Mkurugenzi wa Kampuni ya African Stars Entertainment Tanzania (ASET), Asha Baraka ameishutumu Bendi ya Akudo Impact Wazee wa Masauti kuwa inafanya mapambano ya kichawi dhidi yake...
Asha ambaye kampuni yake inamiliki bendi mbili, African Stars Twanga Pepeta na Vibration Sound, alisema kuwa matukio ya uchawi yapo kwenye muziki wa dansi na kwamba hali ni mbaya.
Katika intavyuu na mwandishi wetu Jumanne wiki hii, Asha alisema kuwa bendi yake ya Twanga Pepeta imekuwa ikipigwa juju kwenye maonesho mbalimbali inayofanya ili kuipoteza kibiashara.
Alisema: Hata kabla ya uzinduzi wetu wa albamu ya Mwana Dar es Salaam hivi karibuni, tulikuta mayai yamevunjwa, tunakutana na vitu mbalimbali vinavyoashiria mambo ya kishirikina kwenye maonesho yetu.
Aidha, Asha bila kutaja jina la Akudo alisema: Mfano ni bendi moja ambayo ilionekana ikifanya mambo ya kichawi, hiki ni kitu cha ajabu sana, tupo kwenye muziki siku nyingi lakini hili linashangaza.
Siwezi kuitaja bendi yenyewe lakini kila kitu kilifanyika kweupe, watu waliona. Hii ni kurogana ingawa mimi siamini kama uchawi unaweza kusaidia, muziki ni kipaji na mazoezi, kwahiyo kama huwezi utabaki kuwa hivyo.
Hata uvae hirizi mia, lakini kama hauna kipaji wala mazoezi, huwezi kuimba wala kucheza kama Luiza (Mbutu). Mambo ya uchawi yapo, yanatokea mengi lakini hilo halitufanyi tutishike.
Hata hivyo, wakati Asha akigoma kulianika jina la Wazee wa Masauti, uchunguzi wa Ijumaa umebaini kuwa bendi inayotajwa kumwaga uchawi kweupe ni Akudo na ilionekana hivi karibuni.
Maelezo ya vyanzo vyetu katika uchunguzi huo, yanaitaja Akudo kwamba Ijumaa iliyopita kwenye Ukumbi wa Mango Garden, Kinondoni, Dar es Salaam majira ya jioni walimwaga kimiminika ukumbini hivyo kutafsiriwa kuwa walikuwa wanaroga.
Kuna mtu mmoja ambaye tunajua kabisa alitumwa na Akudo, akiwa na dumu lenye majimaji alianza kuyamwaga kwenye kona tofauti ukumbini, hii sisi tuliona ni uchawi, alisema mhudumu mmoja wa Mango kwa sharti la kutotajwa gazetini.
Mhudumu huyo aliongeza: Bendi nyingi zinafanya maonesho yao hapa lakini hatujawahi kuona kitu kama hiki. Mimi nina muda mrefu hapa, hata siku moja sijawahi kushuhudia mambo kama haya, hii haifai kabisa.
Katika kunogesha habari hiyo, mwandishi wetu aliongea na baadhi ya wanamuziki wa Twanga ambao waliishutumu Akudo kwa vitendo vya uchawi na kuongeza kuwa wanairoga bendi yao ili kupora mashabiki.
Baada ya kuzinasa nondo hizo, gazeti hili lilifanya spesho intavyuu na Meneja wa Akudo, Michael Andrew ambaye alikiri kumwaga kimiminika Mango Garden.
Akipangua hoja ya uchawi, Michael alisema kuwa kimiminika kilichomwagwa ukumbini ni maji ya kawaida na walifanya vile makusudi ili kumtisha Asha ambaye alikuwa na njama za kuathiri shoo yao.
Tulipata taarifa kuwa Asha alikuwepo ukumbini tangu asubuhi na hakutaka kuondoka. Mpaka jioni inafika yeye yupo tu, unadhani alikuwa anataka nini kama si kututia hasara? Alingangania ukumbini ili kutuwekea gundu watu wasiingie.
Sisi tuliliona hilo, kwahiyo tukaona uamuzi wa busara ni kumtumia mtu amwage maji ili Asha akiona ajue ni dawa aondoke, hivyo ile ilikuwa ni gia ya kumuondoa Asha, lakini hatujaroga kabisa. Kwanza tumroge nani? Akudo ipo juu sana, alisema Michael.
Globalpublishers
Haya nayo sijui yana ukweli? Jamani hizi bendi zina ushirikina pia?