Paroko wa Parokia ya Jina Takatifu la Yesu Bukombe Padre Fabian Bundala amefariki kwa ajali baada ya gari yake ndogo kugongana na basi la Happy Nation maeneo ya Ushirombo wilayani Bukombe saa sita usiku wa Julai 6. 2023.
Taarifa iliyotolewa na Jeshi la Polisi imeeleza kuwa chanzo cha ajali hiyo ni umakini mdogo wa dereva wa gari dogo.
Akizungumza na Mwananchi jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Kamishina Msaidizi wa Polisi ACP, Safia Jongo alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo majira ya saa sita usiku.
“Ajali ilitokea maeneo ya Ushirombo na kosa ni la dereva Padri aliyekuwa akiendesha gari dogo namba T575 CBC aliingia barabarani bila kuchukua tahadhari na kukutana na basi la Happy Nation iliyokuwa barabara kuu ndipo ajali ikatokea.
“Majeruhi kwa hali ya nje alipata majeraha ya kawaida lakini inaonyesha alipata majeraha ya ndani ambayo hayakuonekana,” amesema RPC Jongo.
Taarifa iliyotolewa kwa niaba ya Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama Mhashamu Christopher Ndizeye, Katibu Jimbo Katoliki Kahama, Padre Abraham Maziku alisema Padre huyo alifariki dunia akiwa njiani kupelekwa hospitalini.
“Padre Fabian Bundala aliyekuwa Paroko wa Parokia ya Jina Takatifu la Yesu Bukombe na Gambera wa Seminari ndogo Malkia wa Mitume – Ushirombo alifariki dunia akiwa njiani kupelekwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando, kutokea Hospitali ya Wilaya ya Bukombe iliyopo Ushirombo alikopewa matibabu ya awali,” amesema.
Alisema mara baada ya kufika maeneo ya Geita hali ilibadilika ghafla na kulazimika kuomba msaada wa kitabibu Hospitali ya Geita na wakati madaktari wakihangaika kuokoa maisha yake, alifariki.
“Tuupokee msiba huu kwa Imani kuu, tukimwombea huruma ya Mungu na msamaha wa dhambi zake, apumzike kwa amani,” amesema.
Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Gervas Nyaisonga alisema, “Tumepata taarifa na kama ilivyo desturi tumetuma pole kwa Askofu Ndizeye kwa maana yeye ndiye mfiwa kutokana na taratibu za kanisa. Mpaka sasa bado kamati yake bado hajatoa taarifa kwahiyo tunasubiri kutoka huko na ndipo tutajua taratibu zinakwendaje.”