Mbeya: Mahakama Kuu yatoa baraka Uwekezaji wa DP WORLD Dubai Bandarini. Walalamikaji wajipanga kukata Rufaa ya Hukumu

johnthebaptist

JF-Expert Member
May 27, 2014
84,004
142,036
Tunakumbushana tu leo ndio tarehe 10/08/2023

---- UPDATE----
Mahakama Kuu nchini Tanzania hii leo imetupilia mbali kesi iliyokuwa inapinga mkataba (IGA) wa uwekezaji wa bandari baina ya serikali ya Tanzania na falme ya Dubai.

Kesi hiyo iliyofunguliwa katika mahakama kuu kanda ya Mbeya na walalamikaji wanne ambao walidai mkataba huo unaenda kinyume na matakwa ya Katiba.

Akisoma Hukumu hiyo Jaji Dastan Ndunguru amesema baada ya jopo la majaji wa tatu kusikiliza pande zote mbili mahakama imeamua kuwa hoja zote sita hazina mashiko hivyo kuamua kuwa Mkataba wa IGA hauna dosari za kufanya usitekelezwe.

Misingi minne ilianishwa kwenye malalamiko hayo ni:

- Mkataba kuridhiwa bila kuutoa kwa uma na muda wakushiriki kwa wananchi.

- Mkataba wa IGA uliosainiwa unakiuka sheria.

- Mkataba ni kinyume na maslahi ya umma na rasilimali za umma.

- Mkataba unahatarisha usalama wa nchi kwa baadhi ya vifungu.

Akiongea na waandishi wahabari Wakili wa walalamikaji Bonifasi Mwabukusi amesema wanajipanga kwenda kukata rufaa kwani hawajakubaliana na uamuzi wa mahakama.




===

Sasa ni 09:00 Asubuhi ukumbi wa kwanza umejaa na ukumbi wa pili umejaa na bado kuna idadi kubwa ya watu nje waliendelea kuingia.

Leo majaji wa kesi hii wataandika historia ya maamuzi yao kwa vyovyote watakavyoamua.

Majaji wote watatu wameingia muda huu saa 3:42.

MAJAJI WA KESI HII
  • Mhe. Ndunguru
  • Mhe. Ismail
  • Mhe. Kagomba
Wakili wa serikali anatambulisha mawakili wa pande zote mbili. Na wote wako tayari kupokea hukumu.

Mahakama imetulia kwa ukimya mkuu. Majaji wanazungumza kidogo, Mhe. Ismail na Ndunguru. Kisha, Jaji Kagomba na Ndunguru pia wanazungumza kidogo. Wanaendelea kuandika.Karani wa Mahakama leo ni MAPUNDA.

Majaji wanasema wako tayari kusoma hukumu na kwamba itasomwa kwa kiswahili.

Jaji Ndunguru anaanza kusoma hukumu.

HUKUMU YA MAHAKAMA
Katika lalamiko hili waleta maombi wanne ni raia wa Tanzania wameleta maombi haya dhidi ya Mkataba wa TZ na Emirati ya Dubai.

Jaji Ndunguru: Mkataba huo uliingiwa mwaka 2022 na sehemu ya utangulizi wa Mkataba huo unarejea M.O.U iliyosaiwa tarehe 25/2/2022 wakati wa Maonyesho ya Dubai yaliyosainiwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Tanzania.

Jaji Ndunguru; Baada ya kusainiwa Mkataba huo hatua za kuridhia mkataba huo hapa Tanzania ulianza kwa mujibu wa Ibara ya 25 ya Mkataba huo.Bunge lilitoa taarifa kwa umma tarehe 5 Juni, 2023 na kuelekeza maoni yangepokelewa tarehe 6 Juni, 2023.

Jaji Ndunguru: Kusainiwa kwa Mkataba huo kumezua mgawanyiko mkubwa kimtazamo, na watu wengi wakisema mkataba huo una dosari na kwamba haukustahili kuwepo.

Jaji Ndunguru; Wanaolalamikiwa ni Waziri wa Ujenzi, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Katibu wa Bunge na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye anapaswa kuunganishwa katika mashtaka yanayohusu Serikali.

Jaji Ndunguru: Malalamiko hayo yameletwa katika misingi minne.Misingi hiyo ni pamoja na kwamba IGA ibara zake kadhaa kama zilivyotajwa katika Hati ya Mashtaka, kwamba zinakiuka sheria na Katiba ya Tanzania.

Jaji Ndunguru: Kiapo cha pamoja cha Waleta Maombi kiliunga mkono maombi yaliyowekwa katika Hati ya Malalamiko.Kwa ujumla Kiapo hicho kimelalamikia Mchakato mzima wa Upatikanaji wa Mkataba huo na mwenendo wa Bunge juu ya uvunjifu wa Sheria za nchi.

Jaji Ndunguru: Wajibu maombi walijibu mashtaka hayo kwa kiapo cha watu wawili, MOHAMED SALUM na MARIAM ambaye ni Mwanasheria kutoka Bungeni.

Jaji Ndunguru: Wajibu Maombi wamejibu kwamba mambo yanayolalamikiwa hayana msingi, na kwamba sheria na Katiba zimezingatiwa na masuala ya Usalama yametazamwa kikamilifu katika mkataba huo.

Jaji Ndunguru: Wajibu Maombi wameeleza kwamba Bunge lilitoa taarifa kwa umma ili kupata maoni, na wamesema kwamba watu 72 walijitokeza kutoa maombi. Shauri hilo lilisikilizwa kwa njia ya mdomo, mawakili wa pande zote mbili wakiwakilisha wadaawa.

Jaji Ndunguru: Kabla ya kuanza usililizwaji huo, Mawakili wa pande zote mbili waliunda kwanza viini vya kuamuliwa (Issues) pamoja na kiini kimoja ambacho kiliongezwa na Mahakama.

Jaji Ndunguru: Viini hivyo ni pamoja na kuhoji iwapo Ibara kadhaa ya IGA zinakiuka Ubara ya 1, 8, 28(1)(3) za Katiba ya Tanzania.Pia, kiini kingine kilihoji iwapo IGA ni mkataba.

Jaji Ndunguru: Kiini cha kingine kilihoji iwapo Mkataba wa IGA ulifuata taratibu za uteuzi wa Mzabuni katika kuzingatia sheria ya Manunuzi ya Umma.Hoja zote muhimu zilizingatiwa na Mahakama.

Jaji Ndunguru: Hata hivyo, kabla ya kutoa umauzi Mahakama inapenda kuwashukuru Mawakili wa pande zote mbili kwa kufanya kazi yao nzuri na kusaidia kutupatia Mahakama maarifa na uelekeo mzuri katika kutoa uamuzi.

Jaji Ndunguru: Ukiachia kiini cha tatu, viini vingine vyote havijajielekeza katika uvunjifu wa Katiba.Hata hivyo, kiu ya Watanzania inajikita kupata majibu kwa viini vyote vilivyoletwa mbele ya Mahakama.

Jaji Ndunguru: Hata hivyo, kiu ya Watanzania inajikita kupata majibu kwa viini vyote vilivyoletwa mbele ya Mahakama.

Jaji Ndunguru: Hii ni kwa sababu kila shauri linapaswa kuamuliwa kwa kuzingatia mazingira yake, na pia kwa kuzingatia ibara ya 107A (2)(e) kwamba Mahakama inapotoa uamuzi na haki isifungwe na mambo ya kiufundi.

Jaji Ndunguru: Kwa kuanzia na Kiini cha tano, Walalamikaji wanasema IGA haijakidhi vigezo vya kuwa mkataba kwani hakuna consideration na mambo mengine chini ya Sheria za Mikataba hapa nchini.

Jaji Ndunguru: Mawakili wa Wajibu Maombi wao walijibu kwamba, IGA sio mkataba wa kawaida bali ni makubaliano ya upeo tu, sisi Mahakama tunakubaliana na hoja hiyo.

Jaji Ndunguru: Kuhusu hoja kwamba Emirati ya Dubai sio dola, tumepitia Montevideo Convention, tumeona Emirati ya Dubai inakidhi vigezo vingine lakini tunapata mashaka kuhusu uwezo wa Emirati hiyo kuingia kwenye mikataba ya kimataifa.

Jaji Ndunguru: Mawakili wa Waleta Maombi hawakutuelezea kama Emirati ya Dubai imezuiwa kuingia katika mkataba wa kimataifa.Ni maoni yetu kwamba, katika IGA kila upande ulikuwa na uwezo wa kuingia katika mkataba huo.

Jaji Ndunguru: Hivyo ni maoni yetu kuwa IGA ni mkataba wa Kimataifa hausimamiwi na Sheria za Mikataba za Tanzania.Kuhusu kiini kwamba Mchakato wa IGA ulikiuka sheria za Manunuzi.

Jaji Ndunguru; Ni mtazamo wetu kwamba, Waleta maombi hawakujielekeza vyema katika sheria za kimataifa ambazo zinakataza kutumiwa kwa sheria za ndani katika mikataba ya kimataifa.

Jaji Ndunguru: Mahakama haijaridhishwa na hoja ya Waleta maombi kwamba Sheria ya Manunuzi ya Umma haikuzingatiwa katika kupima uhalali wa IGA.Kuhusu kiini cha kupima iwapo Umma ulipata muda wa kutosha kupata maoni kwa umma.

Jaji Ndunguru: Kukosekana kwa Viambatanisho muhimu kama Mkataba wa IGA katika Tangazo hilo, na kutokea kwa watu 72 tu, ndiyo hoja ya Waleta Maombi.

Jaji Ndunguru: Wajibu maombi wamejenga hoja kwamba suala hilo ni la ndani ya Bunge.Mahakama inatambua kuwa Ibara ya 63(3)(e) na Kanuni ya 108(2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge.

Jaji Ndunguru: Baada ya kupitia hoja za pande zote, tunakubaliana na hoja za wajibu maombi kwamba Bunge halitakiwi kuingiliwa katika majukumu yake.

Jaji Ndunguru: Msimamo huu umeelekezwa pia na Wasomi mbalimbali kuhusu masuala ya Bunge, akiwemo Pius Msekwa.Licha ya dosari inayoonekana katika ushirikishwaji wa umma kutoa maoni, hata hivyo tunajizuia kufanya uamuzi wa kiasi cha kubatilisha mkataba huo.

Jaji Ndunguru: Malalamiko makubwa katika Kiini cha mwisho, ni juu ya kuanzisha mchakato wa kuanzisha mahakama za nje katika migogoro ya rasilimali.

Jaji Ndunguru: Tunakubaliana na hoja ya Waleta Maombi, kwamba ibara za IGA imevunja sheria za ulinzi wa Rasilimali, kwa kupeleka migogoro nje ya nchi. Hata hivyo, dosari hiyo haitatumika kuutangaza IGA kuwa ni batili.

Jaji Ndunguru: Uandishi bora wa vifungu vya IGA unaweza kurekebisha Vifungu hivyo na kuondoa dosari hii.Tunashangaa kwamba IGA itaongozwa na sheria za nchi, na mikataba ya miradi itaongozwa na sheria za ndani lakini migogoro yake itatatuliwa nje ya nchi.

Jaji Ndunguru: Kwa hoja tajwa hapo juu mahakama hii inatupilia mbali hoja za waleta maombi. Anamaliza kusoma hukumu hiyo .Watu wanasimama majaji wanatoka.

Habari zaidi, soma:
  1. Sakata la DP WORLD: Rais Samia asema Serikali itatafuta mbia wa kuiendesha bandari ya Dar, sasa kuchangia robo tatu ya bajeti ya nchi
 

Attachments

  • Hukumu_KESI_YA_BANDARI_Alphonce_Lusako_&_3_Others_v_Attorney_General.pdf
    2.8 MB · Views: 13
Back
Top Bottom