RIWAYA; DUKA LA ROHO
SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA
"Safi sana. Nitawashukuru mkiwanyamazisha hawa washenzi."
"Shaka ondoa." Malocha akamaliza huku anafungia silaha zile kwenye begi kubwa lililokuja nazo.
Wakabeba silaha zile na kuzipakiza kwenye gari lao. Wakaondoka eneo lile kurudi nyumbani kwao kwa matumaini mapya.
Walipofika, wakawapa ujumbe wakundi wao, na kila mmoja alikuwa tayari kwa mapigano dhidi ya kundi la Gunner. Lisa akamchukua Martina aliyekuwa kalala na kumpandisha kwenye gari walilopanga kwenda nalo Arusha.
Kabla ya safari hiyo haijaanza, Martina akapitishwa kwa rafiki kipenzi wa Lisa aitwaye Salome Makala. Martina akaamshwa na kupewa maelekezo kadhaa ambayo hakuwa mbishi katika kuyakubali. Baada ya hapo, gari ikaingia barabarani kwenda Arusha.
****
Likiwa limebaki saa moja ili kauli ya Gunner kwenye ile video itimie kwenda kwa vyombo vya usalama. Askari na wanausalama wa aina zote walijipanga barabarani na mabango wakiandamana ili Masai atoke. Waliimba nyimbo za ukombozi huku wakiwa na silaha za moto mikononi mwao. Lengo la kufanya hivyo ni katika kufikisha ujumbe kwa wale wanaomficha Masai. Hakuna aliyekuwa tayari kuona jeshi lao linaendelea kuhangamia pasi na sababu ya msingi. Waliandamana huku wakishinikiza kuwa Masai asipoonekana, basi vita dhidi ya serikali itaanza mara moja.
Wakati hayo yanaendelea, nyuso za Gunner na Lobo ziliambatana na tabasamu zito kwani ni wazi vita yao ilianza kuzaa matunda. Wakiwa ndani ya gari lao mwanana, walitabasamu na kugonga tano kwa mchanganyo wanaoufanya Tanzania.
Upande mwingine wa shilingi, Malocha, Masai, Lisa, Mubah, na wataalam wa mitambo yao, walikuwa wapo ndani ya gari linalokimbia kwa kasi kwenda Arusha kuwahi muda wa Duka La Roho. Masai akiwa nyuma ya usukani, kavalia kaptula ya kombati na juu kaushi nyekundu, alikuwa kama mwehu aliyeanza kuwehuka zaidi kwa jinsi alivyokuwa analiendesha gari lililobeba roho za wenzake. Licha ya hayo yote, hakuna aliyebisha kwani roho ya vita iliwaingia katika viini vyao vya nafsi na kuwaza vita tu.
Saa mbili asubuhi, kundi la Masai lilikuwa limefunga breki mbele ya hotel moja kubwa iliyopo katika jiji la Arusha. Wanaume wakashuka na mabegi yao yenye silaha, kisha akafuata Lisa ambaye yeye alikuwa kabeba begi la kawaida la nguo.
Moja kwa moja wakaenda mapokezi na kutoa kibali ambacho Rais kawapa kwa ajili ya utambulisho wakifika sehemu ile. Hoteli hiyo inamilikiwa na Rais. Mwanamke aliyekuwa pale mapokezi, baada ya kuona kile kibali, haraka akapiga simu kwa tajiri wake na dakika mbili mbele, meneja wa hoteli ile alikuwa anaongea na Malocha jambo fulani.
"Twendeni wazee wa kazi." Malocha aliwaambia wenzake baada ya kumaliza kuongea na Meneja.
Moja kwa moja wakaongozwa hadi chumba kimoja ambacho mlangoni kiliandikwa 'Conference Room' yaani chumba cha mikutano. Meneja akaondoka ndani ya chumba kile baada ya kuwakabidhi wale watu, na kitendo bila kuchelewa, mabegi ya wale watu yakafunguliwa na kila mmoja akatoa kompyuta yake tayari kwa kuanza kazi ya kumsaka Gunner na washirika wake kwa kutumia kifaa alichokuja nacho Masai toka Italia.
Baada ya dakika kumi, kila mmoja akaanza kutoa mafanikio yake kwa kile alichokuwa anakitafuta.
"Nimepata namba zake alizowasiliana nusu saa iliyopita." Mtaalam wao aliitoa taarifa na kuzitaja namba hizo na Lisa akazinakiri mahala.
"Nimepata maongezi yao waliyoyaongea kwa nusu saa iliyopita." Mtaalamu mwingine alitoa taarifa na kucheza yale maongezi ambayo Gunner alikuwa anawasiliana na wenzake na kuwaelekeza cha kufanya. Masai akatikisa kichwa kukubali kazi ya vijana wake.
"Kuna namba nyingine zimeonekana kabla ya nusu saa ya maongezi ya Gunner. Ni namba ya nchi za mbali na sauti yake hii hapa." Lisa naye akatoa alolichokinasa kwenye kazi aliyopewa.
"Ni The Shadow huyo. Naona anafurahi sana wajinga wanachokifanya. Mshenzi mkubwa." Masai aliongea kwa hasira kuliko siku zote ambazo kawahi kuishi katika dunia hii.
"Na hapa mimi nimepata ramani ambayo walikuwepo nusu saa iliyopita. Yaonekana baada ya mawasiliano haya, wameelekea upande wa Kaskazini lakini sisi tukipita barabara nyingine, tutakutana nao mbele japo wametuwahi." Malocha alitoa taarifa.
"Upande wa Kaskazini kuna nini?" Masai akauliza.
"Hapa Kaka. Kuna kambi ya jeshi ambayo ndio ngome kuu ya Tanzania kwenye upande wa Silaha. Wakifanikiwa kuteka eneo hili, basi Tanzania tutakwisha. Silaha zote watakuwa nazo wao." Malocha alitoa maelezo ambayo yakamfanya Masai apumue pumzi ndefu iliyo na mashaka.
"Naona wamepania sana. Ngoja nijaribu kuwatafuta maana majibu yenu ndio mwongozo wangu." Masai baada ya kuongea hayo, akaanza kubonyeza kompyuta yake harakaharaka na kufanya mle ndani kulie kiparaza kile cha kompyuta.
"Masai. Kuna mawasiliano yanafanyika sasa hivi hapa. Namba ya Gunner na hii namba." Mubah aliongea hayo huku anamgeuzia kompyuta yake Masai.
"Angalia hiyo namba nyingine ni ya nani." Malocha alitoa wazo haraka na Masai akaingiza namba hizo kwenye mtandao wake wa kutafuta mahali inapotokea.
"Shit. Ni ya hotel hii. Wajinga wanataka kutuchoma." Masai aliongea huku macho yake kayakodoa kwa hamaki.
"Ni yule mbwa wa mapokezi ndio katoa taarifa." Mtaalamu mmoja aliongea na kucheza sauti ambayo ilisikika ikiongea na Gunner.
"Wamefanya vizuri sana ili kusimamisha zoezi la kwenda kambini. Tuna dakika kumi za kufanya mambo yetu. Wao baada ya nusu saa watakuwa hapa." Masai aliongea huku akiendelea kutafuta mahali ambapo ataweza kuwaona Gunner na kundi lake kwa kutumia Satellite Trace.
"Okay." Baada ya dakika tano, Masai akatoa sauti yake na wote wakatega sikio. "Kuna makundi matatu ya hawa wajinga. Kuna la wanawake ambalo hili linaendelea kusonga Kaskazini lakini kwa taratibu kwa lengo kuwangoja wakina Gunner, kuna lingine la watu watatu ambao nadhani ni wale wataalamu wao, hili naona lipo katikati ya jiji na karibu sana na AICC. Nadhani wanataka kufanya kitu pale. Na kundi la tatu, ni Lobo na Gunner, hawa wapo njiani wanakuja kwetu." Masai alitoa maelezo hayo lakini kabla hajaendelea, Lisa akaingilia maongezi hayo.
"Naona wanawasiliana na kundi lililo jijini. Wanasema wakutane hapa." Lisa akatoa taarifa.
"Safi wife." Masai akampongeza mchumba wake. Lisa akatabasamu tu.
"Wanadakika ngapi kufika hapa." Malocha akauliza na Masai akabonyeza vitufe fulani kwenye kompyuta yake. Kompyuta ikaonesha gari walilopanda wakina Gunner na umbali lilipo toka pale walipo. Kisha akabadili ule umbali ukawa katika muda. Hapo akapata majibu ya kumjibu Malocha.
"Dakika kumi na tano tu."
"Tufunge vitu tuondoke." Malocha akashauri na kila mmoja akaanza kupakia vitu vyake haraka, lakini Masai akawa anaendelea kubonyeza kiparaza cha kompyuta mpakato yake. Hadi wenzake wanaliza kufunga, na yeye ndio alikuwa anamaliza kazi yake.
Bila kuifunga kompyuta yake, akaiweka mezani na kutoka na wenzake ndani ya chumba kile cha mikutano.
"Kwa nini umeacha mashine." Mubah akamuuliza Masai.
"Kuna meseji ya Gunner na Lobo, wanatakiwa waipate." Masai akajibu huku wakizishuka ngazi baadhi zilizopo katika hoteli ile.
"Huyo dada wa mapokezi msiongee naye chochote. Tupite tu." Malocha akatoa ushauri baada ya kuanza kukaribia mapokezi.
"Heee! Mnaondoka? Mbona mlisema hadi jioni mtakuwepo." Yule mwanamke aliyekuwa na weupe wa 'kosmatiksi' alijibalaguza lakini watu wa kazi walikuwa hawana muda naye zaidi ya kupita pale alipo na kutoka zao nje.
Kwa umbea zaidi, yule dada alikimbia hadi mlangoni na kuwatazama wakina Lisa wanavyoingia katika gari lao. Kwa bahati mbaya Masai akageuka na uso kwa uso wakakutanisha macho. Masai akapinda vidole vyake na kuwa mfano wa bastola, akamuelekezea na kufanya kama anashuti. Yule dada akashtuka na kijasho kikamtoka ghafla, akakimbia hadi katika ofisi yake na kukaa huku akitetemeka kama mgonjwa mwenye kifadulu.
Dakika mbili mbele, ndipo akapata wazo na kunyanyua simu ambayo alipiga namba za wakina Gunner.
"Haloo. Wameondoka wale watu." Dada wa mapokezi aliongea kwa kitete.
"Usijali tumeshaona wanapoelekea." Sauti ya upande wa pili ilijibu.
"Haya. Mkija, njoeni na dau langu." Dada yule akawakumbusha watu anaongea nao kuhusu aluchoahidiwa.
"Usijali." Simu ikakatwa na ahueni ya yule dada ikarudi.
****
Baada ya gari walilopanda wakina Masai kuondoka, zikapita dakika kumi ndipo magari mawili, moja la Gunner na Lobo na lingine la wale wataalam wao akiwemo yule mwenye mapengo, lilifunga breki kwenye hoteli ambayo wakina Masai walishaiacha muda mrefu.
Gunner na Lobo wakashuka na kufuatiwa na wenzao. Wakanyoosha hadi mapokezi walipomkuta yule dada akajipaka 'angel face' na kutengeneza muonekano wa maiti.
"Wapo wapi wale wajinga." Gunner alimuuliza na dada yule akashtuka hasa kwa sababu alikuwa hajawaona wale watu kama wamekuja.
"E.... e..... e.... e......" Yule dada alikuwa anakitete na macho kayatoa.
"Wapo wapi? Hatujifunzi kusoma hapa." Gunner akafoka na kumfanya yule dada arudi nyuma kwa uoga.
"Nili.... nili.... niliwa...pigia nyie ....si... si...si.... simu na kuwaambia wameooondo.... ka. Sasa sijui hamkunielewa." Maneno ya mwisho yakamtoka vema yule mwanamke baada ya yale ya mwanzo kutoka kwa kukatakata.
"Ulimpigia simu nani? We' mbwa nini. Embu usituletee uchuro hapa. Chumba walichokuepo kipo wapi?" Gunner alibwata na dada yule akatoa ufunguo uliobaki na kuanza kuwaelekeza chumba kile kilipo.
"Twende wote." Lobo kwa mara ya kwanza aliongea kwa sauti nzito na kumchomoa yule dada kwenye kitalu chake cha kupokelea wageni. Akamkamata mkono kwa nguvu na kwenda naye hadi chumba cha mikutano. Hata mlango haukufungwa, wakaingia na moja kwa moja macho yao yakatua mezani na kuona kompyuta aliyoiacha Masai ikiwa inapumua kutokana na AC yake kuwa nzima.
Gunner akaifata ile kompyuta na kubonyeza kitufe kimoja. Kioo kikaonesha maneno yasemayo 'Press Enter', Gunner akabonyeza kama alivyoelekezwa. Mara kompyuta ile ikaanza kuonesha gari la wale wanawake linapoelekea kwa kasi. Baada ya kulionesha gari hilo, kamera inayoendeshwa na satellite, ikaonesha gari la wakina Malocha ambalo lilikuwa kasi zaidi ya lile la wale Wairan wa kike. Ikaonesha umbali wa gari zile jinsi zilivyoachana. Kisha ule umbali ukabadilika na kuwa muda. Kutoka umbali wa gari analoendesha Masai hadi kwenye gari la wale wanawake, ni masaa mawili hadi kufikiana kwa mwendo waendao.
Gunner akatabasamu hasa alipoona kuwa ule muda ni mkubwa sana kwa wale wanawake kufanya anachotaka. Lakini wakati anatabasamu, mara kompyuta ile ikaonesha neno 'Plan B'.
Picha waliyokuwa wanaiangalia wakina Gunner, ikavutwa kwa mbali zaidi. Gari zikawa zinaonekana ndogo kiasi lakini zote zilionekana vema vilivyo.
Katika gari walilokuwa wakina Masai, kukaonekana mstari mwekundu, mstari huo ukaanza kuchora gari la Masai litakapopita.
Ni wazi plan B ilikuwa inaonesha njia ya mkato ambayo Masai angepitisha gari lake.
Gunner akawa kakodoa macho asiamini akionacho. Mchoro ule ukazidi kutembea hadi kwenye barabara ambayo itakutana na ile inayopita gari la wale Wairan. Baada ya kukutana ikaonesha muda ambao watakuwa wamezidiana, ni dakika tano tu.
Kompyuta ikazidi kudadavua na sasa ikaonesha baada ya dakika tano kitakachotokea. Neno lililoandikwa kwa herufi kubwa likatokea kwenye kompyuta. "WAR (VITA)" Baada ya neno hilo, kikatokea kibozo kikubwa na kuanza kucheka kwa nguvu. Kikacheka na kucheka lakini kilikuja kunyamaza baada ya Lobo kupiga risasi kioo cha kompyuta ile.
Gunner akiwa anatokwa na jasho la mgongoni, akachomoa simu yake haraka na kuanza kubofya namba za wale wanawake, kisha akaweka sikioni.
"Haloo Gunner. Umeona hiyo?" Badala ya sauti ya mwanamke mmojawapo kuitikia simu ile, akaitikia Frank Masai. Gunner akabaki kinywa wazi.
"Tatizo mnakurupuka nyie. Huyo muhudumu wenu katupa taarifa zote na tumemlipa pesa nyingi kuliko zenu." Masai akamchongea yule dada wa mapokezi. Gunner akamgeukia yule mwanamke aliyejikubua hadi kuwa mwekundu, akamuangalia kwa jicho baya.
"Nitakupata tu Masai. Huwezi kushinda vita vyetu hata siku moja. Wewe ni koko kama yalivyo mambwa koko mengine." Gunner alijibu mapigo kwa chuki nyingi.
"Haijalishi. Baadaye mje kuchukua maiti zenu." Masai akamjibu kwa nyodo.