Simba waliokula watu katika bonde la Rufiji

Simba waliokula watu katika bonde la Rufiji

Wakili wa shetani

JF-Expert Member
Joined
Nov 22, 2022
Posts
2,095
Reaction score
3,938
Miaka ya nyuma wakati wa ukoloni bonde la mto Rufiji lilijaa sana wanyama. Pengine nchi hii hakukuwa na sehemu yenye wanyama wengi kama bonde la Rufiji. Simba walikuwa wengi na waliua sana wenyeji. Wenyeji nao wakawa mafundi sana wa kuwinda na kuua simba. Hata kuna kipindi watu wa huko Singida walikuwa wanasumbuliwa na simba. Serikali ikaenda kuchukua wawinda simba kutoka bonde la Rufiji maana ndiyo walikuwa na uzoefu na hawakuogopa kupambana na simba. Hadithi moja ya simba wala watu ni ya simba aliyeitwa Zima-taa.

16. ZIMA-TAA​

Katika mwaka 1943 kwa muda wa mwezi mmoja tu, simba mla watu ambaye hadithi yake itaelezwa mbele aliuwa watu arubaini na saba (wanaume, wanawake na watoto) katika nchi ya Rufiji na akajeruhi kumi na saba.

Mnyama huyo aliwashambulia watu bila ya kusitasita kokote alikokutana nao; mioto na taa ambazo kila mara huwatisha wanyama ndizo zilizomfanyisha ajue mahali walipo binadamu. Mara wenyeji wakaona bora wafunike taa zao na mioto waizime kila wakishamaliza kazi zao. Mambo yalileta taabu kubwa, wakaanzisha ‘Zima-Taa’ yao ya kienyeji, na hapo yule mnyama akapewa jina la ‘Zima- Taa’.

Wazungu wa serikali na wengineo wakujuao zaidi huku Afrika ya Mashariki wanakubali kwamba bonde la Rufiji limejaa wanyama wengi wa kila aina. Mzungu mmoja aliyenuia kukaa katika nchi ile zamani alitoroka kwa kuogopa wingi wa wanyama, lakini Warufiji na jamii ya wenyeji watokao katika nchi za jirani hukaa na kustahamili tabu za kila namna na kuwa tayari kuzitosa roho zao wanapolinda vyakula vyao vilivyomo mashambani.

Kijiji cha Mohoro ndicho cha zamani katika vyote hapo Rufiji. Kwa kuwa kijiji hicho kipo kusini kabisa ya nchi ya Rufiji, kimekuwa bandari kuu ya majahazi ya shehena na ofisi ya simu. Hapo, mapema usiku mmoja, huyo simba mla watu alijitokeza wasafiri wachache walipokuwa bado wamo njiani na wenyeji bado hawajalala. Mtu mmoja aliyekuwa akiitwa Hassani, aliyetoka Mohoro ya Zamani, alikuwa akivuka daraja la miti. Hassani alikuwa ametumwa kuja hapo kuleta habari fulani. Kabla hajaona taa za madukani ng’ambo, hatua chache chini ya daraja jahazi lilikuwa limefungwa kando ya mto na mlinda wa jahazi hili alikuwa amechutama nyuma ya jahazi.

Ghafla, katikati ya daraja, yule kijana akamwona simba mkubwa, viungo vyake vimekazana na mkia wake ukipigapiga huku na huku kwa kitisho! Hassani akasimama upesi, na hapo wakasimama wakitazamana. Hassani akafikiri kujitosa majini na aogelee mpaka kwenye jahazi, lakini mahali pale palikuwa pabaya sana kwa mamba; jamaa wengi sana wamekamatwa na mamba.

Dakika nyingi zikapita yule mtu na nyama walipokuwa wakitazamana; kisha yule mlinda wa jahazi akapiga kelele “Ruka majini na uogelee mpaka jahazini! Ndio salama yako!”

Yule simba akageuka kule kunakotoka sauti ile, Hassani akaona hakuna wakati wa kuporonyoka ila ule. Akajitupa majini. Kwa dhoruba kali za mikono alizokuwa akipiga alipokuwa akioegelea zilimsaidia kuwatisha mamba, akafika jahazini salama, akakamata mikono ya yule mlinda na akavutwa juu kwenye jahazi.

Wote wawili sasa wakakaa wakimuangalia yule simba aliyekasirika akilivuka daraja na kupotea mnamo vivuli vya miti iliyopandwa barabarani.

Wakati ule ubishi ukaanza huko ng’ambo, na makelele ya watu waliokuwa wakibishana yaliweza kusikilikana mpaka pale mtoni, na taa ilikuwa ikionekana katika nyumba ya Mzungu mmoja aitwaye ‘Mtawa Maporini’. Kwa kujua kuwa yule simba amekwendea upande ule ule, Hassani akaweka mikono mbele ya kinywa chake akapiga ukelele kuwajuvya wakaao pamoja na Mtawa Maporini’. “Juma Juma! Angalia simba darajani!”

Juma alikuwa mwindaji mashuhuri, akienda kuwinda pamoja na bwana wake huweza kuifanya kazi ikiwa bwana wake amechoka: akiwa peke yake huitumia gobore yake vyema.

Baada ya kelele za Juma kukawa kimya; kisha wakasikia mwanamke anawaita watoto wake na kuwakamata akijaribu kuwarudisha nyumbani na kuwaficha. Kwa mara ya pili sauti ya Juma ikasikiwa akitoa amri zake na huku watoto wakilia na kupiga kelele wakiwasikia wakubwa zao wakibabaika kwa woga wa simba. Milango ikafungwa; taa ya ‘Mitwa Maporini’ ikazimwa na kote kukawa kimya. kabisa, ji!

Baada ya dakika chache Juma akajitokeza darajani na gobore lake na wenzie waliobeba mikuki mikali kama wembe. Akasema “Yuko wapi huyo mtu aliyeniita?” Mlinda pahazi akamjibu “Yupo hapa. Tungoje.” Kisha yeye na Hassani wakapanda mtumbwini wakaenda kusini ya pwani. Humo mtumbwini Hassani akaanza kueleza hadithi, akasema, “Nilipambana na simba uso na macho hapo darajani, nikarukia majini na kuogelea mpaka jahazini na yule simba akaaendea huko.”

Juma akaitikia kwa makini, kisha akasema, “Vyema, hatuwezi kufanya jambo lolote sasa hivi, lakini kesho asubuhi lazima tufanye sako kubwa.”

Hassani akashuka mtumbwini akaenda nyumbani kwake hata dukani hakuenda usiku ule. Yule mtu wa jahazini akarudi na mtumbwi wake mpaká chomboni mwake, na kwa kutaka salama, akakisukuma chombo chake katikati ya mto, na akatupa nanga yake yenye kutu. Mabaharia wengine waliokuwako mjini waliweza kuivuta ile jahazi kama wangerudi lakini alidhani kwamba hawatarudi kwa kuogopa simba.

Kabla Juma na wenzie hawajafika nyumbani kwa ‘Mtawa Maporini’ wakasikia kelele zingine za kustusha zikitokea kitambo cha maili moja kusini. Juma akasema “Kelele hizi zinafikirisha kwamba simba yumo mashambulioni!” na mara Juma akawaongoza wenzie kule kule kwenye matata yale. Kabla hawajafika kule waendako wakasikia ngoma ya kujulisha kuwa simba amekamata mtu!

Walipofika katika kijiji kidogo karibu na mto Shera wakawakuta watu wameshika silaha zao, bunduki na mikuki. Mwanamke aliyekuwa ameshikwa na uchungu wa kulia hakuweza kusema neno. Hakuna alilokuwa akijua ila mumewe amekamatwa na simba.

Juma akamwuliza yule bibi, “Tuambie yaliyotokea, tunataka kukusaidia. Yule mnyama amekimbilia upande gani?”

Mwishowe yule bibi akakazana maana maneno ya yule Juma yalikuwa yakimwingia moyoni sana, na akawa anaanza kufahamu kuwa Juma alikusudia kumsaidia kweli. Akasema, “Sote tulikuwa tumekaa nje tukiongea nikamwona simba akitokea kizani akitujia. Kabla sijaweza kumwambia kuwa simba anakuja alikuwa amekwisharukiwa mgongoni na yule mnyama… Sikuweza kusema wala kupiga kelele; Nikakimbilia ndani ya nyumba… Sikujua wapi alikimbilia.”

Alipomaliza kusema maneno hayo kwa sauti ya kutetemeka, akaanza kulia machozi tena. Juma hakuweza kupata habari zaidi kutoka kwa yule bibi. Alipozungusha kichwa chake akakiona kitabu kimelala chini nje ya kibanda cha yule bibi; pia aliweza kusikia harufu ya mafuta ya taa. Mtu mmoja alimwambia kuwa yule mtu aliyekamatwa alikuwa akisoma pale nje na akitumia taa ya kandili, basi yule simba alipokuja kumshambulia, aliipiga chini na kuizima. Jina hilo la ‘Zima-Taa’ lilimstahili sana simba yule!

Juma akazisoma sura za wenziwe wote waliokuwa wakimzunguka na akasema, “Kila ajionae kuwa ni mwanamume asiogope kunisaidia kumtafuta yule mnyama. Tutaanza sasa hivi.”

Wale watu wote pamoja na silaha zao wakausaka msitu kwa saa mbili lakini hawakufanikiwa kumwona yule mnyama. Mwezi mchanga ulipokuwa ukizama chini ya msitu wale wawindaji wote wakashangaa mmoja wao aliponyoosha kidole chake mbele kwa hofu na huku akinong’ona, “Angalieni !”

Dudu moja kubwa jeusi lilikuwa likiwakabili, waliweza uona mgongo usiokuwa na nyele uking’ara kwa maji. Juma akasema taratibu, “Kiboko yule.” Yule mnyama aliposikia sauti ile akageuka na akakimbia mpaka ziwani. Hatimaye kiongozi akaona kuwa hakuna faida yoyote kuendelea kusaka usiku ule, kwa hiyo akawaruhusu wale watu warudi makwao na kufanya mashauri ya kukutana tena subuhi ya pili. Mwangaza wa jua ndio waliotumainia kutafutia nyayo za yule simba.

Juma aliamka alifajiri sana na alikuwa tayari nje akiwazungukia wenziwe na kuwaweka tayari kwa sako la simba. Aliona tabu kidogo kuwapata watu wale wale aliokuwa nao tangu kwanza; wengine walikuwa wamechoka kwa mwendo wa usiku uliopita na hawakuweza kuamka asubuhi mapema. Jamaa wengine walikuwa wamepata habari ya mshindo ule na wakatoka makwao mbali kuja pale kuungana na wenzao kumtafuta yule ‘nduli’ mla watu. Ndugu wa marehemu pia walikuwapo, mioyo yao imejaa ghadhabu nao pia walikuwamo katika sako hilo hilo. Kwa kuwa haikujulikana wapi ataweza kuonekana yule simba, Juma aliona heri ajitulize kidogo mpaka ipatikane habari safi ya yule simba ndipo ajiunge katika kundi mojapo.

Basi Juma akakaa kitako karibu ya moto akijishughulisha kujaza baruti nyingi katika gobore lake ili mshindo mmoja tu umwue simba au kiboko. Baadaye watu wengine wakajiunga naye kushindilia baruti zaidi ndani ya mago- bore yao na kuinoa mikuki yao, na wakaleta habari kuwa hakuna aliemwona simba.

Mchana akaja kijana mmoja mwenye habari nyingi, akasema, “Nimeuona mwili wa Mtungute, ulikuwa kitaruni. Nilikwenda huko kukata kuni nikaona matambara meupe yametanda. Nilipokaribia nikaona kichwa chake na vipande vipande vya kanzu yake…” Juma akamwuliza, “Je uliona upande uliokwendea nyayo,” “ndio” akajibu, “Nilizifuata nyayo zake mpaka nikakuta mabaki ya mwili wake… nikawaita ndugu zake wakakusanya mabaki ya maiti wakenda kuzika.” “Kwa hiyo haina maana kumtafuta yule mnyama mahali pale” Juma akasema. “Madhali maiti yameondolewa, simba yule atakwenda kumtafuta mtu mwingine amle.”

Kutwa nzima ikapita bila ya kupatikana habari yoyote zaidi, na jioni majirani walijikusanya barazani kwa Juma kama ilivyo kawaida yao, na kama kawaida ya watu wengine, walikuwa hawana jambo la kulizungumza ila lile la simba mla watu. Kiza kilipokuwa kikubwa, wote wakajimwaga wakaenda zao majumbani mwao; pia kazi ya kulinda viboko ilibidi ifanywe, maana wangeiacha, viboko wangeliviharibu vyakula vyao vyote mashambani.

Juma aliwasindikiza watu wale kwa kiasi cha maili hivi; kisha alipokumbuka kuwa hakuchukua silaha yoyote alirudi nyuma. Kiasi ya hatua mia baada ya kuachana na wale jamaa, akakutana na mtoto aliyetumwa na mkewe mwenye busara kumpelekea bunduki yake, pembe ya baruti na mfuko wa risasi. Yule mwanamke mwema kila mara alikuwa akimuasa asitembee usiku bila ya silaha katika nchi ile yenye wanyama wabaya.

Jamaa Wakirufiji ni watu wasiogopa hata kidogo wanyama wakali. Mambo yaliendelea kama kawaida tu mle mjini, kama kwamba hakukutokea jambo lolote la kustusha. Usiku ule hakukuwapo jambo lolote. Mbwa walilia huko na huko, na katika vibanda vilivyokuwa mbali kidogo, wanawake walikuwa wakiimba nyimbo zao kwa huzuni sana. Walikuwa wakitumaini kumsikia simba mla watu saa zozote.

Juma alipokwisha ipokea ile bunduki yake kwa yule mtoto, akamwambia arudi nyumbani akamwambie mkewe kuwa yungali na hamu ya kuwinda. Makelele ya madebe yalimjulisha Juma kuwa walinda viboko wamo kazini.

Hapo hapo akakutana na dudu moja kubwa likitokea kwenye Ziwa Shera, akishughulika kung’oa mipunga. Alipotambaa mpaka karibu Juma akawa tayari kumpiga na mara debe likapigwa na yule mnyama akaporomokea ziwani. Bahati ya Juma ikapotea!

Alipokwenda kwenye dungu alilokuwa akikaa mwinda viboko aliyepiga lile debe, wakaanza kuzungumza na wakala ndizi za kuchemsha. Kisha akateremka dunguni akaenda upande mwingine wa ziwa ambako alifikiri kuwa ataweza kupata viboko wengine. Hapo pote palikuwa hakuna miti mingine ila mikoche tu. Mwezi ulikuwa uking’ara zaidi kuliko usiku uliopita na kulikuwa na vivuli vya kuogopesha sana chini ya mikoche hata ilimbidi aende kwa uangalifu sana.

