SEHEMUB YA 22
ILIPOISHIA:
Tukiwa tunalikimbilia kwa tahadhari kubwa huku tukifyatua ovyo risasi, tulishtukia magari mengine mawili ya polisi yakiingia kwa kasi ya kimbunga, askari wengi wakaruka kabla hata hayajasimama na kuanza kutufyatulia risasi kama mvua.
SASA ENDELEA...
Kilichotokea siku hiyo, kilikuja kubadilisha kabisa maisha yangu na naweza kusema kwamba hata ile roho ya ukatili na unyama niliyokuja kuwa nayo, ilisababishwa kwa kiasi kikubwa na kitu kilichotokea siku hiyo.
Hali ilichafuka, risasi zikawa zinamiminwa kama mvua, zote zikielekezwa kwetu. Kumbuka mpaka wakati huo, kundi la kwanza ambalo ndiyo lenye watu wazoefu, akiwemo Bonta, Jombi na wengine, lilishaondoka na tuliobakia, naweza kusema wote tulikuwa wanafunzi.
Tulijaribu kupambana, ikawa na sisi tunafyatua risasi kwa kasi lakini kwa sababu wale askari walikuwa wengi na walikuwa na mafunzo kuliko sisi, walituelemea. Nilijitahidi kadiri ya uwezo wangu kutumia mafunzo yote tuliyopewa na Mamba, ikiwemo staili ya kukimbia kwa kubingirika huku nikiendelea kufyatua risasi.
Pale chini palikuwa pamepigwa ‘pavings’,vile vigae vidogo vinavyowekwa kwenye barabara za nje kwa hiyo kujirusha hakukuwa jambo jepesi lakini ilikuwa ni bora kuvumilia maumivu ya kujirusha kuliko kupigwa risasi.
Sijisifii lakini naweza kusema kwamba kati ya wale tuliobaki, mimi ndiyo nilikuwa shapu kidogo na nilikuwa najua kinachotakiwa kufanyika ni nini.
Mamba aliwahi kutufundisha kule porini kwamba inapotokea mnashambulia, mnatakiwa kusonga mbele lakini mkiwa mnashambuliwa, mnatakiwa kurudi nyuma kwa kasi na alikuwa anatumia zaidi neno la Kiingereza la ‘retreat’, yaani kurudi nyuma kwa lengo la kukimbia au kujipanga upya.
Mimi nilishaona kwamba hali imechafuka na badala ya sisi kuwa washambuliaji, sasa tulikuwa tukishambuliwa, kwa hiyo nikaitumia vizuri ile dhana ya ‘retreat’ lakini wenzangu walionesha kwamba hawajaiva.
Nasema hivyo kwa sababu yule mmoja tuliyekuwa naye kwenye lile gari lililotuacha, yeye alikuwa akikimbia kwa staili ya kuwapa mgongo wale askari, yaani akili zake zilikuwa ni kuwahi kufika kwenye gari tu bila kujua hatari iliyopo.
Wala hakukumbuka hata kutumia ile mbinu niliyokuwa naitumia mimi, ya kujirusha kama unapiga ‘samasoti’, ukitua chini unageuka na kushambulia kisha unaruka tena! Yeye alikuwa anakimbia mzimamzima bila kujua kwamba kitendo cha kugeuka na kuwapa mgongo watu wenye silaha, kinatosha kumaliza kazi kwa sababu watakulenga bila kizuizi chochote.
Nikiwa namshuhudia kwa macho yangu, alishonwa risasi kibao mgongoni, akapiga yowe moja tu, akadondoka kama mzigo huku damu zikianza kuvuja mithili ya bomba lililopasuka. Sijawahi kushuhudia mtu akikata roho kwa kupigwa risasi, hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza.
Moyo wangu ulikufa ganzi, nikajua anayefuatia ni mimi na kamwe hakuna atakayeweza kutoka salama!
Nilimtazama pale chini alipodondoka, nikaingiwa na ujasiri wa ajabu, niliinuka na kuikamata vizuri bunduki, nikaanza kufyatua risasi kwa staili ambayo Mamba alituambia kwamba inaitwa ‘sweeping’, yaani unafagia kutoka kushoto kwenda kulia kisha unarudi tena kushoto.
Kitendo kile kilisaidia kuwapunguza kasi wale askari kwani niliona wengine wakianguka na wengine wakijirusha kukwepa risasi, nikatumia mwanya huo kujirusha mpaka kwenye gari.
Japokuwa mimi ndiye niliyekuwa mbali, niliwatangulia wale wenzangu kuingia kwenye gari, dereva naye alishakanyaga mafuta na gari likawa linatoa moshi, yule mwingine alifanikiwa kupanda lakini mwenzake alipojaribu kuingia kwenye gari, naye alishonwa risasi kibao za mgongoni, akadondoka kama mzigo huku damu zikivuja mithili ya bomba.
