Machi 30, 2026, dunia iliadhimisha Siku ya Kimataifa ya Ugonjwa wa Akili ujulikanao kama Bipolar, siku inayolenga kuongeza uelewa kwa jamii, kupunguza unyanyapaa na ubaguzi pamoja na kuhimiza upatikanaji wa huduma za afya ya akili.
Siku hii huchaguliwa kwa heshima ya siku ya kuzaliwa ya msanii maarufu wa Uholanzi, Vincent van Gogh, ambaye alihusishwa na ugonjwa huo baada ya kifo chake.
Bipolar au Baipola kwa Kiswahili, ni hali ya afya ya akili inayosababisha mabadiliko makubwa ya hisia. Mabadiliko hayo hujumuisha vipindi vya furaha iliyopitiliza na huzuni kali, hali inayoweza kuathiri maisha ya mhusika kwa kiasi kikubwa.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), takribani watu milioni 40 duniani wanaishi na ugonjwa huu, huku tafiti zikionesha kuwa waathirika wanaweza kufariki mapema kwa wastani wa miaka 10 ikilinganishwa na watu wengine.
Wagonjwa wa Bipolar hukumbana na changamoto nyingi, hasa katika jamii zenye uelewa mdogo wa afya ya akili. Unyanyapaa, ubaguzi na kutengwa na familia au jamii ni baadhi ya matatizo yanayowakabili.