Jinsi kila kitu kinavyosambaratika na kuangamia, uharamia, uzembe, ukosefu uadilifu, kukosa uungwana na utu, hujuma, wizi, ufisadi na dhuluma zikiongezeka, vifole vyote vinabidi vimnyokee mtu mmoja, Benjamin William Mkapa, Rais wa Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ndiyo, Mchungaji kanena msilishangae. Ndiyo, Mchungaji kanena pamoja na kumshikia bango Rais wa Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Kikwete kwa kuwa mgumu kufanya maamuzi mazito kuisafisha nchi yetu, lakini badala ya kuendelea kumwagia Kikwete lawama, Mchungaji anasema, turudi kwa yule aliyekuwa madarakani kabla ya Kikwete.
Wengine wenu mtadai turudi nyuma kwa Mzeee Mwinyi hata kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, mimi nasema hapana, tunaanzia na Mkapa wala si kulitafakari Azimio la Zanzibar bali ni utendaji kazi wa Serikali ya Mkapa na uongozi wake Serikalini, Chama cha Mapinduzi na Taifa zima.
Nilipoandika mada kuhusu Andrew, Omari, Cornell na Robert, niliwataja wakuu wa mambo ya sheria na dola, usalama wa Taifa na nchi, katiba na haki na kuwatuhumu kuwa wao katika nyadhifa zao na wakati wa uongozi wao, Tanzania iligeuka kuwa dangulo na handaki la kila aina ya uharamia kuliibia Taifa wazi wazi bila woga wala aibu.
Kikwete katuambia, tumuache "Mzee Mkapa" astaafu kwa amani, mimi nasema hapana, hatuwezi kuendelea mbele bila Mkapa kufikishwa kizimbani na kujibu mashitaka ya matumizi mabaya ya madaraka, kushindwa kulilinda Taifa kutoka maadui na uhalifu na mbaya zaidi kuliingizia Taifa hasara.
Simtuhumu Mkapa kwa wizi, bali nalisema wazi kuwa ndani ya utawala wa Mkapa wa miaka 10, makovu na majeraha tunayoyaona leo hii ya uhujumu na ufisadi, yalianzia nyakati hizo, michubuko na mikwaruzo ilifanyika nyakati hizo na tulichobakishiwa ni uozo ambao unatambaa kama algae na fungi.
- Benki Kuu na kashfa zote; Meremeta, Epa, CIS, Tangold, Minara na menginewe.
- Miundombinu na Nishati: ATC, TRL, Rada, IPTL, Richmond, Kiwira, Ndege ya Rais, Helikopta za Jeshi na mengine.
- Demokrasia butu: uonevu kwa vyama vya siasa na wafuasi wa vyama ambavyo si CCM, kwa kutumia nguvu ya dola kama kule Pemba, mauaji ya Mwembechai, kufilisi au kutoza ushuru na kodi ya kukomoa kwa mwenye kuipinga CCM na Serikali ya Mkapa na mengineyo.
- Uwekezaji: Mikataba mibovu, sheria mbovu ambazo zinawapendelea wawekezaji na kulipunguzia Taifa mapato.
- Sheria na Katiba: kuendelea kuwepo kwa sheria na mambo mabovu katika sheria na katiba ambayo yameondoa kabisa mihimili ya Bunge na Mahakama kuwa na nguvu za kikatiba na mamlaka kuihakiki Serikali kuu.
- Uchumi wa nchi, kudorora kwa uchumi kwa hali halisi ya uzalishaji mali, kudumaa kwa kilimo na kukimbilia utegemezi wa kuagiza chakula, kupungua uzalishaji mali kutokana na kosekana kwa umeme, maji, barabara nzuri.
- Elimu na Afya: kushuka kwa kiwango cha elimu Tanzania kwa kuruhusu matakwa binafsi ya watu wachache waamue kubadili mfumo wa Elimu bila kupata ushauri wa wataalamu wa Elimu. Afya kuendelea kudorora huku kukiwa na uhaba mkubwawa vifaa, madawa na wataalamu wa afya.
- Uongozi mbovu; kukosekana kabisa kwa uwajibikaji ndani ya serikali ambako kumezaa tabaka la viongozi wa Serikali na Mashirika ambao wanajiona ni Miungu wasio na makosa (Mattaka, Chenge n.k). Kukosekana na Sauti ya kuheshimiwa kuliongoza Taifa.
Pamoja na yale machache tuliyoyashuhudia ambayo tunayaona kuwa ni chanya, kama kufutiwa madeni yetu na harakati za kuendeleza Mkukuta na Mkurubita, lakini ukweli wa mambo unabakia kuwa kama kweli Mkapa aliacha misingi imara, basi pamoja na Kikwete kujenga baraka la mawaziri kubwa na la kifahari, uchumi na pato la Taifa lisingeporomoka jinsi lilivyoporomoka kwa haraka.
Ni wajibu wetu wote kama taifa kuwajibika na kuchapa kazi ili kulikwamua Taifa kiuchumi ili kuwepo na elimu na afya bora, ajira na tumaini la kuwa Taifa linalojitegema, lakini kinara, kiranja mkuu ambaye alitutukana kuwa tuna wivu wa kike na ni wavivu, matusi na lawama za Taifa kushindwa kusonga mbele zinarudi kwake na si mtu mwingine.
Ni haki yetu kama Wananchi, kutaka Mkapa awajibishwe kwa kuvurunda kazi. Hata pamoja na kuwa hawezi kupigiwa kura tena, lakini anapaswa afikishwe mahakamani kwa uzembe na matumizi mabaya ya madaraka yake.
Suala la Kinga ni la kitoto na linaendelea kulea uozo, ujuvi na ubabe wa kutishana na kulindana.
Atakapofikishwa Mkapa mahakamani, hata kina Rostam, Lowassa, Chenge na wengine watabaini kuwa Watanzania, hatutaki mchezo. Kila mwenye ndoto ya Ufisadi, Uzembe, utumiaji vibaya madaraka, uvivu na kukosa kuwajibika ama itabidi atafute nchi nyingine ahamie au anyooke na kuanza kuishi kama Mtanzania Mzalendo.
Kura zile za Tsunami hazikuwa za kutuletea Ze Comedy! Bwana Kikwete nakuomba fanya kazi yako, ondoa magugu, visiki na viwavi jeshi walio ndani ya Serikali na Chama chako.
Jaruzelski, pamoja na yote aliyofanya kwa madai ya kutumia madaraka au kwa mujibu wa sheria, leo hii yuko mahakamani kujibu mashitaka. Kila kona dunia hii, kiongozi aliyebainika alifanya kosa anavuliwa kinga na kufikishwa mahakamani, kama rafiki yetu Chiluba alivyofanyiwa.
Hivyo basi, tupaze sauti zetu kwa nguvu tukimtaka Kikwete amfunge paka kengele.
Rais Kikwete, nakuomba usicheze nalenale, ushamfikisha Mramba, Yona na Mgonja, tunamtaka Lowassa, Rostam na zaidi ya yote, tunamtaka Mkapa.
La sivyo, unatupa kazi moja, nikinukuu maneno ya mmoja wa viongozi wa chama cha wafanya kazi Ugiriki walipofanya fujo kutokana na Polisi kuua mtoto mdogo "It is very simple, we want the government to fall". Sentenzo hiyo ilitolewa kwa ghadhabu kwa Serikali kushindwa kufanya kazi yake ipaswavyo.
Ukishindwa kufanya kweli, basi nasi kwetu itakua "it is very simple, we want the government to fall" na kweli kwa kiapo cha kilio cha machungu Serikali yako itashindwa na kuanguka yenyewe. Usitufikishe hapo kwenye mchanga tukakuchukia na kugotesha meli yetu na kutoa kauli hiyo ya kutakia maangamizo ya Serikali yako.
Ili tuendelee mbele, fungua kesi, Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya Benjamin William Mkapa.