2008-02-09 08:39:47
Na Mary Edward, Dodoma
Kambi ya upinzani, imependekeza kuwa, Rais mstaafu Bw. Benjamin Mkapa achukuliwe hatua kwa madai ya kushiriki ufisadi na kujimilikisha mradi wa makaa ya mawe wa Kiwira mkoani Mbeya.
Walimtaka Rais Jakaya Kikwete, aache kumtetea kwa kauli za `mwacheni Mkapa apumzike amestaafu` kwa kuwa hakuna sheria inayomlinda Rais aliyestaafu kushtakiwa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mjini hapa, Naibu Kiongozi wa Upinzani, Dk. Wilbroad Slaa, alisema Bw. Mkapa amejimilikisha asilimia 85 za mradi wa Kiwira, ujasiri alioupata akiwa Ikulu.
``Tutamshtaki Mkapa na sheria ya kumshtaki ipo, hana kinga kisheria,`` alisema kiongozi huyo.
Alisema baadhi ya taarifa alizoandika kwenye Ofisi ya Msajili wa Kampuni (BRELLA) zinaonyesha kuwa, alijisajili kama Ben Mkapa, mjasiriamali. ``Tutamshtaki kama mjasiriamali, si kama Rais,`` alisema.
Katika hatua nyingine, kambi hiyo ya upinzani imetaka maamuzi ya Baraza la Mawaziri yasifanywe kwa siri.
Kiongozi wa kambi hiyo, Bw. Hamad Rashid Mohamed, alisema katika mkutano huo kuwa, wakati umefika yanayoamuliwa katika baraza hilo, yakafahamika kwa wabunge na wananchi walioiweka serikali madarakani.
Alisema taarifa ya kamati ya Richmond imebainisha kuwa, maamuzi ya baraza hilo, yalivunjwa na kulisababishia taifa hasara, lakini kama yangekuwa yanafahamika kwa wabunge, suala hilo lisingekubalika kwani kila hatua ingekosolewa.
``Katika kikao cha Baraza la Mawaziri, iliamuliwa kuwa, TANESCO itafute mzabuni wa kuzalisha umeme wa dharura, lakini Wizara ya Nishati na Madini, ikapuuza agizo hilo kwa shinikizo la Waziri Mkuu aliyejiuzulu na kuvunja agizo la baraza hilo ambalo Rais wa nchi ni kiongozi.``
Akizungumzia Benki Kuu ya Tanzania (BoT), alisema Watanzania hawana imani nayo kwa vile msimamizi wa hazina ya Taifa, amevunja imani ya wananchi kwa kuandika barua na kufungua akaunti ya Richmond licha ya benki za nje kama Citi Bank kukataa kwa vile Richmond ni matapeli.
Alisema miswada ya nishati inayoletwa bungeni, haikubaliki kwa vile imelenga kuwahalalisha vigogo kuendelea kuinyonya TANESCO kwa staili ya Richmond ambayo inalipwa Sh. milioni 152 kwa siku.
``Kampuni ya uzalishaji umeme ya Aggreco, IPTL, Songas na Alstrom huchota kutoka TANESCO jumla ya Sh. bilioni 244 kwa mwaka,`` alisema Bw. Mohamed.
Alisema upinzani utashangaa kama mafisadi watateuliwa katika baraza jipya.
``Hatutamuelewa Rais endapo waliotajwa na kamati kwa namna moja au nyingine kuhusika na Richmond watateuliwa,`` alisema mbunge huyo wa Karatu (CHADEMA).
Walionya kutocheleweshwa kufikishwa Bungeni taarifa ya Ernst & Young inayohusu ufisadi wa BoT na kwamba itakuwa jinamizi kwa serikali na kusisitiza baraza jipya liiwasilishe ripoti hiyo na uchunguzi ufanyike kikamilifu.
``Kwa kilichotokea BoT, hatuna imani na kamati ya uchunguzi, hivyo Rais atafute wataalam wengine hata ikiwezekana kutoka nje na wanaoteuliwa watajwe kwa majina ili tujue namna ya kuwawajibisha,`` alisema.
Mwanasheria Mkuu ndiye Mwenyekiti wa Tume inayochunguza ufisadi wa BoT, na wajumbe ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Fedha za Serikali na Jeshi la Polisi.
SOURCE: Nipashe