Dereva aliondoa gari kwa kasi kubwa, tukajua tumesalimika! Kufumba na kufumbua tukashtukia vioo vya lile gari vikimwagika kuonesha kwamba wale askari bado walikuwa wakiendelea kutufyatulia risasi.
Akili ya haraka ilinituka kulala chini kabisa ya siti, tukamuachia derava afanye kazi yake ambapo alikuwa akiendesha gari kama kichaa, honi kali, breki za ghafla, kona za ajabuajabu na kelele za watu waliokuwa wakikoswakoswa na gari letu zilishereheshwa na milio ya risasi zilizokuwa zikiendelea kufyatuliwa kuelekezwa kwenye lile gari.
Nilijikausha pale chini huku nikishikilia vyuma vinavyoziunganisha siti za gari na ‘chasis’, dereva akaendelea kufanya yake na kiukweli nikiri kwamba maisha yetu kwa wakati huo, yalikuwa yakimtegemea yeye.
Hata sijui alifanikiwa vipi kuwaacha wale askari ambao nao walipoona tumekimbia, waliingia kwenye magari na kuanza kulifukuzia gari letu huku wakifyatua risasi kama mvua.
Dakika kadhaa baadaye, gari likiwa linakwenda kwa mwendo ambao huwezi kuuelezea kwa urahisi, milio ya risasi iliacha kusikika, nikajikaza kiume na kuinua kichwa changu kutazama kule nyuma, sikuweza kuona chochote kutokana na jinsi gari lilivyokuwa linatimua vumbi, nilichoamini ni kwamba tayari tumeshawaacha wale askari.
Bado moyo wangu ulikuwa ukienda mbio kuliko kawaida, kitendo cha kushuhudia wenzetu wawili wakipigwa risasi mbele ya macho yetu, kilinifanya niwe ni kama nimechanganyikiwa.
Niliikamata vizuri bunduki yangu, nikachomoa ‘magazine’ ambayo ilikuwa imeshaisha risasi, nikachukua nyingine kwenye koti langu na kuipachika, nikaikoki bunduki huku nikitetemeka kuliko kawaida. Niliielekezea kule nyuma kwa ajili ya kujihami, huku moyo wangu ukipiga kwa nguvu na kusababisha mwili wote ulowe kwa jasho.
Kioo cha nyuma na vile vya pembeni vilikuwa vimevunjwavunjwa kwa risasi na kama unavyojua, kioo cha gari kikikutana na kishindo cha kutosha, hakiishii tu kutoboka bali kinamwagika chote! Ndivyo ilivyotokea.
Kwa muda wote huo, sikuwa nimemtazama yule mwenzangu mmoja tuliyefanikiwa kuingia naye kwenye gari, kwa sababu nilimuona akiingia akiwa mzima, niliamini amejibanza chini ya siti kama nilivyokuwa nimefanya mimi lakini nilipogeuka na kumtazama, nilishtuka kupita kawaida.
Macho yake alikuwa ameyakodoa mpaka mwisho, tena yakitazama upande wa juu! Damu nyingi zilikuwa zimetapakaa pale alipolala, ni hapo ndipo nilipogundua kwamba kumbe naye alikuwa amepigwa risasi.
Niliiinama haraka na kujaribu kumtingisha, lakini hakutisikika! Nilijaribu kusikiliza mapigo ya moyo wake, nikagundua kwamba hayakuwa yakipiga. Ulikuwa ni mshtuko mkubwa mno kwangu, kwa tafsiri nyepesi, katika lile kundi la watu wanne kutoka kikosi B, ni mimi peke yangu ambaye nilikuwa hai mpaka muda huo na hata sikuwa na uhakika kama nitafika kambini nikiwa hai.
Nilishindwa kujizuia, machozi yakawa yananitoka huku nikiwa bado siamini, kila kitu kilitokea kwa kasi kubwa sana kiasi kwamba kuna wakati nilikuwa najihisi kama nipo kwenye ndoto. Hata sikuelewa dereva amepita njia gani, akili zilipokuja kunikaa sawa, nilishtukia tukiwa getini, walinzi wakafungua geti haraka na gari likaingizwa ndani kwa kasi kubwa.
Halikupaki pale ninapofahamu kwamba magari huwa yanapaki, nilishangaa geti jingine likifunguka kutokea chini ya ardhi na kutengeneza kama ngazi fulani ya kuingilia chini, gari likaingia kisha lile geti likafungwa.
