RIWAYA:CABO DELGADO-PART 18
Inspekta Mark alirudi nyuma nyuma, kama hatua tatu halafu akajifanya kama kajikwaa kitu anataka kuanguka kwa kuugongesha mguu wake wa kushoto juu ya mguu wake wa kulia kisha kama umeme akajibidua sarakasi hewani akatua miguu yake juu ya kifua cha Kachero Manu ambaye hakujiandaa na shambulio la ghafla na alikuwa anatembea kuingia chumbani.
Shambulio ambalo lilimwangusha kizembe mpaka chini na bastola yake mkononi ikadondoka chini. Haraka haraka Inspekta Mark akajizoa chini kuikimbilia bastola yake, Kachero Manu naye bila ajizi akainuka na kumpiga teke aina ya "SAVATE".
Huo ni upigaji wa teke ambao asili yake ni nchini Ufaransa. Huwa ukipigwa na fundi wa upigaji lazima utenguke kiungo labda uwe na bahati ya mtende kuota jangwani, na ndio hiyo bahati ilimkuta Mark. Hilo teke halikutua vizuri kwenye maungio ya goti liliteleza kidogo kutokana na kuwa katika mwendo wa kuiendea bastola yake ndio ikawa salama yake likamuangusha chini lakini akiwa na maumivu makali.
Akajikaza kisabuni akanyanyuka ghafla na kutupa makonde ya haraka haraka kama matatu, makonde mawili yakampata Kachero Manu kisawa sawa yakampasua kwenye kona ya mdomo. Damu zikaanza kuvuja taratibu, akarusha konde la tatu usawa wa jicho la kushoto la Kachero Manu, Kachero akalikwepa kiustadi mkubwa.
Mark akapatwa na wazo jipya baada ya kutambua Kachero Manu ni farisi katika fani ya mapambano, na asingeweza kumshinda kirahisi. Akaanza kurudi kinyumenyume mpaka akakaribia usawa wa dirisha la chumbani alilotumia kuingilia chumbani kwa Dr.Muganyizi.
Kachero Manu akadhani ni mbinu ya kujipanga kwa shambulio akasimama kwa umakini anamsubiria maana alitia akili Inspekta Jenerali Mark sio wa kawaida kwenye sanaa za mapigano.
Kumbe ile ilikuwa ni "janja ya jani kula hindi bichi", kama nyani vile aligeuka kwa haraka kwa kudandia kitanda kisha akaparamia dirisha la chumbani kwa Dr.Muganyizi alilotumia kuingilia akatokomea nje ya nyumba kisha akatimkia mtaani kwenye giza totoro.
Kachero Manu alisimama kama kapigwa ganzi alishangazwa na umahiri wa Inspekta Mark, hakutegemea kama Mark atamkimbia usiku ule. Akatanabahi kuwa Inspekta Mark atakuwa amepitia mafunzo makubwa sana ya sanaa za mapigano.
Alifahamu Mark hatoweza kuitumia gari yake kwa kuwa kaitoa upepo, lakini kwa kasi aliyotoka nayo hapa ingetosha kutafuta mbinu mbadala za kuondoa eneo lile. Akaamua aachane kwanza afahamu alipo Dr.Muganyizi maana ndio kipaumbele cha kwanza kumuokoa yeye na sio kumsaka Mark.
Kachero Manu akaiendea bastola yake akaiokota akamrudia yule kijana aliyefungwa kamba kwenye veranda. Akamfungua kamba zote na kisha akaanza kumuuliza, "wewe ni nani humu, pole sana.." alisema Kachero Manu.
”Mimi ni msaidizi wa kazi za nyumbani, kibarua wa Dr.Muganyizi” alijibu kijana Yule. ”Sasa Dr. kalala wapi usiku huu”? aliuliza Kachero Manu kiudadisi ili apate ukweli mahali alipo.
"Dr kasafiri kwenda Tanzania na ndege ya saa moja usiku wa kuamkia leo, kaenda kuangalia familia yake kipindi hiki cha mwezi wa mwezi wa pili katika mapumziko ya siku ya wapendano "Valentine Day". Kasema atarudi wiki ijayo” alimalizia maelezo yake kijana Yule.
Kachero Manu akatabasamu akajua Dr.Muganyizi bado siku zake za kuishi zipo sana hapa duniani, kakikwepa kifo chake mbele ya mtutu wa Inspekta Jenerali Mark. Pia akatambua Dr.Muganyizi safari zake zilikuwa za siri maana hata mamluki watoa taarifa kwa watu wa Alfredo wa kazini kwake hawakufahamu hiyo safari.
”OK.. kuwa na amani kijana endelea na maisha yako, ikiwezekana katoe taarifa kituo cha polisi, kwaheri...” akaondoka Kachero Manu bila kumpa nafasi yule kijana ya kujibu chochote, akatokomea zake nje ya nyumba, usiku ule kama wa saa tisa kasoro dakika kumi.
Huku ving'ora vya gari za polisi vikisikika kwa mbali akafahamu huenda majirani wametoa taarifa baada ya kusikia mlio wa risasi iliyomuua mlinzi wa nyumba ya Dr.Muganyizi au Mark kawashtua polisi waje kumtia mbaroni.
Akafanya haraka kupotea eneo lile ili asije kufanywa asusa kwenye jambo asilohusika nalo, wakamtoa kafara.














SURA YA KUMI
Kachero Manu aonyeshwa cha mtema kuni
Nyumba ya Dr.Muganyizi usiku huo ikazingirwa na mapolisi lukuki waliokuja kuchunguza mauaji yaliyotokea ndani ya nyumba hiyo.
Kachero alipotoka nyumbani kwa Dr.Muganyizi, akawa hajui anaelekea wapi maana hata eneo alilokuwepo alikuwa halijui linaitwaje kutokana ugeni wake. Kama ujuavyo "kuku mgeni hakosi kamba mguuni". Lakini akafanya haraka kuondoka eneo lile asije kukutwa na polisi akapewa kesi ya mauaji ikawa habari ingine tena.
Akatembea kwa muda wa kama robo saa kwa miguu. Akiwa anakata mitaa usiku huo, akakutana na "taksi bubu" moja inapiga tripu za mitaani. Akafanya maamuzi ya kuisimamisha kwa kuipungia mkono. Dereva yule akatii amri na kuisimamisha gari yake.
Alichomwambia dereva taksi yule ni kitu kimoja tu, apelekwe Nautilus Hoteli. Akafikishwa salama salimini hapo hotelini na ile taksi. Kabla hajashuka kwenye taksi bubu, akamuuliza dereva taksi, "wapi naweza kupata sehemu nzuri ya kulala lakini ya gharama ya kawaida hapa Naitilus hoteli ni matawi ya juu sana sipawezi" akadanganya wakati alikuwa na pesa sufufu za kumuwezesha kulala hata Hoteli ya nyota 5 hata kwa muda wa mwaka mzima.
Lengo lilikuwa ni kutopoteza muda na kutafuta sehemu ya haraka ya kulala ili asubuhi ikifika ajue anajipanga vipi kuwakabili mabaradhuli wa Alfredo. Haraka haraka dereva yule akajibu, "nenda "Pemba Magic Lodge" ipo kama kilometa 3 kutokea ufukwe wa Wimbi hapo ni sehemu tulivu huwezi kukosa nafasi usiku huu" alimalizia maelezo yake dereva taksi akitumia ulimi wake wa ulimbo kumnasa Kachero mtegoni.
Akalipa pesa aliyotajiwa akaingia ndani ya Nautilus Hoteli kuchukua gari yake ya kazi 'Volvo s60' aliyoacha maegesho ya magari tokea saa 3:05 usiku alipowasili eneo hilo. Gari ilikuwa imechafuka matope ya barabarani halitamaniki hata kuliangalia.
Alipolisogelea gari yake akatabasamu kwa jinsi ilivyofanikisha salama safari yake ya kumtoa Montepuez mpaka Pemba kwa muda mfupi sana, akamsifu kimoyomoyo Komandoo "JS" kwa kumchagulia gari lenye ufanisi mkubwa.
Akaingia ndani ya gari akawasha gari huku anaitafuta ilipo 'Pemba Magic Lodge' kwa kutumia mtandao wa simu yake ya mkononi, akarekebisha GPS yake kwenye simu ikawa inamuelekeza barabara za kupita mpaka kumuwezesha kufika karibu na ilipo 'Pemba Magic Lodge' ndani ya nusu saa tu kutokea Nautilus Hoteli.
Akiwa ndani ya gari bado hajang'oa nanga, akawasha Kompyuta yake mpakato kwa ajili ya kutuma taarifa ofisini za kuhusu Dr.Muganyizi. Taarifa aliyotuma ilieleza kuwa Daktari anatafutwa kwa udi na uvumba ili auliwe na Mafioso wa Cabo-Delgado, hivyo azuiwe asirudi kwanza nchini Msumbiji, asalie Tanzania mpaka hali ya usalama wake itakavyotengamaa.
Pia ahojiwe haraka ili kufahamu ni watu gani walikuwa wanahitaji kupewa tenda ya ujenzi wa barabara katika mradi wa "PEMOVACHA", na apewe ulinzi madhubuti yeye na familia yake.
Ikiwezekana alipendekeza wapelekwe mafichoni kwenye nyumba maalumu za usalama wa taifa 'safehouse' kuhofia mtandao mpana wa Alfredo kuwanyakua. Baada ya kutuma taarifa hiyo nyeti akazima kompyuta yake akahifadhi vizuri vifaa vyake muhimu kwenye sanduku dogo lililopo chini ya miguu ya kukanyagia breki.
Safari yake fupi ya kuelekea 'Pemba Magic Lodge' kwa ajili ya kulaza mbavu zake ikaanzaa, ili kesho yake aendeleze libeneke lake la kuwatafuta mahasimu zake. Baada ya muda wa nusu saa akawasili kwenye jengo moja jirani na Pemba Magic Lodge. Hisia zake hazikumtuma kabisa kuegesha gari lake hapo kwenye nyumba ya wageni. Akaamua kutii hisia zake bila kupingana nazo. Akafunga vizuri gari lake akashuka na kamzigo chake cha nguo chache.
Alichokuwa hajui Kachero Manu ni kuwa ile "taksi bubu" iliyombeba maeneo ya nyumbani kwa Dr.Muganyizi, ilikuwa ni ya mmoja wa wakala wa Inspekta Jenerali Mark. Baada ya Mark kufanikiwa kumtoroka Kachero nyumbani kwa Dr.Muganyizi alitoa taarifa kwa wakubwa wake juu ya ujio wa Kachero Manu katika Mji wa Pemba, na namna alivyopambana nae kindakindaki nyumbani kwa Dr.Muganyizi.
Ikapangwa mikakati kabambe ya kumkamata kupitia 'taksi bubu' na nyumba za kulala wageni zote usiku huo. Pia ulinzi wa barabarani uliimarishwa vilivyo ili asiweze kuwatoroka tena. Zikasambazwa 'taksi bubu' zaidi ya 20 usiku ule zikijifanya zinatoa huduma kwa watembea kwa miguu usiku ule.
Yule dereva alivyomuacha Kachero Manu pale nje ya Naitilus Hoteli alipeleka taarifa moja kwa moja juu ya Kachero Manu kuwa atafikia 'Pemba Magic Lodge'. Hivyo hiyo ikachaguliwa kuwa ni sehemu muafaka kufanyia Umafia wao usiku ule.
Kingine kilichompa uhakika dereva taksi juu ya
Sent using
Jamii Forums mobile app