Kama maendeleo yanakuja kwa majibu mazuri ya viongozi wa kisiasa, basi nchi ya WADANGANYIKA tungekuwa na maendeleo kuzidi CHINA. Ningefurahi kuona midahalo yenye tija kwa maisha na Taifa la Watanzania na si inayolenga kujenga umaarufu wa mtu binafsi, taasisi au chama fulani cha siasa. Tunahitaji zaidi vitendo kuliko maneno kutoka kwa wanasiasa. Kwa kifupi nchi yetu imekosa wanasiasa na watendaji wenye vision na ndio maana hatuna mwelekeo rasmi wa kisiasa, kiuchumi ukiachia mbali mustakbali wa kijamii. Hata waandaaji wa midahalo wanauliza maswali mepesi yasiyolenga mustakbali wa taifa kwa kipindi kirefu bali ni matazamio ya kukidhi haja za muda mfupi. Nchi inaendeshwa kwa kutatua matatizo ya muda mfupi na ndio yanayodictate vision ya nchi kwa wakati huu. Mfano Leo hii tuna tatizo la upatikanaji wa nishati na nguvu zote zimeelekezwa huko. Kabla hili halijapata majibu tuna njaa kali inatunyemelea na hivi punde utasikia njaa ni janga la kitaifa na litachukua fikra za wanasiasa wote pamoja na watendaji serikalini kabla hata la nishati kupata ufumbuzi. Mara kilimo kwanza, kabla hatujaona matokeo utasikia elimu kwanza, maji kwanza n.k kauli zisizo na tija wala mashiko. Hizi kwangu ni siasa uchwara zisizo na matokeo dhahiri kwa uchumi wa taifa na uendelevu wa maisha bora kwa vizazi vyetu.
Ushauri kwa waandaaji wa midahalo:
"Acheni kuandaa midahalo ya kisiasa kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya watanzania: Andaeni midahalo ya wataalam, wasomi katika fani mbalimbali kama Wachumi, Wahandisi, Madaktari, wanasheria, Waalimu, wanadiplomasia, wataalam wa kilimo n.k. waliobobea katika maeneo ya uchumi na kijamii ili wajadili matatizo yanayotukabili kitaifa katika sekta mbalimbali na wapendekeze njia muafaka za kutatua matatizo hayo kitaalam. Wanasiasa hawana majibu yenye mashiko kwani wanazungumza chini ya vivuli vya vyama vyao na si utaalam walionao. Zaidi ya hapo wanasiasa hutoa majibu yasiyo na ithibati za kisayansi na hivyo hawakosi majibu 'mepesi' yasiyokidhi matakwa ya maswali wanayoulizwa. Vinginevyo midahalo yenu itabaki kuwa majukwaa ya kuwajengea baadhi ya watu umaarufu na matatizo ya nchi yetu yakizidi kuongezeka siku hadi siku.