Harakaharaka niliruka kupitia vioo vilivyovunjwa, nikasimama huku nikitetemeka kuliko kawaida, bunduki ikiwa mkononi. Dereva naye aliteremka na kunifuata, naye akionesha kuchanganyikiwa sana.
“Safi sana braza!” aliniambia huku akinikumbatia na kunipigapiga mgongoni!”
“Wenzetu wote wamekufa!”
“Vitani hatuhesabu waliokufa! Tunahesabu tuliorudi salama,” alisema huku na yeye akitetemeka! Sekunde chache baadaye, tulikuwa tumezungukwa na akina Bonta, Jombi na wenzake.
“Mmerudi wangapi?” aliuliza Jombi huku akisogea kibabe, mdomoni akitoa moshi mwingi wa kile kilichoonekana kuwa ni bangi kutokana na harufu yake! Hakuna aliyemjibu. Macho yangu yalicheza kwa haraka, nikamuona Bonta na wale wengine tuliokuwa nao eneo la tukio wakiwa wameshawasili.
Walikuwepo wengine kadhaa ambao nikiri kwamba sijawahi kuwaona, Jombi akazidi kutusogelea, akasimama jirani na yule dereva tuliyekuja naye, akamkumbatia huku akimpigapiga mgongoni.
“Kazi nzuri sana! Safi sana,” alisema kisha akanifuata na mimi.
“Umewezaje kurudi salama! Umenishangaza sana,” alisema huku akinikumbatia kwa nguvu, akaninyanyua juujuu na kupiga kelele kwa nguvu!
“Mmemuona mwanaume mwenzetu?” alisema huku akiwa bado ameninyanyua, akicheka kicheko ambacho hata sijui nikiiteje! Wenzake wote wakawa wanapiga makofi. Bado machozi yalikuwa yananitoka, akanishusha na kunikumbatia tena!
Wenzake nao walisogea, kila mmoja akawa ananipongeza kwa kazi nzuri na wa mwisho alikuwa ni Bonta ambaye yeye hakusema maneno mengi zaidi ya kunipa mkono kisha akatoa ishara kama ananipigia saluti.
“Sikukosea kukuchagua,” alisema kisha akageuka na kunipa mgongo, akarudi kule kwa wenzake, harakaharaka niliwaona wanaume wengine wawili ambao sikuwahi kuwaona kabla, wakaja pale kwenye gari wakiwa na machela, wakautoa mwili wa yule mwenzetu na kutoka naye.
Hata sijui walielekea wapi lakini nadhani walimpeleka kwenye vyumba vingine kulekule chini. Kitu ambacho nilikuwa sikijui, kumbe kwenye ile kambi kulikuwa na sehemu nyingine ya chini ya ardhi ambako nako kulikuwa na watu kibao kama kule juu, nikabaki nimepigwa na butwaa.
Bado nilikuwa siamini kama hatimaye nipo salama, nikawa hata sijui nijipongeze au niendelee kulia. Bonta alinipa ishara kwamba nimfuate, basi lile kundi lote likawa linaelekea upande wa pili kulikokuwa na lile gari jingine ambalo nalo lilikwenda eneo la tukio.
Lile sanduku tuliloliiba kule benki, lilikuwa limeshateremshwa, wanaume wenye nguvu wakawa wanasaidiana kulibeba na tulitokezea kwenye chumba kilichokuwa kama karakana fulani hivi. Bosi Mute alikuwa amekaa juu ya meza, naye akivuta sigara na kutoa moshi mwingi.
Alipotuona tukiingia tu, alisimama na kuanza kupiga makofi, basi tuligawanyika makundi mawili, wale ambao sijawahi kuwaona walikaa upande wao na sisi tuliokuwa eneo la tukio tulisimama upande wetu, Bosi Mute akatusogelea na kuanza kutukumbatia, mmoja baada ya mwingine.
“Chalii umerudi salama! Aisee,” alisema huku akinikumbatia na kama ilivyokuwa kwa Jombi, naye aliniinua juujuu kwa furaha, akanipongeza sana. Nilijiuliza maswali mengi sana kwamba kauli zao zilikuwa zinamaanisha nini.
Kwa lugha nyepesi, hakuna aliyetegemea kwamba nitarudi salama, kwa hiyo walitutoa wakijua kwamba wote kutoka Kikosi B tunaenda kufa? Nilishindwa kupata majibu. Harakaharaka lile sanduku lilisogezwa kwenye mashine kama za kukatia vyuma, wanaume wanne wakawa wanasaidiana kuliweka vizuri kisha mashine ikawashwa, likaanza kukatwa pale kwenye kitasa.
Sent using
Jamii Forums mobile app