Usiniite Mfalme, Niite Daudi: Kisa cha Daudi na mke wa Uria-1
Siku moja Mfalme Daudi alikuwa ana barizi kwenye paa la hekalu lake. Kama wanavyosema waswahili macho hayana pazia. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Mfalme Daudi. Macho yake yakatua kwa binti mmoja mrembo, aliyekuwa bafuni anaoga. Kwa sekunde kadhaa mwili wa Daudi ulikufa ganzi. Hakuamini kama aliyekuwa anamuona alikuwa ni mtu kweli au malaika.
Daudi akatuma wapambe wake. Wapambe hawakuchelewa. Wakarudisha jibu.
"Mfalme yule binti uliyemuona ni mtu kweli. Na ni mke wa mtu." Mpambe alimueleza Mfalme Daudi.
"Mke wa mtu?" Mfalme Daudi aliuliza kwa mshangao
"Ndio Bwana wangu. Ni mke wa Uria. Uria Mhiti. Yule mpiganaji wako hodari." Mpambe alimjibu Daudi.
Daudi alikuwa na kikosi cha watu 37. Hawa walikuwa wapiganaji hodari wa mfalme. Na Uria alikuwa ni mmojawapo. Wakati huu Uria alikuwa vitani.
"Hakikisha jioni unamleta kwangu " David aliongea kwa sauti nzito, kisha akageuka na kuondoka. Mpambe akainama na kuondoka pia.
Jioni ya siku hiyo yule mpambe akafanya kama alivyoagizwa na Mfalme. Daudi ni Mfalme wa pili wa Israel. Alichukuwa uongozi kutoka kwa Mfalme Sauli.
"Unaitwa nani mama", Mfamle Daudi alimuuliza yule mwanamke mrembo aliyemuona siku kadhaa zilizopita akiwa anaoga.
"Naitwa Bethsheba Bwana wangu" yule mrembo alijibu huku ameinamisha kichwa chake chini.
"Niite Daudi mrembo, usiniite Bwana wangu," Daudi alimwambia huku akimshika kichwa
"Sawa Daudi" mke wa Uria aliitikia.
Huwezi kuamini Daudi mwenye nguvu. Daudi mpakwa mafuta wa Mungu. Yule aliyemuuwa Goliath kwa kombeo. Sasa alikuwa mdogo. Mdogo zaidi ya piriton. Hapa hata angeombwa himaya yote ya Israel angeikabidhi kwa huyu kiumbe Bethsheba
Kwa kifupi Daudi alikuwa mateka. Alikuwa mateka kwa Bathsheba. Daudi alikuwa amekufa, alikuwa amekufa ameoza.
Jioni ya siku hiyo Daudi akafanikiwa kulala na mke wa Uria. Baada ya siku kadhaa mke wa Uria akarudi.
"Daudi sioni siku zangu" mke wa Uria akamwambia na kuongeza
"Nimepitiliza wiki mbili sasa"
Daudi akamuangalia kisha akasema
"Usiogope, nina jua cha kufanya"
"Si unajua mme wangu yuko vitani, sijakuatana nae zaidi ya mwezi sasa" mke wa Uria alimwambia Mfalme Daudi.
Itaendelea.....