CABO-DELGADO-PART 29
Akakaa kitambo kifupi akifikiria mbinu nyingine ya kufanya, akaamua aanze kuvingirika kuelekea kwenye pipa la takataka. Matarajio yake huko yalikuwa huenda akakuta mkasi umetupwa ili ukiwepo aubane kwenye meno kisha autumie kukatia kamba ya mikononi. Akajipa matumaini atapata kifaa cha kujifungua.
"Kwa namna Dr.Anabella alivyokuwa anatupa kitu kwenye pipa, alivyoniangalia sana ile ni ishara kuna kitu cha kuniokoa aliniwekea" mawazo chanya yalipita kwenye fikra zake. Akaanza kujisogeza huku jasho linamtiririka mwilini kama maji kutokana na joto la mule selo.
Alipokuwa yupo karibu na nusu kufikia kwenye pipa la taka, ghafla akasikia vishindo vya mabaradhuli wanakuja selo kuu, hapo hapo akaanza kukata tamaa ya kutoroka akajua amekwisha wanakuja kumchukua. "Lakini mbona mapema sana wanakuja kunichukua kulikoni!" aliwaza sana Kachero Manu. Akaanza kusali sala maarufu kwa Wakatoliki, ya Baba yetu wa mbinguni akijua hapa tena hana ujanja alishakubali shingo upande kushindwa na maadui zake. Wakati amefunga macho yako yuko katika hisia nzito ghafla lango likafunguliwa wakaingia mabaradhuli wawili wapya ambao hawafahamu wakiwa wamembeba mzobe mzobe mtu mmoja.
Alikuwa ni shaibu wa makamo hakosi miaka 55 kwenda juu ukimkadiria. Alikuwa kirambi cha mtu, mfupi kama mbirikimo ana tumbo kubwa ambalo linatokana na ulaji mbovu wa vyakula na uvivu wa mazoezi na kujisaidia haja kubwa mara kwa mara. Cha kusikitisha huyu Mzee alikuwa yupo uchi wa mnyama analia kwa sauti mbaya kama ya punda kilongwe wa majumbani. Alitoa kilio mpaka sauti yake ikampwelea kabisa.
Walipoingia wale mabaradhuli hawakumjali kabisa Kachero Manu ambaye alijikunyata na kujifanya tongo hajui chochote kinachoendelea. Wakamfunga juu kwa juu yule Mzee kama nyama ya mbuzi wa ndafu anayesubiri kuliwa na maharusi. Mzee wa watu ukawa inamtoka mikojo ya uoga mfululizo utasema anaumwa ugonjwa wa kisukari hawezi kujizuia mkojo, au anaumwa ugonjwa unaoitwa nasuri uwapatao akina mama waliotoboka tundu la mkojo maarufu mtaani kama fisitula.
Kumbe kihoro chake ni cha uoga wa kifo cha kishenzi na cha kidhalili ugenini. Kachero Manu akawa anajichekea kimoyo moyo kuwa huyu Mzee atakuwa yupo ndani ya kumi bora ya watu waoga duniani. Kisha walivyomfunga wakamuacha anabembea huku kichwa kinaning'inia halafu wakafunga mlango na kuondoka. Mzee uso wake ulivimba vimba kidogo ulikuwa na manundu, inaonyesha alikuwa kuna kitu anakaidi kutekeleza wakamnasa mambata ya haja ya usoni. Na mdomo wa chini ulipasuka kidogo ukawa unamwaga damu.
Kachero Manu akavuta taswira ya huyu Mzee, akili yake ikamwambia kuwa anamfahamu vilivyo tena anamjua sana na ni mtu maarufu ila tu kupondeka kwa sura yake ikawa sura inaingia na kuondoka. Mwishowe Kachero Manu akaanza kuangua kicheko cha sauti kubwa na dharau mpaka Mzee wa watu akaanza kuogopa kuwa huenda kaletwa gereza la vichaa.
"Kumbe ni Mzee Andenga Kazimoto, kaletwa selo kuu, kazi ipo mwaka huu" alijiwazia baada ya kumtambua. Waswahili walisema "shukrani ya punda ni mateke. Amekipata alichokitafuta kwa mafia Alfredo. Inaonyesha Alfredo kaona hana umuhimu wa kuingia kwenye kikao wakati nyaraka wameshazipata" akazidi kuwaza Kachero Manu.
Kweli tamaa ilimuua fisi, 'kakosa mwana na maji ya moto'. Maana kwa Cheo cha huyu Mzee Andenga, alikuwa amebakiza miaka michache ya kustaafu angepata kiinua mgongo na pensheni nzuri tu ya kula na familia yake mpaka mwisho wa uhai wake.















"Komandoo Mstaafu uso kwa uso na NACATANAS"
Komandoo mstaafu Jacob Steven (JS) alipofanikiwa kugundua gari lililowapeleka akina Kachero Manu 'Gorongosa Camp', akaenda moja kwa moja kwenye kampuni ya helikopta ya kukodisha ili aelekee Gongorosa kumkomboa kijana wake.
Masaa matatu tu ya kufa au kupona yalikuwa yamebaki kabla ya Kachero Manu kuletwa kiwanda cha Korosho cha Monte Branco Ltd. Ilitakiwa komandoo 'JS' atumie 'kipawa cha liwa kutibu harara', afanye vyovyote iwavyo amnasue kijana wake. Kama angekwenda na gari asingeweza kufika wakati muafaka wa kuweza kumuokoa.
Umbali wa kutoka Pemba mpaka Gongorosa ni kama kutoka Dar esalaam mpaka Mbeya kwenda na kurudi. Eneo la Gongorosa lipo jimbo la kati la Sofala zaidi ya kilometa 1635.
Bahati nzuri akapata nafasi kwenye helikopta hiyo ya kukodi inayoelekea "Gongorosa National Park" (GNP) inayopeleka watalii mbugani. Mpaka saa 11 jioni akawa ameshawasili Gongorosa. Sasa kilichokuwa kinachomsumbua kichwani mwake ni kufahamu Kachero Manu kafichwa wapi?. Maana ni sawa na mwenyeji wako akuambie nipo Dar es salaam, lakini Sinza, Manzese, Mbagala, Kawe, Goba, Mbezi, Rehema, Masaki zote ni Dar es Salaam. Lakini bado hata ukifahamu ni Sinza bado Sinza ni kubwa sana, Kwa Remmy, Kumekucha, Palestina, Madukani, Shekilango bado vyote hivyo ni vitongoji vya Sinza.
Akaumiza kichwa akapata jawabu ni kuuliza wapi kuna Ukumbi wa starehe maarufu kuliko zote, huko ndio atapata majibu. Maana haiwezekani viongozi wa Gorongosa Camp wanaolipwa pesa nzuri sana washindwe kustarehe. Tabia za watu majambazi na maharamia ni kustarehe sana, ndio maana pesa wanazopata hazina fidi. Ukitaka kumsaka mtu swalihina basi ni kwenye nyumba ya ibada, lakini mtu fedhuli pesa zake huwa zinaishia kwenye pombe, muziki na kustarehe na vidosho.
Akauliza uliza kwa wenyeji klabu za fauka kwa starehe, wengi wao walimtajia kiwanja cha kisasa cha kujivinjari ukiwa Gongorosa kinaitwa "Montebelo Pub". Akafanikiwa kufika "Montebelo Pub" anayasoma mazingira.
Ilikuwa ni "Pub" yenye kuvutia kimazingira, ilijengwa ikajengeka vilivyo. Geti la kuingilia lilipambwa na bango kubwa lenye maandishi makubwa lililoandikwa jina la "Montebelo Pub". Kisha ilizungukwa na fensi fupi ya ukuta iliyopandwa miti iliyoshonana kuzunguka ukuta wote. Kwa ndani kulikuwa na midule mingi mingi iliyozungukwa ukumbi mzima kwa umbo la duara huku katikati kukiwa na ukumbi wa wazi uliozibwa kwa paa la makuti yanayotokana na mti wa mnazi.
Pia kulikuwa na wahudumu ambao ni wasichana wabichi na vipusa ambao wengi wao wapo katika rika la kufanana la kuanzia miaka 20 mpaka 25 wakiwa wamevalia mavazi yao ya sare za minisketi zenye kuacha sehemu kubwa ya mapaja yao nje nje bila kufunikwa vizuri, juu wana fulana nyeupe zilizowabana na kuzichongoa vilivyo chuchu zao konzi.
Alipoingia alikuta nje kuna magari mengi ya kifahari yameegeshwa kwenye maegesho kuonyesha kuwa ni "Pub" ya watu wazito wa Mji. Alipofika akachagua meza iliyokaribu na ukumbi wa kutumbuizia akavuta kiti na kukaa. Maana kulikuwa na "LIVE BAND" kutoka kwenye bendi maarufu ya "DJAAKA BAND".
Hiyo ni bendi ya muziki ya vijana wa Jimboni hapo hapo la Sofala. Bendi hiyo iliwahi kushinda tuzo ya "Crossroads in Southern Africa mwaka 2001. Watu walijaa pomoni kuja kuwaona vijana wao wakiwa wamerudi toka ziara za kimuziki nchi za ng'ambo za Uholanzi na Denmark ambapo walikuwa wamekaa huko zaidi ya mwezi mmoja huko Ughaibuni.
Alipotulia kwenye kiti akaja dada mmoja mrefu kavalia sare ambazo zilikuwa zinamtambulisha kuwa ni mhudumu wa hapo akiwa ameshika karatasi ngumu ya "MENU za aina na bei za vyakula na vinywaji" alipofika karibu na Komandoo mstaafu akamsalimia kwa unyenyekevu kisha akamkaribisha na kumpa Komandoo Jacob Steven (JS) ile karatasi ya orodha ya vinywaji na vyakula.
Komandoo akaipokea na kuisoma kimya kimya kisha akamwambia mhudumu "Naomba uniletee "Limoncello" ya baridi sana na maji ya moto ya kuzimulia tafadhali" alisisitiza Komandoo Jacob.
"Limoncello" kilikuwa ni kinywaji kimachotengenezwa kwa kutumia ndimu. Asili yake kinywaji hiki ni Italia ya kusini. Yule mhudumu akawa anaondoka kuelekea kaunta huku anatembea kwa madahiro huku anatikisa makalio yake kiufundi anayapandisha juu na kuyashusha kwa kuyapishanisha. Lakini madahiro hayo hayakumzuzua komandoo 'JS' alishazoea kukutana na vishawishi vya warembo mbalimbali tena wa nchi mbalimbali duniani. Akili yake ilikuwa inawaza kazi tu kwa sasa sio kitu kingine alitambua mshika mawili moja humponyoka.
Baada ya dakika kama tano, yule mhudumu akawa amesharudi mezani kwa Komandoo Jacob, wakati yule mhudumu anasaidia kumfungulia kinywaji komandoo ghafla umati wa watu wakawa wanashangilia kwa nderemo na vifijo huku macho yao yanaelekea mlango wa kuingilia. Kulikuwa na kipande cha mtu kibushuti mfupi kanyoa upara kichwani anatembea mguu mmoja kama mfupi huku amevaa miwani nyeusi, na pembezoni ana wapambe kama wawili wamenyoa nywele zao katika mtindo wa kishungi wanamsindikiza. Miondoko yao ilitambulisha kuwa ni watu mafedhuri na wajuba.
Huyu jamaa ndio yule aliyemtesa Kachero Manu katika handaki la mateso la "Gongorosa Camp" siku ya kwanza alivyopelekwa. Wakapita jirani kabisa na meza ya Komandoo Jacob kisha wakasogea jirani na meza ya kaunta ya "Pub".
Walipopita tu Komandoo Jacob akapatwa na hisia hawa ni mabaradhuli wa tabia sio watu wazuri hata kidogo. Akakata shauri amuulize yule dada mhudumu, "samahani mwanangu huyu ni nani aliyeingia hapa hivi sasa, naona watu wanashangilia kama mpira". Akaongea kwa sauti ya kumnong'oneza yule mhudumu.
"Babu wewe ni mgeni kumbee, yatakukuta mambo usiingie ngomani ukashindwa kuicheza bure, huyo ndio "Bob Chinanga" tunaskia tu ni Bosi wa kambi inayosemekana ni ya Usalama wa Taifa, anaogopwa zaidi ya kifo kinavyoogopwa hapa Sofala..!". Kisha haraka haraka akaondoka yule mhudumu kwa mwendo wa madaha akiwafuata wateja wengine aweze kuwahudumia.
Komandoo 'JS' akawa anaendelea kunywa kinywaji chake huku anafuatilia nyendo za yule "Bob-Chinanga", jitu katili lenye kuogopwa. Wakati muziki wa bendi unazidi kupamba moto, akamuona yule "Bob Chinanga anaelekea stejini kuwatunza pesa wanamuziki wa bendi huku wanamtaja taja jina na kumsifia sifia maneno ya kumpamba kama vile "Boob-Chinanga baba ya mapesa mengi, mlezi wa wana" na maneno kedekede ya kumsifu na kumpaka mafuta kwa mgongo wa chupa, ili mradi wamle pesa zake.
Alikuwa anawapa pesa za kigeni mfano wa dola au paundi maana stejini kulikuwa na mwanga khafifu. Kilichomshangaza Komandoo Jacob no kumuuona yupo peke yake wale wapambe wake wawili hawapo.
Akajiuliza wameenda wapi, kengele ya tahadhari ikagonga kichwani mwake akahisi kuna jambo wanafanya wale wapambe wake. Alipotupa macho kwenye meza waliyokuwa wamekaa hakuona mtu zaidi ya msitu wa bia zilizoachwa bila kuwa na mnywaji. Machale yakamcheza akaamua anyanyuke aende chooni huenda atakutana nao huko halafu atajua mbivu na mbichi wakikutana huko huko. Akanyanyuka kuelekea uelekeo wa chooni, huku akiiweka vizuri bastola yake yenye kiwambo cha kuzuia sauti.
Alipofika karibu na vyoo vya wanawake akasita kidogo kwenda, akawa anasikia kama kuna sauti ya kike inalalamika kwa maumivu makali. Akaichomoa kiunoni bastola yake tayari kwa matumizi itakapobidi. Akaanza kujongea taratibu akawa sasa amekaribia kabisa anaskia sauti ya mtu anayeugulia maumivu. "Naku....f...waaaa nisa..i... di... eeee...!" akakaza mwendo kusogelea inapotokea ile sauti.
Lahaula! alitanabahi kuwa yule dada mhudumu wa "Pub" aliyempa huduma ya kinywaji amechomwa kisu cha kwenye titi la kushoto, kimepenya kisawa sawa chini ya ziwa huku damu zinachuruzika kama bomba la maji la DAWASCO lililopasuka mtaani kutokana na shinikizo kubwa la maji. Akamfikia akamshika kichwani kwenye nywele zake na kuanza kumhoji.
"Umepatwa na nini mwanangu..nani kakufanyia unyama huu..."?. Akajibu yule dada kwa tabu sana huku pumzi zake za kuokoteza okoteza, "wame... n.. i...uaaa wame....ni...uli... zaaa we... we ni nanii...na nimeku....ku.... a.. mbi... a nii...ni, niokooooee pliiz". Komandoo Jacob Steven akapatwa na taharuki akajua hapa akijifanya msamaria mwema itakula kwake, atashushiwa jumba bovu la mauaji, akaondoka kama mwehu anarudi ukumbini kuwatafuta wale wapambe wa Bob Chinanga akimuacha yule dada anapigania roho yake.
Akakuta meza yao ipo tupu hawapo wameshasepa na hata Bob Chinanga mwenyewe karibu na pale stejini anapowatazama waimbaji hayupo. Haraka haraka akatoka nje ya lango la kuegesha magari, akaona kwa mbele yake kuna gari limewasha indiketa linataka kuondoka huku Bob Chinanga ndio anafungua mlango wa nyuma kuingia kwenye gari huku mkononi ameshika chupa yake ya pombe kali.
Hapo hapo akajikuta anapigiwa honi na gari aina ya "Range Rover" rangi nyeusi inataka kuegeshwa pale aliposimama Komandoo Jacob. Akili ya Komandoo ikachemka haraka haraka akaona fursa imejitokeza katika wakati muafaka, hakuondoka akazidi kulisogelea lile gari kisha ghafla akashtuka pembeni mwa upande wa mlango wa dereva, hapo hapo dereva akashusha kioo chake kisha akaanza kuporomosha bomba la matusi akamnyambua komandoo "JS" kwa kadri alivyoweza.
Komandoo Jacob hakuwa na muda wa kujibizana nae alimpa kisogo, alichofanya ni kuchomoa bastola yake na kumuamrisha yule dereva, "shuka chini haraka sana usilete utani na wanaume wakiwa kazini" alisema Komandoo Jacob huku anatishia kama anaweka sawa bastola yake kufyatua risasi. Bila ubishi yule baba cha matusi, akawa amegwaya akafungua mlango wake wa dereva. Alikuwa mpole ghafla kama "Mmasai anayesifika ushujaa wa kuua simba lakini anaogopa kula samaki eti macho ya samaki yanamtisha".
Aliposhuka tu kwenye gari yule jamaa, kufumba na kufumbua Komandoo Jacob akaingia kwenye gari na kuligeuza kuelekea uelekeo wa inapoelekea gari ya akina Bob Chinanga. Akaanza kuwakimbiza wabaya wake akina Bob Chinanga, akiwa ndani ya "Range Rover" huku wanatokomea nje ya Mji. Akimuacha yule baba wa kuporomosha matusi akiwa mikono kaweka kichwani, ametaharuki nusu majinuni hajui afanye kitu gani kuipata gari yake tena.
Sent using
Jamii Forums mobile app