Ijapo comment yako imekuwa ya siku nyingi na bahati mbaya sikuwahi kuiona, lakini imebeba majibu ya kweli na uliiandika kisomi sana.
Mleta mada kajibiwa majibu mengi kwa jazba sana na wengi waliomjibu hawakumuelewa.
Jibu lake lilikuwa ni fupi sana kwamba mishahara ya wanajeshi hulipwa kwa vyeo na si kwa viwango cha elimu kama zilivyo taasisi zingine, period
Ingawa kuna malipo ya elimu, hizo ni posho tu na si mshahara.
Duniani pote, mtu hawezi kupaparikia kazi flani bila kuelewa manufaa yake hasa kimaslahi.
Awe rais, awe mbunge awe jaji nk nk, hawezi kutaka ama kukipokea hicho cheo bila kujua manufaa na maslahi yake.
Kweli tunapokuwa wadogo, kila mtu hutamani kufanya kazi flani atakapokuwa mtu mzima na hufurahi sana akiajiriwa nayo, maana moyo wake ndiko unakopenda.
Lakini wengine hubadilishia gia angani kwa kuona wanakokupenda hapawafai maana si lolote si chochote kimaslahi, kwani jambo hilo ni siri?
Kama ulivyosema katika comment yako, sisi wazee ndiyo tulikuwa tunaingia kazi za namna hiyo kwa kupigwa hamasa kwamba huo ndiyo uzalendo uliotukuka, kuifia nchi na kwamba unapoingia kazi hizo unalitumikia taifa lako na kulijenga.
Hizo zote huwa ni blah blah, lakini ukweli tunafuata mishahara na maslahi yahusuyo.
Maana huwa inafikia sehemu unaambiwa ukweli kabisa kwamba, na hayo maneno nilishawahi kuelezwa mimi mwenyewe kutokana na kuringia taaluma niliyokuwa nimetoka kuisomea na kuanza kujiona mimi wa muhimu na ninategemewa sana:..."wewe kamwe hautegemewi na taifa hili, isipokuwa wewe ndiyo unalitegemea taifa kwa njaa zako, ukitaka kutoroka wee toroka uone kama kuna mtu atakufuatilia kwa ajili ya hako kaujuzi kako"....
Maneno ya dharau sana, lakini baadaye hasira zikikushuka, unaanza kuuona mwanga wa ukweli na kujijibu kisukuma 'iii lakini ni kweliii'.
Ninakumbuka, wakati tujiandaa kuingia vitani Msumbiji(awamu ya mzee ruksa), kuna maswali ya kimaslahi niliwahi kumuuliza mkuu wa majeshi wa enzi hizo alipokuja kutuaga tulipokuwa "concentration area" kabla hatujaondoka.
Wenzangu walinishangaa sana kwa maswali yangu hayo ya kimaslahi, kutokana na nidhamu ya uoga ya enzi hizo, maana waliona kama ninamwaga mboga kabla ya kumwagwa kwa ugali live!
Tulifundwa kwamba kwa mfano; mkuu wa majeshi ama rais anapowatembelea, mnapeleka maswali yenu kwa viongozi na kisha maswali hayo kupimwa na kuchujwa, swali lililokosa kibali cha kuulizwa ni marufuku kuliuliza na ukiliuliza ki makame nguvu, kiongozi huyo aliyekuja ziara akishaondoka, unarundikwa ndani kwa makosa ya utovu wa nidhamu.
Eti swali ama ombi lolote unalomuuliza mheshimiwa, huwa siyo swali ama ombi, bali huwa ni amri umempa akatekeleze, kwa hiyo viongozi wa wakati huo walikuwa makini sana juu ya uulizaji maswali ya wafuasi wao.
Hili lina ukweli kiasi, maana maswali yote niliyoyauliza yalikuja kutekelezwa baadaye.
Wauliza maswali ya kimaslahi enzi hizo, ilikuwa saazingine kiongozi anapokuja ziara, unazuliwa ishu ya kinidhamu hata kwa kosa dogo tu la kusahau kufunga kisikizo cha shati, unatupwa mahabusu hadi kiongozi amalize ziara yake, ili kukukata ngebe zako.
Niliuliza swali moja na kutoa ombi moja, jumla mawili.
La kwanza lilikuwa:...." huko Msumbiji tunakopelekwa hivi sasa, tayari tulishawasaidia sana kabla hadi wakapata uhuru..."wenzetu waliouawa huko na kupata vilema vya kudumu, mpaka sasa hakuna malipo yoyote ya operesheni wanayostahili kulipwa waliyokwisha kupewa baada ya operesheni hiyo kumalizika na kurejea numbani,....". Tunavyorudishwa tena huko wakati nchi zimeingia mikataba ya kiulinzi, tunaomba tuelezwe safari hii tutalipwaje ama maslahi yetu yatakuwaje?"....
La pili ambalo lilikuwa ni ombi:
..." wenzetu waliouawa Uganda kwa vita vya Amin walizikwa kishujaa Kaboya.... lakini waliouawa Msumbiji walizikwa huko huko, huo ni ubaguzi, lengo la vita zote ni kutetea nchi na uhuru wa watu wake... operesheni zote ni sawa, je mashujaa ni wa Unganda tu na wa Msumbiji si mashujaa?... Niombe sasa, safari hii tutakaokwenda kufia huko, maiti zetu zirejeshwe kuzikwa nyumbani na tuzikwe kishujaa kama wenzetu..... Na kama jambo hilo halijaandaliwa kama kwa Kaboya, basi maiti zetu zirejeshwe nyumbani wakabidhiwe wazazi wetu watuzike wenyewe.....yangu yalikuwa ni hayo tu fandee" .
Wakati nikiuliza hayo, viongozi wamekazana kuandika kwenye note book zao.
Majibu niliyopewa sasa[emoji38][emoji38][emoji38][emoji38], yalikuwa ni ya kiugumu, yaani kavu kavu.
...."wewe ni mwenyeji wa wapi unauliza mambo ya pesa kama malaya?...
Halafu ombi lako la sijui maiti kurejeshwa nchini, jambo hilo halitawezekana,.... Kwa hivi sasa tuna ndege moja tu ya utawala.... sasa kama mjuavyo operesheni, vifo vinaweza kutokea hata zaidi ya mara tano kwa siku moja,...ndege imekwenda imebeba imerejea,... sasa itarudi mara ngapi hukoo?.... wote mtakaofia huko mtazikwa huko huko".
Hayo yakawa ndiyo majibu.
Majibu ya kijeshi ni mafupi na yenye kueleweka, hayatakiwi kurembwa rembwa.
Ieleweke kwamba, unapofika mstari wa mbele kukabiliana na adui, adui ambaye saazingine mwerevu kukushinda hata wewe, huwa kuna mtihani mkubwa sana.
Uongo tunaojidanganya kwamba unalilinda taifa huwa unakutoka kichwani kiwepesi mno pindipo unapoingia kwenye moto wa udui kindaki ndaki, ndiyo hapo utaelewa kwamba unalilinda taifa kweli ama unajilinda mwenyewe na nafsi yako.
Kama nilivyosema hapo juu, ingawa nilijibiwa kibabe na mkuu wangu huyo, lakini swali langu na ombi langu, vyote vilikuja kufanyiwa kazi.
Jibu la kuelezwa tutakachoenda kulipwa huko, lilikuja kabla ya wiki1, mara tu mkuu wa majeshi huyo alipomaliza ziara yake.
Tulielezwa kwamba maafisa na askari wanaoenda huko, wataenda kulipwa dollar ngapi ngapi kwa kila mwezi, pia wale wanaoacha familia zao kambini, familia hizo(wives) zitalipwa ration allowance kila mwezi hadi watakaporejea(hapo ndipo malipo ya Ration allowance yalipoanzia).
Ombi langu la kuzikwa nchini, ingawa lilichelewa kwa wenzetu tuliokwendanao kupoteza maisha na kuzikwa huko, lakini ombi hilo lilikuja kutekelezwa na serikali ya awamu ya tatu kwa kwenda kuichukua miili yote iliyokuwa imezikwa huko na kuja kuizika upya kwa heshima nchini.
Wote wanaosema kujitolea, sijui wanasukumwa na moyo wa uzalendo hata bila kutega sikio kusikia stahili zinazohusu kazi wanazoenda kuzifanya, mi huwa ninasema ni waongo'mbwa na ni wanafiki wakubwa.
Sent using
Jamii Forums mobile app