Wakati huo Juma alikuwa amekaza macho kwenye kitu kilichokuwa kikitembea polepole mbele yake. Kilikuwa si kiboko alikuwa na hakika kabisa lakini kwa mwangaza wa baramwezi hakuweza kusema kilikuwa ni nini kabla hakijajipoteza. Juma akasimama kimya kwa dakika chache akisikiliza sana lakini hakuweza kusikia sauti yoyote. Alipokaribia kuondoka kwenda zake kusikia sauti kitu kile kile kikaanza kutembea tena na kujijulisha mbele yake, karibu hatua thelathini. Upepo ulikuwa ukivuma polepole ukijia alikokuwa yeye.

Kabla hajaanza kutembeatembea, Juma akavumbua kuwa kile kitu kikubwa kilichokuwa kikitembea polepole kilikuwa simba mkubwa. Alipokuwa bado akimwangalia, yule simba akajinyoosha kama paka aliyetoka usingizini; kisha akaunguruma mlio wake wa hatari. Juma aliposikia mngurumo ule akajua jinsi jamaa walio vibandani wakijitahidi kufunga milango yao, na wasafiri wakiomba Mungu wafike mwisho wa safari zao salama waone jua siku ya pili.

Alipohakikisha kuwa gobore lake limeshindiliwa sawa sawa akazidi kumchungua yule mnyama. Mara yule simba akageukia upande aliokuwako Juma, naye akailinga bunduki polepole. Ingawa alikuwa mwindaji wa siku nyingi lakini hofu ilimwingia na ikampata taabu kidoko kuiweka sawa bunduki yake. Bwana wake alikuwa akimwambia kuwa hao wasiopata kujua hofu ni walevi au wapumbavu; ingawa alikuwa amejawa hofu moyoni mwake alijaribu kujikaza ili asiharibu kazi yake ya kumwua yule mnyama mkali aliyemkalia mbele yake.

Na bunduki yake mkononi, Juma alisimama kama sanamu ya askari iliyoko Dar es Salaam ya ukumbusho wa vita, yule simba alikuja mpaka hatua chache tu kutoka alikokuwa Juma na mara akapata harufu yake akasimama. Juma tena hakungojea kitu, aliifyatua tu, ukatokea mshindo wa ajabu na ulimi mrefu wa moto ukatoka kwenya mdomo wa bunduki. Harufu ya baruti ikajaa pote na kumpalia Juma; moshi ukajaa na kumziba kabisa.

Juma akanyamaa kimya akingoja. Kama asingemwua yule mnyama au angemjeruhi kidogo angekufa yeye; yule simba asingempa nafasi ya kushindilia tena bunduki yake. Lakini risasi ilimwingia simba barabara hata hakuweza kusogea, akalala kama mtu aliyechoka kwa mwendo. Huku akimshukuru Mungu kwa kumsalimisha, Juma akauegemea mkoche akishindilia bunduki yake tena; kisha akasogea majanini kwa uangalifu sana.

Hapo simba kubwa limelala maiti! Kwa hatua fupi alizokuwa yule simba, ile risasi ya Juma ilimwingia sawa sawa. Lakini yote yale Juma aliona bure, maana kama alivyoona yeye, simba yule aliemwua hakuwa ‘Zima-Taa’.

Akajua kwamba madhali yule amekufa mwenzie atataka kulipa kisasi kwa kuuliwa rafiki yake, Juma hakupoteza wakati, akajirudia nyumbani. Nusu ya njia akasita kidogo, akasikiliza kwa makini. Mbali sana ikatokeza sauti ya ngoma hafifu lakini wazi, ikimwambia kuwa huko maporini mtu ameliwa na simba katika kijiji cha Mbwara!

Juma akasema, “Maisha ni jambo la ajabu sana, huku simba ameuawa na mtu; na huko mtu ameuawa na simba.”

Saa mbili asubuhi habari zikafika Mohoro kuwa simba mkubwa aliyejulikana kuwa ndiye yule yule ‘nduli’ mla watu, alishambulia kundi la watu waliokuwa wamekaa karibu ya moto pembeni ya njia huko Mbwara, wakipumzika walipokuwa wakitoka Kilwa kwenda Mohoro. Mtu mmoja alikamatwa na ingawa yule simba alifukuzwa na watu ili amwachie mwenzao alizidi kwenda naye.

Kwa njia hii, kwa miezi mingi, simba yule alikuwa akikamata watu, alikuwa akitembea bila ya woga Rufiji nzima. Askari wa nyama waliletwa katika vijiji vyote walikuwa wawindaji hodari waliozoea sana kazi hiyo na waerevu sana kwa kutega simba. Mitego ya simba ilikuwa ikirushwa ovyo na simba huyo hata ilikuwa haiwezi kumkamata. Kwa ubaya wake hakuogopa taa wala moto, alikuwa akiwakamata watu popote alipopenda na mtu yoyote amtakae.

Kila baada ya siku chache habari mpya za ubaya wa huyo simba ziliwasili Mohoro. Safari moja, mtu mmoja aliacha duka lake wazi kwa upumbavu wake na taa ikiwaka; simba aliruka mpaka ndani akamata mtu mwingine. Mwanamke mmoja aliyekuwa akimkogesha mwanawe kibandani mwake alinyakuliwa na simba. Vifo viwili havikupata kutokea mahali pamoja hata mara moja: ‘Zima-Taa` alikuwa simba mtembezi sana.

Askari nyama walizidi kumiminika, na mitego ikazidi kutegwa lakini ‘nduli’ mla watu aliendelea kufanya kazi yake kwa kitisho sana; uhodari wake wa kujua tabia za binadamu ulimsaidia kuepukana na vifo vingi. Woga ulizidi kutangaa kote kijijini na usiku watu walijifungia mnamo vibanda vyao vyenye kiza.

Jioni moja ngoma ya sherehe ilichezwa karibu maili mia kutoka Mohoro katika kijiji cha Kwangasi. Ilikuwa ngoma ya kusherehekea harusi ya kijana mmoja, wanaume na wanawake waliuzunguka moto na huku wakicheza ngoma. Ghafla, simba mkubwa akaruka mpaka katikati ya wacheza ngoma. Bila ya kuogopa moto, yule simba akamvamia mtu mmoja ambapo wengine walitawanyika ovyo kwa woga.

Mwishowe yule ‘Nduli’ akamkamata mwanamke mmoja aliyekuwa akipigia kelele sana na akaruka naye kizani. Wale waliomwona akichukuliwa walipiga kelele kama walivyoweza, wakijaribu kuwaita wenzao kusaidia kumwokoa yule mwanamke. Wabantu ni watu wenye moyo mgumu sana na shime nyingi; kila mwanamke au mwanamume aliyekuwako alikamata kijinga cha moto na kwanza kumfuata yule simba. Hata wapiga ngoma walikwenda na huku wakipiga ngoma zao.

Lile kundi halikufika mbali kabla hawajasikia mshindo wa bunduki. Wakaharakia mbele wakitazamia kumkuta aliyemuona yule simba. Lakini bila ya kutazamia wakamkuta yule simba na yule mwanamke wamelala wakivuja damu maiti. Uzi uliotegwa na askari nyama ulifyatua risasi kwa shabaha njema, na hapo yule mnyama na mwanamke wakauawa!

‘Zima-Taa’ alikuwa na urefu wa futi kumi; jino moja kubwa lilivunjika, jicho moja limetoka, na mwili umejaa makovu.

Baada ya hapo uuaji wa simba ukamalizika; ‘Zima-Taa’ aliyekuwa akiogopwa hawezi kuitisha Rufiji tena.

Hii hadithi ipo ndani ya kitabu Masimulizi ya Mtawa Maporini kitabu cha 4. Unaweza kisoma chote ndani ya Maktaba
 
Siku moja tuko porini Selous huko ni fisi alituokoa.
Tumekaa tunachoma nyama ya nyati na mastori kibao kumbe Simba kanyata yuko pale jirani tu anaskiliza story na kuvizia.
E bana ile harufu nyamachoma fisi hao na kimbelembele chao wanachekacheka wakaharibu target ya Simba.
Yaani ule mvurugano toka kichakani fisi akipigwa mpaka pale kilingeni wamevuruga moto nyama zote tupa kule,
Si hata hatupo tushakimbia kwenye mahema.
Yule fisi alilia siku hiyo "mama nakufaaa"
Kwa kipigo
 
Dah
Mkuu umenikumbusha mbali sana. Story yako ina ukweli. Mwishoni mwa 1990s kabla daraja halijakamilika nilivuka hapo Rufiji river nikitokea Dar nikiwa na lika chini ya 16. Lengo lililkuwa kwenda Nangurukuru.
Tulifika hapo jioni kivuko hakifanyi kazi na ilikuwa lazima asubuhi niwe Nangurukuru. Ilibidi tupande mtumbwi wa kienyeji. Ilikuwa hatari sana kuvuka, kwani mamba unawaona na kuogerea sijui. Halafu mto upo speed kwani ilikuwa masika. Chakushangaza captain alikuwa haogopi kitu ndio kwanza alikuwa ananipa moyo kuwa tutafika ngambo salama.
Tulipovuka tu, kulia kulikuwa na guest house na kulikuwa na watu wengi balaa. Ufuska uliokuwepo pale Mungu tu ndio anajua. Sasa uwani kwa ile Guest kulikuwa na Mabafu mawili ambapo ukiwa bafu moja aliyekuwa anaoga bafu lingine unamwona. Sasa akaingia mdada wa makamo kuoga nikaanza kumchungulia mara akaniona. Kilichotokea hapo ni siri, lakini mbeya mmoja akaenda kumtonya mume. ile natoka tu mume huyo kafika na kuanza kumshtumu mke kwamba alikuwa na mtu. cha ajabu akunishtukia kutokana na kimo na lika langu. Ila sikufanya zambi zaidi ya kuchungulia na kubalishana maoni.
Kesho yake asubuhi tukapanda baiskeli kwenda Nangurukuru, baada ya ya dk 10 tunakutana na simba ana vitoto. Mzee akanambia nisikimbie akitusogera nichune. bahati nzuri yule simba alituangalia baadaye akapotelea porini. Nikaanza kuhisi kuwa ile zambi ya jana usiku ndio imesababisha kukutana na Simba. Mzee akaniambia kukutana au kuliwa na simba eneo hilo siyo story. Hakika nilipata uwoga ambao hadi leo siwezi kusahau.

Kimsingi ni kweli Bondo la Rufiji hasa upende wa lindi ilikuwa hatari wengi wameliwa sana na simba.
Naomba Mungu wa mbinguni mwenye huruma anisamehe na kunifutia zambi ile.
 
Hadithi ya Simba wa mizimu. Hii inapatikana katika kitabu cha pili cha Masimulizi ya Mtawa Maporini. Unaweza kisoma ndani ya website ya Maktaba

SIMBA WA MIZIMU​


Siku moja nilikwenda katika kijiji kimoja kilichokuwa kikishambuliwa na ndovu mara kwa mara. Nilipokuwa nikipitia njiani, nilimwona mtu mmoja juu ya dungu lake akiezeka paa la dungu kwa makuti ya mkoche. Nilipopita pale chini la dungu, yule mtu akanitazama kisha akacheka. Nikamwuliza, “Unacheka nini?” “Ah,” akanijibu, “nimefurahi tu, bwana.” Baada ya kuzungumza naye kwa muda mchache, akanihadithia kuwa akishajenga dungu lake, anataka kulima shamba la mtama mahali pale. Mkewe na wanawe watakuja kukaa mle dunguni kwa kumsaidia katika kazi zao za makulima. Nikapatazama mahali pale nikapaona ni pazuri sana kwa yote aliyokusudia. Kwa mbele kidogo kulikuwa na mkuyu mkubwa uliotandaza matawi yake na kutoa kivuli cha haja. Uwanja mzuri wa majaní mabichi ulitambaa pote na kupapa mahali pale sura nzuri. Palionyesha kuwa swala na wanyama wengine wengine wanaweza kupatikana kwa urahisi sana mahali pale.

Dungu lile lilijengwa na mtu niliyekwisha mtaja, lilinipendeza mno hata nikamwomba yule bwana anipe nafasi nikae mle dunguni mpaka kumaliza kazi yangu na kuhama mahali pale kama ilivyo kawaida yangu. Hata hao ndovu niliowaendea katika kijiji hicho bila shaka ni rahisi kuwapata kwake kama ukikaa katika kibanda au dungu la huyo bwana ninayemhadithi. Tukapatana aniuzie. Akaniuzia kwa shilingi kumi. Nikanunua, yeye akatafuta mahali pengine karibu na pale akajenga dungu lingine.

Tulipokwisha tua mizigo yetu pale chini ya dungu, tukaenda kuwinda nyama karibu karibu kwa chakula chetu cha jioni. Njiani, watu niliofuatana nao wakaanza kunitisha.

Wakasema, “Pale uliponunua dungu, ni mahali pabaya sana. Yuko simba mtu anayependa sana kupitapita. Simba huyo, hapo kale alikuwa mke wa sultani aliyeuawa na Majerumani. Aliuawa katika vita ya maji maji. Hakuna hata mtu mmoja aliyepata kujenga mahali pale isipokuwa yule mpungufu akili aliyekuuzia dungu. Labda naye ni mchawi wa kutosha hata akathubutu kujenga mahali pale. Kwanza Korogeo si mwenyeji wa nchi hii wala si Muislamu.”

Nikaisikiliza hadithi yao ya kuogofya kwa utulivu. Ingawa hadithi yao ilikuwa ni ya mambo ya ushirikina mtupu, nilingiwa na woga kidogo. Yeyote aliye mgeni katika nchi fulani au mahali fulani mara nyingi huogopa jambo lolote la hatari atakaloambiwa. Wakazidi kuniambia kuwa simba huyo huja masika hata masika tu. Hukaa chini ya mkuyu ulio karibu na dungu na kuvizia chochote kitakachopita chini ya mkuyu. Hapakuwa na mti wa kupanda kama mtu akikutana na simba huyo, isipokuwa mkuyu huo huo anaokaa simba chini yake akivizia kinachopita. “Shida sana kuponyoka ukikutana naye,” wakaendelea. “Kama tulivyokwisha sema, kuwa si simba wa kawaida bali ni simba wa mizimu. Yanini kusema mengi; masika sasa ni karibu sana; na kila masika simba hufika kutoka mizimuni; basi kama bado upo, ataona mwenyewe na kuhakikisha badala ya kuhadithiwa.”

Mwezi ukapita pale dunguni bila ya kuona lolote. Masika ya kawaida. Mtama wa Korogeo ukakua na kuonyesha dalili ya mavuno mazuri sana. Korogeo alifurahi sana kwa kuuona mtama wake unaahidi mavuno mazuri. Ulifunga shamba zima hata ukaonekana kama msitu kamili. Uwanda ule wa majani mazuri ukageuka mbuga ya nyasi hata mtu akipita pale chini ya mkuyu ni vigumu kumwona kwa urahisi. Ndovu wakaja kwa wingi katika mashamba ya watu na kuharibu mimea. Niliwaua na kuwafukuza wengi. Korogeo na shemeji yake wakajenga madungu yao hatua mia kulia ya dungu langu.

Usiku mmoja nilisikia kama kishindo cha mnyama fulani anapita nje ya dungu langu. Nikaamka, nikatoka nje na kujibanza. Ulimwengu mzima ulikuwa umelala. Nikamulika kurunzi yangu huko na huko lakini sikuona kitu. Nikarudi dunguni nikalala. Punde si punde nikasikia sauti ya Korogea ikiita kwa hofu. “Bwana! Bwana ! Bwana! Kuna dudu huku!” Bila ya kukawia nikafika dunguni kwa Korogeo na taa na bunduki. Korogeo akashuka akihema na kusema, “Lilikuwa dudu hapa, sasa hivi.” Tukatafutatafuta lakini hatukuona kitu. Nilipomulika taa chini karibu na lile dungu nikaona alama ya unyayo wa simba mkubwa sana. Ni ajabu kabisa lakini unyayo ule ulionekana mmoja tu. Tena, ulijulisha dhahiri kama simba huyo ndiyo kwanza amekanyanga mahali pale. Kwa kuwa ardhi ilikuwa nyevu, ule unyayo ukaanza kujaa maji. He! kumbe upande mmoja wa nyumba ya Korogeo ulikwisha bomolewa. Bila ya shaka simba yule alikuwa amejificha katika majani marefu karibu sana na dungu lake. Nuru ya taa haikuweza kumwonyesha. Kama tulivyokwisha ambiwa na wenyeji, simba wa mizimu alikuwa amekwisha tuingilia.

Upepo wa mvua ukaanza kupepea na mawingu yakafunga na kutia kiza kikuu ajabu. Mara mvua kubwa ikaanza kuanguka. Umeme ukamulika nchi nzima kwa ghafla na kutoa ngurumo kama mzinga wa motoni.

Majani, nyasi na mtama vyote vya ulimwengu ule vikapeperushwa. Radi ikaunguruma mara ya pili. Umeme na ngurumo, na umeme na ngurumo. Korogeo na mimi tukasimama pale pale mbele ya dungu na taa yetu ikazidi kufifia. Umeme ulipomulika mara ya mwisho, kwa mbele tukaliona simba kubwa limesimama. Tukaingia katika chumba cha chini cha dungu na kujificha.

Kila mtu akakaa karibu na mwenzie tukimfikiria simba wa mizimu yule. Hakuna aliyejua nani atakayechukuliwa kwanza kama simba akiingia mle dunguni. Saa nzima ikapita bila ya hatari yoyote. Mvua ikanyamaza na nchi ikwa shwari tena. Kiza kikapungua kidogo. Korogeo na mimi tukaondoka pamoja mpaka dunguni kwangu. Korogeo akakaa karibu nami mahali nilipolala katika kiti cha kulala. Bunduki yangu mapajani na Korogeo mkuki wake mkononi. Hakuna hata mtu aliyeweza kuupata usingizi kwa hofu. Hatukuwa na la kuzungumza wala kufanya. Tukabaki tukitazamana na kucheka kama wapumbavu. Mara nikamwona Korogeo anatazama chini huku macho ameyatoa.

Nikamwuliza, “Nini Korogeo?”

“Tazama!” akanionyesha chini karibu na taa. Lo! nilipotupa macho, nikauona unyayo wa simba pale chini ndani ya dungu langu. Unyayo wenyewe ulifanana sana na ule tuliouona karibu na dungu la Korogeo. Nilipozidi kutazama nikaziona kwa wingi mle ndani ya kibanda changu. Kumbe yule simba alikwenda mle dunguni mwangu nilipokuwa ndani ya dungu la Korogeo. Hatukuweza kujua simba alipokuwa wakati ule. Kila mtu akajitayarisha na kuyakaza macho yake mlangoni; kwani ndiko tulikodhani atatokea kama atakuja. Tukakaa vivi hivi lakini hakutokea.

Bila ya kupenda nikapitiwa na usingizi mdogo. Sikujijua kama nilipitiwa na usingizi mpaka nilipoamshwa na sauti ya kitu kizito kilichonirukia kifuani, Korogeo akaita kwa woga tena; “Bwana !” Aliyenirukia kifuani, alikuwa Korogeo. Nimemwona akichungulia! Sasa hivi tena! Si simba bwana! Nasadiki kama ni simba mtu! Nikatega bunduki yangu na kuilekeza mlangoni, Dungu zima likajaa harufu ya mnyama wa porini hasa ya simba. Nikauona umauti umekaribia saa ile ile. Mara pale mlangoni nikaona kama kitu kinasogeasogea. Kwa woga niliokuwa nao, sikungoja nikione vizuri; nikaelekeza bunduki pale pale na kupiga. Mshindo wa bunduki ukavuma mpaka mbali karibu na alfajiri ile. Mara mkoromo wa maumivu ukasikilikana nje ya dungu. Hakuna aliyethubutu kutoka na kwenda kutazama. Mara kulipoanza kupambazuka tu, tukatoka na kwenda kutazama. Kwa furaha yetu simba lile lilikuwa kaputi hatua ishirini tu toka dunguni kwangu. Watu walipopata habari, walifurahi sana. Wengi wakasema kuwa Mzungu hadhuriki na mashetani ndiyo maana akaweza kumwua simba yule. Wengine wakasema kuwa simba yule hakufa asilani. Yote yale yalikuwa ni mazingaombwe tu. Kwa vyovyote hivyo, kama alikuwa simba wa mizimu au simba wa kawaida, simba yule aliyeitisha nchi kila masika alikuwa amekufa siku ile. Haikosi Korogeo bado anaukumbuka usiku ule kama niukumbukavyo mimi.

 
Hiki kisa kinapatikana ndani ya kitabu Masimulizi ya Mtawa Maporini kitabu cha kwanza. Kinaelezea jinsi watu wa Rufiji walivyowinda simba. win-one

Simba Wanavyowindwa Rufiji​

Tangu mtawa maporini amefika hapa Rufiji Delta ameyajua mambo mawili yasiyojulikana na binadamu kama yapasavyo kujulikana. Lakini kwanza hebu niseme ya kuwa watu wengi wa Dar es Salaam hudhania Rufiji Delta ndiyo jimbo zima la Rufiji, sivyo kabisa; lakini katika sehemu mbalimbali za dola yetu wako watu waliomo gizani kama hao jamaa wa Dar es Salaam kwani wanafikiri nchi za Afrika ya Mashariki, hata zile za Afrika ya Magharibi zote zinahesabika katika nchi za Afrika ya Kusini. Niyarudie mambo hayo mawili: mosi, kima huogelea katika hori zenye maji marefu wakitoka ng’ambo hii hadi ya pili; huogelea kama mbwa. Vile wavulana wapendavyo kuogeleaogelea hali kadhalika kima hao. Pili, simba vilevile huogelea toka kisiwa kimoja hadi cha pili ikiwa hawawezi kuvuka kwa sababu yapo maji mengi katikati hata wakati wa maji mafu. Simba huwasaka nguruwe mwitu. Wasipowapata nguruwe wa kuwashibisha ndipo simba wanapoyashambulia mazizi na kuwanyakua ng’ombe au huwasomba punda wabeba nazi za bwana zao Waarabu. Basi nasimulia hadithi ya kweli.

