Mwisho wa Azra Malama

Mwisho wa Azra Malama

SEHEMU YA 51

“Ni mimi niliyeongoza mapambano ili auawe au afukuzwe kisiwani hapa.” Kalega alimwambia Bonza.

“Wako wapi ndugu zetu kiongozi wa mapambano?” Bonza alimuuliza Kalega huku akishuka kwenye farasi na kumsogelea.

“Tazama,” Kalega alizungumza kwa upole kwani ilibidi ajishushe.

“Ni mashujaa pekee hufia vitani, hatuna budi kuwapa heshima yao katika mazishi huku tukiandaa mauaji ya kinyamakwa adui ambaye tayari yupo mikononi mwetu.”

“Mazishi ya heshima hayawezi kupendeza bila mwili wa dada yako na mama yako,” Bonza alimwambia Kalega.

Watu wengine walishuka pia kwenye farasi zao.
“Hapana,” Kalega alizungumza kwa hamaki kisha akachomoa panga lake. “Si mimi niliyewaua ndugu zenu. Si mama yangu wala dada yangu.”

Hata hivyo kundi lile tayari lilikuwa limekwisha dhamilia kufanya maafa nyumbani hapo kwao Kalega. Lilimvaa kijana huyo na kuanza kupigana naye.

Baada ya kuona hivyo mama Cecilia na mwanaye walikimbilia ndani, harakaharaka walichukua vitu muhimu ikiwemo vipande vya mazao ya uhai kisha wakatoka nje tena.

“Kimbieniiii…” Kalega aliwaambia huku akiendelea kupambana.

Lakini mama yake moyo ulikuwa mzito kumuacha mwanaye akifa kwa ajili yake.
“Mama kimbieni nasema,” Kalega alirudia.

Wakati akimaliza kuzungumza hivyo, mara alichomwa mkuki wa mbavu, Twiii! Akapiga kelele za maumivu. Mama yake tumbo la uzazi lilikata.

Akakimbilia pale alipodondokea mwanaye. Naye akapigwa mshale wa mbavu na kufa papohapo.

Jemima kuona hivyo alamu ya hatari iligonga kichwani kwake na akafahamu ilikuwa ni zamu yake ya kuuawa.
Akiwa ameshika mazao ya uhai mkononi, msichana huyo alianza kukimbia kwa nguvu zake zote.

Hata hivyo baada ya kundi lile kuwamaliza mama Cecilia na Kalega, walianza kumkimbiza pia Jemima.

Jemima moyoni alikuwa ameamua kwamba, kama siku yake ya kufa ilikuwa imetimia basi kifo kingemkuta akijaribu kujiokoa na hakuwa tayari kukisubiri.

Msichana huyo aliedelea kukimbia kwa nguvu zake zote utadhani alikuwa kwenye mashindano ya marathoni na jambo la bahati nzuri kwake, baada ya kukimbia mita takribani elfu moja mia tano, alifika kwenye Msitu wa Sonve, akauvaa msobemsobe huku akiendelea kukimbia akihema kwa uoga.
 
SEHEMU YA 52

Kundi la Bonza pia, baada ya kufika kwenye msitu huo, kila mmoja alishuka kwenye farasi wake na kuzama msituni humo huku wakiwa wameshika mikononi vijiti vya moto, mapanga na mikuki huku wakiimba kwa hasira.

Msako wa kumtafuta Jemima ulikuwa mkali kwelikweli maana kundi hilo lilipita kichaka kwa kichaka tena kwa umakini wa hali ya juu.

Kwa upande wa Jemima, baada ya kukimbia sana alihisi kuchoka. Mwili wake uligoma kabisa kuendelea kusonga mbele hata alipojaribu kujilazimisha bado alishindwa, ikimbidi atafute kichaka na kujibanza chini ya miti yenye miba iliyosongana.

Jemima hakujali maumivu makali aliyoyapata baada ya kuchanwa na miti hiyo yenye miba. Akiwa kichakani hapo akili yake ilipaa mbali na muda wote alikuwa akikumbuka tukio la kuuawa kwa mama yake na kaka yake Kalega.

Ukweli ni kwamba tukio hilo lilimuumiza mno Jemima moyoni kiasi kwamba akajikuta akizidi kulia kwa uchungu.

Hata hivyo akiendelea kulia kutokana na kumbukumbu hiyo ya mauaji, mara Jemima alisikia sauti za watu wakiimba na kutembea kuelekea kwenye uelekeo alipokuwa amejificha.

Mwili wake ulimsisimka Jemima na alihisi uoga ukimzidi mara dufu kwa maana alifahamu kundi hilo likimkamata kulikuwa hakuna mjadala zaidi ya kumuua tu.

Jemima, alijitahidi kujikaza kwa kuziba mdomo wake kwa viganja vya mkono kuzuia asipumue ili hata kundi hilo likipita karibu na hapo alipokuwepo lisiweze kumgundua. Lakini akili nyingine ilimwambia ni lazima watakugundua tu huwezi kuwakwepa.

Hata hivyo, Waswahili walisema siku ya kufa nyani miti yote hutereza. Jemima akiwa bado hajapata ufumbuzi wa nini cha kufanya ili aweze kujiokoa, mara aliweza kugundua mita chache kutoka mahali hapo alipokuwa amekaa kichakani kulikuwa na joka kubwa aina ya chatu limelala.

Mwili mzima ulimsisimka msichana huyo na uoga ulizidi mara dufu, mawazo yake yote yalihama alikokuwa akilisikia kundi la Bonza, yakabakia hapo kwenye joka hilo.

Jemima akiwa anatetemeka kuliko kawaida, alianza kujiinua taratibu ili akimbie, baada ya kuinuka na kusimama akinyata ili amtoke chatu huyo na kukimbia, mara yule chatu alianza kujinyoosha.
 
SEHEMU YA 53

Mwili ulimsisimka msichana huyo, woga ulizidi mara dufu. Mawazo yake yote yalihama alikokuwa akilisikia kundi la Bonza likijongea, yakabakia hapo kwenye joka.

Jemima akiwa anatetemeka mwili na midomo, alijikuta akipata wazo kwamba kuugulia kwa woga haiwezi kumsaidia. Ilikuwa ni lazima ajivike ujasiri.
Hayo ndiyo mawazo aliyoaamua kuyafuata!

Kwa tahadhari ya nguvu, huku ametoa macho kuliko kawaida alisimika mikono chini na kuanza kujiinua taratibu. Alipoanza tu kufanya kitendo hicho joka hilo ni kama lilikuwa likimuona, likianza kujionyoosha.

Hali ya woga ikazidi kujengeka kwenye moyo wa Jemima kuliko mwanzo. Joka lilivyozidi kujikunjua akajikuta akiinuka kwa pupa ili akimbie.

Alipoinuka likamgisa mguu, Jemima akapiga kelele na kuongeza kasi, akafanikiwa kulitoka hapo lakini kelele zake zilipaa mbali.

Kelel hizo zilipaa na kulifikia kundi la Shebe. Wanaume hao wakasimama na kuelekezana sauti ilikosikikia, wakaanza kufuata uelekeo huo kwa kasi huku wakijua wapo karibu kumkamata Jemima.

Kutokana na umbari uliokuwepo katikati yao wakati Jemima akikimbia aliweza kulisikia kundi hilo lililokuwa linamtafuta. Hakuwa na njia nyingine ya kuikoa nafsi yake zaidi ya kukimbia.

Msichana huyo alizidi kukimbia akipangua vichaka, miti yenye mwiba ilimkwangua mwilini na kumchuna ngozi, majani yenye miiba pia yalimchoma miguuni lakini hakuwa anahisi maumivu. Akili yake yote ilikuwa ni kujiokoa.

Akazidi kukimbia!
Akiendelea kukimbia kwa nguvu zake zote, baada ya kupangua vichaka vingi na kukwepa kujigonga kwenye miti mingi, ghafla Jemima alijikuta akifunga breki na kusimama.

Woga ukamshika zaidi, akageuka nyuma ili arudi alikotoka, lakini akakumbuka nyuma kulikuwa na kundi la Shebo.

Jemima akazidi kutetemeka hasa aliposikia vishondo alivyovibaini mbele yake vikizidi kusogea karibu yake zaidi.
Kilichomchanganya zaidi, Jemima hakufahamu vishindo hivyo ni vya watu au wanyama.

Hata hivyo alipowaza kuhusu watu, kwa haraka alizama na kusikiliza kwa makini. Alijiridhisha hawakuwa watu, kutokana na sauti alizoanza kuzisikia, alibaini lilikuwa ni kundi la wanyama wakali.

Wazo lake la mwanzo likarudi tena. Akajikuta akigeuza shongo kutazama alikotoka, akawasikia kina She
 
SEHEMU YA 54

Msichana huyo alishusha pumzi ndefu na kupiga sala ya chapchap, akiomba kupitia imani yake aweze kupata msaada utakaomuwezesha kumkomboa ghafla katika ya kundi la adui na wanyama wakari wa polini.

Akiwa bado hajachukua uamuzi wowote, mara alishuhudia kundi la mbwa mwitu likitinga mahali hapo.

Kwa mara nyingine Jemima alihisi mwili wake ukipararaizi kwa hofu, akaganda wakati kundi lile likizidi kumsogelea.

Baada ya wanyama hao kufika karibu zaidi, kengele ilivuma kichwani mwake na kuelewa hatari iliyokuwa mbele yake ilikuwa ni ya kumghalimu maisha na wazo likamjia kwamba kuchelewa kwake kwa namna yoyote ile kungewapa nafasi mbwa mwitu hao wamtafune bila huruma.
Jemima alifumba macho na kujiambia moyoni;

“Liwalo na liwe!”
Msichana huyo aligeuka na kuanza kukimbia kurudi alikotoka kule ambako kundi la kina Shebo lilikuwa likisikika.
Baada ya wale mbwa mwitu kuona anakimbia, wakala naye sahani moja kwa kuanza kumfukuza kwa mbio.

Akiwa anazidi kukimbia ila anataka kutokeza eneo walipo kina Bonza, ghafla Mungu saidia aliweza kuiona njia inayochepuka kuelekea sehemu kulipo maporomoko, akili yake ilicheza kwa kasi ya umeme, akapata uamuzi wa kuichukua njia hiyo, akakata kulia na kuifuata.

Mbele kwenye miti mingi Jemima aliweza kuiona kona nyingine lengo lake likawa ni kukimbia mpaka kwenye kona hiyo.
Mbwa mwitu walikuwa nyuma wakimfukuza, kundi la Shebo nalo wakati huu lilikuwa linamkariba zaidi.

Jemima akaongeza kasi, kuikimbilia ile kona, lakini ile anakata tu aingie kwenye kona hiyo ambako ndiko mawazo yake yote yalikuwa, mara alishitukia akidakwa kwa ufundi usio wa kawaida, akajikuta amepakatwa kifuani na mtu huku mikono yenye nguvu na misuli ya mtu hiyo ikimziba mdomo.

Jemima alitoa macho wakati akihangaikia pumzi iliyozibwa kutokana na mtun huyo kumziba mdomo.
 
SEHEMU YA 55

TUKIRUDI kwa Azra alikuwa hoi taaban amelegezwa na kipigo kikali kutoka kwa vijana wa makundi ya wapambanaji wa Swadege ya Rwadege.

Vijana hao baada ya kumkamata na kuhakikisha wamempiga vilivyo, walimfunga minyororo ambayo hata angepata maamuzi ya kujiokoa kwa kuifungua asingeweza kwani ni mzimu pekee ndiyo ungeweza kujiondoa kwenye minyororo hiyo.

Baada ya kumfunga minyororo mikononi waliifungia kwenye farasi, kisha wakaanza kumburuza.

Azra alilia kwa maumivu wakati ngozi yake ikisagika ardhini na akajigonga kwenye mawe na visiki avilivyokuwa kwenye ardhi ya kisiwa hicho.

“Ni muda wa kuonyesha kwamba mimi ndiye mfalme ninayepaswa kukiongoza kisiwa hiki cha Swadege ya Rwadege, si kufa kama ndege aliyenasa mtegoni,” Azra aliwaza wakati akizidi kuburuzwa na kundi lile likishangilia kwa furaha.

Baada ya mawazo hayo Azra alianza kujivuta kwenye mingororo hiyo kuitafuta balansi ambayo alikuwa ameipoteza huku akikusanya nguvu.
Aliendelea kujivuta mpaka pale alipopata balansi.

Mfano wa mtu aliyekuwa anaivuta farasi iliyokuwa amefungiwapo, akavuta kwa bguvu na kusimama, wakati farasi hiyo ikiondoka akawa anaifuata kwa kukimbia, mwili wake wote ulikuwa hautamaniki kwa damu.

Vijana wale walipoona kitendo hicho walishangaa mno, muda mchache mtu huyo aliyesimama alikuwa ni sawa na maiti, lakini alirejewa na uhai na alikuwa amesimama. Wakafahamu Azra siyo mtu wa kawaida.

Hata hivyo hiyo haikuwa sababu ya kumuacha hivihivi. Walisimamisha farasi ili waweze kupambana naye.

Wakamvaa. Ile wamemfikia Azra alijibetua kwa sambasoti akipata balansi kutoka kwenye mingororo aliyofungwa, wakati amejibetua na kufika chini alikuwa amewalaza kwa kichapo vijana kama wanne hivi.

Wakadondoka chini.
Wengine wakazidi kumvaa. Azra naye akaanza kurusha mapigo ya kasi. Miguu yake ndiyo ilikuwa ikifanya kazi.

Hakuruhusu mtu amkaribie, akawa anaruka mfano wa wacheza mpira wanavyopiga tikitaka na minyororo ailiyokuwa imemfunga ndiyo ilikuwa ikimpa sapoti kubwa kwenye kuruka sambasoti.

Likawa patashika la kufa mtu. Piga ni kupige. Alichoamua zaidi kukifanya Azra ilikuwa ni kupiga mapigo ya nguvu kuhakikisha kila ambaye pigo lake linampta haamki, anakwenda moja kwa moja kuzimu!
 
SEHEMU YA 56

Likawa patashika la kufa mtu. Piga ni kupige. Alichoamua zaidi kukifanya Azra ilikuwa ni kupiga mapigo ya nguvu kuhakikisha kila ambaye pigo lake linampata haamki, anakwenda moja kwa moja kuzimu!

Mapigo ya Azra yalizidi kuwapagawisha vijana Waswadege ya Rwadege zaidi yaliwapukutisha. Wapambanaji wengi walizidi kupoteza maisha.

Kitendo cha kuona alikuwa anawamudu vijana hao ndicho kilizidi kumpa Azra nguvu ya kuendelea kupigana kwa uwezo wake wote. Hakutaka kurudi nyuma ilikuwa ni ama afe yeye au wafe vijana hao.

Akaendelea kuruka mateke ya kasi isiyoweza kutoshereza kusimuliwa hapa, mateke yaliyowamaliza vojana wote waliokuwa wamemkamata kwa ajili ya maandalizi ya mauaji yake ya kutisha.
Baada ya kumaliza zoezi la kuwaua vijana hao Azra alikuwa amechoka mfano wa jogoo lililotoka kupigana na mwenzake.

Alipiga goti chini kwa kutumia mguu mmoja na mwingine aliukunja kiaina akainama chini huku jasho ikimchuruzika na kudondoka ardhini.

Azra alikuwa anahema kama mbwa koko aliyekoswa jiwe na kukimbia mbio ndefu. Akiwa mahali hapo alikumbuka hatari iliyokuwa mbele yake kama angeendelea kuzubaa hapo kihayawani.

Mawazo ya kuondoka yakamuingia.
Akajikakamua na kuinuka kwa nguvu zake zote. Kisha akasogea mpaka kwa kinara aliyekuwa analiongoza kundi lile.

Akachomoa ufunguo wa minyororo iliyokuwa imemfunga kwenye suruari yake kisha akajifungua minyororo hiyo na kubaki huru.

Azra abaada ya kujifungua aliangalia mikono yake iliyokuwa na alama za minyororo akagundua ipo fiti kwa ajili ya kazi, akaanza kuondoka katika eneo hilo.

Nia yake ilikuwa ni kwenda kumtafuta mpenzi wake Jemima kwa sababu kwa vyovyote vile alifahamu pia msichana huyo alikuwa kwenye hatari kwa kitendo chake cha kuanzisha uhusiano naye.

Haikumpa shida kufika kwao Jemima kwa sababu wakati huo alikuwa mwenyeji katika maeneo hayo. Kilichomshangaza baada ya kufika mahali hapo alikuta maiti za watu wawili, mama Jemima na mwanaye Kalega!
 
SEHEMU YA 57

AZRA alishituka, alamu ya hatari ilivuma kwa kasi kichwani mwake, akapoteza mapigo ya moyo hasa mawazo ya kwamba huenda mpenzi wake Jemima naye alikuwa amepoteza maisha.
Ikawa kazi ya kumtafuta Jemima mahali hapo.

Aliingia ndani ya nyumba lakini hakufanikiwa kumuona. Alitoka nje na kuizunguka nyumba hiyo pia hakumuona, kila kona ambazo alihisi anaweza kumuona mahali hapo hakuweza kumuona, baada ya kuzunguka alirudi kule mbele uwanjani akiwa anafikiria achukue uamuzi gani.

“Hapo hapo ulipo!” Ilikuwa ni sauti ambayo ghafla Azra aliisikia kutoka nyuma yake baada ya kurudi uwanjani kabla hata hajajiweka sawa.

Alitazama kwa jicho la wizi kupitia kwenye pembe la bega la mkono wake wa kulia na kuona kwenye kivuli kuna mtu alikuwa ameshika mkuki nyuma yake. Na aligundua wazi ni miongoni mwa wapambanaji wa Swadege ya Rwadege.

Azra hakutaka kuwa na papara, alifahamu kosa lolote lile ambalo angefanya ndilo lingemsukuma mpaka kwenye vyumba vya wafu kuzimu. Akatulia kama maji mtungini na kunyoosha mikono juu.

“Umeua ndugu zangu ni muda wako wa kufa,” Yule jamaa aliyekuwa nyuma yake alimwambia huku anavuta mshale.

Azra aliliona jambo hilo kupitia kwenye kivuli, mawazo ya kumuwahi jamaa huyo hapohapo yakaingia, bila kupoteza wakati aliruka sambasoti ya nyuma, ile mshale umeachiwa ukapita kwa kasi wakati anaruka na akapishana nao.

Jamaa akabaki ameduwaa, Azra hakutaka kufanya kosa, akiwa angani alijigeuza kwa namna ambayo ilimuwezesha kurusha teke, jamaa akapata teke la shingo na kuruka pembeni akiugulia kwenye maumivu.

Baada ya teke hilo, jamaa aliinuka na kujipanga kupambana. Akamsogelea. Azra akataka kutumia nafasi hiyo kurusha mateke mengine, jamaa akayaona na kuyakwepa, akaruka kwa namna yake na kumtia Azra teke la tumbo, akaruka juu ile anatua akakutana na teke lingine lililompeleka chini huku akilia kama ndege aliyepigwa na jiwe la manati.

Kipigo hicho ndicho kilichomfungua macho Azra. Akafahamu alikuwa anapambana na mtu wa aina yake. Fundi wa mapigo ambaye kama angemletea shoo game basi angemwendoa jambo ambalo hakuwa tayari litokee.
 
SEHEMU YA 58

AZRA Malama alijipanga tena kwa kujikusanya kutoka ardhini na kuinuka. Akamsogelea jamaa huku wote wakitazamana kwa namna ambayo kila mtu alikuwa akimsubiri mwenziye arushe pigo na amdhibiti.

Katika kupeana nafasi huko Azra ndiyo aliuona mwanya. Akatumia ujanja kwa kupiga teke ardhini, mchanga ukaruka juu , jamaa yule akatoa macho kuutazama mchanga, hilo ndilo kosa kubwa alikuwa amefanya kwa Azra, kwani hakumchelewesha, aliruka juu na kumpiga mateke mawili ya nguvu yaliyompeleka chini, kabla hajainuka Azra alimuwahi mahali hapo na kumnyonga mkono kwa nyuma kwa nguvu zake zote kisha akauvunja.

Mpambanaji yule wa Swadege alilia kwa maumivu yasiyo na mfano na kuanza kufurukata kama samaki aliyenasa kwenye mtego, maumivu hayo yakiwa hayajapona Azra alishika mkono mwingine ili nao pia auvunje.

“Jemima yupo wapi?” Azra aliuliza kwa sauti yenye hasira na mkazo.
“Sifahamu,” jamaa huyo alibwabwaja akiugulia kwenye maumivu.
Jibu hilo ni kama lilimwambia Azra nyonga mkono.

Akaunyonga, jamaa akaanza kupiga kelele za maumivu.
“Niambie Jemima yupo wapi la sivyo nakuvunja kiungo kimoja komoja.”
“Kakimbia…” Jamaa ilimbidi azungumze.
“Kakimbilia wapi?”
“Huko porini.”

Baada ya majibu hayo Azra alimmaliza jamaa huyo kwa kumnyonga shingo. Hakutaka kupoteza muda akiwa mahali hapo. Aliinuka na kukimbilia mpaka kule alikoelekezwa kwamba ndiko Jemima alikuwa amekimbilia.

Baada ya kuingia porini aliweza kuona kwa mbali vizinga vya moto na alizisikia sauti za watu wakiimba nyimbo za mapambano, moja kwa moja alifahamu lilikuwa ni Kundi la Shebo lililokuwa linamtafuta Jemima. Akaongeza tahadhari ya kulifuata kundi hilo, akaamua kupita njia nyingine.

Katika njia hiyo aliyo amua kupita akiwa anasonga mbele, mara ghafla alisikia vishindo kama vya mtu aliyekuwa anakimbia kwa kasi kuja uelekeo aliokuwepo, Azra akachukua kificho mahali kuona mtu huyo ni nani. Akiwa kifichoni hapo mtu huyo alivyokaribia kupita Azra alimrukia na kumdaka kwa kasi kisha akamziba mdomo.

Kumtazama alikuwa ni Jemima!
“Jemima,” Azra aliongea kwa kunong’ona.”

Jemima alizungusha macho na kumuona ni Azra mpenzi wake. “Azra,” akaita kwa uchungu akishindwa kuzuia machozi. Wakakumbatiana!

ITAENDELEA…
 
SEHEMU YA 59

“Pole sana mpenzi,”Azra alimwambia Jemima.
Jemima alishindwa kujibu, alizidi kugugumia kwenye kilio huku uso wake akiusindika zaidi kifuani kwa Azra.

Kwa mbali alianza kuihisi amani moyoni mwake na kuwa kwenye mikono salama.
“Nilifikiri wamekuua,” mwishowe Jemima alimwambia Azra kwa sauti ya taratibu akivuta makamasi ambayo hakuwa nayo.

“Siyo rahisi wanajeshi kumuua mfalme wao mpenzi.” Azra alimjibu.
Jemima alipitisha ukimya wa muda.
“Mama na kaka wameuawa,” kisha alimwambia Azra.

“Ninafahamu.”
“Umefahamu vipi?” Jemima aliinua kichwa chake kutoka kifuani kwa Azra huku akiwa amebaki amemkumbatia tu alimuuliza.

“Nilipokuwa ninakutafuta nilikwenda nyumbani kwenu, ndipo nimekuta maiti zao.”
Jemima alilaza kichwa chake na kurudia kulia upya.

“Naomba unisamehe, ni mimi nimeigharimu familia yako na kusababisha hayo yote yanayoendela kisiwani hapa,” Azra alizungumza kwa sauti iliyomaanisha kuomba radhi.

“Usijali Azra,” Jemima alimjibu. “Wewe ni mtu wa Swadege ya Rwadege ni ujinga wa ndugu zangu kukubali ukweli. Nitasimama upande wako mpaka mwisho kwa sababu ninakuamini Azra na ninaamini unapigania kilicho chako na haki yako.”

“Asante sana Jemima kusikia maneno kama haya kutoka kwako, ninakupenda sana.”

“Ninakupenda pia Azra Malama,” Jemima alimjibu. “Nitakupenda pia siku zote mpaka roho yangu itakapoungana na roho za ndugu zangu.”

Hata hivyo wawili hao wakiendelea kufarijiana, mara walianza kusikia vishindo na fukuto kutoka upande wa pili wa mahali walipokuwa. Ikabidi wakae sawa kusikiliza nini kilikuwa kinaendelea.

Wakiwa wametega masikio sawia, waliweza kugundua yalikuwa ni mapambano lakini ambayo hawakufahamu ni mapambano kati ya kundi la Shebo na kundi gani.

Wakizidi kusikiliza vizuri na kusikia vilio vya watu ndipo kumbukumbu ya kukimbizwa na mbwa mwitu ilipomrejea kichwani Jemima. Moja kwa moja akatambua kwamba kundi la Shebo lilikuwa linapambana na mbwa mwitu hao.

“Tuondoke!” Jemima alimwambia Azra.
“Kuna mapambano huko.”
“Ni kundi la Shebo na mbwa mwitu.”
“Sawa.”
Walipiga hatua za tahadhari na kuondoka katika eneo hilo.
 
SEHEMU YA 60

Azra Malama na Jemima walitembea yapata saa mbili mpaka wakafanikiwa kutoka kwenye pori hilo wakiliacha kundi la Shebo. Jemima alikuwa amekwisha choka na kutepeta, Azra alimkokota na kumwambia ajikaze kwani walikuwa bado na safari ndefu.

Jemima hakuwa na namna zaidi ya kujikaza kama ambavyo alikuwa ameambiwa, safari ikaendelea mpaka kwenye milima ya Uwandani ambako kulikuwa kuna mapango mazuri kwa ajili ya kujificha chimbo ambalo Azra alikuwa amekwisha lifanyia uchunguzi na kuona kwamba linamfaa. Huko alimficha Jemima na kumwambia alihitaji kwenda wanakoishi wazee wa Swadege kwa ajili ya kufuata vitu vyake.

“Nenda kwa tahadhari,” Jemima alimwambia.
“Usijali, hakikisha hutoki hapa.”
“Sawa.”

“Nakupenda.”
“Nakupenda pia Azra.”
Jemima na Azra kwa sekunde kadhaa walinatishiana midomo yao na kupeana busu lenye afya kisha Azra akaondoka katika eneo hilo.

Yapata majira ya saa sita kuelekea saa saba usiku ndipo alipoweza kufika kwenye eneo waliloishi wazee wa Swafege.

Baada ya kufika kwenye maeneo hayo ilibidi aongeze tahadhari kwani kwa maafa aliyokuwa amekwisha yasababisha alifahamu wazi hakuna ambaye alikuwa anampenda, hata mzee Makimbi mwalimu wake kule kwenye kijiji cha Amani alifahamu wazi hakuwa anampenda tena.
Eneo hilo lilikuwa limetawaliwa na ukimya wa hali ya juu.

Azra alizidi kunyata mpaka akafikia nyumba aliyokuwa amepewa aishi mahali hapo, kwa tahadhari ya nguvu akaizunguka nyumba hiyo mpaka mlangoni na kuufungua mlango ambao alikuta umeegeshwa.
Akaingia ndani.

Baada ya kuingia macho yalikuwa upande alipotunza vitu vyake. Kwa namna ambayo hakuitegemea begi lake halikuwepo Azra akatoa macho mfano wa mtu ambaye haamini kile ambacho alikuwa anakiona. Akasogea ili kuthibitisha zaidi.

Ile anapiga hatua akahisi kuna kitu kinarushwa upande wake kutoka nyuma, kumbe lilikuwa ni teke, akapindisha kichwa na kuchezesha mwili kwa kasi, teke hilo likamkosa, Azra akaruka sambasoti kama kawaida yake na kutulia chini kwa staili ya nge kutazama ni nani aliyekuwa anarusha mapigo.
Alikuwa ni Shebo.
Kamanda mkuu wa mapambano Swadege!
 
SEHEMU YA 61

Azra alimfahamu vyema Shebo, sifa zake za mapambano amekwisha zisikia mara kadhaa akizungumziwa, alitambua anapambana na mtu hatari.

Lakini pia kitendo cha Azra kumuona Shebo mahali pale, alifahamu wazi alikuwa amepona kule msituni na alikuja kumsubiri hapo akifahamu ni lazima angekwenda mahali hapo.

“Jisalimishe,” Shebo aliyeonekana kuwa na hasira alimwambia Azra kwa sauti iliyojenga utulivu.

Azra alimtazama mfano wa mtu anayetazama sanamu.

Kitendo cha Azra kuonyesha dharau kilimkasirisha Shebo, Shebo kwa kitendo cha haraka aliruka juu na kupiga teke taa iliyokuwa inamulika mwanga kwenye chumba hicho, ikavunjikavunjika, kukawa giza ghafla.

Azra alitoa macho ili kumtazama mtu huyo yupo wapi lakini ilikuwa ni sawa amefumba macho, alikuwa anaona giza tu, na akiwa bado hajapata maamuzi ya kuchukua alishitukia kitu kizito kikimsukuma kifuani, akaruka na kujipiga ukutani.

Alikuwa amepokea teke la nguvu.
Azra akaanza kuugulia kwenye maumivu huku anajikokota chini. Akiwa hajakaa sawa pigo lingine likamfuata mahali hapo, wakati huu pigo hilo lilimuingia sawasawa mpaka akatoa sauti ya juu ya maumivu.

“Mimi ndiye Shebo, Mswadege ya Rwadege,” Shebo alianza kutamba katikati ya giza hilo akijipigapiga kifuani.
Azra Malama akiwa chini alianza kujikusanya taratibu ili kupambana na mtu huyo.

Shebo ambaye utafikiri gizani ndipo alikuwa anaona zaidi, alimfuata Azra Malama pale chini na kumuinua kisha akaanza kumpiga ngumi za nguvu za usoni.

Damu zikawa zinaruka juu.
Baada ya kumpiga ngumi kadhaa Shebo alimuachia tena Azra, kijana huyo akadondoka chini huku katepeta. Moyoni alianza kuhisi kwamba anakwisha kwani Shebo alionekana kuwa na nguvu zaidi.

Akiwa chini anajaribu kufurukuta ndipo Azra alihisi ameshika kitu chenye ncha kali, alipokishika zaidi, aligundua ni nondo iliyochongoka mbele. Azra aliichukua nondo hiyo na kuichimbia kwenye nguo zake.

Shebo akamfuata tena na kumshika nywele ili amuinue, Azra akajitepetesha na kuinuka, kumbe ilikuwa ni janja yake, Azra baada ya kuinuka juu, kabla Shebo hajamuongezea ngumi za usoni, Azra alichomoa kile chuma na kumpachika Shebo katikati ya kifua.

Shebo alilia kama hayawani akipepesuka kutokana na maumivu!
 
SEHEMU YA 62

SHEBO alidondoka chini kama gunia. Tena gunia lenye mzigo mzito. Damu ikatapakaa kila mahali alipodondokea. Azra alifahamu amemmaliza.

Baada ya kujua kazi imekwisha Azra alijikusanya na kusimama, akapepesuka kabla miguu haijapata stamina nzuri ya kukaza na kusimama imara.

Kisha alipiga hatua mpaka mahali alipokuwa anatunza vitu vyake, akachukua begi lililokuwa na nguo, shajara aliyoandika mambo mbalimbali kuhusu kisiwa hicho cha maajabu, pamoja na vitu vyake vingine vya siri. Akatoka kwenye chumba hicho huku anachechemea.

Alipofika nje alianza kupiga hatua ili kuondoka eneo hilo, baada ya hatua tano aligeuka na kuitazama nyumba ambamo alimuacha Shebo, Azra hakuridhika kuiacha kama ilivyo.

Akarudi na kuchukua kizinga cha moto kwenye kuni zilizokuwa zinawaka nje, kisha akaishikisha moto nyumba hiyo na nyumba zote zilizokuwa jirani. Moto ukawa mkali na kupamba eneo hilo, Azra aliondoka kifua mbele moyo wake ukiwa na imani kwamba ameharibu kila kitu.

*** TAARIFA juu ya Azra Malama kusababisha maafa makubwa ndani ya Kisiwa cha Swadege ya Rwadege zilifika kwa mzee Makimbi na watu wote ambao walikuwa wanafanya shughuli zao za kujikomboa kifikra kwenye kijiji cha Amani.

Watu wote waliozisikia taarifa hizo walisikitika sana. Kilichowachanganya zaidi wengi wao walijiuliza ni kwa nini Azra alikuwa ameamua kufanya jambo hilo la kuivuruga amani ya watu wa Swadege ya Rwadege!

Watu ambao waliishi miaka mingi kwa amani, wakifurahia aina yao ya maisha na zawadi za asili ambazo Mungu aliwajalia.

Kwa upande wa mzee Makimbi matukio aliyoyafanya Azra yalimfanya atumie muda mwingi kumfikiria kijana huyo.

Fikra ndizo zilizomkumbisha siku ya kwanza alipoletwa na vijana wapambanaji kwenye himaya yake na yeye kukabidhiwa akiambiwa kwamba ni ametokea Marekani, lakini alidai ana asili ya Swadege ya Rwadege.

Mzee Makimbi alikumbuka wapambanaji wa kisiwani hapo walivyokuwa wanawasiwasi dhidi yake.

Akaiona hatia ya yeye kumruhusu Azra kuishi naye akiamini kwamba ni mtu mwema aliyeikumbuka asili yake. Mbali na kujivika hatua, mzee Makimbi aliwaza kuingia kwenye uwanja wa mapambano!
 
SEHEMU YA 63

NITAPAMBANA naye v ipi? Hilo ndilo swali alilojiuliza. Akatafakari kwa kina. Wakati wa kutafakari ndipo alipomkumbuka Michael na Jaji Kessy kwamba wanafahamiana na Azra, akapanga kuwauliza juu ya kijana huyo kabla ya kuchukua uamuzi wowote.
Mzee hakuwa na muda wa subira.

Alikutana na wawili hao na kuwaeleza juu ya kile alichohitaji kukifahamu.
“Ni mtu hatari,” Michael alimwambia baada ya kumsikiliza. “Kiasi gani?” Mzee Makimbi aliuliza.

“Zaidi ya fikra za kawaida, na anaweza kuangamiza kisiwa hiki chote!”
Maneno ya Michael na hata Jaji Kessy alipochangia kumhusu Azra Malama yalimshitua mzee Makimbi!

Hata hivyo mzee huyo alihitaji kupambana na Azra. Haikujalisha alikuwa ni hatari namna gani lakini alihitaji kuirejesha amani ya Waswadege kule ilipokuwa.

Alichokifanya mzee huyo ilikuwa ni kuzungumza na wawili hao, kuwaomba wasaidiane naye kwenye mapambano ya kumuondoa Azra Swadege.

Mwanzoni alipowapa wazo hilo, Michael kidogo alisita. Akakumbuka namna Azra alivyomuomba kusaidiana naye kukitawala kisiwa hicho.
Aliweka ngumu, ila kuna muda alikuwa ameanza kulegeza.

Michael akaikumbuka sababu iliyompeleka kisiwani hapo, ilikuwa ni kujikomboa na kuishi maisha nje ya uhalifu, maisha yenye amani na maana katika dunia huru. Aliona hakuna sababu ya kushirikiana na Azra kuiteketeza Swadege ilihali hayakuwa maisha aliyotaka kuishi tena.

Alipowaza hayo yote akakubali kushirikiana na mzee Makimbi kwenye vita ya kupambana na rafiki yake wa zamani Azra Malama.

Mzee Kessy alikubali kushiriki hata kwa mawazo tu. Wakajipanga kwa ajili ya vita. *** Azra alifika kwenye milima ya Uwandani alikokuwa amemuacha Jemima.

Alimkuta msichana huyo kwenye maficho hayo. Akatua begi, wakakumbatiana na kusalimiana.
“Inabidi tusafiri kwa muda,” Azra alimwambia Jemima.

“Twende wapi?” Jemima alimuuliza kwa mshangao.
“Madagasca.”
“Kuna nini?”

“Kuna mawasiliano nataka kufanya Marekani halafu tutarudi.”
Jemima kusikia kwamba Azra anataka kufanya mawasiliano Marekani moyo wake ulishituka.

Haraka mawazo yakakimbilia kufikiri kwamba pengine mpenzi wake huyo anashirikiana na Wamarekani na ndiyo sababu ya kupambana kuwa mfalme wa kisiwa hicho. Lakini bila sababu ya msingi alijikuta ak
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom