Riwaya: "Cabo-delgado"-part 01

Riwaya: "Cabo-delgado"-part 01

RIWAYA: CABO DELGADO-PART 17

Baada ya dakika kama 45, Inspekta Jenerali Mark na Kachero Manu walikuwa tayari wameshafika maeneo ya karibu na nyumbani kwa Dr.Muganyizi. Aliegesha gari mtaa wa pili yake kutoka nyumba anayoishi Dr.Muganyizi. Ilikuwa ni mitaa ya kishua kweli kama wanavyopenda kuiita vijana wa mjini.
Yaani ni mitaa ambayo nyumba zake zimejengwa kwa mpangilio maalumu, kwa ramani za kwenye video na huku barabara zake zimepandwa bustani za miti mirefu yenye kutunzwa kiustadi mkubwa. Huku pembezoni mwa barabara kukiwa na taa za barabarani zinazotumia jua zenye kutoa mwangaza wa wastani usiokera kwa mpita njia.
Barabara zake zilikuwa zimewekwa lami yenye viwango vya hali ya juu. Akashuka haraka haraka Inspekta Jenerali Mark Noble, akachomoa bastola yake akaishika mkono wa kulia inapepea akasahau hata kufunga milango kwa funguo kutokana na pupa zake za kutaka kumnyofoa roho Dr.Muganyizi. Hilo likawa ni kosa namba mbili la kumpa nafasi ya kushuka Kachero Manu kutoka siti za nyuma bila shida na kwa haraka.
Alivyoshuka tu akatoa upepo tairi zote nne za gari la Inspekta Jenerali Mark, ili kama wakizidiana ujanja huko ndani nyumbani kwa Dr.Muganyizi asiweze kumtoroka kirahisi. Kachero Manu akawa anamfuata nyuma nyuma Mark bila Mark kutambua kuwa anafuatwa. Kuna wakati Inspekta Mark akigeuka nyuma kwa machale yake, inabidi ajifiche kwenye kivuli cha miti ya barabarani.
Walipoingia mtaa wa pili, nyumba ya tatu upande alioingia kushoto kwake ndipo alipokuwa anaishi Dr.Muganyizi. Kachero Manu akajibanza kwenye kivuli cha miti iliyopandwa kwa mstari nyumba ya pili kabla kufika kwa Dr Muganyizi. Ilikuwa ni nyumba kubwa imezungushiwa ukuta mrefu wenye meta zisizopungua sita huku ukiwa ukuta huo umenakshiwa kwa rangi nyeupe, huku juu yake kukiwa na nyaya za umeme maalumu kwa ajili ya kuzuia wezi. Na taa za duara zilikuwa zimezunguka ukuta wote kwa ajili ya kuleta mwangaza wa usalama.
Ni nyumba ambayo gharama ya ukuta wake tu unajenga "Nyumba Mjinga" zetu hizi za uswahilini kama 20 na chenji inabaki ya kununulia gari ndogo ya kutembelea mfano wa aina ya "Mark-X". Akaamua ampe dakika 20 kabla hajamshtukiza, huku robo saa zikiwa ni za kupambana na kikwazo chochote.
Zilipopita dakika 10 tu akasikia risasi ya kwanza imepigwa. Akajua kazi imeanza akakurupuka haraka haraka toka mafichoni kuelekea nyumbani kwa Dr.Muganyizi huku akiwa kaichomoa bastola yake mkononi. Akasogea kwa tahadhari kubwa sana mpaka akafika getini, akatulia kidogo akachungulia kwenye uwazi mdogo wa kwenye geti.
Akamuona mlinzi wa getini akiwa na sare zake za rangi ya kaki na kofia nyeusi, na buti nyeusi miguuni, anaogelea katika dimbwi la damu huku bunduki yake imelala pembeni yake anapigania roho yake katika siku yake ya mwisho ya uhai wake wa kufaidi ugali wa duniani.
Alikuwa amelala chali meta kama 5 kutoka usawa wa geti akafahamu ile risasi aliyosikia akiwa nje ya nyumba itakuwa amepigwa huyu mlinzi na Inspekta Jenerali Mark Noble.
“Huenda huyu mlinzi alimuona Mark wakati anaingia kwenye nyumba hivyo labda alimfuata ili kupambana na Mark kwa bahati mbaya hakufahamu kama Mark ni mzoefu wa mapambano, labda alijua ni kama majambazi tu wa kawaida” aliwaza Kachero Manu. Akajiuliza "je aingie kupitia getini kwa tahadhari kubwa au ni mtego anachezewa sinema la kihindi aweze kunaswa kiwepesi?".
Kwa Kachero makini kila unachokitilia mashaka lazima ukifanyie kazi usikipuuzie hata kidogo. Akaghairisha kupitia getini, akarudi kuzunguka ukuta akaparamia kwenye mti miongoni mwa miti iliyopandwa kuzunguka nje ya ukuta kwa pembezoni mwa ukuta.
Alivyofika usawa wa juu kidogo ya ukuta ule wa meta 6 akaruka kutoka kwenye mti na kupaa juu ya nyaya za umeme za ukuta mithili ya mpiga mbizi kwenye bwawa la kuogelea anavyojirusha. Akatua salama kwa mtindo wa sarakasi kwenye nyasi za ukoka za ndani ya ukuta.
Aliponyanyuka akaanza kuisogelea ile maiti mpaka akaifikia huku akiwa na tahadhari kubwa. Akaipiga mateke kidogo, ikabakia imetulia akajihakikishia kweli amekufa sio mtego kwake. Akairuka ile hakuwa na muda wa kupoteza kuichunguza sana asije baradhuli Mark akapata nafasi ya kupoteza uhai wa Dr.Muganyizi.
Akaanza kutembea kwa minyato usawa wa pembezoni mwa bustani ile ya nyasi za ukoka inayoizunguka nyumba mpaka akalifikia karibu dirisha la jiko la ndani. Akaona taa ya jikoni inawaka. Akasogelea dirishani kabisa akakuta dirisha lililotengenezwa kwa madini ya aluminium limefungwa. Akatoa kibati kidogo toka mfukoni mwake akaingiza kibati hicho kufyatua kifungio cha dirisha akakandamiza kibati kikafyatuka. Bila ajizi akasukuma kwa upole dirisha ili lisipige kelele akafanikiwa kulifungua.
Akarukia jikoni, alipoingia, akawa anaskia sauti anayohisi ni ya Mark ya kufoka, "yuko wapi Bosi wako Dr.Muganyizi? kama unamficha hutaki kusema alipo nikigundua nasambaratisha ubongo wako kwa risasi". "Bosi kaniaga anasafiri ila hajaniambia anasafiri kwenda wapi" alijibu huyo mtu kwa sauti ya kutetemeka ilyojaa uwoga wa kupigwa risasi. Katika uhai wake kijana yule leo ndio siku ya kwanza kasikia mlio wa risasi ile iliyompiga mlinzi wa getini.
“Sasa tulia hivyo hivyo”, alisema Inspekta Jenerali Mark, akatoa kamba ya manila ndefu toka kwenye mfuko wa suruali yake akaanza kumfunga kamba kijana yule za mikono na miguuni kwa kuikaza mpaka damu ikawa inapita kwa tabu. Kisha alipomaliza akamsokomezea matambara machafu ya nguo mdomoni ili asiweze kupiga kelele, kisha akarudi tena Mark chumbani kwa Dr.Muganyizi ambapo alikuwa amemkosa mara ya kwanza.
Kachero Manu akasubiri kidogo akaona ukimya umetawala kwa muda. Akanyonga kitasa cha mlango wa jikoni unaotenganisha na ukumbi wa kulia chakula, ukafunguka akaufungua kwa umakini mkubwa ili usitoe kelele akapita akaingia ukumbi wa chakula, akapitiliza mpaka kwenye veranda ya kuelekea vyumba vya kulala.
Huko ndipo alipomuona kijana kafungwa kamba, huku damu zinamvuja mdomoni na puani kila akipumua kutokana na kipigo kizito kisicho na chembe ya huruma alichopokea toka kwa Mark. Alipomkaribia yule kijana akawa anamuona yule kijana ameelekeza macho yake usawa wa mlango wa chumba kimojawapo.
Kachero Manu, akatambua anapewa ishara ya macho kuwa kuna mtu kwenye hicho chumba, na mtu mwenyewe si mwingine bali ni Inspekta Jenerali Mark Noble. Hivyo akamsogelea yule kijana kwa tahadhari huku macho yake yapo uelekeo wa kile chumba. Alipokaribia akakuta mlango upo wazi na Mark ametingwa na kupekua chumbani humo ametupatupa vuruvuru nguo na mafaili mbalimbali chini.
Ilionyesha kama kuna nyaraka za siri anazitafuta chumbani mule kwa Dr.Muganyizi huku mkononi mwake kuna bastola ambayo ameishika kizembezembe kwa kujiamini yupo peke yake ndani ya chumba.
Alichofanya Kachero Manu ni kumshitukiza,"tupa bastola chini na nyanyua mikono juu" alifoka kwa sauti ya juu yenye mamlaka isiyo na chembe ya mzaha. Inspekta Mark moyo wake ulilia paaah..!, alipatwa na mshtuko mithili ya mtu aliyefumaniwa na mke wa mtu saa 6 ya mchana ya jua la utosi.
Hakutegemea usiku ule wa manane kuwe na mtu atakayemsumbua kwa kufuatilia nyendo zake. Akatii amri mara moja na kutupa bastola chini. "Yupo wapi Dr.Muganyizi"? aliulizwa Mark na Kachero Manu. "Sifahamu alipokwenda" alijibu Mark kwa sauti ya kujiamini. Alianza kuondosha uoga alijua akizubaa atakufa kifo cha kijinga bila kupambana. Akaanza ujanja wa kuchelewesha muda.
Akaongea Mark, "wewe maluhuni unajiita Hassan ibn Hussein mpelelezi toka Tanzania" kisha akaangua kicheko cha kebehi. "Utanijua hivi punde..", alijibu Kachero Manu. "Haya rudi kinyumenyume mpaka usawa wa kitanda" alitoa amri huku anaingia vizuri kwenye chumba cha Dr.Muganyizi, hilo lilikuwa ni kosa kubwa.
Inspekta Mark

Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA:CABO DELGADO-PART 18

Inspekta Mark alirudi nyuma nyuma, kama hatua tatu halafu akajifanya kama kajikwaa kitu anataka kuanguka kwa kuugongesha mguu wake wa kushoto juu ya mguu wake wa kulia kisha kama umeme akajibidua sarakasi hewani akatua miguu yake juu ya kifua cha Kachero Manu ambaye hakujiandaa na shambulio la ghafla na alikuwa anatembea kuingia chumbani.
Shambulio ambalo lilimwangusha kizembe mpaka chini na bastola yake mkononi ikadondoka chini. Haraka haraka Inspekta Mark akajizoa chini kuikimbilia bastola yake, Kachero Manu naye bila ajizi akainuka na kumpiga teke aina ya "SAVATE".
Huo ni upigaji wa teke ambao asili yake ni nchini Ufaransa. Huwa ukipigwa na fundi wa upigaji lazima utenguke kiungo labda uwe na bahati ya mtende kuota jangwani, na ndio hiyo bahati ilimkuta Mark. Hilo teke halikutua vizuri kwenye maungio ya goti liliteleza kidogo kutokana na kuwa katika mwendo wa kuiendea bastola yake ndio ikawa salama yake likamuangusha chini lakini akiwa na maumivu makali.
Akajikaza kisabuni akanyanyuka ghafla na kutupa makonde ya haraka haraka kama matatu, makonde mawili yakampata Kachero Manu kisawa sawa yakampasua kwenye kona ya mdomo. Damu zikaanza kuvuja taratibu, akarusha konde la tatu usawa wa jicho la kushoto la Kachero Manu, Kachero akalikwepa kiustadi mkubwa.
Mark akapatwa na wazo jipya baada ya kutambua Kachero Manu ni farisi katika fani ya mapambano, na asingeweza kumshinda kirahisi. Akaanza kurudi kinyumenyume mpaka akakaribia usawa wa dirisha la chumbani alilotumia kuingilia chumbani kwa Dr.Muganyizi.
Kachero Manu akadhani ni mbinu ya kujipanga kwa shambulio akasimama kwa umakini anamsubiria maana alitia akili Inspekta Jenerali Mark sio wa kawaida kwenye sanaa za mapigano.
Kumbe ile ilikuwa ni "janja ya jani kula hindi bichi", kama nyani vile aligeuka kwa haraka kwa kudandia kitanda kisha akaparamia dirisha la chumbani kwa Dr.Muganyizi alilotumia kuingilia akatokomea nje ya nyumba kisha akatimkia mtaani kwenye giza totoro.
Kachero Manu alisimama kama kapigwa ganzi alishangazwa na umahiri wa Inspekta Mark, hakutegemea kama Mark atamkimbia usiku ule. Akatanabahi kuwa Inspekta Mark atakuwa amepitia mafunzo makubwa sana ya sanaa za mapigano.
Alifahamu Mark hatoweza kuitumia gari yake kwa kuwa kaitoa upepo, lakini kwa kasi aliyotoka nayo hapa ingetosha kutafuta mbinu mbadala za kuondoa eneo lile. Akaamua aachane kwanza afahamu alipo Dr.Muganyizi maana ndio kipaumbele cha kwanza kumuokoa yeye na sio kumsaka Mark.
Kachero Manu akaiendea bastola yake akaiokota akamrudia yule kijana aliyefungwa kamba kwenye veranda. Akamfungua kamba zote na kisha akaanza kumuuliza, "wewe ni nani humu, pole sana.." alisema Kachero Manu.
”Mimi ni msaidizi wa kazi za nyumbani, kibarua wa Dr.Muganyizi” alijibu kijana Yule. ”Sasa Dr. kalala wapi usiku huu”? aliuliza Kachero Manu kiudadisi ili apate ukweli mahali alipo.
"Dr kasafiri kwenda Tanzania na ndege ya saa moja usiku wa kuamkia leo, kaenda kuangalia familia yake kipindi hiki cha mwezi wa mwezi wa pili katika mapumziko ya siku ya wapendano "Valentine Day". Kasema atarudi wiki ijayo” alimalizia maelezo yake kijana Yule.
Kachero Manu akatabasamu akajua Dr.Muganyizi bado siku zake za kuishi zipo sana hapa duniani, kakikwepa kifo chake mbele ya mtutu wa Inspekta Jenerali Mark. Pia akatambua Dr.Muganyizi safari zake zilikuwa za siri maana hata mamluki watoa taarifa kwa watu wa Alfredo wa kazini kwake hawakufahamu hiyo safari.
”OK.. kuwa na amani kijana endelea na maisha yako, ikiwezekana katoe taarifa kituo cha polisi, kwaheri...” akaondoka Kachero Manu bila kumpa nafasi yule kijana ya kujibu chochote, akatokomea zake nje ya nyumba, usiku ule kama wa saa tisa kasoro dakika kumi.
Huku ving'ora vya gari za polisi vikisikika kwa mbali akafahamu huenda majirani wametoa taarifa baada ya kusikia mlio wa risasi iliyomuua mlinzi wa nyumba ya Dr.Muganyizi au Mark kawashtua polisi waje kumtia mbaroni.
Akafanya haraka kupotea eneo lile ili asije kufanywa asusa kwenye jambo asilohusika nalo, wakamtoa kafara.


SURA YA KUMI
Kachero Manu aonyeshwa cha mtema kuni
Nyumba ya Dr.Muganyizi usiku huo ikazingirwa na mapolisi lukuki waliokuja kuchunguza mauaji yaliyotokea ndani ya nyumba hiyo.
Kachero alipotoka nyumbani kwa Dr.Muganyizi, akawa hajui anaelekea wapi maana hata eneo alilokuwepo alikuwa halijui linaitwaje kutokana ugeni wake. Kama ujuavyo "kuku mgeni hakosi kamba mguuni". Lakini akafanya haraka kuondoka eneo lile asije kukutwa na polisi akapewa kesi ya mauaji ikawa habari ingine tena.
Akatembea kwa muda wa kama robo saa kwa miguu. Akiwa anakata mitaa usiku huo, akakutana na "taksi bubu" moja inapiga tripu za mitaani. Akafanya maamuzi ya kuisimamisha kwa kuipungia mkono. Dereva yule akatii amri na kuisimamisha gari yake.
Alichomwambia dereva taksi yule ni kitu kimoja tu, apelekwe Nautilus Hoteli. Akafikishwa salama salimini hapo hotelini na ile taksi. Kabla hajashuka kwenye taksi bubu, akamuuliza dereva taksi, "wapi naweza kupata sehemu nzuri ya kulala lakini ya gharama ya kawaida hapa Naitilus hoteli ni matawi ya juu sana sipawezi" akadanganya wakati alikuwa na pesa sufufu za kumuwezesha kulala hata Hoteli ya nyota 5 hata kwa muda wa mwaka mzima.
Lengo lilikuwa ni kutopoteza muda na kutafuta sehemu ya haraka ya kulala ili asubuhi ikifika ajue anajipanga vipi kuwakabili mabaradhuli wa Alfredo. Haraka haraka dereva yule akajibu, "nenda "Pemba Magic Lodge" ipo kama kilometa 3 kutokea ufukwe wa Wimbi hapo ni sehemu tulivu huwezi kukosa nafasi usiku huu" alimalizia maelezo yake dereva taksi akitumia ulimi wake wa ulimbo kumnasa Kachero mtegoni.
Akalipa pesa aliyotajiwa akaingia ndani ya Nautilus Hoteli kuchukua gari yake ya kazi 'Volvo s60' aliyoacha maegesho ya magari tokea saa 3:05 usiku alipowasili eneo hilo. Gari ilikuwa imechafuka matope ya barabarani halitamaniki hata kuliangalia.
Alipolisogelea gari yake akatabasamu kwa jinsi ilivyofanikisha salama safari yake ya kumtoa Montepuez mpaka Pemba kwa muda mfupi sana, akamsifu kimoyomoyo Komandoo "JS" kwa kumchagulia gari lenye ufanisi mkubwa.
Akaingia ndani ya gari akawasha gari huku anaitafuta ilipo 'Pemba Magic Lodge' kwa kutumia mtandao wa simu yake ya mkononi, akarekebisha GPS yake kwenye simu ikawa inamuelekeza barabara za kupita mpaka kumuwezesha kufika karibu na ilipo 'Pemba Magic Lodge' ndani ya nusu saa tu kutokea Nautilus Hoteli.
Akiwa ndani ya gari bado hajang'oa nanga, akawasha Kompyuta yake mpakato kwa ajili ya kutuma taarifa ofisini za kuhusu Dr.Muganyizi. Taarifa aliyotuma ilieleza kuwa Daktari anatafutwa kwa udi na uvumba ili auliwe na Mafioso wa Cabo-Delgado, hivyo azuiwe asirudi kwanza nchini Msumbiji, asalie Tanzania mpaka hali ya usalama wake itakavyotengamaa.
Pia ahojiwe haraka ili kufahamu ni watu gani walikuwa wanahitaji kupewa tenda ya ujenzi wa barabara katika mradi wa "PEMOVACHA", na apewe ulinzi madhubuti yeye na familia yake.
Ikiwezekana alipendekeza wapelekwe mafichoni kwenye nyumba maalumu za usalama wa taifa 'safehouse' kuhofia mtandao mpana wa Alfredo kuwanyakua. Baada ya kutuma taarifa hiyo nyeti akazima kompyuta yake akahifadhi vizuri vifaa vyake muhimu kwenye sanduku dogo lililopo chini ya miguu ya kukanyagia breki.
Safari yake fupi ya kuelekea 'Pemba Magic Lodge' kwa ajili ya kulaza mbavu zake ikaanzaa, ili kesho yake aendeleze libeneke lake la kuwatafuta mahasimu zake. Baada ya muda wa nusu saa akawasili kwenye jengo moja jirani na Pemba Magic Lodge. Hisia zake hazikumtuma kabisa kuegesha gari lake hapo kwenye nyumba ya wageni. Akaamua kutii hisia zake bila kupingana nazo. Akafunga vizuri gari lake akashuka na kamzigo chake cha nguo chache.
Alichokuwa hajui Kachero Manu ni kuwa ile "taksi bubu" iliyombeba maeneo ya nyumbani kwa Dr.Muganyizi, ilikuwa ni ya mmoja wa wakala wa Inspekta Jenerali Mark. Baada ya Mark kufanikiwa kumtoroka Kachero nyumbani kwa Dr.Muganyizi alitoa taarifa kwa wakubwa wake juu ya ujio wa Kachero Manu katika Mji wa Pemba, na namna alivyopambana nae kindakindaki nyumbani kwa Dr.Muganyizi.
Ikapangwa mikakati kabambe ya kumkamata kupitia 'taksi bubu' na nyumba za kulala wageni zote usiku huo. Pia ulinzi wa barabarani uliimarishwa vilivyo ili asiweze kuwatoroka tena. Zikasambazwa 'taksi bubu' zaidi ya 20 usiku ule zikijifanya zinatoa huduma kwa watembea kwa miguu usiku ule.
Yule dereva alivyomuacha Kachero Manu pale nje ya Naitilus Hoteli alipeleka taarifa moja kwa moja juu ya Kachero Manu kuwa atafikia 'Pemba Magic Lodge'. Hivyo hiyo ikachaguliwa kuwa ni sehemu muafaka kufanyia Umafia wao usiku ule.
Kingine kilichompa uhakika dereva taksi juu ya
IMG-20200516-WA0037.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Alichokuwa hajui Kachero Manu ni kuwa ile "taksi bubu" iliyombeba maeneo ya nyumbani kwa Dr.Muganyizi, ilikuwa ni ya mmoja wa wakala wa Inspekta Jenerali Mark. Baada ya Mark kufanikiwa kumtoroka Kachero nyumbani kwa Dr.Muganyizi alitoa taarifa kwa wakubwa wake juu ya ujio wa Kachero Manu katika Mji wa Pemba, na namna alivyopambana nae kindakindaki nyumbani kwa Dr.Muganyizi.
Ikapangwa mikakati kabambe ya kumkamata kupitia 'taksi bubu' na nyumba za kulala wageni zote usiku huo. Pia ulinzi wa barabarani uliimarishwa vilivyo ili asiweze kuwatoroka tena. Zikasambazwa 'taksi bubu' zaidi ya 20 usiku ule zikijifanya zinatoa huduma kwa watembea kwa miguu usiku ule.
Yule dereva alivyomuacha Kachero Manu pale nje ya Naitilus Hoteli alipeleka taarifa moja kwa moja juu ya Kachero Manu kuwa atafikia 'Pemba Magic Lodge'. Hivyo hiyo ikachaguliwa kuwa ni sehemu muafaka kufanyia Umafia wao usiku ule.
Kingine kilichompa uhakika dereva taksi juu ya mtu aliyembeba ndio anayetafutwa ni matone ya damu kwenye fulana ya Kachero Manu upande wa bega lake la kushoto. Matone yalitokana na makonde mawili ya kona ya mdomo aliyopigwa na Inspekta Jenerali Mark Noble wakati wa mapigano nyumbani kwa Dr.Muganyizi. Sasa wakati dereva kawasha taa ya gari kupokea malipo yake akaona damu damu. Akajua huyu ndio mlengwa anayesakwa na akina Mark.
Hivyo ujio wa Kachero Manu pale 'Pemba Magic Lodge' ulikuwa unafahamika tayari. Alipofika tu kuulizia chumba cha kulala, aliambiwa vyumba vimejaa ila kimebaki chumba kimoja tu. "Una bahati sana kaka yangu kimebaki kimoja chumba namba "4A" tena kilishawekwa oda ila hakutokea huyo mtu mpaka saa 6:00 usiku, ndio maana tunakiuza tu sasa..!" alisema msichana ambaye ni mhudumu wa mapokezi ya wageni kwa sauti nyororo yenye kuonyesha imebeba ukweli ndani yake huku uso wake umevaa bashasha mwanana.
"Nipe hicho hicho, nachohitaji ni kupumzika usiku huu, kama sitokipenda kesho Inshallah utanibadilishia chumba...!" alisema huku akiwa amelifumbata kwa mkono wa kushoto begi lake dogo lenye nguo zake huku vifaa vyake muhimu vyote vya kazi akiwa ameviacha kwenye gari aliyoamua kuiacha kwenye maegesho ya jengo la maonyesho ya sinema lililopo takribani meta 200 kutokea 'Pemba Magic Lodge'. Ambapo hapo alipoliacha kulikuwa na magari kadhaa yaliyoegeshwa kwenye eneo hilo ya watu wanaoangalia burudani ya filamu usiku huo.
Aliamua kufanya hivyo ili ayasome vizuri mazingira ya eneo analotaka kufikia ili kama atapata matatizo ajue njia za kutorokea kirahisi. Alipokabidhiwa funguo na kuelekezwa chumba kilipo huku akimpa mgongo mhudumu, yule msichana mshirika wa mabaradhuli wa Alfredo akaunda tabasamu la ushindi katika sura yake akajua wameshamkamata mtuhumiwa wao kiulaini sana, bila rabsha zozote.
Alipofungua tu chumba chake, kabla hata hajafanikiwa kuwasha taa, alihisi hewa ya chumba sio rafiki kabisa, ni nzito sana. Alijiona anaanza kuishiwa nguvu akataka kurudi nyuma asiingie hobelahobela chumbani mume mpaka afanye taftishi kwanza. Lakini alikuwa ameshachelewa, alishtukiwa anapigwa na kitu kizito kwenye kisogo chake na kujikuta macho yake yanaingia giza zito na kujiona anazama kwenye shimo refu lisilofika mwisho. Akaanza kupiga kelele ili apate msaada wa haraka lakini sauti yake haitaki kutoka. Macho yake yakafumba na kupoteza fahamu pale pale.
Taarifa zilipofika za ujio wa Kachero Manu kwenye nyumba ya wageni ya "Pemba Magic Lodge" haraka haraka wakatumwa vijana wa kazi wakachague chumba watakachomshughulikia Kachero Manu.
Wakaingia na kupulizia gesi inaitwa "Methoxyflurane" kwa jina la utani inaitwa "knockout gas" (KO-Gas) ni gesi ambayo ukivuta tu hapo hapo unajiskia kulala usingizi mzito.
Kwa kuijua zaidi hii ndio gesi waliyoitumia Makachero wa Shirika la Kijasusi la Urusi (FSB) waliyoitumia kuwakamata magaidi waliowateka watu zaidi ya 1,000 katika Ukumbi wa maonyesho wa Dubrovka Theatre Jijini Moscow mwaka 2002. Mpaka ilipopulizwa hii kemikali ndio mateka wakafanikiwa kuokolewa.
Watekaji wa Kachero Manu walivyopulizia gesi hiyo wakakifunga vizuri chumba namba "4A" kisha wakaingia chumba namba "4B" ambacho kilikuwa kinatazamana na chumba cha mtego wa Kachero. Alipofungua tu mlango wake nao wakatoka na kiroba cha kokoto cha ujazo wa kilo zisizopungua 60 wakampiga nacho kisogoni akapoteza fahamu, wakaondoka nae.
Afya ya Kachero Manu haikuwa afya mgogoro ndio maana alipoteza fahamu tu, hakuaga dunia vinginevyo mimi na wewe kama tungepigwa na kiroba chenye ujazo huo tungekuwa hivi sasa tupo kaburini zamani sana tunasubiri siku ya kupulizwa parapanda la hukumu na Malaika Israfili huko jongomeo.


SURA YA KUMI NA MOJA
Kachero Manu ndani ya handaki la mateso
Kachero Manu alizinduka saa 10:30 Alasiri ya siku iliyofuata akiwa hafahamu mahali alipo. Alikuwa katika mghafala mkubwa wa kutokumbuka namna alivyofika hapo kitandani alipolazwa. Alikuwa ametimbika vilivyo, uso wote umevimba kutokana na tashdidi ya vipigo toka kwa wajuba waliomteka.
Licha ya kuzimia mule chumbani, walikuwa na hasira nae wakawa wanampiga kama vile yupo mzima na fahamu zake. Walichukizwa sana na kitendo chake cha kumuwinda Inspekta Jenerali Mark Noble na kuhatarisha uhai wake, mtu mahashumu sana Jimboni Cabo-Delgado.
Alijikuta yupo juu ya kitanda kidogo cha chuma na springi huku akiwa amefungwa miguu na mkono wake wa kulia kwa kamba huku akiwa yupo uchi wa mnyama kama siku alivyokuja duniani kutoka kwenye mfuko wa uzazi wa mama yake. Mkono wake wa kulia ukiwa umetundukiwa dripu la kuongeza damu mwilini na mkono wake wa kushoto umefungwa pingu. Kilikuwa ni chumba kidogo chenye uwezo wa kukaa kitandaa cha futi nne kwa sita na kuingia watu watatu mpaka wanne.
Kilikuwa ni chumba chenye mwangaza hafifu sana huku madirisha yake madogo matatu kama matundu ya vyoo vya uswahilini yakiwa juu kabisa hivyo kukisababishia chumba kukosa nuru ya kutosha. Alipofumbua macho tu akaanza kujiuliza "amefikaje hapo?".
Alipoanza kuvuta kumbukumbu namna alivyofika hapo, maumivu ya kichwa makali yakaanza kutawala katika mwili wake, akaamua afumbe macho tena. Ghafla akawa anasikia michakato ya nyayo za viatu vya kike vinakaribia kwenye mlango wa chumba chake. Akafumbua macho na kuangalia geti dogo la chuma, lililo kuu kuu lenye kutu.
Akasikia mgombano wa funguo na kufuli la geti wa kama sekunde takribani 40 kisha geti likafunguka akafumba macho kidogo huku anachungulia kwa jicho pembe. Akaingia ndani mwanamke mrefu wa rika la takribani si chini ya miaka 37, mrembo wa shani, ambaye mwanaume mwenye jicho la nje lazima achepuke nae akipata fursa.
Ni mwanamke ambaye hutegemei afanye kazi za ofisini labda awe Daktari au Mhasibu, bali unategemea awe anafanya shughuli za mitindo na ulimbwende. Aliingia akiwa amevaa shingoni mwake kifaa cha kupimia mapigo ya moyo ya mgonjwa na koti jeupe huku amebeba trei mkononi. Alivyokaribia kitandani akamtikisa Kachero Manu kwa kutumia mikono laini ya kike.
Kachero Manu akasisimkwa mwili na kupandwa na mihemko ya hamu ya kukumbatiana na mwanamke huyo. Akayapuuza mawazo hayo kisha akazuga kama ndio anaamka katika usingizi mzito. "Kunywa dawa za kupunguza maumivu" alisema yule Daktari kwa sauti ya upole na ukarimu huku akiwa anatabasamu.
Akaonyesha nje meno yake ya mbele, mazuri yaliyoacha mwanya, mpaka Kachero Manu akajiona kabisa anapata nafuu ya ghafla. Akatoa dawa kutoka kwenye trei ndogo nyeupe iliyokuwa na kikombe kichakavu cha bati kilichokuwa kinatoa harufu kali ya mkojo kuonyesha ni kikombe kilichochukuliwa chooni kikiwa na maji yake.
Akaitikia kwa kichwa kuonyesha kukubaliana na maelekezo ya Daktari yule mwanamke kisha akawekewa vidonge kwenye ulimi na kumeza vidonge vile vya maumivu kwa maji ya kikombe kichafu cha chooni kwa msaada wa Daktari. kwa mtindo wa kugugumia Kisha hapo hapo baada ya kumeza dawa, akafumba macho yake kuonyesha anahitaji mapumziko zaidi.
Dripu ya damu ilikuwa imebaki robo ujazo kuisha yote ili chupa ibaki tupu. Akasikia sauti ya viatu vya yule Daktari kuondoka huku anamchungulia kwa kupepesa macho, mpaka alipofika mlango akageuka kisha akamwambia "sasa umepata nafuu ulikuwa umezimia kwa zaidi ya saa zisizopungua 12, na ulipoteza damu nyingi sana hiyo ni chupa ya nne kuongezewa. Utakuja kuchukuliwa muda sio mrefu na "NACATANAS" ukahojiwe", alisema yule Daktari kwa sauti ya huzuni, Kisha akafungua geti akalifunga na kufuli akaondoka zake.
Sauti ya mlio wa viatu vya Daktari ikaanza kupotea masikio mwa Kachero Manu mpaka ikapotea kabisa. Akaanza kuvuta taswira kumbukizi ya namna alivyokamatwa. Akakumbuka mara ya mwisho alifika hadi kwenye nyumba ya kulala wageni na haikumbuki vizuri jina lake kisha akajishtukia yupo mikononi mwa maadui.: CABO DELGADO-PART 19

IMG-20200517-WA0088.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
RIWAYA: CABO DELGADO-PART 20


Sauti ya mlio wa viatu vya Daktari ikaanza kupotea masikio mwa Kachero Manu mpaka ikapotea kabisa. Akaanza kuvuta taswira kumbukizi ya namna alivyokamatwa. Akakumbuka mara ya mwisho alifika hadi kwenye nyumba ya kulala wageni na haikumbuki vizuri jina lake kisha akajishtukia yupo mikononi mwa maadui.
Akajilaumu namna alivyoshindwa kuchukua tahadhari ya kutosha na kuingia kichwa mchunga. Pia akaanza kujiuliza hao "NACATANAS" watakaokuja kumhoji ni akina nani hasa..!. Akajaribu kutikisa miguu yake kupima uimara wa kamba za miguuni ikawa ndio kama anaziongezea nguvu ya kuikamata vizuri miguu yake.
Akatulia kidogo kisha akapata wazo jipya la kuondosha dripu ya damu kisha atumie huo mkono kujifungua kamba aweze kujiokoa. Kabla hajaanza harakati zake hizo akasikia vishindo vya miguu ya watu wanakuja kwenye chumba chake, na giza lilianza kushitadi kwenye chumba chake ikabidi asitishe harakati zake hizo.
Alipoangaza macho juu ya dari akaanza kuona panya wakubwa wakubwa wanakimbizana kama vile wanacheza mchezo wa kitoto wa 'foriti' juu ya dari chakavu iliyojaa vumbi la toka mkoloni aondoshwe Msumbiji. Akatulizana kusubiri majaliwa yake toka kwa watekaji wake.
Ghafla baada ya kukurukakara za kufungua kufuli, ukafunguliwa mlango wakaingia watu wawili vipande vya watu. Sura zao ni za kunyata ambazo zinachukiza machoni kama ukibahatika kuwaangalia. Sura ambazo zimejaa makovu na majeraha mbalimbali ilyoshonwa kama nguo yenye viraka. Sura zao watu hao kama utamuonyesha picha zao mama mjamzito wa mimba changa ya wiki mbili tu itatoka mimba hiyo hapo hapo bila hata kutumia vidonge vya kuporomosha mimba na atalazwa hospitalini kwa kihoro.
Miili yao ilikuwa mikubwa vijana wa kileo wanaita "mwili nyumba", mmoja wapo ni mfupi, andunje kibushuti haswa jicho lake la kushoto chongo huku mguu wake mmoja wa kushoto anauvuta kwa mbali, kwa maana ni mfupi kuliko mwingine.
Na huyu mwingine ni mrefu sana kampita yule mcheza basketi wetu wa Tanzania anayetuwakilisha vyema Kimataifa "Hasheem Thabeet" kwa sentimeta chache sana.
Huku macho yao wote wawili yamepambwa kwa rangi nyekundu mithili ya nyanya iliyoivia shambani ikasuswa kuchumwa na mkulima akaachiwa ndege ajipocholee atakavyo. Hizo ni dalili ya kuonyesha ni wavutaji bangi wazuri tu.
Wote walivalia singlendi nyeusi kifuani zina maandishi meusi yameandikwa "NACATANAS" kuziba milima miwili mikubwa vifuani mwao. Fulana ambazo zilikuwa zinazoonyesha ukubwa wa matiti yao kutokana na ubebaji wa vyuma vizito na ukubwa wa lishe wanazokula.
Miguuni walikuwa wamevalia safari buti rangi ya kahawia. "Wewe mwanaharamu amka wakati wako umefika wa kufa kifo cha kijinga bila kujitetea, haupo Hotelini hapa..!" aliongea kwa kufoka yule baradhuli chongo ambaye anaitwa "Bob Chinanga", kumwambia Kachero Manu.
Huyu Bob-Chinanga na timu yake ndio waliotumwa na Inspekta Jenerali Mark Noble kwenda Kijijini Mahiwa kwenda kukata kichwa cha mama mzazi wa Kachero Manu baada ya kupewa taarifa za ujio wake na Bwana Andenga Kazimoto.
Huku yule mwingine mrefu ambaye anaitwa "Nanga Boy" ambaye hakuonekana kuwa ni mtu wa maneno mengi ya mkahawani ila ni mtu wa vitendo akawa anamfungua kamba za miguuni Kachero Manu. Mikono yake ilipogusa miguu ya Kachero Manu, Kachero alihisi kama ameguswa na chuma, kutokana na ukakamavu wa viganja vya mikono yake yule baradhuli.
Ilikuwa viganja vya mikono vimekomaa kama ubao utasema damu imefanya mgomo kutembelea vidole vyake vya mikono. Alipomaliza kumfungua kamba za miguuni, akahamia kufungua kamba ya mkono wa kushoto kisha akachomoa na kutupa pembeni dripu ya damu pembeni. Kisha akamfunga kitambaa cheusi usoni.
Hapo hapo Kachero Manu akaanza kupiga chafya mfululizo kutokana na vumbi pia kilikuwa kina harufu kali ya bangi. Halafu akamkwida Kachero Manu kwa kutumia ngozi ya tumboni akambeba begani mwake mzobemzobe kichwa chini mikono ya baradhuli "Nanga Boy" imekamatia chini ya mapaja akatoka nae nje ya chumba.
Kachero Manu hajui anapelekwa wapi na wajuba wale. Alichohisi ni kuwa walitembea hatua chache wakawa wanashuka chini ya ardhi kwenye ushoroba mwembamba na mteremko mkali. Kadri walivyokuwa wanashuka chini ndipo hali ya hewa ikaanza kubadilika kuwa nzito zaidi na kiza kikazidi kushitadi.
Kuna wakati anajigonga kwenye kiwambaza cha njia hiyo ya chini kwa chini huku wanaburudishwa na sauti za panya wanaokimbizana njiani kwenye giza lile na harufu ya kuchukiza kwenye pua zao. Waliposhuka kama mwendo wa dakika 20 kwenda chini akahisi wanapita njia yenye tope zito lililovunda.
Kichwa chake kinachoning'inia chini kuna wakati kinagusa kwenye tope lile lenye uvundo mzito wa harufu ya vitu vilivyooza kama mabaki ya chakula na maji machafu ya chooni. Kisha wakasimama mahali fulani.
Likafunguliwa lango kisha akatupwa kwenye chumba kilichoonyesha sakafu yake ni ya kokoto ngumu kutokana na kuumizwa na vijiwe hivyo. Alipotua sakafuni akaanza kunusa harufu ya mikojo yenye harufu ya pombe za kienyeji huku anaugulia maumivu ya mgongo.
Akiwa hajui nini cha kufanya akabebwa tena na kuweka kwenye kiti cha chuma kisha mikono yake ikafungwa juu ya bomba kama za kuning'iniza nyama buchani na miguu yake ikafungwa chini ya kiti, kisha akafunguliwa kitambaa alichofungwa usoni. Akatambua sasa yupo kwenye handaki lenye mwanga hafifu sana limejaa dhana mbalimbali za mateso.
Kulikuwa na mashoka na mapanga yaliyogandana damu na mabaki ya ubongo wa mwanadamu. Kulikuwa na mabomba ya sindano za kuchomea ng'ombe na chupa mbalimbali za dawa zikiwa zimetawanyika chini, pia kulikuwa na viti vya mateso vya umeme na minyororo ya kufunga na kufungua kwa kufuli. Kilikuwa ni chumba kinaweza kuingiza watu 10 kwa pamoja bila kubanana sana.
Ukutani kuliandikwa maneno mengi mengi ya lugha ya kireno yenye lengo la kuleta vitisho vya kisaikolojia. Mfano kulikuwa na maneno kama "Matar" likiwa na maana ya "fanya mauaji", pia neno kama "desgraçado" likimaanisha "mtoto wa haramu" na maneno mengi ambayo hakuwa anafahamu maana yake.
Ila aliona neno moja limeandikwa ukutani "Gorongosa Camp". Akawa anajiuliza "hili neno "Gorongosa" nimeliona wapi?". Alipovuta kumbukumbu zake vizuri akakumbuka alilisoma hilo jina kwenye nyaraka za siri la faili rangi nyeusi alilopewa Ofisini Jijini Dar es Salaam.
Akakumbuka ilikuwa ni jina la moja ya kambi ya mateso ya FRELIMO waliyokuwa wanaitumia wakati wanapambana katika vita ya wenyewe kwa wenyewe na kundi la RENAMO. Ndani ya hiyo kambi hiyo ya Gorongosa enzi hizo za vita kulikuwa na kila aina ya ukatili na mateso, akatambua yupo kwenye eneo la hatari sana.
"Kama eneo hili linafananishwa na kambi ya Gorongosa nitapona kweli? " alijiuliza nafsini mwake Kachero Manu huku hofu ikianza kutawala nafsini mwake. "Jina lako kamili ni nani na umekuja kufanya nini"? alishtukizwa na swali kutoka kwa Bob Chinanga huku Kachero akiwa kwenye lindi la mawazo.
"Mimi naitwa "Hassan Ibn Hussein" nafanya kazi kama mtafiti wa mambo ya kale kutoka Zanzibar, Tanzania Visiwani" alijibu kwa kujiamini huku amemtumbulia macho. "Hatujawahi kusumbuliwa ndani ya hii kambi na kidudu mtu wa aina yoyote sasa tutakufunza namna ya kusema ukweli, bila kushinikizwa" alisema yule baradhuli mrefu "Nanga Boy" huku akijiweka sawa kuanza kushusha kipigo kitakatifu.
Aliendelea kusema "Unajifanya mkaidi, kichwa mchungu ngoja tukutie adabu...!" kisha akamchapa kibao kimoja cha kelbu kwenye shavu la kushoto. Kachero Manu aliona nyota nyota nyingi sana usoni mwake na mwezi mchanga mwandamo mmoja, akapiga kelele za maumivu kama abiria aliyesahau mzigo kwenye daladala lenye haraka na lililojaza abiria la kuelekea Mbagala.
Kisha akashtukia nyundo nzito ya kupasulia mawe imetua utosini, hakuweza kuikwepa kwa sababu macho alikuwa amefumba kutokana na kibao kile cha shavuni. Nyundo ile ilisababisha damu ianze kububujika kwa nguvu, kisha yule baradhuli mfupi akawasha kiberiti akamwagia ndevu za Kachero Manu mafuta ya taa kisha akawasha moto zilipoanza kuungua ndevu, akawa anapiga kelele kwa maumivu makali sana huku kinywa kipo wazi hapo hapo yule mfupi akaingiza koleo kinywani mwa Kachero Manu akakamata jino moja la juu akaanza kuling'ang'ania ndani ya dakika moja akawa ameng'oa jino moja bila ganzi huku damu zinamwagika ovyo usoni mwake.
Huku yule mwingine anamchapa mgongoni na mkia wa samaki taa. Mkia ambao ukichapwa nao mwilini miba zake zinanasa kwenye ngozi ukivuta unachana ngozi na damu zinamwagika. Mateso na maumivu ya Kachero Manu yalikuwa makubwa, hayasemeki na wala hayaelezeki. Kabla hajapewa nafasi ya kupumua, kuugulia maumivu akashtukia anapigwa ngumi mfululizo za tumboni kama 6 hivi akajikuta anatoa mashuzi mfululizo bila kizuizi.
Ngumi ambazo kama ukipigwa mimi na wewe tusio na mazoezi, ambao mazoezi yetu ni kupiga matonge tu kwenye sahani ya chakula unaweza kutapika vipande vya utumbo wako na kuaga dunia bila kuchelewa. Akaanza kutapika nyongo hasa ukikumbuka alikula tokea jana yake jioni. Alikuwa sasa ametimiza saa 13 bila kutia chochote kitu tumboni.
Kisha akaanza kuhisi macho yake kuwa mazito, kwa mbali akaskia kengele imebonyezwa, kisha ndani ya dakika 3 wakaingia vijana wawili wakamfungua kwenye kiti na kumfunga tena kamba vizuri kisha wakambeba kama maiti kumtoa mule kwenye chumba cha mateso. Alichofanikiwa kusikia kwa mbali ni maneno ya kuwa "kamtupeni kwenye selo kubwa" kisha akapoteza fahamu kabisa.
IMG-20200517-WA0027.jpg


Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom