wakikumbushia vituko vyango nilivyovifanya siku ile nikiwa nimelewa. Basi niliagiza chakula na kwa sababu ya kukwepa mazoea, sikutaka kukaa pale badala yake nikawaambia wanifungie.
“Najua umechoka sana, unaonaje leo ikienda kukuburudisha? Siku ile ulinikimbia lakini leo wala hujalewa! Nakupenda mwenzio,” alisema yule mhudumu ambaye nilikuwa nimekaa naye siku ile.
Kutokana na jinsi nilivyokuwa najisikia ndani ya moyo wangu, niliona kama nikiwa peke yangu naweza hata nisipate usingizi usiku kucha kutokana na hofu, sijui nilipata wapi ujasiri wa kumkubalia, nikamwambia tuondoke pamoja.
“Ngoja basi niage kwanza, kanisubiri kwenye Bajaj,” aliniambia huku akinikumbatia na kunibusu. Nilitoka na kwenda kwenye ile Bajaj niliyokuja nayo ambayo bado ilikuwa ikinisubiri. Dakika chache baadaye, yule msichana akiwa ameshabadilisha nguo za kazi, alikuja mbiombio mpaka pale.
Kidogo nimsahau kwa jinsi alivyokuwa amebadilika, kigauni kifupi alichokuwa amevaa, kilimfanya aonekane mrembo kwelikweli, basi akaingia kwenye Bajaj na kunibusu.
“Yaani huwezi kujua furaha niliyonayo ndani ya moyo wangu,” aliniambia huku akisaidia kubeba chakula, tukaondoka na Bajaj mpaka pale nilipokuwa naishi. Moyoni nilikuwa bado sijui nini kitaenda kutokea kule ndani kwa sababu kama nilivyowahi kueleza, pamoja na ujanja wangu wote sikuwa namjua mwanamke.
Basi tulipofika, nilimlipa dereva Bajaj fedha zake, kisha nikafungua mlango na kumkaribisha mgeni wangu.
“Unaishi na nani kwani?”
“Naishi na wazazi wangu sema wamesafiri kwa hiyo niko peke yangu,” nilimwambia, akawa anashangaa huku na kule. Aliniambia kwamba naishi maisha mazuri sana, nikawa namkwepesha kwenye hoja yake kwa kumwambia kwamba sifa hizo wanatakiwa kupewa wazazi wangu.
“Mh! Mbona humu ndani hakuna dalili kama unaishi na wazazi wako?” aliniuliza wakati akinisaidia kuandaa chakula, nikawa naendelea kumzuga. Sijui kwa nini sikutaka ajue kama naishi peke yangu!
Basi aliniandalia kila kitu kwa uchangamfu kisha tukakaa na kuanza kula. Yeye hakuwa akila bali alikuwa akiniandalia kila kitu, alinitolea mifupa kwenye nyama na wakati mwingine akawa ananilisha.
“Ujue mimi nakupenda sana, tangu siku ile nimekuona nimejikuta tu nikikupenda.”
‘Tangu lini muuza baa akampenda mwanaume?” nilimuuliza swali ambalo lilionesha kumuumiza sana moyo wake.
“Sijapenda kuwa muuza baa, ni maisha tu ndiyo yamefanya nikawa hivi. Nilikuwa na ndito nyingi maishani mwangu lakini zote zimeyeyuka!” alisema kwa huzuni huku machozi yakianza kumlengalenga.
Nilijilaumu kwa kauli yangu ile kwa sababu siku zote nilikuwa naamini kwamba wauza baa wote, ni wanawake ambao hawajatulia, hawawezi kuwa na uhusiano na mwanaume mmoja na kwao pesa ndiyo kila kitu.
“Kwa hiyo unafikiria na mimi labda huwa najiuza au kwako nimefuata pesa, kwa nini lakini unanifikiria hivyo,” aliniambia baada ya kumaliza kuondoa vyombo nilivyolia, nikamjibu kwa kifupi kwamba naomba anisamehe kama nimemhisi vibaya.
“Vyovyote utakavyonielewa, kama utaniona mimi ni malaya sijatulia, sawa! Ila nataka tu ujue kwamba nakupenda sana,” alisema huku akifanya kitendo ambacho sikutegemea kama atakifanya. Aliinama kidogo, akavua kufuli lake na kulitupa pembeni, akanisogelea pale kwenye kochi nilipokuwa nimejilaza kichovu. Hata sikupata muda wa kutafakari, akanivamia mwilini na kugusanisha ndimi zetu, kwa mara ya kwanza nikapata msisimko ambao sijawahi kuupata.
Sijui alitumia ujanja gani, nilishtukia tu mkono wake mmoja ukiwa umeshapenya na kuingia kwenye himaya ya ‘mkuu wa kaya’ na kumkamata, nikapatwa na mshtuko usioelezeka, mapigo ya moyo yakawa yananienda mbio kuliko kawaida.
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom