Mwisho wa Azra Malama

Mwisho wa Azra Malama

SEHEMU YA 64

JEMIMA akakubali. Safari ya Madagasca ikaanza. Wakiwa njiani walipita kwenye maeneo mbalimbali ambapo mapigano yalifanyika.

Wakashuhudia maiti nyingi za watu zilizokuwa ziking’ong’wa na nzi na ukimya wa ajabu ulikuwa umetawala kisiwani hapo. Bila kutegemea Jemima alijikuta roho ikimuuma.
Mungu wangu! Alijisemea moyoni.

Swadege imebadilika na kuwa hivi? Alijiuliza kwa mshangao akizitazama kwa wahaka maiti zilizosambaa kila mahali. Akiendelea kuzitazama kumbukumbu ya mauaji ya mama yake na kaka yake Kalega ikarejea kichwani.

Uchungu ukajaa moyoni, macho yakaongeza ung’aavu wa machozi kupigania kutoka, Jemima akameza funda kubwa la mate ya baridi yaliyojaa mdomoni kutokana na hasira.

Hata hivyo hakusema lolote, alimtazama Azra na moyoni akakili maisha aliyokuwa anaishi na ndugu zake kisiwani hapo yasingeweza kujirudia tena. Chaguo lake lilikuwa ni kuendelea kumsapoti mpenzi wake huyo. Wakasafiri mpaka Madagasca!

Walipofika Azra aliwasiliana na Marekani na kuwapasha habari ya maafa aliyosababisha. Kina Jaden Smith wakafurahi kwelikweli.

Siku hiyohiyo wakamtumia chopa kama tisa zenye wanajeshi kwa ajili ya kuimarisha ulinzi.
Azra akarudi Swadege na kujitangaza kuwa mfalme wa kisiwa hicho na Jemima ndiye malkia.

Akaagiza kwa kutumia teknolojia iliyotokana na mazao ya uhai ajengewe bangaloo la maana ambalo ndilo litakuwa ikulu atakayoishi kwa raha mustarehe na mpenzi wake Jemima wakitafuna raha za dunia.

Wapambanaji wa Swadege wote waliosalia wakalazimishwa kumuunga mkono. Akawaamuru pia wapambanaji hao kuingia mtaani na kukusanya maiti zote na kwenda kuzitupa mtoni.

Hilo likafanyika, baada ya siku kadhaa Marekani ikaanza kuingia nchini humo na kubeba matani kwa matani ya Mazao ya uhai.

*** Mioyo za watu wa Swadege zilikuwa zinavuja damu. Kila mtu kwa wakati wake alikuwa akilia kuliko kawaida kutokana na hali ilivyokuwa. Kilichowauma zaidi alikuwa ni Jemima kushirikiana na adui aliyeangamizi maelfe ya ndugu zao.

Hata hivyo, huku Waswadege wakiumia, Jemima naye alijikuta kwenye sononeko la nafsi lililotokana na namna mazao ya uhai yalivyokuwa yanachukuliwa kwa kasi na Wamerekani, kingine ilikuwa ni tabia mpya za Azra kupenda wanawake.
 
SEHEMU YA 65

KILA mwanamke mzuri wa Swadege Azra Malama alitamani awe wake. Kitendo hiki kilimuumiza mno Jemima. Akalia na kusononeka.

Mapanzi ya dhati yakamuadhibu.
Ukafika wakati akajuta kumpenda Azra Malama!

Jemima alitamani muda urudi nyuma asahihishe kosa alilofanya. Lakini hakukuwa na uwezekano huo. Akaishia kulia na kujuta. ***

SHEBO akiwa katikati ya maumivu makali baada ya kuchomwa na kitu chenye ncha kali kifuani na Azra Malama, alijikokote chini huku amekishika chuma kilichomo mwilini mwake.

Wakati akijaribu kujikokota ndipo alipoona moto mkubwa unapamba. Shebo alishituka na moja kwa moja alifahamu Azra Malama nia yake ilikuwa ni kumchomea ndani.

Akakaza msuri na kujivuta mpaka mlangoni, Shebo akagalagala katikati ya maumivu mpaka nje huku moto ukizidi kuwa mkali kwenye eneo hilo ambalo waliishi wazee wa Swadege ya Rwadege.
Baada ya kutoka nje, Shebo alishangaa kuona watu watatu wakimkimbilia.

Alikuwa ni mzee Makimbi, Michael na Jaji Kessy.
“Pole Shebo,”Mzee Makimbi alimwambia akiinama karibu yake.

“Huyu mwanaharamu yupo wapi?” Shebo aliuliza akijikakamua kupambana na maumivu aliyokuwa anayahisi.

“Nani?” Mzee Makimbi alimuuliza.
“Azra Malama.”
“Ndiye kakufanya hivi?”
“Ndiyo.”

Mzee Makimbi alishika kiuno na kusimama akihamanika! Alipitisha pia tafakari la muda na kuhakikisha moyoni mwake kwamba Azra Malama alikuwa ni hatari.

SHEBO ni kiongozi wa jeshi lao kwa miaka mingi, walimuaminia kwa uhodari wake kwenye mapambano, iweje Azra amlaze chini? Mzee Makimbi alifahamu kuna kazi ya ziada ya kufanya.

Kilichofanyika muda huo ilikuwa ni kumchukua Shebo na kwenda naye kwenye maeneo ya maficho na kumhudumia kwa kutumia dawa zilizotengenezwa kwa mazao ya uhai. Shebo akarudia kuwa ngangari baada ya kutumia dawa hizo.

Jelaha la kuchomwa na kitu chenye ncha kali likafutika. “Twapasa kujipanga,” mzee Makimbi aliwaambia wenzie. “Lazima tuikomboe Swadege ya Rwadege.”

“Ni kweli ni muda wa kufa kwa ajili ya Swadege ya Rwadege, ardhi ya mama yangu. Sina cha kupoteza, ndugu zangu wengi wameuawa.

Kuliko kuishi nikitazama huyu Mmarekani anaharibu utaratibu wetu wa maisha ni bora kupotelea kwenye uwanja wa kivita.” Shebo alizungumza kwa uchungu.
 
SEHEMU YA 66

“Tupo tayari kuwaunga mkono,” Jaji Kessy alisema akimtazama Michael.
“Ni kweli,” Michael alisema akitikisa kichwa.
Wote wakakumbatiana.

“Yatupaswa kuandaa jeshi,” Shebo aliwaambia.“Nitaanza kuwakusanya vijana taratibu na huku kwenye Kijiji cha Amani, ndiko kutakuwa mafichoni kwetu.”
“Ni kweli, lazima tuandae jeshi,” Mzee Makimbi aliiunga mkono hoja yake.

Shebo akaondoka mahali hapo na kuingia mitaani kwa tahadhali kubwa kwa ajili ya kuwatafuta vijana wa kuunganisha nao nguvu kwa ajili ya kupambana na Azra Malama na Wamarekani.

Akiwa mitaani Shebo alipigwa butwaa!
Wanajeshi wa Kimerakani walikuwa wametanda kila kona na mitutu. Shughuri za kila siku za Swadege zilikuwa hazifanyiki kama ilivyokuwa awali.
Mitaa ilikuwa tupu na kimya!

Hali hiyo aliyoiona ilizidi kumkasirisha mno Shebo. Akawa tayari kufa lakini si kushuhudia watu wa Swadege ya Rwadege wakigeuka kuwa watumwa wa Marekani.

Kwa tahadhari ya nguvu Shebo alikwenda kwenye mitaa ambayo alifahamu ni lazima atakuta watu, sehemu ambapo watu walikusanyika vita inapozuka, na kweli aliwakuta.
Akafurahi.

Akawakusanya vijana na kuwaeleza nia yake.
“Tupo tayari,” vijana walipaza sauti kwa ari kubwa.

“Lazima tupambane kwa ajili ya Swadege yetu,” Shebo aliongea kwa sauti ya juu.
“Ndiyo…” Vijana walipaza sauti.
“Hata ikigharimu uhai wetu.” Shebo aliwaambia tena.

“Ndiyo.” Vijana walikubali kuingia vitani.
Shebo akawaongoza mpaka kwenye Kijiji cha Amani, wakakutana na mzee Makimbi, Jaji Kessy na Michael ambao ndiyo wangeongoza mapambano hayo kwa ushauri na nini kifanyika.

Mipango kabambe ya vita ikaanza kupangwa! ***
“Ni lazima tumtumie Jemima!” Mzee Makimbi alitoa wazo.

“Lakini ametusaliti,” Shebo alibweka.
“Ni kweli, lakini kumbuka wanawake ni vigeugeu.”

“Nguvu ya mapenzi ni kubwa mzee Makimbi, Jemima anaweza kutuangamiza.”

“Hapana,” Mzee Makimbi alipinga. “Si mjinga kiasi hicho ashindwe kuona namna maisha yalivyobadilika Swadege. Upofu wa mapenzi ulimfunga akatenda kosa, lakini ninauhakika tunaweza kumtumia.”
”Kivipi?” Michael aliuliza.

“Yeye ndiye anaweza kutufanya tukafahamu nguvu zaidi za Azra Malama na Wamarekani.” Mzee Makimbi alifafanua.
 
SEHEMU YA 67

Wazo lake likapitishwa. Lakini swali lilikuwa ni kwa namna gani wanaweza kumfikia Jemima, bila Azra kuwagundua ili hali Jemima ndiye alikuwa Malkia wa Swadege ya Rwadege wakati huo?

“Michael itabidi upeleke ujumbe huu,” Mzee Makimbi alimwambia. “Nenda kwa nia ya kuonana na Azra Malama, lakini hakikisha unampa ujumbe tutakaokutuma Jemima.
Michael alikubali. ***

BAADA ya kuwa malkia, Jemima alipewa walinzi watatu. Wawili walikuwa ni Wamarekani na mmoja alikuwa ni kutoka Swadege ambaye alikuwa ni rafiki yake aliyempenda.

Muda mwingi akiwa kwenye kasili ya kifalme, Jemima alipenda kukaa na rafiki yake huyo wa kike aliyeitwa Mimah na kuzungumza mambo mbalimbali.

Huo ndio ulikuwa utaratibu wa kila mara!
Lakini utaratibu huu ulianza kubadilika baada ya Jemima kugundua usaliti wa waziwazi aliokuwa anatendewa na Azra Malama.

Muda mwingi akawa anajifungia chumbani kwake akilia na kusononeka kutokana na maumivu ya moyo.

Hali hii ilimshangaza Mimah, kwa kuwa alikuwa ni mtu wake wa karibu hakuacha kumuuliza mara kwa mara juu ya nini kilikuwa kikimtatiza.

Siku moja Jemima alimwambia.
“Pole sana,” Mimah alimjibu baada ya kumsikiliza.
“Asante Mimah!”
“Sasa utafanya nini?”

“Sijui.” Jemima alijibu uso wake ukijenga hali ya kuchanganyikiwa. “Huyu mtu simpendi Mimah, ninalia na mengi, kumbuka tunaonekana wasaliti kwa Waswadege wenzetu, halafu tunaishi bila raha. Jamani najuta…”

Mimah hakuwa maneno zaidi ya kuongeza ukaribu wake kwa Jemima, ili kumliwaza kutokana na maumivu aliyokuwa anayapata. ***

“Kuna mgeni mkuu,” Mfalme Azra Malama alipewa taarifa na wasaidizi wake.

“Ni nani?” Aliuliza kwa mamlaka.
“Anaitwa Michael.”
“Mmarekani.”
“Ndiyo.”
Mkaribisheni.

Michael alikaribishwa.
“Michael…” Mfalme Azra alimpokea Michael kwa bashasha.

“Azra Malama, utukufu uwe kwako mfalme,” Michael alisalimia kwa heshima.
“Karibu sana.”

Azra alimzungusha Michael kumuonyesha maeneo mbalimbali katika kasiri lake hilo. Wakati wakizunguka Michael alimuulizia Jemima. Akadai anataka kumsalimia. Kumbe alihitaji kumpa ujumbe.

Azra aliagiza Jemima aitwe. Alipokuja wakati Michael akimsalimia kwa mkono, kuna kitu alimpa Jemima. Azra akaona!
 
SEHEMU YA 68

AZRA Malama alimuona mpenzi wake Jemima ameshika kitu cheupe mkononi, lakini hakuwa na uhakika kama kitu hicho alipewa na Michael, au alikuja nacho mahali hapo.

Kwa sekunde zinazohesabika, Azra alijiuliza kama karatasi hiyo amepewa na Michael, ilikuwa na ujumbe gani? Lakini pia Azra hakuwa na kumbukumbu kwamba Michael na mkewe Jemima, walikuwa wakifahamiana.

Akaamua kupotezea kwa muda.
Baada ya Jemima kusalimiana na Michael alitoka na kurudi ndani alikokuwa na moja kwa moja alikwenda mpaka chumbani.
Akili yake yote ilikuwa kwenye karatasi aliyopewa na Michael.

