Rais wa Nigeria, Bola Ahmed Tinubu, ametangaza hali ya dharura ya usalama wa kitaifa kufuatia ongezeko kubwa la mashambulizi ya mauaji na utekaji nyara katika majimbo kadhaa ya nchi hiyo.
Katika agizo kali lililotolewa jana Jumatano, Novemba 26, 2025, Tinubu ameagiza kuongeza kwa dharura idadi ya vikosi vya usalama na kuchukua hatua thabiti dhidi ya kile alichokiita ‘mawakala wa uovu’ wanaodhoofisha taifa.
Kwa mujibu wa agizo hilo, Jeshi la Polisi la Nigeria limeelekezwa kuongeza maofisa 20,000 zaidi, na kufanya jumla ya idadi inayopangwa kufikia 50,000.
Aidha, Rais ameidhinisha kambi za National Youth Service Corps (NYSC), kutumika kama vituo vya muda vya mafunzo ili kuharakisha kupelekwa kwa askari hao katika maeneo yenye changamoto za kiusalama.
Vilevile, ameagiza maofisa wa polisi waliokuwa wakitumika katika ulinzi wa watu mashuhuri warudishwe kazini na kupatiwa mafunzo ya dharura kabla ya kupelekwa katika maeneo hatarishi.
“Idara ya Huduma za Jimbo imepewa mamlaka ya kupeleka mara moja walinzi wote wa misitu waliohitimu mafunzo, ili kukabiliana na magaidi na majambazi wanaojificha msituni, na kuajiri wengine zaidi kwa ajili ya ulinzi.
Hakutakuwa na mahali pa kujificha tena kwa mawakala wa uovu,” amesema Tinubu.
Ameongeza kuwa operesheni za kuwaokoa wanafunzi waliotekwa kutoka Shule ya Katoliki ya St. Mary katika Jimbo la Niger, pamoja na raia wengine waliotekwa nchini humo, zitaendelea bila kukoma.
Katika hatua nyingine, Rais Tinubu amelihimiza Bunge la Nigeria kuanza mchakato wa kupitia sheria ili kuruhusu majimbo yanayotaka kuanzisha jeshi la polisi la kikanda (state police), kufanya hivyo kisheria hoja ambayo imekuwa ikijadiliwa kwa miaka mingi kutokana na kuzorota kwa usalama wa ndani.
Aidha, ametoa onyo kwa serikali za mitaa dhidi ya kuanzisha shule za bweni katika maeneo yaliyotengwa bila ulinzi madhubuti. Amelihimiza pia makanisa na misikiti katika maeneo hatarishi kuimarisha uratibu wa kiusalama ili kulinda jamii zao.