Yupo kijana mmoja wa Kiarabu jina lake Saidi bin Nasoro akaaye katika kisiwa cha Mbwera kilichopambwa na minazi, kila utupapo macho minazi chekwa; kisiwa hiki kipo katika Rufiji Delta. Basi usiku wa manane kijana huyu akazinduka usingizini akalikamata jambia lake na torch yaani kurunzi ndogo. Punda wake aliyefungiwa mnazini kwa mnyororo alikuwa akilia kwa hofu kali; tena bwana Saidi hakuwa na mwingine, huyo huyo tu wa kumbebea mbata mpaka sokoni. Mwarabu akadhania nyoka au chatu anamtisha au anamsumbua punda wake. Mkewe na watoto, mmoja wa kiume mwingine wa kike, wakamfuata nje, kwani walikuwa na hamu ya kukiona kitu hicho pia walitaka kumtetea punda wao asidhurike,

Nuru ya kurunzi ikaonyesha kitisho kweli kweli. Simba wawili walikuwa wakimpiga punda makucha, na masikani punda kukimbia hawezi kwani amefungwa kwa mnyororo, Saidi akawaambia mke na watoto, “Upesi ingieni ndani: mke wangu, niletee mauser (bunduki) yangu.’ Wakaingia katika nyumba ndogo iliyoezekwa kwa makuti.

Punde si punde akapewa bunduki yake, akaiweka mikononi, akajiona naam sina hofu sasa; lakini punda zamani ameukata mnyororo, yumo mbioni katika shamba la minazi, kipande cha mnyororo kinaburura nyuma, simba wanamfukuza kweli kweli. Na Mwarabu akafuata, mauser mkono mmoja, kurunzi mkono wa pili; akakimbia, akakimbia wee maili mbili nzima, akiyafuata makelele ya simba washambuliao na punda awakimbiaye, akapafikia mahali pa Mwarabu mwingine, Ali bin Saidi. Akapapita, anazidi kufuata. Pengine aliposikia kimya, akaiwasha kurunzi yake, akaangaza chini akizifuata nyayo zilizoonekana dhahiri kwani ardhi ilikuwa ya mchanga mchanga na nyasi fupi fupi tu. Akapaza sauti akiwalani simba na kuwaambia, “Mkimmmaliza punda wangu mtanitambua.” Mara akaifikia nyumba ya kaka yake; nyumba hii pia imezungukwa na minazi. Sebuteni akamwona punda wake amelala anatweta, mikwaruzo mwili mzima lakini angali hai. Hapo kale katika nchi ya Uingereza alikuwako mcha Mungu mmoja jina lake Thomas Becket; basi alipojiona ametingwa na maadui walioazimia kumwuulia mbali akajitupa madhabahuni kanisani; hali kadhalika huyu punda, akajitupa masikani pa kaka yake bwana wake aokoke. Akatibiwa utibabu wa vivyo hivyo, bali ulimfaa; akashonwa kila alipochanwachanwa na makucha ya simba, akapakwa chumvi na buluu damu zisizidi kumtiririka.

Alfajiri na mapema Saidi akamwambia boi yake Msenga bin Mpiringu “Nenda ukamwombe jumbe awaamuru watu wake waipige ngoma ya kuwaarifu wenyeji ya kuwa leo ni leo, wanaume kweli watokee.” Kusikia mdundo wakatokea kweli, wanaume labda sitini na bunduki za marisau na mikuki kadha wa kadha.

Saidi akakiongoza kikosi hiki, wakazifuata nyayo za simba wakaenda, wakaenda mpaka wakafika penye kihori chenye kingo za matope yasiyo na kina. Hapo simba walivuka kwenda masikani kwao, yaani walalapo mchana kutwa. Wakati walipovuka simba hapakuwa maji, yalikupwa; bali walipofika akina bwana Saidi wakakuta yamekwisha jaa yana kina cha futi kumi nzima. Tena mamba wengi huishi majini humo. Lakini wenyeji wa Rufiji wana umoja sana katika kupigana na wanyama mwitu ambao ni maadui zao; wakiachiliwa nguvu zao zitazidi, wataweza kuwasumbua watu hadi washindwe kukaa kwa raha hapo wanapoishi wao na walipoishi babu zao.

Basi wote wakaanza kuvuka kwa kuogelea. Vita ya Omdurman yasemekana kwani askari walionyesha ushujaa na umoja; hali kadhalika hapa katika hawa watu wa hadithi yetu. Walikuwapo vijana wawili wasiojua kuogelea, lakini wakajaribu vivyo hivyo kuvuka; maji yakawaingia puani, mengine wakayameza, wakapiga mayowe, “Jamani, maji yanatuaa,” wakazama. Wenzao wakawacheka sana kwani pande za Rufiji wasiojua kuogelea wanadharauliwa sana. Walipokwisha kutapatapa majini wenzao wawili wakawaokoa, wakawalaza matopeni ng’ambo ya pili, masikini wakaanza kutapika na kukohoa moja kwa moja, na wote wengine wakaangua kicheko tena.

Kwa gafla vicheko vikakoma. Yadi kumi na mbili tu toka hapo walipokuwa watu palikuwa mti mkubwa wenye matawi mengi yaliyosambaa huku na huku na shina la mti laini kabisa. Halina magamba magamba kama shina la mwembe, chini paliota nyasi fupi fupi; basi mahali hapo wakainuka simba wawili. Walivyohadithia jamaa baadaye wavulana wengine kuwaona simba hawakujitambua kwa hofu, wakasema lugha isiyofahamika.

Mara jamaa wakaiparamia mikoko dhaifu iliyoota karibu karibu, hadi msomaji wangu ungalipata kwa mbali dakika hiyo ungalifikiri hivi: “Lo, ama kweli ndege wamejenga mji humo mikokoni”; lakini ndege hao hawakuwa na mbawa wala manyoya, bali walikuwa na miguu na wengine walikuwa na ndevu, na wengine bado hazijawaota. Watu wachache wakakosa miti ya kuparamia, yote imekwisha jaa. Wale waliokuwako mitini walipotulia hadi wakaweza kuangaza wakagundua ya kuwa mahali pale ni kisiwa kidogo kiasi chake chapata sehemu kumi na sita kwa moja (1/16) ya eka (acre). Kisiwa hicho kilizungukwa na maji ya hori zilizoenea pote; hakika simba wale walichagua mahali pazuri pa kufichama mchana kutwa. Kivuli cha mti mkubwa ule kiliwasitiri jua lisiwapate, wakajinyosha kwa raha huku matumbo yao yanakifanya kazi chakula walichopakia usiku kucha.

Akatokea Mwidini Ugama, dume barabara mweusi kama Mnubi, akafumua kivumbi kwa kumtia simba moja risasi ya kichwa. Simba akaanguka chini pu, amekwisha kufa fo fo fo, naye simba dume, mkubwa kweli kweli. Ndipo simba jike akawaendea jamaa wale waliokosa miti ya kupanda, upesi wakajitupa majini wakaogelea hadi kwenye maji mengi. Mwarabu mmoja, Seleimani Bin Saidi, akarukia peupe mauser (bunduki) yake tayari, akampiga simba risasi ya ubongo.

Wanaume hawakupiga vigelegele, bali wakawapa mkono wenzao waliowamaliza simba baa wale. Tena kila mmoja akaanza kuhadithia alivyomwuulia mbali mnyama mbaya fulani, hadi mwisho hawakusikilizana kamwe, pakawa wasimulizi tu, wasikilizaji hakuna. Wakapiga domo, mwisho wakachoka ndipo wakakata mipiko na vijiti kwani mikoko tayari pale pale, wakaifunga mizoga ya simba, mahodari wakaogelea nayo hadi ng’ambo ya pili; wanaume kumi na sita wakaichukua mizoga kwani kila mzoga ulihitaji nguvu za watu wanane; wakaingia kijiji cha Mbwera. Hapo mizoga ikachunwa, shahamu ikatolewa, ikawekwa akiba vizuri kwani ni dawa, mtu kijijini akiugua iko tayari, itampa nafuu.

Usiku fisi akaja akainyakua ngozi ya simba mmoja; ilitundikwa ipate kukauka. Pia asubuhi zilionekana nyayo za simba mkubwa kuliko hao waliouawa; alifika kunusanusa ngozi na mizoga ya wenzake.

Halafu simba huyo akaenda kushambulia zili la bwana mmoja, Abudurahamani, akawaua na kuwala kondoo watatu, tena kwa fujo tu akawaua wawili wengine wala hakuwala. Lakini hakuwagusa kamwe ng’ombe wala mbuzi waliokuwamo mle mle zizini. Alfajiri na mapema Waarabu wawili na wenyeji wawili wakazifuata nyayo za simba hadi mwenye matope matope na maji maji mikokoni. Katika kisiwa kidogo karibu na mitende mwitu wakamgundua simba amestarehe anamla kondoo aliyemleta hapo.

Mwenyeji mmoja akampiga simba risasi ya tumbo. Mnyama mkali akaanguka chini pu lakini mara akainuka tena, huyo akakimbilia upande wa kihori chenye maji mengi na matope matope kiitwacho Nyatoti. Hao mabwana wanne na bunduki zao wakamfuata upesi upesi, wakamwahi, kwani walimkuta simba akiogelea kihorini. Wakampiga risasi za kichwa na mabega hadi mzee simba akaiaga dunia pale pale. Mtumbwi ukaletwa, mzoga ukakokotwa mpaka ng’ambo, ukabururwa nchi kavu, ukachunwa, watu wakaupekuapekua wakitafuta shahamu.

Ndivyo wenyeji wa Mbwera walivyowinda simba kwa muda wa siku mbili wala hakuumia mtu, hata kijeraha. Punda aliyepigwa makucha akapona baada ya siku tatu, akatoka hospitali, yaani pale sebuleni, akarudi kwao, mambo makubwa yaliyompata hayakumharibia siha yake, na mnyororo wake ukaungwa na mfua chuma wa pale mtaani.
 
Hiki kisa kinapatikana ndani ya kitabu Masimulizi ya Mtawa Maporini kitabu cha kwanza. Kinaelezea jinsi watu wa Rufiji walivyowinda simba. win-one

Simba Wanavyowindwa Rufiji​

Tangu mtawa maporini amefika hapa Rufiji Delta ameyajua mambo mawili yasiyojulikana na binadamu kama yapasavyo kujulikana. Lakini kwanza hebu niseme ya kuwa watu wengi wa Dar es Salaam hudhania Rufiji Delta ndiyo jimbo zima la Rufiji, sivyo kabisa; lakini katika sehemu mbalimbali za dola yetu wako watu waliomo gizani kama hao jamaa wa Dar es Salaam kwani wanafikiri nchi za Afrika ya Mashariki, hata zile za Afrika ya Magharibi zote zinahesabika katika nchi za Afrika ya Kusini. Niyarudie mambo hayo mawili: mosi, kima huogelea katika hori zenye maji marefu wakitoka ng’ambo hii hadi ya pili; huogelea kama mbwa. Vile wavulana wapendavyo kuogeleaogelea hali kadhalika kima hao. Pili, simba vilevile huogelea toka kisiwa kimoja hadi cha pili ikiwa hawawezi kuvuka kwa sababu yapo maji mengi katikati hata wakati wa maji mafu. Simba huwasaka nguruwe mwitu. Wasipowapata nguruwe wa kuwashibisha ndipo simba wanapoyashambulia mazizi na kuwanyakua ng’ombe au huwasomba punda wabeba nazi za bwana zao Waarabu. Basi nasimulia hadithi ya kweli.

Yupo kijana mmoja wa Kiarabu jina lake Saidi bin Nasoro akaaye katika kisiwa cha Mbwera kilichopambwa na minazi, kila utupapo macho minazi chekwa; kisiwa hiki kipo katika Rufiji Delta. Basi usiku wa manane kijana huyu akazinduka usingizini akalikamata jambia lake na torch yaani kurunzi ndogo. Punda wake aliyefungiwa mnazini kwa mnyororo alikuwa akilia kwa hofu kali; tena bwana Saidi hakuwa na mwingine, huyo huyo tu wa kumbebea mbata mpaka sokoni. Mwarabu akadhania nyoka au chatu anamtisha au anamsumbua punda wake. Mkewe na watoto, mmoja wa kiume mwingine wa kike, wakamfuata nje, kwani walikuwa na hamu ya kukiona kitu hicho pia walitaka kumtetea punda wao asidhurike,

Nuru ya kurunzi ikaonyesha kitisho kweli kweli. Simba wawili walikuwa wakimpiga punda makucha, na masikani punda kukimbia hawezi kwani amefungwa kwa mnyororo, Saidi akawaambia mke na watoto, “Upesi ingieni ndani: mke wangu, niletee mauser (bunduki) yangu.’ Wakaingia katika nyumba ndogo iliyoezekwa kwa makuti.

Punde si punde akapewa bunduki yake, akaiweka mikononi, akajiona naam sina hofu sasa; lakini punda zamani ameukata mnyororo, yumo mbioni katika shamba la minazi, kipande cha mnyororo kinaburura nyuma, simba wanamfukuza kweli kweli. Na Mwarabu akafuata, mauser mkono mmoja, kurunzi mkono wa pili; akakimbia, akakimbia wee maili mbili nzima, akiyafuata makelele ya simba washambuliao na punda awakimbiaye, akapafikia mahali pa Mwarabu mwingine, Ali bin Saidi. Akapapita, anazidi kufuata. Pengine aliposikia kimya, akaiwasha kurunzi yake, akaangaza chini akizifuata nyayo zilizoonekana dhahiri kwani ardhi ilikuwa ya mchanga mchanga na nyasi fupi fupi tu. Akapaza sauti akiwalani simba na kuwaambia, “Mkimmmaliza punda wangu mtanitambua.” Mara akaifikia nyumba ya kaka yake; nyumba hii pia imezungukwa na minazi. Sebuteni akamwona punda wake amelala anatweta, mikwaruzo mwili mzima lakini angali hai. Hapo kale katika nchi ya Uingereza alikuwako mcha Mungu mmoja jina lake Thomas Becket; basi alipojiona ametingwa na maadui walioazimia kumwuulia mbali akajitupa madhabahuni kanisani; hali kadhalika huyu punda, akajitupa masikani pa kaka yake bwana wake aokoke. Akatibiwa utibabu wa vivyo hivyo, bali ulimfaa; akashonwa kila alipochanwachanwa na makucha ya simba, akapakwa chumvi na buluu damu zisizidi kumtiririka.

Alfajiri na mapema Saidi akamwambia boi yake Msenga bin Mpiringu “Nenda ukamwombe jumbe awaamuru watu wake waipige ngoma ya kuwaarifu wenyeji ya kuwa leo ni leo, wanaume kweli watokee.” Kusikia mdundo wakatokea kweli, wanaume labda sitini na bunduki za marisau na mikuki kadha wa kadha.

Saidi akakiongoza kikosi hiki, wakazifuata nyayo za simba wakaenda, wakaenda mpaka wakafika penye kihori chenye kingo za matope yasiyo na kina. Hapo simba walivuka kwenda masikani kwao, yaani walalapo mchana kutwa. Wakati walipovuka simba hapakuwa maji, yalikupwa; bali walipofika akina bwana Saidi wakakuta yamekwisha jaa yana kina cha futi kumi nzima. Tena mamba wengi huishi majini humo. Lakini wenyeji wa Rufiji wana umoja sana katika kupigana na wanyama mwitu ambao ni maadui zao; wakiachiliwa nguvu zao zitazidi, wataweza kuwasumbua watu hadi washindwe kukaa kwa raha hapo wanapoishi wao na walipoishi babu zao.

Basi wote wakaanza kuvuka kwa kuogelea. Vita ya Omdurman yasemekana kwani askari walionyesha ushujaa na umoja; hali kadhalika hapa katika hawa watu wa hadithi yetu. Walikuwapo vijana wawili wasiojua kuogelea, lakini wakajaribu vivyo hivyo kuvuka; maji yakawaingia puani, mengine wakayameza, wakapiga mayowe, “Jamani, maji yanatuaa,” wakazama. Wenzao wakawacheka sana kwani pande za Rufiji wasiojua kuogelea wanadharauliwa sana. Walipokwisha kutapatapa majini wenzao wawili wakawaokoa, wakawalaza matopeni ng’ambo ya pili, masikini wakaanza kutapika na kukohoa moja kwa moja, na wote wengine wakaangua kicheko tena.

Kwa gafla vicheko vikakoma. Yadi kumi na mbili tu toka hapo walipokuwa watu palikuwa mti mkubwa wenye matawi mengi yaliyosambaa huku na huku na shina la mti laini kabisa. Halina magamba magamba kama shina la mwembe, chini paliota nyasi fupi fupi; basi mahali hapo wakainuka simba wawili. Walivyohadithia jamaa baadaye wavulana wengine kuwaona simba hawakujitambua kwa hofu, wakasema lugha isiyofahamika.

Mara jamaa wakaiparamia mikoko dhaifu iliyoota karibu karibu, hadi msomaji wangu ungalipata kwa mbali dakika hiyo ungalifikiri hivi: “Lo, ama kweli ndege wamejenga mji humo mikokoni”; lakini ndege hao hawakuwa na mbawa wala manyoya, bali walikuwa na miguu na wengine walikuwa na ndevu, na wengine bado hazijawaota. Watu wachache wakakosa miti ya kuparamia, yote imekwisha jaa. Wale waliokuwako mitini walipotulia hadi wakaweza kuangaza wakagundua ya kuwa mahali pale ni kisiwa kidogo kiasi chake chapata sehemu kumi na sita kwa moja (1/16) ya eka (acre). Kisiwa hicho kilizungukwa na maji ya hori zilizoenea pote; hakika simba wale walichagua mahali pazuri pa kufichama mchana kutwa. Kivuli cha mti mkubwa ule kiliwasitiri jua lisiwapate, wakajinyosha kwa raha huku matumbo yao yanakifanya kazi chakula walichopakia usiku kucha.

Akatokea Mwidini Ugama, dume barabara mweusi kama Mnubi, akafumua kivumbi kwa kumtia simba moja risasi ya kichwa. Simba akaanguka chini pu, amekwisha kufa fo fo fo, naye simba dume, mkubwa kweli kweli. Ndipo simba jike akawaendea jamaa wale waliokosa miti ya kupanda, upesi wakajitupa majini wakaogelea hadi kwenye maji mengi. Mwarabu mmoja, Seleimani Bin Saidi, akarukia peupe mauser (bunduki) yake tayari, akampiga simba risasi ya ubongo.

Wanaume hawakupiga vigelegele, bali wakawapa mkono wenzao waliowamaliza simba baa wale. Tena kila mmoja akaanza kuhadithia alivyomwuulia mbali mnyama mbaya fulani, hadi mwisho hawakusikilizana kamwe, pakawa wasimulizi tu, wasikilizaji hakuna. Wakapiga domo, mwisho wakachoka ndipo wakakata mipiko na vijiti kwani mikoko tayari pale pale, wakaifunga mizoga ya simba, mahodari wakaogelea nayo hadi ng’ambo ya pili; wanaume kumi na sita wakaichukua mizoga kwani kila mzoga ulihitaji nguvu za watu wanane; wakaingia kijiji cha Mbwera. Hapo mizoga ikachunwa, shahamu ikatolewa, ikawekwa akiba vizuri kwani ni dawa, mtu kijijini akiugua iko tayari, itampa nafuu.

Usiku fisi akaja akainyakua ngozi ya simba mmoja; ilitundikwa ipate kukauka. Pia asubuhi zilionekana nyayo za simba mkubwa kuliko hao waliouawa; alifika kunusanusa ngozi na mizoga ya wenzake.

Halafu simba huyo akaenda kushambulia zili la bwana mmoja, Abudurahamani, akawaua na kuwala kondoo watatu, tena kwa fujo tu akawaua wawili wengine wala hakuwala. Lakini hakuwagusa kamwe ng’ombe wala mbuzi waliokuwamo mle mle zizini. Alfajiri na mapema Waarabu wawili na wenyeji wawili wakazifuata nyayo za simba hadi mwenye matope matope na maji maji mikokoni. Katika kisiwa kidogo karibu na mitende mwitu wakamgundua simba amestarehe anamla kondoo aliyemleta hapo.

Mwenyeji mmoja akampiga simba risasi ya tumbo. Mnyama mkali akaanguka chini pu lakini mara akainuka tena, huyo akakimbilia upande wa kihori chenye maji mengi na matope matope kiitwacho Nyatoti. Hao mabwana wanne na bunduki zao wakamfuata upesi upesi, wakamwahi, kwani walimkuta simba akiogelea kihorini. Wakampiga risasi za kichwa na mabega hadi mzee simba akaiaga dunia pale pale. Mtumbwi ukaletwa, mzoga ukakokotwa mpaka ng’ambo, ukabururwa nchi kavu, ukachunwa, watu wakaupekuapekua wakitafuta shahamu.

Ndivyo wenyeji wa Mbwera walivyowinda simba kwa muda wa siku mbili wala hakuumia mtu, hata kijeraha. Punda aliyepigwa makucha akapona baada ya siku tatu, akatoka hospitali, yaani pale sebuleni, akarudi kwao, mambo makubwa yaliyompata hayakumharibia siha yake, na mnyororo wake ukaungwa na mfua chuma wa pale mtaani.
kwahiyo mpka saivi huko rufijj kunao hao simb? au waliuwawa wote wakaisha
 
Back
Top Bottom