Akaifungua.
Akaisoma.
Ilikuwa imetoka kwa mzee Makimbi. Shebo pia, alitambulishwa kwenye ujumbe huo.

Baada ya kuisoma Jemima alishusha pumzi ndefu.
Akakuna kichwa kwa mbele kama mtu anayewaza.

Akili na mwili wake vikakosa utulivu. Uchungu ukamvamia moyoni, macho yake yakatengeneza machozi na akaanza kulia.
Jemima alilia kwa sababu ya maneno aliyosoma kwenye karatasi.

“Ni raha gani unaipata kwenye kasili la mfalme huku ndugu zako wanakufa na kuteseka Jemima? Ni muda wa kufanya uamuzi sahihi kwa ajili ya Swadege ya mama yako.

“Kila mtu anakosea. Lakini kuna wakati wa kusahihisha makosa. Wakati ni sasa, fanya jambo kwa ajili ya Swadege ya Rwadege. Tupo tayari kupambana, tunahitaki kufahamu nguvu za Azra Malama, na siri baina yake na Wamarekani.

Tusaidie tuikomboe Swadege yetu!” Ndiyo ujumbe aliousoma kutoka kwa mzee Makimbi.
Akiwa bado yupo na karatasi hiyo mkononi mara alishituka mlango ukifunguka.

Jemima akaitupa karatasi pembeni ya makochi. Akatazama mlangoni ni nani alikuwa anaingia, akamuona Mfalme Azra Malama akitokeza.

“Mpenzi…” Azra alimuita Jemima akimsogelea. Pia alikuwa anamtazama usoni kwa makini. “Waonekana mwenye majonzi. Nini hufurahii?” Alimuuliza.
“Nipo sawa.” Jemima alijibu kwa sauti iliyosikika kwa chini.

“Upo sawa, ila haupo kawaida.”
“Nimewakumbuka mama na kaka yangu,” Jemima ilibidi adanganye.

“Ooh!” Azra alimsogelea. Akampakata kifuani. “Pole, Mungu aliwapenda, huna budi kukubaliana na hali halisi.”
Jemima alitikiwa kichwa kukubali.
“Kuna kitu nimeona Michael amekupa?”

Azra alimuuliza.
Jemima alishituka waziwazi, akajinasua kifuani kwa Azra.
 
SEHEMU YA 69

“Kitu gani?” Jemima alimuuliza.
“Wewe ndiye uniambie ni nini?” Azra aliuliza kwa utulivu, akiongeza umakini kumtazama Jemima!
“Alinipa mkono.”

“Kwenye mkono kulikuwa na nini?”
Jemima alisita kidogo kujibu. Akili yake ikamwambia moja kwa moja Azra aliona kilichotokea.

Miguu ikaanza kumtetemeka hasa alipowaza akimwambia kuhusu karatasi na Azra akaiomba aisome.
Kwa namna yoyote, Jemima alifahamu, Azra akiisoma karatasi hiyo, hata maisha yake mwenyewe yatakuwa hatarini. Hata muamini tena.

Zaidi atahitaji kufahamu watu hao wanaohitaji msaada wake walikuwa wapi ili akawamalizie mbali. Jambo ambalo hakuwa tayari kuona linatokea.

“Hakukuwa na kitu, mimi ndiye nilikuwa nimeshika kitu,” Jemima alijibu akijaribu kujenga hali ya utulivu.
“Kitu gani?”
“Tishu.”

Azra alikaa kimya. Ni kama alikuwa akitafakari jambo kwa kina. Kisha akamsogeza Jemima kifuani kwake na kumkumbatia tena.
“Jemima…” Azra alizungumza kwa upole.
“Bee…”

“Unafahamu ni kiasi gani ninakupenda?”
Jemima alikaa kimya.
Azra akauinua uso wa Jemima kutoka kifuani kwake.

“Mbona hunijibu mpenzi?”
“Unanidanganya Azra.”
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Hunipendi, ungekuwa unanipenda usingenisaliti.”

Azra alipiga kimya.
“Ni kweli ninakusaliti.” Kisha alijibu. “Lakini wewe ndiye malkia na hakuna atakayechukua nafasi yako hii.

Mwanamke yoyote yule ambaye ningempa hii nafasi ni lazima angesherehekea hata ikiwa ninamsaliti na wanawake wa dunia nzima.”

Maneno ya Azra Malama yalichipua hasira moyoni mwa Jemima. Kwake suala la umalikia haikuwa sababu kuu ya kuwa kwenye uhusiano huo.

Alikuwa naye kwa sababu alimpenda. Kuwa malkia bila kuwa na furaha kwake ilikuwa ni sawa na bure.

Akizidi kumsikiliza Azra alikuwa ni sawa anabwabwaja masikioni kwake. Maneno ya Azra yalifanya kumbukumbu ya ujumbe alioupata kwenye karatasi aliyopewa na Michael ulijirudie kichwani kwake.

Jemima akakiri kuna haja ya kuwasaidia ndugu zake wa Swadege, kuna haja ya kupigania ardhi yake mama.

Hilo ndilo aliona pia ni suluhisho pekee la kejeli kutoka kwa Azra Malama, na uhuru wa maisha yake na maisha ya Waswadege ya Rwadege.

Jemima alihitaji kusahihisha makosa aliyoyafanya. Juu ya hilo alimshirikisha rafiki yake Mimah.
 
SEHEMU YA 70

“Azra akifahamu atakuua,” Mimah alimwambia.
“Ni bora afahamu na kuniua, kuliko kuendelea kuishi maisha haya Mimah.”
Mimah alikaa kimya.

Alifahamu masaibu ambayo rafiki yake alikuwa anapitia. Lakini Waswadege wote kwa jumla walikuwa wanapitia wakati mgumu, walikuwa wamegeuka kuwa watumwa wa Wamarekani.
Mwisho alimuunga mkono rafiki yake Jemima!

Jemima akaianza kazi.
Kila mara alipopata nafasi ya kuwa faragha baada ya kufanya mapenzi alimuuliza Azra mambo mbalimbali.
“Kuna kitu naomba nimwambie,” Jemima alimwambia Azra.

Walikuwa wamelala kitandani huku wote wakiwa watupu. Walijitanda kwa shuka pekee. Ilikuwa ni baada ya kukonga nyoyo zao.
“Kitu gani malkia?” Azra aliuliza, akigeuka na kulalia ubavu.

“Wewe ni shujaa,” Jemima aliongea kwa sauti ya taratibu huku anamuangalia Azra. Macho yake yalituma ujumbe kwa Azra kwamba alikuwa kweli anamaanisha maneno hayo aliyoyazungumza.

Azra alitabasamu.
“Kwa nini unasema hivyo?”
“Hiki kisiwa mataifa mengi yalikishindwa.”

“Ni kweli.”
“Lakini huoni umekuwa mtumwa wa Wamarekani?”
“Hata wao nikiamua ninawafukuza.”
“Heee!”
“Kweli.”

“Sindiyo wanakusaidia?”
“Hapana. Mimi ninanguvu za asili za kwangu mwenyewe.”
“Ni zipi hizo.”
“Si hizi ambazo zipo hapa Swadege! Mazao ya uhai.”
“Ndiyo yanakusaidia?”

“Ndiyo. Mfano Shebo, ningezubaa angenimaliza, lakini kwa sababu nilikuwa na mazao ya uhai niliyochukua kwa mzee Makimbi alishindwa. Lakini nilichofanya kwa ajili ya kujilinda, mazao yale nilipochukua kule kwenye kijiji cha Amani niliyachoma moto.

“Ninayo mimi tu. Ndiyo maana hakuna wa kuniweza kwa sasa Swadege.”
“Hongera sana kwa kujilinda.”
“Asante mpenzi.”

Azra siku hii alifunguka mambo mengi juu ya siri ya nguvu zake. Jemima alinukuu kila kitu na akamueleza Mimah. Kisha akamtuma Mimah kuzipeleka habari hizo kwa mzee Makimbi na kundi lake la kina Shebo.

Mimah akazipeleka habari hizo.
Akawaeleza.
Wakafurahia kuzipata siri c za Azra Malama!

Lakini jambo ambalo Mimah hakulifahamu ni kwamba wakati anakwenda huko alikuwa anafuatiliwa na watu waliotoa taarifa kwa Mfalme Azra Malama, kwamba Mimah alikuwa akiwasaliti.
Azra akatoa agizo Mimah auawe!
 
SEHEMU YA 71

AGIZO la Mimah kuuawa lilionekana kuwa gumu kwa kamanda Samson Cole, ingawa lilikuwa ni agizo rahisi kutamkwa na Mfalme Azra Malama, tena alilitamka kwa ufupi.

Kamanda Cole, mwanajeshi wa Kimarekani ambaye Azra aliamua kumpa majeshi yake ayaongoze, akiwa mkuu wa majeshi, hakuwa tayari kumuua Mimah kwa sababu alikuwa anampenda.
Kamanda Cole alimpenda Mimah kwa dhati.

Tena alipanga siku moja ikiwezekana amuoe na kumpeleka Marekani ingawa mpaka wakati huo agizo hilo linatolewa, hakuwahi kumtamkia Mimah nia yake ya kuwa naye kwenye uhusiano.

Kamanda Cole hakumtakia Mimah nia hiyo kwa sababu alikuwa hajapata wasaa muafaka ambao alikuwa anausubiri kukamilisha suala hilo.

Sasa wakati hajakamilisha nia yake na anasubiri muda ufike, anaambiwa amuue msichana anayempenda!

Kwake ulikuwa ni mtihani mzito, ambao alipaswa kuushinda kwa namna yoyote ile.
Sasa, baada ya kupewa agizo hilo na Mfalme Azra Malama, Kamanda Cole alikwenda na kujifungia ndani ya chumba chake huku kichwa kikiwaka moto.

Moyo ulivuja damu na mawazo yake yalikuwa ni kwa namna gani anaweza kumuokoa msichana anayempenda kwenye tanuru la umauti.

Kamanda Cole, akizidi kuwaza, alijikuta akisema kwa nguvu “nooo!” Maneno hayo yalimaanisha bado alikuwa kwenye kizungumkuti cha nafisi, akiwaza jambo gani sahihi afanye ili kumuokoa Jemima.
“Ni lazima nizungumze na Malkia…” Kamanda Cole alipania.

Hicho ndicho akakifanya.
Alivizia wakati Mfalme Azra Malama hayupo, Kamanda Cole alikwenda moja kwa moja mpaka kwenye kasili la mfalme na kumwambia kila kitu Jemima, juu ya mipango ya kuuawa kwa Mimah.

Jemima alishituka sana. Hakuweza kuamini wala kufikiria kwamba rafiki yake alikuwa kwenye hatari kubwa kiasi hicho.

“Tunamsaidiaje?” Jemimah aliuliza akionyesha wazi alikuwa amechanganyikiwa kwa taarifa alizopewa.

“Inabidi Mimah apewe taarifa hizi?” Kamanda Cole alimwambia Jemima.
“Halafu…?”

“Awaeleze ndugu zake.”
“Kisha?”
“Wao ndiyo watafahamu ni kwa namna gani wanaweza kumlinda.”

Wazo hilo Jemima alikubaliana nalo. Hata hivyo, zoezi ambalo lilibaki likionekana kuwa gumu ni namna ya taarifa hizo kumfikia Mimah!
 
SEHEMU YA 72

HATA hivyo hakuna kinachoshindikana pale pawapo na nia. Nia ya dhati ambayo walikuwa nayo Jemima na Kamanda Cole, kumnusuru Mimah kwenye tanuru la kifo iliweza kufanikiwa baada ya kufanikisha kumpenyezea taarifa bila watu kufahamu kwamba anatakiwa kuuawa.


Alipozipata taarifa hizo Mimah alichanganyikiwa. Hata hivyo bila kuchelewa alikimbilia mpaka kwenye kijiji cha Amani na kuwaeleza wanzake juu ya taarifa hizo.
“Upo mahali salama Mimah! Tutakulinda,” Shebo alimwambia.

“Tutakulinda Mimah!” Michael alimwambia.
“Sisi sote tutakulinda Mimah!” Vijana wapambanaji pia walimhakikishia Mima, kwamba yupo sehemu salama.

Taarifa alizotoa Mimah ziliongeza hasira kwenye mioyo ya kina Shebo, Michael, Mzee Makimbi na watu wengine kutoka Swadege ya Rwadege na Wamarekani, walioamua kuwasaidia watu wa Swadege.
Zikawa ni kichocheo cha kwenda kupambana.

Mapambano ya kufa na kupona na ambayo kwa namna moja au nyingine yangeirudisha Swadege ya Rwadege, mikononi mwao.
“Tupo tayari kupambana?”

Shebo alipaza sauti.
“Ndiooo…” Kundi la vijana lilimuitikia
“Tupo tayari kwenda vitani?”
“Ndiyo…”

Kila mmoja alikuwa na ari ya kupambana ili Swadege ya Rwadege irudi kwenye mikono ya Waswadege!

Makundi ya vijana tofautitofauti, yakaingia mitaani. Vijana hao walikuwa wameshika mapanga na silaha mbalimbali za jadi, tayari kwa ajili ya mapambano na hawakuwa na mchezo na mtu yeyote yule.

Wanajeshi wa Wamarekani wakiwa mitaani walishitushwa na mashambulizi ambayo yaliwakumba kwa kushitukizwa, yaliyoambatana na michale kama mvua.
Wanajeshi wa Marekani wakachanganyikiwa.

Walikuwa wamewahiwa, wengine wakaanza kukimbia ili kuyaokoe maisha yao, Waliobaki kupambana wote wakafyekwa kwa mishale na mapanga.

Mbali na kuwaua wanajeshi wa Kimarekani, vijana hao pia walikuwa wakiharibu kila kilichoitwa mali za Wamarekani pamoja na vituo walivyokuwa wamejenga kwa ajili ya kuendeshea shughuli zao.

Mitaani ikawa vurugu mechi, ambapo vijana hao kutoka Swadege wakiwa bado mitaani walikuwa wakiimba kwa sauti ya juu wakisisitiza kwamba wanamtaka Azra Malama, popote alipo ajitokeza.

Hawezi kuwa Mfalme wa Swadege ya Rwadege! Ni lazima aangushwe chini! Kila mmoja alikuwa anazungumza lake,
 
SEHEMU YA 73

TAARIFA za kuvamiwa na majeshi ya Swadege ya Rwadege, mbali na kuwachanganya wanajeshi wa Kimarekani ambao alikuwa amewaleta katika kisiwa hicho ili wamsaidie, mfalme Azra Malama naye alichanganyikiwa mno.

Mbali na kuchanganyikiwa alijiuliza kwamba ni nini kimetokea mpaka Waswadege wamepata nguvu za kuweza kupambana naye. Lakini Azra Malama hakupata jibu.

Kilichomshangaza zaidi, baada ya vita tu kuanza malkia ambaye alikuwa ni mpenzi wake, Jemima alipotea katika mazingira ya kutatanisha.

Azra akatuma watu kila mahali kumtafuta Jemima, lakini hakuna ambaye alifanikiwa kumpata na wengi waliishia kukutana na mikono ya Swadege, wakauawa!

Kwa upande wa Azra, baada ya kuona nambo yanazidi kuwa magumu hakuwa na muda tena wa kupoteza zaidi ya kuamrisha majeshi yake yaingie mitaani na kupambana na majeshi ya Swadege.

Majeshi hayo yalitii na kuingia mitaani. Vita ikapamba moto kila kona. Ikawa piga nikupige. Silaha za moto zilitumika pamoja na silaha za jadi.

Watu wakazidi kuuawa.
Majeshi ya Swadege hayakuwa tayari kurudi nyuma. Yalisonga mbele bila kujali nani anauawa au nani ameuawa.

Vita kati ya majeshi hayo mawili ikazidi kukua na hatimaye ikachukua saa 12 kwenye siku, majeshi hayo yakipambana.
Hatimaye siku moja ikakatika, bado mapambano yakiwa ni makali kuliko kawaida. Kila kona kulinuka damu.

Wakati inaelekea siku ya pili ya mapambano jeshi la Marekani, lilianza kuzidiwa nguvu na kurudi nyuma.
Kitendo hicho cha jeshi lake kuzidiwa nguvu ndicho kilimchanganya mno Azra Malama. Hakuweza kuamini kama jeshi lake imara kutoka Marekani ndilo lilikuwa limezidiwa nguvu.

Alichoamua kufanya, ilikuwa ni yeye mwenyewe kujifunga mkanda na kuingia kwenye uwanja wa mapambano. Kama kawaida yake akiwa kwenye uwanja wa mapambano, Azra alikuwa ni hatari mno.

Alifyeka vichwa vya watu kwa kutumia panga lake, lakini siku hii Waswadege walikuwa wamekwisha amua liwalo na liwe, lakini lazima Azra Malama wammalize na kubaki na kisiwa chao.

Kwa hiyo hawakukata tamaa ingawa ndugu zao wengi walikuwa wanauawa. Wakazidi kupambana lengo likiwa ni moja tu, kummaliza Mfalme Azra Malama!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom