Mwisho wa Azra Malama

Mwisho wa Azra Malama

SEHEMU YA 74

KATIKA maisha yake, hata siku moja Azra Malama hakuwahi kukubali kushindwa jambo. Alikuwa ni mwanaume wa vita na kwa miaka mingi vita ndiyo ilikuwa maisha yake.

Kwa hiyo hakuwa mtu wa kurudi nyuma kwenye mapambano. Kila pambano kwake kwa njia yoyote alikuwa na kawaida ya kupania ushindi.

Lakini tofauti na matarajio na kawaida yake, awamu hii mambo kwa upande wake yalionekana kuwa magumu.

Waswedege walikuwa wamechachamaa. Ilikuwa ni wafe wao au waikomboe Swadege ya Rwadege, kisiwa cha amani ambacho kilikuwa kimegeuka kuwa utumwani.

Vijana wa Swadege walitawanyika mitaani kila kona. Walimuua mtu yeyote mwenye nasaba za Marekani au aliyeonyesha kulishadadia taifa hilo kulitawala hata kukomba mazao yao ya uhai na kuyapeleka nje kwa ajili ya kuyauza.

Hali ikawa tete!
Azra alihisi kuchanganyikiwa. Kifo alikiona mbele yake hasa baada ya wanajeshi wake kuzidi kuuawa kuliko kawaida na majeshi ya Waswadege.

Azra baada ya kuona amezidiwa, alikimbilia kwenye ghala lake ndani ya kasili lake ili kuweza kuchukua mazao ya uhai ambayo alikuwa anaamini yangemuwezesha kupona kwenye vita hiyo, lakini hakuweza kukuta zao la uhai hata moja.
Mazao yote yalikuwa yameibiwa.

Azra Malama alibaki akiwa ameduwaa, haamini kile ambacho alikuwa anakiona. Akizidi kutazama kuna wakati alikuwa anahisi kwamba pengine alikuwa ndotoni. Akafikicha macho Lakini hali halisi iliendelea kuwa vilevile, hakukuwa na zao la uhai hata moja!

Akili ikamcheza mara moja. Azra Malama akafikiri nani ambaye angeweza kumuibia mazao hayo, jibu akalipata.
Alikuwa ni Jemima.
Jemima mpenzi wake, ndiye alikuwa amemsaliti.

Azra moja kwa moja alijua kwa kitendo hicho alichokifanya Jemima, alikuwa ameamua kugeukia upande wa ndugu zake Waswadege na hakuwa upande wake tena, hasira zikabebana kichwani kwake, wakati huo Azra Malama, alikuwa tayari kukikata kichwa cha Jemima, ikiwa angekutana naye ana kwa ana.

Hata hivyo kuyakosa mazao hayo ya uhai kwake lilikuwa ni pigo kubwa sana, kwa sababu hakuna njia nyingine ambayo Azra alifahamu angeitumia hata kupona na kutoroka kwenye kisiwa hicho.
 
SEHEMU YA 75

JEMIMA, aliamua kumsaliti Azra Malama kwa sababu ya Swadege. Alilipenda mno taifa lake hilo na alijutia kwa makosa ya mwanzo ambayo alikuwa ameyafanya.

Baada ya kuiba mazao ya uhai na kuyapeleka kwa kina mzee Makimbi na kamanda wa vita Shebo, Jemima naye aliamua kujifunga kibwebwe na kuingia vitani.

“Lazima aondoke huyu!” Msichana huyo alikuwa akihamasisha.
“Ni kweli, Swadege ya Rwadege lazima irudi mikononi mwetu.

“Tumechoka utumwa!”
Hakukuwa na jambo lingine ambalo lilikuwa linafanyika taifani hapo zaidi ya vita. Damu ilinuka kila kona ya kisiwa hicho. Hata watoto walikuwa wakipigana kwa sababu ya taifa lao.

Majeshi ya Swadege yalizidi kusonga kwenye uwanja wa mapambano, kwa upande wa majeshi ya Marekani yalianza kurudi nyuma.

Yalikuwa yamezidiwa.
Hatimaye majeshi ya Swadege yakaliteka kasili la mfalme kwa kulizunguka kila kona.
“Tunamtaka Azra Malama!” Shebo alizungumza kwa kipaza sauti nje ya kasili hilo.

Lakini ukimya ulitawala.
“Kuna mahandaki huko, tukienda kimyakimya watatumaliza.” Jemima aliwaambia.
“Tufanyeje.”

“Inabidi kutafuta mbinu mbadala.”
Mbinu mbadala ikafikiriwa, ikaonekana ni lazima wapatikane watu wa kujitoa muhanga kwa kuliparamia kasili hilo ili kuweza kuona adui alikuwa upande gani.
Jemima akajitoa wa kwanza.

“Hapana Jemima,” Shebo alimwambia.
“Niache nife kwa ajili ya Swadege.”
“Wapo watu watajitoa si wewe, bado tunakuhitaji.”
“Hakuna ambaye hahitajiki, nipo tayari kufa.” Jemima alisisitiza.

Shebo alimtazama msichana huyo kwa huzuni. Mzee Makimbi, Michael na hata Jaji Kessy wote walimtazama Jemima kwa huzuni. Wakamsogelea na kukumbatiana naye.

“Kwa herini,” Jemima aliwaambia macho yaking’aa zaidi. “Kila mmoja wetu anawajibu wa kuilinda Swadege ya Rwadege, hii ni tunu pekee ambayo tuliopewa NA Mungu. Ni taifa la ahadi la mababu zetu. Ilindeni kwa machozi na damu.”
“Tunakupenda Jemima.”
“Ninawapenda pia.”

Watu wote machozi yaliwabubujika wakati wanaagana na Jemima pamoja na vijana wengine watano walioamua kujitoa muhanga kwa ajili ya Swadege,ili kwenda kuvamia kichwakichwa kwenye kasili la mfalme na kujua adui alikuwa mahali gani.
 
SEHEMU YA 76

BAADA ya kuagana, Shebo aliwapanga wote na kuyapanga majeshi yake kuwa tayari kuwapa sapoti kwa kurusha silaha zao za jadi pale tu mashabulizi yatakapoanza.

walipojipanga, ShebO aliwaruhusu watu wale kukimbilia kwenye uwanja wa kasili la mfalme, wakakimbia Jemima akiongoza mbele.

ile wanakimbia, risasi zikaanza kumiminika kama njugu. Shebo na kundi lake wakaziona wakaanza kushambulia kwa mishale yenye sumu iliyomwagika kama mvua.

Mapambano yakawa makali.
Jemima akikimbia, alishitukia risasi ikitua kifuani kwake chini ya ziwa la upande wa kushoto, TIII! Akacheua kwa maumivu na kupepesuka, nyingine ikatua tumboni, hiyo ndiyo ilimmaliza nguvu akadondokea magoti.

Alipotua ardhini risasi nyingine ilitua kichwani na kusambaratisha ubongo. Jemima akadondoka chini kama gunia. Huo ndiyo ukawa mwisho wake. Na wale vijana wengine waliojitoa muhanga, waliuawa.

Kuuawa kwao ndio ulikuwa msaada mkubwa wa majeshi ya Swadege ya Rwadege kufahamu adui alikuwa upande upi, yakavamia kwa kasi ya ajabu mpaka kwenye kasili la mfalme na kuingia ndani kwa kuruka ukuta huku yakipambana na wanajeshi wa Kimarekani.

Mapambano yalipamba moto kwelikweli. Lakini kutokana na wingi wa wanajeshi wa Swadege, majeshi ya Marekani yaliyokuwa yanaongozwa na Azra Malama yalianza kuzidiwa.

Lakini Azra aliamrisha hakuna mwanajeshi wake yeyote aliyepaswa kunyanyua mikono juu, ilikuwa ni lazima kufia kwenye uwanja wa mapambano.

Yakazidi kujikakamua kupigana, lakini mwisho yakazidiwa. Wanajeshi wote wakauawa kwa mishale yenye sumu, Azra akakimbia kujificha kwenye handaki lake lililokuwa ndani ya kasili hilo.

Msako mkali ukaanza kufanyika huku maelezo ya Jemima ambaye alikuwa ni marehemu wakati huo yakifuatwa, kwani kabla ya kifo chake alielekeza juu ya handaki ambalo Azra angejificha.

Wanajeshi wa Swadege wote ambao walikuwa wamesalia wakaingia kwenye handaki hilo, Mungu mkubwa wakaweza kumkuta Azra Malama, akiwa amejificha kwenye bomba la maji.

Wakamchomoa na kumtoa handakini.
Wakamfunga minyororo na kutoka naye kwenye kasili hilo.

Walipomtoa nje, walianza kuimba nyimbo za shangwe na ushindi huku wakimpiga kwelikweli Azra Malama.
Alilia kama mbwa!

ITAENDELEA KESHO... Usikose!
 
SEHEMU YA 77

HOIHOI za kusherehekea ushindi zilipamba moto kisiwani Swagede. Kila kona watu walikuwa na furaha baada ya Azra Malama kukamatwa.

Watu walipiga madebe mitaani, vijana walifanya fujo za kila aina, ilimradi ilikuwa kila mtu kujirusha kwa kusherehekea ushindi huo.

Ushindi ambao ulirudisha uhuru kwao.
Uhuru wa maisha yao, na aina ya kuishi watakavyo kwa kufurahia vivutio na fahari nyingi ambazo Mungu alikuwa amewajaalia. ***

Huku Waswadege ya Rwadege wakisherehekea ushindi, Azra Malama alikuwa kwenye maumivu makali. Mauamivu yaliyotokana na kuburutwa mtaani kama mnyama.
Kitendo hicho cha kuburutwa kilimfanya Azra alie kama mtoto, ngozi yote ilichunika chini na damu ikamtapakaa mwili mzima.

Kutokana na hali aliyokuwa nayo, Azra akiwa amening’inia kwenye minyororo alijiambia moyoni kwamba hatimaye amefika mwisho. Roho ikamuua mno.
“Mwisho wa ubaya ni fedha!” Alikumbuka maneno ambayo alikuwa akiambiwa mara kwa mara na watu aliowafanyia ubaya.
Ni kweli kifo chake kilikuwa kinakwenda kuwa cha fedheha!

Azra alikumbuka mambo mengi aliyofanya. Alikumbuka juu ya mauaji ya kinyama aliyotenda, namna alivyotesa watu na kuwatumikisha kutokana na kiu ya kupata madaraka kuwa mfalme wa Swadege ya Rwadege na mambo mengine mengi.

Kumbukumbu yote hiyo ilikuwa inamuumiza moyoni. Akajikuta akijuta. Kwa mara ya kwanza moyoni akakiri hakustahiri kufanya yote hayo. Hakuiona haja hasa kuyafanya kwa ndugu zake wa Swadege wakati watu pekee walioitesa familia yake ni Wamarekani.
Jambo la kushangaza Wamarekani haohao ndiyo aliowasaidia!

Vijana Waswadege waliendelea kumburuza Azra wakizunguka kila mahali kulipokuwa na watu ili kila mmoja amuone mtu ambaye alikuwa anawatesa.
Walipomaliza ziara hiyo ya mateso, walimpeleka Azra kwenye uwanja ambao mauaji mengi ya halaiki yalikuwa yakifanyikia hapo.

Walipofika mahali hapo walimfunga kwenye nguzo nene zilizojengwa kwa zege imara ili waweze kummalizia kwa kumlenga mishale mingi yenye sumu kali, kisha mwili wake kuuacha hapohapo, uliwe na ndege pamoja na wadudu mpaka utakapoisha kama ambavyo ulikuwa utaratibu wao.

Azra alifungwa kwenye nguzo na wanajeshi wa Swadege walikaa tayari kumlenga kwa mishale yenye sumu.
 
SEHEMU YA 78

WAKATI wa zoezi hilo, Jaji Kessy na Michael pia walikuwa uwanjani hapo kuushuhudia mwisho wa Azra Malama.
Jaji Kessy akimtazama Azra alijikuta roho ikimuua mno.

Roho ilimuuma kutokana na kumbukumbu iliyovagaa ubongoni mwake, akakumbuka siku ya kwanza alivyokutana na Azra Malama kwenye gereza la Guantanamo na kijana huyo kugeuka kuwa rafiki yake mkubwa.

Rafiki ambaye alimpa uhuru wa maisha yake, hata akasafiri kutoka Marekani mpaka kwenye kisiwa hicho kwa ajili ya kuitafuta maana ya maisha kwa wazee wa Swadege ya Rwadege, ambao walikuwa wanasifika duniani kote kwa kuwa na busara, pamoja na kuishi aina ya maisha iliyowapa furaha kila siku.

“Kwa heri Azra,” Jaji Kessy alijikuta akitamka kimyakimya huku akimtazama Azra ambaye alikuwa ametepeta vilivyo.

Kwa upande wa Michael, yeye pia moyoni mwake hakuwa na furaha kabisa. Ni kweli alifahamu kwa vitu alivyovifanya Azra Malama, alistahiri malipo hayo lakini kitendo cha kumuona akiwa kwenye hali ile kilimhuzunisha sana.

Azra aliwahi kuwa rafiki yake mkubwa. Rafiki ambaye waliambizana kwamba urafiki wao ulikuwa ni wa kufa na kuzikana. Lakini urafiki huo ulikoma pale tu Michael, alipofahamu anahitaji nini kwenye maisha yake.

“Ulikuwa mwanaume wa kazi,” Michael alizungumza moyoni. “Nitakukumbuka siku zote,” aliendelea kuelea kwenye mawazo akimtazama Azra ambaye alikuwa yupo nusu hai na nusu Marehemu.

Wakati Jaji Kessy na Michael wakielea kwenye mawazo ya kuwaumiza, wanajeshi wa Swadege wapatao mia tano walikuwa wamejipanga mstari mmoja huku wamechuchumaa kwa goti moja, tayari kwa kumlenga kwa mishale yenye sumu Azra Malama.

Baada ya kujipanga vizuri, mkubwa wa majeshi Shebo aliyekuwa mbele aliwaamrisha kujiandaa kwa ajili ya zoezi hilo.
Wanajeshi walijiandaa kikakamavu.
Shebo akawaamrisha tena watupe mishale.

Mishale kama mvua iliachiwa kutoka kwa kila mmoja wao, ikapaa angani na yote ikaenda moja kwa moja kumchoma Azra Malama, kwenye kila kona ya mwili wake. Azra Malama akapoteza maisha.
Huo ndiyo ukawa mwisho wake.
 
SEHEMU YA 78

WASWADEGE walipiga shangwe ya nguvu baada ya kuhakikisha Azra Malama, amepoteza maisha.

Zoezi hilo lilipomalizika , Shebo ambaye aliyaongoza kwa ushujaa mkubwa mapambano hayo dhidi ya Azra Malama, akatangaza watu wote warudi majumbwani kwa ajili ya msiba wa kitaifa ambao walikuwa wamepata, kutokana na watu wengi kufariki kisiwani hapo.
Hicho ndicho kilichofuatwa. Watu wakarudi nyumbani kwa ajili ya msiba.

***
Mimah hakuwa na raha hata kidogo, muda mwingi aliutumia akilia na kusononeka kutokana na kifo cha rafiki yake Jemima, kilichomuua mno moyoni mwake.

Mbali na kusikitika, Mimah ndiye aliuchukua mwili wa mwanadada huyo Malkia wa Swadege ya Rwadege kwa ajili ya kuuzika, aliuchukua akisaidiana na Shebo.

Wawili hao walifanya msiba na kwenda kuuzika mwili huo kwenye makaburi ya halaiki ambapo marehemu wote waliofariki kwenye vita hiyo, walizikwa.
Hiyo ndiyo ikawa safari ya mwisho ya Jemima duniani.

Wakati wa mazishi yake alipigiwa mizinga ya heshima, na wanajeshi wa Swadege, tena zaidi ya mara moja, kuonyesha namna walivyouheshimu na kuuthamini mchango wake kwenye zoezi zima la kumuua Azra Malama..

Mazishi ya halaiki yalipomalizika, zilitolewa siku chache kwa ajili ya kumalizia maombolezo. Baada ya siku hizo kupita pia, Waswadege ya Rwadege wakaendelea na maisha yao. ***

“Ni lazima dunia ifike mahali ikubaliane na sisi,” Mzee Makimbi alikuwa akimwambia Shebo. “Tuna aina ya maisha yetu na hatuwezi kuishi kama mtu yeyote atakavyo.

“Maisha yetu ni amani, furaha na kusherehekea zawadi mbalimbali ambazo Mungu ametujalia. Ikiwa dunia inataka tuwasaidie. Tutawasaidia! Lakini si kulazimisha tuishi kama watakavyo wao tena kwa kututawala.”
Mzee Makimbi alipumzika na kumeza mate.

“Nakutuma, nenda katangaze juu ya msimamo wetu na ueleze wazi tunahitaji kuachwa tuishi kwa namna tutakavyo sisi!
Shebo hakuweka pingamizi lolote lile.

Alikubaliana na mzee huyo na maandalizi ya shujaa huyo kwenda kuzungumza kwenye kikao cha Umaja wa Mataifa, ambacho walikuwa wamealikwa huko Uingereza, yalianza.
Shebo alipanga kuwawakilisha vyema Waswedege!
 
SEHEMU YA 78

WASWADEGE walipiga shangwe ya nguvu baada ya kuhakikisha Azra Malama, amepoteza maisha.

Zoezi hilo lilipomalizika , Shebo ambaye aliyaongoza kwa ushujaa mkubwa mapambano hayo dhidi ya Azra Malama, akatangaza watu wote warudi majumbwani kwa ajili ya msiba wa kitaifa ambao walikuwa wamepata, kutokana na watu wengi kufariki kisiwani hapo.
Hicho ndicho kilichofuatwa. Watu wakarudi nyumbani kwa ajili ya msiba.

***
Mimah hakuwa na raha hata kidogo, muda mwingi aliutumia akilia na kusononeka kutokana na kifo cha rafiki yake Jemima, kilichomuua mno moyoni mwake.

Mbali na kusikitika, Mimah ndiye aliuchukua mwili wa mwanadada huyo Malkia wa Swadege ya Rwadege kwa ajili ya kuuzika, aliuchukua akisaidiana na Shebo.

Wawili hao walifanya msiba na kwenda kuuzika mwili huo kwenye makaburi ya halaiki ambapo marehemu wote waliofariki kwenye vita hiyo, walizikwa.
Hiyo ndiyo ikawa safari ya mwisho ya Jemima duniani.

Wakati wa mazishi yake alipigiwa mizinga ya heshima, na wanajeshi wa Swadege, tena zaidi ya mara moja, kuonyesha namna walivyouheshimu na kuuthamini mchango wake kwenye zoezi zima la kumuua Azra Malama..

Mazishi ya halaiki yalipomalizika, zilitolewa siku chache kwa ajili ya kumalizia maombolezo. Baada ya siku hizo kupita pia, Waswadege ya Rwadege wakaendelea na maisha yao. ***

“Ni lazima dunia ifike mahali ikubaliane na sisi,” Mzee Makimbi alikuwa akimwambia Shebo. “Tuna aina ya maisha yetu na hatuwezi kuishi kama mtu yeyote atakavyo.

“Maisha yetu ni amani, furaha na kusherehekea zawadi mbalimbali ambazo Mungu ametujalia. Ikiwa dunia inataka tuwasaidie. Tutawasaidia! Lakini si kulazimisha tuishi kama watakavyo wao tena kwa kututawala.”
Mzee Makimbi alipumzika na kumeza mate.

“Nakutuma, nenda katangaze juu ya msimamo wetu na ueleze wazi tunahitaji kuachwa tuishi kwa namna tutakavyo sisi!
Shebo hakuweka pingamizi lolote lile.

Alikubaliana na mzee huyo na maandalizi ya shujaa huyo kwenda kuzungumza kwenye kikao cha Umaja wa Mataifa, ambacho walikuwa wamealikwa huko Uingereza, yalianza.
Shebo alipanga kuwawakilisha vyema Waswedege!
Asante sana kipenzi changu,mwenyezi mungu akubariki sana
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom