Tatizo moja kubwa la hawa viongozi wetu wakienda nje ya nchi wanakuwa kama watoto wadogo! Wameona mji wa Singapore ulivyojengeka wameupenda. Badala ya kukaa chini na kujiuliza ni nini haswa siri ya hayo maendeleo? Wanakimbilia kusema na sisi tunataka mtutengenezee master plan. Hawajajiuliza hawa tu wana taratibu au sheria gani zinazofanya miji yao ikue kwa mpangilio. Kusema ukweli, kitu anachopendekeza Mheshimiwa wetu ni tusi kubwa kwa wasomi wetu wa pale Ardhi. Kwani, huitaji watu wa Singapore wakutengenezee master plan. Na wakati mwingine watu local wanaweza kuwa wazuri zaidi kwa kazi hiyo kwani wanaijua culture yetu kwa undani.
Mwalimu Nyerere, aliwahi kusema ya kuwa maendeleo sio lele mama bali ni mapambano. Ni lazima viongozi wetu wajue ya kuwa maendeleo sio kitu cha siku moja, na kinahitaji mipango madhubuti ili kukifanikisha. Na wakati mwingine Kiongozi husika anaweza hasifaidike au kupata sifa kwa kile alichokianzisha. Kama kweli Mama Tibaigana anataka akukumbukwe basi inabidi afanye mabadiliko ya kweli katika wizara ya Ardhi. Kama watu na wafanyakazi wa wizara walidharau master plan ya Mbezi Beach na kuichakachua, nini kinachomfanya afikiri ya kuwa awataichakua ya Kivukoni?
Niliwahi kuongea na rafiki yangu mmoja ambaye nu muhandisi wa maji taka kwenye mji mmoja mkubwa huko Marekani. Aliwahi kuniambia kuhusu gharama za kujenga mabomba ya maji machafu (drainage system) zilivyo juu. Nilimwuliza kwa nini gharama zinakuwa juu kiasi hicho? Aliniambia wanapo-design ukubwa wa pipe wanajaribu kukadiria population ya hiyo sehemu miaka hamsini ijayo. Nikamwuliza kwa nini mnafanya hivyo? Alisema ni kweli gharama zinaweza kuonekana kubwa lakini ni rahisi kufanya hivyo kuliko kubadilisha hayo mabomba baada ya miaka kumi. Na huu ni mmoja wa mfano mdogo wa jinsi wenzetu wanavyofikiria mbali. Ni maswali kama haya inabidi tujiulize kabla ya kuomba master plan.