NASIKIA Paul Pogba amepona. Nasikia kuna uwezekano akarudi kwenye mechi ya Manchester Derby.
Hajarudi na tayari ameshaanza kuandikwa. Mchezaji wa kwenye vyombo vya habari. Hapo kati, Man United ilipocheza bila ya huduma yake, hakuna mengi yaliyokuwa yakiandikwa kuhusu Man United. Ikishinda, ikifungwa au kutoka sare, ripoti zinakuwa za kawaida tu.
Lakini, shida ni kama matokeo hayo ingeyapata wakiwa na huduma ya Pogba uwanjani. Habari zingekuwa tofauti zaidi kama Man United ingepoteza au kutoka sare ikiwa na Pogba uwanjani. Vyombo vya habari vingeizungumzia Man United kidogo, lakini vingehamishia mjadala mkubwa kwa Pogba. Sasa yanini kuwa na mchezaji wa hivyo? Mchezaji wa vyombo vya habari?
Sawa, wachezaji wa aina hiyo kuna wakati mwingine wana umuhimu wake kuwapo kwenye timu, lakini wakati mwingine unahitaji kuwakwepa. Sasa hivi, kocha Ole Gunnar Solskjaer amekuwa akipanga mambo yake bila ya presha kwa sababu vyombo vya habari ni kama vimemsahau kimtindo. Hilo ni kwamba hakuna mchezaji kivutio kwenye vyombo vya habari. Makosa ya David de Gea yangekuwa yamefanywa na Pogba, habari ingekuwa kubwa zaidi na pengine wiki nzima ingekuwa mjadala. Lakini, kwa sasa mambo yanakwisha siku ya pili tu.
Hili linamfanya Solskjaer kuwa na muda wa kuandaa kikosi chake kwa utulivu na kuepuka presha ya vyombo vya habari. Wachezaji wote wa hivyo walikosekana kwenye kikosi hicho kwa siku za karibuni. Pogba amekuwa mgonjwa kwa muda mrefu na Romelu Lukaku amepigwa bei tangu mwaka jana. Vyombo vya habari vimekuwa vikilazimisha kuandika kuhusu Anthony Martial. Lakini, hailipi sana. Kwa sasa wamehamia kwa Bruno Fernandes. Hata hivyo, bado hajaanza kukiki sana na soko lao. Sasa mtu wao, Pogba yupo njiani kurejea kwenye kikosi. Kwa sasa tochi zote zitamulikwa kwao, atafanya nini kwenye kurejea kwake katika kumalizia siku zilizobaki kwenye msimu. Si muda mrefu, vyombo vya habari vitaibuka na taarifa za kwamba Solskjaer anapasuka kichwa, hajui Pogba ampange wapi. Utasikia Fred hafai, utasikia Bruno hawezi kucheza pamoja na Pogba. Chanzo kikuu kitakuwa mchezaji wa vyombo vya habari, Pogba. Sasa mchezaji wa hivyo wa nini? Ningekuwa Solskjaer nisingefikiria mara mbili uamuzi wa kumuuza Pogba, hasa kwa kipindi hiki ambacho timu imekuwa kwenye utulivu mkubwa wakati yeye alipokosekana kwenye kikosi. Uamuzi ni wake Ole, kama atakubali kuendelea kufuatwafuatwa na vyombo vya habari kujadiliwa mambo yake kwa ajili ya mchezaji huyo mmoja, au kumwondoa na kuepukana na presha ya timu yake kumulikwa kila uchao. Ukweli ni kwamba kama kuna mchezaji ambaye amekuwa akiifanya Man United kutotulia kwa sababu zisizokuwa za maana basi ni Pogba. Leo utasikia anasema kwenye vyombo vya habari anafurahia kocha akimpanga upande wa kushoto, kesho utasikia anasema kocha amempa majukumu ya kukaba, yeye sio soka lake, lakini keshokutwa utasikia anasema anataka kwenda kukabiliana na changamoto mpya kwingineko. Ni presha tu kwenye timu. Vitu kama hivyo vinapendwa na vyombo vya habari.
Ni kitu kinachopendwa pia na wakala wa mchezaji huyo, Mino Raiola. Wakala Raiola anataka kila wakati mchezaji wake huyo awe kwenye vyombo vya habari hata kwa sababu zisizokuwa na maana. Hivi karibuni alivurugana na Ole kwa kumzungumzia mchezaji ambaye hata kucheza hachezi. Anawachimba mkwara kwamba wasipomaliza ndani ya Top Four na kufuzu kucheza michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao, basi wasijiamini kwamba wataendelea kuwa na huduma ya mteja wake msimu ujao. Sasa mchezaji wa hivyo wa nini?
Jambo la kujiuliza, je Pogba tangu aliporudi Man United kuna kitu kikubwa amekifanya? Hakuna cha maana, zaidi ya kutokea tu kwenye vyombo vya habari na kubadili mitindo yake ya nywele kila mechi. Bruno anatamba kwa sasa amekuta utulivu mkubwa kwenye timu. Pogba atakaporejea, sasa hivi ataanza kujadiliwa hata nafasi yake anayocheza ndani ya uwanja. Litakuwa tatizo na kila kitu kitatibuka.
Uamuzi ni wake mwenyewe Ole kwa sababu yeye ndiye mtu wa karibu anayefanya kazi na Pogba na ndiye anayefahamu usumbufu wa wakala Raiola. Lakini, ukiniuliza mimi kuhusu Pogba, nitakwambia aendee tu.
Sent using
Jamii Forums mobile app