Mkapa na Bulyanhulu, Kikwete na North Mara!
Julai 23, 2009
NAPENDA kuliendeleza kidogo suala lile nililolijadili toleo lililopita la vifo vilivyotokea katika mgodi wa Barrick wa North Mara, na pia vifo tunavyovitarajia kutokea vya wafanyakazi wa kampuni ya TanzaniteOne kutokana na ukaguzi wa kupitishwa, kila siku, kwenye mashine za mionzi kinyume cha matakwa ya Kamisheni ya Mionzi Tanzania (TAEC).
Hata hivyo, napenda kuanza kwa kukumbusha kidogo ya Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa. Alikuwa ni mtawala asiyetetereka wala kuyumba kimsimamo katika jambo aliloliamini (au mwenye maslahi nalo); hata kama jambo hilo linapingwa na wengi.
Kwa mfano, aliamini kwa dhati kwamba jibu la matatizo ya uchumi wa nchi yetu ni wawekezaji wa kigeni. Kwamba tatizo litapungua kama wawekezaji wengi wa kigeni watakuja nchini kuvinunua viwanda na pia kuwekeza katika migodi na kwenye sekta ya utalii.
Kwa sababu ya kuamini hivyo, ingawa wapinzani wa sera ya uwekezaji ya Serikali ya CCM walipiga kelele sana, ilikuwa sawa na kumpigia mbuzi gitaa ukitarajia acheze.
Kwa kumbukumbu zangu, mahali pekee alikopata kushindwa na akanyoosha mikono, ni kwenye mradi wa kamba kwenye Delta ya Rufiji.
Mkapa alitaka mwekezaji wa Ireland, John Nolan awekeze huko; hata kama mradi huo ungesambaratisha maisha ya mamia ya wavuvi wadogo wadogo katika delta hiyo. Lakini kishindo cha kuupinga mradi huo cha wanamazingira, mabalozi na wahisani wa nje kilikuwa kikubwa kiasi kwamba, hatimaye, Mkapa alinyoosha juu mikono!
Hata hivyo, kusambaratika kwa mradi wa kamba katika Delta ya Rufiji hakukumkatisha tamaa Mkapa; kwani aliendelea kuwakaribisha wawekezaji wa kigeni katika sekta nyingine kwa nguvu zake zote.
Kwa hakika, kila alipopata jukwaa la kuzungumzia suala hilo, Mkapa hakusita kulitumia kuwahakikishia wawekezaji wa nje kwamba anawaamini (yawezekanaje umuamini mwekezaji wa nje?), atawalinda na anawakaribisha nchini.
Kwa mfano, pamoja na kelele nyingi zilizopigwa na wananchi kuhusu jinsi machimbo ya Mererani na Geita yanavyowanufaisha wageni (makaburu) badala ya wazawa, bado Mkapa alikwenda Afrika Kusini kuwakaribisha wawekezaji zaidi wa sekta ya madini kutoka nchi hiyo.
Kama vile hiyo haikutosha, Mkapa aliamua kuwapa majaji na mahakimu nchini changamoto ya kuwalinda wawekezaji wa kigeni (badala ya wazawa) alipokwenda Arusha kufungua mkutano wao.
Kwa hiyo; tunapolalamika, leo hii, suala la mikataba mibovu katika sekta ya madini mikataba isiyozingatia maslahi ya nchi, asili yake ni Mkapa; kwani aliweka mazingira ya wawekezaji wa kigeni katika sekta hiyo kulindwa iwezekanavyo; hata pale maslahi ya taifa yanapokuwa hatarini!
Kwa hakika, uumini wake kwa sera za uwekezaji wa kigeni katika sekta ya madini unaweza kupimwa vizuri na kauli aliyopata kuitoa wakati akifungua mgodi wa Bulyanhulu uliopo Kahama, Shinyanga. Mkapa alisema hivi: Wanaopinga sera za uwekezaji katika migodi ni wenye uchovu wa akili lakini waliojificha katika mwavuli wa wanataaluma.
Mapenzi hayo ya kupindukia kwa wawekezaji wa kigeni katika sekta ya madini ndiyo yaliyomfanya Mkapa kukataa katakata kuundwa tume huru kuchunguza madai mazito ya mwaka 1996 kwamba watu 30 walikufa kwa kufunikwa na matingatinga wakati zilipochukuliwa hatua za kuwahamisha kwa nguvu wachimbaji wadogo wadogo katika eneo hilo ili mwekezaji wa kigeni (Barrick) apate kuingia.
Japo wanaharakati wa haki za binadamu wa ndani na nje ya nchi waliwasha moto hadi Benki ya Dunia (WB) na kwa serikali ya Canada kutaka wafute udhamini kwa Barrick kwa sababu ya kuhusika na mauaji hayo, Mkapa aliendelea kuikingia kifua mwanzo hadi mwisho, na hakutaka kamwe tume huru kuundwa kuchunguza.
Kwa sababu ya hulka yake hiyo ya kuibeba Barrick na kukataa tume huru kuundwa; ukweli kuhusu madai yale kwamba kuna watu 30 waliofukiwa katika eneo la mradi huo, haukuweza kuthibitishwa hadi Mkapa anaondoka Ikulu.
Mkapa na wasaidizi wake walikanusha kwa nguvu zote madai ya kufukiwa watu hao, lakini hapo hapo hawakutaka kabisa tume huru iundwe na ufukuaji mpya ufanyike ili ukweli ufahamike! Kwa nini walikataa? Jibu ni dhahiri; nalo ni kwamba hatua hiyo isingekuwa na maslahi kwa Barrick; hata kama ni maiti moja tu ingepatikana!
Hayo ndiyo ya Mkapa. Alimaliza muda wake wa urais na kuondoka Ikulu mwaka 2005 bila kukitegua kitendawili hicho cha Bulyanhulu. Na ukweli ni kwamba hakutaka kukitegua.
Sasa tunaye katika Ikulu yetu Rais wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete. Naye huyu, hivi karibuni, ametwishwa kitendawili kingine kinachowahusu pia wawekezaji wa kigeni katika sekta ya madini.
Kitendawili hicho ni kile kinachouhusu Mgodi wa North Mara unaomilikiwa na kampuni ya Barrick. Mgodi huo umekuwa ukiachia sumu kuingia katika mto Tingithe, na hivyo kusababisha vifo vya zaidi ya watu 25; huku wengine wakiwa wamechubuka na kuvimba miili.
Idadi ya waliokufa (ikiwemo mifugo) inatarajiwa kuongezeka kwa sababu sumu hiyo aina ya cyanide huutafuna mwili kidogo kidogo, na hivyo athari zake ni za muda mrefu.
Hiyo ina maana kwamba waathirika wataendelea kufariki kidogo kidogo miaka mingi tu baada ya Barrick kuondoka North Mara wakati dhahabu katika mgodi huo itakapomalizika. Kwa ufupi; makovu na machozi yanayotokana na uwekezaji wao tutabakinayo miaka mingi tu baada ya wao (Barrick) kufungasha virago!
Hata hivyo, wakuu wa mgodi huo wamekuwa wakikanusha kuhusika na uingiaji wa sumu hiyo katika mto Tingithe ambao maji yake hutumiwa na wananchi kwa ajili ya mifugo na matumizi ya nyumbani. Na si tu wanakanusha kuhusika, lakini pia wanailaumu serikali kwa kuruhusu wanavijiji kulikaribia eneo la mgodi kinyume cha sheria.
Suala hili nyeti la mgodi wa North Mara linalohusu maisha ya Watanzania wenzetu limeibua mjadala mkubwa sehemu mbalimbali nchini; kama lilivyokuwa suala lile la mwaka 1996 la madai ya kufukiwa wachimbaji wadogo weadogo katika mgodi wa Bulyanhulu.
Kwa sababu ya kishindo cha kelele za wanavijiji wa North Mara, wanaharakati wa haki za binadamu, wabunge na vyombo vya habari, timu ya Bunge ilikwenda huko kufanya utafiti, na tayari imeshawasilisha ripoti yake kwa Spika. Ripoti hiyo bado haijawekwa wazi bungeni na kujadiliwa.
Aidha, Serikali mpaka sasa imepeleka watendaji wake wawili waandamizi (mawaziri wawili) kwenda North Mara kutafuta ukweli na kuuwasilisha kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Lakini mpaka sasa bado hatujui kilichomo kwenye ripoti zao. Hata hivyo, tunachofahamu (kupitia kwa mmojawao - Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Khamis Kagasheki), ni kwamba Barrick walimficha ukweli kwa kutompeleka kwenye maeneo yaliyoathirika hadi raia mwema mmoja alipoamua kumpeleka kwenye maeneo hayo!
Ukizingatia mienendo ya nyuma ya kampuni hiyo katika mgodi wake mwingine wa Buzwagi ambako fidia kwa wanavijiji, mpaka sasa, hazijalipwa; huku baadhi yao wakiwa ndani, hupaswi kuishangaa hila hiyo ya Barrick ya kutompeleka Waziri Kagasheki kwenye maeneo yaliyoathirika.
Ukizingatia yote hayo; swali kuu la kujiuliza ni hili: Je, Serikali ya Rais Kikwete itasimamia haki ya wananchi wake na kuhakikisha Barrick inaadhibiwa kwa unyama iliyoutenda North Mara? Je, Kikwete atahakikisha waathirika na familia za wafiwa wanalipwa fidia na Barrick?
Sina hakika na majibu ya maswali hayo; lakini nina hakika kwamba utakuwa mtihani mgumu kwa Rais Kikwete kuiadhibu Barrick; hata kama ripoti za uchunguzi mbalimbali wa kashfa hiyo ya North Mara zitainyooshea kidole kampuni hiyo ya Barrick.
Nasema hivyo kwa sababu Kikwete naye, kama alivyokuwa Mkapa, amejenga mapenzi makubwa mno na wawekezaji wa kigeni katika sekta ya madini nchini; kiasi kwamba hapendi kabisa kuwaudhi; hata pale maslahi ya wananchi (wanavijiji) au ya taifa yanapoumizwa.
Hii inaeleza ni kwa nini mpaka sasa serikali yake haijaifanyia kazi ripoti ya timu ya Jaji Bomani kuhusu sekta ya madini ripoti ambayo baadhi ya mapendekezo yake yamewaudhi kina Barrick.
Itakuwa pia vigumu kwa Rais Kikwete kuiadhibu ipasavyo Barrick kutokana na unyama huo wa North Mara, kwa kuwa kigogo mkuu wa kampuni hiyo ni swahiba wake wa muda mrefu.
Si siri kwamba Rais Kikwete ni rafiki wa muda mrefu (zaidi ya miaka 14) wa bosi mkuu wa kampuni ya Barrick Gold Corporation ya Canada, James Sinclair. Kampuni hiyo ya Canada ndiyo inayomiliki mgodi huo wa North Mara na mingine kadhaa nchini.
Inaaminika kwamba uhusiano kati ya Rais Kikwete na Sinclair ulianza wakati Kikwete akiwa Waziri wa Nishati na umeendelea hadi sasa ambapo ni rais.
Kwenye toleo la Raia Mwema la Desemba 19, 2007, Lula wa Ndali Mwananzela (mwandishi wa safu), aliyaita mahusiano kati ya Rais Kikwete, Sinclair na Barrick kuwa ni mahusiano ya pembetatu ya machozi.
Kama hivyo ndivyo, hatutashangaa kama unyama huo wa Barrick huko North Mara utafumbiwa macho na Rais Kikwete kwa suala hilo kupigwa danadana hadi mwishowe life kifo cha asili!
Akizungumza bungeni, wiki iliyopita, mbunge wa Kahama, James Lembeli (CCM) alisema kwamba Barrick ni kampuni yenye kiburi cha ajabu na yenye jeuri.
Labda kiburi hicho kinatokana na mahusiano ya Rais Kikwete, Sinclair na Barrick katika hiyo pembetatu ya machozi.
Lakini nihitimishe kwa kusisitiza tena kwamba
makovu na machozi ya North Mara tutabakinayo Tanzania miaka mingi tu baada ya Barrick kufungasha virago kutokana na kumalizika kwa dhahabu katika mgodi huo!
Tafakari.