mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 919
- 2,007
- Thread starter
- #61
RIWAYA: CABO DELGADO-PART 21
SURA YA KUMI NA MBILI
"Mjue Daktari wa handaki la mateso"
Moja ya kazi ambayo ina miiko yake madhubuti hapa duniani ukiachilia kazi ya Ualimu basi ni kazi ya Udaktari. Ni kazi ambayo siku ya mwisho ya kuhitimu elimu hiyo, madaktari hula kiapo cha utii wa maadili ya kazi yao.
Kiapo ambacho huwa kinawafunga kutenda kazi zao kwa kufuata weledi wa kazi yao hiyo kwa kuwataka kuwahudumia wagonjwa wao bila ubaguzi, wawe na moyo wa huruma na uvumilivu na kutanguliza kuokoa uhai wa wagonjwa wao kwa gharama yoyote.
Ni kazi ya wito ambayo hautakiwi kutanguliza maslahi yako binafsi, kazi ya udaktari ni kama vile umechagua kifo ni bora kwako kuliko uhai, ndio maana ukitokea mlipuko wa ugonjwa wowote wa hatari wa kuambukiza kama "Ebola", "Covid-19" na mengineyo huwezi kusikia madaktari wametoka nduki na kuwatelekeza wagonjwa wao hospitalini.
Sasa ukiona mtu ni daktari kama alivyo Dr.Anabella anashirikiana na wahalifu kwa kutoa huduma kwa wagonjwa na amepewa Cheo kama "Daktari wa Mateso", kengele ya tahadhari lazima ilie kichwani mwako.
Lazima utajiuliza zaidi ya mara mbili, "huyu daktari anaijua kweli miiko ya kazi yake au anatanguliza mbele maslahi yake binafsi au nini kimemsibu mpaka anashirikiana na wahalifu?". Lakini kumbe mazonge na maswahibu tunayokumbana hapa duniani huwa kuna wakati yanawabadilisha watu wema kuwa waovu na waovu kuwa wema.
Mfano wapo watu hapo zamani walikuwa majambazi, walawiti, wanyang'anyi lakini wakarejea kumtumikia Mungu wao baada ya kupatwa na ajali, au magonjwa yasiyotibika. Na wapo watu ambao zamani walikuwa swalihina sana, kwenye nyumba za ibada hawakosekani, wanashinda mahospitalini kuangalia wagonjwa, wanatoa zaka na sadaka kila wakati lakini misukosuko ya walimwengu iliyowasibu ikawabadilisha na kuwafanya wawe watu waovu maishani, Ibilisi mwenyewe ambaye ni Shetani Mkuu anasubiri nyuma.
Nakama na misukosuko aliyokumbana nao maishani mwake, Dr.Anabella pamoja na familia yake ndio iliyomsababisha ajiunge na kundi hili ovu na katili la NACATANAS linaloongozwa na Inspekta Jenerali Mark Noble.
Dr."Anabella Julio" ni mzaliwa wa kijiji cha Nthoro katika wilaya ya Montepuez, nchini Msumbiji. Alizaliwa mwaka 1979 miaka minne tokea kupatikana uhuru wa Msumbiji. Alimaliza masomo yake ya udaktari wa binadamu katika chuo kikuu cha "The Eduardo Mondlane University" kilichopo ndani ya viunga vya Jiji la Maputo, nchini Msumbiji. Hicho ndio Chuo Kikuu kikubwa zaidi nchini Msumbiji kikiwa na uwezo wa kudahili wanafunzi takribani elfu 40 katika kila mwaka wa masomo.
Baba yake mzazi, Mzee "Julio Munambo" alikuwa ni mkulima mdogo wa mihogo na korosho. Ni Mzee ambaye amewahi kuishi Tanzania kwa miaka 13 mtawalia katika kambi ya wakimbizi ya Rutamba mkoani Lindi. Hiyo ilikuwa ni kati ya mwaka 1971-1984.
Alitoroka Msumbiji kama mkimbizi na kuja kuishi Tanzania, kipindi cha vita baina ya Wareno na Wapigania Uhuru wa FRELIMO. Baada ya uhuru wa Msumbiji uliopatikana mwaka 1975, Mzee Mnambo alikuwa ana mipango ya kurudi nyumbani akalijenge Taifa lake changa. Ila vilipoibuka vita ya wenyewe kwa wenyewe baada ya Uhuru kati ya vyama hasimu nchini Msumbiji, chama cha RENAMO na FRELIMO akakata shauri la kuendelea kubakia Tanzania mpaka amani ya kweli ipatikane nchini Msumbiji.
Dr.Anabella, kifungua mimba wa Mzee Mnambo, akawa ni mhanga wa sarakasi zisizokoma baina ya FRELIMO na RENAMO. Akajikuta anazaliwa na kukulia ukimbizini nchini Tanzania bila hata kuwahi kunusa harufu ya udongo wa nchi yake ya asili. Sarakasi ambazo zilizaa Mkataba wa NKOMAT na kusababisha Dr.Anabella anapelekwa nchini Msumbiji na baba yake kwa mara ya kwanza katika maisha yake.
Chama cha RENAMO kiliundwa mwaka 1975 kilikuwa kikipinga sera za ukomonisti za chama tawala cha FRELIMO. Chama hiki kilianzishwa kwa msaada wa serikali ya wazungu wa Rhodesia (Zimbabwe) na serikali ya makaburu wa Afrika ya Kusini.
Lengo la wazungu kuanzisha na kuipa misaada RENAMO ilikuwa ni kuivunja nguvu serikali ya Msumbiji inayoongozwa na FRELIMO kuwasaidia wapigania uhuru wa Afrika ya kusini na Zimbabwe. Baada ya uhuru yakaibuka mapigano ya wenyewe kwa wenyewe nchini Msumbiji kati ya chama cha FRELIMO na RENAMO, mapigano ambayo yalikuwa ni janga la kimataifa kwa wapenda amani na uhuru wote duniani.
Miundo mbinu kama shule, vyuo, hospitali na barabara ziliharibiwa, wananchi waliuliwa na kuchinjwa ovyo kama kuku, huku wengine wakiambulia ulemavu wa maisha na maelfu kwa maelfu ya wakazi wa Msumbiji hasa waishio kaskazini walitorokea nchini Tanzania kama wakimbizi.
Duniani tumepata kuona na kusikia vikundi mbalimbali vya waasi ambao ni wakatili kama Talebani wa kule nchini Afghanistani, au Al-Shabaab wa kule Somalia na makundi mengineyo lakini hawafikii hata robo ya ukatili wa askari wa RENAMO, waasi hao walikuwa kiboko yao.
Katika baadhi ya simulizi za kuelezea ukatili wao zinasema ulikuwa ukikamatwa na waasi wa RENAMO kama ukiwa adui yao unaulizwa swali kwa lugha ya Kimakonde "ulambela kununa au kusunala"? (Unachagua kununa au kucheka). Ukichagua kununa unatobolewa mdomo wa juu na wa chini kisha unafungwa na kufuli, ukichagua kucheka unakatwa midomo ya juu na chini.
FRELIMO ilifanya makosa kadhaa ya kiufundi yaliyowafanya wakazi wa upande wa Kaskazini mwa nchi kuiunga mkono RENAMO licha ya kwamba walitambua kuwa sio kundi sahihi kwao. Moja ya makosa yaliyofanywa na FRELIMO baada ya nchi kupata uhuru ni kunyakua nafasi nyingi za juu za uongozi na kuwapatia watu wa kusini mwa Msumbiji, hivyo watu wa kaskazini kujiona kama ni watoto wa kambo. Wametengwa ndani ya nchi yao waliyoipigania uhuru wake kwa kuvuja jasho na damu, kwa kupoteza uhai na mali zao.
Pia sera za Ukomonisti zilitekelezwa vibaya na baadhi ya viongozi wa FRELIMO. Mpaka ikafikia hatua baadhi yao kuamuru makanisa na misikiti ifungwe kwa kigezo cha kwamba Msumbiji ni nchi ya kisekula isiyo na dini yoyote. Maelfu ya viongozi wa dini walinyanyaswa na kuteswa mpaka wengineo kuikimbia nchi yao ya Msumbiji.
Zipo taarifa ambazo zinaenezwa sana na wafuasi wa RENAMO kuwa mmoja wa viongozi wa juu kabisa wa FRELIMO alipata kuingia kanisani siku moja na nyundo yake mkononi inapepea hewani kama kishada. Kwa kutumia nyundo ile akavunjavunja 'Altare' siku ya Ibada ya Jumapili huku waumini wamejaa pomoni kanisani na kutangaza Msumbiji hairuhusu ibada zozote.
Mapigano kati ya makundi haya hasimu, FRELIMO na RENAMO yalizidi kushika moto zaidi mara baada ya Maafisa wa usalama wa serikali ya Msumbiji kumuua Bwana "André Matsangaissa" kiongozi mkuu wa RENAMO. Bwana Matsangaissa mwanzoni alijiunga na FRELIMO mwaka 1972 kisha baada ya uhuru mwaka 1975 aliajiriwa kama mwanajeshi akapewa cheo cha "Mfawidhi Mkuu wa Kikosi" (quartermaster).
Kituo chake cha kazi kilikuwa maeneo ya Dondo karibu na Beira, akihusika na manunuzi, uhifadhi na ugawaji wa vifaa vya jeshi. Baada ya muda mfupi tu akafukuzwa kazi akituhumiwa kwa wizi kisha akapelekwa jela ya Gorongosa.
Sasa mwaka 1977 kambi ya Gorongosa ikavamiwa na wazungu wa Rhodesia wakamtorosha Bwana "André Matsangaissa" wakaenda nae Rhodesia baadae akatangazwa kama mkuu wa kikundi cha RENAMO.
Kwa hiyo FRELIMO wakawa wanapambana na mtu ambaye anawajua nje ndani katika medani zao za kivita, ni kama kinyago walichokichonga wenyewe kinawatisha sasa.
Amani ya kwanza kati ya FRELIMO na RENAMO ilianza kupatikana tarehe 16 mwezi Machi mwaka 1984 kuliposainiwa mkataba maarufu unaitwa "NKOMAT ACCORD". Mkataba huu ulikuwa ni kati ya serikali ya Msumbiji ikiwakilishwa na Rais Samora Machel na Waziri Mkuu wa serikali ya kikaburu ya Afrika ya Kusini kipindi hicho Bwana P. W. Botha.
Huyu Kaburu Botha ndiye ambaye wazalendo weusi wa Afrika ya kusini wanamuita kwa jina la utani la "The great crocodile". Ile miaka ambayo watoto wa shule wanapigwa risasi hadharani 1976 huko Afrika ya kusini, na mpaka filamu maarufu ya Sarafina ikaigiza tukio hilo la kinyama, huyu Bwana mkubwa Botha alikuwa ndio Waziri wa ulinzi na baadae kuanzia mwaka 1984-1989 alikuja kuwa Rais wa Afrika ya kusini.
Huyu ndio ndio mhandisi aliyeufuma na kuusuka vilivyo mkataba wa NKOMAT. Mkataba huo uliweka matakwa ya serikali ya Msumbiji kuacha kusaidia wapigania uhuru wa Afrika ya kusini wa chama cha "African National Congress"(ANC), pia uliwataka serikali ya makaburu kuacha kuwapa msaada wa vifaa na pesa chama cha upinzani cha RENAMO.
Mkataba huu ulikuwa ni pigo takatifu kwa wapigania uhuru wa ANC na nchi zote zilizokuwa zinazosaidia kupatikana kwa uhuru wa Afrika ya kusini.
Siku ya kusainiwa kwa mkataba huo, Marais wote wa SADC kuanzia Mwalimu Nyerere, Keneth Kaunda na wenzao walisusia mkataba huu hawakutokea kwenye sherehe licha ya kwamba Rais wa Msumbiji Bwana Samora aliwapa mualiko.
Waliona ni kama vile Rais Samora amewasaliti, amekuwa mbinafsi kwa kujali maslahi yake kwa kuamua kukaa meza moja na adui yake wanafaidi mapochopocho na mahanjumati wakati wapigania uhuru wenzao wa nchini Afrika ya Kusini wanateseka.
Baada ya mkataba wa NKOMAT kusainiwa, Mzee "Julio Martine Munambo", baba wa Dr.Anabella aliamua kurejea nchini Msumbij. Akiambatana na mkewe, Binti yake mkubwa, Anabella, na wadogo zake Anabella wakiume wawili, Munambo Jr na Athanas. Hawa watoto wote walikuwa wanarejea Msumbiji kwa mara ya kwanza, kwa maana walizaliwa katika kambi ya wakimbizi hawaijui hata Msumbiji inafananaje kimuonekano.
Mzee Julio Munambo akaanza maisha mapya katika kijiji chao cha asili ya mababu zake cha "Nthoro".
Kipindi hicho kulikuwa na watu wachache vijijini, wengi wao wakiwa wamekimbia kutokana na mfumo ulioachwa na RENAMO vijijini unaoitwa "Gandira". Mfumo huo ulitaka vijiji viwe vinazalisha chakula kwa ajili ya wapiganaji wa RENAMO, pia wanakijiji wahusike kusafirisha bidhaa na silaha za RENAMO na pia wanawake wa kijiji baadhi yao wawe ni watumwa wa kingono wa wanajeshi wa RENAMO.
Kipindi hicho cha miaka ya 1980's chama cha RENAMO kilikuwa kina nguvu zaidi katika Majimbo ya Kaskazini na Mashariki kuliko hata FRELIMO. Sasa huu mfumo wa Gandira ulikuwa unasababisha baadhi ya wanakijiji wakimbilie tena Tanzania hasa msimu wa kilimo kwenda kufanya vibarua katika mashamba ya wanakijiji wa mpakani ili wafaidike na jasho lao.
Watanzania walikuwa wakiwapata hawa vibarua wanashangilia maana "Wamakonde" wa Msumbiji kwa uhodari wao wa kulima waliwapa lakabu ya "trekta", hawachoki kwa haraka wakiingia shambani.
Katika mazingira magumu hayo hayo aliyoyakuta Mzee Julio alihamasisha na kuamsha ari mpya na nguvu mpya kwa wanakijiji wenzake akiwaelekeza namna nzuri ya kuboresha maisha yao na kuwa bora kupitia kilimo. Hasa ukichukulia ametoka kuishi maisha ya kambini ambayo ni maisha ya nidhamu na utiifu kama shuleni.
Pia alijifunza mfumo wa uendeshaji wa vijiji vya Ujamaa na Kujitegemea kutoka Tanzania alipoishi kwa muda mrefu hivyo mpaka kufika mwaka 1992 wakati wa mkataba wa kusitisha mapigano ya yenyewe kwa wenyewe kati ya FRELIMO na RENAMO unasainiwa. Ndani ya muda mfupi kwa hamasa na ushawishi wa Mzee Julio Munambo, kijiji cha "Nthoro" kikawa ni kijiji cha kupigiwa mfano kwa katika namna ya kujiletea maendeleo yao, kati ya vijiji vyote vya Jimbo la Cabo-Delgado.
Kwa umoja wao walijenga shule ya msingi hapo hapo kijiji kwao, shule ambayo ndio Dr.Anabella alianzia hapo darasa la kwanza mwaka 1989 na kumaliza 1995. Mwanzoni masomo yalikuwa magumu kwa Dr.Anabella kwa sababu yalikuwa yanafundishwa kwa lugha ya Kireno na sio kwa lugha yake ya asili ya kimakonde, lakini baada ya muda mfupi alikuwa anaongea kireno kizuri kana kwamba kazaliwa katika viunga vya "Lisbon" huko nchini Ureno.
Alipomaliza elimu yake ya msingi akafaulu kwenda kusoma sekondari katika shule ya sekondari Montepuez. Alisoma hapo kwa muda wa miaka mitano mfululizo. Kwa mfumo wa elimu ya nchi ya Msumbiji, elimu ya sekondari imegawanywa mafungu mawili, kidato cha kwanza mpaka cha tatu mwisho halafu ukifaulu unaendelea kidato cha tano na cha sita kwa muda wa miaka miwili.
Alivyomaliza sekondari alifaulu vizuri sana, alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi kumi bora kwa jimbo zima la Cabo-Delgado na akiwa ni wa kwanza katika wilaya yake ya Montepuez. Siku ya kutoka kwa matokeo na kujulikana kuwa binti yao mpendwa Anabella kachaguliwa Chuo kikuu bora kuliko vyote nchini Msumbiji cha 'Eduardo Mondlane' kusomea Shahada ya Udaktari wa Binadamu "Doctor of Medicine" ilikuwa ni hoihoi, shangwe, nderemo, vigeregere na vifijo kijijini kizima.
Walimuona kama ndio mkombozi wao kielimu atakayekuja kuwatoa kwenye utumwa wa umasikini uliotopea na kuwaletea maisha bora kwa kutumia kipawa chake cha elimu.
Furaha ya kusomea udaktari Dr. Anabella ilitumbukia nyongo kuanzia mwaka 2008 akiwa ndio yupo mwaka wa mwisho wa masomo yake. Hiyo ni baada ya kuwa wazazi yake hawapatikani mara kwa mara kwenye simu ya mkononi kama alivyozoea kuwasiliana nao. Na siku akibahatika kuongea na baba yake basi alikuwa anaonekana ni kama mtu mwenye wasiwasi mwingi. Kama vile kulikuwa kuna kitu wanamficha binti yao wakihofia wasije wakamchanganya kwenye masomo yake.
Subira yavuta heri, Aliweka nia thabiti moyoni mwake, Dr. Anabella kuwa akimaliza masomo yake ataenda kijijini kwao kiguu na njia kutafiti nini kinachowasibu wazazi wake haswa. Na kama akikuta kuna matatizo yasiyotatulika kwa haraka itabidi awachukue wazazi wake na kwenda kuishi nao katika Jiji la Maputo. Huko ndio alipanga aendeshe maisha yake baada ya kumaliza Chuo Kikuu. Ingawa alijua ni ngumu sana kwa baba yake mzazi kukubali kuondoka kijiji cha Nthoro, kijiji ambacho ameshiriki kwa asilimia nyingi kukipa hadhi inayoonekana leo akiwa kama muasisi.
Alikuwa anatamani arudi kijijini mara kwa mara ila umbali ulikuwa ni kikwazo kikubwa. Kutoka Maputo mpaka Montepuez kwa usafiri wa gari ni zaidi ya saa 35, na kulipa nauli ya ndege ambayo angetumia saa 2 tu hakuwa nazo hizo pesa, hivyo ikawa kila mwaka anarudi mara moja nyumbani kusalimia familia yake.












Sent using Jamii Forums mobile app
SURA YA KUMI NA MBILI
"Mjue Daktari wa handaki la mateso"
Moja ya kazi ambayo ina miiko yake madhubuti hapa duniani ukiachilia kazi ya Ualimu basi ni kazi ya Udaktari. Ni kazi ambayo siku ya mwisho ya kuhitimu elimu hiyo, madaktari hula kiapo cha utii wa maadili ya kazi yao.
Kiapo ambacho huwa kinawafunga kutenda kazi zao kwa kufuata weledi wa kazi yao hiyo kwa kuwataka kuwahudumia wagonjwa wao bila ubaguzi, wawe na moyo wa huruma na uvumilivu na kutanguliza kuokoa uhai wa wagonjwa wao kwa gharama yoyote.
Ni kazi ya wito ambayo hautakiwi kutanguliza maslahi yako binafsi, kazi ya udaktari ni kama vile umechagua kifo ni bora kwako kuliko uhai, ndio maana ukitokea mlipuko wa ugonjwa wowote wa hatari wa kuambukiza kama "Ebola", "Covid-19" na mengineyo huwezi kusikia madaktari wametoka nduki na kuwatelekeza wagonjwa wao hospitalini.
Sasa ukiona mtu ni daktari kama alivyo Dr.Anabella anashirikiana na wahalifu kwa kutoa huduma kwa wagonjwa na amepewa Cheo kama "Daktari wa Mateso", kengele ya tahadhari lazima ilie kichwani mwako.
Lazima utajiuliza zaidi ya mara mbili, "huyu daktari anaijua kweli miiko ya kazi yake au anatanguliza mbele maslahi yake binafsi au nini kimemsibu mpaka anashirikiana na wahalifu?". Lakini kumbe mazonge na maswahibu tunayokumbana hapa duniani huwa kuna wakati yanawabadilisha watu wema kuwa waovu na waovu kuwa wema.
Mfano wapo watu hapo zamani walikuwa majambazi, walawiti, wanyang'anyi lakini wakarejea kumtumikia Mungu wao baada ya kupatwa na ajali, au magonjwa yasiyotibika. Na wapo watu ambao zamani walikuwa swalihina sana, kwenye nyumba za ibada hawakosekani, wanashinda mahospitalini kuangalia wagonjwa, wanatoa zaka na sadaka kila wakati lakini misukosuko ya walimwengu iliyowasibu ikawabadilisha na kuwafanya wawe watu waovu maishani, Ibilisi mwenyewe ambaye ni Shetani Mkuu anasubiri nyuma.
Nakama na misukosuko aliyokumbana nao maishani mwake, Dr.Anabella pamoja na familia yake ndio iliyomsababisha ajiunge na kundi hili ovu na katili la NACATANAS linaloongozwa na Inspekta Jenerali Mark Noble.
Dr."Anabella Julio" ni mzaliwa wa kijiji cha Nthoro katika wilaya ya Montepuez, nchini Msumbiji. Alizaliwa mwaka 1979 miaka minne tokea kupatikana uhuru wa Msumbiji. Alimaliza masomo yake ya udaktari wa binadamu katika chuo kikuu cha "The Eduardo Mondlane University" kilichopo ndani ya viunga vya Jiji la Maputo, nchini Msumbiji. Hicho ndio Chuo Kikuu kikubwa zaidi nchini Msumbiji kikiwa na uwezo wa kudahili wanafunzi takribani elfu 40 katika kila mwaka wa masomo.
Baba yake mzazi, Mzee "Julio Munambo" alikuwa ni mkulima mdogo wa mihogo na korosho. Ni Mzee ambaye amewahi kuishi Tanzania kwa miaka 13 mtawalia katika kambi ya wakimbizi ya Rutamba mkoani Lindi. Hiyo ilikuwa ni kati ya mwaka 1971-1984.
Alitoroka Msumbiji kama mkimbizi na kuja kuishi Tanzania, kipindi cha vita baina ya Wareno na Wapigania Uhuru wa FRELIMO. Baada ya uhuru wa Msumbiji uliopatikana mwaka 1975, Mzee Mnambo alikuwa ana mipango ya kurudi nyumbani akalijenge Taifa lake changa. Ila vilipoibuka vita ya wenyewe kwa wenyewe baada ya Uhuru kati ya vyama hasimu nchini Msumbiji, chama cha RENAMO na FRELIMO akakata shauri la kuendelea kubakia Tanzania mpaka amani ya kweli ipatikane nchini Msumbiji.
Dr.Anabella, kifungua mimba wa Mzee Mnambo, akawa ni mhanga wa sarakasi zisizokoma baina ya FRELIMO na RENAMO. Akajikuta anazaliwa na kukulia ukimbizini nchini Tanzania bila hata kuwahi kunusa harufu ya udongo wa nchi yake ya asili. Sarakasi ambazo zilizaa Mkataba wa NKOMAT na kusababisha Dr.Anabella anapelekwa nchini Msumbiji na baba yake kwa mara ya kwanza katika maisha yake.
Chama cha RENAMO kiliundwa mwaka 1975 kilikuwa kikipinga sera za ukomonisti za chama tawala cha FRELIMO. Chama hiki kilianzishwa kwa msaada wa serikali ya wazungu wa Rhodesia (Zimbabwe) na serikali ya makaburu wa Afrika ya Kusini.
Lengo la wazungu kuanzisha na kuipa misaada RENAMO ilikuwa ni kuivunja nguvu serikali ya Msumbiji inayoongozwa na FRELIMO kuwasaidia wapigania uhuru wa Afrika ya kusini na Zimbabwe. Baada ya uhuru yakaibuka mapigano ya wenyewe kwa wenyewe nchini Msumbiji kati ya chama cha FRELIMO na RENAMO, mapigano ambayo yalikuwa ni janga la kimataifa kwa wapenda amani na uhuru wote duniani.
Miundo mbinu kama shule, vyuo, hospitali na barabara ziliharibiwa, wananchi waliuliwa na kuchinjwa ovyo kama kuku, huku wengine wakiambulia ulemavu wa maisha na maelfu kwa maelfu ya wakazi wa Msumbiji hasa waishio kaskazini walitorokea nchini Tanzania kama wakimbizi.
Duniani tumepata kuona na kusikia vikundi mbalimbali vya waasi ambao ni wakatili kama Talebani wa kule nchini Afghanistani, au Al-Shabaab wa kule Somalia na makundi mengineyo lakini hawafikii hata robo ya ukatili wa askari wa RENAMO, waasi hao walikuwa kiboko yao.
Katika baadhi ya simulizi za kuelezea ukatili wao zinasema ulikuwa ukikamatwa na waasi wa RENAMO kama ukiwa adui yao unaulizwa swali kwa lugha ya Kimakonde "ulambela kununa au kusunala"? (Unachagua kununa au kucheka). Ukichagua kununa unatobolewa mdomo wa juu na wa chini kisha unafungwa na kufuli, ukichagua kucheka unakatwa midomo ya juu na chini.
FRELIMO ilifanya makosa kadhaa ya kiufundi yaliyowafanya wakazi wa upande wa Kaskazini mwa nchi kuiunga mkono RENAMO licha ya kwamba walitambua kuwa sio kundi sahihi kwao. Moja ya makosa yaliyofanywa na FRELIMO baada ya nchi kupata uhuru ni kunyakua nafasi nyingi za juu za uongozi na kuwapatia watu wa kusini mwa Msumbiji, hivyo watu wa kaskazini kujiona kama ni watoto wa kambo. Wametengwa ndani ya nchi yao waliyoipigania uhuru wake kwa kuvuja jasho na damu, kwa kupoteza uhai na mali zao.
Pia sera za Ukomonisti zilitekelezwa vibaya na baadhi ya viongozi wa FRELIMO. Mpaka ikafikia hatua baadhi yao kuamuru makanisa na misikiti ifungwe kwa kigezo cha kwamba Msumbiji ni nchi ya kisekula isiyo na dini yoyote. Maelfu ya viongozi wa dini walinyanyaswa na kuteswa mpaka wengineo kuikimbia nchi yao ya Msumbiji.
Zipo taarifa ambazo zinaenezwa sana na wafuasi wa RENAMO kuwa mmoja wa viongozi wa juu kabisa wa FRELIMO alipata kuingia kanisani siku moja na nyundo yake mkononi inapepea hewani kama kishada. Kwa kutumia nyundo ile akavunjavunja 'Altare' siku ya Ibada ya Jumapili huku waumini wamejaa pomoni kanisani na kutangaza Msumbiji hairuhusu ibada zozote.
Mapigano kati ya makundi haya hasimu, FRELIMO na RENAMO yalizidi kushika moto zaidi mara baada ya Maafisa wa usalama wa serikali ya Msumbiji kumuua Bwana "André Matsangaissa" kiongozi mkuu wa RENAMO. Bwana Matsangaissa mwanzoni alijiunga na FRELIMO mwaka 1972 kisha baada ya uhuru mwaka 1975 aliajiriwa kama mwanajeshi akapewa cheo cha "Mfawidhi Mkuu wa Kikosi" (quartermaster).
Kituo chake cha kazi kilikuwa maeneo ya Dondo karibu na Beira, akihusika na manunuzi, uhifadhi na ugawaji wa vifaa vya jeshi. Baada ya muda mfupi tu akafukuzwa kazi akituhumiwa kwa wizi kisha akapelekwa jela ya Gorongosa.
Sasa mwaka 1977 kambi ya Gorongosa ikavamiwa na wazungu wa Rhodesia wakamtorosha Bwana "André Matsangaissa" wakaenda nae Rhodesia baadae akatangazwa kama mkuu wa kikundi cha RENAMO.
Kwa hiyo FRELIMO wakawa wanapambana na mtu ambaye anawajua nje ndani katika medani zao za kivita, ni kama kinyago walichokichonga wenyewe kinawatisha sasa.
Amani ya kwanza kati ya FRELIMO na RENAMO ilianza kupatikana tarehe 16 mwezi Machi mwaka 1984 kuliposainiwa mkataba maarufu unaitwa "NKOMAT ACCORD". Mkataba huu ulikuwa ni kati ya serikali ya Msumbiji ikiwakilishwa na Rais Samora Machel na Waziri Mkuu wa serikali ya kikaburu ya Afrika ya Kusini kipindi hicho Bwana P. W. Botha.
Huyu Kaburu Botha ndiye ambaye wazalendo weusi wa Afrika ya kusini wanamuita kwa jina la utani la "The great crocodile". Ile miaka ambayo watoto wa shule wanapigwa risasi hadharani 1976 huko Afrika ya kusini, na mpaka filamu maarufu ya Sarafina ikaigiza tukio hilo la kinyama, huyu Bwana mkubwa Botha alikuwa ndio Waziri wa ulinzi na baadae kuanzia mwaka 1984-1989 alikuja kuwa Rais wa Afrika ya kusini.
Huyu ndio ndio mhandisi aliyeufuma na kuusuka vilivyo mkataba wa NKOMAT. Mkataba huo uliweka matakwa ya serikali ya Msumbiji kuacha kusaidia wapigania uhuru wa Afrika ya kusini wa chama cha "African National Congress"(ANC), pia uliwataka serikali ya makaburu kuacha kuwapa msaada wa vifaa na pesa chama cha upinzani cha RENAMO.
Mkataba huu ulikuwa ni pigo takatifu kwa wapigania uhuru wa ANC na nchi zote zilizokuwa zinazosaidia kupatikana kwa uhuru wa Afrika ya kusini.
Siku ya kusainiwa kwa mkataba huo, Marais wote wa SADC kuanzia Mwalimu Nyerere, Keneth Kaunda na wenzao walisusia mkataba huu hawakutokea kwenye sherehe licha ya kwamba Rais wa Msumbiji Bwana Samora aliwapa mualiko.
Waliona ni kama vile Rais Samora amewasaliti, amekuwa mbinafsi kwa kujali maslahi yake kwa kuamua kukaa meza moja na adui yake wanafaidi mapochopocho na mahanjumati wakati wapigania uhuru wenzao wa nchini Afrika ya Kusini wanateseka.
Baada ya mkataba wa NKOMAT kusainiwa, Mzee "Julio Martine Munambo", baba wa Dr.Anabella aliamua kurejea nchini Msumbij. Akiambatana na mkewe, Binti yake mkubwa, Anabella, na wadogo zake Anabella wakiume wawili, Munambo Jr na Athanas. Hawa watoto wote walikuwa wanarejea Msumbiji kwa mara ya kwanza, kwa maana walizaliwa katika kambi ya wakimbizi hawaijui hata Msumbiji inafananaje kimuonekano.
Mzee Julio Munambo akaanza maisha mapya katika kijiji chao cha asili ya mababu zake cha "Nthoro".
Kipindi hicho kulikuwa na watu wachache vijijini, wengi wao wakiwa wamekimbia kutokana na mfumo ulioachwa na RENAMO vijijini unaoitwa "Gandira". Mfumo huo ulitaka vijiji viwe vinazalisha chakula kwa ajili ya wapiganaji wa RENAMO, pia wanakijiji wahusike kusafirisha bidhaa na silaha za RENAMO na pia wanawake wa kijiji baadhi yao wawe ni watumwa wa kingono wa wanajeshi wa RENAMO.
Kipindi hicho cha miaka ya 1980's chama cha RENAMO kilikuwa kina nguvu zaidi katika Majimbo ya Kaskazini na Mashariki kuliko hata FRELIMO. Sasa huu mfumo wa Gandira ulikuwa unasababisha baadhi ya wanakijiji wakimbilie tena Tanzania hasa msimu wa kilimo kwenda kufanya vibarua katika mashamba ya wanakijiji wa mpakani ili wafaidike na jasho lao.
Watanzania walikuwa wakiwapata hawa vibarua wanashangilia maana "Wamakonde" wa Msumbiji kwa uhodari wao wa kulima waliwapa lakabu ya "trekta", hawachoki kwa haraka wakiingia shambani.
Katika mazingira magumu hayo hayo aliyoyakuta Mzee Julio alihamasisha na kuamsha ari mpya na nguvu mpya kwa wanakijiji wenzake akiwaelekeza namna nzuri ya kuboresha maisha yao na kuwa bora kupitia kilimo. Hasa ukichukulia ametoka kuishi maisha ya kambini ambayo ni maisha ya nidhamu na utiifu kama shuleni.
Pia alijifunza mfumo wa uendeshaji wa vijiji vya Ujamaa na Kujitegemea kutoka Tanzania alipoishi kwa muda mrefu hivyo mpaka kufika mwaka 1992 wakati wa mkataba wa kusitisha mapigano ya yenyewe kwa wenyewe kati ya FRELIMO na RENAMO unasainiwa. Ndani ya muda mfupi kwa hamasa na ushawishi wa Mzee Julio Munambo, kijiji cha "Nthoro" kikawa ni kijiji cha kupigiwa mfano kwa katika namna ya kujiletea maendeleo yao, kati ya vijiji vyote vya Jimbo la Cabo-Delgado.
Kwa umoja wao walijenga shule ya msingi hapo hapo kijiji kwao, shule ambayo ndio Dr.Anabella alianzia hapo darasa la kwanza mwaka 1989 na kumaliza 1995. Mwanzoni masomo yalikuwa magumu kwa Dr.Anabella kwa sababu yalikuwa yanafundishwa kwa lugha ya Kireno na sio kwa lugha yake ya asili ya kimakonde, lakini baada ya muda mfupi alikuwa anaongea kireno kizuri kana kwamba kazaliwa katika viunga vya "Lisbon" huko nchini Ureno.
Alipomaliza elimu yake ya msingi akafaulu kwenda kusoma sekondari katika shule ya sekondari Montepuez. Alisoma hapo kwa muda wa miaka mitano mfululizo. Kwa mfumo wa elimu ya nchi ya Msumbiji, elimu ya sekondari imegawanywa mafungu mawili, kidato cha kwanza mpaka cha tatu mwisho halafu ukifaulu unaendelea kidato cha tano na cha sita kwa muda wa miaka miwili.
Alivyomaliza sekondari alifaulu vizuri sana, alikuwa ni miongoni mwa wanafunzi kumi bora kwa jimbo zima la Cabo-Delgado na akiwa ni wa kwanza katika wilaya yake ya Montepuez. Siku ya kutoka kwa matokeo na kujulikana kuwa binti yao mpendwa Anabella kachaguliwa Chuo kikuu bora kuliko vyote nchini Msumbiji cha 'Eduardo Mondlane' kusomea Shahada ya Udaktari wa Binadamu "Doctor of Medicine" ilikuwa ni hoihoi, shangwe, nderemo, vigeregere na vifijo kijijini kizima.
Walimuona kama ndio mkombozi wao kielimu atakayekuja kuwatoa kwenye utumwa wa umasikini uliotopea na kuwaletea maisha bora kwa kutumia kipawa chake cha elimu.
Furaha ya kusomea udaktari Dr. Anabella ilitumbukia nyongo kuanzia mwaka 2008 akiwa ndio yupo mwaka wa mwisho wa masomo yake. Hiyo ni baada ya kuwa wazazi yake hawapatikani mara kwa mara kwenye simu ya mkononi kama alivyozoea kuwasiliana nao. Na siku akibahatika kuongea na baba yake basi alikuwa anaonekana ni kama mtu mwenye wasiwasi mwingi. Kama vile kulikuwa kuna kitu wanamficha binti yao wakihofia wasije wakamchanganya kwenye masomo yake.
Subira yavuta heri, Aliweka nia thabiti moyoni mwake, Dr. Anabella kuwa akimaliza masomo yake ataenda kijijini kwao kiguu na njia kutafiti nini kinachowasibu wazazi wake haswa. Na kama akikuta kuna matatizo yasiyotatulika kwa haraka itabidi awachukue wazazi wake na kwenda kuishi nao katika Jiji la Maputo. Huko ndio alipanga aendeshe maisha yake baada ya kumaliza Chuo Kikuu. Ingawa alijua ni ngumu sana kwa baba yake mzazi kukubali kuondoka kijiji cha Nthoro, kijiji ambacho ameshiriki kwa asilimia nyingi kukipa hadhi inayoonekana leo akiwa kama muasisi.
Alikuwa anatamani arudi kijijini mara kwa mara ila umbali ulikuwa ni kikwazo kikubwa. Kutoka Maputo mpaka Montepuez kwa usafiri wa gari ni zaidi ya saa 35, na kulipa nauli ya ndege ambayo angetumia saa 2 tu hakuwa nazo hizo pesa, hivyo ikawa kila mwaka anarudi mara moja nyumbani kusalimia familia yake.












Sent using Jamii Forums mobile app
