Riwaya: "Cabo-delgado"-part 01

Riwaya: "Cabo-delgado"-part 01

RIWAYA: "CABO-DELGADO"-PART 10

Chikulubu, Utingo msaliti hana fadhila
"Chikulubu Wa Chipoku" ni kijana aliyechukuliwa na dereva Masebbo tokea akiwa ghulamu wa miaka 15, na kwa bahati mbaya sana hakujaaliwa kusoma hata darasa moja maishani mwake, mbumbumbu mzungu wa reli hana lolote alijualo hapa duniani kuhusu elimu ya darasani.
Wazazi wake walikuwa ni Wamakonde Chale wa Msumbiji ambao kipindi cha msimu wa kilimo wanavuka mpaka na kwenda Tanzania kufanya vibarua vya kilimo katika vijijini vya mpakani kwa malipo ya mshahara tonge, mkia wa mbuzi usiokidhi mahitaji yao ipasavyo.
Msimu wa kilimo ukiisha wanarejea kwao Msumbiji kusubiri msimu ujao wa kilimo. Hayo ndio yalikuwa maisha yao daima dawamu wanacheza katika mnyororo wa umasikini.
Ilitokea siku moja isiyo na jina dereva Masebbo akiwa na Lori lake alipata pancha ya lori lake jirani na kijiji cha akina Chikulubu na utingo wake wa kawaida hakuwepo kwenye safari bila kutoa taarifa kwa dereva Masebbo hivyo kumpelekea dereva kusafiri bila Utingo.
Chikulubu ndio alimsaidia dereva Masebbo kubadili tairi la gari pamoja na kumtafutia chakula na maji. Kama zali la mentali vile, hiyo ikawa ni sababu ya Chikulubu kula maisha akapata ajira kama Taniboi wa Mzee Masebbo.
Sasa safari za mipakani kwenda Tanzania, Zambia na Zimbabwe zikawa kama kuingia chooni kwa Chikulubu, kismati kinamtembelea. Maisha yake sasa yakapata naizesheni na nafuu kubwa na akahama kijijini na kupanga chumba katika Mji wa Cabo-Delgado.
Amedumu na dereva Masebbo kwa muda wa miaka 10 mtawalia. Lakini hivi karibuni akaanza kubadilika tabia mambo yake yakaanza kuwa tumbitumbi yasiyo na kichwa wala miguu. Hasa baada ya kuanza kukaa vijiweni, akaanza kupenda wanawake, pombe na kila aina ya starehe za vijana wa Mjini.
Vijiwe vya vijana wa kihuni wenye hadithi za kwenda kutafuta maisha bora Afrika ya kusini na ulaya kwa kuzamia meli, na kupata maisha bora bila kufanya juhudi na maarifa. Akaanza tabia ya kuiba mafuta kwenye gari la Mzee Masebbo. Vijana wa mjini wanaita "kupiga nyoka" gari.
Mzee Masebbo alimuonya sana zaidi ya mara tatu hasa akimchukulia kama mtoto wake aliyemtoa kijijini zaidi ya miaka 10 iliyopita mpaka amebaleghe mikononi mwake. Lakini kama ujuavyo mtoto akinyea kiganja hakikatwi kinasafishwa tu, ndivyo namna Mzee Masebbo alivyokuwa anamvumilia Chikulubu.
Sasa kilichomzuzua Chikulubu ni tukio la hivi karibuni la Taniboi mwenzake ambae ni rafiki yake kipenzi cha kuwasakizia Wafanyabiashara wa madini kutoka Tanzania waliokuwa wamewapakiza kwenye gari lao kwa Mafioso wa Alfredo. Ambapo baada ya wale Wafanyabiashara kuporwa madini yao Taniboi huyo alilipwa pesa nzuri sana.
Pesa ambayo iliyomuwezesha kupanga nyumba nzima na kununua bodaboda mbili zinazovuka mpaka kati ya Tanzania na Msumbiji kubeba mizigo. Toka siku hiyo Chikulubu nae akawa ni mtu wa macho juu juu, shingo feni mwenye wahaka mkubwa kwa kila abiria anayehisi ni Mtanzania wanayempakia kwenye gari lao.
Sasa siku ile ya safari nadhani unakumbuka alikuwa anamtazama sana Kachero Manu mpaka Kachero akashtukia. Sasa hisia zake kuwa Kachero Manu ni mtu muhimu na anaingia nchini mwao Msumbiji kinyemela ni pale waliposimamishwa na askari barabarani halafu alipoulizwa dereva Masebbo kama wote ni raia wa Msumbiji, na dereva Masebbo akajibu wote ni raia hapo hapo akaanza kushikwa na tamaa ya utajiri kupitia Kachero Manu.
Akajua ni mtu muhimu ndio maana Mzee Masebbo anamficha kwa wale askari wasimkamate. Pia kitendo cha Mzee Masebbo kuzuga gari limeharibika ili kumsubiria Kachero Manu, Taniboi Chikulubu alishtukia mchezo mzima.
Kitendo hicho cha usanii wa dereva Masebbo kilimpa maono kuwa Kachero Manu sio mtu mzuri ndio maana analindwa na dereva Masebbo kwa hali na mali. Na kama akifikisha taarifa zake kwa Mafioso wa Alfredo chini ya uongozi wa Inspekta Mark Noble atalipwa pesa sufufu za kumfanya aishi maisha mazuri.
Hivyo walipofika tu Cabo-Delgado, pale Msikitini hakupata hata muda wa kuagana hata na dereva wake kwa kile kimuhemuhe na kiroho papu cha pesa ya madili. Akatokomea zake mtaani kumtafuta yule rafiki yake ampeleke kwa Mafioso wa Cabo-Delgado ili awape penyenye za Kachero Manu kuwa amebebwa kwenye gari la Bosi wake Mzee Masebbo.
Vijana wa kazi wa Inspekta Jenerali Mark Noble walivyoletewa taarifa tu kitu cha kwanza walienda kwenye kituo cha taksi na kuwaelezea wajihi wa mtu wanayemtafuta bahati nzuri wakampata yule dereva aliyempeleka Kachero Manu pale Nzuwa Lodge.
Mafioso walipofika Nzuwa Lodge, walijitambulisha kama maafisa usalama wakakagua kompyuta inayorekodi taarifa za wageni. Bahati mbaya mlengwa wao hakuandika taarifa zake mapema hivyo ikazidi kuwatia mashaka kuwa Kachero Manu sio mtu mzuri.
Hivyo wakaingia chumbani kufanya upekuzi nako hawakupata wanachokikusudia. Wakiwa mule chumbani wakapigiwa simu na kupewa taarifa mbaya ya kuuliwa Askari 6 wanaokagua Watanzania wanaoingia kupitia mpakani.
Pale pale ndio wakaondoka mbio mbio kuelekea nyumbani kwa dereva Masebbo kumfanyia mahojiano juu ya yule mgeni aliyembeba kwenye gari ni ni nani na kaja kufanya nini Cabo-Delgado, kama walivyopewa taarifa na Taniboi wake Chikulubu.
Taniboi msaliti asiyejua kulipa fadhila, ama kweli "shukrani ya punda ni mateke, daima tenda wema uende zako usingoje shukrani, fadhila mfadhili mbuzi utaambulia mchuzi, binadamu ana maudhi".

Mauaji mtaa wa Ruvuma nyumba namba 23B
Mzee Masebbo aliporudi safari yake baada ya kufikisha mzigo wa magendo wa watu salama alienda kwenye kampuni ya tajiri wake akaliegesha gari na kurudi nyumbani kwake kupumzika. Nyumbani kwake alikuwa amebaki peke yake, mkewe na watoto wake watatu wanaosoma sekondari walikuwa wamekwenda likizo eneo la Muidumbe moja ya Wilaya za "Cabo-Delgado".
Huko Muidumbe ndipo ambapo ndio walipo wakwe zake Mzee Masebbo. Alivyofika nyumbani kwake kwanza alikunywa chai kwa mkate alionunua njiani wakati anarejea nyumbani kisha alipitiliza kuoga. Baada ya hapo akaingia kulala kwa nia ya kuamka mchana, afanye usafi wa nyumba na kupika chakula ale.
Alivyopanda kitandani hii asubuhi Mzee Masebbo alikuwa na mawazo mengi sana, hasa juu ya uamuzi anaotaka kuchukua wa kuacha kazi. Alikuwa hapendezwi na namna kampuni yao ya usafirishaji ilivyoanza sasa kushiriki kubeba mizigo haramu ya Mafioso wa Alfredo.
Kitu ambacho hakupendezwa na dhulma anazoshiriki kufanya kwa kuiba Maliasili za Tanzania na kuwafanyia vitendo vya kikatili Watanzania. Aliweka nia mwisho wa mwezi ukifika akipokea mshahara wake tu, ndio utakuwa mwisho wa ajira yake.
Lakini pia akawa anawaza ataendeshaje familia yake bila kazi, hasa katika Mji mkubwa kama huu wa Cabo-Delgado ambao gharama za maisha zipo juu kupitiliza kutokana na ujio wa Watalii toka pande mbalimbali za dunia. Watoto wake bado wanasoma sekondari kwenye shule za kulipia gharama kubwa na mkewe ni mama wa nyumbani, golikipa maarufu mtaani hawezi hata kujitafutia senti tano nyeusi.
Pia na kijijini wazee wake wameshakuwa watu wazima wanamtegemea yeye kwa hali na mali, hawajiwezi kwa sukari wala si kwa chumvi. Fikra hizo zikamfanya ajiweke njia panda, achague mwenyewe kusuka ama kunyoa.
Lakini mwishowe akapiga moyo konde kuwa lolote liwalo na liwe atapeleka barua ya kuacha kazi itakapofika mwisho wa mwezi, hilo ndio likawa hitimisho lake.
"Penye nia pana njia, nitakapoacha kazi nitatafuta sehemu nyingine ya kupatia mkate wangu wa siku na Mungu atanifungulia njia", aliujaza moyo wake ushujaa. Akajikuta anapitiwa na usingizi muda huo wa saa 4 asubuhi.
Mzee Masebbo aliamshwa usingizini na sauti za vishindo vya kugongwa kwa mlango wake kwa nguvu. Mwanzoni alidhania kama yupo ndotoni lakini aliposhtuka akajua kuna watu wanagonga kiukweli sio njozi.
Akapatwa na hofu ya kutaka kufahamu nini kimetokea mpaka anaongewa mlango wake kibabe. Maana namna alivyokuwa anaishi na majirani zake kila mtu anashika hamsini zake.
Huwa wanaonana kwenye matukio ya msiba au sherehe lakini hawana utamaduni wa Kitanzania wa kutembeleana kujuliana hali hujambo sijambo. Akakurupuka toka kitandani, kitambi wazi na pajama yake mbio mbio kwenda kwenda kufungua.
"Nani mwenzangu"? aliuliza Mzee Masebbo wakati anajiandaa kukitegua kitasa cha mlango kwa funguo. Akajibiwa toka nje ya mlango "fungua sisi ni wana usalama tuna mahojiano na wewe". Mwili wake ukapigwa na ubaridi wa ghafla kwa sekunde kadhaa, haja zote kubwa na ndogo anazihisi zinagonga chupi kwa uoga.
Akaanza kutetemeka, kijasho chembamba kinamvuja huku akijiuliza bila kupata majibu kafanya kosa gani. Akapiga moyo konde, akajikaza kisabuni akaamua awafungulie maadamu dhamira yake ipo safi moyoni na hana kosa lolote.
Alipofungua tu wakaingia vijana wawili kwa kishindo. Walivalia suti za bluu na miwani.
"Yupo wapi abiria wako toka Tanzania uliyekuja nae leo usiku?" aliulizwa swali la kushtukiza Mzee Masebbo kwa ukali tena kuwa na ustaarabu. Akajibu kwa sauti ya kitete "mie sijapakiza Mtanzania, walikuwa wanafunzi wa madrasa na Maustaadhi wao basi", alidanganya Mzee Masebbo, huku akiomba Mungu kimya kimya uwongo wake ukubalike.
Hakujua kama wanazo taarifa zake zote, nje ndani toka kwa Taniboi wake Chikulubu. "Mzee mzima kama wewe unasema uwongo hata huoni aibu? Taniboi wako katueleza kila kitu usicheze na akili zetu wewe kikaragosi", alisema mmoja wao wale majambazi kwa hasira, huku akimsogelea amuadabishe.
Mzee Masebbo uso wake ukavaa taharuki, sasa akijua Chikulubu ameshamuuza. Chikulubu aligeuka zigo la misumari habebeki tena. Sasa tutakufundisha namna ya kusema ukweli, alisema mmoja wapo huku anamfuata Mzee Masebbo na kumpiga ngwara, Mzee Masebbo alianguka mzima mzima kama gunia la mahindi toka Zimbabwe la uzito wa kilo mia.
Akaangukia mdomo na kuvunja meno kadhaa. Damu zikaanza kumchuruzika kinywani bila kizuizi. Kisha akamkaba roho kwa kabali juu kidogo ya koo la Mzee Masebbo. Akaanza kukosa hewa safi, "mtani...u....aa.. bu... r.... .......e, mi...mi... simf....a.... h... a..... mu" alisema Mzee Masebbo kwa tabu sana, akikataa kuwa Yuda dhidi ya Kachero Manu.
"Jimmy muache kwanza huenda atasema, eheee wewe babu eleza haraka hatuna muda wa kupoteza tutakupoteza sasa hivi ukifanya mchezo" alisema mmoja wa wajuba wale aliyejipambanua kama ni kiongozi wa mwenzake.
Jimmy akamuachia koo Mzee Masebbo, akaanza kuhema kwa tabu kisha akakohoa makohozi yaliyochanganyika na damu, kisha akaanza kujieleza. "Ni kweli nilimpakia Mtanzania lakini simfahamu kiukweli shughuli zake, nilimsaidia tu kiubinadamu, kwa sababu hamna usafiri wa uhakika kwa sasa. Huo ndio ukweli wangu mtaniua bure lakini sina ninachokijua juu yake", alijieleza Mzee Masebbo kwa uchungu akijua fika anataka kutolewa sadaka bila kosa lolote.
"Kwanini sasa walipokuja Askari kukuuliza kama wote ni raia wa Msumbiji uliamua kumficha mgeni wako?" aliendelea kusailiwa na Jimmy. Mzee Masebbo akawa hana la kujibu anaangalia chini tu, amepatwa na fadhaa huku anajifuta damu kwenye ncha mdomo wake.
"Je unafahamu kuwa huyo mgeni wako uliyemleta mpaka Cabo-Delgado ameua askari wetu 6?, Sasa malipo ya umamluki ni risasi ya ubongo ukasimulie huko jongomeo unakokwenda kuwa usaliti haufai", bila kuchelewa Jimmy akafyatua risasi iliyompata Mzee Masebbo kisawasawa kwenye paji lake la uso na kukifumua kichwa chake kama tikitimaji lililopasuka.
Mzee Masebbo akaanguka chini na kuanza kufafaruka kwa kutupa tupa miguu yake kama mgonjwa kifafa akipigania roho yake. Bila kuchelewa wakatoka nje na kupanda gari lao wakatokomea zao, na kumuachia Mzee Masebbo anapigania uhai wake katika dakika za mwisho mwisho kabla hajaelekea jongomeo.


Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA-CABO DELGADO-PART 11


"Mwiba wa Tasi" kazini
Kachero Manu baada ya kutoka nje ya Nzuwa Lodge akiwa na kibegi chake alielekea upande wa kushoto wa barabara akatembea kama meta 70 na ushee hivi akakatiza barabara ya kushoto kwake. Akajikuta ametokezea stendi ya daladala ya kuelekea Pemba, makao makuu ya jimbo la Cabo-Delgado.
Nyuma ya stendi hiyo kulikuwa na vibanda vingi vya biashara vilivyochangamka ikiwemo kibanda cha "Internet Cafe" kinachotoa huduma za wavuti. Mlango wake kibanda hicho ulikuwa umetengenezwa kwa mbao ya Mninga, ukiwa umenakshiwa kwa marembo marembo ya maua yenye kupendezesha.
Alikata shauri kwanza awasiliane na Mzee Jacob Steven au ukipenda muite Komandoo "JS", Komandoo mkongwe na tegemeo wa nchi ya Msumbiji, lakini alikuwa ni kama lulu iliyotupwa jangwani, hatumiki tena. Ni mmoja wa Makomandoo watano bora barani Afrika waliofuzu mafunzo pamoja na Bosi wake Kachero Manu, Mzee Mathew Kilanga.
Kwa sasa alikuwa anafanya kazi zake binafsi za uvuvi na pia alikuwa na kampuni binafsi ya upelelezi ambayo aliwaachia vijana wake aliowapika kwenye upelelezi waiendeshe. Alipoingia kwenye "Internet-Cafe" akalipia muda wa nusu saa wa kuperuzi mtandao.
Akafungua barua pepe yake ili kurambaza taarifa zozote muhimu alizotumiwa kisha alituma ujumbe wa barua pepe kwa komandoo JS. Kwa bahati nzuri Komandoo JS alikuwa yupo kwenye mtandao muda huo huo hivyo wakaanza kuchati.
Akajitambulisha kwa kutuma namba za siri maalumu alizopewa na Bosi wake za utambulisho, hivyo komandoo Jacob Steven akamtambua Kachero Manu kuwa ni kijana wa komandoo mwenzake wa Tanzania Bwana Mathew Kilanga. Gari aliloomba apatiwe kwa kukodi akapewa ahadi kuwa baada ya dakika 45 atalikuta gari kwenye maegesho ya duka la mikate "Bakery padaria".
Pia ndani yake atakuta namba za gari feki mbili za kubadilisha zipo kwenye gari pamoja na funguo za nyumba ya vyumba viwili ambayo ipo katika mtaa wa "Stadium". Pia akapewa ahadi ya kusaidiwa vijana wa kazi wawili kama atawahitaji.
Akafanya malipo ya gharama zote kwa njia ya mtandao kwa kuhamisha pesa kutoka kwenye akaunti yake kwenda kwenye akaunti ya Komandoo Jacob Steven. Ndani ya dakika 25 tu akawa ameshamalizana na Komandoo JS.
Alipomaliza huduma ya wavuti aliyotumia akatoka nje ya "Internet Cafe" akawasha data ya simu yake ya mkononi yenye namba iliyosajiliwa kabisa ya mtandao wa "Mcel" ambayo alipewa Tanzania na Sekretari wa Bosi wake Mathew Kilanga. Akaingia kwenye ramani ya kimtandao ya "google map" akaitafuta wapi ilipo "Bakery padaria".
Akajikuta anatabasamu mwenyewe na kujiona mjinga, akazima data ya simu yake. Kumbe hakuhitajika hata kukodi taksi ni mtaa wa tatu tu kutoka pale alipo ndio ilipo "Bakery Padaria". Zilikuwa zimebaki dakika chache tu kutimia muda alioahidiwa kulikuta gari. Akaanza kutembea mdogo mdogo huku akibarizi Mji, kuelekea "Bakery padaria".
Alipofika hapo moja kwa moja akapitiliza ndani ya duka kwa ajili ya kununua mchapalo wake. Humo akakuta aina mbalimbali za mikate karibia ya sehemu tofauti za dunia kwa mapishi yake. Alikuta mikate ya boflo iliyotengenezwa kwa ngano ina umbo la mstatili, pia kulikuwa na mikate ya mofa yenye umbo la duara inayotengenezwa kwa unga wa mtama, uwele au mahindi na akakuta mikate ya unga wa ngano iliyochanganywa na unga wa mhogo.
Akachagua mikate mitatu iliyokatwa silesi ya mchanganyiko wa unga wa ngano na unga wa muhogo. Moja ya mikate mitamu sana na inapendwa sana maeneo ya Afrika magharibi hasa nchini Naijeria. Alijua huenda akakosa muda wa kula usiku huu, hivyo akiba haiozi akabeba na juisi ya chupa ya plastiki ya machungwa yenye ujazo wa lita moja pamoja na paketi moja la mboga mbichi mchanganyiko zilizofungashwa.
Akalipia akatoka nje jengo haraka. Alivyotoka tu akaona gari aina ya "Volvo S60" imejitenga peke yake akatambua ndio gari yake aliyoletewa kwa sababu alivyokuja pale hakuiona hiyo na ndio hiyo aliahidiwa na Komandoo JS. Haraka haraka akaenda kwenye lile gari alivyolikaribia tu gari hilo akashuka kijana mwenye umbile la miraba minne, kifua cha mataruma ya reli, kavaa fulana nyeupe amevaa miwani.
Wakasalimiana kwa bashasha, kisha kijana yule akajitambulisha kwa Kachero Manu. Kisha akakabidhiwa kila kitu na yule kijana wa Komandoo Jacob Steven wakaagana. Akaingia ndani ya gari akaanza kuikagua, akaipenda sana ilikuwa ni gari toleo la kisasa na inakwenda mpaka mwendokasi wa 230km/hr kitu ambacho Volvo nyingi za zamani zilikuwa hazifikii mwendokasi huo.
Uzuri wake ni kuwa adui yako ni rahisi kukupuuza anapokukimbiza kama haijui vizuri "Volvo S60" ambayo ina silinda nne na nguvu ya "450hp". Akaweka vizuri vitu vyake kwenye gari akaiwasha gari akaanza kuelekea mtaa wa Ruvuma nyumba namba 23B nyumbani kwa Mzee Masebbo lakini hakujui.
Gari ilikuwa imejazwa mafuta ya kutosha akaenda mpaka karibu na mwisho wa mtaa wa "Bakery padaria" akakutana na mataa akayavuka mataa na kusimamisha gari pembeni ya kijana ambaye ana kibanda cha kuuza vocha za simu na vifaa vya simu.
Akashuka kwenye gari akamsalimia kwa nidhamu "habari yako kijana, samahani nataka kwenda mtaa wa Ruvuma ila sipafahamu naomba unielekeze" alisema Kachero Manu huku anachezesha funguo za gari mkononi.
"Ahaaa..... bila samahani kaka yangu sio mbali sana kutokea hapa tulipo. Unaona ile Hoteli kwenye lile jengo refu rangi nyeupe mbele yako?sasa ile Hoteli inaitwa "Complexo Hoteleira". Ukifika pale kata barabara ya pili yake kulia kwako, ni barabara ya vumbi ndio mtaa huo huo unaotakiwa kwenda" alielekeza kijana yule kwa uchangamfu mkubwa huku akitumia mpaka na ishara ya vidole.
"Ahsante sana, kazi njema" alishukuru kisha akapanda ndani ya gari yake akawasha akaanza kuelekea mtaa wa Ruvuma nyumba namba 23B kwa mwendokasi wa wastani.


Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO DELGADO-PART-12

Mtaa wa Ruvuma ulikuwa ni mtaa wa watu wa kipato cha kati, na inasemekana baadhi ya wapigania Uhuru wa Msumbiji waliokwenda Msumbiji wakitokea nchini Tanzania kusaidia vita vya ukombozi baadhi yao waliishi mtaa huu na familia zao za wanawake raia wa Msumbiji.
Hivyo waliupa jina hilo la utani ili wajihisi kama bado wapo nyumbani Tanzania. Nyumba namba 23B ilikuwa ipo upande wa kushoto wa njia aliyoingilia Kachero Manu, ilikuwa imezungukwa na fensi ya michongoma mirefu iliyokosa matunzo kutokana na ukosefu wa kumwagiliwa maji ya kutosha.
Kachero Manu aliwasili nyumbani kwa Mzee Masebbo saa kumi kasorobo alasiri. Alipofika akagesha gari yake mwishoni kabisa mwa fensi. Mgeni yoyote asingefahamu kama anakusudia kuingia nyumbani kwa Mzee Masebbo kwa jinsi gari lililovyoegeshwa kijanja. Kisha akashuka nje ya gari, akajongea taratibu mpaka akaifikia baraza ya simenti iliyojaa vumbi zito linalotokana na kukosa kupigwa deki kwa siku kadhaa.
Ilikuwa ni nyumba ambayo mazingira yake ya nje kwa ujumla yalikuwa mchafukoge. Hapo Kachero Manu akatambua nyumba hii haina mwanamke ndani, fikra zake zikimtuma labda Mzee Masebbo hajaoa, au ni mgane au mkewe kasafiri, vinginevyo baraza isingekuwa chafu kiasi hicho cha kutisha. Alipofika mlangoni tu akagonga hodi. Kimya kikatawala bila kujibiwa kitu.
Akagonga tena zaidi ya mara tatu, lakini ukimya ukatawala, bila kujibiwa. Kachero Manu akataka kurudi kwenye gari amfanyie subira kidogo huenda ametoka nyumbani na mbaya zaidi hakumpa namba yake ya simu huenda angemtafuta. Ghafla alipoangalia chini ya mlango aliposimama akapatwa na mshtuko asioutegemea.
Alipatwa na wasiwasi juu ya usalama wa dereva Masebbo baada ya kuona kuna damu imechuruzikia mpaka mlangoni pale aliposimama. Akapigwa na taharuki kubwa, kwa sekunde kadhaa asijue la kufanya. Akafanya maamuzi ya kuingia ndani liwalo na liwe, akajaribu kushika kitasa cha mlango kikakubali kufunguka akazidi kustaajabisha, akaingia ndani.
Alichokiona ndani kwa macho yake hakuamini, alijiona kama yupo ndotoni vile. Alimkuta Mzee Masebbo, rafiki yake waliyejuana masaa machache yaliyopita amelala kifudifudi huku ametumbua macho juu ishara ya kwamba amepoteza uhai wake. Hapo hapo akachomoa bastola yake toka kiunoni mwake akaishika mkononi huku anaisogelea maiti ya Mzee Masebbo kwa tahadhari kubwa.
Alipoifikia ile maiti, akatoa kinga mpira "gloves" mfukoni mwake akazivaa mikononi kisha akaanza kuikagua ile maiti. Damu yake akakuta bado ina ubichi ubichi kwa mbali, kuonyesha mauaji hayajafanyika muda mrefu sana. Akaanza kujilaumu kuchelewa kwake kuja kumuona Mzee Masebbo ndio kumesababisha kifo chake.
Akawa anajiambia kimoyomoyo kuwa huenda angeharakisha kuja huku kabla hajaenda "Internet-Cafe" angeweza kuokoa uhai wake. Alipoliangalia jeraha ilipoingilia risasi akaona alama ya nyota akatambua kuwa mpigaji alipiga kwa ukaribu zaidi, na kwa kuwa kapiga risasi ya kichwani akatambua mpigaji sio mzoefu katika fani.
Maana walifundishwa kwenye kozi ya ulengaji shabaha ukitaka kumpoteza mtu maisha kwa haraka mpige risasi ya kwenye moyo au unatengeneza shabaha ya pembe tatu kutoka kwenye usawa wa pua na pembe ya mdomo, ili risasi ikaharibu neva za uti wa mgongo "spinal cord".
Akawa anajiuliza "kwanini kauliwa kinyama Mzee Masebbo? kosa lake hasa ni nini? labda wananitafuta wamenikosa wameamua kumfuata Mzee wa watu awaelekeze nilipo na maadamu kashindwa kuwapa taarifa zangu wamemuua kikatili" akajikuta anashikwa na hasira zisizo kifani.
Akaamua ailaze chali maiti ya Mzee Masebbo kupunguza usambaaji wa damu sakafuni akawa anamvuta kwa tahadhari asijichafue damu. Alivyomsogeza kidogo tu akaona kitambulisho cha kazi kwa pembeni kuna kikaratasi kimechomekwa.
Akakivuta kile kitambulisho alipokifungua kina jina la "James Penteleo" ni muajiriwa wa jeshi la polisi Msumbiji, na kikaratasi kidogo cheupe lakini kigumu kimeandikwa NAUTILUS HOTEL-"PEMOVACHA" saa 3:00 usiku.
Akachukua kitambulisho na kile kikaratasi akavisunda kwenye suruali yake ya kazi ambayo ina mifuko ya siri. Akaendelea na ukaguzi ndani ya nyumba ya Mzee Masebbo kutafuta kitu kitakachomsaidia kwenye upelelezi wake hakupata kitu chochote cha maana.
Wakati anajiandaa kutoka asije akakutwa ndani akasingiziwa yeye ndio aliyefanya mauaji, maana anayekutwa na ngozi ndio mwenye kesi. Alipofika mlangoni anajiandaa kushika kitasa cha mlango atoke nje akasikia mlio wa bodaboda kwa nje usawa wa mlango wa mzee Masebbo akachomoa bastola yake haraka haraka akasitisha zoezi la kutoka nje kisha akarudi ndani.
Akakimbilia kwenye sofa kubwa la ukumbini akajibanza pembeni mwake upande wa nyuma, anasubiria kama mtu huyo anakuja kwa Mzee Masebbo au ni mpita njia tu. Ghafla mlango ukafunguliwa kwa nguvu moja kwa moja, mtu aliyevaa suti na miwani nyeusi akaingia ndani. Kachero Manu mara moja akamtambua kuwa ni mmoja wa wale waliokuja kupekua chumba chake kule Nzuwa Lodge.
Akapata jibu la asilimia mia moja kuwa kifo cha Mzee Masebbo kina uhusiano wa moja kwa moja na msako wake yeye. Yule jamaa alivyoingia akaenda kwenye maiti ya Mzee Masebbo akaipindua pindua kama kuna kitu anakitafuta. Kwa jinsi alivyojawa na taharuki hakuwa hata na umakini wa kuangalia jinsi maiti walivyoiacha ipo kifudifudi na sasa ameikuta imelala chali, hivyo ilitakiwa awe na tahadhari.
Akaanza kuzunguka sebuleni kama mwendawazimu alipokuwa anatembea simu ya mkononi ya yule mtu ikaanza kuita. Akaipokea baada ya kuitoa mfukoni, akaanza kuongea huku anazunguka ukumbini pote pale.
"Hellow...! Kamanda Mark, kitambulisho changu cha kazi sikioni aisee na kile kikadi cha kuniruhusu kuingia kwenye chumba maalumu pale Nautilus Hotel nacho sijakiona, kijasho kinanitoka hapa nilipo maana bila kadi siwezi kuruhusiwa..! ". Akawa amefika karibu na usawa wa sofa ambalo amejificha Kachero Manu.
"Nyanyua mikono yako juu na tupa simu yako chini, usijaribu kuleta ujanja wowote...!" alitoa sauti ya amri Kachero Manu isiyo na chembe ya masihara. Yule jamaa alipatwa na mshtuko kama amepewa taarifa ya msiba wa mtu wake wa karibu, hakutegemea kama kulikuwa na mtu mle ndani, hapo hapo akatii amri na kunyoosha mikono juu huku akiitupa simu yake kwenye sofa.
"Haya geuka nyuma kisha anza kwenda mbele" alitoa maelekezo Kachero Manu. Hilo lilikuwa ni kosa kubwa, kwani alipogeuka yule jamaa alirukia sofa lililopo mbele yake kisha akajigeuza juu kwa juu utasema mtoto wa marehemu 'Bruce Lee' kisha akaachia teke moja matata sana lililotua sawia kwenye mkono wa kushoto wa Kachero Manu.
Mkono ambao ulikuwa umeshikilia bastola yake na kusababisha bastola kudondokea pembeni mwa sofa. Kachero Manu hakutaka kumkawiza, akajongea pembeni kidogo, akamuona anakuja kwa kasi kama mbogo ili amvamie, alichofanya Kachero ni kumkwepa kisha akamtega kwa mguu akaanguka kifudifudi hapo hapo hakumchelewesha akamrukia kwa kabali ya miguu, ikawa baradhuli yule anafurukuta lakini hawezi kutoka, mpaka pumzi zake za uhai zikaanza kukata zikawa zinapita kwa shida.
Kachero Manu akamuachia kidogo kisha akachomoa kisu kidogo cha kukunja akamuwekea shingoni. Akaanza kumfanyia mahojiano, "kwanini mmemuua Mzee Masebbo bila kosa lolote mbwa nyie? na nani amewatuma?". Kabla hajaanza kujibu akaanza kumkata ngozi laini ya kwenye koo ili kumtia uoga aropoke kila kitu, lakini yule jamaa akaonyesha haogopi, akajibu "siwezi kukujibu chochote, fanya utakacho mbwa mwenyewe...! ".
Kachero Manu akajua hana muda wa kupoteza akamshika mikono yake huku goti amelikandamiza kwenye shingo ya mwanaharamu yule, akaivuta mikono kwa kasi kuelekea mgongoni kwa kasi mpaka akategua viungo vya mabegani.
Jimmy akagugumia kwa maumivu makali, haraka haraka Kachero Manu akachomoa kichupa kidogo cha dawa mfukoni mwake na sindano ndogo. Kichupa cha dawa kimeandikwa "PENTOTHAL" akavuta dawa kwenye sindano akamdunga nayo mwilini. PENTOTHAL ni dawa ambayo ukidungwa inakufanya uongee ukweli tupu huwezi kuficha kitu. Ukiulizwa hata idadi na majina ya michepuko yako unaotaka bila hofu hata mbele ya mkeo.
"Jina lako ni nani?" aliuliza Kachero Manu ili kupata uhakika kile kitambulisho kama ni kweli cha jeshi la polisi. Akajibu "naitwa "James Penteleo" alijibu. "Kwanini wewe ni polisi lakini unashirikiana na wahalifu"? aliulizwa huku akirekodi mahojiano hayo kwa kutumia kalamu yake maalumu.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA:CABO DELGADO-PART 13

Kachero Manu akajua hana muda wa kupoteza akamshika mikono yake huku goti amelikandamiza kwenye shingo ya mwanaharamu yule, akaivuta mikono kwa kasi kuelekea mgongoni kwa kasi mpaka akategua viungo vya mabegani.
Jimmy akagugumia kwa maumivu makali, haraka haraka Kachero Manu akachomoa kichupa kidogo cha dawa mfukoni mwake na sindano ndogo. Kichupa cha dawa kimeandikwa "PENTOTHAL" akavuta dawa kwenye sindano akamdunga nayo mwilini. PENTOTHAL ni dawa ambayo ukidungwa inakufanya uongee ukweli tupu huwezi kuficha kitu. Ukiulizwa hata idadi na majina ya michepuko yako unaotaka bila hofu hata mbele ya mkeo.
"Jina lako ni nani?" aliuliza Kachero Manu ili kupata uhakika kile kitambulisho kama ni kweli cha jeshi la polisi. Akajibu "naitwa "James Penteleo" alijibu. "Kwanini wewe ni polisi lakini unashirikiana na wahalifu"? aliulizwa huku akirekodi mahojiano hayo kwa kutumia kalamu yake maalumu.
"Mimi sijui chochote, ila yule mkuu wangu wa kazi Mark ndio anawajua hao wakubwa wanaotutuma akina ALF....... aaaah nakufw......a.. a..aaaa.." aligugumia Jimmy kwa maumivu makali ya risasi aliyopigwa usawa wa moyo kupitia dirishani.
Kachero Manu alijitupa pembeni kama samaki mkizi akachukua ile bastola yake iliyokuwa imedondokea pembeni ya sofa kisha akaharakisha kufungua mlango wa mbele. Akasikia muungurumo wa gari linaondoka kwa kasi ya ajabu linatimua vumbi katika barabara ya vumbi ya mtaa wa Ruvuma. Akaegesha mlango akatoa kijitabu kidogo mfukoni mwake akaangalia namba ya kutoa taarifa polisi akapiga 10111 kuwapa taarifa hiyo ya mauaji.
Akazima simu yake na kupanda gari huku akienda kujiandaa na usiku wa mapambano. Lakini akawa anatafakari "huyu ALF.. ni nani? mzee Masebbo kafariki na siri yake moyoni ya huyu ALF..., na huyu baradhuli Jimmy nae kafa na siri ya huyu ALF.., huyu ni nani na ana nguvu gani, mpaka ukitaka kumtaja tu jina lake huwezi kumalizia na Malaika mtoa roho anakujia ghafla kuchukua roho yako..!.. "Dawa yake inachemka, supu ya mbwa yanywewa ikiwa ya motomoto....", aliwaza kimoyomoyo huku anachochea mwendokasi wa gari lake anapasua mitaani.


SURA YA NANE
Mkutano wa siri Nautilus Hoteli
'Nautilus Hotel' ni moja ya Hoteli yenye hadhi ya nyota 5 iliyojengwa katika ufukwe wa bahari ya Wimbi katika wilaya ya Pemba. Pemba ndio Wilaya kubwa kuliko zote katika Wilaya za Jimbo la Cabo-Delgado nchini Msumbiji. Huu Mji kuanzia mwaka 1904 ulikuwa unaitwa kwa jina la "Porto-Amelia" kwa heshima ya Malkia wa Ureno. Baada ya uhuru wa Msumbiji mwaka 1975 ndio Mji huo ukaitwa Pemba.
Moja ya kivutio cha Mji wa Pemba ni uwepo wa wazawa halisi wa Mji huo ambao wametunza utamaduni wao mpaka leo. Makabila wazawa wa Pemba ni Wamakonde, Wamakuwa na Wamwani. Ni jambo la kawaida kukutana na mwanamke wa Kimakonde amejichora tatoo mwilini, amejipaka rangi nyeupe usoni au kukutana na ngoma za asili zinazoitwa "Mapico" au kukutana na watu wanachonga vinyago.
Vitu ambavyo vilikuwa vinawavutia watalii kutoka pande mbalimbali za Ulaya kumiminika Wilayani Pemba. Kuifikia Hoteli ya Nautilus kutokea uwanja wa ndege wa Pemba ni kilometa zisizopungua 3. Hivyo ingekuchukua robo saa kwa mwendo wa wastani. Ilikuwa ni Hoteli ya kisasa yenye vyumba vya kulala zaidi ya 21 na kumbi mbalimbali za mikutano zisizopungua 7.
Kila chumba cha kulala kilikuwa kimeunganishwa na waya wa DSTV, runinga ya kisasa za inchi 32, waya wa mawasiliano ya kieletroniki na kipoza hewa. Pia vyumba vilikuwa vimenakshiwa vinyago vya urembo wa asili wa tamaduni za Kimakonde. Kulikuwa na mabwawa makubwa ya kuogelea, vyumba vya kisasa vya mazoezi 'Gym', Mkahawa wa kulia chakula pamoja na Baa.
Kwa uzuri wake tu ni moja ya fahari za Mji wa Pemba, ambayo kila mwananchi wa Pemba alikuwa anajivunia nayo.
Kampuni ya "Monte Branco Ltd" iliukodisha ukumbi 'Na. 03' wa mikutano katika Hoteli hiyo kwa muda wa siku 2. Wakaulipia kwa muda wa Juma zima huku wakiwa hawataki Mfanyakazi yoyote wa Hoteli hiyo kusogelea ukumbi huo. Kila kitu walijiandaa kivyao, kuanzia vyakula na vinywaji vyao. Waliweka walinzi wao na kufunga mitambo yao ya kuzuia udukuzi wa kikao chao cha siri kinachotegemea kufanyika saa saa 3:00 usiku.
Ilikuwa kuanzia meta 100 kutoka ukumbi wa mkutano kuna walinzi wao wenye vifaa vya kisasa. Asiyehusika na kikao kile kufanikiwa kuwapenya walinzi wale mpaka uingie kwenye chumba cha mkutano ilikuwa ni sawa na muujiza wa ngamia kupita kwenye tundu la sindano. Mkutano huo ulihusisha Wakurugenzi Wakuu wa Kampuni ya Monte Branco Ltd, Inspekta Jenerali Mark Noble na baadhi ya vijana wake na baadhi ya Vigogo wa serikali ya Msumbiji wasio waaminifu ambao ni washirika wao.
Kulikuwa kunapangwa mikakati ya kufanikisha dili haramu lenye pesa ndefu la ujenzi wa barabara unaogharamiwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika 'ADB'. Kama ujuavyo Alfredo na Mafioso wenzake walikuwa wapo kwenye harakati za kujinufaisha kiuchumi kwenye dili lolote lile lenye pesa.
Usiri mkubwa ulihitajika sana kutokana na maamuzi yatakayopitishwa na kikao hicho. Maamuzi ambayo yangeweza kugharimu maisha ya baadhi ya vigogo wanaokwamisha kufanikiwa kwa dili hilo haramu. Mkutano huo pia ulikuwa upitie taarifa ya udhibiti wa wahamiaji toka Tanzania, na ripoti ya uchimbaji wa madini ya rubi katika machimbo yaliyopo Jimboni Cabo-Delgado. Kilikuwa ni kikao ambacho moto mkali wa majadiliano ulitegemewa kuwaka.

Kachero Manu atinga mkutanoni kwa teknolojia
Alivyotoka nyumbani kwa Marehemu Mzee Masebbo kule mtaa wa Ruvuma, moja kwa moja aliekea kwenye nyumba yake aliyotafutiwa ya kupanga. Aliwasili nyumbani hapo muda wa saa 10:45 alasiri, alipofika akazunguka mazingira yote ya nyumba kujiridhisha na usalama wake.
Kisha akaanza kuhisi njaa akakumbuka alinunua mkate, juisi ya matunda chupa bonge na saladi alivyovihifadhi ndani ya gari. Akala mkate alioununua kisha akashushia na juisi. Baada ya hapo akafanya maamuzi ya kujinyoosha usingizi wa muda mchache, tayari kwa safari ifikapo saa 12 magharibi kuelekea mji wa Pemba.
Kabla hajalala aliingia kwenye mtandao wa simu yake ya kiganjani kuitafuta ilipo "NAUTILUS HOTEL" kupitia wavuti wa "Google Map". Akapata majibu ni hoteli ya kitalii ipo wilaya ya Pemba, umbali wa kilometa takribani 185 kutoka mji alipo wa Montepuez.
Akajiapiza lazima aende akafahamu kuna mafungamano gani yaliyojificha kati ya wale mabaradhuli waliofanya mauaji ya Mzee Masebbo na mkutano huo. Na pia hilo neno "PEMOVACHA" kwenye kikaratasi cha marehemu Jimmy alikuwa anataka kufahamu undani wake. "Majibu nitayapata Nautilus hoteli sina haja ya kuumiza kichwa", alijiambia mwenyewe kimoyomoyo Kachero Manu.
Ilipofika saa 11:45 alasiri alikuwa tayari ameshajiandaa kwa ajili ya safari hiyo. Hivyo akapitia kituo cha mafuta cha jirani na alipo akajaza mafuta yaliyojaa tenki. Akang'oa nanga kuelekea Pemba akiwa ndani ya gari alilokodi la 'Volvo s60' toleo jipya la mwaka 2012. Ilikuwa ni safari ya umbali kama wa Dar es Salaam kwenda Morogoro ukifananisha kwa hapa kwetu Tanzania. Ni safari ambayo kwa mwendo wa kawaida ilitakiwa atumie saa 4. Hivyo anavyotoka hiyo saa 12 itambidi aingie saa 4 usiku nyuma ya muda wa mkutano anaotaka kuhudhuria kwa lisaa limoja.
Akaamua aende kwa mwendo wa kasi huku akiomba Mungu asipate ajali yoyote au kukamatwa na askari usalama barabarani. Mipango yake ilifanikiwa mpaka saa 1:15 usiku mbichi alikuwa tayari kashafika katika kijiji cha Metoro umbali ambo ni nusu ya safari. Alisimama kukagua gari na kuchimba dawa kidogo ili kukipa ahueni kibofu chake cha mkojo.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA:CABO DELGADO-PART 14


Akaamua aende kwa mwendo wa kasi huku akiomba Mungu asipate ajali yoyote au kukamatwa na askari usalama barabarani. Mipango yake ilifanikiwa mpaka saa 1:15 usiku mbichi alikuwa tayari kashafika katika kijiji cha Metoro umbali ambo ni nusu ya safari. Alisimama kukagua gari na kuchimba dawa kidogo ili kukipa ahueni kibofu chake cha mkojo.
Aliondoka Metoro saa 1:25 usiku huku mvua ya mkaragazo ikinyesha kwa kishindo, lakini hakuijali sana. Malengo yake yalikuwa afike saa 2:45 usiku. Kwa mwendokasi aliokuwa anaenda nao utadhania ni mshindani wa mashindano ya mbio za magari za "Dacar Rally", mbio ambazo ni za hatari sana na hutokea mara nyingi baadhi ya madereva kupoteza uhai. Mashindano hayo ya "Dacar Rally" huanzia Jijini Paris, Ufaransa mpaka kuishia Jijini Dakar, Senegali.
Alipofika kitongoji cha Nanlia bado kama kijiji kimoja afike Pemba kutokana na utelezi wa barabara uliosababisha na mvua kali aliwakosa kosa kuwagonga kundi kubwa la ng'ombe waliokuwa wanaswagwa kurudisha nyumbani, akanusurika na ajali mbaya sana. Alipofika kijiji cha Murrebu akapata pancha ya tairi lake, hapo sasa safari ikabidi isimame kwa muda.
Ilikuwa ni muda wa saa 2:25 usiku. Bahati nzuri kulikuwa na tairi la akiba akabadililisha haraka haraka tairi lenye pancha na kuendelea na safari yake. Mpaka kufika majira ya 3:05 usiku ndio alikuwa anapaki gari lake kwenye maegesho ya magari ya Nantilius Hoteli tayari kashaingia kwenye himaya ya mabaradhuli wake anaopambana nao.
Akashuka akajikagua vitu vya kazi alivyonavyo kuanzia bastola yake kibindoni ndani wa suruali yake ya dangirizi, pia kuna bisibisi, mkasi, mkungu wa funguo bandia na koleo. Akaenda mapokezi pale Hotelini akawa anazuga kuulizia bei ya vyumba na gharama mbalimbali za vyakula na gharama za kukodi ukumbi wa mikutano huku anasoma ramani nzima ya jengo la Hoteli iliyowekwa pale mapokezi.
Alipoielewa ramani vizuri akaomba aelekezwe chooni. "Tembea na hii veranda kisha utakata kushoto utakutana na vyoo vya wanaume" alielekeza mhudumu wa Hoteli kwa sura ya bashasha, akijua ni mmoja wa wateja wao wapya bila kuelewa mipango ya Kachero Manu, kuwa yupo kazini wala hana haja na chumba wala chochote. "Ahsante sana, ngoja niwahi kwanza maliwatoni" alisema Kachero Manu huku akaondoka kwa mwendo wa haraka.
Alipofika usawa wa maliwato, kulia kwake kulikuwa na lifti inayokupeleka mpaka roshani ya 3 ambapo ndio kuna vyumba maalumu vya mikutano. Akaita lifti ilivyokuja akapanda haraka akabonyeza kitufe cha kuifanya isimame ghorofa ya 3. Bahati nzuri alikuwa yupo peke yake ndani ya lifti ile akashukuru Mungu, bahati bado ipo upande wake.
Aliposhuka tu akaipa ubavu wa kushoto lifti aliyoshukia kisha akatembea kuelekea mbele kwa mwendo wa kunyatia kwenda kwenye chumba cha kudhibiti umeme wa jengo zima la Hoteli. Alipofika akakuta chumba hicho, kimefungwa. Akatoa mkungu wa funguo malaya toka mfukoni mwake, akaingiza funguo moja wapo, kisha akaitekenya kufuli kidogo tu ikafunguka.
Bila kufanya ajizi akaufungua mlango kisha akaingia zake bila kusahau kuurudishia mlango wa chumba hiko. Humo ndipo akaanza vimbwanga vyake tatanishi. Akafungua mfumo wa kukata umeme kwa kutumia bisibisi yake akaunganisha waya wa "earth" na "neutral" kwa pamoja hapo hapo umeme wa jengo zima la hoteli ukazimika kwa kupiga shoti ya kubutuka kwa kishindo kikubwa.
Giza totoro likatawala ndani ya jengo zima la hoteli. Akatabasamu kuwa mbinu yake namba moja imetimia, akatoka nje ya chumba akafunga kufuli na kurudi kujibana kwenye ukuta wa pembeni unaotenganisha chumba cha kudhibiti mfumo wa umeme na stoo ndogo ya kutunzia vifaa vya usafi, sehemu ambayo sio rahisi kwa anaekuja kumuona.
Alijua tu lazima fundi umeme wa hoteli atakuja kwenye chumba cha mfumo wa umeme kuja kuangalia chanzo cha tatizo, akawa anamsubiria afike. Akaangalia saa yake ikawa inasoma ni saa 3:30 usiku. Akajipa matumaini kuwa kikao hakijaanza na kama kimeanza basi kwa kuchelewa kama Waafrika ilivyo tabia yetu hatuwezi kuchunga muda. Mungu si athumani hazikupita hata dakika 5 akasikia lifti inagota ghorofa ya 3.
Akaombea awe ni fundi umeme ndio anayekuja na hiyo lifti. Kweli bana lifti ilivyofunguka akashuka kijana wa makamo ana mwili wa wastani amebeba sanduku lake la vifaa vya ufundi alivyoshuka tu na tochi yake akawa anaelekea upande wa chumba cha kudhibiti mfumo wa umeme. Akamsubiria afike mpaka aufikie mlango huo ndio amfungie kazi. Alipofungua tu mlango na kuingia kwenye chumba, fundi hakuubugaza mlango aliuacha wazi. Kachero akamfuata taratibu kwa mwendo wa kunyatia bila kumshtua.
Alipomfikia akamgusa begani, ile kugeuka tu akampiga kareti moja matata sana ya shingoni, fundi umeme akaanguka chini pale pale kama gogo la mti. Akamvuta pembeni ya chumba akajua atakuwa amezimia atakuja kuzinduka masaa mawili mbele. Haraka haraka akamvua nguo yake ya kazi, bwelasuti rangi buluu. Nguo maalumu wanayovaa mafundi yenye nembo ya jina la Hoteli akavaa yeye Kachero ikamkaa vizuri kama vile fundi nguo alimpimisha yeye vipimo wakati wa kushona vazi lile.
Haraka haraka akatoka na lile sanduku la vifaa la fundi akaongoza mwendo kuelekea veranda ya upande wa vyumba vya mikutano, ambao ni kinyume na kile chumba alichotoka. Akakutana na walinzi kama watano walipomuona na vazi la fundi umeme wakaharakisha kumlaki, "fundi tatizo nini? kuna mkutano muhimu chumba namba tatu umeshindwa kuendelea kwa sababu ya umeme na tumelipia fedha sufufu ili tupate huduma za viwango", alisema mmoja wa walinzi akionyesha kukasirishwa na kitendo cha kukatika umeme ghafla.
"Poleni sana huenda katika moja ya soketi za chumba hicho cha mkutano ina shoti maana nimetoka kukagua chumba cha kudhibiti umeme wa jengo zima sasa hivi hamna tatizo lolote, na chumba cha mkutano pekee kinachotumika kwa sasa ni hiki namba 03" alijibu Kachero Manu kwa unyenyekevu mkubwa.
Akaruhusiwa kuingia chumba kile bila kizuizi wala kikwazo chochote. Alivyoingia tu, akakuta watu wamekaa kwa mtindo wa mduara huku mbele kuna projekta kubwa ya kuwasilishia mada iliyounganishwa na kompyuta. Kwa haraka haraka hakuweza kuwaona vizuri sana kutokana na mwanga hafifu wa taa za kuchaji iliyowashwa.
Akawa anazungukia kwenye soketi zote akazuga anazikagua kwa kutumia bisibisi "testa" kisha kwenye baadhi ya soketi akavisha kifaa kinachofanana na soketi lakini chenye kazi ya kudukua mawasiliano yoyote ya simu itakayochajiwa eneo hilo. Baada ya hapo akaenda kwenye meza ambayo kuna projekta ya kuwasilisha maelezo ukutani akaikagua kisha akatoka haraka nje ya chumba cha mkutano.
Akarudi katika chumba cha kudhibiti umeme, baada ya dakika tano tu umeme ukarudi kwenye jengo zima la hoteli. Akavua nguo za yule fundi, akaegesha mlango akatoka haraka haraka akaifikia lifti akaidandia na kushuka nayo mpaka sakafu ya chini.
Akapitiliza moja kwa moja mgahawani na kuagiza soda aina ya Coca-Cola baridi sana ya kopo. Akalipia na kurejea kwenye gari yake huku ameshika kinywaji chake mkononi anatabasamu, tabasamu la ushindi wa kishindo. Akajisifu kimoyomoyo ujanja mwingi na wa hali ya juu aliioutumia.


Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA-CABO DELGADO-PART 15
Dr.Muganyizi Lazima afe
"Dr.Fredrick Muganyizi" ni Mkurugenzi Mkuu, mwakilishi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kanda ya kusini mwa jangwa la Sahara. Alikuwa ni shaibu wa makamo mwenye umri usiopungua 55.
Ni Daktari wa Falsafa aliyebobea katika fani ya maendeleo vijijini "Rural Development" aliyehitimu katika Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA)-Morogoro. Mwanzoni alikuwa ni mhadhiri katika Chuo cha Mipango, Jijini Dodoma.
Mara tu alivyomaliza masomo yake ya Uzamivu akapata ajira Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) kama Meneja Miradi Kanda ya Afrika Magharibi kuanzia mwaka 2005-2013. Kabla ya mwaka 2014 kupandishwa Cheo na kuwa Mkurugenzi Mkuu mwakilishi kanda ya kusini mwa jangwa la Sahara na kituo chake cha kazi kipya kikawa ni nchini Botswana.
Miongoni mwa tabia za Dr.Muganyizi ni uwazi, uwajibikaji na ukweli. Tabia ambazo zilimtengenezea maadui wengi na kumpatia marafiki wachache. Hasa ukichukulia serikali nyingi za Afrika zilikuwa zinanuka rushwa na ufisadi.
Watendaji katika serikali za Kiafrika tabia zao wakipata nyadhifa nyeti za uteuzi kama Uwaziri au Ukurugenzi wa Shirika fulani basi wanapongezana na familia zao kuwa wameula maisha. Kwa Tanzania Ikaibuliwa misamiati mitaani ya kurathimisha ufisadi wao, ikawa yakipita mitaani magari yenye namba za shirika la umma (SU) wao wakatafsiri maana yake ni "SOMA ULE".
Na ikiwa kiongozi kapata madaraka na hataki kupokea rushwa wala kutengeneza mirija ya ufisadi atapachikwa maneno ya kebehi kama anajifanya "Mnyerere", wakifananisha uzalendo wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Sasa Dr.Muganyizi alikuwa "Mnyerere" haswa, alikuwa hataki kutumia senti hata moja katika njia ya ubadhirifu.
Alikuwa hata akisafiri kikazi pesa za masurufu zote zinazobakia anazirudisha kwenye idara ya uhasibu. Tokea anafundisha Chuo Kikuu hakuwahi kufaulisha wanafunzi waliofeli, alikuwa tayari hata kama ni darasa zima wafeli mtihani wake lakini sio kuwapa alama za bure bure bila kutolea jasho.
Hii ilimfanya achukiwe na Wanachuo wasiopenda kujisomea walio wengi na apendwe na wanafunzi wachache wanaopenda kujituma kimasomo.
Siku aliyowaaga wanafunzi wake kuwa amepata kazi benki ya "ADB" baadhi ya wanachuo walifanya sherehe ya kufurahi kuondoka kwake. Walikesha usiku kucha wanacheza muziki na kunywa pombe kudhihirisha furaha yao ya kuondoka kwa mhadhiri wao mnoko.
Alivyokwenda Afrika Magharibi, moja ya miradi iliyompatia sifa ni ujenzi wa barabara ya juu kwa juu kuunganisha jiji la Dakar na mji wa Diamnadio. Mradi uliofadhiliwa na Benki ya Afrika kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Dakar, Senegal. Alisimamia kwa umakini na uaminifu mkubwa mchakato wote wa kumtafuta mkandarasi bila ufisadi wowote.
Kabla mradi hujaanza kutekelezwa akahamishwa baada ya kunusurika kupigwa risasi zaidi ya mara mbili kutoka kwa majambazi waliotumwa na wakandarasi waliozoea kupata tenda kifisadi. Akahamishiwa kusini mwa jangwa la Sahara sasa akiwa kama Mkurugenzi na ofisi yake ikiwa Jijini Gaborone, Botswana.
Toka mwaka 2015 alikuwa anasafiri mara kwa mara kutoka Gaborone kuja Pemba, Msumbiji kwa ajili ya ujenzi wa barabara na bandari. Barabara ambayo itaunganisha miji ya Pemba, Montapuez, Vanduzi na Changare kwa kifupi "PEMOVACHA-PROJECT".
Ni mradi ambao asilimia tisini (90%) ya pesa zingetolewa na Benki ya Afrika (ADB) na asilimia kumi (10%) ya pesa zingetolewa na serikali ya Msumbiji kutoka kwenye makusanyo yake ya mapato ya ndani. Ulikuwa ni mradi wenye lengo la kuboresha miundombinu iliyoharibiwa wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe kati ya serikali ya FRELIMO na waasi wa RENAMO.
Kutokana na umuhimu wa mradi na gharama za ujenzi kuwa kubwa ilibidi umakini mkubwa uhitajike hivyo Dr. Muganyizi akaamua kuhamishia makazi yake katika Mji mkuu wa Cabo-Delgrado, Pemba, ili kusimamia mchakato wa ujenzi kwa umakini na ukaribu zaidi.
Huo ukaribu katika ufuatiliaji akagundua madudu makubwa ya ufisadi yanayotaka kufanyika na watendaji wa serikali ya Msumbiji ambao sio waaminifu, wa kutaka kuipa tenda ya utengenezaji barabara hiyo kampuni ya "Monte Branco Ltd" ambayo haijawahi hata kutengeneza barabara sehemu yoyote ile Msumbiji.
Dr.Muganyizi akawa anakataa kuidhinisha kampuni hiyo ipewe tenda hiyo, msimamo uliomtia matatizoni, mpaka kuwekwa kwenye orodha ya wanaotakiwa kuonja kifo kutoka kwa Mafioso wa Alfredo.

Mkutano uliokuwa unatakiwa kufanyika kuanzia saa tatu chumba namba 03 pale Nautilus Hoteli ulichelewa kuanza kwa sababu mbili.
Kwanza ilikuwa ni kukatika kwa umeme kwa ghafla kusikotarajiwa, lakini jambo la pili ilikuwa ni taarifa ya mauaji ya James Penteleo mwana usalama ambaye alikuwa kwenye kikosi cha kudhibiti wimbi la wahamiaji kutoka Tanzania, ambaye alipewa jukumu la kuondosha uhai wa dereva Masebbo.
Taarifa hiyo ya mauaji toka kwa Inspekta Jenerali Mark Noble ilileta mshtuko na taharuki kubwa kwa vigogo hao. Hawakutegemea kama kuna mtu anayejipenda na kuuthamini uhai wake anaweza kujaribu kutia mkono wake kwenye mzinga wao wa nyuki, Mafioso uliojaa asali inayolindwa na nyuki wakali wanaokula maua ya bangi.
Ilipofika saa 4:00 usiku baada ya majadiliano ya hapa na pale ndipo kikao ndio kikao hicho kikaanza kwa kufunguliwa rasmi.
"Ndugu wajumbe wa kamati ya siri ya "Monte Branco Ltd" na washirika wetu waalikwa, tumeitana usiku huu kujadili mchakato wa utekelezaji wa ajenda zetu za kikao kilichopita. Ajenda ya kwanza ni kupokea ripoti ya utekelezaji wa zoezi la kuwafukuza Watanzania nchi Msumbiji hasa maeneo ya machimbo ya madini ya Montepuez na kuhakikisha biashara na njia zote kubwa za kiuchumi zinakuwa chini ya kampuni yetu ya "Monte Branco Ltd". Ripoti hii itawasilishwa na Inspekta Jenerali Mark Noble karibu sana....!", alimaliza kuzungumza mwakilishi wa mmiliki wa kampuni akimuwakilisha Bosi mkubwa Alfredo kwenye kikao hicho.
Muwakilishi huyo aliyekuwa amevalia kaunda suti ya kijivu akazima maiki yake na kukaa chini ya kiti chake. Inspekta Jenerali Mark, aliandaa hotuba yake kwa mtindo wa kugotoa bila kurefusha mazungumzo yasiyo na msingi asije kuwachosha vigogo wenzake ambao hawana muda wa kusikiliza porojo.
"Waheshimiwa wajumbe wenzangu kwa heshima na taadhima napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa kupewa nafasi hii ya kuwasilisha taarifa ya kitengo changu nyeti. Kwa ufupi zoezi limefanikiwa kwa zaidi ya asilimia tisini (90%), tumefanikiwa kuwafurusha Watanzania walio wengi waliohajiri nchini kwetu kutoka Tanzania na tumedhibiti uingiaji wao nchi Msumbiji hasa maeneo yetu ya kujidai ya Montepuez kupitia mipakani. Na propaganda tunazozisambaza katika vyombo vya habari, ni kuwa tunawaondosha wahamiaji haramu wa mataifa yote sio Tanzania pekee, ambao wanaishi bila kibali cha ukaazi nchini Msumbiji". Akapumzika kuongea Bwana Mark kwa muda akameza mate kisha akaendelea.
"Lakini leo asubuhi saa moja tulipokea taarifa za kiintelijinsia za uingiaji wa mtu anayedhaniwa ni Kachero kutoka Tanzania kupitia njia ya daraja la umoja la Mtambaswala linalounganisha Tanzania na Msumbiji. Hasa tulivyowakamata na kuwaua wale wapelelezi sita toka mkoa wa Mtwara tulitegemea lazima atatumwa mtu toka Tanzania kuja kutuchunguza. Tulipotaka ripoti kwa askari wetu wa ukaguzi mipakani ambao ni sehemu ya mfumo wetu, tukakuta amewaua askari wetu 6 wa mpakani.
Pia tukapata penyenye zake muhimu toka kwa kidinga popo mmoja. Ndipo kumfuatilia mpaka kwenye vituo vya taksi vya Mji wote wa Montepuez. Kwa bahati nzuri mpaka kufikia muda wa saa 6:30 mchana tukafanikiwa kuelekezwa alipo huyo mtu kuwa anaweza kuwa amefikia Nzuwa Lodge. Tulipofika hapo tulipojitambulisha ni Maafisa Usalama tukakagua Kompyuta ya kujifadhia kanzi ya wageni lakini hakuweka taarifa zake na alikuwa ametoka.
Wanasema aliwaambia amechoka ataandika baadae, lakini yote ni janja janja yake tu. Tulipoingia chumbani kwake hakuwepo tukafanya ukaguzi wetu hatukupata lolote la kutusaidia zaidi ya kukuta mavazi yake ya kanzu na tasbihi, na begi lake lenye vitu vingine kabisa. Hivyo tukaenda nyumbani kwa dereva aliyesaidia kumuingiza Msumbiji kwa mficho huku tukiwa nia ya kurudi kumsaka tena Nzuwa Lodge.
Huko nyumbani kwa dereva ndipo tulipojua kuwa huyu mtu ni hatari sana, alifanikiwa kumdhibiti mwanausalama mwenzangu Jimmy, inaonyesha alikuwa anafuatilia nyendo zetu na mpaka ripoti za sasa hivi kwa watu wetu tuliowaacha Nzuwa lodge wanasema hajarudi mpaka sasa hivi na kahamisha vitu vyake vyote ingawa chumba alikilipia. Hivyo namalizia kwa kusema tayari Tanzania wamejibu mapigo kwa kuleta mtu wao kuja kutuchunguza na mpaka sasa vijana wangu wa kazi 7 ameshawapeleka jongomeo. Tusipokuwa makini nae tutaumbuka, Tanzania wakitaka jambo lao huwa hawashindwi, ahsante sana ndugu wajumbe". Alimalizia Inspekta Jenerali Mark hotuba yake iliyowasilishwa kiufasaha na weledi mkubwa.
Ukumbi mzima ulizizima kwa hofu na uwoga kama vile wamemwagiwa maji ya baridi. Kipindi chote cha uwasilishaji wa ripoti hizi, Kachero Manu alikuwa ndani ya gari lake "Volvo s60" gari la kipelelezi lililofungwa vifaa vya kisasa vya kudaka sauti kutoka kwenye ukumbi wa mkutano. Hivyo kila kitu kinachozungumzwa anakisikia, na anakirekodi.
Walichokuwa hawafahamu ni kuwa yule fundi umeme wa Nantilius hoteli, aliyeingia kwenye chumba cha mkutano kurekebisha hitilafu pindi ulipokatika umeme alikuwa ni Kachero Manu na alifanikiwa kufunga vifaa vya kunasa sauti kutoka kwenye ukumbi namba 03 wa mkutano.
Pia simu za baadhi ya vigogo zilizokuwa zinachajiwa ukumbini mule zote zilikuwa zinadukuliwa na Kachero Manu bila wao wenyewe kujua. Kila mmoja mule ndani akawafahamu kwa majina yao na magari waliyokuja nayo usiku ule kwenye mkutano ule.
Akawa yupo ndani ya gari anasikiliza mazungumzo yao kwa kutumia kifaa kinaitwa "personal sound amplifier" ni vifaa vinavyotumiwa sana na Makachero wanapopeana taarifa wakiwa umbali mrefu, hasa wakiwa kwenye misafara ya viongozi wa kitaifa. Ilipofika zamu ya kuwasilishwa ripoti ya udhibiti wa kitengo cha madini, gesi na mafuta, ndio moja ya ripoti iliyompa mshtuko mkubwa Kachero Manu.
Hapo iliwasilishwa ripoti kuonyesha nchini Msumbiji imegundulika gesi mapipa bilioni 20 katika pwani yake inayopakana na Tanzania. Mapipa ambayo yataingiza pesa dola za kimarekani bilioni 39, na zitaweza kuikwamua Msumbiji kutoka kuwa miongoni mwa nchi ya 7 kwa umaskini duniani.
Kilichomshangaza Kachero Manu ni mikakati ya kampuni ya "Monte Branco Ltd" kuhujumu uchimbaji wa gesi Tanzania, ili kuwafukuza wawekezaji kwenye sekta ya gesi Tanzania. Mikakati ilikuwa ni kutumia sintofahamu ya kizungumkuti cha watu wa mkoa wa Mtwara Tanzania kuzuia gesi isisafirishwe mpaka Dar es salaam mpaka watakapopewa ithibati ya namna watakavyonufaika na gesi inayochimbwa mkoani kwao.
Kumbe "Monte Branco Ltd" walipandikiza mamluki wao watakaohamasisha raia wa kawaida wafanye fujo ili kuwatia khofu wawekezaji waone Tanzania sio sehemu salama kwa uwekezaji. Pia kwenye vigogo wa serikali ya Tanzania wanaohusika na gesi kuhujumu kwa kuweka kodi zisizo na kichwa wala miguu, sera mbovu za uwekezaji na masharti magumu kwa wawekezaji ili wakimbie Tanzania. Kisha wao "Monte Branco Ltd" watakapodhibiti biashara ya gesi na mafuta nchini Msumbiji wauze kwa bei ya kupaa bila ushindani kutoka Tanzania.
Hivyo maazimio ya kikao ilikuwa ni kumuita nchini Msumbiji Meneja Mkuu wa masuala ya gesi na mafuta wa Tanzania, Bwana Andenga Kazimoto, ambaye ni mamluki wa Bwana Alfredo kwa upande wa Tanzania ndani ya siku mbili zijazo. Ili akutanishwe na Bwana Alfredo ana kwa ana kutoa ripoti za siri na nyaraka nyeti za alipofikia katika mikakati yake ya hujuma.
Kachero Manu alivyosikia jina la Mkurugenzi Andenga Kazimoto linatajwa tu fikra zake zikarudi siku ya kwanza kuitwa Ofisini kwa Bosi wake Mathew Kilanga alivyomtilia mashaka Bwana Andenga Kazimoto kuwa sio mtu mzuri hata kidogo. Sasa leo alikuwa anakithibitisha kile kitu ambacho alikuwa anakidhania kuwa ni kweli. Kachero Manu alichukizwa sana na ulafi wa kiongozi huyu ambaye alikuwa ni mtu msharafu na mwenye heshima kubwa nchini Tanzania na kujitambulisha mbele ya jamii kuwa ni mchapakazi na mzalendo mwenye kuitakia mema nchi yake.
Hapo ndipo akafahamu kwanini alikuwa huyu Bwana Andenga alikuwa anapenda sana vyombo vya habari. Ilifika hatua hata sherehe ya kipaimara tu ya mjukuu wake basi ataita vyombo vya habari si chini ya vitatu ili mradi tu asikauke midomoni mwa Watanzania. Pia Bwana Andenga alikuwa na urafiki na uswahiba uliopitiliza na matajiri wapenda sifa jiji Dar es Salaam, jambo ambalo kimaadili ya uongozi ilikuwa haileti muruwa mzuri.
Akaamini msemo wa wahenga "Kikulacho kinguoni mwako", na "chema chajiuza kibaya chajitembeza". Akajisemea Kachero Manu nafsini mwake "kumbe Tanzania wapo viongozi na watendaji ambao ni wachapakazi wazuri tu lakini kwa kuwa hawapendi kuuza sura kwenye vyombo vya habari basi wanaonekana ni wavivu na mapoyoyo".
Kachero Manu akaendelea kuwaza baadhi ya viongozi wa serikali ambao ni mfano wa kuigwa. "Mfano katika Mkoa wa Simiyu, Mkuu wa Mkoa wake Bwana "Anthony Mtaka" ni mmoja wa watendaji bora kuwahi kutokea nchini Tanzania. Anapendwa kuanzia na watoto, wazee, vijana, akina mama na watumishi wa serikali katika mkoa wake lakini sio kiongozi mpenda kiki katika vyombo vya habari".
Ikafika zamu ya kuwasilisha ripoti ya tenda mbalimbali za serikali zilizopelekwa Monte Branco Ltd, ndipo jina la Dr.Muganyizi lilipotawala kikao. Ilielezwa kuwa mradi wa PEMOVACHA kwa upande wa serikalini umeshapita na hamna kikwazo chochote, ila tatizo lipo kwa mwakilishi wa Benki ya ADB Dr. Muganyizi huyu alionekana ni kikwazo maana inahitajika aweke saini yake tu pesa zitoke.
"Nakuamrisha wewe Inspekta Jenerali Mark Noble huyu mtu afuatwe nyumbani kwake usiku huu wa leo, ukitoka hapa tu uende nyumbani kwake utafute nyaraka ya siri ya "PEMOVACHA PROJECT" ambayo lazima umlazimishe aweke saini yake kwa mtutu wa bunduki ili benki iweze kutoa pesa na baada ya hapo auwawe ikifika asubuhi tuwe tunajiandaa kutuma rambirambi tu, hawezi kujifanya ana uchungu na pesa za msaada kwa wana Msumbiji kuliko sisi wazawa wenyewe huu ni muendeleo wa kiherehere cha Watanzania kujitia wana uchungu sana na nchi za wenzao, sasa wajiandae kupokea maiti ya msomi wao tegemeo pale uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere.
Taarifa tulizonazo toka kwa watu wetu wa ofisini kwake Dr. Muganyizi wanasema huwa nyaraka muhimu zote anapenda kutembea nazo huwa hana imani na mtu yoyote. Na huyo Kachero wao anayejiita Hassan ibn Hussein kama tulivyopata taarifa zake toka Nzuwa Lodge, asakwe na aletwe akiwa hai kwanza aonane na Bosi Alfredo ana kwa ana tujue ana kitu gani anakijua kuhusu sisi kisha nae auliwe. Tutaonana kesho kutwa tarehe 17/02/2016 kwa wale watu maalumu wanajua muda wa mkutano kwenye kiwanda cha kusindika korosho karibu na soko la Baraca," alimalizia mwakilishi wa Bwana Alfredo kwa kufunga kikao hicho saa sita kasoro dakika tano usiku, waalikwa wote wakatawanyika.
Mwenyewe Bwana Mkubwa Alfredo hakuhudhuria mkutano huo, kutokana na kutingwa na majukumu ya kikazi nje ya nchi. Pia ilikuwa ni tabia yake haonekani ovyo mbele za watu kuleta tabia ya kuogopwa katika mioyo yao.




Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA,: CABO DELGADO-PART 16

SURA YA TISA
Hali bado ni tete Jijini Dar es Salaam
Bosi Mathew Kilanga, Mkuu wa Idara ya Usalama nchini Tanzania, alikuwa hajapata usingizi wa starehe kwa siku ya tatu mfululizo tokea tarehe 14/02/2016 siku ambayo Kachero wake mtiifu Manu alipoaga kuwa anaelekea Cabo-Delgado, Msumbiji.
Alikuwa analala usingizi wa mang'amung'amu utasema kitanda chake kina kunguni kutokana na kuzongwa na mawazo juu ya kazi aliyomkabidhi kijana wake kachero Manu kama itakamilika kwa wakati aliompangia.
Kwa mtu ambaye ana umri zaidi ya miaka 70 kama yeye, ni mbaya sana kwa afya kukosa usingizi wa utulivu. Ingeweza kumpelekea kupata magonjwa kama ya mshtuko wa moyo na shinikizo la damu. Ukosefu huu wa usingizi haukuwa wa bure bali ulisababishwa na kutopata taarifa zozote za Kachero Manu tokea aondoke, sio arafa yake, wala barua ya pepe, wala simu.
Akajawa na hofu na wasiwasi wa jakamoyo, "je ni mzima Kachero Manu? au katekwa na maadui kauawa na yeye kama walivyopotea Maafisa upelelezi 6 kutoka mkoa wa Mtwara". Pia ukosefu wa usingizi ulikuja kutokana na maswali anayoulizwa na wakubwa wake wa kazi, kuwa amefikia wapi kwenye uchunguzi wa matukio ya Msumbiji dhidi ya raia wa Tanzania.
Uongozi katika zama hizi za uwazi na utandawazi ni shida sana. Uwajibikaji wa serikali ukilegalega katika kutatua changamoto za wananchi, hukumu yao dhidi watawala hufanyika kwenye sanduku la kupigia kura. Wanaadhibiwa na wananchi kwa kunyimwa kura zitakazowapa mamlaka ya kukamata dola. Hivyo viongozi wa serikali walikuwa wanahitaji majibu ya haraka kutoka kwa Mkuu wa Usalama wa Taifa ili waweze kuwajuza raia kinachoendelea.
Hali ilikuwa tete pia kwa Katibu Muhtasi wake, dada Kokunawa. Maana sasa alikuwa anakaa mkesha ofisini kama nesi wa zamu ya usiku kwa ajili ya wagonjwa mahututi. Kila wakati alikuwa yupo kwenye mtandao anasubiria barua pepe ya ripoti kutoka kwa Kachero Manu. Akaamua awe anarudi nyumbani saa 7 usiku lakini ikifika saa 12:30 asubuhi tayari yupo ofisini.
Ikafikia wakati baadhi ya wafanyakazi wa usafi kwenye jengo la ofisi yao wakawa wanadhani analala ofisini. Maana jioni wanapoondoka ofisini wanamuacha na asubuhi wanapowahi mapema kuja kusafisha jengo wanamkuta kashafika zamani.
Kazini kwao watu wa ofisi za jirani kila mmoja akawa na tafsiri yake kwa Kokunawa, wapo waliokuwa wanadhani hajaolewa na wala hana mchumba. Kumbe ni mchumba wa mtu na mtarajiwa wake alikuwa yupo nje ya nchi kimasomo.
Huko mtaani kwake majirani zake walikuwa wakimuona anajifanya mzungu na anajidai hana muda wa vikao vya umbea mtaani, hana muda wa kuhudhuria msiba wala sherehe ya mtu yoyote pale mtaani. Kumbe hawajui hata Kokunawa alikuwa hapendezwi na mazingira ya kazi yake namna yanavyomuweka mbali na jamii inayomzunguka na hata ndugu zake.
Maana ilikuwa ni kawaida kwake wakati mwingine yupo likizo lakini anakatishwa likizo yake kwa sababu ya kikazi. Kokunawa akiwa katika lindi la mawazo ya kazi yake, ghafla akaona meseji ya barua pepe yenye kichwa cha habari "Mwiba wa Tasi:Cabo-delgado", akajua kazi imeanza huko akatabasamu na kushusha pumzi ndefu mithili ya mtu aliyenusurika kupigwa dafrao na gari barabarani.
Akaifungua, kisha akaisoma na kuidurufu kisha akaweka kwenye faili na akapeleka ripoti hiyo ya Kachero Manu mezani kwa Bosi Mathew Kilanga. Akafunga ofisi na kuanza msafara wa kurejea nyumbani kwake Kigamboni ilikuwa imeshafika saa saba kamili usiku tarehe 16/02/2018. Alijua Bosi wake sasa ataanza kulala kwa raha maadamu amepata taarifa ya kijana wake Kachero Manu toka Jimboni Cabo-Delgado.

Mahasimu uso kwa uso nyumbani kwa Dr.Muganyizi
Mara baada ya kikao cha siri cha 'Monte Branco Ltd' kufungwa haraka haraka saa 6:45 usiku, Kachero Manu akatuma ujumbe wa barua pepe mfupi ofisini Dar es salaam ukitaka Meneja Mkuu wa Mafuta na Gesi Bwana Andenga Kazimoto afuatiliwe kwa karibu na wana usalama na mali zake zote anazomiliki na akaunti zake za benki zifuatiliwe miamala yake na kuhakikiwa.
Pia washirika wake wa karibu nao wachunguzwe kwa ukaribu na apewe taarifa yoyote kama atakuwa na safari ndani siku mbili hizi, na asizuiwe kusafiri. Lengo la Kachero Manu lilikuwa ni kutaka kumkamata Bwana Andenga Kazimoto katika ardhi ya Msumbiji akiwa na ushahidi kamili wa nyaraka za siri anazokuja kuziuza kwa Bwana Alfredo.
Baada ya kutuma barua pepe alishuka kwenye gari kwa haraka akaanza kuzunguka kwenye maegesho kuitafuta gari anayohisi wataitumia wabaya wake kwenda kufanya mauaji ya Dr.Muganyizi. Gari aina ya "Toyota Land cruiser" rangi nyeupe yenye namba inayoanzia na MBA-08...ambayo aliliona lilipomfuatilia kule Nzuwa Lodge. Alizunguka karibu eneo zima la maegesho ya magari, hakuona gari lenye namba hizo. Kijacho chembamba kikaanza kumvuja usoni, akashtushwa roho yake huenda kapigwa chenga ya mwili na wabaya wake.
Ingawa ilikuwa ni msimu wa baridi, kijacho kilitokana na hisia za kutorokwa na maadui zake bila kuwaona na hasa ukichukulia yeye ndio pekee anafahamu kuwa Inspekta Jenerali Mark ndio kapewa jukumu la kumuua Dr.Muganyizi.
Alipokuwa karibu na kukata tamaa, akapata wazo jipya la kwenda kwa mlinzi wa getini anayeandika namba za magari yanayoingia na kutoka hotelini, akajua hapo getini ndipo atapata majibu kuwa hilo gari lipo au limeshaondoka.
Akatembea kama meta 10 kwa mwendo wa kupega mpaka kwenye kibanda cha mlinzi wa getini. Alipofika akasalimiana nae "Hellow... habari za usiku kijana wangu, aisee nimepigiwa simu na mteja wenu mmoja, kaniambia kaharibikiwa na gari lake yupo hapa hotelini kwenu, gari lake limekataa kuwaka sasa simu yangu imezima chaji na nimelitafuta hapa maegesho silioni, sasa sijui unanisaidiaje?", alimaliza uwongo wake mtakatifu Kachero Manu huku akimkazia macho mlinzi yule.
"Wewe unatokea wapi? Alipigwa swali papo kwa hapo na mlinzi yule. "Mimi ni fundi magari wa kampuni ya magari ya kukodishwa ya "PAPADIOT"" alidanganya tena Kachero Manu huku akimkazia macho bila kupepesa.
Mlinzi yule alionyesha amechoka choka hataki usumbufu akaashiria kwa kidole, "kama hapa maegesho ya mbele hujaliona hilo gari unalolisaka basi fuata njia hii kwa mbele kushoto kuna maegesho ya chini kwa chini kwa baadhi ya magari maalumu huenda gari unalolitafuta lipo huko" alielekeza mlinzi yule huku akisogelea kiti chake ili aendelee kusinzia zake.
Akaaga Kachero Manu bila mlinzi yule kuitikia, kwa mwendo wa haraka tena akafanikiwa kuingia kwenye maegesho ya chini kwa chini. Kwa bahati nzuri gari hilo analolisaka liliegeshwa usawa na lango la kuingia.
Akalisogelea gari hilo, akachomoa mfukoni mwake mkungu wa funguo malaya na bahati ilikuwa kwake hakukuwa na mtu yoyote kule chini. Akajaribisha funguo kama sita zote zikawa zinagoma, akaijaribisha funguo ya saba mara mlango wa gari ukafunguka.
Bila simile akafungua mlango wa gari, akaingia akafunga. Akafungua droo ya upande wa siti ya mbele ya abiria kwa msaada wa kurunzi yake ndogo aliyoiwasha na kuanza kupekua. "Shabaaashi.......! kumbe nimepatia kwelikweli hii ni gari ya Inspekta Jenerali Mark Noble..! " aliropoka hivyo baada ya kuona kadi ya umiliki wa gari hilo.
Akairudisha hiyo kadi kisha akaenda kujibanza chini ya siti ya nyuma kabisa akimsubiria mbaya wake. Akaangalia saa yake ilikuwa inasoma saa 7:15 usiku. Akawaza kuwa leo mkesha mwingine bila usingizi, lakini alishazoea maana katika mafunzo ya Ukomandoo huwa wanakaa miezi miwili mfululizo bila kulala.
Mchana kutwa wanafanya mazoezi, ikifika usiku ni kuimba nyimbo za hamasa mpaka kunakucha tena. Hivyo hili la kukosa usingizi halikumpa tabu sana. “Kwanza Mwanausalama utapataje usingizi mororo haliyakuwa raia ambao wanakulipa mshahara kwa kodi zao hawana amani”, alijisemeza peke yake moyoni mwake huku akijipa hamasa ya mapambano.
Akawa yupo makini kumsubiria Inspekta Jenerali Mark aje waende pamoja nyumbani kwa Dr.Muganyizi kama ataamua yeye mwenyewe kutekeleza jukumu hilo kama alivyoagizwa na wakubwa wake. Nyumbani kwa Dr.Mganyizi ndio alipanga kuwe machinjio ya Inspekta Jenerali Mark Noble.
Akawa anavuta taswira namna serikali ya Msumbiji inatakavyoduazwa na itakavyofanya maombolezo ya Kitaifa kwa kifo cha Inspekta Jenerali Mark Noble. Wakati kwa upande wa Tanzania itakuwa ni furaha fokofoko kwa kuliangamiza joka jangwa la hatari kwa uhai wa Watanzania.

Upepo mwanana wa ziwa Nkwita ulikuwa unavuma usiku huo na kuleta hali ya hewa safi na yenye kuvutia kwa wakazi wa maeneo ya jirani na ziwa. Pembezoni mwa ziwa kulikuwa na msitu wa savana wenye miti inayovutia ndege wa kila aina kufanya makazi yao. Watalii toka sehemu mbalimbali walikuwa wanavutika kulitembelea ziwa Nkwita kwa ajili ya shughuli za kitalii.
Dr.Muganyizi alikuwa anaishi karibia na ziwa Nkwita katika Mji wa Pemba, makao makuu ya Jimbo la Cabo-Delgado umbali wa takribani saa moja kwa kutumia usafiri wa gari ukitokea Nautilus Hoteli, sehemu kilipofanyika kikao cha Mafioso wa Cabo-Delgado na kutoa hukumu ya kifo kwa Dr.Muganyizi.
Lilikuwa ni eneo tulivu sana lililojitenga na mji. Maofisa wengi wa taasisi za kimataifa wanaofanya kazi katika Mji wa Pemba na vibopa wa Mji walikuwa wanaishi huko kujiepusha na fujo fujo na makelele ya mjini. Kwa Tanzania tungefananisha na maeneo ya Masaki au Oysterbay.
Inspekta Jenerali Mark Noble alichelewa kutoka Nantilius Hoteli usiku ule, alikuwa anapokea taarifa juu ya usafirishwaji wa maiti ya kijana wake Jimmy kuelekea kwa wazazi wake Jijini Maputo. Huyu Jimmy alipigwa risasi na Inspekta Jenerali Mark nyumbani kwa dereva Masebbo kutokana na kutaka kutoboa siri za Mafioso wa 'Monte Branco Ltd' kwa Kachero Manu.
Baada ya hapo aliulizia hali ya mpakani kama hakuna lolote jipya, akapewa taarifa kila kitu kipo shwari. Kisha baada ya hapo ndio akapanga aelekee nyumbani kwa Dr.Muganyizi kutekeleza maagizo ya kikao cha usiku huu aliyopewa.
Alivyoingia ndani ya gari hakuchukua tahadhari yoyote na hilo ndio lilikuwa kosa lake, ndani ya gari alimpakiza adui yake namba moja Kachero Manu bila yeye mwenyewe kujua. Alipowasha gari lake tu akafungulia wimbo wa mwanamuziki wa Kimarekani “Louie V Gutta” unaoitwa “Kill The Streets” upate kumburudisha akiwa safarini.
Wimbo ambao huwa daima anapotaka kwenye kufanya tukio la mauaji huwa anaupenda kuuskiliza ili umpe morali kutokana na mashairi ya wimbo huo. Humo humo ndani ya gari lake akabusha bangi lake na kuanza kulipuliza bila aibu.
Kwa Cheo chake kama Inspekta Jenerali hakutakiwa kuwa mvunjivu namba moja wa sheria. Tabia yake ilifanana na Daktari anayekukataza usivute sigara utapata kansa wakati yeye ndio mvutaji aliyekubuhu. Au sawasawa na Sheikh anayehubiria waumini wake msikitini kuwa fuateni maneno yangu msifuate matendo yangu.
Baada ya dakika kama 45, Inspekta Jenerali Mark na Kachero Manu walikuwa tayari wameshafika maeneo ya karibu na nyumbani kwa Dr.Muganyizi. Aliegesha gari mtaa wa pili yake kutoka nyumba anayoishi Dr.Muganyizi. Ilikuwa ni mitaa ya kishua kweli kama wanavyopenda kuiita vijana wa mjini.

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom