Kampuni ya Taifa Gas ya Tanzania imetangaza uwekezaji mkubwa nchini Zambia wa uzalishaji umeme kwa kutumia Gesi itokanayo na mafuta (LPG).
Taifa Gas itashirikiana na Kampuni ya wazawa ya Delta Marimba Limited kuzalisha megawati 100 za umeme ambao utaingizwa kwenye gridi ya Taifa la Zambia.
Makubaliano hayo yametangazwa na pande hizo mbili leo Jumatatu, Juni 26, 2023 jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Taifa Gas, Hamis Ramadhan amesema, kampuni hiyo itakua ya kwanza ya uzalishaji wa umeme kwa kutumi gesi ya LPG na mradi huyo utatekelezwa kwa Taifa hilo maarufu kwa uzalishaji wa shaba.
Vilevile Ramadhan amesema Taifa Gas itatazama fursa nyingine za biashara ya gesi ikiwemo matumizi ya kupikia biashara amabyo tayari inafanywa hapa nchini.
“Taifa Gas itaongoza uwekezaji kwenye mradi huu nchini Zambia ambao utafikia dola za Marekani milioni 100 (zaidi ya Sh240 bilioni),” amesema.
Ramadhan amesema, “uamuzi huu wa kuwekeza Zambia umechochewa na mazingira mazuri ya uwekezaji na sera madhubuti za Rais Hakainde Hichilema na chama chake cha UPND.”
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa Gas, Rostam Azizi amesema, Tanzania na Zambia zimekuwa na uhusiano wa muda mrefu, “na uhusiano huu unapaswa kuuendeleza kwenye shughuli za kiuchumi.”
“Zambia ni nchi ambayo kwa sisi Watanzania tumekuwa na historia nao wakati wa shida na raha na mambo yanapokwenda vizuri kwenye uchumi maana yake tunapaswa kutafasiri mahusiano ya nchi mbili hizi kwa kuangalia fursa,” amesema.
Rostam amesema kampuni zake zitaendelea kutafuta fursa maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi.