Riwaya: "Cabo-delgado"-part 01

mpasta

JF-Expert Member
Jan 17, 2011
917
1,997
SURA YA KWANZA
Makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia, Kijijini Mahiwa, Lindi.
Kadamnasi ya watu walikuwa wamekusanyika wakiwa wamejikunyata vikundi vikundi. Nyuso zao zimegubikwa na majonzi na huzuni katika makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia vya kwanza, yaliyopo kijijini Mahiwa.

Kijiji ambacho kipo katika Wilaya ya Lindi Vijijini katika Mkoa wa Lindi. Waombolezaji hao walikuwa wamekusanyika katika harakati za kuhitimisha shughuli ya arobaini kutokana na msiba wa Bi.Josephina Charles Nyagali aliyezikwa kwenye makaburi hayo ya mashujaa. Ni makaburi ambayo hayatambuliki Kitaifa lakini wenyewe wenyeji wanalitambua na kulienzi kuwa ni eneo walilolazwa mashujaa wa vita vya dunia.

Anga nayo ilitandaza wingu zito, lililofunika jua utadhania nalo lilikuwa linajumuika na waombolezaji kwenye kumaliza msiba huo. Kijiji kilifurika wageni mahashumu wa ndani na nje ya nchi waliokuja kuhitimisha msiba huo. Miongoni mwa wageni hao, alikuwepo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Nchi ya Msumbiji, Mheshimiwa Allan Fernando, aliyetumwa kumwakilisha Rais wa Msumbiji katika msiba huo.

Pia alikuwepo Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa nchini Msumbiji Bwana Jacob Steven au maarufu kwa lakabu ya Komandoo 'JS' akiwa ni mteule mpya kwenye idara hiyo. Pia alikuwemo katika msafara huo toka nchini Msumbiji, Daktari Anabella Munambo akiwa ni Daktari Mkuu katika hospitali mpya ya "Quelimane Central Hospital" iliyopo katika jimbo la Zambezi. Hao walikuwa ni baadhi tu ya vigogo wazito toka msafara viongozi wa Msumbiji.
Kwa upande wa Tanzania, mkururu wa vigogo nao walifurika kijijini Mahiwa, kuanzia wa Mkoa na wa Kitaifa. Mawaziri, Makatibu Wakuu na Mkuu wa Idara ya Usalama ya Taifa Bwana Mathew Kilanga alikuwepo kundini. Wasioelewa kinachoendelea na kushangazwa na ugeni ule mzito pale kijijini walikuwa wanajiuliza bila kupata majibu.

Swali kubwa vichwani mwao lilikuwa "huyu Bi.Josephine Nyagali alikuwa ni nani haswa katika historia ya nchi ya Tanzania mpaka apate bahati ya kulazwa malaloni pamoja na wanajeshi mashujaa waliokufa katika vita vya kwanza vya dunia?". Heshima ya Bi.Josephina kuzikwa hapo, ilitokana na babu yake mzaa baba, hayati "Nyagali Wa Nyagali" aliyekuwa mpiganaji wa Jeshi la Mjerumani enzi za vita vya dunia na kuzikwa katika makaburi hayo. Vita vya Mahiwa katika ya Mjerumani na Muingereza vilipiganwa mwaka 1917.

Ambapo Jeshi la Mjerumani likiongozwa na Jenerali Paul Emil von Lettow-Vorbeck walichuana vikali na Jeshi la Muingereza likiwa chini ya uongozi wa Luteni Jenerali Jacob van Deventer. Vita hivyo vya Mahiwa vilisababisha vifo vya askari si chini ya 2,000 wengi wao wakiwa ni Wanajeshi wa upande wa Uingereza. Katika baadhi ya Wanajeshi waliofariki, babu yake Bi Josephina, Koplo Nyagali Wa Nyagali nae alikuwemo, akabahatika kuzikwa eneo hilo na baadhi ya wanajeshi wachache waliozikwa hapo.

Pia mtoto wake Bi.Josephina, Kachero Manu ndio ambaye alipendekeza mama yake mzazi azikwe hapo kando ya kaburi la babu yake mzaa mama, kwenye eneo ambalo hata yeye Kachero Manu atakavyofariki atapendelea azikwe hapo. Muda wote wa shughuli hiyo Dr.Anabella, Kachero Manu na Komandoo 'JS' walikuwa hawaachani wamegandana kama kupe. Wasiowafahamu wakadhania ni watoto mapacha walioachwa na marehemu Bi.Josephina Nyagali wanafarijiana wenyewe kwa wenyewe.

La hasha..! hawakuwa na udugu wowote wa damu, ila walikuwa ni marafiki waliosafishiana moyo ambao kufahamiana kwao katika urafiki huo ulitokana na kazi pevu waliyoshirikiana kuifanya siku chache zilizopita huko nchini Msumbiji. Dr.Anabella alishindwa kuyazuia machozi yake wakati anaweka shada la maua juu ya kaburi la Bi.Josephina. Alivuta taswira jinsi mama yake na baba yake mzazi na nduguze walivyochinjwa kikatili shingo zao na wahusika hao hao waliopoteza uhai wa mama mzazi wa rafiki yake.

Wote watatu walikuwa wanafarijiana na kumpoza mpambanaji mwenzao Kachero Manu aliyefikwa na maswahibu mazito. Kachero ambaye alifiwa na mama yake mzazi kwa kuchinjwa kikatili na mahasimu zake toka nchini Msumbiji katika usiku wa kuamkia siku ya Wapendanao "Valentine Day" ya mwaka 2016. Yeye hakuwahi kuhudhuria mazishi ya mama yake kwa sababu alikuwa na safari ya muhimu sana ya kikazi nchini Msumbiji isiyowezekana kughairishwa kwa sababu yoyote ile. Hivyo alivyorejea toka safarini, ikabidi aunganishe moja kwa moja Kijijini kwao Mahiwa kwenye maandalizi ya arobaini ya kuhitimisha msiba wa mama yake.

Kwa uzalendo wake huo wa kukubali kukacha kushiriki msiba wa mama yake mzazi kwa ajili ya kujitoa mhanga kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Msumbiji, ndio maana nchi ya Msumbiji na Tanzania kwa ujumla wakaipa uzito shughuli hiyo kwa kutuma wawakilishi wao wazito. Baada ya shughuli zote zilizopangwa kufanyika hapo makaburini kuhitimishwa, na kuashiria msiba huo kumalizika kwa kupanda msalaba juu ya kaburi la marehemu, msafara huo ukarejea nyumbani kwao Kachero Manu kwa ajili ya kutoa rambirambi zao.

Mpaka kufikia majira ya saa 12:30 magharibi shughuli zote zikawa zimehitimishwa na wageni mbalimbali wakaanza kurudi kwenye makazi yao waliyofikia kabla ya kurejea makwao.
"Mbona huufanyii kazi msemo wa waswahili ule wa Mgeni njoo Mwenyeji apone, unaniacha mrembo naenda kulala peke yangu Mjane mimi, wewe wa wapi wewe....!" alisema Dr.Anabella kiutani, akimpa shutuma rafiki yake Kachero Manu wakati tayari anajiandaa kupanda gari aliloandaliwa na serikali tayari kwa kuondoka. "Ng'ombe wa kuazima anakamuliwa wima, nisingekuacha bahati yako mmiliki yupo hapa msibani anakaba mpaka penati, hapa alipo amefura kwa hasira, wivu juu yako..!" alijibiwa Dr.Anabella huku akipewa tahadhari ya kuwa makini na mchumba wake Kachero Manu, Faith Magayane.

"Kwaheri...niagie kwa niaba yangu, maana asubuhi nimemsalimia kaninunia utasema mie mke mwenza wake, na Wamakonde tunavyoogopeka kwenye sekta ya chumbani, alipo hana amani kabisa na mimi...!" alisema Dr.Anabella, huku wakikumbatiana kwa sekunde kadhaa na Kachero Manu nyuso zao zikiwa na bashasha mpwito mpwito kisha akapanda kwenye gari na kuondoka msibani.

Komandoo JS alikuwa amejitenga kando wanapeana michapo na mkongwe mwenzake Bosi Mathew Kilanga. Hawa walikuwa ni maswahiba wakongwe waliofanya pamoja mafunzo ya Ukomandoo na sasa wote ni Wakuu wa Idara za Usalama wa Taifa, katika nchi za Msumbiji na Tanzania.

Kachero Manu akawaacha waendelee kusogoa na kukumbushiana enzi zao, na kuamua kujumuika na familia yake wakiendelea kubadilishana mawazo mbalimbali. Giza likazidi kutanda eneo ile na watu wa karibu kuanza kurejea majumbani kwao na wa mbali kuondoka zao ili maisha ya kawaida yapate kuendelea.


Februari ya huzuni na majonzi
"Piga risasi wale kule wanakimbia, fanya haraka sana hamna kuwaonea huruma manyang'au hawa. Hamna kuwachekea wezi wa rasilimali za nchi yetu ya Msumbiji" ova ova. "Sawa mkuu tutawapa kipigo cha mbwa koko" ova ova ". Msiache majeruhi hakikisheni vizuri wafe mara moja hatuna bajeti ya kutibu majeruhi, na hakikisheni mizoga mnawafukia katika mahandaki kuficha ushahidi ova ova".

Yalikuwa ni maelekezo ya kwenye redio za upepo baina ya Afisa Mkuu, Operesheni maalumu ya kutokomeza wahamiaji haramu kwenye jimbo la Cabo-Delgado, Inspekta Jenerali Mark Noble kwenda kwa askari wake waliokuwa wametawanywa mitaani kuwashughulikia wahamiaji hao. Milio ya risasi na mabomu ya machozi yalisikika kwenye kila kichochoro cha kijiji cha Namanhumbire, kilichopo kilometa 30, mashariki mwa Jimbo la Cabo-Delgado.

Hakuna mhusika waliyemkusudia kwenye operesheni hiyo aliyesalimika, wote walikumbwa na dhahama na sekeseke hilo. Balaa na belua kubwa ilizuka ndani ya Jimbo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini ya rubi. Magari ya polisi yakiwa yamejaza polisi idadi ya kutosha yalikuwa yanaranda mitaani pamoja na magari maalumu ya kumwaga maji ya kuwasha kwa waandamanaji nayo yalikuwepo, yamekaa mkao wa tayari tayari kwa lolote.

Msako wa mtaa hadi mtaa, nyumba hadi nyumba, chumba hadi chumba, duka hadi duka ulikuwa unaendelea kuwabaini hao wanaoitwa wahamiaji haramu. Ving'ora vya magari ya polisi vyenye sauti ya kuogofya vilikuwa vinasikika kila kona. Cha kushangaza zaidi kwenye msako huo walengwa wakuu hawakuwa raia wa mataifa mengine bali walikuwa ni Watanzania.

Tena wengi wao ni wale wanaoishi kwa kufuata sheria za nchi kwa kupata viza ya kuingia Msumbiji na pia wakapata hati za ukazi. Mpaka kufikia majira ya saa tano usiku ya siku hiyo tayari mamia ya watu walikuwa wamefariki na wengine kujeruhiwa vibaya. Akina mama nao walikuwa wahanga wa uhalifu huo, wakajikuta wamebakwa hobelahobela na askari hao. Watoto wadogo wakajikuta wengine wao wamekuwa mayatima bila kutarajia. Mali za thamani kubwa zinazomilikiwa na Watanzania hao zikaporwa na askari hao madhalimu. Wale majeruhi waliosalimika wakapokonywa nyaraka zao muhimu kama vitambulisho na hati za kusafiria ili waonekane waliingia Msumbiji kwa kuzamia bila kufuata sheria.

Ili kuficha takwimu halisi za waliofariki, maiti hizo zilikusanywa na kuzikwa kwenye kaburi la pamoja la halaiki ili kupoteza ushahidi wa unyama uliofanyika. Walikuwa wanaogopa tukio lisije kuvuta macho na masikio ya wapenda haki na amani duniani, wakaanza kupaza sauti zao wakakitia kitumbua chao mchanga, wakaja kujikuta wapo kwenye mahakama ya uhalifu duniani iliyopo kule "The Hague", Uholanzi, wamepandishwa kizimbani.

Vyombo vya habari vya nchini Msumbiji vikalishwa habari potofu na Maafisa hao madhalimu walioendesha zoezi hilo haramu lenye malengo mahususi nyuma ya pazia. Wakazidi kuupotosha umma kwa kuwalisha matango pori kuwa waliouliwa ni wahalifu na wahujumu uchumi waliokuwa wanapora na kuchimba madini ya nchi ya Msumbiji kinyume na taratibu za nchi.

Wakasisitiza kuwa wahalifu hao walikuwa wamejihami kwa silaha kali za kivita, hivyo wameuliwa wakati wa mapambano ya ana kwa ana ya kurushiana risasi na wanausalama. Pongezi mbalimbali zikawa zinapeperushwa na viongozi wa juu serikalini kwa Bwana mkubwa, Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kuzihami rasilimali za nchi ya Msumbiji.

Silaha za kivita zinazosemekana kukamatwa eneo la tukio zikawa zinaonyesha kwenye runinga ili kuthibitisha umma wa Watu wa Msumbiji kuwa waliouliwa ni wahalifu wasiostahili kuonewa hata chembe ya huruma. Watanzania mamluki waliohongwa ngwenje za kutosha wakajifanyisha wamekamatwa kwenye tukio hilo, baadhi yao wakiwa wameshikishwa silaha, na kujitia wanatoa ushuhuda mbele ya vyombo vya habari kuwa walikuwa ni genge la uhalifu lililokuwa limejipanga kwa mbinu za medani za kivita, hivyo wanaomba msamaha toka vyombo vya dola.

Magazeti yakapambwa na picha za Afisa Mkuu kwenye operesheni hiyo, Inspekta Jenerali Mark Noble akisifiwa kama shujaa wa nchi, mzalendo na mfia nchi wa kiwango cha kutukuka. Mmoja wa Mawaziri waandamizi, hakubaki nyuma kubariki operesheni hiyo akatoa ahadi ya donge nono kwa askari wote walioshiriki kuwashikisha adabu wahalifu hao wa Cabo-Delgado, iwe motisha kwao kuzidi kujitolea kiuzalendo katika siku za usoni.

Watanzania wachache waliofanikiwa kutoroka kwenye sokomoko hilo, wakaja kutoa ripoti ya kina ya tukio hilo nchini Tanzania. Wakapaza sauti zao kwa kutumia vyombo vya habari, wakitaka ufanyike uchunguzi huru.

Ikabidi sasa Inspekta Jenerali wa Polisi wa Tanzania afunge safari mpaka nchini Msumbiji kwenda kuonana na Mkuu mwenzake wa Jimbo la Cabo-Delgado Bwana Mark Noble ili wayaweke sawa. Baada ya majadiliano ya karibia wiki nzima baina yao, Inspekta Jenerali wa Tanzania akarejea. Alipokanya tu ardhi,pale Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, waandishi wa habari walijikusanya wakiwa na kimuhemuhe na kiherehere cha kujua kilichojiri katika kikao hicho cha ujirani mwema baina ya vigogo hao wawili wa polisi.

"Tumekubaliana kimsingi pande zote mbili kwamba wahalifu siku zote hawana mipaka. Hii mipaka iliyowekwa na Wakoloni isitufanye tukashindwa kupambana na uhalifu na hasa haya makosa yanayovuka mipaka ni lazima tushirikiane. Na kikubwa zaidi ni kubadilishana taarifa na kufanya operesheni za pamoja, mara kwa mara” maelezo hayo mepesi ya uzani wa nyoya la kuku ya Inspekta Jenerali wa Tanzania yakaonyesha kabisa amezidiwa kete na mwenzake Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kupewa taarifa za uwongo juu ya tukio hilo.

Jambo usilolijua ni kama usiku wa giza, vijana wa Mjini wanasema "Alilishwa matango pori na kutiwa ndimu juu ya matukio hayo hatarishi". Ndugu, jamaa na marafiki wa wahanga wa tukio hilo, wakakata tamaa ya kuona haki inatendeka kwa ndugu zao walioathirika kwenye uhalifu huo. Taarifa hiyo ilibaraganya kabisa ukweli halisi wa tukio hilo, kwani ilionyesha kama vile matukio hayo hayajafanywa kabisa na polisi wa Jimbo la Cabo-Delgado, bali ni mtifuano baina ya wahalifu wa Tanzania na Msumbiji.

Wakati shuhuda za wahanga wenyewe zinasema kuwa polisi wa Cabo-Delgado ndio watuhumiwa haswa wa vitendo hivyo wakishiriki kuvilinda vikundi vya kihalifu mitaani. Mategemeo na matarajio yao waathirika wa matukio hayo yalikuwa ni kuletewa taarifa yenye fusuli ya kutosha isiyoacha hata chembe yoyote ya mashaka. Ushindi ukawa umeelemea mikononi mwa genge hilo la wahalifu lililopo ndani ya mfumo rasmi wa nchi.

Walilolikusudia genge la wahalifu ndani ya mfumo rasmi likawa limeshatimu, wakiwa wamefanikiwa kumuongopea mpaka Inspekta Jenerali wa nchi ya Tanzania. Bila kujua ya kwamba wamekumbatia waya wa umeme mkubwa vifuani mwao utawateketeza bila kuacha masalio yao.

Chambilecho "Daima hamna marefu yasiyo na ncha, na haki siku zote ni kama mfano wa boya majini, haiwezi kufichwa kwa kuzamishwa, tabia ya haki siku zote ni kuelea juu".
Idara ya Usalama wa Taifa, Tanzania ilikuwa macho kodo, haijalala usingizi wa pono. Iikuwa ipo kwenye pembe za chaki inafuatilia matukio hayo kwa umakinifu na ukaribu zaidi. Wahalifu hao walichokoza nyuki, wakati wa kukiona kilichomtoa kanga manyoya ulikuwa unakaribia kwa upande wao.


Matukio hayo ya uhalifu yanayowawinda Watanzania pekee hayakukoma. Yakazidi kushamiri na kutamalaki katika Jimbo hilo la Cabo-Delgado lenye kusifika kwa utajiri mkubwa wa madini ya rubi nchini Msumbiji.

Watanzania hao wanyonge na madhulumu hawakuwa na mtetezi wa kuwasemea na kuwaokoa. Wakawa wanapopolewa mitaani kama mbogo msituni anavyowindwa na majangili.

Likaja kutokea tukio lingine la kutisha, tukio ambalo likavifanya Vyombo vya Usalama vya Tanzania vikose simile, na kuamua sasa kwa kauli moja kuwashughulikia Mafioso wote wa Jimbo la Cabo-Delgado wanaopenda kuwachokoa Watanzania.

Ilikuwa ni tarehe 08/02/2016 ya huzuni, simanzi na majonzi makubwa kwa nchi ya Tanzania. Watanzania wapatao 16 walipigwa risasi na kufariki hapo hapo huku makumi kadhaa wakijeruhiwa wakati wakiwa kwenye maduka yao ya kubadilisha fedha za kigeni na kununulia madini, kisha wakaporwa pesa zote na madini yao.

Watanzania hawa walikuwa wakiishi na kufanya kazi katika eneo lenye madini ya rubi liitwalo Montepuez, kwenye Jimbo la Cabo Delgado kaskazini mwa nchi ya Msumbiji.

Yalikuwa ni mauaji ya kinyama na yasiyokubalika kwa jamii ya watu waliostaarabika. Mauaji ambayo yalisababisha kilio katika kila kona ya nchi ya Tanzania, Bara na Visiwani, huku wananchi wakigubikwa na simanzi isiyomithilika na joto la hasira likichemka vifuani mwao.
Lakini kabla ya mauaji hayo, wiki mbili zilizopita serikali ya eneo hilo ilitoa muda wa siku 5 kwa raia wote wa Tanzania wapatao 5,000 waishio hapo Cabo Delgado kuondoka mara moja na kurudi nchini kwao Tanzania.

Hii haikuwa taarifa yenye kupendeza hata kidogo masikioni mwa wananchi wa Tanzania, hasa wakikumbuka udugu wa asili kati ya wananchi wa Tanzania na Msumbiji. Ni kama vile kuna watu walikuwa wanachezea sega la nyuki ili kuwagombanisha ndugu wa damu walioshibana.

Ni tukio ambalo lilileta simanzi na fadhaa kubwa kwa ndugu wa wahanga na Watanzania kwa ujumla. Mikasa hio endelevu ilikusudia kuchimbia kaburini mahusiano mema baina ya hizi nchi mbili.

Ilitaka kufuta mema yote ya siku za kisogoni yaliyotendwa na Watanzania kwa watu wa Msumbiji. Watanzania wengi haikuwahi kuingia akili mwao wala katika fikra zao hata siku moja kuwa itafika siku Watanzania watatendewa unyama kama huu na ndugu zao wa Msumbiji.

Ndugu zao kabisa wa damu wanaotenganishwa tu na mipaka ya wakoloni. Katu hawakutegemea msaada wao wa asali na maziwa katika kipindi cha kupigania Uhuru wa Msumbiji kutoka kwenye makucha ya mabeberu wa Kireno malipo yake yangekuwa shubiri.
Watu wa Msumbiji baada ya kufanikiwa kumng'oa Mkoloni, wakaanza kupigana vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuzalisha maelfu wakimbizi. Bado Watanzania hawakuwafungia vioo ndugu zao, waliwakaribisha kwa mikono miwili waje nchini mwao, wakaishi nao kwa amani na utulivu. Wakashirikiana nao kutwa kucha katika shida na raha, katika mvua na jua bila utengano wowote.

Bila ya shaka tukio hili la mauaji ya watu 16 likasababisha uhusiano baina ya nchi ya Tanzania na Msumbiji kwenda zigizaga, Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake nchini Msumbiji ukawa upo makini kufuatilia na kutoa msaada unaohitajika kwa wahanga wote wa machafuko hayo.

Pia ubalozi ukajitwika jukumu zito la kuwarejesha nyumbani wahanga wote wa kadhia hii mbaya, huku wakitega sikio kusubiri tamko toka kwa viongozi wa juu wa nchi ya Msumbiji.
Lakini ukimya ukazidi kutawala toka kwenye Vyombo vya Dola vya Msumbiji utasema waliokufa ni nguruwe pori wasio na thamani yoyote.

Kwa upande wa maadui wa Umoja wa nchi za Kiafrika, chokochoko hiyo baina ya nchi ya Msumbiji na Tanzania kwao ilikuwa ni furaha sheshe.

Mabeberu hao walikuwa wanajimwashamwasha pindi wakiona nchi huru za Kiafrika zinavyogombana wenyewe kwa wenyewe.

Lengo lao kubwa ni kuona Afrika nzima inaingia kwenye machafuko ya wenyewe kwa wenyewe kama ilivyo nchi za Congo, Sudani Kusini, Afrika ya Kati, Somalia, Mali na kwingineko ili wajichotee rasilimali bwerere bila jasho.

Lengo la mabeberu hao lilikuwa ni kuziona nchi za Afrika, kamwe hazijikomboi kutoka kwenye lindi la umasikini, ujinga na maradhi.

Walitamani wawe ni nchi ombaomba na tegemezi kwao miaka nenda miaka rudi. Moto wa kuni za fitina ulishawashwa na kuchochewa na maadui, ni busara tu za viongozi wa Tanzania na Msumbiji ndizo zinalizokuwa zinahitajika kuzuia uhasama na kukatana baina ya nchi zao.


Tarehe 11/02/2016 siku 3 baada ya mauaji hayo ya Msumbiji, muda wa saa 4:30 usiku kwa majira ya saa za Afrika Mashariki, Kachero nambari wani nchini Tanzania Bwana "Manu Yoshepu" maarufu kwa lakabu ya “Mwiba wa Tasi” ndio alikuwa anaingia nyumbani kwake maeneo ya Mbezi-Juu akiwa hana hili wala lile.

Alikuwa anaishi eneo linaloitwa “Kwa Pembe” akiwa amechoka vibaya kutokana na mazoezi magumu aliyotoka kuyafanya muda mfupi uliopita. Alikuwa ameloa jasho chepechepe mwili mzima huku anatwetwa kwa uchovu.

Alikuwa amejiwekea ratiba yake binafsi kuwa akitoka ofisini kwake saa 9:30 Alasiri juu ya alama maeneo ya Posta jijini Dar es Salaam, huwa anapitia ukumbi wa kufanyia mazoezi "GYM" maeneo ya Mwenge jengo jirani na kiwanda cha madawa ya binadamu cha SHELLYS.

Huwa anafika hapo kwenye ukumbi kisha anafanya mazoezi mazito kwa muda wa masaa yasiyopungua mawili mpaka saa 12 ya jioni. Hapo atafanya mazoezi ya kuongeza pumzi kwa kuendesha baiskeli na kukimbia, pia atafanya mazoezi ya kuongeza stamina katika mwili kwa kubeba vitu vizito, mwisho anamalizia kwa mazoezi ya viungo.

kisha akitoka hapo mazoezini atapitia kwenye jengo la maduka ya kuuzia bidhaa maarufu kama "Mlimani City Mall" iliyopo barabara ya Sam Nujoma kununua mahitaji mbalimbali ya nyumbani anayohitaji. Kwa kawaida maduka ya hapo unaweza kupata kuanzia bidhaa za chakula, nguo, vifaa vya elektroniki na kila kitu unachohitaji kinapatikana hapo.

Kama hana ratiba ya kujipikia nyumbani siku hiyo basi akitoka "Mlimani City Mall" atapitia kwenye mgahawa mdogo ulio nje ya "Mlimani City Mall" uliopo mkabala na kituo maarufu cha kujazia mafuta vyombo vya moto cha "TOTAL", hapo atakula chakula chake cha chajio atakachopenda.

Ila mara nyingi usiku huo halafu chakula kizito sana kinakuwa chepesi kukwepa kutoka kitambi. Kisha baada ya hapo ataondoka na gari yake pendwa aina ya "Nissan Navara" rangi nyeusi akipitia njia ya 'Makongo Juu' anakuja kutokezea Goba Kati, kisha anashika njia ya uelekeo wa kulia kwake mpaka muda wa saa 1:30 ya usiku mbichi anakuwa tayari amesharejea maskani kwake zamani.

Ambapo akifika nyumbani atapumzika nusu saa kisha ataanza mazoezi ya karate na taikondo kwa muda wa nusu saa tena, siku yake kwa upande wa mazoezi inakuwa inaishia. Baada ya hapo ataenda kuoga bafuni kwake kwa ajili ya kujiandaa kupumzika.

Alikuwa akipenda ataangalia televisheni yake mpaka saa 4 au 5 usiku halafu anaenda kujitupa kitandani kwake. Kama hajisikii kuangalia runinga basi atajichimbia ndani ya maktaba yake kujisomea vitabu mbalimbali vya kujiongezea ufahamu na maarifa.

Hiyo ndio ilikuwa ratiba yake ya mizunguko ya baada ya kazi aliyojipangia na kuiheshimu vilivyo ratiba yake. Ikifika mwishoni mwa juma ndio anapumzika nyumbani muda wote hatoki ila kwa dharura au kuwatembelea ndugu, jamaa na marafiki. Ila siku hiyo alichelewa mno kurudi nyumbani, na sababu ilikuwa wazi kulikuwa na msongamano mkubwa wa magari yaliyoshonana barabarani.

Foleni ya magari ilianzia maeneo ya Mwenge mpaka kufika Ubungo kwa hiyo magari yalikuwa yanakwenda kwa mwendo wa kinyonga au kama msafara wa Bwana na Bibi harusi wanaoelekea kwenye ukumbi wa kufanyia tafrija. Kwa kuwa yeye ni mzoefu wa Jiji la Dar es Salaam hilo halikumpa shinikizo wala wahaka wa moyo, zaidi ya kubaki kuchukia tu moyoni.
Maana Jiji la Dar es Salaam ni Jiji ambalo huwezi kukadiria utafika kwa muda muafaka sehemu unayoikusudia. Jiji hili wewe unaijua saa ya kutoka tu lakini saa ya kufika ni majaliwa yake Mola. Ukiwa mgonjwa huwezi kufika kwa wakati hospitalini, ukiwa muajiriwa huwezi kuripoti kibaruani kwako kwa muda muafaka na ukiwa mwanafunzi ukifanya masihara daima utakuwa unachezea viboko vya walimu wako.

ITAENDELEA BAADAE
kukipata kitabu-Full Nicheki
0625920847/0684900249
IMG-20200427-WA0086.jpeg


Muendelezo bonyeza link hizi

Sehemu ya pili
Sehemu ya tatu

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Umbali ambao unapaswa kutumia nusu saa tu kufika unaweza ukatembea kwa masaa mawili kutegemeana na mabadiliko ya siku na siku ya msongamano wa magari. Na bado kila siku bandarini yalikuwa yanaingizwa magari mapya utasema yaliyopo hayatoshi. Foleni hizo barabarani zilikuwa zinachangiwa na mengi, ikiwemo ulimbukeni wa matumizi ya magari. Hapo ndio unakuta familia moja inaleta barabarani kwa siku gari zaidi ya 4.

Baba, Mama, Watoto na Mtumishi wa nyumbani kila mmoja anatoka na gari lake. Pia ubovu wa miundombinu ya barabara nacho ni chanzo kikubwa cha kusababisha msongamano wa magari Jijini Dar es Salaam. Ndio maana serikali katika kutatua changamoto ya msongamano katika Jiji la Dar es Salaam, ikabuni njia mbalimbali kama mabasi ya mwendokasi maarufu kama UDART, ili watu washawishike kuacha magari yao nyumbani watumie usafiri wa umma. Pia ikajenga barabara ya kupita juu kwa juu kwenye makutano ya barabara eneo la TAZARA maarufu kwa jina la "Mfugale Flyover".

Pia serikali katika kuzidi kutatua changamoto ya foleni ikaanzisha ujenzi barabara ya njia nane kutokea eneo la Kimara Mwisho kuelekea Chalinze. Foleni hiyo siku hiyo iliharibu kabisa mipango yake ya kufika nyumbani kwa wakati.

"Nadhani serikali ikihamia rasmi Dodoma na ikahamisha ofisi zake na watumishi wake, magari yatapungua sana hapa Jijini. Pia kama itaboresha huduma muhimu kama afya na elimu huko Mikoani pia itapunguza wimbi la watu wanaokuja Dar es salaam kusaka matibabu na kukata kiu ya elimu katika Vyuo mbalimbali vilivyopo Jijini Dar es Salam.

Pia kama itawasaidia wakulima kupata masoko ya uhakika ya mazao yao itawasaidia watu wa vijijini hasa vijana kujikita kwenye kilimo kubakia huko huko walipo wasihamie Dar es salaam kusaka vibarua viwandani na kufanya uchuuzi wa bidhaa mitaani",

alikuwa amezama kwenye fikra tunduizi kichwani mwake huku akiwa ameshikilia usukani wake wa gari lake ambalo lilikuwa linajivuta taratibu kwenye mnyororo huo wa magari. Mpaka alipoingia barabara ya Chuo Kikuu cha ardhi "UCLAS" ndipo foleni ikakatika akawa anaendesha gari yake kwa madahiro yote, kwa kujinafasi bila kikwazo chochote.

Alipofika nyumbani kwake getini, akapiga honi mara mbili, mlinzi kirungu wake akaja mbio mbio kumfungulia geti. "Shwari hapa, kuna la zaidi? " alisalimia Kachero Manu huku anashusha kioo chake cha gari wapate kusikilizana vizuri na mlinzi wake. "Tumesalimika Mkuu amani tupu, shaka ondoa." alijibu kiunyenyekevu huku akiunda tabasamu pana usoni mwake.

"Haya usiku mwema, kazi njema..!" akaaga kwa sauti ya kichovu kisha akapita zake getini na kwenda moja kwa moja kulisweka gari lake kwenye sehemu maalumu aliyoitenga kwa ajili ya maegesho ya magari. Baada ya kulizima gari lake, akatoa begi lake lenye kompyuta kutoka kwenye gari akalipachika begani kisha akawa anakagua usalama wa mazingira ya nje ya nyumba yake.

Macho yake yalikaribishwa na mandhari nzuri ya bustani ya maua na nyasi za ukoka iliyonawiri, inayotunzwa kiumaridadi mkubwa. Baada ya kushangaa hapo nje kwa muda mchache tu, akaingia zake ndani ya nyumba yake hiyo ya kisasa ya roshani moja.
Nyumba ambayo kuanzia mchoraji wa ramani mpaka fundi muashi aliyeijenga walisugua bongo zao vilivyo na kuzitendea haki fani zao. Kila mtu aliyeiona nyumba hiyo kwa mara ya kwanza alistaajabishwa na uzuri wake.

Wapo ambao hawakuamini kama hiyo nyumba ipo Tanzania, wapo waliofikicha macho yao kujidhania labda wapo ndotoni wanaota mchana mchana, na wapo wale wenye vijiba vya roho waliozusha kuwa sio nyumba yake ni ya serikali. Na pia kuna waliokataa kama nyumba hii imejengwa na mafundi wazalendo wa hapa hapa nyumbani Tanzania.

Ilimradi uzuri wa nyumba hii ulikuwa wa kupigiwa simulizi kwenye kila kona kwa kila aliyebahatika kuitia machoni. Bosi wake kazini walikuwa wanagombana na Kachero Manu juu ya nyumba hiyo. Alikuwa anamtaka aipangishe kisha apewe nyumba ya kawaida ya kuishi na serikali. Kiusalama mtu nyeti kama Kachero Manu hakutakiwa kuishi nyumba ya kifahari itakayoibua mjadala wa kuleta taftishi kwa watu juu ya aina ya kazi anayoifanya.

Mubashara tu alivyoingia ndani alielekea jikoni kwenye jokofu lake la kisasa aina ya “Samsung” yenye mlango unaoitwa “French door”. Jokofu ambalo ilikuwa limejazwa mashrabu mbalimbali kochokocho kuanzia maji ya chupa, soda, juisi na vinywaji mbalimbali vikali. Moja kwa moja akaichomoa chupa ya maji yenye ujazo wa lita 1 kutoka kweye trei yake, akaifungua na kuanza kufakamia chupa hiyo ya maji baridi kama anafukuzwa kutokana na kiu kali aliyo nayo kutokana na mazoezi.

Baada ya sekunde 25 akawa tayari ameshaimaliza chupa yake. Alikuwa anayapenda sana maji hayo safi aina ya “USAMBARA SOFT DRINKING WATER” maji matamu sana kutoka safu ya milima ya Usambara, Tanga kutoka kwenye kiwanda cha Predeshee mmoja anaitwa "Zombe" ambaye anajulikana Mji mzima wa Tanga.

Akaitupa chupa ile ndani ya pipa la kutupia takataka. Baada ya kutoka jikoni akashika uelekeo wa kuelekea kwenye chumba cha kulala. Nyumba ya Kachero Manu ilikuwa na chumba tatu huku kila chumba kikiwa kinajitegemea choo na bafu na sehemu ya kubadilishia nguo.

Chumba hizo zilikuwa zipo kwenye roshani ya kwanza. Pia ilikuwa na jiko la kisasa lililosakafiwa kwa umaridadi na marumaru kutoka nchini Hispania. Nyumba hiyo ilikuwa na sehemu pana ya kulia chakula iliyotenganishwa na vioo na sebule kubwa iliyowekwa kutani mwake paneli za plastiki za “polypropylene” (PEPP) zenye kazi ya kuzuia sauti (sound proof), ambavyo hivi vyote vilikuwa vimejengwa chini ya nyumba.

Kiasi kwamba ukiwa sehemu ya kulia chakula unaweza kuwaona watu waliokaa sebuleni ila huwezi kusikiliza mazungumzo yao, utakachoambulia ni kuona midomo yao inacheza cheza wakati wa maongezi yao. Ndani ya uzio kulikuwa na uwanja wa kuchezea mpira wa mikono wa basketi bila kusahau bwawa kubwa la kuogelea huku ikiwa imezungukwa na ukuta mkubwa wenye urefu usiopungua meta 10.

Alielekea moja kwa moja chumbani kwake ili ajimwagie maji na kulala moja kwa moja maana kwa kawaida huwa analala saa tano juu ya alama ila siku hiyo alikuwa amechoka kupitiliza.
Alipoufikia mlango wa chumbani kwake akachomoa ufunguo kutoka kwenye suruali yake akafungua mlango na kuingia ndani ya chumba. Akawasha taa akalivua begi lake la mgongoni lenye kompyuta mpakato "laptop" ndogo ya kisasa na kuliweka juu ya meza ndogo, na simu zake mbili za mkononi nazo akaweka juu ya meza hiyo, meza ambayo kwa kawaida anaitumia kufanyia shughuli zake za kuandikia akiwa chumbani humo kama hajisikii kwenda maktaba.

Kisha akaamua apitilize bafuni kwake. Akiwa tayari ameshika kitasa cha mlango wa chumba cha kubadilishia nguo zake anajiandaa kukinyonga kimpe ruhusa ya kuingia akasikia muito wa simu yake unalia mlio ambao ulimshtua sana. Mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda mbio mithili ya saa mbovu akijua tu kuna jambo kubwa lipo mbele yake litamkabili tu.

Mshtuko ulimpata kwa sababu huo ni mlio maalumu aliouweka kwa ajili ya kuitambua simu anayopigiwa na Bosi wake Mkuu, Mkurugenzi wa Idara ya Usalama wa Taifa. Akazidi kushikwa na tumbo joto, moyoni mwake akiyakinisha kuwa kuna tukio kubwa limetakadamu ndio maana Bosi wake huyo anamtafuta kwenye simu.

Akaachana na kitasa hicho akageuka na kukimbilia moja kwa moja kwenye meza yenye simu hiyo. Bado swali lilikuwa linajifanyia takiriri kichwani mwake anajiuliza mara mbili mbili "Saa tano na dakika mbili usiku huu, Bosi anapiga simu kuna dharura gani? mbona sio kawaida yake?".

Kisha haraka haraka akaipokea kabla haijakatika kwa kubonyeza kitufe cha kupokelea simu na kuisogeza simu kwenye sikio lake la kushoto kisha akatangulia kumsalimia "Shikamoo Kiongozi". Alijizoesha kumuita Bosi wake kwa jina la "kiongozi", kisha akaitikiwa na kubandikwa swali la ghafla,"Marhaba kijana wangu Manu, umeangalia taarifa ya habari ya televisheni ya "AZAM TWO" ya saa 2:00 usiku leo?".

Kachero Manu akajibu kwa unyenyekevu mkubwa "Hapana Kiongozi", nimechelewa kurudi nyumbani kutokana na foleni ya barabarani, je kuna tukio gani nilifuatilie Kiongozi?. Bosi akamjibu haraka haraka "nenda kawahi sasa hivi kuangalia marudio ya taarifa ya habari muda huu saa tano usiku, ufuatilie kwa umakini kusikiliza tukio la kuuawa na kujeruhiwa na kufukuzwa kwa Watanzania waishio katika jimbo la Cabo-Delgado, huko Msumbiji kisha kesho asubuhi saa tatu kamili asubuhi bila kuchelewa tukutane ofisini kwangu.

Pia simu yangu nikiikata tu ufanyie kazi ujumbe nitakaokutumia haraka iwezekanavyo", kisha kabla Kachero Manu hajatoa maelezo yoyote, Bosi wake akawa tayari ameshakata simu yake zamani sana. Hapo hapo akafahamu Bosi wake kakasirika kutokana na kutokuwa na habari na tukio hilo nyeti kwa usalama wa nchi.

Moja ya sifa ya Kachero bora ni kuwa na habari anazohitaji Kiongozi wake kwa wakati muafaka, hatakiwi kuwa mtu boya boya au mtu zumbukuku mzungu wa reli asiyefahamu kinachoendelea ulimwenguni na nchini mwake kwa ujumla. Akiwa bado kapigwa na butwaa hajui hata pa kuanzia akasikia mlio wa meseji kuashiria kuwa kuna ujumbe umetumwa kwake, akaupuuzia kwanza, hakutaka kuufungua.

Himahima akakimbilia sebuleni kuwasha king'amuzi chake cha AZAM-TV akaanza kuitafuta chaneli ya "AZAM-TWO" kwa kutumia kisengeretua chake, kwa bahati akakutana na taarifa ya mwandishi wa televisheni ya "AZAM-TWO" Mkoani Mtwara, Ndugu "Mohammed Mwaya" anadadavua kwa ufasaha maelezo ya mauaji hayo ya tarehe 8/02/2016 na manyanyaso yanayoendelea huko katika Jimbo la "Cabo-Delgado" kwa ufasaha na umahiri mkubwa.

Alipomaliza kuangalia taarifa hiyo akazima televisheni yake na kuamua kuisoma meseji ya kwenye simu yake iliyoingia punde tu. Ujumbe huo aliotumiwa ulikuwa unasomeka kama ifuatavyo; "Black Bag Job kwa Birdwatcher toka Msumbiji, anakusubiria haraka sana kwenye uwanja wa mpira Chambezi, Bagamoyo usiku huu, fanya hima uende kuonana nae".

Alipomaliza tu kuusoma ujumbe huo akajikuta anafumba macho yake huku anazidi kuishiwa nguvu kabisa, ikabidi kwanza avute kiti chake na kukaa chini. "Kazi imeanza upya, kufa au kupona, mgeni wa usiku mwenye ujumbe wangu..!" alijisemea mwenyewe kimoyomoyo huku anazidi kuogelea kwenye bahari ya fikra.

Akajikaza kisabuni akanyanyuka kitini na kwenda kuoga haraka haraka ili aondoke usiku huo huo kuelekea Bagamoyo. Wakati anaoga mawazo yalimjaa kichwani kuwa lazima atapewa kazi ya kwenda Msumbiji. Alichukia sana moyoni moyoni mwake hasa kipindi hiki ambacho alipanga awe karibu zaidi na mchumba wake kuzidi kupalilia penzi lake.

"Kazi yetu hii ya Ukachero ni kama starehe ya mbwa kukalia mkia wake, kwa maana tunapata muda mfupi wa kustarehe lakini muda mwingi tunakuwa kwenye tabu na mahangaiko" aliwaza Kachero Manu huku anajipakaza povu sabuni mwilini mwake na kuiruhusu mvua ya maji ya bomba la juu ianze kulowanisha mwili wake. Alivyomaliza kuoga, akaingia chumbani kwake kwa ajili ya maandalizi ya safari. Akavalia fulana yake nyeupe na suruali ngumu ya dangirizi ya rangi buluu bila kusahau kubeba bastola yake ndogo yenye kiwambo cha kuzuia sauti.

Alivyojiona yupo tayari kwa kuondoka akaangalia simu yake akaanza kuperuzi mitandao ya kijaamii kama "FACEBOOK" na "WHATSUPP", akatuma meseji mbili tatu za mahaba kwa mchumba wake kisha akazima mtandao wa simu yake. Akazima taa ya chumbani mwake na kufunga mlango wa chumba chake tayari kwa kuanza safari ya kuelekea Bagamoyo usiku huo.

Wakati anaelekea kwenye maegesho ya magari alikuwa akizidi kuwaza na kuwezua mkutano wake wa kesho saa 3:00 asubuhi na Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa wa nchi. Alipazwa kwa fikra za jambo analoitiwa na Bosi wake kesho kazini. Alitambua tu wito wake unakuwa ni wito wa kupewa shughuli maalumu ya kufanya ambayo inakuwa na sura ya kufa au kupona.
Vinginevyo angemsubiria tu afike kazini kesho asubuhi ndio ampashe hiyo taarifa. Akajuta kidogo kwa Mungu kwa kumpa kazi inayompatia mkate wake wa siku kupitia kuiweka roho yake rehani chini ya vivuli vya risasi. Sawa waswahili wanasema fuata nyuki ule asali lakini wanasahau pia fuata nyuki upate manundu usoni, kazi yake ilikuwa ni sawa na kuchezea shilingi karibu na tundu la choo.

Akaweka nadhiri kama atatumwa aende "Cabo-Delgado-Msumbiji" akifanikiwa kurudi salama atahakikisha anafunga ndoa haraka na mpenzi wake wa siku nyingi tokea wapo mwaka wa kwanza Chuo Kikuu-Dodoma (UDOM). Mrembo mwenye uzuri wa shani kama angekuwa ni jamii ya ndege angekuwa ni tausi, alikuwa anaitwa "Faith Magayane" anayeishi Dodoma akifanya kazi katika benki ya KCB tawi la Dodoma kama Afisa mikopo.

Alikuwa ni mlimbwende wa viwango vya kimataifa mwenye sifa ya kupewa ithibati ya uzuri na shirika la viwango la kimataifa la "ISO". Njia nzima Kachero Manu wakati anaendesha gari lake kuelekea Bagamoyo alikuwa anavuta fikra kwa mtriririko wa matukio moja baada ya jingine namna walivyokutana na mpenzi wake enzi wapo Chuo Kikuu. Chuo kizima kuanzia Wahadhiri mpaka Wanachuo wenzake walikuwa wanalimezea mate ya fisi penzi la mrembo huyu mkamilifu wa kila idara katika mwili wake kuanzia sura, sauti, umbile, makalio, miguu, kiuno na kila kitu chake utakipenda tu utake usitake.

Vijana wa mjini wangesema "Faith Magayane" alikuwa ni kama maji, upende usipende, utayatamua tu usipoyanywa, utakutana nayo kwenye chakula, au utakutana nayo bafuni wakati wa kuoga. Mrembo huyu kama jina lake linavyosema basi na tabia zake zilisadifiana hivyo hivyo alikuwa ni mwenye imani na muaminifu.

Alikuwa hapapatikii wala kushobokea pesa za Mapredeshee na Vibopa wa Jiji la Dodoma. Ilishawahi kutokea siku moja, mmoja ya mawaziri wastaafu alienda benki anapofanyia kazi mrembo huyu. Wakati anahudumiwa na mrembo Faith akampa bahashishi ya milioni 5 na akamuachia na kadi ya mawasiliano yenye namba zake za simu amtafute akitoka kazini. Lakini wahuni wanasema "aliisoma namba", hata kutumiwa meseji ya asante hakuambulia.
"Kiendacho cha mganga hakirudi", pesa zote hizo milioni 5 alizohongwa, aliamua kuzipeleka kwenye kituo cha watoto yatima kilichopo maeneo ya kitongoji cha Msalato. Hakuwa kama wale warembo ambao kutokana na uzuri wao basi sehemu zao za siri zinapata tabu kutokana na tamaa ya pesa.

Tuachane na mrembo Faith hadithi na simulizi zake namna alivyokuwa anawapa tabu vigogo wenye pesa na ahadi kemkem kwake au wahadhiri wa chuo wenye uchu wa fisi na ahadi za kumpa daraja la juu kwenye mitihani yake, hao wote simulizi zao haziwezi kuisha leo wala kesho, wewe tosheka tu kuwa uzuri wa Faith Magayane sio wa dunia hii, ni moto wa kuotea mbali.

Ukaribu wa Kachero Manu na mchumba wake ulianzia siku ya kwanza tu kuja kuripoti chuoni. Wote walipanda basi moja la "SHABIBY LINE", na kwa bahati walikaa siti sambamba. Sasa safari ya kutoka Dar es salaam mpaka Dodoma ni zaidi ya masaa 8 kwa mwendo wa wastani ingekuwa ni vigumu kukaa pamoja masaa yote bila kupiga stori mbili tatu baina yao. Hapo ndipo ukaribu ulipoanzia, walibadilisha namba zao za simu. Wakawa wanasalimiana mara kwa mara kwa kupigiana na kutumiana meseji. Kwa kuwa walikuwa wanasoma kozi tofauti kuna wakati mpaka wiki mbili mtawalia hawatiani machoni.

Kachero Manu alikuwa anasoma kozi ya Digrii ya mambo ya kudhibiti uhalifu "Criminology" na Faith alikuwa anasoma Digrii ya Uhasibu. Faith alimpenda sana Kachero Manu kutokana tu na upole wake na ustaarabu wake. Maana wengi wa wanaume waliokuwa wanaomba namba ya simu ya Faith walishindwa kudhibiti nafsi zao, waliishia kumtongoza siku hiyo hiyo kutokana na pupa na haraka zao.

Walisahau msemo wa wahenga wa kuwa "haraka haraka haina baraka" na "subira yavuta kheri". Wao walikuwa wanafanyia kazi msemo mwingine wa wahenga wa "ngoja ngoja yaumiza matumbo" lakini kwa Faith waliula wa chuya. Hakuwa wale wasichana wanaoitwa mitaani "maharage ya Mbeya", maji mara moja tu umekula tayari.

Mpaka walipofika mwaka wa kwanza muhula wa mwisho ndipo penzi zao likaanza kuchipua kwa kasi. Ilitokea siku moja isiyo na jina walienda kupata chakula cha pamoja katika kantini ya Chuo. Ghafla mvua kubwa ya kidindia ikaanza kunya. Bahati nzuri Kachero Manu alikuwa amebeba mwavuli wake kutokana na wingu lililokuwa limetanda siku hiyo. Hivyo wakawa wanautumia kujikinga na mvua wakati wanaondoka kurejea hosteli.

Njiani mvua ikazidi kutamalaki, zikaanza sasa kupiga radi za sauti ya kuogofya, Faith akajikuta tu bila kupanga amemkumbatia Kachero Manu kwa hofu ya radi. Matiti yake madogo na laini yaliyochongoka kama konzi na kusimama dede yakamchoma choma kifuani Kachero Manu. Nae bila kufanya ajizi akajishtukia ameutupa mwavuli wake kando na amemkumbatia kindakindaki hataki kumuachia. Mapigo ya moyo wake yakawa yanadunda kama moyo unataka kuchomokea kifuani, kutokana na kupandwa na hawaa ya nafsi.

Akajikuta anatamka kwa sauti ya mahaba "Faith nakupenda sana kuliko kitu chochote hapa duniani, wewe ni msichana wa maisha yangu yote". Faith nae hakulaza damu hii nafasi ya kupendwa na mwanume aliyekuwa anamtamani kwa udi na uvumba. Akisubiria kwa hamu na tashiwishi kubwa, siku ya kuambiwa kuwa anapendwa naye. "Nami nakupenda pia Manueli, usije utesa moyo wangu, ninakukabidhi funguo zake uufanye utakavyo" wewe alijibu Faith kwa sauti nyororo ya puani. Kuja kushtukia, wote wawili wameloana mvua chapachapa na mwavuli wameshautupa kando muda mrefu.

Hapo ndipo safari yao ndefu ya mapenzi ilipoanzia na kama ingekuwa mapenzi ni kitabu huo ndio ungekuwa ukurasa wao wa kwanza. Baada ya hapo Kachero Manu akasafiri kwenda nchi za ng'ambo kwa zaidi ya miaka mitatu lakini Faith alifanikiwa kuvishinda vishawishi akatunza ubikira wake na uaminifu kwa mchumba wake. Alitamani siku ya ndoa yake avikwe kisarawanda.

Mila za kabila lao, mwali ambae ni bikira alikuwa anavikwa nguo nyeupe kiunoni inayoitwa kisarawanda na bibi yake mzaa kuthibitisha ubikira wake. Lilikuwa ni penzi la siri hamna mtu alifahamu mahusiano yao mpaka Faith anamaliza chuo. Wengi walijua anaringa sana maana hawajawahi kumuona hata kusimamishwa chemba na mvulana yoyote pale chuoni, kumbe mchumba wake yupo Marekani.

Hakuwa kama wale wasichana malimbukeni wanaojitangaza kwenye mitandao kila akipata mchumba mpya. Sasa Kachero Manu mipango yake ili afunge nae ndoa haraka mpenzi wake Faith.

Ulishapita muda mrefu wa kuweza kumsoma tabia zake na alijiridhisha pasina mashaka yoyote kuwa Faith anafaa na ana vigezo vyote vya kuwa mama mtarajiwa wa watoto wake. Alishamtambulisha tayari kwa baadhi ya ndugu na jamaa zake ilibakia yeye tu kwenda kujitambulisha rasmi kwa wazazi wa mpenzi wake, ili taratibu zinazofuata za ndoa zifuatie.

Alitambua wasichana warembo ambao ni waaminifu kama mpenzi wake Faith katika zama zetu hizi ni wa kutafuta na tochi au darubini ya kuangalizia vijidudu. Wasichana wengi warembo mitaani ni wahonyoaji au vijana wa mjini wamewapa lakabu ya wachunaji mabuzi hawana mapenzi ya dhati. Wanachoangalia ni kama wewe ni pochi nene ili aweze kukutumia umlipie pango la nyumba, uweze kumpeleka kwenye maduka makubwa kwa ya kufanya nanunuzi ya nguo na viatu vya gharama, uwezo wa kumpeleka kwenda kustarehe ziara za kitalii nchi za Ughaibuni.

Pia huyo mwanaume awe anafanya kazi yenye mshahara sufufu, awe anamiliki gari la kifahari na kuwa na nyumba yake. Lakini wanawake hao wakijiwa na mwanaume asiye na ukwasi ili wajenge maisha yao kwa pamoja kuanzia chini hawana muda nao. Kachero Manu alianza kutamani afanikiwe walau kuacha mtoto duniani kama atapoteza uhai kwenye kazi zake za Kikachero ambazo uhai na umauti ni asilimia hamsini kwa hamsini vinatenganishwa na uzi mwembamba sana. Maana walilishana yamini yeye na mchumba wake kutoshiriki tendo la ndoa kabla ya ndoa ili waepuke kuzaa nje ya ndoa.

Hawakutaka watoto wao wapachikwe majina yasiyofaa na jamii kama mtoto wa haramu au mtoto wa kikopo. Pia wazazi wa mchumba wake walikuwa ni wafia dini wazuri wa Madhehebu ya Kisabato. Wakwe zake hao hawakuwa tayari binti yao ajifungue mtoto nje ya ndoa. Kwao ilikuwa wanahesabu ni laana kama binti yao akizaa nje ya ndoa. Hivyo Kachero Manu aliandaa "jazua" maalumu ya kumtuza mchumba wake siku ya ndoa kwa ajili ya kutunza ubikira wake.

Alipanga kumzawadia gari ndogo ya kisasa, atakalotumia kuendea kazini. Vikao vya familia ya akina Kachero Manu vya kujiandaa kupeleka posa vilishaanza kukaliwa. Tayari alishateuliwa mmoja wa wajomba zake kwa kupewa jukumu la kupeleka posa na kiasi cha pesa kama kifungua mlango nyumbani kwa wazazi wa Faith Magayane.

Mjomba mtu alikuwa anasubiri Kachero Manu apungukiwe na majukumu ya kikazi aweze kupewa ruksa ya kupeleka posa ya mpwa wake. Sasa mambo yanakaribia kukamilika, ghafla linaibuka jipya hili la "Cabo-Delgado" ambalo "piga ua" alijua atatumwa yeye tu. Akawa anawaza kama akipewa jukumu la kwenda Msumbiji kitumbua cha posa kitakuwa kimeingia mchanga tayari, na hana uchaguzi, kazi kwanza mapenzi baadae.

Ingawa alijua mpenzi wake Faith ataumia sana kwa kuvurugika kwa mipango yao kabla hawajatimiza ndoto zao.

Akiwa kwenye lindi zito hilo la mawazo hayo ya mpenzi wake akashtuliwa na honi nzito sana ya Lori lililokuwa lipo mbele yake kwenye hiyo barabara ya kuelekea Bagamoyo. Ilikuwa nusra limpige dafrao lakini bahati ikaangukia kwake, kwa umahiri mkubwa akalikwepa. Akajutia sana uzembe wake wa kuruhusu mawazo yamtawale akiwa barabarani, tena katika nyakati mbaya za giza la usiku.

Akaanza kuwa makini barabarani sasa mawazo yake akiyaelekeza kwenye kazi. Alikuwa anakaribia Chambezi, kwenye Shamba la Utafiti linalomilikiwa na Wizara ya Kilimo, kwenda kuonana na Jasusi Mtanzania mwenye nyaraka za siri alizitorosha toka nchini Msumbiji.


SURA YA PILI
Ofisini kwa "Kiongozi" tarehe 12/02/2016, saa 3:00 asubuhi
Jina lake rasmi anaitwa Bwana Mathew Kilanga au ukipenda muite kwa lakabu ya "Kiongozi" au "Mti mkavu hauchimbwi dawa". Alikuwa ni Kachero Bobezi na mkongwe aliyeanza kuhudumu katika Idara ya Usalama wa Taifa tokea enzi za Rais wa Awamu ya Kwanza wa Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Alijiunga na idara hiyo tokea mwaka 1970 mara tu alipomaliza mafunzo yake ya JKT kambi ya Makutupora, Dodoma. Kambi ambayo ipo takribani kilometa 25 kutokea Dodoma Mjini.

Kujiunga kwake kwenye idara nyeti kama hiyo haikuwa kwa ganda la ndizi, bali Hii ilitokana na bidii na nidhamu kubwa aliyokuwa anaionyesha kipindi chote cha mafunzo yake ya JKT. Akiwa JKT alitunukiwa nishani ya Uongozi bora, Nidhamu na Ukakamavu siku ya kuhitimu mafunzo yake mbele ya Mgeni Rasmi, Waziri wa Mambo ya Ndani wa kipindi hicho Mheshimiwa Saidi Maswanya.

Kisha baada ya kusajiliwa kwenye idara hiyo, akapelekwa Ughaibuni nchini Urusi kwa muda wa miaka 6 mtawalia kwenda kufanya kozi mbalimbali za Ujasusi. Baada ya hapo alirudi nchini mwaka 1976 akahudumu katika idara ya usalama kwa miaka mitatu mpaka 1979 ilipozuka vita vya Kagera, baina ya mahasimu wawili wa enzi hizo, Tanzania na Uganda.

Rais wa nchi ya Uganda wakati huo wa vita alikuwa ni "Nduli Iddi Amini Dada". Katika medani ya vita Bwana Mathew Kilanga alikuwa ni mmoja wa vijana machachari sana waliofanikisha ushindi maridhawa wa jeshi la Tanzania. Alifanikiwa kuingia mpaka viunga vya Jiji la Kampala, Uganda akiwakwepa maafisa usalama wa Nchi ya Uganda kwa mbinu ya kipekee kabisa.

Alijifanya yeye ni mwanamke mfanyabiashara wa vitenge toka Mombasa, Kenya aliyejitanda vazi la baibui lenye mahadhi ya pwani. Alipofanikiwa kupeleleza alichotumwa akaleta mrejesho wa penyenye za udhaifu na nguvu ya jeshi la Uganda ilipo. Baada ya kumalizika vita hivyo, alikuwa ni miongoni mwa mashujaa waliotunukiwa nishani ya heshima ngazi ya juu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hiyo kama haitoshi, mwaka 1981 akapelekwa nchini Israel kwa ajili ya mafunzo mazito na magumu ya Ukomandoo Daraja la-I kwa muda wa miaka miwili. Mafunzo ambayo kwa nchi zote za Afrika, waliteuliwa vijana 25 tu ambao ni shupavu na wenye nidhamu. Lakini waliofanikiwa kuhitimu mafunzo hayo ni watano pekee, akiwemo Mathew Kilanga toka Tanzania, Okola Ochoga wa Uganda, Kwesi Appiah wa Ghana, Ahmed Taleeb wa Misri na Jacob Steven wa Msumbiji.

Wengine wote waliobakia walikufa kabla ya kumaliza mafunzo yao na wengine walipata ulemavu wa kudumu kama kuvunjika miguu na upofu wa macho hali ambayo iliwafanya washindwe kuhitimu mafunzo yao. Alivyorejea nchini mwaka 1983 ndipo alipokabidhiwa rasmi rungu la madaraka makubwa ya kuiongoza Idara ya Usalama huku akifanikiwa kuiletea heshima kubwa idara hiyo ndani na nje ya mipaka ya nchi.

Ndio zile zama za hofu ya kuwa vichaa wengi barabarani ni "Makachero vidole" au kwenye kila maskani mtaani kuna "Kachero kidole", mbinu hizo zote zilikuwa ni mipango thabiti ya Bwana Mathew Kilanga kuhakikisha nchi inakuwa katika hali ya usalama na amani wakati wote. Nje ya Tanzania moja ya kazi zake za kukumbukwa ni namna alivyokabidhiwa jukumu la kuratibu vikosi vya Afrika vilivyomuondosha madarakani tarehe 25/03/2008, Rais wa zamani wa visiwa vya Anjouan Kanali Mohammed Bacar.

Ambaye alikuwa ana'ang'ania kubaki madarakani kinyume na katiba ya nchi. Hivyo Kiongozi Mathew Kilanga ndio aliandaa mpango mkakati uliosababisha Kanali Mohammed Bacar abwage manyanga mwenyewe bila kupenda. Pia Bwana Mathew Kilanga anakumbukwa kwa namna alivyozima mapinduzi ya kijeshi ya Rais wa Burundi yale ya tarehe 3/05/2015, yaliyotaka kumtoa madarakani Mheshimiwa "Pierre Nkurunzinza" akiwa mkutanoni nchini Tanzania. Kiasi ya kwamba nchi ya Burundi mpaka leo inammezea mate ya uchu Bwana Kilanga, akahudumu nchini kwao kama mshauri wa Rais wa mambo ya usalama.

Hizi shughuli zote zilizompatia ujiko Bwana Kilanga, aliziratibu chini ya mwongozo wa kijana wake makini kwa kazi, kijana "Manu Yosepu" au kwa jina la kazi la utani akijulikana kama "Mwiba wa tasi". Kijana ambaye Bwana Mathew Kilanga ukimuamsha hata usiku wa manane ukamwambia kuna jukumu zito na gumu la kumtoa mtu mharifu mfu ambaye yupo kuzimu na anahitajika kurudishwa duniani akiwa hai aje kuhukumiwa, basi bila kusita atakwambia hilo jukumu hilo mkabidhi "Manu Yosepu" ataliweza.

Kwake yeye kijana wake huyo alimuona ni moja ya lulu za Bara la Afrika ambazo ni adimu sana kupatikana, na huenda wanazaliwa mara moja tu katika kila karne moja.

Bwana Kilanga umri ulikuwa umemtupa arijojo sasa, akiwa ameshakula chumvi ya kutosha akiwa na umri takribani wa miaka 70 na ushee. Alishafanya majaribio kadhaa ya kuandika barua zaidi ya mara 10 akiomba kustaafu kazi ili apumzike na jukumu la utumishi wa umma lakini kila wakati jibu toka kwa wakubwa wake wa kazi lilikuwa ni moja tu, "Taifa bado linakutegemea, hatuna mbadala wako".

Ila alishapanga liwalo na liwe kuwa ikifika mwaka 2020 liwake jua, inyeshe mvua lazima aondoke kazini. Akisimamia vyema jukumu lake la Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge akijaaliwa uzima ndio utakuwa mwisho wa utumishi wake kwa usalama wa nchi. Hasa akijivunia ameshawapika vijana mahiri kama akina Kachero Manu Yosepu wakapikika, hivyo hana sababu ya kuwa mkiritimba wa kung'ang'ania utumishi wa umma, mwisho aje kufia ofisini bure. Kutokana na ajira hii alikuwa anakosa muda timilifu wa kucheza na wajukuu zake, pia muda wa kusimamia mashamba yake ya mifugo na kilimo huko kwao Madaba, Ruvuma.

Lakini jana yake tu alikabidhiwa na wakubwa zake jukumu la kuchunguza mauaji ya huko Cabo-Delgado, Msumbiji ndio maana akampigia simu Kachero Manu ili amkabidhi jukumu hilo. Yeye mwenyewe alishafika kazini tokea saa 12:30 asubuhi na alikuwa hajakaa chini anazunguka zunguka ndani ya ofisi yake kama kishada kinachosukumwa na upepo, hatulii sehemu moja.

Bwana Kilanga mikono yake alikuwa kaitumbukiza kwenye mifuko yake ya suruali akiwa amevalia Kaunda suti ya rangi ya kijivu, soli ya viatu vyake vya mokasini rangi nyeupe vinatoa mlio wa malalamiko kila vinapogusa sakafu ya ofisi yake. Alizama kwenye tafakuri pevu ya kupangilia mbinu mbalimbali za kutumia ili kufanikisha kuwatia mbaroni wahalifu.
Yeye alikuwa anajifananisha na kocha na Kachero Manu ndio mchezaji wake.

Timu ikifanikiwa kupata ushindi sifa zinaenda kwa wachezaji, lakini ikifungwa lawama zinaenda kwa kocha. Hivyo yeye ndio jumba bovu daima linamuangukia yeye mambo yakienda mlama. Kila wakati alikuwa macho yake hayabanduki kwenye saa yake ya mkononi kuangalia kama muda umefika wa mkutano wake na kijana wake. Ilivyobaki nusu saa akaeleka mpaka dirishani na kuanza kuchungulia magari yanayopita chini ya ghorofa na kuelekea kwenye maegesho ya magari.

Kwenye kikao hicho kulikuwa na vigogo wengine waalikwa toka idara nyeti mbalimbali za serikalini, hivyo kijinga cha moto cha kuwamulika wahalifu wa Cabo-Delgado popote walipo kilikuwa kinategemewa kuwashwa rasmi ofisini hapo saa 3:00 asubuhi. Mpaka kufikia saa 2:30 asubuhi juu ya alama, vigogo wote walikuwa wameshawasili kwenye ofisi za Bwana Mathew Kilanga, wakapokelewa na kukirimiwa vinywaji.

Sasa wakajitega mkao wa kula wakiwa macho juu wanamsubiria Kachero Manu aje wampe maagizo ya kutekeleza.



KUPATA KITABU
NICHEKI 0625920847/0684900249
IMG-20200427-WA0086.jpeg


Sent using Jamii Forums mobile app
 


Ofisi hizo za Bwana Mathew Kilanga, ambapo mkutano huo mzito ulipangwa kufanyikia humo, zilikuwa zipo katika jengo maarufu Jijini Dar es Salaam la "Benjamin William Mkapa Pension Tower" roshani ya 5 katika mtaa wa Azikiwe.

Zamani jengo hili lilikuwa linajulikana kama "Mafuta House". Ilikuwa ni ofisi ya wastani isiyo na mbwembwe nyingi kama zinavyokuwa Ofisi za vijana wa Mjini, huku akisaidiwa na Katibu Muhtasi wake mwanamke kisura, makini na mwerevu "Kokunawa Rweikiza" mhaya mzaliwa wa Bukoba vijijini.

Alikuwa mwanamke kidosho lakini anayejitambua vilivyo, Waingereza wanasema "Beauty with brain" hivyo hakupata tabu sana kufanya kazi na Bosi Mathew Kilanga. Wengi walishindwa kuendana na kasi ya Bwana Mathew Kilanga katika utendaji wake wa kazi wa kasi na viwango. Lakini Koku yeye akawa anamjulia Bwana Mathew Kilanga, akawa anajifanya yeye ni mithili ya jini mchapa kazi, hachoki.

Hali hiyo ikamfanya adumu nae kwa muda wa miaka isiyopungua 8 mfululizo bila kuharibu kazi yoyote anayoagizwa kutekeleza, wala kupewa barua ya karipio kazini ya kuharibu kazi.
Alikuwa anaishi maeneo ya Kigamboni ili asiwe anachelewa kufika kazini kwa wakati na hata ikitokea dharura ya kuhitajika kazini usiku wa manane iwe rahisi kwake kuripoti kazini. Maana sumu namba moja ya kushindwa kupatana damu zenu na Bwana Mathew Kilanga ilikuwa ni kuchelewa kuripoti kazini katika muda ambao anaokuhitaji. Sumu namba mbili ni kushindwa kutekeleza majukumu ya kikazi aliyokupa uyatekeleze.

Kwa kulitambua hilo ndio maana akafanya maamuzi ya kuhamia Kigamboni kwenye nyumba ya kupanga ili kazi yake iwe na ufanisi. Tarehe 12/02/2016, Kokunawa aliingia ofisini tokea saa 6:05 za usiku, akiwa na kazi moja tu ya kupokea barua pepe za taaarifa za kiintelijinsia kutoka Ofisi ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Mtwara. Pia alikuwa anapokea taarifa kutoka Ubalozi wa Tanzania nchini Msumbiji. Kisha taarifa hizo za kiintelijinsia alikuwa anazidurufu na kuzipeleka kwa Bosi wake Bwana Mathew Kilanga azipitie kwa ajili ya kuzifanyia kazi na kama kuna zinazohitajika kujibiwa zijibiwe.

Kwa ufupi ni kwamba alikesha mfano wa nesi wa zamu anavyokesha na wagonjwa wake wenye hali mbaya. Mida ya saa saa 3:05 asubuhi majira ya dhuha, jua likiwa limeshachomoza vizuri kabisa linamwaga katika uso wa dua miale yake ya rangi ya shaba, mifugo imeshafunguliwa kwenye malishoni zamani, Kachero Manu Yosepu alikuwa ndio kwanza anapanda ngazi kwa madaha kuelekea roshani ya 5 ofisini kwa Bosi wake kama vile hana haraka..

Kachero Manu Yosepu alikuwa hapendi kutumia "Lift" anapopanda ngazi za jengo la ghorofa lolote lile. Huo ulikuwa ni utamaduni wake aliojiwekea na huwezi kumbadilisha asilani. Kwake yeye mtambo huo unaotumika kubebea watu kutoka roshani za chini na kuwapeleka roshani za juu kwenye majengo makubwa alikuwa anauona ni maalumu kwa wagonjwa, wazee, watoto na akina mama wajawazito.

Ilikuwa ni moja ya mazoezi yake ya kuimarisha misuli ya miguu katika upandaji wa ngazi. Bwana Mathew Kilanga alishaanza kuulizia kwa Sekretari wake kama Kachero Manu kashatia nanga ofisini. Ilipofika saa 3:08 asubuhi Kachero Manu akagonga mlango wa ofisi kisha akanyonga kitasa bila kusubiri sauti ya kukaribishwa kuingia ndani. Akapokewa kwa tabasamu mwanana la Sekretari wa Bosi wake, Kokunawa.

Moto wa utani baina yao hao watani wa jadi ukatawala kama kawaida yao wanapokutana. "Habari za asubuhi dada "Koku" uliyehajiri kuja Jijini kwa hisani za mbio za mwenge wa uhuru, Bukoba wanasemaje? alitania Kachero Manu kumtania Kokunawa.

"Habari za asubuhi ni nzuri, Bukoba nimeongea nao mambo yao ni mpwitompwito, hongera zako unaetoka usingizini, mimi na Bosi wako tuko kazini tokea saa 6 usiku wa jana, kupenda kwako kitanda kutakuotesha kitambi shauri yako ushindwe kazi zote mbili za nyumbani na za ofisini zinazokupa mkate wako wa siku" wakacheka wote kwa pamoja kicheko cha nguvu huku wakigonganisha viganja vyao vya mikono.

"Kazi za nyumbani lazima zitushinde na bodaboda lazima watusaidie hamna jinsi, kwa maana maisha yanavyotukimbiza mchakamchaka, Mungu pekee ndio anajua" aliongea Kachero Manu huku akiwa ameinamia dirisha la Sekretari huyo huku amepinda mgongo wake ili waonane vizuri sura zao.

"Sasa Afisa mzima kama wewe, mshahara mnono na marupurupu kochokocho unalalamika maisha magumu je sisi wenye mishahara ya mkia wa mbuzi tutasema nini..!" alisema Kokunawa kwa sauti ya kinyonge akionekana anachokiongea sio utani kinatoka moyoni mwake, akiwakilisha kilio cha watumishi wengi wa umma cha kulipwa mishahara kiduchu isiyoendana na gharama halisi za maisha ya kila siku.

Ghafla bin vuu wakiwa kwenye soga zao simu ya mezani ya Sekretari Kokunawa ikaita tena, ilikuwa inapigwa toka kwa Bosi akiulizia kama Kachero Manu kasharipoti ofisini, akajibiwa ndio ameingia hivi sasa.

Alivyokata simu tu, Kokunawa akamwambia Kachero Manu "Kaka yangu kimenuka huko, ukisikia hasira za ndovu kumla mwanawe ndio leo, fanya haraka uende Babu yako anasema hana muda wa kupoteza kukusubiria wewe, na sauti yake inaonyesha kashaanza kukasirika, si unamjua Bosi wako kama kazaliwa na kazi vile". "Sawa ngoja nimuone haraka, tutaonana nikitoka nataka nikupeleke kula mlo wa usiku kwenye hoteli kubwa kubwa binti mrembo upumzike kula senene kila siku" akajibu Kachero Manu huku akitokomea kwenye veranda ya kuelekea kwenye mlango wa ofisi ya Bosi wake, akimuacha Sekretari Kokunawa yupo hoi kwa kicheko hana mbavu.

Alivyofika akagonga hodi na kufungua mlango moja kwa moja. Alipoingia ofisini ndani, Kachero Manu alijikuta anapigwa na bumbuwazi baada ya kuona Bwana Mathew Kilanga yupo na wageni wengine wawili ambao sio wageni katika macho ya Kachero Manu.

Ukweli wa kutoka sakafu ya moyo wake hakupendezwa na uwepo wa wageni wale kwenye mazungumzo nyeti kama yale. Kachero Manu akapotezea ule mfadhaiko alioshikwa na akajizuia kuonyesha hasira zake, akasalimia "Shikamoo Kiongozi, habari za asubuhi"...! kisha akawasalimia wale wageni waalikwa wengine wawili kwa tabasamu lenye bashasha feki.

Bosi wake alimkuta bado amesimama hajakaa kwenye kiti chake, akajibu salamu hiyo. "Habari za asubuhi ni mbaya sana, karibu kiti ukae" huku akimuashiria kwa mkono kiti cha kukaa. "Ahsante sana...!" akajibu Kachero Manu, kisha akavuta kiti kilichopo tupu akakaa na akatoa kompyuta mpakato yake kutoka kwenye begi lake akaiwasha, kisha akaitafuta pragramu ya uandishi ya "microsoft word" tayari kwa kuandika vitu vya msingi kwenye majukumu ya kazi atakayopewa na wakubwa zake hao.

Kikapita kimya cha kama dakika moja utasema shetani kapita vile. Bosi Kilanga akajikohoza kikohozi kikavu, kisha nae akaja karibu yao na kuvuta kiti chake akakaa.

Akachukua chupa yake ya kahawa akamimina kikombe kimoja kikubwa akaifunga, kisha akapiga mafunda matatu mfululuzo huku amefumba macho yake mithili ya mnywaji pombe haramu ya "Gongo", kuonyesha uchungu wa kahawa hiyo. Halafu akaisogeza chupa pale alipoketi Kachero Manu kumpa ishara kuwa anaruhusiwa kunywa kahawa, kisha akaanza kuongea huku anamkazia macho. Wale wageni wengine nao wakaongeza umakini kwa ajili ya kushiriki mazungumzo hayo.

"Kama ulivyoona jana kwenye taarifa ya habari ya jana AZAM-TWO usiku kuhusiana na madhila ya Watanzania wenzetu waishio nchini Msumbiji. Sina haja ya kurudia kukuelezea kile ulichokiona kwenye televisheni kama nilivyokuelekeza uangalie. Sasa haya matukio yametikisa mahusiano ya kidiplomasia ya nchi zote mbili Tanzania na Msumbiji.

Jana Rais wa wa Msumbiji amenukuliwa katika televisheni ya taifa ya Msumbiji "Televisão dê Moçambique" akihutubia taifa kuwa amesikitishwa na matukio hayo yaliyojitokeza. Rais huyo pia tayari ameagiza vyombo vya dola vya Msumbiji vichunguze chanzo cha madhila hayo na wahusika wote wachukuliwe hatua, pia ametumia fursa huyo kuwaomba radhi wananchi wa Tanzania kwa matukio hayo aliyoyaita ya kishenzi na kinyama yasiyoendana na utu wa kibinadamu.

Pia ameahidi kuandika barua rasmi yenye maelezo ya kina kwa serikali ya Tanzania ikielezea sakata lote kwa ujumla na njia za kufuata ili lisijirudie tena siku za usoni. Lakini habari za kiintelijinsia za kushtua toka Mtwara tulizozipata jana jioni ni kuwa mara baada ya matukio hayo kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa iliyo chini ya Mkuu wa Mkoa ilipitisha maamuzi ya kuwatuma askari kanzu 6 kwenda kupata ithibati ya habari, lakini tokea waondoke tarehe 9/02/2016 hawajulikani walipo mpaka hivi sasa ninavyozungumza na nyinyi.

Ubalozi wetu nchini Msumbiji umejaribu kufanya kila linalowezekana kuwatafuta, lakini leo ni siku ya 4 haijulikani kama wapo hai au wameshafariki. Na mbaya zaidi habari zilizonifikia asubuhi hii ni kuwa machafuko yanayowalenga Watanzania yameanza kusambaa katika Wilaya zingine za Jimbo hili la Cabo-Delgado.

Ripoti toka ubalozini kwetu zinasema Watanzania waishio katika wilaya za "Mueda" na "Palma" nao wameporwa mali zao na kuchaniwa hati zao za kusafiria kwa makusudi ili kuhalalisha kuwa wamekuja nchi Msumbiji kinyume cha sheria. Kwenye msafara wa mamba na kenge wapo hatukatai kuwa lazima wapo Watanzania waliokuwa wanaishi kinyume na sheria za Msumbiji, kwa maana ni wahamiaji haramu lakini hilo halihalalishi vitendo walivyofanyiwa vinakiuka sheria na haki za binadamu za umoja wa mataifa.

Kwa hali ilivyo inaonyesha dhahiri serikali ya Msumbiji imeshindwa kuwalinda raia wetu wa Tanzania. Iwe wameshindwa kwa bahati mbaya au kwa kukusudia, sisi hatufahamu maana moyo wa mtu ni kichaka. Inavyoonekana pia kuna kikundi cha watu ndani ya serikali ya Msumbiji wanatumika na mabeberu kutoka ughaibuni kutaka kuvuruga mahusiano mema yaliyopo kati ya Tanzania na Msumbiji yaliyoasisiwa na Baba wa taifa la Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere na muasisi wa chama cha kupigania uhuru wa Msumbiji "FRELIMO" Bwana Erduado Chivamba Mondlane tokea mwaka 1962, kisha mahusiano yakatiliwa nguvu na Rais wa kwanza wa Msumbiji Bwana Samora Machel.

Sasa maagizo niliyopokea jana usiku toka kwa wakubwa huko serikalini, maagizo ambayo yakanilazimu nikupigie simu usiku huo huo ni kuwa wanataka tuchunguze nini chanzo cha fujo hizo na nani yupo nyuma ya hawa wanaotumika kuvuruga mahusiano mema baina ya hizi nchi mbili, ili watiwe mbaroni na sheria iweze kuchukua mkondo wake dhidi yao.

Sasa nakuagiza unatakiwa ujiandae kusafiri kwenda Msumbiji kwa kazi hii maalumu. Kazi ambayo serikali ya Msumbiji hatutaki wajue kuwa tumetuma Kachero wetu kuchunguza ndani ya nchi yao, itaharibu mahusiano yetu mema na itakiuka pia mikataba ya Umoja wa Mataifa ya kutokuingilia uhuru wa ndani wa nchi ingine.

Lakini hatuna jinsi Watanzania wenzetu wananyanyasika, wanaporwa mali zao na hata kuuliwa na askari kanzu wetu tuliowatuma wametoweka. Hivyo ni jukumu letu kulinda maslahi ya raia wetu hata kama ni nje ya mipaka yetu. Sina maongezi zaidi kama kauli mbiu ya Tanzania hivi sasa ya "HAPA KAZI TU", naomba ukachape kazi uwashikishe adabu vibaraka wa mabeberu mpaka wajutie uovu wao ili iwe funzo na fundisho kwa watu wengine wanaotamani kuichokonoa Tanzania yetu iliyojengwa katika misingi imara ya umoja, mshikamano na amani na Baba yetu wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Hii kazi naomba imalizike mtondogoo ukihesabu kuanzia kesho, ukizidisha sana iwe juma moja kamilifu. kuanzia sasa naomba ukitoka hapa utamuona Katibu Muhtasi wangu "Kokunawa" atakukabidhi makabrasha yote yenye taarifa zote za yanayoendelea Msumbiji mpaka jana usiku pia atakupa makabrasha ya historia ya mahusiano ya kidugu yaliyopo baina ya Msumbiji na Tanzania, ili upate kufahamu nini unachoenda kukitetea, yakujenge uzalendo wako uone upuuzi wanaoufanya hawa vibaraka wa mabeberu.

Pia atakupa hati zako za kusafiria na tiketi za ndege, akaunti za benki mbalimbali na mawasiliano yote ya mtu wetu muhimu nchini Msumbiji Bwana Jacob Steven atakayekupa msaada wowote unaouhitaji ukiwa Msumbiji". Muda wote Bosi alikuwa anaongea huku Kachero Manu anamsikiliza kwa umakini mkubwa sana ili asije akapitwa na mambo muhimu, huku kukiwa kuna jambo anaogopa kusahau analiandika kwenye kompyuta yake.

"Mie nimemaliza je una lolote unataka kuongea?" aliulizwa Kachero Manu, huku macho sita ya watu watatu yakimkodolea yeye kama washabiki wa mpira wanavyomuangalia mchezaji mpira mahiri anayesakata kabumbu uwanjani.

"Sina lolote, ila leo alasiri nitaonana na yule kijana niliyeonana nae jana usiku Bagamoyo, ameniahidi kunipatia kifaa kingine cha kieletroniki kilichohifadhi nyaraka zingine nyeti, amesema nitamkuta "New Star Hotel", Mwenge saa 10:00 alasiri, huenda nikikamilisha kuzisoma nitakuwa na lolote la kuongea lakini kwa sasa sina chochote..!" aliongea Kachero Manu huku akijiandaa kuzima kompyuta yake.

"Nakutakia maandalizi mema ya safari, kuwa makini sana taifa linakutegemea, Watanzania zaidi ya milioni 55 na ushee wameweka matarajio kwetu sisi watu wa Usalama ya kuwalinda hatutakiwi kuwaangusha hata kidogo na ndio kiapo cha kazi yetu tulichokiapa cha kulinda maslahi ya nchi yetu kwanza hata ikibidi kupoteza uhai wetu.

Hawa wenzangu uliowaona hapa nafahamu unawajua kiundani, wanatoka idara mbalimbali ndani ya serikali nao ni wanakamati walioteuliwa kushirikiana na sisi, wamekula viapo vya utumishi wa umma hivyo hatuna wasiwasi nao" alimaliza maelezo yake marefu yenye kusisimua Bwana Mathew Kilanga Mudiru wa Idara ya Usalama wa Taifa, nchi nzima.

"Sawa Kiongozi nimekuelewa kama nilivyokueleza nitasoma hizo nyaraka za siri kwa kina nikimaliza nitakujuza lini nitaondoka kuelekea Msumbiji kutekeleza wajibu niliotumwa na taifa langu nilipendalo kwa dhati la Tanzania. Nadhani safari itakuwa baada ya siku mbili maana nahitaji muda mpana wa kupitia makabrasha vizuri sana ili nijue wapi pa kuanzia" alijibu Kachero Manu kwa unyenyekevu na kujiamini.

Baada ya maelezo ya Kachero Manu Bosi wake akaonyesha kuafikiana nae. Bosi wake akawa wa kwanza kusimama na wale wageni waalikwa ambao muda mwingi walikuwa ni wasikilizaji tu huku wakichukua nukuu mbalimbali za maandishi kwenye vipengele wanavyoona vinawafaa, nao wakasimama.

Wakaagana kwa kupeana mikono, Kachero Manu akahisi ugumu wa kiganja cha Bosi wake Bwana Mathew Kilanga, shaibu wa miaka 70 lakini bado mkakamavu. Kilikuwa kiganja hicho cha mkono ni kigumu mithili ya jiwe la kusugulia gaga za miguuni katika nje ya mabafu ya nyumba za uswahilini kule maeneo ya Tandale na Mbagala.

"Kuwa makini kijana wangu, usiache kumtafuta Bwana Jacob Steven ni komandoo mwenzangu mstaafu, atakusaidia sana utakapokwama" alisema kwa kumnong'oneza sikioni. Hakujibu kitu bali alitikisa tu kichwa chake kuonyesha ishara ya kukubali kupokea ushauri huo na kufungua mlango wa ofisi na kutoka nje.

Alichokuwa hakifahamu Kachero Manu kuhusu ukakamavu wa Mudiru wake wa kazi Mzee Kilanga ni kuwa alikuwa ni mwanaume wa shoka, kwanza anaamka jogoo la kwanza saa saa kumi za alfajiri kufanya mazoezi magumu, yakiwemo mazoezi ya kukimbia na tairi la trekta milimani. Hivyo umri kwake ulikuwa ni namba tu lakini mwili ulikuwa fiti mithili ya kijana wa miaka 30.

Kachero Manu Akawa anatembea kwenye korido kuelekea mahali alipo Katibu Muhtasi Koku huku ameinamisha kichwa chini kama kobe anayetunga sheria, mkononi amebeba mkoba wa kompyuta yake mawazo kibao yamemzonga.

Alishtushwa na sauti ya Katibu Muhtsasi wa Bosi wake dada Kokunawa, "kulikoni mbona kama umepewa taarifa ya kulazimishwa kuchumbia maiti pole sana...!" alirushiwa kijembe na Kokunawa.

Kachero akashtuka toka kwenye dimbwi la mkururu wa mawazo na kisha akatabasamu, akasema "Ahsante...Kwanza wewe mbaya sana hukunipa taarifa kama kuna wageni wengine zaidi ya Bosi, pili kazi imeanza upya tena natakiwa nisafiri na kila kitu nitakipata toka kwako, naomba tumalizane kabisa nipe kila kinachonihusu niondoke zangu mie, pia Bosi kasema usisahau kunifungia senene wa kutafuta njiani maana huko Msumbiji chakula chao kikuu ni panya kwa ugali wa muhogo, na mie si unajua nataka kuchumbia kwa Wasabato sasa wakwe zangu nitakosa mwana na maji ya moto, wakisikia nimekula panya tu watanipa kadi nyekundu mke nitanyimwa tena mchana kweupe kabisa" alisema Kachero Manu kumuambia Kokunawa huku anamkonyeza ukope wa jicho kiutani.

Wote wakaangusha kicheko cha furaha sheshe isiyo kifani, maswahiba hawa wa kazini. Kachero Manu akavuta kiti cha wageni akaketi, akawa anamsubiria Kokunawa amkabidhi makabrasha yote kama alivyoagizwa ili aondoke zake.

Kokunawa akabakia ameinamia mtoto wa meza yake kuyatoa makabrasha anayotakiwa amkabidhi. Akiwa pale kwenye kiti, wale wageni wawili nao wakatoka ofisini mwa Bosi Mathew Kilanga wakamkuta Kachero Manu ametulia tuli anasubiria mzigo wake aondoke zake. Mmoja wapo katika wale, mfupi, mnene ana kitambi kikubwa kampa mpiga ngoma ya besi katika bendi ya shule fulani, akajitia kumpa mkono wa kumuaga.

"Safari njema kijana wetu, Mungu akufunike kwa rehema zake" aliongea kwa sauti kubwa huku Kachero Manu akijilazimisha kwa mara ingine kutabasamu. Hisia zake zilikuwa zinamtuma mapema kabisa kuwa huyu sio mtu mzuri. Alikuwa hana ushahidi wowote ila dhana ikimtuma hivyo na hakutaka kupuuzia dhana na hiyo ndio moja ya tabia ya Kachero makini.

Kokunawa alipozipata nyaraka zote alizotakiwa amkabidhi, akaziweka kwenye bahasha ngumu akaifunga vizuri bahasha hiyo kwa gundi na kumkabidhi mkononi. "Nikutakie kazi njema, Mungu akutangulie akushushie malaika wake wa ulinzi, urudi salama My Bestfriend forever..!" aliombewa dua na Kokunawa huku machozi yakiwa yanamlenga lenga kwa mbali kwenye mboni zake za macho.

Kokunawa alitambua rafiki na Mkuu wake wa kazi, Kachero Manu anaenda kuupanda mlima mrefu ulioko mbele yake huko Cabo-Delgado, wenye vigingi, vichuguu, vichaka na makorongo juu yake. "Ahsante dada Koku usijali, nitawashinda na kurudi salama nikiwa na zawadi ya ushindi" alijibu Kachero Manu kwa ufupi.

"Eheee... nimekumbuka kitu nikitaka kusahau sasa vipi lini sasa nikutoe ile ofa ya mlo wa usiku niliyokuahidi usijisahaulishe mrembo" Kachero Manu alitaka kupotezea mawazo ya kuonewa huruma na kikubwa alikuwa hapendi kuanza kutiwa uoga kuwa anaenda kufanya jambo gumu.

"Aaah...mchumba wako yule mtu wa kanda ya ziwa kama mimi, sisi wenyewe tunajijua kwa wivu, usitake nitiwe kilema bure kama mtaalamu wa ofa sana kawape watoto mayatima, mie nalipwa mshahara mnono Babu wewe sibabaishwi na ofa zako uchwara...!" alijibu kwa mbwembwe zote akiipangulia hewani ofa ya kununuliwa mlo.

"Shauri yako kwenye miti hamna wajenzi ngoja nikawape ofa watoto warembo wa kimakonde huko Msumbiji, ambao nasikia wamefundwa na makungwi hodari na hawana madahiro na mbwembwe kama nyie akina nshomile wajivuni wakubwa nyie...!" akajibu Kachero Manu kimasihara wakafa tena kwa kicheko wote kwa pamoja.

"Ebibi kwaheri asije akanikuta hapa Mzee wako nikageuziwa kibao cha uzembe kazini nikafukuzwa kazi, huko mtaani wananchi wanasema vyuma vimebana sijui nitakuwa mgeni wa nani bila ajira, chezea mshahara usichezee kazi, tchaoooo....!" akaaga Kachero Manu na kufungua mlango wa kutokea ofisini kwa Katibu Muhtasi wao bila kusubiria madongo atakayorushiwa.

Muda ulikuwa unasoma ni saa 4:30 asubuhi, hivyo moja kwa moja Kachero Manu akafanya maamuzi ya kuelekea nyumbani kwake kujipumzisha kwa ajili ya kujiandaa na miadi yake ya saa 10:00 alasiri, ya kuonana na kijana Alex Turabu toka nchini Msumbiji.


Kachero Manu alitoka nyumbani kwake majira ya saa 8:45 mchana akijiwekea kadirio la mpaka kufikia saa 10:00 alasiri atakuwa ameshakanyaga katika eneo la Hoteli mpya ya 'New Star Hotel'.

Alipeana miadi ya kukutana na mtumishi mwenzake mchanga wa Idara ya Usalama kijana Alex Turabu. Kijana huyu alikuwa anasomea Udaktari wa Falsafa 'PhD' katika Chuo Kikuu cha 'Joaquim Chissano University' kilichopo Jijini Maputo.

Alikuwa katika mpango wa mabadilishano ya wanafunzi katika ushirikiano wa kielimu kati ya Tanzania na Msumbiji. Katika mpango huo baadhi ya wanafunzi toka Msumbiji walikuwa wanapewa udhamini wa masomo katika Vyuo Vikuu vya Tanzania, hali kadhalika hivyo hivyo, kwa wanafunzi wa Tanzania kwenda Msumbiji.

Katika mpango huo, Alex Turabu akachomekwa, akijifanya ni mwanafunzi anayesomea magonjwa ya mimea 'Plant Diseases', kumbe yupo kazini analinda maslahi ya nchi yake ya Tanzania huko ughaibuni. Kijana Alex alikuwa mahiri wa kuzungumza kwa ufasaha lugha ya Kireno na Kimakonde utasema ni mzawa wa Msumbiji kumbe ni Mdigo wa Tanga.
Sekeseke la mauaji ya yanayowalenga Watanzania yalipoanza tu akaanza kuyafanyia taftishi matukio hayo. Akafanikiwa kukusanya taarifa za kutosha zenye usahihi, tatizo likabakia namna atakavyosafirisha nyaraka hizo bila kutiwa mbaroni.

Inspekta Jenerali 'Mark Noble' na washirika wake walihakikisha wanaweka ulinzi mkali mpakani unaodhibiti Watanzania wanaotoka na kuingia nchini Msumbiji. Bahati aliyoipata kijana Alex Turabu ya kupenya ni wakati wa kuja kufanya utafiti wake nchini Tanzania kwenye magonjwa ya mihogo kama batobato na michirizi ya kahawia alifuata na Profesa wake anayemsimamia.

Mizigo yake ya nyaraka za shule akaichanganya na mizigo ya Profesa wake, hivyo ikapita kiulaini kabisa bila purukushani zozote za kupekuliwa. Walipofika Tanzania wakafikia kiota kipya kabisa cha 'New Star Hotel' kilichopo maeneo ya Mwenge, na kila sehemu wanayokwenda lazima waambatane, Bwana Alex akiwa kama mkalimani wake.

Siku aliyomchomoka na kumkabidhi nyaraka za siri Kachero Manu, alimuongopea kuwa kapigiwa simu ya ghafla na mlinzi anayelinda majaribio yake ya utafiti wa mihogo huko Chambezi kuwa kuna moto umewashwa kwenye shamba la mmoja wa wanakijiji unaweza kuunguza majaribio yake.

Hivyo kwa mbinu hiyo akafanikiwa kumtoroka kiaina kwenda kukabidhi nyaraka za siri lakini kikwazo kikabakia kwenye nyaraka laini 'soft copy' alizokuwa amezihifadhi kwenye kifaa maalumu chenye mafaili yenye nywira ya siri. Kifaa hicho alikuwa nacho Profesa wake usiku huo anafanyia kazi baadhi ya nyaraka za mwanafunzi wake.

Hivyo Alex akakusudia leo saa 10:00 alasiri saa chache kabla hawajaelekea Uwanja wa ndege kupaa hewani na Profesa wake kurejea nchini Msumbiji, lazima waonane kwa mara ya pili, 'New Star Hotel' alipofikia maeneo ya Mwenge ili aweze kumkabidhi.

Mpaka kufikia saa 9:30 Alasiri alikuwa amefanikiwa kufika kambi ya jeshi ya Lugalo kituo cha daladala kinachoitwa 'Super'. Alipoangalia saa yake ya mkononi tena, Kachero Manu akatabasamu akijiamini kuwa ndani ya dakika 10 zilizobaki kama pale Mwenge Mataa kutakuwa hamna foleni atakuwa ameshawasili 'New Star Hotel'.

Alipofika Mwenge Mataa akakutana na nyororo ya foleni isiyosimulika. "This is too much indeed...Afrika tunapoteza pesa nyingi kutokana na foleni za barabarani, Vyama vya siasa vina jukumu la kuwasimamisha kwenye Chaguzi wagombea Uongozi wenye maono na nia thabiti ya kutatua kero za wananchi kama hizi za miundombinu ya usafiri, afya, elimu na kadhalika. Wasipeane vyeo kwa misingi ya udugu, udini na ukabila bali uwajibikaji uwe ndio kigezo mama... !" alifoka Kachero huku anajimwagia sera za siasa peke yake ndani ya gari, anapigapiga ngumi kwenye usukani wa gari yake kwa hasira.

Alipotupia jicho tena kwenye saa yake ya mkononi akaona inasoma saa 9:50 alasiri, hii ni kuonyesha amebakiza dakika 10 tu kufikia muda wa miadi. Akatoa simu ya mkononi na kuitafuta namba ya kijana Alex aliyompa jana.

Alikuwa anataka kumfahamisha juu ya foleni hiyo hivyo awe na subira. Alichoshangazwa simu aliyokuwa anapiga ikawa inaita bila kuleta majibu mpaka ikakatika. Akarudia tena mara ya pili kuipiga simu ya Alex ikaita kidogo halafu ikakatwa.

Alipopiga tena mara ya tatu, akakutana na jibu lililompa mashaka, ni lile linalosema "Mtumiaji wa simu unayempigia hapatikani kwa sasa, jaribu tena baadae". Hapo hapo machale yakamcheza akahisi kuna jambo litakuwa limetokea kwa yule kijana wao, iweje mpaka simu yake ikatwe.

Akapiga simu kwa kijana wake wa gereji hapo hapo maeneo ya Mwenge aje kulichukua gari. Baada ya dakika 10 yule kijana wake wa gereji akawasili wakakabidhiana gari.

Kachero Manu akashuka kwenye gari na kudaka bodaboda akashika uelekeo wa kuelekea 'Mlimani City Mall'. Foleni ilikuwa imezidi kutia fora uelekeo wa kwenda mpaka Ubungo.

"Lazima kuna ajali imetokea sio bure foleni hii" alijisemesha Kachero Manu kwa sauti ya wastani ili kuweza kudukua taarifa zozote kutoka kwa huyu bodaboda. "Sio ajali kaka yangu, nasikia kuna mauaji yametokea muda mfupi uliopita kwenye hiyo Hoteli mpya ya 'New Star Hotel', watu wawili wameuliwa kikatili, hivyo askari ndio wamefunga kwa muda pale kwenye mzunguko wa barabarani mbele" alijibu Bodaboda huyo huku wakiwa wamefika kituo cha Daladala cha Lufungila.

Maelezo yale ya muendesha bodaboda yalikuwa kama mkuki wa moyo kwa Kachero Manu, na kuamua kufanya maamuzi ya haraka mara moja bila kupepesa macho. "Nishushe hapa hapa tafadhali" aliongea huku akirukia chini wakati hata kabla bodaboda haijasimama vizuri. Akatoa noti ya shilingi 5,000/= halafu bila kusubiria chenji akaanza kukimbia kuelekea uelekeo wa 'New Star Hotel'.

Dereva bodaboda alijaribu kumpayukia Kachero Manu arudi kuchukua chenji yake lakini wapi, akatia pamba masikioni na kuzidi kutimua mbio. Bodaboda yule akabakia amepigwa na bumbuwazi huku kwenye fikra zake akitilia mashaka utimamu wa akili wa abiria wake yule. Fikra za Kachero Manu zilimtuma kuwa aliyeuliwa lazima mmoja wapo atakuwa ni kijana wake Alex tu na sio mwingine.

"Pisha pisha, sogea pembeni...!" alitoa amri Kachero Manu huku mkono wake wa kushoto unapepea angani na bastola mkononi. Alikuwa ameshauvaa uso wa kazi, macho yake yanaonyesha kuwa fanya fyoko akudonyoe risasi, hataki masihara na kiumbe chochote kwenye kazi. Akafanikiwa kupenyapenya mpaka ndani ya Hoteli hiyo.

Ndani humo, askari kanzu lukuki wa jeshi la polisi walikuwa wametanda wanaendelea na uchunguzi wao kwa kufanya mahojiano na watumishi mbalimbali wa Hoteli hiyo. Akaonyesha kitambulisho chake cha kazi, wakamruhusu nae aungane nao katika harakati za kuwabaini wahalifu hao.

"My God....They will pay the price of this crime..!" aliropoka Kachero Manu baada ya kuuona mwili wa kijana Alex Turabu ukiwa umelazwa chali sakafuni, damu zinamchuruzika kutokea kifuani huku ametobolewa macho. Akawa anakumbuka taswira ya jana yake usiku walipoongea na kuonana na Alex kwa mara ya kwanza na ya mwisho, kwenye uwanja wa mpira wa miguu wa Chambezi, Bagamoyo.
IMG-20200427-WA0086.jpeg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Alipoangaza ndani ya chumba kile kuangalia kama ataambulia chochote kitu kwenye upelelezi wake, akaona vitu mbalimbali zimetawanyika sakafuni kuonyesha kuna vitu walikuwa wanavitafuta chumbani mule wale wahalifu. Pia akashuhudia matone ya damu yamesambaa sehemu mbalimbali za chumba mpaka kwenye mashuka, kuonyesha kuwa Alex hakufa kikondoo, alipambana nao maadui zake hakukubali kusalimu amri kwao kirahisi.
Kachero Manu akafanikiwa kuingia kwenye chumba kingine alichoelekezwa napo kuna mauaji yametokea. Kilikuwa ni chumba mkabala na kile alichouliwa Alex. Huko akakutana na mwili wa mtu mzima wa makamo umri wake takribani kama miaka 55, nae akiwa amelazwa kifudifudi tumbo wazi na chini amevalia pajama rangi nyeupe, akiwa amepigwa risasi ya kisogoni damu zinamchuruzika toka kichwani.
Akatanabahi kuwa huyo ni Profesa wake kijana Alex, raia wa Msumbiji aliyekuja kumsimamia utafiti wake kwenye zao la muhogo kama alivyosimuliwa na Alex jana yake usiku. Hapo baada ya kufanya speksheni ya muda mfupi ile ya haraka haraka hakuambulia kitu chochote kinachoweza kumsaidia kubaini wahalifu wa tukio hilo.
Mwishoni kabisa kabla hajafanya maamuzi ya kuondoka Hotelini pale akapatwa na wazo. Akaomba kufanya mahojiano na Meneja wa Hoteli hiyo ya 'New Star Hotel', akakaribishwa kwa moyo mkunjufu kwenye Ofisi ya Meneja.
Kachero Manu: "Habari yako Bwana Meneja, mimi ni Afisa upelelezi toka Polisi Makao, Makuu Tanzania, kwanza pole na matukio haya yaliyotokea Hoteli mwako" alijitambulisha huku akidanganya kituo chake cha kazi kwa makusudi.
Meneja: "Habari yangu ni nzuri, namshukuru Mungu, tumeshapoa ingawa ni tukio lililotusikitisha kwa sababu litatupotezea wateja kwenye Hoteli yetu mpya", kwa kutupaka matope kuwa hatuna ulinzi madhubuti "
Kachero Manu: "Je tukio mmeligundua utokeaji wake saa ngapi? "
Meneja: " Tukio tumeligundua saa 8:45 mchana baada ya mhudumu wetu kushuhudia damu inavuja chini ya mlango wa kijana Alex, ndipo tulipofungua mlango tukakuta ameshafariki. Tulipotaka kwenda kumpa taarifa huyu Mzee wake aliyekuja nae pamoja nae tukakutana ameuliwa kinyama" aliongea kwa uchungu mkubwa huku machozi yakianza kumlengalenga.
Akachomoa hanchifu yake toka kwenye mfuko wa suruali yake na kuanza kuyadhibiti machozi yasibubujike kwa kuyafuta kisha akairudisha.
Kachero Manu: "Pole sana, jikaze tumalizie mahojiano yetu, je kuna watu wowote unamuhisi kuhusika na matukio haya?
Meneja: "Mmmhhh..... Kuna wateja wanne waliingia kwa kupishana siku moja na hawa marehemu, wanazungumza Kireno na Kimakonde, hao tunawahisi kwa sababu wametoweka wote kwa pamoja. Pia usiku wa kuamkia leo nimepewa taarifa kuwa manane ya usiku alikuja Mzee mmoja amechanja chale za kimakonde usoni kuonana nao wageni waliotoweka ingawa hatujui walichokuwa wanaongelea, kaondoka majira ya alfajiri jogoo la kwanza"
Kachero Manu: "Nitahitaji kwenda kwenye chumba chenye CCTV Kamera, nikawaangalie sura zao hao washukiwa"
Meneja: "Bila ya shaka Mkuu" akajibu huku akinyanyuka kitini na kuongoza njia mguu kwa mguu kuelekea kwenye chumba cha kuhifadhi mtambo wa Kamera.

Hisia za Kachero Manu dhidi ya Bwana "Andenga Kazimoto", Meneja Mkuu Shirika la Gesi na Mafuta, Tanzania (SGMT) kuwa ni kibaraka wa wahalifu wanaoua raia wa Tanzania nchini Msumbiji zilianza kujipa taratibu.
Utakumbuka Kachero Manu siku alivyoitwa Ofisini kwa Bosi wake wa Idara ya Usalama Bwana Mathew Kilanga kukabidhiwa jukumu la kuelekea nchini Msumbiji katika Jimbo la Cabo-Delgado kufanya taftishi yakinifu ya kuwabaini wahalifu wanaowafanyia unyama Watanzania, alikosa imani kabisa na mmoja wa wajumbe waalikwa wa kikao kile.
Hakuwa na ushahidi wala sababu kuwa na dhana mbaya dhidi yake isipokuwa ni hisia zake tu ndio zilimuongoza kuwa sio mtu mzuri na hakustahiki kuhudhuria kikao kile. Sasa hisia zake dhidi ya Bwana Andenga Kazimoto kumbe zilikuwa sahihi. Gari yenye namba ya usajili ya Shirika la Gesi na Mafuta, Tanzania (SGMT) ndio lililokuwa limetumika kuwaleta washukiwa hao wa mauaji katika Hoteli ya 'New Star Hotel' siku ya kwanza walipowasili Hotelini hapo.
Hii ni kutokana na picha mnato za CCTV-Kamera alizozichunguza Kachero Manu. Busara zikamuongoza kutokufanya pupa ya kumtia mbaroni Bwana Andenga Kazimoto ili washirika wake wasigutuke mapema wakaharibu ushahidi. Kwa kawaida nyoka anagongwa kichwani ili afe kirahisi, hivyo kichwa cha wahalifu hawa ni Jimboni Cabo-Delgado, hana jinsi lazima aende huko.
Pia hata kama angefanya maamuzi ya kumtia mbaroni, bado ulibakia kuwa ni ushahidi wa kimazingira tu usingetosha kumuhusisha kwa asilimia 100% Bwana Andenga Kazimoto. Pia kwenye kamera hizo, alifanikiwa kuzinyaka picha za wahalifu idadi yao 5 na kuamuru siku ya pili yake tu zichapishwe kwenye magazeti mbalimbali kusaidia upatikanaji wao vidagaa hao mamluki wa uhalifu.
Huku kiangaza macho cha shilingi milioni 5 kikiwekwa kwa mtu atakayefanikisha kutoa taarifa za kukamatwa kwa mhalifu yoyote katika hao. Wa kwanza kugundulika katika vidagaa hao wa uhalifu alikuwa ni Mzee mmoja wa kimakonde anayejulikana kama Mzee Mnangwa. Mzee huyu alikuwa ni mmoja wa walinzi vibarua wa muda mrefu tokea miaka ya 70's kwenye Shamba la Utafiti la Chambezi, Mjini Bagamoyo.
Wakazi wa pale walikuwa wanamfahamu kama kibarua tu, mlinzi wa shamba lakini kumbe alikuwa ni zaidi ya wanavyomjua. Huyu Mzee ni veterani wa Jeshi la ukombozi wa nchi ya Msumbiji kupitia kambi ya vijana ya FRELIMO enzi hizo. Alikuja Tanzania na wenzake kupata mafunzo ya kijeshi katika kambi ya Ruvu, Mkoani Pwani.
Baada ya kurejea nchini kwao kuendesha mapambano ya Kivita na Wakoloni wa Kireno na nchi ya Msumbiji kufanikiwa kupata Uhuru mwaka 1975, Mzee Mnangwa na baadhi ya wenzake walirudishwa Tanzania kwa mara ya pili kinyemela, wakiwa kama majasusi mwenye kulinda maslahi ya nchi ya Msumbiji nchini Tanzania.
Mzee Mnangwa akapangiwa eneo la Bagamoyo, maisha kwake yakawa yanasonga, akipata kibarua cha kuzugia cha ulinzi katika mashamba ya Chambezi kumbe ni jasusi. Akawa anaishi kwenye kitongoji chenye idadi lukuki ya Wamakonde, kinaitwa 'Makondeko', jirani kabisa na shamba la Chambezi.
Ndipo vibaraka wa Dola walipozitilia mashaka nyendo za kijana Alex na Profesa wake wakamkabidhi rungu la kuwadodosa na kuwapekenyua kama kweli wapo kwenye utafiti wa kilimo au wana ajenda zao nyuma ya pazia. Mzee Mnangwa alifanikiwa kuzipata namba za gari la Kachero Manu aliloenda nalo shambani Bagamoyo usiku usiku wakati anaenda kukutana na kijana Alex.
Kama ujuavyo zege halilali, Usiku huo huo akazileta zile namba kwa waliomtuma ambao walifikia pia 'New Star Hotel'. Mpaka kufikia majira ya alfajiri wakafanikiwa kulitambua kuwa hilo ni gari la Kachero nambari wani wa nchi ya Tanzania. Hivyo hukumu ya kifo ikasomwa toka Jimboni Cabo Delgado, nchini Msumbiji kuwa Alex na Profesa wake wauliwe kwa njia yoyote.
Kachero Manu baada ya kupata penyenye za kutambuliwa kwa Mzee Mnangwa, akatuma vijana wake mahiri kuelekea Bagamoyo kuhakikisha wanamtia mbaroni mzee huyo. Kachero Manu alikuwa anamsubiria kwa hamu kubwa ili awe ndio chanzo cha kuwataja wahusika waliomtuma. Vijana wa kazi walivyorudisha mrejesho walikuja na majibu ya kukatisha tamaa.
Baada ya kuelezea kuwa Mzee Mnangwa ameyeyuka kama samli juu ya kikaango cha moto, hajulikani alipotokomea. Kila aina ya juhudi ilifanyika ili kumtia mbaroni lakini wakaambulia manyoya tu, ameshawachurupuka tayari.
Kachero Manu akaanza kuumiza kichwa mpaka akaamua ajilipue kwa kumfuatilia dereva wa gari la "Shirika la Gesi na Mafuta Tanzania" (SGMT) ili huenda akatoa penyenye za wapi alipowachukua wale wahalifu na wapi walipo hivi sasa. Alichokutana nacho kwenye taftishi yake hiyo kilitisha mno.
Afisa Rasilimali watu wa Ofisini kwake alitoa taarifa kuwa ameanza likizo yake ya mwaka tokea jana yake. Alipoenda nyumbani kwake ndipo akakutana na tukio la kutisha na kuogofya. Alikuta nyumba yake imefungwa kama vile wakazi wake wamesafiri safari ya mbali. Alipofanikiwa kuingia ndani ya nyumba hiyo kwa utundu wake anaoujua, akakuta maiti ya dereva huyo, mkewe na mtoto wake mmoja mchanga, wote wameuliwa kinyama wakiwa wamefungwa kamba.
Hii hali aliyokutana nayo ikampa hofu kubwa Kachero Manu na kumuongezea umakini kwa kutambua ya kuwa anapambana na genge la wahalifu ambao wapo makini sana, hawataki kuacha hata chembe ya ushahidi utakaosababisha watiwe hatiani.
Sasa rasmi Kachero Manu akatakiwa asafiri kichwa mchunga kuelekea Msumbiji akiwa hana bee wala chee ya sehemu atakayoenda kuwafuma Mafioso hao wa Cabo-Delgado.


SURA YA TATU
Kachero Manu “Mwiba wa Tasi”
Kachero anajulikana kwa jina la ubatizo kama 'Emmanuel Joseph' akiwa ni mtoto wa pekee katika familia ya Mzee Joseph Mbali na Bi.Josephina Nyagali. Alizaliwa mwaka 1985 kipindi cha hekaheka za Uchaguzi wa Rais wa Awamu ya Pili, Ndugu Ali Hassan Mwinyi, katika kijiji cha Mahiwa kilichopo wilaya ya Lindi Vijijini.
Baba yake mzazi Mzee Joseph taaluma yake alikuwa ni dereva aliyeajiriwa katika hospitali ya Misheni ya Nyangao, na mama yake Bi Josephina alikuwa ni mama wa nyumbani tu, anayejishughulisha na kazi za kilimo na ujasiriamali mdogo mdogo.
Sasa huyu kijana wao alipachikwaje hili jina la "Manu Yoshepu"?. Hili jina ni mbwembwe tu za utamkaji katika kabila lake la asili la Wamwera. Jina kama Emmanuel wao wanaita "Manu", na Joseph wanalitamka "Yoshepu".
Katika nchi hii, Wamwera ni moja ya kabila ambalo wana lugha ya kiswahili yenye vionjo vya aina ya kipekee kabisa. Mfano sentensi ya kiswahili ukisema "Nataka kuvua nguo" wanasema "Nataka kuchojoa nguo", pia ukisema "huyu ana sura mbaya" utawasikia wakisema huyu "ntu ana sura ya kunyata" na vionjo vinginevyo vingi vitakavyokufanya uwapende tu utake usitake.
Kabila hili tabia zao za ujivuni hutaniwa kuwa mapacha zao ni Wahaya. Mtu wa kabila hili akienda shule hutomtaka kwa hizo mbwembwe zake. Wamwera ni kabila linalopatikana kwa wingi katika mkoa wa Lindi katika maeneo ya wilaya ya Nachingwea, Ruangwa, na Lindi vijijini.
Inasemekana asili yao ni Kaskazini Magharibi mwa nchi ya Msumbiji. Waliingia Tanzania katika kipindi cha kati ya karne ya 12 mpaka 16 wakimkimbia kiongozi wao mkatili akiitwa Sultani Sadala.
Kwa asili Wamwera ni mashujaa sana, hasa ikikumbukwa katika vita ya Majimaji, Wamwera wa Nachingwea wakiwa juu ya milima Ilulu, walishiriki bega kwa bega kwenye vita hivyo, wakiwaporomeshea mawe na mishale askari wa Kijerumani.
Manu alilelewa katika maadili mufti kabisa ya dini ya Kikristo, madhehebu ya Kikatoliki. Manu tokea utoto wake hakuwaki kuwa goigoi abadani. Daima alikuwa ni mtoto shujaa, mkakamvu, mchapakazi, mwerevu na mwenye umbile lililogangamala la kikubwa. Kiasi kwamba wengi walikuwa wanajua anadanganya umri wake kama wanavyodanganya watu wa nchi za Afrika ya magharibi kama Naijeria, Ghana, Togo na Cameroon ili wapate kucheza timu za soka la kulipwa huko Ulaya.
Ukakamavu wake unaokumbukwa na kijiji kizima, ni kwenye tukio lililotokea akiwa darasa la 6. Tukio lake hilo lilikuwa la kumkimbiza mwizi aliyepora mkoba wa mwalimu wake wakati wa mashindano ya shule za msingi UMITASHUMTA yaliyokuwa yanafanyika katika viwanja vya shule ya sekondari Mahiwa.
Alikimbizana na huyo kibaka kwa umbali wa kilometa 4, akafanikiwa kumtia mbaroni kibaka huyo peke yake maeneo ya Nyangao Sokoni. Mpaka walivyofika raia wema kumuokoa kibaka huyo walikuta tayari kashavimbishwa manundu ya kutosha usoni mwake na Manu.
Kutokana na uwezo huo mkubwa wa mbio aliouonyesha wa kumkimbiza umbali mrefu mwizi huyo bila kuchoka, kamati ya UMITASHUMTA Mkoa kwa kauli moja ikampitisha moja kwa moja kuwa mshiriki wa mbio ndefu za meta 5000 Kitaifa bila kushindanishwa na mwanafunzi yoyote.
Alipomaliza elimu ya shule ya msingi mwaka 1998 alichaguliwa kujiunga na sekondari ya wavulana “SONGEA BOYS” akiwa ni miongoni mwa wanafunzi bora 10 kwa mkoa mzima wa Lindi. Lakini mama yake Manu, Bi. Josephina alikuwa ni muumini mzuri sana wa madhehebu ya kikatoliki, tena Mfia dini haswa akafanya maamuzi ya kumpeleka mtoto wake katika shule ya Sekondari ya Seminari ya Namupa, ambayo ni kijiji cha jirani tu kutoka Mahiwa.
Lengo alitaka mtoto wake aje kuwa Padri amtumikie Mungu, katika maisha yake yote ya duniani. Mtoto wao akadurusu Namupa Seminari mpaka kidato cha 6 mwaka 2005 akafaulu kwa kiwango cha daraja la I na pointi 5 katika mchepuo wa Historia, Jiografia na Uchumi "HGE". Baada ya hapo akachaguliwa kujiunga na Seminari Kuu ya Peramiho, huko Ruvuma kuendelea na masomo ya Upadri.
Lakini siku zilivyokuwa zinasonga akawa kashapoteza wito wa kuitumikia dini katika maisha yake yote. Hasa ukichukulia kwa wazazi wake yeye alikuwa ndio mtoto wao wa pekee, hivyo kama angejiunga na upadri maana yake ni kuwa wazazi wake wasingepata wajukuu hata wa dawa. Hivyo kupelekea kupunguza idadi ya wana ukoo wao.
Akaamua kufanya maamuzi magumu na mazito ya kukacha masomo ya Upadri na kuamua kujiunga na Chuo Kikuu cha Dodoma, akisomea shahada ya sanaa ya mambo ya kudhibiti uhalifu "BA Criminology". Akiwa mwaka wa kwanza tu Chuo Kikuu mwaka 2006 ndipo Bosi wake Mathew Kilanga alipoenda kuwafanyia usaili wa kujiunga na idara ya usalama wa nchi.
Hasa ukichukulia digrii ya “Criminology” ilikuwa ndio imeanza kufundishwa hapa nchini na Chuo Kikuu cha Dodoma kikiwa ndio chuo pekee kinachofundisha elimu ya kupambana na uhalifu.
Katika darasa lao la wanafunzi 20 ni “Manu” pekee ndiye aliyefikia viwango vya Bosi Mathew Kilanga. Ikabidi aombewe ruhusa ya kusimamisha masomo ya Chuo Kikuu kwa muda kwa ajili ya kupelekwa nchini Marekani kwenye mafunzo ya juu zaidi ya usalama na ukomandoo kwa muda wa miaka mitatu (3), kwa masharti ya kupewa ajira pindi tu akifanikiwa kumaliza vizuri mafunzo yake.
Hapo ndipo alipotenganishwa na mpenzi wake, asali wa moyo wake Faith Magayane. Lakini kutokana na umahiri wake katika medani za mapambano ilibidi amalize mafunzo yake kwa muda wa miaka miwili pungufu kwa mwaka mmoja.
Tukio lililomjengea historia ya kukumbukwa na idara zote kubwa duniani za usalama ni kitendo chake cha kumtoboa utumbo kwa bahati mbaya mwalimu wake wa sanaa za mapigano kutoka China wakati anajifunza mtindo wa mapigano ya kutumia ncha za vidole unaitwa “Dim Mak”.
Kutokana na tukio hilo mwalimu wake huyo alipendekeza apewe cheti cha kuhitimu kabla ya muda na hapo hapo akapachikwa jina la utani na wanachuo wenzake la “Mwiba wa Tasi”.
Tasi ni aina ya samaki asiye na magamba anapatikana baharini ila ana miba mbaya sana, ikikuchoma maumivu yake yanaweza kudumu hata wiki nzima. Sasa wenzake walifananisha tukio lake la kudonyoa utumbo wa mwalimu wake wa Kichina kwa kutumia vidole na maumivu ya mwiba wa tasi.
Aliporejea nchini Tanzania mwaka 2008, akapewa ajira rasmi ya kuitumikia Idara ya Usalama akianzia na cheo cha Kachero Msaidizi, na mtihani wake wa kwanza mwezi mmoja tu baada ya kurejea nchini ikawa ni kushirikiana na kikosi cha Umoja wa Afrika kumuondoa madarakani muasi Janali Mohammed Bacar wa visiwa vya Anjouan.
Vikosi vya Comoro na vya Umoja wa Afrika vikijumuisha majeshi ya Tanzania na Sudan, vilianza uvamizi wao katika mji mkuu wa Nzouni-Mutsamadu na katika uwanja wa ndege. Kachero Manu ndio alikuwa mtu wa kwanza kuingia katika Kasri la Kanali Mohamed Bacar linaloitwa "Dar el Najah" huko Anjouan, si mbali na mji mkuu wa Mutsamadu.
Aliingia kwenye jumba hilo kupitia mfumo wa maji taka wa hapo mtaani, na ilibaki kidogo tu amtie mbaroni kwa mikono yake mwenyewe ila Kanali Muhammed akawahi kutoroka kwa kutumia ndege ndogo ya kukodi iliyoruka kutoka kwenye uwanja mdogo wa nyumbani kwake na kukimbilia nchini Madagascar.
Baada ya kuitekeleza kazi hii kwa uaminifu na umahiri mkubwa, akapandishwa cheo mpaka kuwa Kachero namba moja wa nchi nzima. Kisha mwaka 2009 akarejea Chuo Kikuu cha Dodoma kuendelea na masomo yake ya shahada ya kwanza, ambayo aliimaliza mwaka 2012.
Kitendo chake cha kurejea tena Dodoma ndio kilimfanya mpenzi wake Faith Magayane atafute kazi Jijini Dodoma ili awe karibu na Kachero Manu aweze kupalilia vizuri penzi lake lichanue bila shida. Alivyomaliza masomo yake akajenga nyumba yake maeneo ya Mbezi juu, wilaya ya Kinondoni, Dar es salaam akawa anaishi huko tokea mwaka 2014 mpaka sasa.
Chambilecho "Mzigo mzito mtwishe Mnyamwezi", sasa Kachero Manu alikuwa amepewa mtihani mzito wa kwenda Msumbiji kuchunguza chanzo cha machafuko dhidi ya Watanzania wanaoishi huko. Muda wa mapumziko kwake ulikuwa umeisha, alitakiwa aende kuwa kinara kwenye uwanja wa vita, akavuje jasho na damu, kufa au kupona, punda afe, mzigo ufike.
Kwake yeye "Mwiba wa tasi" ilikuwa ni ufahari mkubwa kuaminiwa na Taifa lenye vichwa zaidi ya milioni 55. Minghairi ya hiyo, lakini pia kurudi nchini Msumbiji sehemu ambayo ndio asili za mababu zake wa kimwera kwake ilikuwa ni moja ya fursa adhimu.
Kama ujuavyo kwa asili Msumbiji na Tanzania ni ndugu wa damu, hivyo alikuwa na hamu ya kuwatambua vinara wa chokochoko hizo zinazoendelea. Kisha awashikishe adabu iwe onyo kali kwa wengine wenye kutamani kuchafua mahusiano maridhawa baina ya Tanzania na Msumbiji. Mahusiano yaliyorithishwa na mababu tangu na tangu.

Historia ya Uhuru wa Msumbiji
Kachero Manu kwa muda wa siku mbili mtawalia, kuanzia tarehe 12/02/2016 alikuwa amejifungia ndani nyumbani bila kutoka nje kama mwali anayetawa. Alikuwa anapata mahitaji yote muhimu maskamoni, akimuagiza mtumishi wake wa kiume wa nyumbani amletee kila anachohitajia.
Kwanza kabisa alianza kubukua kabrasha la faili la rangi nyeusi lenye karatasi nyeupe ila zimepoteza nuru yake kutokana na kukaa muda mrefu kwa zaidi ya miaka 56. Alipoanza kulisoma akarejesha kumbukumbu zake miaka ile yupo Sekondari, Seminari ya Namupa anasoma somo la Historia, moja ya masomo ambayo alikuwa analimudu kwa kiwango cha juu sana.
Humo akakuta historia ya chama cha ukombozi cha Msumbiji chenye jina la lugha ya kireno "Frente de Libertação de Moçambique" (FRELIMO). FRELIMO ilianzishwa mwaka 1962 na muasisi wa ukombozi wa Msumbiji Bwana "Edwardo Mondlane" kwa msaada mkubwa wa Rais wa Tanganyika wakati huo Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Lengo la FRELIMO ilikuwa ni kuiweka huru nchi ya Msumbiji na dahari ya dhulma za mkoloni wa Kireno. Makao makuu ya FRELIMO yakawa ni Dar és Salaam kwa muda wa miaka 13 kuanzia 1962-1975. Ili kuhakikisha nchi za Kusini mwa Afrika zinapata ukombozi, Mwalimu Nyerere aliunda kamati maalumu, wakiwemo Jenerali Sarakikya, Brigedia Hasheem Mbita, Kanali Ally Mahfoudh, na Kanali Ameen Kashmeer.
Hivyo vichwa vilivyoteuliwa na Nyerere vilikuwa ndio injini ya kuamsha vuguvugu la kupigania Uhuru wa Msumbiji. Wakaanza kupokea vijana wa Msumbiji mwishoni mwa 1964 waliokuwa wanasoma Vyuo Vikuu nchini Ureno, lakini wakakacha masomo yao kwa sababu ya kutaka kupigania uhuru wa Msumbiji kutokana na kusukumwa na wimbi la uzalendo wa nchi yao.
Baadhi ya vijana hao walikuwa ni Samora Machel, Philipe Magaie, Joachim Chisano, Raimundo Pachinuapa na Marcelino Dos Santos. Vijana hawa walipewa mafunzo kamili ya kijeshi na ya kisiasa kisha wakapelekwa Algeria kwa mafunzo zaidi, hasa ukichukulia kipindi hiko Algeria walikuwa wametoka kwenye vita ya kumuondoa Mfaransa.
Hivyo Algeria ilichukuliwa kama ni sehemu sahihi ya kujifunza mbinu za medani ya vita. Serikali ya Cuba nayo haikubaki nyuma kwenye kuunga mkono harakati za kupigania Uhuru wa nchi za Kiafrika, ikamleta nchini Tanzania Balozi Pablo Ribalta.
Huyu balozi ndiye, ambaye alikuja kama mshauri wa mbinu za ukombozi na ndio alifanikisha ujio wa bingwa wa vita vya msituni Ernesto Che Guevara 1965. Che Guevara, Muajentina huyu mwenye misimamo mikali ya siasa za kimapinduzi, kwanza alifanya mkutano na viongozi wote wa ukombozi wa kusini mwa bara la Afrika. Kwa bahati nzuri kwenye mkutano huo, kiongozi wa FRELIMO, Bwana Mondlane nae alihudhuria.
Kikubwa Che Guevara aliwasisitiza kushikamana kwa umoja baina yao ndio silaha yao kubwa itayowawezesha kuyaangusha majeshi makubwa, tena yenye silaha na zana nzito za kivita. Sumu hizi walizolishwa akina Mondlane na mwanaharakati wa kutukuka Bwana Che Guevara zikawasha moto wa mapambano katika mioyo yao na kuunguza kabisa chembechembe zote za uoga katika miili yao.
Vijana wa Msumbiji wale waliopelekwa nchini Aljeria, walivyorudi nchini Tanzania walipelekwa moja kwa moja kambini eneo linaloitwa "Farm seventieen "Nachingwea, Lindi. Huko kambini sasa wakaanza kuandaliwa kwenda kuanzisha vita vya ukombozi kwa njia ya mtutu wa bunduki.
Wapiganaji hao wa FRELIMO hawakuwa wengi, walikuwa hawazidi hata elfu moja (1,000), lakini idadi kubwa ilikuwa ni wanajeshi wa Tanzania (JWTZ). Alipofika kwenye maelezo hayo, Kachero Manu akapigia mstari, na kuanza kufanya tafakuri jadidi na kuanza kujiuliza.
"Inawezekana vipi watu ambao wamesaidiwa kujikomboa kwa kutumia mali na damu za raia wa nchi nyingine leo wawageuke kuwafukuza nchini mwao tena kwa ukatili, ubakaji na mauaji?. "Lazima tu kuna nguvu ya mabeberu toka za Ughaibuni lakini wanaficha ajenda zao za siri kwenye migongo ya watu wa Msumbiji wale wasiofahamu historia ya Uhuru wa nchi yao na wenye tamaa za kujinufaisha kiuchumi bila kujua thamani ya Watanzania kwao".
Kisha akaendelea kuperuzi kabrasha hilo humo akakutana na maelezo kina yakielezea jinsi Kanali Mahfoudh Mtanzania chotara wa kiarabu aliyehitimu mafunzo ya kikomandoo namna alivyofanikiwa kujipenyeza kwenye kambi za Wareno huko katika miji ya Cabo-Delgado na Xai-Xai kufanya upelelezi wa kujua nguvu za jeshi la Wareno na udhaifu wao.
Hapo tena Kachero Manu akavuta tafakuri jadidi, "ina maana Wareno toka mwanzoni walijikita Cabo-Delgado, na sasa machafuko dhidi ya Watanzania yameanzia Cabo-Delgado, hapa kuna kitu maalumu chenye mahusiano kati ya wakoloni na huu mji wa Cabo-Delgado sio bure" alitafakari kwa kina Kachero Manu.
Akatambua hapa kuna siri nzito imejificha ambayo inabeba fumbo kubwa la machafuko hivyo anahitajika kuitegua siri hiyo na kuiweka bayana. Na kama akifanikiwa kuitegua hiyo siri ndio kitajulikana kiini halisi cha machafuko dhidi ya Watanzania wasio na hatia yoyote. Kisha humo akaendelea kusoma akakuta namna mapambano yalivyoendeshwa kwa muda wa miaka 13 mpaka Uhuru kamili wa Msumbiji ulivyopatikana tarehe 25/06/1975.
Kingine cha kilichomstaajabisha kwenye nyaraka hizo ni kuwa Marais wote wa Msumbiji kwa awamu zote waliishi Tanzania, kuanzia Samora Machel, Dr.Joachim Chissano, Armando Gwebuza na mpaka Rais wa sasa Filipe nyusi wote kwa ujumla waliishi katika kambi mbalimbali za hapa Tanzania kuanzia Nachingwea, Tunduru, Liwale na Kongwa. Kwa ufupi unaweza ukaleta hitimisho kuwa Tanzania ndio Chuo Kikuu cha kuwapika Marais wa nchi ya Msumbiji.
"Huu nao ni uthibitisho wa wazi kuwa huwezi kutenganisha mafanikio ya Msumbiji na nchi ya Tanzania" aliwaza Kachero Manu. Baada ya kumalizana na kabrasha hilo akafungua lingine linaloelezea kwa kina vita baina ya wapigania uhuru wa Msumbiji dhidi ya Wareno iliyoanza tarehe 25/09/1964. Ambapo wapigania uhuru wa jeshi la ardhini walivamia ofisi za serikali ya Wareno zilizopo Cabo Delgado, huku jeshi hilo kllikitokea nchini Tanzania.
Hii ikampa udadisi wa kutaka kulifahamu kinagaubaga Jimbo hilo la Cabo-Delgado. Ikabidi avute mtoto wa meza yake ya kusomea, akaitoa ramani ndefu kama mkeka. Akafungua ramani hiyo kubwa ya nchi ya Msumbiji na viunga vyake vyote iliyokuwa imehifadhiwa humo kisha akaitundika ukutani. Akawa analitafuta jimbo la Cabo-Delgado kwa kutumia fimbo yake nyembamba, mpaka akaliona kwenye ramani.
Akakuta ni jimbo lililopo kaskazini kabisa mwa nchi ya Msumbiji. Likiwa na kilomita za mraba zisizopungua 82,625 na idadi ya wakazi isiyopungua watu milioni 2,333,278, likiwa ni jimbo lenye wilaya 16. Huku makabila matatu yakitamalaki ndani ya jimbo hilo, nayo ni Makonde, Makua na Mwani. Makao makuu ya jimbo yakiwa yanaitwa Pemba na miji mingine muhimu ni Montepuez na Mocimboa da Praia.
Baada ya kumaliza kuisoma kwa kina ramani hiyo kwa ujuzi mkubwa hasa ukichukulia shuleni alikuwa mahiri sana kwenye somo la Jiografia usomaji wa ramani 'Map Reading'.
Akaanza kupitia ripoti mbalimbali za kiuchunguzi zinazoelezea hatua mbalimbali zilizochukuliwa mpaka sasa na jeshi la polisi nchini Msumbiji lakini hakuona chochote cha maana zaidi ya maelezo ya mkahawani yasiyoweza kumsaidia chochote kwenye kazi yake mpya anayoitarajia kuianza.
Akaona kazi ni mbichi kabisa anatakiwa aanze uchunguzi wa alifu kwa ujiti. Akafunga makabrasha akaweka nia ya kuelekea Cabo-Delgado kuanza kazi mara moja bila kuchelewa.


SURA YA NNE
"Safari ya Cabo-Delgado yaingia nyongo"
Tarehe 14/02/2016 saa 11:00 kamili alfajiri mwanana yenye kibaridi chepesi, ikiwa ni siku ya Jumamosi, Kachero Manu maarufu kwa jina la "Mwiba wa Tasi" alikuwa amedamka mapema sana kuliko kawaida yake.
Kama sio safari ya kikazi iliyopo mbele yake kwenye hiyo siku angekuwa yupo karibu na mchumba wake kipenzi Faith Magayane wanaendelea kuufaidi usingizi wao. Walipanga siku hiyo ya Wapendanao "Valentine Day" kukicha tu wajiandae kwenda Mbuga ya wanyama ya Mikumi, mkoani Morogoro kufurahia miaka 8 ya safari ya mapenzi yao yalioanza kumea na kuchipua wakiwa tokea Chuo Kikuu cha Dodoma "UDOM".
Sikukuu hiyo ambayo iliyozoeleka sana kwenye tamaduni za Wazungu, lakini kutokana na utandawazi kushamiri na dunia kuwa kama kijiji, ilikuwa pia inaazimishwa mpaka katika nchi za Kiafrika kama Tanzania.
Ila kazi kwanza mapenzi baadae, ilikuwa hamna jinsi lazima Kachero Manu aondoke kwa haraka sana Tanzania kwenda nchini Msumbiji kutekeleza majukumu yake ya kitaifa aliyokabidhiwa kazini kwake. Alipoamka kitandani akafanya mazoezi ya viungo kwa muda wa kama robo saa kisha akaenda kujimwagia maji maliwatoni.
Baada ya kutoka bafuni akaanza maandalizi ya safari. Wakati anavaa ndipo akakumbuka kuwa alipolala saa 6:00 usiku baada ya kumaliza kudurusu nyaraka zake muhimu alitaka mapumziko timilifu hivyo akaamua azime simu zake zote asipate usumbufu wowote.
Akaelekea sehemu alipozihifadhi simu zake na kuziwasha. Simu anayoitumia sana kwa shughuli za kiofisi alipoiwasha haikuwa na ujumbe wowote, akashukuru Mungu maana kama angekuwa ametafutwa na Bosi wake halafu hakupatikana ungekuwa msala mwingine kwa upande wake.
Alipoiangalia simu yake ya matumizi binfasi akakutana na namba ya simu ya Mjomba wake imempigia saa 7:15 usiku kwa zaidi ya mara 8 wakati namba yake haipo hewani.
"Mjomba kama kawaida yake ikifika mwishoni mwa juma ni kupiga vizinga tu vya kuomba hela ya pombe...!" alipuuzia kwanza kumtafuta Mjomba wake hewani akiona simu hiyo haina kipaumbele chochote. Akaanza kuitafuta namba ya mpenziwe Faith ili waagane vizuri kabla hajapaa.
Alishamgusia kwa juu juu kuhusu safari ya ghafla inayomkabili tokea juzi, lakini Faith aliona kama vile anataniwa tu na muhibu wake. Akaipiga simu ikaanza kuita kisha ikapokelewa. "Baby ina maana huko kazini kwenu hamna mwingine wa kutumwa hiyo kazi ila wewe tu?" ilikuwa ni sauti ya mang'oro na kulalamika ya mpenzi wake baada tu ya kupokea simu hiyo.
Hakukuwa na salamu wala nini, alikuwa ametibuka nyongo kwelikweli. "Baby usijali ni ndani ya wiki moja tu nitakuwa nimesharejea kikubwa niombee dua tu nirudi salama, natamani sana nibaki na wewe asali wa moyo wangu ila majukumu ya kikazi ndio yananilazimisha niwe mbali nawe" alijibu Kachero Manu kwa sauti ya kubembeleza hakupenda kabisa kumpa maudhi mpenzi wake.
"Mhhh....haya isije ikawa unaniongopea unaenda safari ya kikazi kumbe unaenda na mchepuko wako huko Cabo-Delgado, na kwanini kwanza mpaka usafiri siku ya wapendanao usingesubiri ipite kwanza, wenzangu wote ofisini watakuwa na wapenzi wao mimi peke yangu nitabaki peke yangu kama kinda wa njiwa aliyefiwa na wazazi" mpenzi wake Faith aliendelea kujilalamisha huku analia kwenye simu kilio cha kwikwi akionyesha haipendi kabisa hiyo safari.
Ongea yake ilionyesha ana joto joto la wivu limeshampanda. Ilibidi Kachero Manu atumie zaidi ya nusu saa kumlainisha mpenzi wake, kwa maneno ya mahaba ya kumtoa nyoka pangoni mpaka akaeleweka. Mwishoni Faith akakubali matokeo kuwa hawezi kuitengua safari hiyo, akamtakia safari njema ingawa alihuzunika sana kushindwa kuwa pamoja na mchumba wake siku kubwa kama hiyo.
Hakuna mtu aliyefahamu kama Kachero Manu anaelekea Mtwara isipokuwa Bosi wake Mzee Mathew Kilanga tu, hata mpenzi wake Faith alimuaga kwa ujumla tu kuwa anaenda Cabo-Delgado lakini atakavyosafiri hakuwa anafahamu atasafiri kwa njia gani.
Kawaida ya Kachero Manu huwa hana imani na mtu yoyote inapokuja suala la usalama wake kwenye kazi. Baada ya hapo akaelekea mesini kupata staftahi ya mkate uliopakwa siagi, mayai mawili ya kuchemsha na kahawa kavu isiyo na sukari. Baada ya hapo akabeba kibegi chake tayari kwa safari.
Ghafla akiwa ameshafunga mlango wa chumbani kwake anaelekea kwenye ngazi aanze kushuka chini, akasikia mlio wa kengele ya nyumba yake kuashiria mtu anataka kuingia ndani ya nyumba. Akaweka chini kibegi na kuanza kushuka ngazi kwa haraka kutaka kujua nani anayegonga mlango.
"Samahani Bosi...mzigo wako umeletwa toka manane ya usiku na mwanadada mmoja, alikuja na gari la kifahari kasema ni zawadi yako ya Valentine Day..!" aliongea Mlinzi wa getini kiunyenyekevu mkubwa huku akiwa anakabidhi boksi hilo kubwa wastani lililonakshiwa kwa mapambo ya rangi nyekundu kwa nje kuashiria ni zawadi maalumu ya siku ya wapendanao.
"Ahsante..!" alijibu kwa ufupi huku akilipokea boksi lile lililokuwa na uzito wa wastani. "Mwanadada..! Gari la kifahari...Tena zawadi ya Valentine..!" yalikuwa maswali anayojiuliza kwa udadisi Kachero Manu wakati anapandisha ngazi kurudi chumbani kwake akiwa amejawa na tashiwishi ya kulifungua boksi hilo ili kujua nani aliyetuma zawadi hiyo kwake.
Zaidi ya mpenzi wake Faith hakuwa na mazoea ya kutumiana zawadi na wanawake. Akaingia chumbani na kujibweteka juu ya tandiko kisha vidole vyake ndio vikawa vinaongea vikianza kulifungua boksi hilo. Alipolifungua tu kwanza akakutana na kadi kubwa imefungwa kwenye karatasi maalumu ya zawadi yeye mng'aro 'gift paper', akaiweka pembeni hiyo kadi akili yake ikiwa ipo kwenye zawadi ya ndani ya boksi.
Ghafla bin vuuu....akapigwa na mshtuko wa mwaka huku akilitupa kwa nguvu boksi hilo alilokuwa amelishikilia juu ya kitanda kwa uoga. Kijasho chembamba kikaanza kumvuja juu ya paji lake la uso licha ya kuwa kiyoyozi kilikuwa kinafanya kazi huku akitwetwa kwa nguvu. Mapigo ya moyo yalianza kukimbia kwa kasi utasema moyo unataka kumchomoka kifuani.
Akawa ametumbua macho yake kuelekea alipolitupia boksi hilo kama fundi saa aliyepoteza nati ndogo sana ya saa anayoitengeneza. Alikuwa haamini kitu ambacho macho yake yanamshuhudisha asubuhi hiyo kilazima. Machozi yakaanza kumvuja bila kizuizi chochote, alishindwa kabisa kujizuia. Alichokiona kwa macho yake kilikuwa ni chenye kuogofya kwenye mboni za macho yake, hakuna cha ukomandoo wakati wa shida, maumivu yanakuwa ni yale yale kama binadamu wengine.
JE KACHERO MANU KAPOKEA ZAWADI GANI YA VALENTINE DAY????
ENDELEA KUFUATILIA


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Iko vizuri mkuu ila maelezo ya watu binafsi yamezidi badala ya kuzingatia maudhui ya riwaya. Huo ni mtizamo wangu tu.
 
RIWAYA: "CABO-DELGADO-PART 05
Kichwa cha kipenzi chake, mama yake mzazi, Bi. Josephina Nyagali kilichokatwaa kwa mtindo wa kuchinjwa na panga kilikuwa ndio kipo ndani ya boksi la zawadi aliloletewa usiku wa manane nyumbani kwake. Kilichokuwa kinamliza ni kifo cha kikatili cha mama yake mzazi, tena akiwa hana hatia yoyote masikini wa Mungu. Yeye akiwa ndio chanzo cha mama yake kupoteza hai kutokana na maelezo ya kwenye barua aliyoikuta ndani ya boksi hilo ikiwa na maandishi makubwa tu. Barua hiyo ilikuwa ikisomeka kama ifuatavyo;
"TUNAJUA UNAJIANDAA KUJA CABO-DELGADO KARIBU SANA MACHINJIONI, LAKINI TAMBUA YA KWAMBA BAADA YA SHINGO YA MAMA YAKO MZAZI, ITAFUATIA YA BABA YAKO MZAZI, YA MCHUMBA WAKO NA JAMAA ZAKO WA KARIBU. KWA USALAMA WAKO NA WA FAMILIA YAKO KAMA KWELI UNAWAPENDA USITHUBUTU KUKANYANG'A CABO-DELGADO"
BY-"BOB-CHINANGA"
Majuto ni mjukuu Kachero Manu akaanza kujilaumu kwa maamuzi yake ya kuzima simu usiku kucha uliopita. Huenda simu zilizopigwa na Mjomba wake zilikuwa zinamfahamisha juu ya tukio hilo. Pia huenda tarishi aliyetumwa kuleta mzigo huo wa kichwa nyumbani kwake angefanikiwa kumtia mbaroni. Akili zikamrudia akatanabahi kuwa yeye ni mtoto wa kiume lazima ajikaze kisabuni ili mambo yaweze kwenda.
Hapo hapo akapiga simu hospitali yao ya kitengo maalumu waje kukichukua kichwa hicho ili wafanye harakati za kukituma Kijijini Mahiwa kikaunganishwe na mwili wa mama yake. Hakuwa na jinsi zaidi ya kusafiri tu kuelekea Cabo-Delgado, kazi yake ya ulinzi wa amani ya nchi ilikuwa ni kazi ya kutanguliza maslahi ya nchi kwanza kabla ya maslahi binafsi.
Alishajipanga kisaikolojia kuwa ataenda kuhani msiba wa mama yake mzazi kama akifanikiwa kurejea salama toka nchini Msumbiji. Hamu kuja kuliona kaburi la mama yake ikawa ni kichocheo kwake cha kujitahidi kuwa na tahadhari ya hali ya juu ili asiuliwe akiwa kwenye uwanja wa vita.
Akampigia simu Bosi wake akimuelezea kwa kinagaubaga mkasa mzima uliomkumba muda mfupi Kabla hajasafiri. Bosi Mathew Kilanga, akampa pole na kumhakikishia kuwa serikali itashirikiana na familia kwa niaba yake kuhakikisha inampa mama yake maziko yenye hadhi ya juu. Wakaagana kwenye simu na Kachero Manu kujiandaa kuelekea Uwanja wa ndege tayari kwa safari.

Kachero Manu alifunga mkanda ndani ya ndege aina ya "Bombardier Dash-8 Q400" kikwangua anga kipya kabisa, mali ya shirika la ndege la Tanzania-ATCL akielekea zake Manispaa ya Mtwara. Alikuwa ameshakabidhiwa na Sekretari wa Bosi wake "Kokunawa" tiketi ya ndege ya kuelekea nchini Afrika ya kusini-Johannesburg, kisha ndege ya kuunga kwenda Pemba makao makuu ya jimbo la Cabo-Delgado.
Taarifa alizopata ni kuwa kuna ndege zaidi ya tano zinazoenda Pemba kwa wiki kutokea Johannesburg, nyingi zikiwa zimejaza watalii. Pia alishapewa hati ya kusafiria mpya yenye jina jipya la Hassan Ibn Hussein, mzaliwa wa Kisiwani, Unguja. Alikuwa amepanga aingie Cabo-Delgado kama mtaalamu wa mambo ya elimu ya kale, anayetafiti majengo ya asili yaliyojengwa na Mreno nchini Msumbiji.
Ili kuendana na muonekano wa utamaduni wa Waunguja kabla hajaondoka alishaenda Kariakoo msikiti wa Kwamtoro ambao upo karibu na soko kuu la Kariakoo, Dar es Salam kununua kanzu na barakashia za kutosha bila kusahau tasbihi ya kiislamu atakayotumia kuzugia kumsabihi Mwenyezi Mungu akiwa barabarani. Aliondoka kwa usafiri wa teksi ya UBBER iliyomfuata nyumbani kwake Mbezi juu na kumpeleka mpaka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere.
Kachero Manu akiwa ndani ya vazi la kanzu rangi ya samawati huku akiwa amevaa makubazi ya rangi nyeusi yenye mkanda katikati unaotenganisha kidole gumba na vidole vingine, huku kichwani akiwa amevalia kofia ya kushonwa na mkono ya rangi nyeusi bila kusahau mkono tasbihi ya rangi ya kijani anaichezesha chezesha laiti ungefanikiwa kumuona ungedhania ni Shekhe wa Mkoa fulani mwenye unyenyekevu na utiifu mkubwa kwa mola wake.
Lakini kabla hajatoka nyumbani kwake kuelekea uwanja wa ndege tayari machale yalishamcheza kusafiri na ndege ya moja kwa moja mpaka nchini Afrika ya kusini. Hasa kutokana na tukio la kuuliwa kwa mama yake mzazi na kukatwa kichwa kisha akatumiwa kichwa hicho, zilikuwa ni salamu kwake kuwa anapambana na genge kubwa la waharifu ambao wana ujuzi na maarifa makubwa.
Hivyo akabadili mawazo ya kwenda Afrika ya kusini na ndege ya shirika la Afrika ya kusini badala yake akakata shauri ya kwenda Msumbiji kwa njia ya barabara kupitia Mtwara kwa ndege ya ATCL. Akaingia kwenye mtandao wa ATCL kupitia kwenye simu yake ya kiganjani, akatoa oda ya tiketi ya Mtwara ya asubuhi akapata na akailipia tiketi ya saa 5:00 asubuhi kwa njia ya pesa mtandao.
Hivyo akawapiga chenga ya mwili maadui zake waliokuwa wanamsuburia kwa hamu wampokee kwa kumteka kwenye Uwanja wa ndege wa Oliver Tambo, Jijini Johanesburg. Akiwa angani akawa anapanga na kupangua namna atakavyoingia katika jimbo la Cabo-Delgado bila kujulikana na maadui zake, huku tukio la kuchinjwa kwa mama yake mzazi akiwa ameshalizika kwenye kaburi la sahau.
Ilikuwa ni safari ya dakika 45 tu kutoka Dar es Salaam mpaka uwanja wa ndege wa Mtwara. Aliposhuka akafanya haraka kutoka nje ya uwanja hakuwa na muda wa kupoteza, nje ya uwanja akakutana na kundi kubwa la madereva taksi wanaogombania wateja. Akaichomoa miwani yake yenye vioo vya giza toka kwenye koti lake, akaifuta miwani hiyo kwa kitambaa laini akaivaa kuzidi kuficha wajihi wake.
Huku akiwa anaburuza begi lake la matairi akaenda kwa mmoja wapo wa wale madereva aliyekuwa amejitenga na wenzake hana papara na wateja. "Salamu Aleikum Ustaadhi, sema nikupeleke wapi bei zangu poa tu hatuwezi kushindwana" aliongea kistaarabu yule dereva huku tayari ameshafungua buti la gari lake kujiandaa kupakiza begi. Akamuambia ampeleke kwenye nyumba ya wageni ambayo ina utulivu mkubwa, haina fujo fujo na haipo mbali sana na kituo cha mabasi.
"Nitakupeleka "Lole Grand Lodge" iliyopo mtaa wa Chikongola utafurahi na roho yako" alisema huku tayari ameshapakiza begi lile kwenye buti na kulifunga. Msafara ukaanza kuelekea kwenye nyumba hiyo ya wageni huku akiwa amekaa siti ya nyuma. Macho yake alikuwa anayatupa, kuangaza huku na kule kupitia kioo cha madirishani ili mradi kuchunga usalama wake wake.
Hakutaka kuanza kupoteza mpambano mbele ya adui zake hata kabla bado mechi haijaanza Mjini Cabo-Delgado. Ndani ya robo saa tu wakawa wameshawasili katika Nyumba hiyo ya wageni. Akamalizana nae malipo yake kisha akatoa begi lake na kutokomea ndani ya jengo hilo.
Bahati nzuri akapata chumba bila shida yoyote. Alivyolipia chumba chake tu, akaanza kunusanusa kama mbwa wa polisi, kuikagua nyumba nzima kujiridhisha usalama. Akagundua kuwa kumefungwa mfumo wa CCTV-Kamera unaorekodi matukio yote hapo "Lodge".
Akatabasamu kisha akaingia chumbani kwake kuweka begi lake na kuweka vitu sawa chumbani kwake. Nako akajipa kama dakika 10 za kukikagua usalama wa chumba, akihofia asije akawa amejiingiza kwenye mdomo wa mamba bila mwenyewe kutanabahi akaja kulia kilio cha kusaga na meno.
Baada ya kujiridhisha, akakifunga chumba kisha akatoka kuelekea kwenye mgahawa mdogo wa hapo hapo alipofikia. Maana njaa ilikuwa inamkwangua vilivyo tumboni utasema ana ugomvi na minyoo ya kwenye utumbo. Alijiwahi mapema kula kabla kasheshe halijanza maana Kachero Manu akiwa na jambo linalomshughulisha hakumbuki kula mpaka atulizane.
Akamuita mhudumu mgahawa akasalimiana nae, kisha akaomba karatasi ya MENU yenye orodha ya vyakula mbalimbali vinavyopikwa hapo mgahawani. Akaipitia haraharaka kisha akataka kuagiza, Ugali kwa samaki samsuli rosti.
"Inachukua muda gani kuandaliwa chakula ninachokitaka"? aliuliza huku akiwa amemkazia macho mhudumu kwa umakini.
Akajibiwa na mhudumu wa upande wa vyakula, "oda yoyote unayotoa ni ndani ya dakika ishirini hadi nusu saa kutegemeana na aina ya chakula unachohitaji". "Basi naomba Ugali kwa samsuli rosti, usiweke chumvi nyingi tafadhali " alisema Kachero Manu kumwambia mhudumu yule.
"Hamna shida, mteja ni mfalme kwetu, je utapenda kinywaji gani nikuletee pia" aliuliza mhudumu yule." "Nitahitaji juisi ya matunda halisi lakini baada ya kumaliza mlo wangu nitakuambia nahitaji juisi ya kitu gani" alijibu kimkato bila kustawisha maneno.
Ndugu msomaji samaki samsuli kama humjui ndio yule alikuwepo kwenye picha ya senti tano ya enzi za Nyerere, ni samaki mwenye mnofu wakati mwingine anaitwa ng'ombe wa baharini unaweza hata kumpikia pilau. Baada ya dakika ishirini na tano kupita, kilihudhurishwa chakula chake mezani.
Akaanza kukishambulia kwa pupa mithili ya mtu aliye kwenye mashindano ya kula au mkimbizi wa Somalia aliyekosa chakula kwa muda wa wiki nzima. Aliupiga mlo huo bila kusaza mabaki yoyote, sahani nyeupe kabisa utasema imetoka kuoshwa.
Alipomaliza akaagiza juisi ya ndimu yenye sukari chache sana kwa ajili ya kushushia mlo. Akanywa, na mara baada ya kumaliza akaletewa bili yake akailipia na kisha moja kwa moja akaenda kulala tayari kwa kujiandaa na safari ya kuondoka usiku kwa usiku kuelekea Msumbiji.

Usiku wa heka heka
Kachero Manu aliamka saa kumi na moja jioni baada ya mapumziko mafupi aliyoyafanya. Alijikuta amelala kwa muda wa masaa manne mfululizo bila hata kushtuka usingizini, dalili ya kuonyesha amechoka sana.
Akafanya mazoezi ya kunyoosha viungo ya muda wa robo saa kisha akaelekea maliwato moja kwa moja akajimwagia maji ya baridi. Alipomaliza akaanza kujiandaa na safari, wakati wa kuvaa nguo ndani akavaa fulana aina ya "ballistic vest" yenye uwezo wa kuzuia risasi kupenya.
Kisha akachagua kuvaa nusu kanzu yake nyeusi mtindo wa Pajama toka Pakistani ili imuwezeshe kupambana kirahisi hasa katika mitindo ya urushaji wa mateke itakapobidi kupambana, pia rangi nyeusi inakufanya usionekane kirahisi hasa kwenye giza hivyo kumpa wakati mgumu adui yako kukutambua.
Chini akavalia viatu vya 'kung-fu' ili kuepusha sauti wakati wa kutembea. Akakagua vifaa vyake vyote muhimu kama vipo salama ikiwemo kalamu maalumu ya kipelelezi 'spy pen' yenye uwezo wa kuchukua video kwa muda wa nusu saa, kupiga picha na kurekodi sauti mpaka umbali wa meta 50.
Bila kuwasahau rafiki zake muhimu sana anaowatumia inapobidi kuondosha roho ya mtu duniani, bastola zake mbili za kisasa aina ya Glock G42 zilizotengenezwa na kampuni toka Australia.
Alipomaliza ukaguzi wake na kujiridhisha kuwa kila kitu kipo katika mustawa sahihi akalifunga vizuri begi lake. Akachomoa pochi lake la kuhifadhia pesa na vitambulisho nalo akalifanyia uhakiki wa haraka haraka. Akakuta kadi zake mbili za benki za Msumbiji kadi moja ya benki ya United Bank of Africa (UBA) na ingine ni ya benki ya Barclays zote zikiwa zimejazwa mkwanja wa kutosha wa kumuwezesha kuishi nchini Msumbiji hata mwaka mzima kama itabidi.
Akasifu kimoyomoyo kazi nzuri ya Sekretari wa ofisini kwao mrembo Kokunawa, kwa kuratibu safari yake kwa viwango kabisa. Ilipofika majira ya usiku mbichi wa saa moja, aliufungua mlango wa kwenye chumba chake kwa tahadhari kubwa, huku macho yake akiyageuza kama kinyonga. Bahati nzuri hakuonwa na mtu yoyote wakati anaufungua mlango. Kabla hajaanza kutembea kwenye veranda ya kuelekea mapokezi, akiwa amesimama pale pale mlangoni pake akiutoa mkono wake nje ya mlango na sehemu ya kichwa chake, akachomoa kifaa chake chenye ukubwa wa kalamu ya kuandikia kinaitwa kitaalamu "Laiser pointer" cha rangi nyeusi akakielekeza kifaa hicho usawa wa Kamera ya CCTV iliyopo juu ya mlango wa kuingilia mapokezi.
Alivyoelekeza kile kifaa hapo hapo CCTV-Kamera ikaacha kurekodi matukio yote kutokana na kuunguzwa na miale ya kifaa chake kile. Uso wake ukavaa tabasamu la ushindi, akakirudisha mfukoni kile kifaa, kisha akatoka nje ya mlango. Akaurudishia mlango aste aste bila kuufunga na funguo kuepusha kelele za funguo kusikika. kisha akachomoa kitambaa chake cha kujifutia jasho akafuta alama za vidole kwenye kitasa cha mlango.
Hakutaka kudharau nguvu ya adui yake hata kidogo, hivyo alichukua umakini mkubwa kwenye kila hatua tokea mwanzo. Akatembea na veranda kinyume na ofisi ya mapokezi akajikuta ametokeza kwenye mlango wa nyuma unaotenganisha vyumba na bustani ya upande wa nje. Kwa bahati mlango ulikuwa umerudishiwa tu, akaufungua na kutembea kama umbali wa meta 10, juu ya kibaraza cha vitofali vilivyolazwa juu ya ardhi 'pavement blocks', akarusha begi lake nje ya ukuta kwanza. Kisha bila kufanya ajizi akajikunja na kuruka ukuta wa kutokea nje kama samaki mkizi. Ukuta ambao ulikuwa na urefu wa zaidi ya meta 7 na juu yake kuna nyaya za umeme maalumu kwa ajili ya kudhibiti wezi.
Akatokemea zake kichochoroni kwenye giza, nia na madhumuni yakiwa ni kuelekea Stendi Kuu ya Mabasi ya Mkoa. Akafanikiwa kupenyapenya kwa kuhangaika bila kumuuliza mtu mpaka akatokeza Stendi Kuu, akashukuru Mwenyezi Mungu.
Stendi Kuu ya Mtwara Mjini, ni Stendi ambayo ina mzunguko wa watu wengi kipindi cha kuanzia majira ya jogoo la kwanza mpaka kufikia magharibi, baada ya hapo kunakuwa na watu wachache tu wenye kujipatia bidhaa za majumbani katika maduka yaliyozunguka stendi hiyo lakini hamna wasafiri. Kachero Manu alivyofika Stendi hapo, kwa usiku ule hakukuwa na Basi dogo la kuelekea Wilaya ya Masasi ambapo anahitaji kwenda.
Lengo lilikuwa afike kwanza Masasi kisha hapo atapanda tena usafiri wa kwenda Wilaya mpya ya Nanyumbu akavizie usafiri wa kuelekea nchini Msumbiji. Akaanza kubuzibuzi maeneo ya hapo hapo Stendi huku akiweka matumaini huenda ukajitokeza usafiri wa ghafla bin vuu, na kama ikishindikana hana budi atasubiria mpaka alfajiri apande Basi dogo.
Mungu si Athumani bwana, kwa bahati nzuri katika kuhangaika kwake kupata usafiri, likaja gari dogo aina ya "Toyota Pick-up" limezungushiwa turubai kwa nyuma, lilikuwa ni gari la idara ya Halmashauri, Wilaya mpya ya Nanyumbu. Gari hilo lilimpeleka Afisa Elimu Wilaya Mjini Mtwara, alikuwa anasafiri kesho yake na ndege ya saa kumi na mbili asubuhi kutokea Mtwara kwenda Dar es Salaam. Dereva huyo alijiongeza, akaamua apate vichwa viwili vitatu wakati anarejea Nanyumbu ili kupunguza ukali wa maisha.
Wenyewe watumishi wa umma wana msemo wao wa kuonyesha kuwa maisha ni magumu kuwa vyuma vimebana hivyo inabidi vilainishwe. Sheria ilikuwa inamkataza kabisa dereva wa gari la serikali kumpakiza mtu asiye mtumishi ndani ya gari la serikali, ila tamaa ya kipato cha ziada ndio ilikuwa inamilikiwa avunje sheria. Walikuwa ni abiria wawili tu usiku huo wenye nia ya kufika Nanyumbu, nao ni yeye Kachero Manu na msichana mmoja mbichi.
Katika maongezi yao na Kachero Manu wakati wanaanza safari alijitambulisha kuwa ni Mwalimu mpya, bobezi wa somo la "Sayansi-kimu" wa shule ya msingi anaenda kuripoti kituo kipya cha kazi akitokea Chuo cha Ualimu Mpwapwa, Dodoma.
Umbali kutoka Mtwara Mjini mpaka kufika Nanyumbu ni kama kilometa 282 kwa mwendo wa wastani. Kachero Manu aliamua kuingia Cabo-Delgado Kininja kwa kutumia njia ya barabara kupitia daraja jipya linalounganisha Msumbiji na Tanzania.
Pia ipo njia ya rahisi zaidi ya kuingia Msumbiji kupitia kivuko cha kijiji cha Kilambo kilichopo kilometa 40 kutoka Mtwara mjini, ila kipindi cha masika hasa cha mwezi Februari sio nzuri sana kutumia njia hiyo kwa sababu mto unajaa maji sana, na ni rahisi kupata ajali ya kivuko. Hivyo kwa kuufanyia kazi msemo wa kimombo unaosema "Short cut wrong cut", au waswahili tuna msemo wetu "rahisi aghali", Kachero Manu akaamua atumie njia ya daraja la Mtambaswala ili afike safari yake salama.
Akafanya maamuzi ya bora azunguke njia ndefu lakini awe na uhakika wa usalama wa safari yake. Lile gari likaondoka Mtwara Mjini usiku ule wa saa mbili na dakika kumi, huku Kachero Manu akipiga mahesabu yake kwa mwendo wa kawaida wa mwendokasi wa 80-120 km/hr akakadiria wataingia Mangaka, Makao Makuu ya Wilaya ya Nanyumbu muda wa saa sita usiku.
Gari lilikuwa linaendeshwa kwa kasi na barabarani hakukuwa na askari wa barabarani wale wenye vitochi vya kudhibiti mwendokasi wa gari kama mwenge wa uhuru. Ilipofika muda wa saa 5:15 usiku ikiwa imebaki kama kilometa 15 kufika mwisho wa safari, Kachero Manu hakutaka kupoteza muda alimshukuru Mungu kwake yeye alijiona ameshafika tayari.
Bila kupoteza muda akamuangalia yule mwalimu mwanamke abiria mwenzake gwiji wa "Sayansi-kimu" alikuwa yupo hoi, amezidiwa usingizi wa samaki pono anayumba kushoto na kulia kama mwali anayenema. Akatumia mwanya huo vizuri kwa kutelemka pole pole kutoka kwenye gari bila kishindo. Akashika mlango wa nyuma ya "pick-up" akateremka taratibu mithili ya mjusi anayeogopa kubanwa na mlango akatokomea kwenye kichaka pembezoni mwa barabara.
Akaanza kuambaa ambaa pembezoni mwa barabara huku akijiandaa kujificha kwenye kichaka iwapo itatokea gari au pikipiki barabarani itakayomulika mwanga. Baada ya mwendo kama wa saa moja wa kutembea na miguu akawa ameshafika Mangaka Mjini muda kama saa 7:20 usiku.
Kwa bahati mbaya muda ulikuwa umeyoyoma sana, watu wengi wapo majumbani kwao wamelala. Katika zunguka zunguka yake mitaani, akakutana na kijiwe kimoja cha madereva bodaboda na kabakia bodaboda mmoja tu kavalia barakashia ya kiislamu huku ameliinamia pikipiki lake.
Bodaboda wana tabia ya kuogopa abiria hasa nyakati za usiku hii ni kutokana na uporwaji wa pikipiki zao na hata kuuliwa, lakini Kachero Manu mavazi yake ya kiislamu yalimbeba aonekane ni mwema akatanguliwa kusalimiwa na dereva bodaboda yule "Assalamu Alekum" ustaadh..". Kachero Manu akajibu "Waleikum salaam kijana", haraka haraka dereva bodaboda akadakia kumuuliza "vipi unaelekea kwenye sherehe ya Maulidi ya wilaya? hii ilitokana na mavazi ya Kiislamu aliyotinga usiku ule.
Kachero Manu akatabasamu kuwa mbinu yake ya kuvaa uhusika usio wake umeanza kufanikiwa mpaka sasa anaitwa Ustaadhi. "Hapana, mie nataka nielekee "Cabo-Delgado" sijajua usafiri unakuaje hapa wa kufika huko?" alisema huku analikumbatia vizuri begi lake. Akajibiwa na bodaboda, kwamba usafiri unaanza saa nne asubuhi, ila sasa inapata wiki magari hayaendi Cabo-Delgado kutokana na machafuko yanayoendelea huko.
"Kabla ya machafuko kulikuwa kuna daladala nne zinatoka huku kwenda Cabo-Delgado na mbili zinarudi, ni daladala za Kibopa mmoja wa Mtwara mjini anaitwa "Panchoo Jalaby" ila leo una bahati sana ustaadhi wangu inaelekea wewe kweli ni mtu wa Allah sana, kuna madrasa imetoka Wilaya ya Montepuez, Cabo-Delgado imealikwa na kwa kawaida huwa wanaondoka saa 9 za usiku safari zao, nakushauri uwahi kwenda ukaongee na dereva mapema hivi sasa akufanyie mpango" alisema kwa kirefu muendesha pikipiki yule huku akiwa tayari ameshalitia moto pikipiki lake analiungurumisha.
Dereva huyo aliyekuwa anayedadavuliwa na muendesha bodaboda, asili yake ni Tanzania, lakini alikuwa ana zaidi ya miaka 30 yupo Msumbiji na amepata uraia huko huko Msumbiji. Alikuwa ni maarufu sana huyu Mzee, anajulikana Mangaka nzima na vitongoji vyake. Bila kuchelewesha muda Kachero Manu akamlipa bodaboda Sh.1,500/= ili amfikishe nje ya msikiti mkuu wa Mangaka ambapo hayo maulidi yalikuwa yanafanyikia hapo.
Alipofikishwa wakaagana na bodaboda akawa anaangaza angaza kutafuta gari kubwa aliloelekezwa linalotoka Montepuez, hakuliona gari lolote zaidi ya kuona magari madogo madogo, pikipiki na baisikeli za waumini waliokuja maulidini. Akashikwa na taharuki kuwa huenda kadanganywa na yule bodaboda ili labda apate tu pesa za kumsafirisha hadi hapo Maulidini. Akasimama na begi lake pembeni anaushangaa umati mkubwa wa waislamu wale wanaimba kaswida na kuyumbayumba kwa furaha mipigo ya ngoma za dufu wakiwa wapo umbali wa meta kama 20 kutoka pale aliposhushwa na dereva bodaboda. Akaamua kuegemea kwenye mti wa Msonobari wa jirani akiwa ametulizana kama kobe anayetunga sheria, akitafakari kitu cha kufanya.
Ghafla bin vuu akiwa hana hili wala lile, akasikia muungurumo wa lori aina la Isuzu linakaribia eneo la shughuli linajongea pembeni ya Msonobari ule ule alioegemea. Dereva alipofika sehemu aliyoikusudia kuegesha gari lake, akazima gari kisha haraka haraka akashuka chini ya gari. Akasogea pembeni kidogo ya gari lake yule dereva, akaingiza mkono mfukoni akachomoa paketi ya sigara rangi ya dhahabu. Kachero Manu kwa mbali akafanikiwa kusoma maandishi ya paketi hiyo kwa kutumia mwangaza hafifu wa taa ya Mungu, mbalamwezi chapa ya juu ya maandishi meusi yaliyokolezwa jina la "Kingdom".
Hizi ni sigara kutoka nchini Afrika ya kusini zinazopatikana kwa wingi nchini Msumbiji. Kachero akawa anajipanga namna ya kumvaa dereva akaanza kutafakari. "Inaonyesha hili gari baada ya kuwashusha wanafunzi wa Madrasa kuna sehemu ilikwenda sasa ndio inarudi tayari kuwachukua kwa safari".
Dereva alipovuta mikupuo mitatu ya sigara na kutoa moshi angani, Kachero Manu bila kupoteza muda akamkabili dereva uso kwa uso kujaribu bahati yake kuomba nafasi ya kusafiri kwenye gari. "Salamu aleikum, natumaini wewe ndio dereva wa hili gari eeh?" alisalimia na kutupa swali kabisa. "Bila ya shaka Ustaadh wangu, hujakosea sijui nikusaidie nini?" akajibu dereva huku aliweka sigara yake pembeni kumsikiliza Kachero Manu. Bila kujivunga Kachero Manu akakohoa kidogo ili kulisafisha koo lake ili sauti itoke vizuri kisha akaanza kujieleza.
"Nina shida ya kwenda Cabo-Delgado kikazi, sasa usafiri ni shida sana wiki nzima nipo hapa ninatangatanga hamna usafiri wowote, sasa nimeelekezwa wewe unaelekea Cabo-Delgado hivyo naomba unisaidie kama kuna uwezekano huo tafadhali...!", alidanganya uwongo mtakatifu uliopangika ukajipanga vizuri.
Uwongo ambao hata mbele ya Jalali unakubalika kwa ajili ya manufaa ya safari hiyo kwa nchi ya Tanzania. Akajibu yule dereva kwa ufupi, "huogopi mauaji yanayoendelea huko? Watanzania wenzako wanatoroka wewe ndio unajipeleka mwenyewe kwenye mdomo wa mamba?". "Kutokana na kazi zangu za utafiti wa mambo ya kale inanibidi tu maana naskia mbali ya machafuko haya ya kibaguzi kwa Watanzania pia kuna kikundi cha kigaidi hapo Cabo-Delgado hofu yetu ni kuwa magaidi wasije wakalipua majengo ya kale kama walivyofanya wale magaidi wa kule Timbuktu, nchini Mali, tukakosa kuandika historia sahihi kwa vizazi vijavyo", aliongea Kachero Manu kwa msisitizo mkubwa akijifanya ana uzalendo na kazi yake, kumbe ni jasusi wa Kimataifa.
"Sawa mimi nitakusaidia kukupa msaada wa usafiri kwenye hili lori lililobeba wanafunzi wa madrasa, ila uwe makini sana maana Watanzania Cabo-Delgado hawapo salama, mimi mwenyewe napata staha kwa sababu nimeishi Msumbiji zaidi ya miaka 30 na nimeolea Msumbiji lakini bado naonekana kama kidudu mtu. Heshima tuliyokuwa tunaipata Watanzania wakati wa utawala wa awamu ya kwanza wa Samora Machel ni mbingu na ardhi ukilinganisha na sasa. Wanawabagua Watanzania lakini tayari wameanza kubaguana wenyewe kwa misingi ya makabila, ukanda na dini ndio unakuta vikundi vya kigaidi vimeanza kuibuka" aliongea dereva wa Lori lile la Madrasa.
Bila kupoteza muda Kachero Manu akatumia fursa ya muda mchache uliobaki kabla ya safari kuanza kumdadisi dereva yule mambo mawili matatu yanayoendelea Jimboni Cabo-Delgado. Dereva yule aliyeonyesha fika kutopendezwa kabisa na mambo yanayoendelea nchini Msumbiji hivyo akawa anafunguka vilivyo mambo mbalimbali.
"Sasa kwanini watoto wadogo mnawapandisha kwenye lori gari ambalo sio rasmi kwa abiria, ina maana Cabo-Delgado yote hamna Mabasi na Daladala kubwa"? alitupa swali la taftishi. Dereva yule kabla hajajibu, alimuangalia Kachero Manu kwa umakini kisha akapiga pafu la mwisho la sigara yake akaupumulia moshi wake angani, kisha akakitupa chini kipisi na kuisaga kwa kisigino cha soli ya kiatu chake.
Kisha akamsogelea kwa ukaribu akaanza kumuelezea kwa kunong'ona, "ndugu yangu hii ni mipango tu ya kimaisha hapa hamna sherehe ya dini kikweli, bali kuna uharamia mkubwa unaendeshwa. Hapa haipiti miezi 3 utaskia kuna sherehe ya kidini inafanyikia Nanyumbu, lakini kinachofanyika hizi sherehe zinafadhiliwa na tajiri mmoja tena Mkristo anaishi Cabo-Delgado, inasemekana huyo anajishughulisha na biashara haramu nyingi tu hasa za mipakani, hata haya machafuko dhidi ya Watanzania inasemekana ndio anafadhili.
Ukikodiwa kuwaleta wanafunzi, basi mtapakia mzigo wa magendo kwenda Tanzania na mnaporudi Cabo-Delgado mtapakia mzigo wa haramu kama meno ya tembo au madini. Madini yanayoibiwa huko Mererani, Jijini Arusha yanatoroshwa kwenda kuuzwa nchini Afrika ya kusini. Hivyo kwenye lori inapangwa mizigo chini kisha baada ya hapo inatandikwa mikeka ya wanafunzi kukakaa chini, ndio maana hawapendi kukodi Mabasi..!". "
Anaitwa nani huyo tajiri? alidodosa kachero Manu swali fupi ambalo alihisi litamfungulia wepesi wa kuanzia upelelezi wake akiwa Jimboni Cabo-Delgado. Dereva kabla ya kujibu akaangalia kulia na kushoto kama mtu anayesikiliza maongezi yao, akionyesha ana hofu moyoni mwake kumtaja huyo kigogo.
Kisha akavuta pumzi kwa nguvu akijianda kulitamka jina la huyo tajiri. "Anaitwa "ALF.....! " kabla dereva hajamalizia kutamka jina hilo kikamilifu akaskia anaitwa jina lake.
NANI HUYO ANAMUITA JINA DEREVA ANAPOJIANDAA KUMTAJA KIONGOZI WA MAFIOSO WA CABO-DELGADO?
ENDELEA KUFUATILIA

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Iko vizuri mkuu ila maelezo ya watu binafsi yamezidi badala ya kuzingatia maudhui ya riwaya. Huo ni mtizamo wangu tu.
Nashukuru kwa maoni yako nitayafanyia kazi.
Ila lengo langu lilikuwa ni kuwafundisha kizazi kipya Historia ya mahusiano ya MSUMBIJI NA TANZANIA tokea enzi za waasisi. Maana kama historia hiyi isipoandikwa itakuja siku itapotea

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO-DELGADO-PART 06
Anaitwa nani huyo tajiri? alidodosa kachero Manu swali fupi ambalo alihisi litamfungulia wepesi wa kuanzia upelelezi wake akiwa Jimboni Cabo-Delgado. Dereva kabla ya kujibu akaangalia kulia na kushoto kama mtu anayesikiliza maongezi yao, akionyesha ana hofu moyoni mwake kumtaja huyo kigogo.
Kisha akavuta pumzi kwa nguvu akijianda kulitamka jina la huyo tajiri. "Anaitwa "ALF.....! " kabla dereva hajamalizia kutamka jina hilo kikamilifu akaskia anaitwa jina lake.
"Mzee Masebbo eeeh.... muda unayoyoma huu, tutafika asubuhi sana iwe msala kwetu kwa waliokodisha gari oooh...!" ilikuwa ni sauti ya taniboi wake akimpa msisitizo waondoke haraka kuelekea Jimboni Cabo-Delgado. Dereva yule akakurupuka kama vile amemuona simba kichakani, akamwambia kachero Manu.
"Twenzetu safari imeiva tutaongea zaidi Cabo-Delgado. Nitafute rafiki yangu naishi mtaa wa Ruvuma nyumba namba 23B, haya twende maana wenyewe wanataka saa 12:00 asubuhi uwe umeshafika". Kachero Manu akaitikia kwa vitendo kwa kubeba begi lake mkononi na kumfuata dereva nyuma nyuma wakielekea kupanda Lori lile tayari kwa safari.


SURA YA TANO
Safari ya kuelekea Cabo-Delgado ilianza kama saa 9:15 usiku kutoka pale uwanja wa sherehe ya maulidi.
Kachero Manu alikuwa amepanda nyuma ya lori akijichanganya pamoja na wanafunzi wa madrasa pamoja na Maustaadhi na Taniboi wa gari.
Safari ilipoanza tu ndani ya muda mfupi tu, Kachero Manu akagundua kitu toka kwa yule Taniboi wa dereva Masebbo, alikuwa anamuangalia sana kwa jicho pembe la kuibia. Ingawa kulikuwa na mwangaza hafifu wa mbalamwezi angani, Kachero Manu alitambua kuwa sio mtu mzuri kwake.
Akajifanya kama hamuoni, anasinzia huku anajaribu kupasua kitobo kwenye mikeka waliyokalia watoto wa madrasa kwa kutumia mkasi wake mdogo aliouchomoa mfukoni mwake. Lengo alitaka ajihakikishie kama kweli kuna mzigo wa meno ya tembo umebebwa na hilo lori kama alivyodokezewa na mzee Masebbo.
Lakini hakufanikiwa kuona kitu baada ya kutoboa mkeka. Meno yale yalipangwa kwa ustadi mkubwa kisha yakazuiwa na mbao ngumu zilizopangwa na juu ya mbao ndio ikawekwa mikeka ya kukalia wanafunzi wa madrasa, hivyo kila alipokuwa akipitisha mkasi ukawa unagota kwenye mbao.
"Inaonyesha hili gari halikuwepo hapo kwenye sherehe ndio lilienda kupakia mzigo", aliwaza Kachero Manu akiwa tayari ameshaurudisha mkasi mfukoni. Akapotezea huo mpango wake na kuamua kujiegemeza kwenye begi lake akiutafuta usingizi.
Alimuona Mzee Masebbo ni kama malaika msaidizi ambaye ametumwa kumrahisishia kazi yake katika namna asiyoitarajia. Akashukuru kwa hatua aliyofikia, hasa ya kumtambua tajiri wa kuvusha biashara haramu, jina lake linaanza na herufi tatu “ALF”.
Akajijengea mawazo chanya huenda huyu ndio kiini cha machafuko yote. "Kwanini machafuko yameanza kwa Watanzania, Wafanyabiashara wa madini!" ndio swali lililokuwa linamsumbua kichwani mwake. Wafanyabiashara ambao biashara zao zinaendana na huyu tajiri “ALF”. "Je anawaogopa Watanzania wanahatarisha biashara zake?" aliendelea kujiuliza maswali yasiyo na majibu ya papo kwa hapo.
Alikuja kushtuka yupo kwenye dimbwi hili la mawazo wapo juu ya daraja jipya linalounganisha Tanzania na Msumbiji. Ni daraja lenye urefu wa meta 720, limejengwa kusini mwa Tanzania eneo la Mtambaswala wilaya ya Nanyumbu kuelekea upande wa Kaskazini wa Msumbiji wa jimbo la Gabo-Delgado.
Akawa anahesabu nguzo za daraja ambalo lina nguzo 18, akapata nguzo 9 zipo upande wa Tanzania na 9 zingine zilizobaki ni nguzo za upande wa Msumbiji. Akatabasamu kwa sababu alisoma kwenye moja ya kabrasha kuwa ujenzi wa daraja hilo la la Umoja la kuvukia mto Ruvuma ni matokeo ya wazo lililotolewa na Marais waasisi wa nchi mbili ambao ni Hayati Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania na Hayati Samora Machel wa Msumbiji mwaka 1975.
Marais hao walikuwa na lengo la kuunganisha nchi za Tanzania na Msumbiji kupitia mikoa ya Mtwara upande wa Tanzania na Gabo Delgado upande wa Msumbiji. Kachero Manu akatamani mawazoni mwake kuwa Nyerere na Samora wangekuwepo hai leo waone ndoto yao ya kuunganisha nchi zao ilivyotekelezwa na warithi wao.
Lakini wangekuwa hai pia wangepatwa na kihoro kutokana na mpasuko uliopo baina ya wananchi wa nchi zao mbili kinyume na matarajio yao. Marais hao walitaka wananchi hao wawe wamoja kama ndugu mpaka kupelekea kupatikana kwa Umoja wa Afrika.
Usingizi ukaanza kumnyemelea mpaka akaanza kuwa nusu amelala nusu yupo macho, ghafla bin vuu akashtuka usingizini kwa kuona dereva mzee Masebbo anapangua gia kudhihirisha kuwa anapunguza mchepuo wa wa gari. Akakaa vizuri kisha akajituliza na kuchungulia kwenye ncha ya turubai inayounganisha kwenye vyuma vya lori ili ajue sababu ya kupunguza mwendo.
Akashuhudia kwa mbali kuna askari takribani 6 mpaka 7 ambao wamening'iniza bunduki mabegani mwao. Gari likasota pole pole mpaka likasimama. Kachero Manu akajua tayari kimenuka mambo hamkani sio shwari tena, akajipa subira kuona mwisho wake.
Liliposimama tu askari mmoja akasogelea mpaka usawa wa mlango wa dereva huku wengine wakibaki kwa nyuma yake usawa kama wa mita 5, kisha kwa sauti kubwa yule askari akamsalimia dereva kwa kireno.
"Como você esta"( habari yako), dereva Mzee Masebbo akajibu "eu estou bem"(nipo vizuri) , "De onde você esta vindo?" (mnatokea wapi?), "A partir de Nanyumbu, Tanzania" (Tunatokea Tanzânia), "Todos os cidadãos? "(wote ni raia wa Msumbiji?) , akajibu Mzee Masebbo "sim"(ndio) lengo la yule askari alikuwa anataka kufahamu huyu dereva anajua kireno.
Kama angeshindwa kujibu tu kimbembe kingeanza hapo, baada ya kujiridhisha na majibu akaanza kuzunguka gari kuanzia mbele mpaka nyuma. Kipindi hicho dereva Masebbo anahojiwa, tayari yule Taniboi ameshashuka zamani chini ya gari anaongea na baadhi ya askari wale kirafiki.
Kisha askari mmoja wapo mwenye umbo la miraba minne mithili ya mchezaji wa mpira wa kikapu wa ligi ya NBA-Marekani, katika wale aliokuwa anaongea nao Taniboi ghafla akachomoka na kurukia kwa nyuma kwenye lile lori.
Kachero Manu akajikausha bila kutikisika huku akijiweka tayari kwa lolote litakalotokea. Hakusema chochote yule askari ndani ya umati ule wa watu huku akiwa amewasha tochi yake kali anamulika kama vile kuna kitu anakitafuta. Akazidi kusogea kwa ukaribu mpaka akafika pale alipokaa Kachero Manu, kisha akasimama mbele yake kabisa.
Kachero Manu alijiinamia chini uso wake huku akisali kila aina ya dua apate kukiepuka kikombe cha kukamatwa na maadui zake kabla hata hajawasili uwanja wa vita, Jimboni Cabo-Delgado. Ghafla askari yule akamkwida Kachero Manu kwenye nusu kanzu yake aliyovaa juu na kumnyanyua juu kwa nguvu.
Kachero Manu akawa anachuchumia kwa ncha ya vidole vyake ya viatu vyake vyepesi alivyovaa. Kama umeme Kachero Manu akarushwa nje ya gari na kudakwa juu juu na askari waliobakia nje ya gari. Wakaanza kumgombania kama mpira wa kona, huku askari mmoja wapo akienda kumshusha dereva Masebbo chini ya gari. Wakaanza kumgombeza Mzee Masebbo kwa kuwapa taarifa za uwongo kuwa hajambeba Mtanzania kwenye gari lake.
Mzee Masebbo katika kujiokoa roho yake akajitetea kwa kumkana kuwa hamfahamu Kachero Manu, na sio jukumu lake kukagua abiria ila ni jukumu la Taniboi. Baada ya majadiliano mafupi baina yao wakamruhusu Mzee Masebbo aondoke zake pale na wamuache Kachero Manu wamchezeshe kindumbwendumbwe. Wakati Mzee Masebbo anataka kuondoka eneo lile wakagonganisha macho kati yake na Kachero Manu, kana kwamba kuna ishara alipewa Mzee Masebbo na Kachero Manu.
Askari wale wakamkwida Kachero Manu na kutokomea nae porini kidogo, nje ya barabara. Siku zote mdharau mwiba, guu huota tende, dharau zao kwa Kachero Manu ziliwaponza wale Askari. Walipomsachi na kumuona hana kitu chochote, wakajua ni mtu wa kawaida tu mwenye nia na madhumuni ya kwenda Msumbiji kiholela.
Askari wawili tu ndio wakabakia kutaka kumuadabisha Kachero Manu huku wengine wakibakia kutega pale barabarani. "Leo takuwa chakula cha simba wewe...!" alifoka mmoja wapo kwa kiswahili kibovu. Alikuwa tayari ameshachomoa bastola yake ipo hewani hewani tayari kwa kuifyatua, wakiwa sasa wameshazama kwenye kimsitu chepesi.
Askari mwingine alionekana yupo kama hayupo anayumba kama vile kazidiwa na kileo. Kachero Manu alikuwa anaongoza mbele amenyoosha mikono juu kuomba amani huku wale askari wanamfuata kwa nyuma. Kadri walivyokuwa wanaelekea kichakani ndipo harufu kali kama ya maiti zilizoharibika ilikuwa inafika katika pua za Kachero Manu ikitokea kule machakani wanakoelekea.
Akaanza kupatwa na kihoro kuwa huenda anapelekwa kuuliwa kwenye chimbo lao maalumu la mauaji. Akajiongeza kichwani mwake kuwa hana budi kuzichanga vyema karata zake za kujiokoa. Alitanabahi akili mwake kuwa anatakiwa apate nafasi moja tu ya wale maadui kufanya makosa halafu yeye aitumie vizuri kujiokoa. Kachero Manu alijua hana muda wa kupoteza, begi lake na kila kitu chake kilikuwa kwenye Lori la Mzee Masebbo hivyo alitakiwa afanye juhudi kuliwahi njiani.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO-DELGADO-PART 07
Bahati ya mwenzio usiilalie mlango wazi, yule Askari mlevi ambaye alikuwa ameikamatia tochi akaliparamia jiwe na kujikuta anakula mwereka kwa kuserereka mpaka chini kwa kishindo kikubwa. Bila kufanya ajizi, kosa moja goli moja, Kachero Manu akajipindua hewani kinyumenyume na moja kwa moja teke lake lenye nguvu la mguu wa kushoto likaenda kutua kwenye mkono wa Askari mwenye kushikilia bastola, mpaka ikamponyoka kiganjani. Akiwa bado amepigwa na butwaa hajui kinachoendelea Kachero Manu akaiwahi ile bastola na kuwafyatulia risasi mbili za haraka haraka na kuwaua pale pale.
Risasi zile mbili mlio wake uliiwashtua wale Askari wengine waliobakia barabarani na kuwafanya waje wanguwangu bila kuchukua tahadhari ya kutosha. Walitaka kujihakikishia kama wenzao wapo salama. Kachero Manu bila kufanya ajizi tena kwa mara ya pili akawa anawatungua akiwa amebana pembezoni ya kichaka mmoja baada ya mwingine kama nyumbu vile mpaka akawamaliza.
Na kwa bahati risasi zikawa zimeishia zake, akairushia porini bastola hiyo. Akajipa muda wa matazamio kama wa dakika 5 anapima upepo, baada ya kuona hali ni shwari hamna shari wala rabsha zozote, akachomoka zake toka porini. Akaiokota ile tochi ikawa msaada kwake anaitumia kusogea mbele kidogo kule porini alikokuwa anapelekwa. baada ya mwendo wa kama dakika 5 akakutana na maiti zilizoharibika zinazotoa harufu mbaya zimetapakaa ovyo.
Alivyozidi kuchunguza akaona wawili kati yao pembeni yao kuna hati ya kusafiria ya nchi ya Tanzania, ikiwa imelowanishwa na maji ya mvua. Akamshukuru Mungu wake kwa kumuokoa kutoka kwenye bonde la mauti alilokuwa anapelekwa kuuliwa muda mfupi uliopita. Hima hima akashika uelekeo wa kutoka kule bondeni akawa anaelekea barabarani anafuata uelekeo wa Lori la Mzee Masebbo.
Alipotupa jicho lake kwenye mishale ya saa yake ilikuwa inaonyesha kuwa zimepita takribani dakika kama 22 tokea lile Lori limtelekeze pale porini. Hapo ndipo alipoona faida ya mazoezi ya mbio anayoyafanya kila siku. Akaamua aanze kufyatuka nduki kwa kasi kubwa. Alikuwa na uwezo wa kutimua mbio kwa spidi ya dakika 4 kwa kila kilometa 1.
Hakujali hofu ya wanyama wakali katika giza lile totoro la porini usiku ule, hamu na shauku yake ilikuwa ni kuliwahi Lori lile kabla halijamuacha njiani.
Alifahamu akikosa usafiri ule ndio amekwisha habari yake hamna tena usafiri mwingine. Na kama alikamatwa kwa kuhusishwa na vifo vya wale Askari 6 aliowateketeza porini kwa mtutu wa bunduki hatosalimika tena, watamshukia kama mwewe anavyokishukia kifaranga cha kuku.

Kachero Manu baada ya kutoka nduki kwa zaidi ya dakika 45 bila kupumzika tena akiwa ameshakimbia kwa zaidi ya kilometa 17 kwa mbali sana alipotupa macho akaona kitu kama taa nyekundu zinawaka mbele yake. Alikuwa anatweta kwa uchovu kama swala anayemkimbia simba mkali mwenye uchu wa kutaka kumshambulia.
Akashusha pumzi na kuanza kujipa matumaini huenda hilo ni gari la Mzee Masebbo hivyo azidi kuongeza kasi alifikie kabla halijang'oa nanga. Akashukuru kwa jinsi Mzee Masebbo alivyokuwa makini kuzisoma ishara alizompa kuwa amsubirie mbele pale alivyokamatwa na Askari pale kizuizini.
Baada ya mbio za kama dakika 10 zaidi, akawa ameshalifikia lile gari. Abiria wote watoto wa madrasa na Maustadhi wao walikuwa ndani ya gari wanakoroma kwa usingizi wa uchovu. Mzee Masebbo na taniboi wake wapo chini ya gari wanalikorokochoa gari likae sawa safari iweze kuendelea.
"Uuukh.....Uuukh.......Uffff......Uffff... Afadhali nimewakuteni, maana nisingewapata sijui ningekuwa mgeni wa nani...! " alisema Kachero Manu kwa uchovu huku mikono yake imekamatia kiuno, jasho jekejeke linamchuruzika mwilini mithili ya mchoma mikate kwenye tanuri la kuni.
Moyoni Kachero Manu alijisifu kwa maamuzi yake ya kuvaa viatu vyepesi vilivyomrahisishia mbio zake ndefu alizozikata mbuga.
"Ooh.....pole sana una bahati sana, tungeshakuacha ila gari imepata hitilafu katika mfumo wa breki ndio narekebisha hapa tuondoke, Chikulubu wewe lete grisi, acha kulala muda unayoyoma...!" aliongea Mzee Masebbo kumjibu Kachero Manu kisha akaanza kumpigia makelele Taniboi wake achangamkie kazi.
Yule Taniboi alikuwa hataki hata kumuangalia Kachero Manu usoni baada ya kuona unaa wake kwa wale Askari umefeli. Kachero Manu akampuuza tu akadandia ndani ya Lori, na kuwakuta watoto wale wamelewa usingizi wa fofofo hawajitambui.
Kachero akaenda moja kwa moja mpaka kwenye begi lake na kuanza kulifanyia speksheni ya usalama wa vitu vyake alivyoviacha. Akajikuta anafyonya peke yake kwa hasira baada ya kugundua kuwa begi lake limepekuliwa. Akili yake ikamtuma kuwa hamna mshenzi mwingine yoyote mwenye kiherehere cha kumchunguza zaidi ya huyu Taniboi kijana Chikulubu.
Akazigusa silaha zake kwenye mfuko wa ndani kwa ndani alipozihifadhi, akazikuta zipo salama. Kama angezikuta zimechokonolewa, pasingetosha lazima angemtia adabu huyo kijana. Kabla hata hajatulia vizuri akamuona Mzee Masebbo ameshapanda ndani ya gari na kuliwasha akiwa bado amevalia bwelasuti yake ya gereji zikiwa zimechakazwa kwa uchafu wa grisi na mafuta machafu.
Gari likaanza kuondoka huku sasa Chikulubu akiwa ameamua kukaa mbele na dereva wake. Kachero Manu akatanbahi kuwa hizo ni dalili za kumkwepa kwa kuona aibu kutokana na kitendo chake cha kumchomea utambi mbele ya wale Askari.
Barabara ilikuwa na utelezi uliotokana na mvua iliyokuwa imenyesha hivyo Mzee Masebbo alikuwa anatembea kwa tahadhari kubwa asije kuwabwaga barabarani yakaibuka majanga mapya. Kachero Manu hakuchukua raundi kutokana na uchovu wake akajikuta analala usingizi mzito wa pono.
Ni Mwenyezi Mungu pekee ndio ambaye hakumshiki kusinzia wala kulala, lakini binadamu wote hata uwe komandoo au Amiri Mkuu wa Majeshi yote lazima utafika wakati ambao mwili utahitaji mapumziko ili kuhuisha nishati mpya.
Walifanikiwa kufika salama safari yao saa 11:30 ya alfajiri, walishushwa nje ya jengo la Madrasa ambapo pembezoni kuna msikiti mdogo. Watoto wa madrasa wakaanza kuhangaika kushusha mizigo yao pamoja na ngoma zao za dufu walizokuwa wanazipiga kule Maulidini.
Baada ya mizigo kushushwa Mzee Masebbo alionekana ana haraka sana hana tena muda wa kupoteza eneo lile huku yule kijana wake Chikulubu akiwa haonekani eneo lile.
Kachero Manu hakuwa tena na pupa ya kuongea na Mzee Masebbo, aliona mustahabu zaidi kwenda kuonana nae Mzee Masebbo nyumbani kwake kama walivyopeana miadi. Walipowasili tu sauti ya adhana "Allahu Akbar Allahu Akbar..." ya wito wa swala ya alfajri ulikuwa unatolewa kwenye kipaza sauti cha msikitini.
Wito ulikuwa unawatangazia Waislamu wake kwa waume kuwa wakati wa kuitekeleza ibada ya swala ya alfajiri umewadia Hivyo wanatakiwa waviachie vitanda vyao kwa ajili ya kujiandaa na swala.
Mtoa adhana bila kusahau, akaweka na vikorombwezo vya kuwafanya waumini hao waingiwe na woga waamke kwa haraka, akaanza kuongea kwenye kipaza sauti "Eeeh...Muislamu wewe kitanda chako hicho ndio jeneza lako, shuka hiyo uliyojifunika ndio sanda yako, Swali leo Baba, swali leo Mama, swali leo Kaka, swali leo Dada, kesho kesho kila siku kesho kiama".
Yalikuwa ni maneno ya kuogofya ambayo mtu mwenye roho ngumu tu ndio ataendelea kuuchapa usingizi, lakini mtu swalihina lazima anayanyuke kuswali hata kama amezidiwa na usingizi.
Kachero Manu nae haraka haraka akajiunga na kundi la waumini wachache waliokuwa wanatia udhu kwenye mabomba ya maji nje ya msikiti kujiandaa na sala hiyo ya asubuhi. Alikuwa mjanja anatia udhu taratibu sana huku anapiga jicho upembe anaigizia namna waumini wa kweli wanavyoosha mikono yao, nyuso zao, vichwa vyao na kumalizia miguu yao.
Hakutaka kujitia kimbelembele halafu ashtukiwe hajui kutia udhu wakati amevalia kiislamu na kuwatia ndimu kuwa yeye ni Mzanzibari. Waislamu wa Msumbiji ukiwaambia unatoka Zanzibari wanakuheshimu kama kile unatokea Mji wa Maka alipozaliwa Kiongozi wa waislamu duniani Mtume Muhammad (S. A. W).
Hivyo ingekuwa ni kituko cha karne kwao uwe Mzanzibari halafu hujui jambo dogo katika dini ya Uislamu kama kutia udhu. Wakati anamalizia udhu wake, akasikia mnadi wa sala anasoma maneno ya kiarabu ya ikama kuashiria sala inataka kuanza, hivyo waumini hao wajipange safu safu tayari kwa swala kuanza.
Imamu aliposimama na kuelekea kibla kwa ajili ya kuanza kuswalisha na kutamka maneno ya "Allahu Akbar" kisha akafunga swala na kuanza kusoma sura ya ufunguzi wa swala, ikiwa ndio sura ya kwanza kwenye Kurani, kitabu kitakatifu kwa waislamu.
Kachero Manu hakutaka kuremba, alichofanya ni kutoka nje ya mlango mdogo wa nyuma ya msikiti na bila kusitasita akavaa viatu vyake vilaini vya "Kung-Fu" vilivyokuwa vimechafuka vumbi haswa kutokana na mbio zake ndefu alizozitimua.
Kisha akatokomea mtaani, akawa anatembea mashimashi huku anaelekea sehemu asiyoifahamu ikiwa ni saa 11:40 za alfajiri alipoiangalia saa yake ya mkononi. Ilikuwa ni asubuhi ya tarehe 15/02/2016 ndani ya viunga vya Cabo-Delgado ameshawasili, tayari kwa mapambano.
Akamshukuru Mungu kwa kumfikisha salama katika uwanja wa mapambano. Akajikuta anaropoka tu kimoyomoyo "Hapa kazi tu...!" kwa lengo la kujishajiisha na kujipa morali ya mapambano na mahasimu zake anaotarajia kuonana nao.


Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO DELGADO-PART 08
SURA YA SITA
Mafioso wa Biashara haramu ya madini hadharani
"Alfredo Afonsio Alexis" ni jina ambalo kwanza ukitaka kulitamka kwa ufasaha zaidi inabidi upitie masomo ya ziada ya lugha ya Kihispaniola, vinginevyo ujiandae kupata ajali ya ulimi wakati wa matamshi.
Alikuwa ni chotara, mchanganyiko wa Kireno na Kimakonde, kijana mwenye kukimbilia kwenye rika la utu uzima. Ulikuwa kama ukibahatika kuonana nae mubashara unaweza kumkadiria umri takribani wa miaka 55 na fauka ya hapo, lakini utakuwa umemkosea sana.
Umri wake halisi ulikuwa hauzidi miaka 48. Ila kutokana na mwili wake mkubwa, wa nyama uzembe, ukijumlisha na pesa sufufu anazomiliki wengi walikuwa wanajua ni mtu shaibu kiumri. Tabia yetu Waafrika mtu akimiliki uchumi wa kutosha hata kama ni mdogo kiumri tunamzeesha hapo hapo kwa majina kama Mzee, Mshua, Bosi Kubwa na mengineyo kedekede ya kumpamba.
Baba yake mzazi, Mzee "Afonsio" alikuwa ndio mmiliki wa kampuni kubwa ya ukoo inayoitwa "Monte Branco Ltd" iliyoanzishwa tokea 1885 ikijishughulisha na biashara ya kununua na kusafirisha korosho na mihogo mikavu nje ya Msumbiji tokea enzi hizo za mkoloni.
Biashara ambayo ilimuingizia pesa sufufu kuliko matajiri wengi wa Msumbiji wa wakati huo. Baadae kampuni hiyo ikajitanua ikawa inajishughulisha pia na uvuvi katika bahari kuu na uchimbaji na uuzaji wa vito vya madini. "Alfredo" alizaliwa na pacha mwenzake akiitwa "Negredo" ambaye kwa bahati mbaya sana alifariki akiwa mtoto mchanga kwa ugonjwa wa Nimonia "Pneumonia".
Mama yao ni mmakonde aliajiriwa kama mpishi katika hekalu la Mzee Afonsio ambaye aliwapata mapacha hawa akiwa na umri wa miaka 50 mwaka 1970.
Inasemekana huyo mama wa kimakonde alibakwa na Mzee Afonsio Alexis lakini katika kutaka kuficha aibu ilipogundulikana mpishi wake ni mjamzito akampa ahadi ya kutunza watoto wake ila asivujishe siri yoyote ya tukio hilo.
Alipata kuwa na mke wa Kireno siku za nyuma lakini hawakujaaliwa kupata mtoto, na mkewe huyo alifariki wakati wa mapambano ya vita vya ukombozi mwaka 1966, alipigwa risasi kwa bahati mbaya na wapiganaji wa FRELIMO akiwa dukani kwake Jijini Maputo.
Siku ya mazishi ya mkewe, Mzee Afonsio aliweka nadhiri hadharani mbele ya sahibu zake ya kulipiza kisasi kwa damu iliyomwagwa ya mkewe kupitia kwenye kizazi chake kwa serikali ya FRELIMO kama itafanikiwa kuchukua madaraka ya nchi.
Inasemekana Mzee Afonsio ndio alikuwa mmoja wa wafadhili wakubwa wa kikundi pinzani za FRELIMO cha RENAMO. Hii yote ni katika harakati zake za kuwaadabisha FRELIMO kwa kusababisha kifo cha mkewe.
RENAMO ni ufupisho wa maneno yafuatayo ya lugha ya Kireno, (Resistência Nacional Moçambicano ), kikianzishwa 1975 kwa ufadhili wa matajiri wa Kireno, Rhodesia (Zimbabwe) na Afrika ya kusini mara tu baada ya Msumbiji kupata uhuru wake.
Malengo ya kuanzishwa kwa RENAMO yakiwa ni kuhujumu maendeleo ya Msumbiji, na pia kuzuia serikali ya Msumbiji kutoa misaada kwa wapigania uhuru wa Rhodesia na Afrika ya Kusini.
Hujuma zote ndani ya Msumbiji zilizokuwa zinafanywa na chama cha RENAMO za kulipua mashule, mahospitali, na kuharibu miundo mbinu ya reli na barabara zilikuwa zinafadhiliwa na Mzee Afonsio na genge lake.
Pia inasemekana kifo cha Samora Machel Rais wa kwanza wa Msumbiji mwaka 1986 kina mkono wa Mzee Afonsio na genge lake.
Jumba bovu la tuhuma linamuangukia yeye kwa sababu miezi miwili kabla ya kifo cha Rais Samora Machel inasemekana Mzee Afonsio alijichimbia zake nchini Malawi na Mafioso wenzake kwa ajili ya kupanga na kupangua mikakati mizito ya kuiangamiza FRELIMO na Rais Samora Machel.
Ilipotimu mwezi mmoja kabla ya kifo cha Samora Machel, viongozi wa Zimbabwe, Zambia na Msumbiji, Bwana Robert Mugabe, Keneth Kaunda na Samora mwenyewe walikwenda Malawi kwa Rais Kamuzu Banda kumtaka aache kufadhili kikundi cha uasi cha RENAMO.
Kwa hasira Rais Kamuzu Banda aliwajibu "hakuna Rais wa nchi asiyekufa". Wadadisi wa mambo wanajenga hoja kuwa jeuri ya Rais Banda kutabiri kifo cha Samora dhahiri shahiri tena mbele ya vigogo wazito ilitokana na mikakati mizito iliyowekwa na akina Afonsio.
Moja ya mikakati yao ilikuwa ni kufunga kifaa chenye nguvu ya kuingilia mawasiliano ya ndege "Decoy beacon", hivyo kuipoteza dira ndege aina ya Tupolov 134A ndege ya kirusi iliyokuwa inatumiwa na Rais Samora Machel.
Siku ya tukio la kifo cha Samora tarehe 19/10/1986, siku ambayo ni ya huzuni na majonzi makubwa kwa wazalendo wa bara zima la Afrika. Lakini kwake Mzee Afonsio siku hiyo ilikuwa ni sikukuu kubwa kwa kufanikisha kulipiza kisasi cha kifo cha mkewe aliyeuliwa na wanamgambo wa FRELIMO.
Siku hiyo alisafiri asubuhi na mapema kwenda nchini Afrika ya Kusini kuungana na Mafioso wenzake kusubiria taarifa za kifo kitakachoitikisa Afrika. Rais Samora alisafiri kwenda kwenye mkutano wa nchi za mstari wa mbele katika ukombozi wa bara la Afrika.
Mkutano huo ulikuwa unafanyikia nchini Zambia katika eneo la Mbala, kwa bahati mbaya sana mkutano huo uliisha muda wa saa 12:45 magharibi, giza likiwa linaanza kutamalaki angani.
Kiusalama Rais Samora alishauriwa asisafiri usiku huo na rubani wake wa Kirusi lakini waswahili wanasema siku ya kifo marehemu anakuwa mbishi mbishi sana. Rais Samora akapingana vikali na rubani wake, akamtaka waondoke usiku huo mbichi kwa sababu kesho yake alikuwa na mkutano mwingine muhimu sana.
Rubani yule kwa shingo upande akapeperusha mwewe angani, wakaondoka kwenye ndege moja na msafara wa Maofisa 33 wazito wa Msumbiji. Kutoka kwenye taarifa zilizodukuliwa za jeshi la anga la Afrika ya Kusini (SAAF) zinasema 2:45 usiku, ndege iliyombeba Samora ilikuwa tayari imeshafika mpakani mwa Msumbiji na Afrika ya Kusini.
Kwenye muda wa kati ya saa 3:00 na saa 3:15 usiku ndege hiyo ikalipuliwa katika eneo la Mbuzini, Afrika ya Kusini meta 200 kutoka mpaka wa Msumbiji na Afrika ya Kusini. Mlipuko ambao ulimpelekea jongomeo Rais Samora Machel na Maofisa wake waandamizi serikalini, bila kusaza mtu yoyote.
Mzee Afonsio alizipata taarifa ya kifo cha Samora Machel saa 4:00 usiku baada ya Majasusi wao waaminifu kwenda mpaka eneo la tukio na kujiridhisha kuwa kwa namna ndege ile ilivyolipuliwa ni ngumu kwa Rais Samora kutoka salama kama ilivyokuwa ni vigumu kumpata mwanamke bikira kwenye wodi ya wazazi.
Furaha fokofoko aliyojawa nayo Mzee Afonsio ilikuwa haiwezi kupimika katika mizania ya kawaida ya vipimo vya furaha. Walikesha na Mafioso wenzake wakisheherekea usiku kucha kwenye ufukwe wa bahari wa Clifton kwa kula kunywa na vinywaji anuwai mbalimbali.
Ufukwe huo maridhawa unapatikana ndani ya Jiji la Capetown. Mvinyo wa gharama ya juu kabisa aina ya "Cheval Blanc" unaouzwa zaidi ya Sh. milioni 300 pesa za Kitanzania kwa chupa moja nao ulikuwepo kwenye sherehe hiyo.
Kifo cha Rais Samora Machel kilikuwa ni kipigo kitakatifu cha Mafioso hawa kwa Nchi Huru za Kiafrika. Lengo ni kwamba nchi hizo zijione kuwa bado wao ni dhaifu, hawawezi kupiga hatua mbele katika mambo ya kiuchumi, kilimo, kisiasa, kiutamaduni na mambo mengineyo bila kuwahusisha wao wakoloni.
Baada ya sherehe hiyo, Mzee Afonsio na wenzake wakapanga mipango mipya ya kuandaa mapigo matakatifu zaidi ya kiuchumi ili kuzifanya nchi za Kiafrika zisiweze kujitegemea zenyewe. Ndipo ilipopangwa mipango ya kutekelezwa miaka 30 ijayo kutoka mwaka 1986.
Mipango ya Mzee Afonsio ilikuwa ni kumuachia mamlaka yote ya kampuni ya "Monte Branco Ltd" mwanawe Alfredo. Hivyo akaamua kumuandaa kielimu, hivyo alimpeleka mtoto wake Marekani kusoma elimu bora kuanzia elimu ya sekondari mpaka alivyohitimu chuo kikuu cha "Chicago" moja ya vyuo bora nchini Marekani.
Hakutaka mtoto wake asome Afrika kwenye elimu za kubahatisha. Alisomea Shahada ya Utawala wa Biashara akibobea kwenye sekta ya mafuta na gesi kwa mwongozo wa baba yake kuwa asomee masomo hayo. Tofauti na watoto wa Walalahoi mpaka wanafika hadi Chuo Kikuu hawajui hata wakasomee kitu gani, hawana mtu wa kuwaongoza.
Kwa sababu utakuta baba kazi yake ni ngariba, mama mkulima, mjomba ni dobi, shangazi ni kungwi. Pia inasemekana Alfredo alipikwa akapikika vilivyo katika mafunzo ya ujasusi wa kiuchumi katika kuzitafuta na kuzivumbua fursa mbalimbali zilizomo barani Afrika.
Mwaka 1993 akiwa na umri wa ujana mbichi wa miaka 20 tu, Alfredo akakabidhiwa mikoba rasmi ya madaraka yote ya kampuni. Wakati watoto wa kiswahili miaka 20 bado ni mtoto wa kimawazo, ni kiongozi tu wa makundi ya mitandao ya kijamii kama Facebook, Whatsapp na mingineyo.
Mzee Afonsio kwa kujiamini kabisa, akamrithisha mikoba ya kuiendesha kampuni mtoto wake kisha akarejea kwao Ureno kwenda kumalizia uhai wake. Huku akiyakinisha kuwa ameacha Msumbiji mtoto, ambaye ni Kirusi kibaya kwenye mambo ya ufisadi wa kiuchumi zaidi ya Kirusi cha Corona kinachowatesa Wachina.
Mtoto ambaye atakayekuja kumiliki njia kuu za uchumi za Msumbiji hasa katika sekta ya mafuta, gesi na madini. Haraka haraka kwa kutumia mbinu za kijasusi alizojifunza nchini Marekani.
Ndani ya miaka 2 tu ya uongozi wake wa kampuni, Alfredo alitengeneza mchanganuo wa kujua kiasi cha utajiri wa madini, gesi na mafuta kilichopo nchini Msumbiji na nchi za jirani na Msumbiji.
Kisha akatengeneza mtandao uliokita mizizi yake kuanzia serikalini, vyombo vya dola na mahakama mpaka bungeni ili kuhakikisha zabuni kubwa kubwa zote za serikali lazima zipitie kwenye mgongo wake.
Akafanikiwa kutengeneza mtandao na makampuni makubwa duniani ambayo yakawa yanamtumia kama kibaraka wao kutafuta fursa mbalimbali za kiuchumi kusini mwa janga la Afrika kisha kupanga mipango ya kimafia namna watakavyonufaika na hizo fursa kwa kupewa kamisheni yake nono kama nundu la ng'ombe.
Sasa taarifa za kiintelijinsia za kampuni ya Alfredo zilionyesha tishio la Wafanyabiashara wa kutoka Tanzania namna wanavyohamia Cabo-Delgado kwa kasi na kushika njia kuu za kiuchumi katika nyanja za biashara ya madini, vituo vya mafuta na biashara ya vyakula.
Kibaya zaidi taarifa zilieleza asilimia tisini (90%) ya wazawa Cabo-Delgado hawana elimu ya kutosheleza katika kukabiliana na ushindani wa soko la utandawazi hivyo ujanja ujanja wa raia wa Tanzania ulimtisha sana Alfredo.
Hivyo akaandaa mikakati kwa kutumia viongozi wa dola la Msumbiji ambao wapo mfukoni mwake waandaae mipango ya kuwavuruga, kuwatisha na kuwafyekelea mbali Wafanyabiashara wa Kitanzania ili waogope kuwekeza nchini Msumbiji.
Ili kuendelea kuacha mirija ya uchumi chini ya kibaraka Alfredo na mabwana zake wa nchi za ng'ambo. Hivyo kudhoofisha ndoto za waasisi wa Msumbiji za kuhakikisha kunakuwa na Msumbiji huru kiutawala na kiuchumi.

Inspekta "Mark Noble" ni wakala wa Alfredo toka jeshi la polisi
"Mark Noble" akiwa kama Afisa Mkuu wa Jeshi la Polisi katika Jimbo la Cabo-Delgado alikuwa ndio mkono wa kuume wa Alfredo katika utekelezaji wa operesheni mbalimbali haramu.
Hata ule mkutano wake wa kujadili machafuko ya Cabo-Delgado na kigogo mwenzake, Inspekta Jenerali wa upande wa Tanzania alikuwa analeta unafiki tu. Anajifanya hapendezwi maswahibu wanayowasokota Watanzania waishio Cabo-Delgado kumbe yeye ndio mratibu mkuu wa vitendo hivyo haramu.
Akiwa kijana mdogo wa makamo mwenye ubongo unaochaji haswa utasema utotoni amelishwa vichwa vya samaki. Alipanda vyeo haraka haraka kama umeme kutokana na elimu yake, nidhamu na kujituma kwake katika kazi.
Alikuwa ndio kwanza amehamishiwa kikazi akitokea Wilaya ya Montepuez. Waswahili wanasema ujana ni kaburi la tamaa zote, unazozijua wewe duniani.
Ukiwa kijana damu inachemka ndio unatamani kila msichana mrembo awe wako wewe, kila gari zuri la fasheni mpya lililoingia katika Mji ulimiliki wewe na hawaa kedekede za nafsi zenye kutamanisha katika starehe za duniani.
Mark Noble alikuta vijana wenzake wadogo tu Jimboni Cabo-Delgado wanamiliki biashara kubwa kubwa za madini. Walikuwa wanaishi kifahari na wanamiliki mali za gharama kubwa.
Alfredo mmiliki wa "Monte Branco Ltd" akamsoma pupa yake ya utajiri wa njia za mkato, akapenyeza rupia kwa kwenye udhia kwa Afisa Mkuu wa polisi huyo Mark Noble. Chambo alichorushiwa Mark Noble kikafanikiwa kumuingiza kwenye ndoano mzimamzima na kumnasa kooni vilivyo.
Wakamkalisha kitako chini wakimsomesha madhumuni yao "Monte Branco Ltd" namna wanavyotaka kuliteka soko la biashara ya madini, mafuta na gesi. Akakubali kuwa mmoja wa washirika wao katika kutekeleza mikakati yao haramu. Wakafanikiwa kutengeneza mfumo wa siri ndani ya mfumo rasmi wa serikali.
Mfumo ambao ulikusanya vibaraka wao, waliokosa soni na uzalendo wa nchi yao kuanzia kwenye Mabenki, Polisi, Mahakama, Hospitali, Vyombo vya habari na sekta zote muhimu unazozijua wewe wakahakikisha wanaweka mtu wao wa kuyatelezesha mambo yao kiulaini bila kikwazo.
Ndani ya muda mfupi tu Inspekta Jenerali Mark Noble akaanza kumiliki mali za kifahari karibia kwenye Wilaya zote za Cabo-Delgado. Kutimiza msemo kuwa ukila na kipofu usimshike mkono asije kukushtukia kuwa unampunja, basi mali nyingi za Mark Noble ziliandikishwa kwa majina ya ndugu na marafiki kukwepa mkono mrefu wa sheria siku za usoni usije ukamkamata.
Ndio ikawadia hii operesheni ya kuwafagia Watanzania wote wanaomiliki biashara za madini. Inspekta Jenerali Mark Noble akapewa jukumu hilo zito la utekelezaji wa kuwafurusha na Bwana Alfredo. Mark Noble akaliendesha zoezi hilo kwa umakini na ufanisi mkubwa sana tena bila chembe ya huruma.
Aliwachakaza kichapo kizito cha mbwa koko Watanzania walioingia kwenye rada zake. Wakubwa zake akina Alfredo walifurahishwa na utendaji wake wa kazi ikawa huwambii chochote juu yake wakuelewe, na hawafanyi kitu chochote bila kumshirikisha Mark Noble.
Huku wakimpa ahadi ya kumpigia chapuo kwa wakuu zake wa kazi apandishwe Cheo na kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi 'IGP' wa nchi ya Msumbiji. Mark Noble akaota mapembe, mgema ukimsifia tembo hulitia maji, ikafika hatua analeta ushawishi serikalini wa kuupanua mpaka wa nchi ya Msumbiji uishie mkoani Mtwara, Tanzania.
Huku vijana wake wa kazi akiwatuma mpaka ndani ya mipaka ya Tanzania kufanya uhalifu wanavyojisikia wao. Vijana wa Inspekta Jenerali Mark Noble ndio waliofanya mauaji ya Profesa na mwanafunzi wake kijana Alex katika Hoteli ya 'New Star Hotel'.
Kama hiyo haitoshi vijana wa Inspekta Mark Noble ndio hao hao waliovuka mpaka kinyemela na kwenda mpaka kijijini Mahiwa Mkoani Lindi kwenda kumkata kichwa kikatili mama mzazi wa Kachero Manu.
Lakini kitendo cha Kachero Manu kuwaswaga bila huruma, Askari 6, vijana wa Mark Noble kule barabarani kuliibua mshtuko wa mwaka. Kwa mara ya kwanza tokea ajiunge na jeshi la polisi Inspekta Jenerali Mark Noble alikoseshwa usingizi.
Alipewa penyenye za uhakika kuwa Kachero Manu ni mtu wa hatari sana, mwenye uwezo wa akili wa zaidi ya makomandoo 10. Alishatambua uzembe wa aina yoyote ile utamsababishia kitumbua chake kuingia mchanga na hata kupoteza mali zake na uhai wake.
Alishatambua kuwa Kachero Manu tayari kashatua nchini Msumbiji kwa njia ya barabara, tofauti na matarajio yao kuwa atatua kwa njia ya anga.
Machale ya Kachero Manu kutumia usafiri wa nchi kavu yalimbeba sana vinginevyo angetiwa mikononi na maadui zake hata kabla hajaikanyaga ardhi ya nchi ya Msumbiji.
"Huyu mtu ni hatari sana, kama amefanikiwa kutupiga chenga ya mwili na kufanikiwa kutuvamia nyumbani kwetu basi na sisi tumpe somo takatifu, lakini kabla hamjamuua, akamatwe akiwa hai, Wakubwa wanataka waonane nae...!" yalikuwa ni maigizo ya wazi ya Inspekta Mark Noble kwenda kwa Makamanda wake walioteuliwa kuendesha operesheni ya kumdhibiti Kachero Manu.
Sasa rasmi msako wa Kachero Manu ukawa ni operesheni ya kufa au kupona iliyozinduliwa.


SURA YA SABA
Kachero Manu anasakwa na mabaradhuli kwa udi na uvumba
Kachero Manu baada ya kufanikiwa kuondoka pale msikitini wakati wa sala ya alfajiri bila kuonekana na mtu, sasa alikuwa anakata mitaa bila wasiwasi utasema ni mzawa wa Cabo-Delgado na kibegi chake.
Alitembea katika mtaa ule ule wa msikiti mpaka karibu kufikia nyumba ya nane kutoka pale msikitini, huku kukiwa na giza giza kwa mbali akatoa miwani yake maalumu yenye uwezo wa kukuza vitu na pia kupiga picha kisha akaivaa.
Akapinda kulia kwake, kulikuwa na ushoroba mwembamba ambao unaenda kutokeza kwenye kituo cha madereva taksi. Akatembea mpaka akawa amewasili kituoni hapo. Kwa muda ule wa saa 11:50 za asubuhi zilionekana zimebaki taksi chache zisizozidi 6, huku ikionekana wengi wameenda kujipumzisha maskamoni mwao baada ya pilikapilika za usiku kucha.
Akaifuata teksi ya mwanzo mwanzo na uelekeo wake, cha kwanza alichokumbuka ni kukariri namba za taksi hiyo kichwani mwake kwa tahadhari tu kisha akasogelea mpaka usawa wa mlango wa dereva ambao kioo chake kilikuwa kimeshushwa nusu.
Akaugonga mara tatu, bila kuitikiwa na mtu. Alipogonga mara ya nne tu, dereva akakurupuka toka kwenye usingizini mzito. "Samahani sana, nina uchovu mwingi, Karibu mteja wangu, nikupeleke wapi..?", alisema dereva kwa sauti yenye viashiria vya uchovu wa usingizi.
"Usijali naelewa, nipeleke nyumba ya kulala wageni tulivu lakini ipo katikati ya Mji", alisema Kachero Manu huku akilinyanyua begi lake tayari kujiandaa kuingia nalo ndani ya gari, kisha akafungua mlango mlango wa nyuma ya dereva akaingia.
"Nitakupeleka nZuwa Lodge, ni sehemu tulivu na ni ya kisasa...!", kisha baada ya dereva kusema hivyo akatia gari moto na kuanza kuondoka kwa mwendo wa wastani.
Kwa taaluma yake ya upelelezi, Kachero Manu alikisoma kitu toka kwa dereva yule, alikuwa anamuangalia kwa wasiwasi kwa jicho la kuibia kwa kutumia kioo chake cha juu kinachompa uwezo wa kuona nyuma ya gari kinachoendelea.
Kachero Manu hakujali, baada ya kama umbali wa kutembea robo saa wakawa wameshafika kwenye nyumba hiyo ya wageni. "Kiasi gani cha pesa unanidai?" aliuliza akiwa bado hajashuka nje ya gari. "Mpaka hapa gharama ni mitikashi 100" alisema yule dereva kwa kujiamini.
Mitikashi ni aina ya pesa zinazotumika nchini Msumbiji, kama ilivyo Ksh. ya kule nchini Kenya na Tsh. ya nchini kwetu Tanzania. Hilo ni jina lenye asili ya lugha ya kiarabu, "Mithqal" kizio kinachotumika kupimia uzito wa dhahabu na kilikuwa kinatumika sana katika nchi nyingi za Afrika mpaka kwenye karne ya 19 mwanzoni.
Kachero Manu hakutia neno lolote zaidi ya kuchomoa noti toka kwenye pochi lake, akalipa kisha akashuka chini.
Dereva yule akasema huku akiwa tayari anajiandaa kuondoka ameshawasha motakaa yake, "Mzee ukinitaka muda wowote nipigie simu chukua namba yangu ya simu basi..!". "Sina laini ya simu bado sijanunua laini mimi ni mgeni hapa..", akadanganya Kachero Manu.
Maana alivyokuja, alikuwa anayo simu yenye laini aliyopewa ofisini ikiwa na laini ya simu ya mtandao wa "Mcel" aliyopewa na Kokunawa Sekretari wa Bosi wake.
Ili asimkatishe tamaa akamwambia "ila nitajie yako niiandike nitakupigia, nikinunua laini..!". "Natumia "mtandao wa "Mcel" namba zangu ni +258 44526378 nipigie muda wowote nitakupeleka popote unapotaka ndani ya Jimbo hili, nalijua nje ndani...! " alisema dereva teksi.
Kachero Manu akazuga kama anaandika kweli ile namba lakini hakuwa anaandika hakuwa na haja ya kumtumia tena dereva mmoja isije ikawa rahisi maadui zake kumfuatilia.
Baada ya hapo akaagana nae kwa kupungiana nae mkono wa kwaheri. Akachomoa mshikio wa begi lake na kuanza kuliburuta kwa kutumia matairi ya begi lile. Akafika mapokezi na kueleza shida yake ya kupata sehemu ya kulala kwa siku kadhaa.
Akapokelewa kwa bashasha na mhudumu wa mapokezi kisha akaingia kwenye mfumo wa kompyuta iliyopo mezani kwake ili kuangalia chumba kilicho tupu. Akapewa chumba kwenye roshani ya pili, akakilipia na kusindikizwa mpaka chumbani.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SURA YA KWANZA
Makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia, Kijijini Mahiwa, Lindi.
Kadamnasi ya watu walikuwa wamekusanyika wakiwa wamejikunyata vikundi vikundi. Nyuso zao zimegubikwa na majonzi na huzuni katika makaburi ya mashujaa wa vita vya dunia vya kwanza, yaliyopo kijijini Mahiwa.

Kijiji ambacho kipo katika Wilaya ya Lindi Vijijini katika Mkoa wa Lindi. Waombolezaji hao walikuwa wamekusanyika katika harakati za kuhitimisha shughuli ya arobaini kutokana na msiba wa Bi.Josephina Charles Nyagali aliyezikwa kwenye makaburi hayo ya mashujaa. Ni makaburi ambayo hayatambuliki Kitaifa lakini wenyewe wenyeji wanalitambua na kulienzi kuwa ni eneo walilolazwa mashujaa wa vita vya dunia.

Anga nayo ilitandaza wingu zito, lililofunika jua utadhania nalo lilikuwa linajumuika na waombolezaji kwenye kumaliza msiba huo. Kijiji kilifurika wageni mahashumu wa ndani na nje ya nchi waliokuja kuhitimisha msiba huo. Miongoni mwa wageni hao, alikuwepo Waziri wa Mambo ya Ndani wa Nchi ya Msumbiji, Mheshimiwa Allan Fernando, aliyetumwa kumwakilisha Rais wa Msumbiji katika msiba huo.

Pia alikuwepo Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa nchini Msumbiji Bwana Jacob Steven au maarufu kwa lakabu ya Komandoo 'JS' akiwa ni mteule mpya kwenye idara hiyo. Pia alikuwemo katika msafara huo toka nchini Msumbiji, Daktari Anabella Munambo akiwa ni Daktari Mkuu katika hospitali mpya ya "Quelimane Central Hospital" iliyopo katika jimbo la Zambezi. Hao walikuwa ni baadhi tu ya vigogo wazito toka msafara viongozi wa Msumbiji.
Kwa upande wa Tanzania, mkururu wa vigogo nao walifurika kijijini Mahiwa, kuanzia wa Mkoa na wa Kitaifa. Mawaziri, Makatibu Wakuu na Mkuu wa Idara ya Usalama ya Taifa Bwana Mathew Kilanga alikuwepo kundini. Wasioelewa kinachoendelea na kushangazwa na ugeni ule mzito pale kijijini walikuwa wanajiuliza bila kupata majibu.

Swali kubwa vichwani mwao lilikuwa "huyu Bi.Josephine Nyagali alikuwa ni nani haswa katika historia ya nchi ya Tanzania mpaka apate bahati ya kulazwa malaloni pamoja na wanajeshi mashujaa waliokufa katika vita vya kwanza vya dunia?". Heshima ya Bi.Josephina kuzikwa hapo, ilitokana na babu yake mzaa baba, hayati "Nyagali Wa Nyagali" aliyekuwa mpiganaji wa Jeshi la Mjerumani enzi za vita vya dunia na kuzikwa katika makaburi hayo. Vita vya Mahiwa katika ya Mjerumani na Muingereza vilipiganwa mwaka 1917.

Ambapo Jeshi la Mjerumani likiongozwa na Jenerali Paul Emil von Lettow-Vorbeck walichuana vikali na Jeshi la Muingereza likiwa chini ya uongozi wa Luteni Jenerali Jacob van Deventer. Vita hivyo vya Mahiwa vilisababisha vifo vya askari si chini ya 2,000 wengi wao wakiwa ni Wanajeshi wa upande wa Uingereza. Katika baadhi ya Wanajeshi waliofariki, babu yake Bi Josephina, Koplo Nyagali Wa Nyagali nae alikuwemo, akabahatika kuzikwa eneo hilo na baadhi ya wanajeshi wachache waliozikwa hapo.

Pia mtoto wake Bi.Josephina, Kachero Manu ndio ambaye alipendekeza mama yake mzazi azikwe hapo kando ya kaburi la babu yake mzaa mama, kwenye eneo ambalo hata yeye Kachero Manu atakavyofariki atapendelea azikwe hapo. Muda wote wa shughuli hiyo Dr.Anabella, Kachero Manu na Komandoo 'JS' walikuwa hawaachani wamegandana kama kupe. Wasiowafahamu wakadhania ni watoto mapacha walioachwa na marehemu Bi.Josephina Nyagali wanafarijiana wenyewe kwa wenyewe.

La hasha..! hawakuwa na udugu wowote wa damu, ila walikuwa ni marafiki waliosafishiana moyo ambao kufahamiana kwao katika urafiki huo ulitokana na kazi pevu waliyoshirikiana kuifanya siku chache zilizopita huko nchini Msumbiji. Dr.Anabella alishindwa kuyazuia machozi yake wakati anaweka shada la maua juu ya kaburi la Bi.Josephina. Alivuta taswira jinsi mama yake na baba yake mzazi na nduguze walivyochinjwa kikatili shingo zao na wahusika hao hao waliopoteza uhai wa mama mzazi wa rafiki yake.

Wote watatu walikuwa wanafarijiana na kumpoza mpambanaji mwenzao Kachero Manu aliyefikwa na maswahibu mazito. Kachero ambaye alifiwa na mama yake mzazi kwa kuchinjwa kikatili na mahasimu zake toka nchini Msumbiji katika usiku wa kuamkia siku ya Wapendanao "Valentine Day" ya mwaka 2016. Yeye hakuwahi kuhudhuria mazishi ya mama yake kwa sababu alikuwa na safari ya muhimu sana ya kikazi nchini Msumbiji isiyowezekana kughairishwa kwa sababu yoyote ile. Hivyo alivyorejea toka safarini, ikabidi aunganishe moja kwa moja Kijijini kwao Mahiwa kwenye maandalizi ya arobaini ya kuhitimisha msiba wa mama yake.

Kwa uzalendo wake huo wa kukubali kukacha kushiriki msiba wa mama yake mzazi kwa ajili ya kujitoa mhanga kwa maslahi ya Taifa la Tanzania na Msumbiji, ndio maana nchi ya Msumbiji na Tanzania kwa ujumla wakaipa uzito shughuli hiyo kwa kutuma wawakilishi wao wazito. Baada ya shughuli zote zilizopangwa kufanyika hapo makaburini kuhitimishwa, na kuashiria msiba huo kumalizika kwa kupanda msalaba juu ya kaburi la marehemu, msafara huo ukarejea nyumbani kwao Kachero Manu kwa ajili ya kutoa rambirambi zao.

Mpaka kufikia majira ya saa 12:30 magharibi shughuli zote zikawa zimehitimishwa na wageni mbalimbali wakaanza kurudi kwenye makazi yao waliyofikia kabla ya kurejea makwao.
"Mbona huufanyii kazi msemo wa waswahili ule wa Mgeni njoo Mwenyeji apone, unaniacha mrembo naenda kulala peke yangu Mjane mimi, wewe wa wapi wewe....!" alisema Dr.Anabella kiutani, akimpa shutuma rafiki yake Kachero Manu wakati tayari anajiandaa kupanda gari aliloandaliwa na serikali tayari kwa kuondoka. "Ng'ombe wa kuazima anakamuliwa wima, nisingekuacha bahati yako mmiliki yupo hapa msibani anakaba mpaka penati, hapa alipo amefura kwa hasira, wivu juu yako..!" alijibiwa Dr.Anabella huku akipewa tahadhari ya kuwa makini na mchumba wake Kachero Manu, Faith Magayane.

"Kwaheri...niagie kwa niaba yangu, maana asubuhi nimemsalimia kaninunia utasema mie mke mwenza wake, na Wamakonde tunavyoogopeka kwenye sekta ya chumbani, alipo hana amani kabisa na mimi...!" alisema Dr.Anabella, huku wakikumbatiana kwa sekunde kadhaa na Kachero Manu nyuso zao zikiwa na bashasha mpwito mpwito kisha akapanda kwenye gari na kuondoka msibani.

Komandoo JS alikuwa amejitenga kando wanapeana michapo na mkongwe mwenzake Bosi Mathew Kilanga. Hawa walikuwa ni maswahiba wakongwe waliofanya pamoja mafunzo ya Ukomandoo na sasa wote ni Wakuu wa Idara za Usalama wa Taifa, katika nchi za Msumbiji na Tanzania.

Kachero Manu akawaacha waendelee kusogoa na kukumbushiana enzi zao, na kuamua kujumuika na familia yake wakiendelea kubadilishana mawazo mbalimbali. Giza likazidi kutanda eneo ile na watu wa karibu kuanza kurejea majumbani kwao na wa mbali kuondoka zao ili maisha ya kawaida yapate kuendelea.


Februari ya huzuni na majonzi
"Piga risasi wale kule wanakimbia, fanya haraka sana hamna kuwaonea huruma manyang'au hawa. Hamna kuwachekea wezi wa rasilimali za nchi yetu ya Msumbiji" ova ova. "Sawa mkuu tutawapa kipigo cha mbwa koko" ova ova ". Msiache majeruhi hakikisheni vizuri wafe mara moja hatuna bajeti ya kutibu majeruhi, na hakikisheni mizoga mnawafukia katika mahandaki kuficha ushahidi ova ova".

Yalikuwa ni maelekezo ya kwenye redio za upepo baina ya Afisa Mkuu, Operesheni maalumu ya kutokomeza wahamiaji haramu kwenye jimbo la Cabo-Delgado, Inspekta Jenerali Mark Noble kwenda kwa askari wake waliokuwa wametawanywa mitaani kuwashughulikia wahamiaji hao. Milio ya risasi na mabomu ya machozi yalisikika kwenye kila kichochoro cha kijiji cha Namanhumbire, kilichopo kilometa 30, mashariki mwa Jimbo la Cabo-Delgado.

Hakuna mhusika waliyemkusudia kwenye operesheni hiyo aliyesalimika, wote walikumbwa na dhahama na sekeseke hilo. Balaa na belua kubwa ilizuka ndani ya Jimbo hilo lenye utajiri mkubwa wa madini ya rubi. Magari ya polisi yakiwa yamejaza polisi idadi ya kutosha yalikuwa yanaranda mitaani pamoja na magari maalumu ya kumwaga maji ya kuwasha kwa waandamanaji nayo yalikuwepo, yamekaa mkao wa tayari tayari kwa lolote.

Msako wa mtaa hadi mtaa, nyumba hadi nyumba, chumba hadi chumba, duka hadi duka ulikuwa unaendelea kuwabaini hao wanaoitwa wahamiaji haramu. Ving'ora vya magari ya polisi vyenye sauti ya kuogofya vilikuwa vinasikika kila kona. Cha kushangaza zaidi kwenye msako huo walengwa wakuu hawakuwa raia wa mataifa mengine bali walikuwa ni Watanzania.

Tena wengi wao ni wale wanaoishi kwa kufuata sheria za nchi kwa kupata viza ya kuingia Msumbiji na pia wakapata hati za ukazi. Mpaka kufikia majira ya saa tano usiku ya siku hiyo tayari mamia ya watu walikuwa wamefariki na wengine kujeruhiwa vibaya. Akina mama nao walikuwa wahanga wa uhalifu huo, wakajikuta wamebakwa hobelahobela na askari hao. Watoto wadogo wakajikuta wengine wao wamekuwa mayatima bila kutarajia. Mali za thamani kubwa zinazomilikiwa na Watanzania hao zikaporwa na askari hao madhalimu. Wale majeruhi waliosalimika wakapokonywa nyaraka zao muhimu kama vitambulisho na hati za kusafiria ili waonekane waliingia Msumbiji kwa kuzamia bila kufuata sheria.

Ili kuficha takwimu halisi za waliofariki, maiti hizo zilikusanywa na kuzikwa kwenye kaburi la pamoja la halaiki ili kupoteza ushahidi wa unyama uliofanyika. Walikuwa wanaogopa tukio lisije kuvuta macho na masikio ya wapenda haki na amani duniani, wakaanza kupaza sauti zao wakakitia kitumbua chao mchanga, wakaja kujikuta wapo kwenye mahakama ya uhalifu duniani iliyopo kule "The Hague", Uholanzi, wamepandishwa kizimbani.

Vyombo vya habari vya nchini Msumbiji vikalishwa habari potofu na Maafisa hao madhalimu walioendesha zoezi hilo haramu lenye malengo mahususi nyuma ya pazia. Wakazidi kuupotosha umma kwa kuwalisha matango pori kuwa waliouliwa ni wahalifu na wahujumu uchumi waliokuwa wanapora na kuchimba madini ya nchi ya Msumbiji kinyume na taratibu za nchi.

Wakasisitiza kuwa wahalifu hao walikuwa wamejihami kwa silaha kali za kivita, hivyo wameuliwa wakati wa mapambano ya ana kwa ana ya kurushiana risasi na wanausalama. Pongezi mbalimbali zikawa zinapeperushwa na viongozi wa juu serikalini kwa Bwana mkubwa, Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kazi nzuri aliyoifanya ya kuzihami rasilimali za nchi ya Msumbiji.

Silaha za kivita zinazosemekana kukamatwa eneo la tukio zikawa zinaonyesha kwenye runinga ili kuthibitisha umma wa Watu wa Msumbiji kuwa waliouliwa ni wahalifu wasiostahili kuonewa hata chembe ya huruma. Watanzania mamluki waliohongwa ngwenje za kutosha wakajifanyisha wamekamatwa kwenye tukio hilo, baadhi yao wakiwa wameshikishwa silaha, na kujitia wanatoa ushuhuda mbele ya vyombo vya habari kuwa walikuwa ni genge la uhalifu lililokuwa limejipanga kwa mbinu za medani za kivita, hivyo wanaomba msamaha toka vyombo vya dola.

Magazeti yakapambwa na picha za Afisa Mkuu kwenye operesheni hiyo, Inspekta Jenerali Mark Noble akisifiwa kama shujaa wa nchi, mzalendo na mfia nchi wa kiwango cha kutukuka. Mmoja wa Mawaziri waandamizi, hakubaki nyuma kubariki operesheni hiyo akatoa ahadi ya donge nono kwa askari wote walioshiriki kuwashikisha adabu wahalifu hao wa Cabo-Delgado, iwe motisha kwao kuzidi kujitolea kiuzalendo katika siku za usoni.

Watanzania wachache waliofanikiwa kutoroka kwenye sokomoko hilo, wakaja kutoa ripoti ya kina ya tukio hilo nchini Tanzania. Wakapaza sauti zao kwa kutumia vyombo vya habari, wakitaka ufanyike uchunguzi huru.

Ikabidi sasa Inspekta Jenerali wa Polisi wa Tanzania afunge safari mpaka nchini Msumbiji kwenda kuonana na Mkuu mwenzake wa Jimbo la Cabo-Delgado Bwana Mark Noble ili wayaweke sawa. Baada ya majadiliano ya karibia wiki nzima baina yao, Inspekta Jenerali wa Tanzania akarejea. Alipokanya tu ardhi,pale Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, waandishi wa habari walijikusanya wakiwa na kimuhemuhe na kiherehere cha kujua kilichojiri katika kikao hicho cha ujirani mwema baina ya vigogo hao wawili wa polisi.

"Tumekubaliana kimsingi pande zote mbili kwamba wahalifu siku zote hawana mipaka. Hii mipaka iliyowekwa na Wakoloni isitufanye tukashindwa kupambana na uhalifu na hasa haya makosa yanayovuka mipaka ni lazima tushirikiane. Na kikubwa zaidi ni kubadilishana taarifa na kufanya operesheni za pamoja, mara kwa mara” maelezo hayo mepesi ya uzani wa nyoya la kuku ya Inspekta Jenerali wa Tanzania yakaonyesha kabisa amezidiwa kete na mwenzake Inspekta Jenerali Mark Noble kwa kupewa taarifa za uwongo juu ya tukio hilo.

Jambo usilolijua ni kama usiku wa giza, vijana wa Mjini wanasema "Alilishwa matango pori na kutiwa ndimu juu ya matukio hayo hatarishi". Ndugu, jamaa na marafiki wa wahanga wa tukio hilo, wakakata tamaa ya kuona haki inatendeka kwa ndugu zao walioathirika kwenye uhalifu huo. Taarifa hiyo ilibaraganya kabisa ukweli halisi wa tukio hilo, kwani ilionyesha kama vile matukio hayo hayajafanywa kabisa na polisi wa Jimbo la Cabo-Delgado, bali ni mtifuano baina ya wahalifu wa Tanzania na Msumbiji.

Wakati shuhuda za wahanga wenyewe zinasema kuwa polisi wa Cabo-Delgado ndio watuhumiwa haswa wa vitendo hivyo wakishiriki kuvilinda vikundi vya kihalifu mitaani. Mategemeo na matarajio yao waathirika wa matukio hayo yalikuwa ni kuletewa taarifa yenye fusuli ya kutosha isiyoacha hata chembe yoyote ya mashaka. Ushindi ukawa umeelemea mikononi mwa genge hilo la wahalifu lililopo ndani ya mfumo rasmi wa nchi.

Walilolikusudia genge la wahalifu ndani ya mfumo rasmi likawa limeshatimu, wakiwa wamefanikiwa kumuongopea mpaka Inspekta Jenerali wa nchi ya Tanzania. Bila kujua ya kwamba wamekumbatia waya wa umeme mkubwa vifuani mwao utawateketeza bila kuacha masalio yao.

Chambilecho "Daima hamna marefu yasiyo na ncha, na haki siku zote ni kama mfano wa boya majini, haiwezi kufichwa kwa kuzamishwa, tabia ya haki siku zote ni kuelea juu".
Idara ya Usalama wa Taifa, Tanzania ilikuwa macho kodo, haijalala usingizi wa pono. Iikuwa ipo kwenye pembe za chaki inafuatilia matukio hayo kwa umakinifu na ukaribu zaidi. Wahalifu hao walichokoza nyuki, wakati wa kukiona kilichomtoa kanga manyoya ulikuwa unakaribia kwa upande wao.


Matukio hayo ya uhalifu yanayowawinda Watanzania pekee hayakukoma. Yakazidi kushamiri na kutamalaki katika Jimbo hilo la Cabo-Delgado lenye kusifika kwa utajiri mkubwa wa madini ya rubi nchini Msumbiji.

Watanzania hao wanyonge na madhulumu hawakuwa na mtetezi wa kuwasemea na kuwaokoa. Wakawa wanapopolewa mitaani kama mbogo msituni anavyowindwa na majangili.

Likaja kutokea tukio lingine la kutisha, tukio ambalo likavifanya Vyombo vya Usalama vya Tanzania vikose simile, na kuamua sasa kwa kauli moja kuwashughulikia Mafioso wote wa Jimbo la Cabo-Delgado wanaopenda kuwachokoa Watanzania.

Ilikuwa ni tarehe 08/02/2016 ya huzuni, simanzi na majonzi makubwa kwa nchi ya Tanzania. Watanzania wapatao 16 walipigwa risasi na kufariki hapo hapo huku makumi kadhaa wakijeruhiwa wakati wakiwa kwenye maduka yao ya kubadilisha fedha za kigeni na kununulia madini, kisha wakaporwa pesa zote na madini yao.

Watanzania hawa walikuwa wakiishi na kufanya kazi katika eneo lenye madini ya rubi liitwalo Montepuez, kwenye Jimbo la Cabo Delgado kaskazini mwa nchi ya Msumbiji.

Yalikuwa ni mauaji ya kinyama na yasiyokubalika kwa jamii ya watu waliostaarabika. Mauaji ambayo yalisababisha kilio katika kila kona ya nchi ya Tanzania, Bara na Visiwani, huku wananchi wakigubikwa na simanzi isiyomithilika na joto la hasira likichemka vifuani mwao.
Lakini kabla ya mauaji hayo, wiki mbili zilizopita serikali ya eneo hilo ilitoa muda wa siku 5 kwa raia wote wa Tanzania wapatao 5,000 waishio hapo Cabo Delgado kuondoka mara moja na kurudi nchini kwao Tanzania.

Hii haikuwa taarifa yenye kupendeza hata kidogo masikioni mwa wananchi wa Tanzania, hasa wakikumbuka udugu wa asili kati ya wananchi wa Tanzania na Msumbiji. Ni kama vile kuna watu walikuwa wanachezea sega la nyuki ili kuwagombanisha ndugu wa damu walioshibana.

Ni tukio ambalo lilileta simanzi na fadhaa kubwa kwa ndugu wa wahanga na Watanzania kwa ujumla. Mikasa hio endelevu ilikusudia kuchimbia kaburini mahusiano mema baina ya hizi nchi mbili.

Ilitaka kufuta mema yote ya siku za kisogoni yaliyotendwa na Watanzania kwa watu wa Msumbiji. Watanzania wengi haikuwahi kuingia akili mwao wala katika fikra zao hata siku moja kuwa itafika siku Watanzania watatendewa unyama kama huu na ndugu zao wa Msumbiji.

Ndugu zao kabisa wa damu wanaotenganishwa tu na mipaka ya wakoloni. Katu hawakutegemea msaada wao wa asali na maziwa katika kipindi cha kupigania Uhuru wa Msumbiji kutoka kwenye makucha ya mabeberu wa Kireno malipo yake yangekuwa shubiri.
Watu wa Msumbiji baada ya kufanikiwa kumng'oa Mkoloni, wakaanza kupigana vita vya wenyewe kwa wenyewe na kuzalisha maelfu wakimbizi. Bado Watanzania hawakuwafungia vioo ndugu zao, waliwakaribisha kwa mikono miwili waje nchini mwao, wakaishi nao kwa amani na utulivu. Wakashirikiana nao kutwa kucha katika shida na raha, katika mvua na jua bila utengano wowote.

Bila ya shaka tukio hili la mauaji ya watu 16 likasababisha uhusiano baina ya nchi ya Tanzania na Msumbiji kwenda zigizaga, Serikali ya Tanzania kupitia ubalozi wake nchini Msumbiji ukawa upo makini kufuatilia na kutoa msaada unaohitajika kwa wahanga wote wa machafuko hayo.

Pia ubalozi ukajitwika jukumu zito la kuwarejesha nyumbani wahanga wote wa kadhia hii mbaya, huku wakitega sikio kusubiri tamko toka kwa viongozi wa juu wa nchi ya Msumbiji.
Lakini ukimya ukazidi kutawala toka kwenye Vyombo vya Dola vya Msumbiji utasema waliokufa ni nguruwe pori wasio na thamani yoyote.

Kwa upande wa maadui wa Umoja wa nchi za Kiafrika, chokochoko hiyo baina ya nchi ya Msumbiji na Tanzania kwao ilikuwa ni furaha sheshe.

Mabeberu hao walikuwa wanajimwashamwasha pindi wakiona nchi huru za Kiafrika zinavyogombana wenyewe kwa wenyewe.

Lengo lao kubwa ni kuona Afrika nzima inaingia kwenye machafuko ya wenyewe kwa wenyewe kama ilivyo nchi za Congo, Sudani Kusini, Afrika ya Kati, Somalia, Mali na kwingineko ili wajichotee rasilimali bwerere bila jasho.

Lengo la mabeberu hao lilikuwa ni kuziona nchi za Afrika, kamwe hazijikomboi kutoka kwenye lindi la umasikini, ujinga na maradhi.

Walitamani wawe ni nchi ombaomba na tegemezi kwao miaka nenda miaka rudi. Moto wa kuni za fitina ulishawashwa na kuchochewa na maadui, ni busara tu za viongozi wa Tanzania na Msumbiji ndizo zinalizokuwa zinahitajika kuzuia uhasama na kukatana baina ya nchi zao.


Tarehe 11/02/2016 siku 3 baada ya mauaji hayo ya Msumbiji, muda wa saa 4:30 usiku kwa majira ya saa za Afrika Mashariki, Kachero nambari wani nchini Tanzania Bwana "Manu Yoshepu" maarufu kwa lakabu ya “Mwiba wa Tasi” ndio alikuwa anaingia nyumbani kwake maeneo ya Mbezi-Juu akiwa hana hili wala lile.

Alikuwa anaishi eneo linaloitwa “Kwa Pembe” akiwa amechoka vibaya kutokana na mazoezi magumu aliyotoka kuyafanya muda mfupi uliopita. Alikuwa ameloa jasho chepechepe mwili mzima huku anatwetwa kwa uchovu.

Alikuwa amejiwekea ratiba yake binafsi kuwa akitoka ofisini kwake saa 9:30 Alasiri juu ya alama maeneo ya Posta jijini Dar es Salaam, huwa anapitia ukumbi wa kufanyia mazoezi "GYM" maeneo ya Mwenge jengo jirani na kiwanda cha madawa ya binadamu cha SHELLYS.

Huwa anafika hapo kwenye ukumbi kisha anafanya mazoezi mazito kwa muda wa masaa yasiyopungua mawili mpaka saa 12 ya jioni. Hapo atafanya mazoezi ya kuongeza pumzi kwa kuendesha baiskeli na kukimbia, pia atafanya mazoezi ya kuongeza stamina katika mwili kwa kubeba vitu vizito, mwisho anamalizia kwa mazoezi ya viungo.

kisha akitoka hapo mazoezini atapitia kwenye jengo la maduka ya kuuzia bidhaa maarufu kama "Mlimani City Mall" iliyopo barabara ya Sam Nujoma kununua mahitaji mbalimbali ya nyumbani anayohitaji. Kwa kawaida maduka ya hapo unaweza kupata kuanzia bidhaa za chakula, nguo, vifaa vya elektroniki na kila kitu unachohitaji kinapatikana hapo.

Kama hana ratiba ya kujipikia nyumbani siku hiyo basi akitoka "Mlimani City Mall" atapitia kwenye mgahawa mdogo ulio nje ya "Mlimani City Mall" uliopo mkabala na kituo maarufu cha kujazia mafuta vyombo vya moto cha "TOTAL", hapo atakula chakula chake cha chajio atakachopenda.

Ila mara nyingi usiku huo halafu chakula kizito sana kinakuwa chepesi kukwepa kutoka kitambi. Kisha baada ya hapo ataondoka na gari yake pendwa aina ya "Nissan Navara" rangi nyeusi akipitia njia ya 'Makongo Juu' anakuja kutokezea Goba Kati, kisha anashika njia ya uelekeo wa kulia kwake mpaka muda wa saa 1:30 ya usiku mbichi anakuwa tayari amesharejea maskani kwake zamani.

Ambapo akifika nyumbani atapumzika nusu saa kisha ataanza mazoezi ya karate na taikondo kwa muda wa nusu saa tena, siku yake kwa upande wa mazoezi inakuwa inaishia. Baada ya hapo ataenda kuoga bafuni kwake kwa ajili ya kujiandaa kupumzika.

Alikuwa akipenda ataangalia televisheni yake mpaka saa 4 au 5 usiku halafu anaenda kujitupa kitandani kwake. Kama hajisikii kuangalia runinga basi atajichimbia ndani ya maktaba yake kujisomea vitabu mbalimbali vya kujiongezea ufahamu na maarifa.

Hiyo ndio ilikuwa ratiba yake ya mizunguko ya baada ya kazi aliyojipangia na kuiheshimu vilivyo ratiba yake. Ikifika mwishoni mwa juma ndio anapumzika nyumbani muda wote hatoki ila kwa dharura au kuwatembelea ndugu, jamaa na marafiki. Ila siku hiyo alichelewa mno kurudi nyumbani, na sababu ilikuwa wazi kulikuwa na msongamano mkubwa wa magari yaliyoshonana barabarani.

Foleni ya magari ilianzia maeneo ya Mwenge mpaka kufika Ubungo kwa hiyo magari yalikuwa yanakwenda kwa mwendo wa kinyonga au kama msafara wa Bwana na Bibi harusi wanaoelekea kwenye ukumbi wa kufanyia tafrija. Kwa kuwa yeye ni mzoefu wa Jiji la Dar es Salaam hilo halikumpa shinikizo wala wahaka wa moyo, zaidi ya kubaki kuchukia tu moyoni.
Maana Jiji la Dar es Salaam ni Jiji ambalo huwezi kukadiria utafika kwa muda muafaka sehemu unayoikusudia. Jiji hili wewe unaijua saa ya kutoka tu lakini saa ya kufika ni majaliwa yake Mola. Ukiwa mgonjwa huwezi kufika kwa wakati hospitalini, ukiwa muajiriwa huwezi kuripoti kibaruani kwako kwa muda muafaka na ukiwa mwanafunzi ukifanya masihara daima utakuwa unachezea viboko vya walimu wako.

ITAENDELEA BAADAE
kukipata kitabu-Full Nicheki
0625920847/0684900249View attachment 1443705

Muendelezo bonyeza link hizi

Sehemu ya pili
Sehemu ya tatu

Sent using Jamii Forums mobile app
Hardcopy ?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Nicheki 0625920847
Mikoani vipo DODOMA, ARUSHA, MOROGORO, MBEYA, TANGA, MTWARA NA LINDI

Sent using Jamii Forums mobile app

"CABO-DELGADO" KIPO MTAANI TAYARI KWA BEI YA TSHS.10,000/=
"Cabo-Delgado" ni Jimbo lililopo Kaskazini mwa nchi ya Msumbiji. Ni Jimbo ambalo Wafanyabiashara wa Kitanzania walipatwa na madhila makubwa kutokana na kujihusisha Biashara ya madini ya Rubi.
KUKIPATA KITABU HIKI WASILIANA KWA NAMBA ZIFUATAZO:
(1)DAR ES SALAAM/PWANI-0625920847
(2)UBUNGO/DAR ES SALAAM-0784033820
(3)MTWARA-0625065669
(4)TANGA-0713514946
(5)MBEYA-0717075364
(6)ARUSHA-0625920961
(7)MOROGORO-0718077763

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO-DELGADO-PART 09
Alipoingia akakikagua vizuri na kuridhishwa nacho kisha akamwambia mhudumu yule, "nitaandikisha taarifa zangu nikiamka, sasa nataka nipumzike kwanza nimechoka sana".
Mhudumu akajibu "hamna shida ila usiache kuandika ukiamka maana sasa kila baada ya masaa huwa wanapita polisi kukagua wageni waliofika katika Mji wetu, tusipokuandika tutaingia matatizoni". "Don't worry..!, nitaandika" alisema huku akiubugaza mlango wake.
Moyoni mwake aliweka nia ya kutafuta nyumba ndogo ya kukodi kuepusha usumbufu wa polisi kabla hajamaliza kazi yake iliyomleta. Kazi ambayo alitaka kuimaliza ndani ya wiki moja tu isizidi awe ameusambaratisha mtandao wote.
Akaingia chumbani akapangilia vitu vyake kiumakini mkubwa kisha akalala usingizi mzito wa masaa yasiyopungua saba. Aliamka saa 7:15 mchana akiwa na njaa kali sana ndipo akakumbuka hajatia chochote kitu tumboni kwa muda mrefu tokea alivyokula Mtwara mjini.
Ila anachokumbuka ni kuwa alimeza vidonge vyake anavyotumia kupoteza njaa aina "Phentermine" akiwa yupo ndani ya "pick-up" ya Halmashauri ya Nanyumbu baada ya hapo hakusikia njaa tena.
Harakaharaka akajizoa kitandani akaanza mazoezi mafupi ya viungo ya muda wa robo saa kama kawaida yake kila anaposhtuka usingizini. Baada ya hapo akakimbilia maliwato kujimwagia maji ili achangamke na kujisikia vizuri.
Baada ya kuvaa akatoka nje ya nyumba hiyo ya wageni ya "Nzuwa lodge". Alipotokeza hapo nje akaona bango kubwa la mgahawa ambalo linaelekeza kuwa kando ya Lodge kama meta 20 ndipo ulipo.
Ulikuwa ni mgahawa uliojikita zaidi kwente kupika maakuli ya asili. Wageni wengi hasa watalii waliokuwa wanatembelea Cabo-Delgado walikuwa wanapenda kwenda kula vyakula vya kienyeji kwenye mkahawa huo.
Hapo ukifika asubuhi ukihitaji kifungua kinywa utapata uji wa totori. Huo ni uji unaotengenezwa kwa kutumia unga unaoitwa "Nalungutu".
Unga wa Nalungutu unaotokana na makapi ya mwanzoni ya nafaka ya mtama. Matayarisho yake makapi hayo ya mtama huwa yanafunikiwa kwenye kinu ili yavunde kidogo afu yanachanganywa na mabibo ya korosho wakati wa kupika au unaweza kuchanganya jivu la majani ya ufuta ili kuleta uchachu.
Uji huo wakati unakunywa unapewa utumie majani ya mnazi kuchotea. Hapo ndio utamu wake unazidi kuliko kunywa na kijiko. Uji huo ni shibe ambayo ukila sasa hivi unaweza kukaa masaa mpaka 8 shambani unalima tu bila kuhisi njaa.
Kachero Manu akakata shauri ya kwenda mgahawani huko akapate maakuli ya asili. Alipofika tu Mkahawani bila hata salamu akaagiza kwa mhudumu uji wa Totori, Machoba na Pure, usicheze na njaa wewe. Hayo Machoba ni futari ya mihogo mikavu iliyoungwa na nazi. Na pure ni chakula mchanganyiko wa mahindi na maharage, maarufu kama Makande.
Alipoletewa chakula chake tu akaanza kufakamia chakula hicho kwa pupa kutokana na njaa yake huku akijua usiku mwingine wa misuko suko unakuja. Chakula hicho alikuwa amewahi kula sana utotoni mwake, hivyo kilikuwa kinamkumbusha mbali sana. Alipomaliza mlo wake akaagiza juisi ya dafu baridi sana kwa ajili ya kushushia mlo wake.
Alipomaliza kula akatoka nje ya mgahawa akakaa kwa nje kwenye kiti uzembe cha kujikunja akipunga upepo na kuruhusu vimeng'enyo vya mwili vifanye kazi yake maridhawa ili viupe mwili virutubisho stahiki. Wakati huo huo macho yake yamekodoa kodo uelekeo wa Nzuwa Lodge pale alipofikia.
Hakuwa amekaa kiboyaboya, kwenye usalama wake alikuwa makini sana. Baada ya dakika kadhaa akawa amefungua gazeti la lugha ya kireno liitwalo "Domingo" linalotoka kwa wiki mara moja anazuga anasoma kumbe anapoteza watu maboya tu, kwa sababu hakijui Kireno hata tone.
Gazeti ambalo alilichukua mapokezi kule nyumba ya wageni alipofikia, wakati anaacha funguo wa chumba chake wakati anatoka kuja kula. Kwa mbali maeneo ya pale "Lodge" akaona gari "Toyota Land-cruser" rangi nyeupe limepaki kwa nje bila kufuata utaratibu wa kukaa kwenye maegesho.
Hisia zake zikamtuma awe makini nalo hilo gari, kwa vyovyote vile itakavyokuwa linaendeshwa na dereva mjuba asiye na chembe ya ustaarabu. Kwa Kachero mzoefu kila kitu unachokitilia mashaka lazima uwe makini nacho usikipuuzie hata kidogo.
Akiwa bado ametumbua macho uelekeo wa pale iliposimama ile gari, fajaa kwa mshangao mkubwa akaona linatoka lile gari kwa kasi kuja uelekeo wa njia ile ile ya mgahawa aliopo. Tumbo lake likaanza kupata joto na kumvuruga, akidhania labda anafuatwa yeye pale alipo.
Akajigusa maeneo ya tako lake la kushoto akauhisi mguu wake wa kuku alioufumbata kiunoni upo, akatulizana. Alichofanya ni kulinyanyua gazeti lake juu zaidi ya uso wake kujificha nalo lakini huku anatupa jicho pembe aweze kuzisoma namba za gari kama ataweza.
Kwa kasi iliyopita nayo aliambulia namba mbili za mwanzo tu "MBA-08.." likawa limeshatimuwa vumbi limetokomea mitaani. Akashukuru uamuzi wake wa kubeba gazeti ambalo limemsaidia kujificha nalo licha ya kwamba hafahamu kabisa lugha hiyo ya kireno.
Hima hima akafunga gazeti lake akamuita mhudumu kisha akalipa pesa ya chakula chake alichokula na kinywaji chake na kurejea "Lodge" kuangalia usalama wake.
Alipofika mapokezi kuchukua funguo wakati anaelekea kwenye chumba chake akasikia sauti ya mhudumu wa mapokezi, "kaka samahani asubuhi hakuandika kwenye kitabu cha wageni, ulisema umechoka sana" alisema dada yule.
"OK... sawa" akarejea Kaunta pale na kujaza jina lake la uwongo la kizanzibari "Hasan Ibn Hussein" kama linavyoonekana kwenye hati ya kusafiria aliyokuja nayo Msumbiji.
Alivyomaliza kujaza akaelekea chumbani kwake na alipoingia tu kengere ya hatari ikagonga kichwani akawa anajiuliza "kuna watu wameingia chumbani, je ni wahudumu wa usafi? hapana sio wahudumu alijiambia maana wamefanya upekuzi lakini huwezi kufahamu mpaka uwe mtaalamu".
Akaurudishia mlango wake akatabasamu baada ya kukiona kitabu chake alichokiacha kipo mezani. Nyaraka zake muhimu zote kama hati ya kusafiria, kadi za benki, baadhi ya pesa zake na vinginevyo vilikuwa kwenye kitabu hicho maalumu cha kijasusi kinaitwa kitaalamu "Hollow Book Safe".
Kitabu ambacho ukikiona kijuujuu utadhania ni kitabu tu cha kujisomea kama vilivyo vitabu vingine lakini katikati ya kitabu hicho kilikuwa hakuna kurasa bali kuna uwazi unaoweza kutunzia vitu vyako muhimu.
Kisha akaelekea kwenye kingo ya dirisha akachomoa kiberiti chake cha kuwashia sigara aina ya "HDALTH" lakini hakikuwa kiberiti cha kawaida, ni kiberiti cha kijasusi ambacho kina uwezo wa kurekodi video. Akatoa "chip" kutoka kwenye kiberiti hicho akahamishia kwenye kompyuta mpakato yake ndogo aliyoitoa kwenye begi lake.
Akaiwasha Kompyuta na kuanza kuangalia wavamizi wake. Akaanza kuona watu wawili wote wamevaa miwani nyeusi na suti za rangi bluu wapo chumbani wakiwa na haraka na sura za wasiwasi wanapekuwa pekuwa mpaka chini ya godoro.
Wakaingia bafuni wakatoka na sabuni ya kuogea wakaikata katikakati kutafuta kitu wanachokitaka kisha wakaweka sabuni mpya kama ile ya mwanzoni wakaenda kwenye pipa dogo la taka la chumbani nako hawakuona chochote.
Baada ya hapo wakatoka kwa haraka wakafunga chumba. Baada ya kumaliza kuangalia video ile fupi, akashusha pumzi ndefu, ya kushukuru Mungu.
Akaanza kuwaza kuwa kazi imeanza na wameshajua kuwa yupo Cabo-Delgado, je wamejuaje? ndani ya masaa machache tu wameshafanikiwa kufika mpaka alipofikia, akajiapiza lazima agangamale na awe makini.
Anapambana na genge la watu makini na hatari sana tena wanaoijua vizuri kazi yao. Hivyo akaweka nia ya kwenda haraka nyumbani kwa mzee Masebbo mtaa wa Ruvuma nyumba namba 23B huenda akapata dondoo za kuwasaka wabaya wake.
Lakini kwanza atahitaji msaada wa Mzee Jacob Steven maarufu kama "Komandoo JS", komandoo mstaafu aliyepewa mawasiliano yake na Bosi wake kazini, kuwa lazima amsake Komandoo JS aweze kumuwekea ganda la ndizi la kutekeza nalo.
Alikuwa anataka kumtafuta Mzee Jacob kwanza amsaidie kupata gari la kutumia la kukodisha mwezi mzima, pili amsaidie kupata namba za usajili wa gari za kufoji hizo ndio atazitumia kwenye gari ili kuwapoteza vyombo vya dola kufuatilia nyendo zake za nyendo za hilo gari.
Na tatu alitaka apate msaada wa nyumba ya kupanga kwa muda wa mwezi mzima, hakutaka tena kuwindwa windwa kwenye nyumba za wageni kama changudoa.
Akajiandaa kuondoka kwa kuvaa nguo zake za kazi akaitoa bastola yake kiunoni na kuibusu. Akapiga magoti chini akasali sana kwa muda wa robo saa mpaka machozi yakawa yanabubujika kwenye paji lake la uso kama maji.
Huyu ndio Kachero Manu anakuwa karibu sana na Mungu hasa kwenye wakati mgumu.
Daima Mseminari atabaki kuwa Mseminari tu huyu ndio Manu yule wa Namupa Seminari ni Padre aliyegeukia gwanda za kuleta amani ya mwili kwa mtutu wa bunduki kwa watu ambao ni vichwa maji kama akina Alfredo na vibaraka wenzake.
Akafunga chumba chake na kurudisha funguo mapokezi mgongoni akiwa na begi dogo huku akitia nia kutokurudi tena pale.


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom