SEHEMU YA UAMUZI WA SPIKA SAMUEL SITTA
8.0 TUHUMA KWA WABUNGE KUPEWA RUSHWA
8.1 Kabla ya Kamati kuwasilisha taarifa yake kwangu, mjumbe wa Kamati Mhe. Ndesamburo alielezea mkasa ambao ulihusisha suala la rushwa.
8.2 Kwa bahati mbaya, katika suala hilo, Mhe. Ndesamburo katika nyakati mbalimbali, amelitolea kauli ambazo zinakinzana. Kwanza aliieleza Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuwa Bw. Mengi alimlalamikia kwa njia ya simu kwamba:-
"anaamini Bw. Mengi Kamati hiyo haingemtendea haki Bw. Mengi, kwa kuwa kulikuwa na vitendo vilivyoashiria maamuzi ya Kamati kuingiliwa na Serikali, na pia alikuwa na taarifa na ushahidi kuwa Bw. Mengi aliitwa na Waziri Mkuu ambaye alimshauri ajitoe katika ‘kesi' hiyo, kwa kuwa Wabunge wamehongwa na Bw. Manji, hivyo hatashinda."
8.3 Alipokuja kuniona ofisini Dar es Salaam, Mhe. Ndesamburo akiwa pamoja na Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Nh'unga na Makamu Mhe. Masilingi, tarehe 10 Januari, 2007 mimi nikiwa na Naibu Spika, alitueleza nia yake ya kujiuzulu ujumbe wa Kamati ikiwa Kamati haitawahoji Bw. Mengi na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nilimjibu kuwa, ikiwa tuhuma ni dhidi ya Wabunge wengi au dhidi ya Kamati, isingewezekana Wabunge waitwe na kuwahoji, kama mashahidi wakati wao wenyewe Wabunge ndiyo watuhumiwa. Isitoshe kwa nini aamini mazungumzo ya simu kwa jambo zito kama hilo?
8.4 Hata hivyo siku hiyo hiyo akaniletea barua yake ya kujiuzulu ujumbe wa Kamati ambamo alidai umetokana na:
"(a) kuwepo kwa madai kwamba Wabunge wamepewa rushwa na Manji na Kamati kutofuatilia suala hilo kujua ukweli wa mambo kabla ya kesi ya msigni kuamuliwa."
"(b) kuwepo kwa mazingira ya Mhimili wa Utawala (Executive) kuingilia Mhimili wa Bunge (Legislature) ambayo ni kinyume na utawala bora na mgawanyo wa madaraka."
8.5 Lakini taarifa za vyombo vya habari tarehe 11 Januari, 2007 vikinukuu aliyoyasema kwenye mkutano wa waandishi wa habari jana yake zilidai kuwa, Mhe. Ndesamburo alieleza kuwa, wenye kutiliwa mashaka ya kula rushwa ni wanakamati wenzie na siyo Wabunge "wengi" kama alivyonieleza ofisini au "wabunge" bila kubainisha kama alivyoniandikia. Pia alielekea kusema kuwa alikutana na Bw. Mengi kuyapata maneno na siyo kwa simu tu kama alivyotamka awali.
8.6 Kwa hiyo, ili kuondoa utata, nilimwandikia barua aweke bayana zaidi tuhuma zake, ili niweze kuamua hatua za kuchukua. Ikiwa ni wajumbe wa Kamati ndiyo watuhumiwa wa rushwa nilikuwa na uwezo wa kuagiza utaratibu wa Kibunge utumike katika kuchunguza. Lakini ikiwa ni "Wabunge wengi" au "Wabunge" kwa idadi isiyo wazi isingewezekana kutumia utaratibu wa Bunge. Hii ni kwa sababu ya msingi kwamba, Bunge/Wabunge wasingeweza, wao wenyewe wakiwa ni watuhumiwa, kujichunguza na kujisafisha au kujihukumu.
8.7 Barua ya Mhe. Ndesamburo aliyonijibu tarehe 24 Januari, 2007 bado imeendeleza utata kwa kudai kwamba, wanaohisiwa kula rushwa ni Wabunge kwa ujumla. Habainishi kwamba, ni Wajumbe wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, au Wabunge wengineo nje ya Kamati hiyo. Wakati wote huu suala hili la tuhuma za Mhe. Ndesamburo kuhusu rushwa limeendelea kuchukuliwa kisiasa na chama chake cha CHADEMA ambao wamenukuliwa na vyombo vya habari wakisema kwamba wamepeleka barua kwa Mhe. Waziri Mkuu. Aidha, wamekuwa wakizungumzia uvumi kwenye mikutano mbalimbali ya wananchi.
8.8 Taarifa za karibuni zinaelezea kwamba, Mhe. Ndesamburo sasa anachapisha kitabu kuelezea jinsi suala la Bw. Mengi na Mhe. Malima lilivyoshughulikiwa vibaya na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.
8.9 Katika hali inayozidi kukanganya katika barua yake ya tarehe 24/1/2007, Mhe. Ndesamburo akinijibu kuainisha tuhuma amedai kwamba:
"Na hata katika barua yangu sijamtaja Yusufu Maji aliyenitukana magazetini. Mini nilimtaja MANJI tu ambaye anamjua Bwana Mengi na huenda siyo Yusufu Manji."
8.10 Tuhuma za "Wabunge kupewa rushwa" ni nzito na ukizingatia kuwa zimetolewa na Mbunge mtu mzima na mzoefu, haziwezi kupuuzwa hata kidogo. Kutokana na sababu hiyo, na kwa kuzingatia ukweli kuwa, kupokea au kutoa rushwa ni kosa la jinai kwa mujibu wa sheria za nchi;
8.11 Na kwa kuwa, kwa kosa la jinai Wabunge hatuna kinga yoyote, na kwa kuwa kuna chombo mahsusi cha kisheria cha kushughulikia uchunguzi wa rushwa, niliamua kumwagiza Katibu wa Bunge awasiliane kwa maandishi, na Mkurugenzi wa Tume ya Kudhibiti Rushwa (TAKURU) ili uchunguzi ufanywe kubaini ukweli, na hatimaye kuachia sheria ichukue mkondo wake.
8.12 Katibu wa Bunge aliandika barua tarehe 26 Januari, 2007 kukabidhi suala hili kwa TAKURU. Aidha, kwa nakala ya barua hiyo, Mhe. Ndesamburo amehimizwa kutoa ushirikiano kwa TAKURU, ili ukweli kamili ufahamike.
8.13 Aidha, nimemwagiza Katibu wa Bunge anipatie ushauri kamili wa uhalali au vinginevyo, wa Mhe. Ndesamburo akiwa mjumbe wa Kamati ya Bunge, kufanya mawasiliano yasiyo rasmi na mmoja wa wanaochunguzwa wakati uchunguzi unaendelea.
8.14 Ingewezekana kuiagiza Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kufuatilia jambo hili, lakini nimeona si hekima kufanya hivyo kwa sasa. Nachelea kuchukua hatua zozote ambazo zitaonekana kumwekea vipingamizi Mhe. Ndesamburo, hasa kwa sababau tuhuma za rushwa anazielekeza kwa Waheshimiwa Wabunge wenzake.
9.0 UAMUZI (RULING)
9.1 Kwa kuzingatia matokeo ya uchunguzi na ushauri wa Kamati ya Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge, na pia kwa kuzingatia ushauri wa wajumbe wawili wa Kamati hiyo waliotoa mawazo tofauti na pia uchambuzi na ufafanuzi nilioutoa hapo juu, na vile vile na kwa kuzingatia mwenendo wa suala lenyewe na yote yaliyojitokeza wakati Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ikifanya uchunguzi wake;
9.2 Na kwa kuzingatia uzito wa tuhuma za Mhe. Malima dhidi ya Bw. Mengi zimemuathiri Bw. Mengi zenye athari ya kumgonganisha na viongozi wakuu wa nchi;
9.3 Na kwa kuwa, kitendo cha Bw. Mengi cha kukosea utaratibu kwa kutumia lugha ya kuudhi kukanusha matamshi ya Mhe. Malima kupitia vyombo vya habari na kuwa pia imemuathiri Mhe. Malima;
9.4 Na kwa kuwa, itakuwa ni kwa manufaa ya wahusika, ambao ni watu maarufu kwamba, suala hili limalizwe na kufikia mwisho wake;
9.5 Na kwa kuwa, linapotokea suala lolote Bungeni au kwenye Kamati ya Bunge, suala hilo linapaswa liamuliwe kwa mujibu wa utaratibu za Kibunge (Parliamentary usage and practice);
9.6 Na kwa kuzingatia kuwa, malalamiko husika hayakuwa ni ‘kesi' kati ya Mhe. Malima na Bw. Mengi, bali ni malalamiko ya wote wawili, kila mmoja akimlalamikia mwenzake, yaliyowasilishwa kwangu kwa utatuzi;
9.7 Na kwa kuwa, busara zangu zinanituma kwamba, njia nzuri na iliyo bora ya kuyashughulikia na kuyamaliza malalamiko ya watu hawa wawili, ni kwa usuluhishi (reconciliation) kati yao; kwa hiyo basi, ili kuleta suluhu hiyo, naelekeza kwamba:
(i) Katibu wa Bunge awasiliane na wahusika ili tukutane ofisini kwangu Dar es Salaam, kwa siku nitakayopanga na iliyo muafaka kwao tuweze kuongea pamoja kwa madhumuni ya kukubaliana nami, utaratibu muafaka, utakaojenga suluhu endelevu baina yao na kuepuka hatari ya suala hili kushamirisha makundi yaliyochomoza ambayo yameonekana kuibua masuala ya udini, rangi na tofauti za vipato katika jamii.
Uamuzi huu nimeutoa Dodoma leo tarehe 08 Februari, 2007.
Mhe. Samuel J. Sitta (Mb.)
SPIKA WA BUNGE