SEHEMU YA 79
WAWAKILISHI kutoka mataifa mbalimbali walikua wamekusanyika kwenye Ukumbi wa St. Lois Elizabeth, jijini London, Uingereza.
Katika ukumbi huo kulikuwa na kikao mahususi kilichokuwa kinahusu nchi washiriki wa Jumuiya ya Umoja wa Mataifa, ambapo kisiwa cha Swadege ya Rwadege kuliomba kushiriki kama mgeni mualikwa, kwa sababu hakikuwa kwenye jumuiya hiyo.
Kilikaribishwa.
Shamlashamla zikashamili, na kikao hicho kilikuwa kinaogozwa na katibu wake James Vero, kutoka nchini Ghana.
Kwenye kikao hicho, mambo mengi yalijadiliwa na wawakilishi hao ambapo baada ya ratiba zote kufanyika alikaribishwa muwakilishi kutoka kisiwani Swadege ya Rwadege, kupanda jukwaani kwa ajili ya kuzungumza ujumbe alio uandaa kwa wana jumuia wa Umoja wa Mataifa.
Kamanda wa Jeshi la Swadege ya Rwadege, Shebo, alisimama.
Alikuwa amevaa mavazi ya asili. Shati lake lilikuwa ni la sufi lililonakishiwa kwa urembo wa ngozi ya simba na vikorombwezo vingine.
Chini alikuwa amevaa pensi iliyotengenezwa kwa ngozi ya chui, pembeni ya kiuno chake alichomeka ala yenye panga.
Shebo taratibu alikatiza katika ya wanajumuiya hao na kwenda kusimama mbele yao kabisa akawa anawatazama wao.
Ukumbi mzima ulikuwa kimya kumsikiliza yeye. Kijana huyo ambaye alionekana kivutio mahali hapo kutokana na mavazi yao, yaliyokuwa yanawawakilisha wana Swadege ya Rwadege, alirekebisha sauti ili azungumze;
“Hii ni simulizi ya kaka zangu na dada zangu, tunaoishi katikati ya maji,” Shebo alianza kuzungumza. Watu wote wakaongeza umakini kumsikiliza.
“Kwa muda mrefu dunia imekuwa ikipambana na sisi ili tu, iharibu aina ya maisha ambayo tumechagua kuishi. Mataifa makubwa na watu mbalimbali wanatamani tuishi kama wao, tuvae kama wao, tutembee kama wao na tutende kama wao.
“Lakini sisi tunaamini kupitia kile Mungu alichotubariki. Katuwekea upendo katikati yetu, katupa vipaji vinavyoongeza ustadi kwenye aina ya maisha tunayoishi na ametupa fahari ambazo zinatusaidia kuboresha miundo mbinu na kutibu wagonjwa.
“Tunajivunia kuwa Waswadege. Tutaishi tutakavyo na si dunia itakavyo. Hii ni kwa ajili ya mtu mmojamoja duniani pia. Ishi wewe na si uishi vile mtu mwingine anahitaji uishi.