mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 917
- 1,997
SURA YA KWANZA
Makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia, Kijijini Mahiwa, Lindi.
Kadamnasi ya watu walikuwa wamekusanyika wakiwa wamejikunyata vikundi vikundi. Nyuso zao zimegubikwa na majonzi na huzuni katika makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia vya kwanza, yaliyopo kijijini Mahiwa.
Kijiji ambacho kipo katika Wilaya ya Lindi Vijijini katika Mkoa wa Lindi. Waombolezaji hao walikuwa wamekusanyika katika harakati za kuhitimisha shughuli ya arobaini kutokana na msiba wa Bi.Josephina Charles Nyagali aliyezikwa kwenye makaburi hayo ya mashujaa. Ni makaburi ambayo hayatambuliki Kitaifa lakini wenyewe wenyeji wanalitambua na kulienzi kuwa ni eneo walilolazwa mashujaa wa vita vya dunia.
Anga nayo ilitandaza wingu zito, lililofunika jua utadhania nalo lilikuwa linajumuika na waombolezaji kwenye kumaliza msiba huo. Kijiji kilifurika wageni mahashumu wa ndani na nje ya nchi waliokuja kuhitimisha msiba huo. Miongoni mwa wageni hao, alikuwepo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Nchi ya Msumbiji, Mheshimiwa Allan Fernando, aliyetumwa kumwakilisha Rais wa Msumbiji katika msiba huo.
Pia alikuwepo Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa nchini Msumbiji Bwana Jacob Steven au maarufu kwa lakabu ya Komandoo 'JS' akiwa ni mteule mpya kwenye idara hiyo. Pia alikuwemo katika msafara huo toka nchini Msumbiji, Daktari Anabella Munambo akiwa ni Daktari Mkuu katika hospitali mpya ya "Quelimane Central Hospital" iliyopo katika jimbo la Zambezi. Hao walikuwa ni baadhi tu ya vigogo wazito toka msafara viongozi wa Msumbiji.
Kwa upande wa Tanzania, mkururu wa vigogo nao walifurika kijijini Mahiwa, kuanzia wa Mkoa na wa Kitaifa. Mawaziri, Makatibu Wakuu na Mkuu wa Idara ya Usalama ya Taifa Bwana Mathew Kilanga alikuwepo kundini. Wasioelewa kinachoendelea na kushangazwa na ugeni ule mzito pale kijijini walikuwa wanajiuliza bila kupata majibu.
Swali kubwa vichwani mwao lilikuwa "huyu Bi.Josephine Nyagali alikuwa ni nani haswa katika historia ya nchi ya Tanzania mpaka apate bahati ya kulazwa malaloni pamoja na wanajeshi mashujaa waliokufa katika vita vya kwanza vya dunia?". Heshima ya Bi.Josephina kuzikwa hapo, ilitokana na babu yake mzaa baba, hayati "Nyagali Wa Nyagali" aliyekuwa mpiganaji wa Jeshi la Mjerumani enzi za vita vya dunia na kuzikwa katika makaburi hayo. Vita vya Mahiwa katika ya Mjerumani na Muingereza vilipiganwa mwaka 1917.
Ambapo Jeshi la Mjerumani likiongozwa na Jenerali Paul Emil von Lettow-Vorbeck walichuana vikali na Jeshi la Muingereza likiwa chini ya uongozi wa Luteni Jenerali Jacob van Deventer. Vita hivyo vya Mahiwa vilisababisha vifo vya askari si chini ya 2,000 wengi wao wakiwa ni Wanajeshi wa upande wa Uingereza. Katika baadhi ya Wanajeshi waliofariki, babu yake Bi Josephina, Koplo Nyagali Wa Nyagali nae alikuwemo, akabahatika kuzikwa eneo hilo na baadhi ya wanajeshi wachache waliozikwa hapo.
Pia mtoto wake Bi.Josephina, Kachero Manu ndio ambaye alipendekeza mama yake mzazi azikwe hapo kando ya kaburi la babu yake mzaa mama, kwenye eneo ambalo hata yeye Kachero Manu atakavyofariki atapendelea azikwe hapo. Muda wote wa shughuli hiyo Dr.Anabella, Kachero Manu na Komandoo 'JS' walikuwa hawaachani wamegandana kama kupe. Wasiowafahamu wakadhania ni watoto mapacha walioachwa na marehemu Bi.Josephina Nyagali wanafarijiana wenyewe kwa wenyewe.
La hasha..! hawakuwa na udugu wowote wa damu, ila walikuwa ni marafiki waliosafishiana moyo ambao kufahamiana kwao katika urafiki huo ulitokana na kazi pevu waliyoshirikiana kuifanya siku chache zilizopita huko nchini Msumbiji. Dr.Anabella alishindwa kuyazuia machozi yake wakati anaweka shada la maua juu ya kaburi la Bi.Josephina. Alivuta taswira jinsi mama yake na baba yake mzazi na nduguze walivyochinjwa kikatili shingo zao na wahusika hao hao waliopoteza uhai wa mama mzazi wa rafiki yake.
Wote watatu walikuwa wanafarijiana na kumpoza mpambanaji mwenzao Kachero Manu aliyefikwa na maswahibu mazito. Kachero ambaye alifiwa na mama yake mzazi kwa kuchinjwa kikatili na mahasimu zake toka nchini Msumbiji katika usiku wa kuamkia siku ya Wapendanao "Valentine Day" ya mwaka 2016. Yeye hakuwahi kuhudhuria mazishi ya mama yake kwa sababu alikuwa na safari ya muhimu sana ya kikazi nchini Msumbiji isiyowezekana kughairishwa kwa sababu yoyote ile. Hivyo alivyorejea toka safarini, ikabidi aunganishe moja kwa moja Kijijini kwao Mahiwa kwenye maandalizi ya arobaini ya kuhitimisha msiba wa mama yake.
Kwa uzalendo wake huo wa kukubali kukacha kushiriki msiba wa mama yake mzazi kwa ajili ya kujitoa mhanga kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Msumbiji, ndio maana nchi ya Msumbiji na Tanzania kwa ujumla wakaipa uzito shughuli hiyo kwa kutuma wawakilishi wao wazito. Baada ya shughuli zote zilizopangwa kufanyika hapo makaburini kuhitimishwa, na kuashiria msiba huo kumalizika kwa kupanda msalaba juu ya kaburi la marehemu, msafara huo ukarejea nyumbani kwao Kachero Manu kwa ajili ya kutoa rambirambi zao.
Mpaka kufikia majira ya saa 12:30 magharibi shughuli zote zikawa zimehitimishwa na wageni mbalimbali wakaanza kurudi kwenye makazi yao waliyofikia kabla ya kurejea makwao.
"Mbona huufanyii kazi msemo wa waswahili ule wa Mgeni njoo Mwenyeji apone, unaniacha mrembo naenda kulala peke yangu Mjane mimi, wewe wa wapi wewe....!" alisema Dr.Anabella kiutani, akimpa shutuma rafiki yake Kachero Manu wakati tayari anajiandaa kupanda gari aliloandaliwa na serikali tayari kwa kuondoka. "Ng'ombe wa kuazima anakamuliwa wima, nisingekuacha bahati yako mmiliki yupo hapa msibani anakaba mpaka penati, hapa alipo amefura kwa hasira, wivu juu yako..!" alijibiwa Dr.Anabella huku akipewa tahadhari ya kuwa makini na mchumba wake Kachero Manu, Faith Magayane.
"Kwaheri...niagie kwa niaba yangu, maana asubuhi nimemsalimia kaninunia utasema mie mke mwenza wake, na Wamakonde tunavyoogopeka kwenye sekta ya chumbani, alipo hana amani kabisa na mimi...!" alisema Dr.Anabella, huku wakikumbatiana kwa sekunde kadhaa na Kachero Manu nyuso zao zikiwa na bashasha mpwito mpwito kisha akapanda kwenye gari na kuondoka msibani.
Komandoo JS alikuwa amejitenga kando wanapeana michapo na mkongwe mwenzake Bosi Mathew Kilanga. Hawa walikuwa ni maswahiba wakongwe waliofanya pamoja mafunzo ya Ukomandoo na sasa wote ni Wakuu wa Idara za Usalama wa Taifa, katika nchi za Msumbiji na Tanzania.
Kachero Manu akawaacha waendelee kusogoa na kukumbushiana enzi zao, na kuamua kujumuika na familia yake wakiendelea kubadilishana mawazo mbalimbali. Giza likazidi kutanda eneo ile na watu wa karibu kuanza kurejea majumbani kwao na wa mbali kuondoka zao ili maisha ya kawaida yapate kuendelea.
Februari ya huzuni na majonzi
"Piga risasi wale kule wanakimbia, fanya haraka sana hamna kuwaonea huruma manyang'au hawa. Hamna kuwachekea wezi wa rasilimali za nchi yetu ya Msumbiji" ova ova. "Sawa mkuu tutawapa kipigo cha mbwa koko" ova ova ". Msiache majeruhi hakikisheni vizuri wafe mara moja hatuna bajeti ya kutibu majeruhi, na hakikisheni mizoga mnawafukia katika mahandaki kuficha ushahidi ova ova".
Yalikuwa ni maelekezo ya kwenye redio za upepo baina ya Afisa Mkuu, Operesheni maalumu ya kutokomeza wahamiaji haramu kwenye jimbo la Cabo-Delgado, Inspekta Jenerali Mark Noble kwenda kwa askari wake waliokuwa wametawanywa mitaani kuwashughulikia wahamiaji hao. Milio ya risasi na mabomu ya machozi yalisikika kwenye kila kichochoro cha kijiji cha Namanhumbire, kilichopo kilometa 30, mashariki mwa Jimbo la Cabo-Delgado.
Hakuna mhusika waliyemkusudia kwenye operesheni hiyo aliyesalimika, wote walikumbwa na dhahama na sekeseke hilo. Balaa na belua kubwa ilizuka ndani ya Jimbo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini ya rubi. Magari ya polisi yakiwa yamejaza polisi idadi ya kutosha yalikuwa yanaranda mitaani pamoja na magari maalumu ya kumwaga maji ya kuwasha kwa waandamanaji nayo yalikuwepo, yamekaa mkao wa tayari tayari kwa lolote.
Msako wa mtaa hadi mtaa, nyumba hadi nyumba, chumba hadi chumba, duka hadi duka ulikuwa unaendelea kuwabaini hao wanaoitwa wahamiaji haramu. Ving'ora vya magari ya polisi vyenye sauti ya kuogofya vilikuwa vinasikika kila kona. Cha kushangaza zaidi kwenye msako huo walengwa wakuu hawakuwa raia wa mataifa mengine bali walikuwa ni Watanzania.
Tena wengi wao ni wale wanaoishi kwa kufuata sheria za nchi kwa kupata viza ya kuingia Msumbiji na pia wakapata hati za ukazi. Mpaka kufikia majira ya saa tano usiku ya siku hiyo tayari mamia ya watu walikuwa wamefariki na wengine kujeruhiwa vibaya. Akina mama nao walikuwa wahanga wa uhalifu huo, wakajikuta wamebakwa hobelahobela na askari hao. Watoto wadogo wakajikuta wengine wao wamekuwa mayatima bila kutarajia. Mali za thamani kubwa zinazomilikiwa na Watanzania hao zikaporwa na askari hao madhalimu. Wale majeruhi waliosalimika wakapokonywa nyaraka zao muhimu kama vitambulisho na hati za kusafiria ili waonekane waliingia Msumbiji kwa kuzamia bila kufuata sheria.
Ili kuficha takwimu halisi za waliofariki, maiti hizo zilikusanywa na kuzikwa kwenye kaburi la pamoja la halaiki ili kupoteza ushahidi wa unyama uliofanyika. Walikuwa wanaogopa tukio lisije kuvuta macho na masikio ya wapenda haki na amani duniani, wakaanza kupaza sauti zao wakakitia kitumbua chao mchanga, wakaja kujikuta wapo kwenye mahakama ya uhalifu duniani iliyopo kule "The Hague", Uholanzi, wamepandishwa kizimbani.
Vyombo vya habari vya nchini Msumbiji vikalishwa habari potofu na Maafisa hao madhalimu walioendesha zoezi hilo haramu lenye malengo mahususi nyuma ya pazia. Wakazidi kuupotosha umma kwa kuwalisha matango pori kuwa waliouliwa ni wahalifu na wahujumu uchumi waliokuwa wanapora na kuchimba madini ya nchi ya Msumbiji kinyume na taratibu za nchi.
Wakasisitiza kuwa wahalifu hao walikuwa wamejihami kwa silaha kali za kivita, hivyo wameuliwa wakati wa mapambano ya ana kwa ana ya kurushiana risasi na wanausalama. Pongezi mbalimbali zikawa zinapeperushwa na viongozi wa juu serikalini kwa Bwana mkubwa, Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kuzihami rasilimali za nchi ya Msumbiji.
Silaha za kivita zinazosemekana kukamatwa eneo la tukio zikawa zinaonyesha kwenye runinga ili kuthibitisha umma wa Watu wa Msumbiji kuwa waliouliwa ni wahalifu wasiostahili kuonewa hata chembe ya huruma. Watanzania mamluki waliohongwa ngwenje za kutosha wakajifanyisha wamekamatwa kwenye tukio hilo, baadhi yao wakiwa wameshikishwa silaha, na kujitia wanatoa ushuhuda mbele ya vyombo vya habari kuwa walikuwa ni genge la uhalifu lililokuwa limejipanga kwa mbinu za medani za kivita, hivyo wanaomba msamaha toka vyombo vya dola.
Magazeti yakapambwa na picha za Afisa Mkuu kwenye operesheni hiyo, Inspekta Jenerali Mark Noble akisifiwa kama shujaa wa nchi, mzalendo na mfia nchi wa kiwango cha kutukuka. Mmoja wa Mawaziri waandamizi, hakubaki nyuma kubariki operesheni hiyo akatoa ahadi ya donge nono kwa askari wote walioshiriki kuwashikisha adabu wahalifu hao wa Cabo-Delgado, iwe motisha kwao kuzidi kujitolea kiuzalendo katika siku za usoni.
Watanzania wachache waliofanikiwa kutoroka kwenye sokomoko hilo, wakaja kutoa ripoti ya kina ya tukio hilo nchini Tanzania. Wakapaza sauti zao kwa kutumia vyombo vya habari, wakitaka ufanyike uchunguzi huru.
Ikabidi sasa Inspekta Jenerali wa Polisi wa Tanzania afunge safari mpaka nchini Msumbiji kwenda kuonana na Mkuu mwenzake wa Jimbo la Cabo-Delgado Bwana Mark Noble ili wayaweke sawa. Baada ya majadiliano ya karibia wiki nzima baina yao, Inspekta Jenerali wa Tanzania akarejea. Alipokanya tu ardhi,pale Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, waandishi wa habari walijikusanya wakiwa na kimuhemuhe na kiherehere cha kujua kilichojiri katika kikao hicho cha ujirani mwema baina ya vigogo hao wawili wa polisi.
"Tumekubaliana kimsingi pande zote mbili kwamba wahalifu siku zote hawana mipaka. Hii mipaka iliyowekwa na Wakoloni isitufanye tukashindwa kupambana na uhalifu na hasa haya makosa yanayovuka mipaka ni lazima tushirikiane. Na kikubwa zaidi ni kubadilishana taarifa na kufanya operesheni za pamoja, mara kwa mara” maelezo hayo mepesi ya uzani wa nyoya la kuku ya Inspekta Jenerali wa Tanzania yakaonyesha kabisa amezidiwa kete na mwenzake Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kupewa taarifa za uwongo juu ya tukio hilo.
Jambo usilolijua ni kama usiku wa giza, vijana wa Mjini wanasema "Alilishwa matango pori na kutiwa ndimu juu ya matukio hayo hatarishi". Ndugu, jamaa na marafiki wa wahanga wa tukio hilo, wakakata tamaa ya kuona haki inatendeka kwa ndugu zao walioathirika kwenye uhalifu huo. Taarifa hiyo ilibaraganya kabisa ukweli halisi wa tukio hilo, kwani ilionyesha kama vile matukio hayo hayajafanywa kabisa na polisi wa Jimbo la Cabo-Delgado, bali ni mtifuano baina ya wahalifu wa Tanzania na Msumbiji.
Wakati shuhuda za wahanga wenyewe zinasema kuwa polisi wa Cabo-Delgado ndio watuhumiwa haswa wa vitendo hivyo wakishiriki kuvilinda vikundi vya kihalifu mitaani. Mategemeo na matarajio yao waathirika wa matukio hayo yalikuwa ni kuletewa taarifa yenye fusuli ya kutosha isiyoacha hata chembe yoyote ya mashaka. Ushindi ukawa umeelemea mikononi mwa genge hilo la wahalifu lililopo ndani ya mfumo rasmi wa nchi.
Walilolikusudia genge la wahalifu ndani ya mfumo rasmi likawa limeshatimu, wakiwa wamefanikiwa kumuongopea mpaka Inspekta Jenerali wa nchi ya Tanzania. Bila kujua ya kwamba wamekumbatia waya wa umeme mkubwa vifuani mwao utawateketeza bila kuacha masalio yao.
Chambilecho "Daima hamna marefu yasiyo na ncha, na haki siku zote ni kama mfano wa boya majini, haiwezi kufichwa kwa kuzamishwa, tabia ya haki siku zote ni kuelea juu".
Idara ya Usalama wa Taifa, Tanzania ilikuwa macho kodo, haijalala usingizi wa pono. Iikuwa ipo kwenye pembe za chaki inafuatilia matukio hayo kwa umakinifu na ukaribu zaidi. Wahalifu hao walichokoza nyuki, wakati wa kukiona kilichomtoa kanga manyoya ulikuwa unakaribia kwa upande wao.
Matukio hayo ya uhalifu yanayowawinda Watanzania pekee hayakukoma. Yakazidi kushamiri na kutamalaki katika Jimbo hilo la Cabo-Delgado lenye kusifika kwa utajiri mkubwa wa madini ya rubi nchini Msumbiji.
Watanzania hao wanyonge na madhulumu hawakuwa na mtetezi wa kuwasemea na kuwaokoa. Wakawa wanapopolewa mitaani kama mbogo msituni anavyowindwa na majangili.
Likaja kutokea tukio lingine la kutisha, tukio ambalo likavifanya Vyombo vya Usalama vya Tanzania vikose simile, na kuamua sasa kwa kauli moja kuwashughulikia Mafioso wote wa Jimbo la Cabo-Delgado wanaopenda kuwachokoa Watanzania.
Ilikuwa ni tarehe 08/02/2016 ya huzuni, simanzi na majonzi makubwa kwa nchi ya Tanzania. Watanzania wapatao 16 walipigwa risasi na kufariki hapo hapo huku makumi kadhaa wakijeruhiwa wakati wakiwa kwenye maduka yao ya kubadilisha fedha za kigeni na kununulia madini, kisha wakaporwa pesa zote na madini yao.
Watanzania hawa walikuwa wakiishi na kufanya kazi katika eneo lenye madini ya rubi liitwalo Montepuez, kwenye Jimbo la Cabo Delgado kaskazini mwa nchi ya Msumbiji.
Yalikuwa ni mauaji ya kinyama na yasiyokubalika kwa jamii ya watu waliostaarabika. Mauaji ambayo yalisababisha kilio katika kila kona ya nchi ya Tanzania, Bara na Visiwani, huku wananchi wakigubikwa na simanzi isiyomithilika na joto la hasira likichemka vifuani mwao.
Lakini kabla ya mauaji hayo, wiki mbili zilizopita serikali ya eneo hilo ilitoa muda wa siku 5 kwa raia wote wa Tanzania wapatao 5,000 waishio hapo Cabo Delgado kuondoka mara moja na kurudi nchini kwao Tanzania.
Hii haikuwa taarifa yenye kupendeza hata kidogo masikioni mwa wananchi wa Tanzania, hasa wakikumbuka udugu wa asili kati ya wananchi wa Tanzania na Msumbiji. Ni kama vile kuna watu walikuwa wanachezea sega la nyuki ili kuwagombanisha ndugu wa damu walioshibana.
Ni tukio ambalo lilileta simanzi na fadhaa kubwa kwa ndugu wa wahanga na Watanzania kwa ujumla. Mikasa hio endelevu ilikusudia kuchimbia kaburini mahusiano mema baina ya hizi nchi mbili.
Ilitaka kufuta mema yote ya siku za kisogoni yaliyotendwa na Watanzania kwa watu wa Msumbiji. Watanzania wengi haikuwahi kuingia akili mwao wala katika fikra zao hata siku moja kuwa itafika siku Watanzania watatendewa unyama kama huu na ndugu zao wa Msumbiji.
Ndugu zao kabisa wa damu wanaotenganishwa tu na mipaka ya wakoloni. Katu hawakutegemea msaada wao wa asali na maziwa katika kipindi cha kupigania Uhuru wa Msumbiji kutoka kwenye makucha ya mabeberu wa Kireno malipo yake yangekuwa shubiri.
Watu wa Msumbiji baada ya kufanikiwa kumng'oa Mkoloni, wakaanza kupigana vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuzalisha maelfu wakimbizi. Bado Watanzania hawakuwafungia vioo ndugu zao, waliwakaribisha kwa mikono miwili waje nchini mwao, wakaishi nao kwa amani na utulivu. Wakashirikiana nao kutwa kucha katika shida na raha, katika mvua na jua bila utengano wowote.
Bila ya shaka tukio hili la mauaji ya watu 16 likasababisha uhusiano baina ya nchi ya Tanzania na Msumbiji kwenda zigizaga, Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake nchini Msumbiji ukawa upo makini kufuatilia na kutoa msaada unaohitajika kwa wahanga wote wa machafuko hayo.
Pia ubalozi ukajitwika jukumu zito la kuwarejesha nyumbani wahanga wote wa kadhia hii mbaya, huku wakitega sikio kusubiri tamko toka kwa viongozi wa juu wa nchi ya Msumbiji.
Lakini ukimya ukazidi kutawala toka kwenye Vyombo vya Dola vya Msumbiji utasema waliokufa ni nguruwe pori wasio na thamani yoyote.
Kwa upande wa maadui wa Umoja wa nchi za Kiafrika, chokochoko hiyo baina ya nchi ya Msumbiji na Tanzania kwao ilikuwa ni furaha sheshe.
Mabeberu hao walikuwa wanajimwashamwasha pindi wakiona nchi huru za Kiafrika zinavyogombana wenyewe kwa wenyewe.
Lengo lao kubwa ni kuona Afrika nzima inaingia kwenye machafuko ya wenyewe kwa wenyewe kama ilivyo nchi za Congo, Sudani Kusini, Afrika ya Kati, Somalia, Mali na kwingineko ili wajichotee rasilimali bwerere bila jasho.
Lengo la mabeberu hao lilikuwa ni kuziona nchi za Afrika, kamwe hazijikomboi kutoka kwenye lindi la umasikini, ujinga na maradhi.
Walitamani wawe ni nchi ombaomba na tegemezi kwao miaka nenda miaka rudi. Moto wa kuni za fitina ulishawashwa na kuchochewa na maadui, ni busara tu za viongozi wa Tanzania na Msumbiji ndizo zinalizokuwa zinahitajika kuzuia uhasama na kukatana baina ya nchi zao.
Tarehe 11/02/2016 siku 3 baada ya mauaji hayo ya Msumbiji, muda wa saa 4:30 usiku kwa majira ya saa za Afrika Mashariki, Kachero nambari wani nchini Tanzania Bwana "Manu Yoshepu" maarufu kwa lakabu ya “Mwiba wa Tasi” ndio alikuwa anaingia nyumbani kwake maeneo ya Mbezi-Juu akiwa hana hili wala lile.
Alikuwa anaishi eneo linaloitwa “Kwa Pembe” akiwa amechoka vibaya kutokana na mazoezi magumu aliyotoka kuyafanya muda mfupi uliopita. Alikuwa ameloa jasho chepechepe mwili mzima huku anatwetwa kwa uchovu.
Alikuwa amejiwekea ratiba yake binafsi kuwa akitoka ofisini kwake saa 9:30 Alasiri juu ya alama maeneo ya Posta jijini Dar es Salaam, huwa anapitia ukumbi wa kufanyia mazoezi "GYM" maeneo ya Mwenge jengo jirani na kiwanda cha madawa ya binadamu cha SHELLYS.
Huwa anafika hapo kwenye ukumbi kisha anafanya mazoezi mazito kwa muda wa masaa yasiyopungua mawili mpaka saa 12 ya jioni. Hapo atafanya mazoezi ya kuongeza pumzi kwa kuendesha baiskeli na kukimbia, pia atafanya mazoezi ya kuongeza stamina katika mwili kwa kubeba vitu vizito, mwisho anamalizia kwa mazoezi ya viungo.
kisha akitoka hapo mazoezini atapitia kwenye jengo la maduka ya kuuzia bidhaa maarufu kama "Mlimani City Mall" iliyopo barabara ya Sam Nujoma kununua mahitaji mbalimbali ya nyumbani anayohitaji. Kwa kawaida maduka ya hapo unaweza kupata kuanzia bidhaa za chakula, nguo, vifaa vya elektroniki na kila kitu unachohitaji kinapatikana hapo.
Kama hana ratiba ya kujipikia nyumbani siku hiyo basi akitoka "Mlimani City Mall" atapitia kwenye mgahawa mdogo ulio nje ya "Mlimani City Mall" uliopo mkabala na kituo maarufu cha kujazia mafuta vyombo vya moto cha "TOTAL", hapo atakula chakula chake cha chajio atakachopenda.
Ila mara nyingi usiku huo halafu chakula kizito sana kinakuwa chepesi kukwepa kutoka kitambi. Kisha baada ya hapo ataondoka na gari yake pendwa aina ya "Nissan Navara" rangi nyeusi akipitia njia ya 'Makongo Juu' anakuja kutokezea Goba Kati, kisha anashika njia ya uelekeo wa kulia kwake mpaka muda wa saa 1:30 ya usiku mbichi anakuwa tayari amesharejea maskani kwake zamani.
Ambapo akifika nyumbani atapumzika nusu saa kisha ataanza mazoezi ya karate na taikondo kwa muda wa nusu saa tena, siku yake kwa upande wa mazoezi inakuwa inaishia. Baada ya hapo ataenda kuoga bafuni kwake kwa ajili ya kujiandaa kupumzika.
Alikuwa akipenda ataangalia televisheni yake mpaka saa 4 au 5 usiku halafu anaenda kujitupa kitandani kwake. Kama hajisikii kuangalia runinga basi atajichimbia ndani ya maktaba yake kujisomea vitabu mbalimbali vya kujiongezea ufahamu na maarifa.
Hiyo ndio ilikuwa ratiba yake ya mizunguko ya baada ya kazi aliyojipangia na kuiheshimu vilivyo ratiba yake. Ikifika mwishoni mwa juma ndio anapumzika nyumbani muda wote hatoki ila kwa dharura au kuwatembelea ndugu, jamaa na marafiki. Ila siku hiyo alichelewa mno kurudi nyumbani, na sababu ilikuwa wazi kulikuwa na msongamano mkubwa wa magari yaliyoshonana barabarani.
Foleni ya magari ilianzia maeneo ya Mwenge mpaka kufika Ubungo kwa hiyo magari yalikuwa yanakwenda kwa mwendo wa kinyonga au kama msafara wa Bwana na Bibi harusi wanaoelekea kwenye ukumbi wa kufanyia tafrija. Kwa kuwa yeye ni mzoefu wa Jiji la Dar es Salaam hilo halikumpa shinikizo wala wahaka wa moyo, zaidi ya kubaki kuchukia tu moyoni.
Maana Jiji la Dar es Salaam ni Jiji ambalo huwezi kukadiria utafika kwa muda muafaka sehemu unayoikusudia. Jiji hili wewe unaijua saa ya kutoka tu lakini saa ya kufika ni majaliwa yake Mola. Ukiwa mgonjwa huwezi kufika kwa wakati hospitalini, ukiwa muajiriwa huwezi kuripoti kibaruani kwako kwa muda muafaka na ukiwa mwanafunzi ukifanya masihara daima utakuwa unachezea viboko vya walimu wako.
ITAENDELEA BAADAE
kukipata kitabu-Full Nicheki
0625920847/0684900249
Muendelezo bonyeza link hizi
Sehemu ya pili
Sehemu ya tatu
Sent using Jamii Forums mobile app
Makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia, Kijijini Mahiwa, Lindi.
Kadamnasi ya watu walikuwa wamekusanyika wakiwa wamejikunyata vikundi vikundi. Nyuso zao zimegubikwa na majonzi na huzuni katika makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia vya kwanza, yaliyopo kijijini Mahiwa.
Kijiji ambacho kipo katika Wilaya ya Lindi Vijijini katika Mkoa wa Lindi. Waombolezaji hao walikuwa wamekusanyika katika harakati za kuhitimisha shughuli ya arobaini kutokana na msiba wa Bi.Josephina Charles Nyagali aliyezikwa kwenye makaburi hayo ya mashujaa. Ni makaburi ambayo hayatambuliki Kitaifa lakini wenyewe wenyeji wanalitambua na kulienzi kuwa ni eneo walilolazwa mashujaa wa vita vya dunia.
Anga nayo ilitandaza wingu zito, lililofunika jua utadhania nalo lilikuwa linajumuika na waombolezaji kwenye kumaliza msiba huo. Kijiji kilifurika wageni mahashumu wa ndani na nje ya nchi waliokuja kuhitimisha msiba huo. Miongoni mwa wageni hao, alikuwepo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Nchi ya Msumbiji, Mheshimiwa Allan Fernando, aliyetumwa kumwakilisha Rais wa Msumbiji katika msiba huo.
Pia alikuwepo Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa nchini Msumbiji Bwana Jacob Steven au maarufu kwa lakabu ya Komandoo 'JS' akiwa ni mteule mpya kwenye idara hiyo. Pia alikuwemo katika msafara huo toka nchini Msumbiji, Daktari Anabella Munambo akiwa ni Daktari Mkuu katika hospitali mpya ya "Quelimane Central Hospital" iliyopo katika jimbo la Zambezi. Hao walikuwa ni baadhi tu ya vigogo wazito toka msafara viongozi wa Msumbiji.
Kwa upande wa Tanzania, mkururu wa vigogo nao walifurika kijijini Mahiwa, kuanzia wa Mkoa na wa Kitaifa. Mawaziri, Makatibu Wakuu na Mkuu wa Idara ya Usalama ya Taifa Bwana Mathew Kilanga alikuwepo kundini. Wasioelewa kinachoendelea na kushangazwa na ugeni ule mzito pale kijijini walikuwa wanajiuliza bila kupata majibu.
Swali kubwa vichwani mwao lilikuwa "huyu Bi.Josephine Nyagali alikuwa ni nani haswa katika historia ya nchi ya Tanzania mpaka apate bahati ya kulazwa malaloni pamoja na wanajeshi mashujaa waliokufa katika vita vya kwanza vya dunia?". Heshima ya Bi.Josephina kuzikwa hapo, ilitokana na babu yake mzaa baba, hayati "Nyagali Wa Nyagali" aliyekuwa mpiganaji wa Jeshi la Mjerumani enzi za vita vya dunia na kuzikwa katika makaburi hayo. Vita vya Mahiwa katika ya Mjerumani na Muingereza vilipiganwa mwaka 1917.
Ambapo Jeshi la Mjerumani likiongozwa na Jenerali Paul Emil von Lettow-Vorbeck walichuana vikali na Jeshi la Muingereza likiwa chini ya uongozi wa Luteni Jenerali Jacob van Deventer. Vita hivyo vya Mahiwa vilisababisha vifo vya askari si chini ya 2,000 wengi wao wakiwa ni Wanajeshi wa upande wa Uingereza. Katika baadhi ya Wanajeshi waliofariki, babu yake Bi Josephina, Koplo Nyagali Wa Nyagali nae alikuwemo, akabahatika kuzikwa eneo hilo na baadhi ya wanajeshi wachache waliozikwa hapo.
Pia mtoto wake Bi.Josephina, Kachero Manu ndio ambaye alipendekeza mama yake mzazi azikwe hapo kando ya kaburi la babu yake mzaa mama, kwenye eneo ambalo hata yeye Kachero Manu atakavyofariki atapendelea azikwe hapo. Muda wote wa shughuli hiyo Dr.Anabella, Kachero Manu na Komandoo 'JS' walikuwa hawaachani wamegandana kama kupe. Wasiowafahamu wakadhania ni watoto mapacha walioachwa na marehemu Bi.Josephina Nyagali wanafarijiana wenyewe kwa wenyewe.
La hasha..! hawakuwa na udugu wowote wa damu, ila walikuwa ni marafiki waliosafishiana moyo ambao kufahamiana kwao katika urafiki huo ulitokana na kazi pevu waliyoshirikiana kuifanya siku chache zilizopita huko nchini Msumbiji. Dr.Anabella alishindwa kuyazuia machozi yake wakati anaweka shada la maua juu ya kaburi la Bi.Josephina. Alivuta taswira jinsi mama yake na baba yake mzazi na nduguze walivyochinjwa kikatili shingo zao na wahusika hao hao waliopoteza uhai wa mama mzazi wa rafiki yake.
Wote watatu walikuwa wanafarijiana na kumpoza mpambanaji mwenzao Kachero Manu aliyefikwa na maswahibu mazito. Kachero ambaye alifiwa na mama yake mzazi kwa kuchinjwa kikatili na mahasimu zake toka nchini Msumbiji katika usiku wa kuamkia siku ya Wapendanao "Valentine Day" ya mwaka 2016. Yeye hakuwahi kuhudhuria mazishi ya mama yake kwa sababu alikuwa na safari ya muhimu sana ya kikazi nchini Msumbiji isiyowezekana kughairishwa kwa sababu yoyote ile. Hivyo alivyorejea toka safarini, ikabidi aunganishe moja kwa moja Kijijini kwao Mahiwa kwenye maandalizi ya arobaini ya kuhitimisha msiba wa mama yake.
Kwa uzalendo wake huo wa kukubali kukacha kushiriki msiba wa mama yake mzazi kwa ajili ya kujitoa mhanga kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Msumbiji, ndio maana nchi ya Msumbiji na Tanzania kwa ujumla wakaipa uzito shughuli hiyo kwa kutuma wawakilishi wao wazito. Baada ya shughuli zote zilizopangwa kufanyika hapo makaburini kuhitimishwa, na kuashiria msiba huo kumalizika kwa kupanda msalaba juu ya kaburi la marehemu, msafara huo ukarejea nyumbani kwao Kachero Manu kwa ajili ya kutoa rambirambi zao.
Mpaka kufikia majira ya saa 12:30 magharibi shughuli zote zikawa zimehitimishwa na wageni mbalimbali wakaanza kurudi kwenye makazi yao waliyofikia kabla ya kurejea makwao.
"Mbona huufanyii kazi msemo wa waswahili ule wa Mgeni njoo Mwenyeji apone, unaniacha mrembo naenda kulala peke yangu Mjane mimi, wewe wa wapi wewe....!" alisema Dr.Anabella kiutani, akimpa shutuma rafiki yake Kachero Manu wakati tayari anajiandaa kupanda gari aliloandaliwa na serikali tayari kwa kuondoka. "Ng'ombe wa kuazima anakamuliwa wima, nisingekuacha bahati yako mmiliki yupo hapa msibani anakaba mpaka penati, hapa alipo amefura kwa hasira, wivu juu yako..!" alijibiwa Dr.Anabella huku akipewa tahadhari ya kuwa makini na mchumba wake Kachero Manu, Faith Magayane.
"Kwaheri...niagie kwa niaba yangu, maana asubuhi nimemsalimia kaninunia utasema mie mke mwenza wake, na Wamakonde tunavyoogopeka kwenye sekta ya chumbani, alipo hana amani kabisa na mimi...!" alisema Dr.Anabella, huku wakikumbatiana kwa sekunde kadhaa na Kachero Manu nyuso zao zikiwa na bashasha mpwito mpwito kisha akapanda kwenye gari na kuondoka msibani.
Komandoo JS alikuwa amejitenga kando wanapeana michapo na mkongwe mwenzake Bosi Mathew Kilanga. Hawa walikuwa ni maswahiba wakongwe waliofanya pamoja mafunzo ya Ukomandoo na sasa wote ni Wakuu wa Idara za Usalama wa Taifa, katika nchi za Msumbiji na Tanzania.
Kachero Manu akawaacha waendelee kusogoa na kukumbushiana enzi zao, na kuamua kujumuika na familia yake wakiendelea kubadilishana mawazo mbalimbali. Giza likazidi kutanda eneo ile na watu wa karibu kuanza kurejea majumbani kwao na wa mbali kuondoka zao ili maisha ya kawaida yapate kuendelea.
Februari ya huzuni na majonzi
"Piga risasi wale kule wanakimbia, fanya haraka sana hamna kuwaonea huruma manyang'au hawa. Hamna kuwachekea wezi wa rasilimali za nchi yetu ya Msumbiji" ova ova. "Sawa mkuu tutawapa kipigo cha mbwa koko" ova ova ". Msiache majeruhi hakikisheni vizuri wafe mara moja hatuna bajeti ya kutibu majeruhi, na hakikisheni mizoga mnawafukia katika mahandaki kuficha ushahidi ova ova".
Yalikuwa ni maelekezo ya kwenye redio za upepo baina ya Afisa Mkuu, Operesheni maalumu ya kutokomeza wahamiaji haramu kwenye jimbo la Cabo-Delgado, Inspekta Jenerali Mark Noble kwenda kwa askari wake waliokuwa wametawanywa mitaani kuwashughulikia wahamiaji hao. Milio ya risasi na mabomu ya machozi yalisikika kwenye kila kichochoro cha kijiji cha Namanhumbire, kilichopo kilometa 30, mashariki mwa Jimbo la Cabo-Delgado.
Hakuna mhusika waliyemkusudia kwenye operesheni hiyo aliyesalimika, wote walikumbwa na dhahama na sekeseke hilo. Balaa na belua kubwa ilizuka ndani ya Jimbo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini ya rubi. Magari ya polisi yakiwa yamejaza polisi idadi ya kutosha yalikuwa yanaranda mitaani pamoja na magari maalumu ya kumwaga maji ya kuwasha kwa waandamanaji nayo yalikuwepo, yamekaa mkao wa tayari tayari kwa lolote.
Msako wa mtaa hadi mtaa, nyumba hadi nyumba, chumba hadi chumba, duka hadi duka ulikuwa unaendelea kuwabaini hao wanaoitwa wahamiaji haramu. Ving'ora vya magari ya polisi vyenye sauti ya kuogofya vilikuwa vinasikika kila kona. Cha kushangaza zaidi kwenye msako huo walengwa wakuu hawakuwa raia wa mataifa mengine bali walikuwa ni Watanzania.
Tena wengi wao ni wale wanaoishi kwa kufuata sheria za nchi kwa kupata viza ya kuingia Msumbiji na pia wakapata hati za ukazi. Mpaka kufikia majira ya saa tano usiku ya siku hiyo tayari mamia ya watu walikuwa wamefariki na wengine kujeruhiwa vibaya. Akina mama nao walikuwa wahanga wa uhalifu huo, wakajikuta wamebakwa hobelahobela na askari hao. Watoto wadogo wakajikuta wengine wao wamekuwa mayatima bila kutarajia. Mali za thamani kubwa zinazomilikiwa na Watanzania hao zikaporwa na askari hao madhalimu. Wale majeruhi waliosalimika wakapokonywa nyaraka zao muhimu kama vitambulisho na hati za kusafiria ili waonekane waliingia Msumbiji kwa kuzamia bila kufuata sheria.
Ili kuficha takwimu halisi za waliofariki, maiti hizo zilikusanywa na kuzikwa kwenye kaburi la pamoja la halaiki ili kupoteza ushahidi wa unyama uliofanyika. Walikuwa wanaogopa tukio lisije kuvuta macho na masikio ya wapenda haki na amani duniani, wakaanza kupaza sauti zao wakakitia kitumbua chao mchanga, wakaja kujikuta wapo kwenye mahakama ya uhalifu duniani iliyopo kule "The Hague", Uholanzi, wamepandishwa kizimbani.
Vyombo vya habari vya nchini Msumbiji vikalishwa habari potofu na Maafisa hao madhalimu walioendesha zoezi hilo haramu lenye malengo mahususi nyuma ya pazia. Wakazidi kuupotosha umma kwa kuwalisha matango pori kuwa waliouliwa ni wahalifu na wahujumu uchumi waliokuwa wanapora na kuchimba madini ya nchi ya Msumbiji kinyume na taratibu za nchi.
Wakasisitiza kuwa wahalifu hao walikuwa wamejihami kwa silaha kali za kivita, hivyo wameuliwa wakati wa mapambano ya ana kwa ana ya kurushiana risasi na wanausalama. Pongezi mbalimbali zikawa zinapeperushwa na viongozi wa juu serikalini kwa Bwana mkubwa, Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kuzihami rasilimali za nchi ya Msumbiji.
Silaha za kivita zinazosemekana kukamatwa eneo la tukio zikawa zinaonyesha kwenye runinga ili kuthibitisha umma wa Watu wa Msumbiji kuwa waliouliwa ni wahalifu wasiostahili kuonewa hata chembe ya huruma. Watanzania mamluki waliohongwa ngwenje za kutosha wakajifanyisha wamekamatwa kwenye tukio hilo, baadhi yao wakiwa wameshikishwa silaha, na kujitia wanatoa ushuhuda mbele ya vyombo vya habari kuwa walikuwa ni genge la uhalifu lililokuwa limejipanga kwa mbinu za medani za kivita, hivyo wanaomba msamaha toka vyombo vya dola.
Magazeti yakapambwa na picha za Afisa Mkuu kwenye operesheni hiyo, Inspekta Jenerali Mark Noble akisifiwa kama shujaa wa nchi, mzalendo na mfia nchi wa kiwango cha kutukuka. Mmoja wa Mawaziri waandamizi, hakubaki nyuma kubariki operesheni hiyo akatoa ahadi ya donge nono kwa askari wote walioshiriki kuwashikisha adabu wahalifu hao wa Cabo-Delgado, iwe motisha kwao kuzidi kujitolea kiuzalendo katika siku za usoni.
Watanzania wachache waliofanikiwa kutoroka kwenye sokomoko hilo, wakaja kutoa ripoti ya kina ya tukio hilo nchini Tanzania. Wakapaza sauti zao kwa kutumia vyombo vya habari, wakitaka ufanyike uchunguzi huru.
Ikabidi sasa Inspekta Jenerali wa Polisi wa Tanzania afunge safari mpaka nchini Msumbiji kwenda kuonana na Mkuu mwenzake wa Jimbo la Cabo-Delgado Bwana Mark Noble ili wayaweke sawa. Baada ya majadiliano ya karibia wiki nzima baina yao, Inspekta Jenerali wa Tanzania akarejea. Alipokanya tu ardhi,pale Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, waandishi wa habari walijikusanya wakiwa na kimuhemuhe na kiherehere cha kujua kilichojiri katika kikao hicho cha ujirani mwema baina ya vigogo hao wawili wa polisi.
"Tumekubaliana kimsingi pande zote mbili kwamba wahalifu siku zote hawana mipaka. Hii mipaka iliyowekwa na Wakoloni isitufanye tukashindwa kupambana na uhalifu na hasa haya makosa yanayovuka mipaka ni lazima tushirikiane. Na kikubwa zaidi ni kubadilishana taarifa na kufanya operesheni za pamoja, mara kwa mara” maelezo hayo mepesi ya uzani wa nyoya la kuku ya Inspekta Jenerali wa Tanzania yakaonyesha kabisa amezidiwa kete na mwenzake Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kupewa taarifa za uwongo juu ya tukio hilo.
Jambo usilolijua ni kama usiku wa giza, vijana wa Mjini wanasema "Alilishwa matango pori na kutiwa ndimu juu ya matukio hayo hatarishi". Ndugu, jamaa na marafiki wa wahanga wa tukio hilo, wakakata tamaa ya kuona haki inatendeka kwa ndugu zao walioathirika kwenye uhalifu huo. Taarifa hiyo ilibaraganya kabisa ukweli halisi wa tukio hilo, kwani ilionyesha kama vile matukio hayo hayajafanywa kabisa na polisi wa Jimbo la Cabo-Delgado, bali ni mtifuano baina ya wahalifu wa Tanzania na Msumbiji.
Wakati shuhuda za wahanga wenyewe zinasema kuwa polisi wa Cabo-Delgado ndio watuhumiwa haswa wa vitendo hivyo wakishiriki kuvilinda vikundi vya kihalifu mitaani. Mategemeo na matarajio yao waathirika wa matukio hayo yalikuwa ni kuletewa taarifa yenye fusuli ya kutosha isiyoacha hata chembe yoyote ya mashaka. Ushindi ukawa umeelemea mikononi mwa genge hilo la wahalifu lililopo ndani ya mfumo rasmi wa nchi.
Walilolikusudia genge la wahalifu ndani ya mfumo rasmi likawa limeshatimu, wakiwa wamefanikiwa kumuongopea mpaka Inspekta Jenerali wa nchi ya Tanzania. Bila kujua ya kwamba wamekumbatia waya wa umeme mkubwa vifuani mwao utawateketeza bila kuacha masalio yao.
Chambilecho "Daima hamna marefu yasiyo na ncha, na haki siku zote ni kama mfano wa boya majini, haiwezi kufichwa kwa kuzamishwa, tabia ya haki siku zote ni kuelea juu".
Idara ya Usalama wa Taifa, Tanzania ilikuwa macho kodo, haijalala usingizi wa pono. Iikuwa ipo kwenye pembe za chaki inafuatilia matukio hayo kwa umakinifu na ukaribu zaidi. Wahalifu hao walichokoza nyuki, wakati wa kukiona kilichomtoa kanga manyoya ulikuwa unakaribia kwa upande wao.
Matukio hayo ya uhalifu yanayowawinda Watanzania pekee hayakukoma. Yakazidi kushamiri na kutamalaki katika Jimbo hilo la Cabo-Delgado lenye kusifika kwa utajiri mkubwa wa madini ya rubi nchini Msumbiji.
Watanzania hao wanyonge na madhulumu hawakuwa na mtetezi wa kuwasemea na kuwaokoa. Wakawa wanapopolewa mitaani kama mbogo msituni anavyowindwa na majangili.
Likaja kutokea tukio lingine la kutisha, tukio ambalo likavifanya Vyombo vya Usalama vya Tanzania vikose simile, na kuamua sasa kwa kauli moja kuwashughulikia Mafioso wote wa Jimbo la Cabo-Delgado wanaopenda kuwachokoa Watanzania.
Ilikuwa ni tarehe 08/02/2016 ya huzuni, simanzi na majonzi makubwa kwa nchi ya Tanzania. Watanzania wapatao 16 walipigwa risasi na kufariki hapo hapo huku makumi kadhaa wakijeruhiwa wakati wakiwa kwenye maduka yao ya kubadilisha fedha za kigeni na kununulia madini, kisha wakaporwa pesa zote na madini yao.
Watanzania hawa walikuwa wakiishi na kufanya kazi katika eneo lenye madini ya rubi liitwalo Montepuez, kwenye Jimbo la Cabo Delgado kaskazini mwa nchi ya Msumbiji.
Yalikuwa ni mauaji ya kinyama na yasiyokubalika kwa jamii ya watu waliostaarabika. Mauaji ambayo yalisababisha kilio katika kila kona ya nchi ya Tanzania, Bara na Visiwani, huku wananchi wakigubikwa na simanzi isiyomithilika na joto la hasira likichemka vifuani mwao.
Lakini kabla ya mauaji hayo, wiki mbili zilizopita serikali ya eneo hilo ilitoa muda wa siku 5 kwa raia wote wa Tanzania wapatao 5,000 waishio hapo Cabo Delgado kuondoka mara moja na kurudi nchini kwao Tanzania.
Hii haikuwa taarifa yenye kupendeza hata kidogo masikioni mwa wananchi wa Tanzania, hasa wakikumbuka udugu wa asili kati ya wananchi wa Tanzania na Msumbiji. Ni kama vile kuna watu walikuwa wanachezea sega la nyuki ili kuwagombanisha ndugu wa damu walioshibana.
Ni tukio ambalo lilileta simanzi na fadhaa kubwa kwa ndugu wa wahanga na Watanzania kwa ujumla. Mikasa hio endelevu ilikusudia kuchimbia kaburini mahusiano mema baina ya hizi nchi mbili.
Ilitaka kufuta mema yote ya siku za kisogoni yaliyotendwa na Watanzania kwa watu wa Msumbiji. Watanzania wengi haikuwahi kuingia akili mwao wala katika fikra zao hata siku moja kuwa itafika siku Watanzania watatendewa unyama kama huu na ndugu zao wa Msumbiji.
Ndugu zao kabisa wa damu wanaotenganishwa tu na mipaka ya wakoloni. Katu hawakutegemea msaada wao wa asali na maziwa katika kipindi cha kupigania Uhuru wa Msumbiji kutoka kwenye makucha ya mabeberu wa Kireno malipo yake yangekuwa shubiri.
Watu wa Msumbiji baada ya kufanikiwa kumng'oa Mkoloni, wakaanza kupigana vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuzalisha maelfu wakimbizi. Bado Watanzania hawakuwafungia vioo ndugu zao, waliwakaribisha kwa mikono miwili waje nchini mwao, wakaishi nao kwa amani na utulivu. Wakashirikiana nao kutwa kucha katika shida na raha, katika mvua na jua bila utengano wowote.
Bila ya shaka tukio hili la mauaji ya watu 16 likasababisha uhusiano baina ya nchi ya Tanzania na Msumbiji kwenda zigizaga, Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake nchini Msumbiji ukawa upo makini kufuatilia na kutoa msaada unaohitajika kwa wahanga wote wa machafuko hayo.
Pia ubalozi ukajitwika jukumu zito la kuwarejesha nyumbani wahanga wote wa kadhia hii mbaya, huku wakitega sikio kusubiri tamko toka kwa viongozi wa juu wa nchi ya Msumbiji.
Lakini ukimya ukazidi kutawala toka kwenye Vyombo vya Dola vya Msumbiji utasema waliokufa ni nguruwe pori wasio na thamani yoyote.
Kwa upande wa maadui wa Umoja wa nchi za Kiafrika, chokochoko hiyo baina ya nchi ya Msumbiji na Tanzania kwao ilikuwa ni furaha sheshe.
Mabeberu hao walikuwa wanajimwashamwasha pindi wakiona nchi huru za Kiafrika zinavyogombana wenyewe kwa wenyewe.
Lengo lao kubwa ni kuona Afrika nzima inaingia kwenye machafuko ya wenyewe kwa wenyewe kama ilivyo nchi za Congo, Sudani Kusini, Afrika ya Kati, Somalia, Mali na kwingineko ili wajichotee rasilimali bwerere bila jasho.
Lengo la mabeberu hao lilikuwa ni kuziona nchi za Afrika, kamwe hazijikomboi kutoka kwenye lindi la umasikini, ujinga na maradhi.
Walitamani wawe ni nchi ombaomba na tegemezi kwao miaka nenda miaka rudi. Moto wa kuni za fitina ulishawashwa na kuchochewa na maadui, ni busara tu za viongozi wa Tanzania na Msumbiji ndizo zinalizokuwa zinahitajika kuzuia uhasama na kukatana baina ya nchi zao.
Tarehe 11/02/2016 siku 3 baada ya mauaji hayo ya Msumbiji, muda wa saa 4:30 usiku kwa majira ya saa za Afrika Mashariki, Kachero nambari wani nchini Tanzania Bwana "Manu Yoshepu" maarufu kwa lakabu ya “Mwiba wa Tasi” ndio alikuwa anaingia nyumbani kwake maeneo ya Mbezi-Juu akiwa hana hili wala lile.
Alikuwa anaishi eneo linaloitwa “Kwa Pembe” akiwa amechoka vibaya kutokana na mazoezi magumu aliyotoka kuyafanya muda mfupi uliopita. Alikuwa ameloa jasho chepechepe mwili mzima huku anatwetwa kwa uchovu.
Alikuwa amejiwekea ratiba yake binafsi kuwa akitoka ofisini kwake saa 9:30 Alasiri juu ya alama maeneo ya Posta jijini Dar es Salaam, huwa anapitia ukumbi wa kufanyia mazoezi "GYM" maeneo ya Mwenge jengo jirani na kiwanda cha madawa ya binadamu cha SHELLYS.
Huwa anafika hapo kwenye ukumbi kisha anafanya mazoezi mazito kwa muda wa masaa yasiyopungua mawili mpaka saa 12 ya jioni. Hapo atafanya mazoezi ya kuongeza pumzi kwa kuendesha baiskeli na kukimbia, pia atafanya mazoezi ya kuongeza stamina katika mwili kwa kubeba vitu vizito, mwisho anamalizia kwa mazoezi ya viungo.
kisha akitoka hapo mazoezini atapitia kwenye jengo la maduka ya kuuzia bidhaa maarufu kama "Mlimani City Mall" iliyopo barabara ya Sam Nujoma kununua mahitaji mbalimbali ya nyumbani anayohitaji. Kwa kawaida maduka ya hapo unaweza kupata kuanzia bidhaa za chakula, nguo, vifaa vya elektroniki na kila kitu unachohitaji kinapatikana hapo.
Kama hana ratiba ya kujipikia nyumbani siku hiyo basi akitoka "Mlimani City Mall" atapitia kwenye mgahawa mdogo ulio nje ya "Mlimani City Mall" uliopo mkabala na kituo maarufu cha kujazia mafuta vyombo vya moto cha "TOTAL", hapo atakula chakula chake cha chajio atakachopenda.
Ila mara nyingi usiku huo halafu chakula kizito sana kinakuwa chepesi kukwepa kutoka kitambi. Kisha baada ya hapo ataondoka na gari yake pendwa aina ya "Nissan Navara" rangi nyeusi akipitia njia ya 'Makongo Juu' anakuja kutokezea Goba Kati, kisha anashika njia ya uelekeo wa kulia kwake mpaka muda wa saa 1:30 ya usiku mbichi anakuwa tayari amesharejea maskani kwake zamani.
Ambapo akifika nyumbani atapumzika nusu saa kisha ataanza mazoezi ya karate na taikondo kwa muda wa nusu saa tena, siku yake kwa upande wa mazoezi inakuwa inaishia. Baada ya hapo ataenda kuoga bafuni kwake kwa ajili ya kujiandaa kupumzika.
Alikuwa akipenda ataangalia televisheni yake mpaka saa 4 au 5 usiku halafu anaenda kujitupa kitandani kwake. Kama hajisikii kuangalia runinga basi atajichimbia ndani ya maktaba yake kujisomea vitabu mbalimbali vya kujiongezea ufahamu na maarifa.
Hiyo ndio ilikuwa ratiba yake ya mizunguko ya baada ya kazi aliyojipangia na kuiheshimu vilivyo ratiba yake. Ikifika mwishoni mwa juma ndio anapumzika nyumbani muda wote hatoki ila kwa dharura au kuwatembelea ndugu, jamaa na marafiki. Ila siku hiyo alichelewa mno kurudi nyumbani, na sababu ilikuwa wazi kulikuwa na msongamano mkubwa wa magari yaliyoshonana barabarani.
Foleni ya magari ilianzia maeneo ya Mwenge mpaka kufika Ubungo kwa hiyo magari yalikuwa yanakwenda kwa mwendo wa kinyonga au kama msafara wa Bwana na Bibi harusi wanaoelekea kwenye ukumbi wa kufanyia tafrija. Kwa kuwa yeye ni mzoefu wa Jiji la Dar es Salaam hilo halikumpa shinikizo wala wahaka wa moyo, zaidi ya kubaki kuchukia tu moyoni.
Maana Jiji la Dar es Salaam ni Jiji ambalo huwezi kukadiria utafika kwa muda muafaka sehemu unayoikusudia. Jiji hili wewe unaijua saa ya kutoka tu lakini saa ya kufika ni majaliwa yake Mola. Ukiwa mgonjwa huwezi kufika kwa wakati hospitalini, ukiwa muajiriwa huwezi kuripoti kibaruani kwako kwa muda muafaka na ukiwa mwanafunzi ukifanya masihara daima utakuwa unachezea viboko vya walimu wako.
ITAENDELEA BAADAE
kukipata kitabu-Full Nicheki
0625920847/0684900249
Muendelezo bonyeza link hizi
Sehemu ya pili
Sehemu ya tatu
Sent using Jamii Forums mobile app