Wanafunzi 150 wa udaktari kutoka Chuo Kikuu cha Tiba, Sayansi na Teknolojia (UMST) cha Khartoum nchini Sudan wamehamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ili kukamilisha masomo yao kufuatia machafuko yanayoendelea nchini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuwakaribisha wanafunzi hao, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Profesa, Mohamed Janabi amesema hali ya mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yanayoendelea nchini Sudani yamesitisha baadhi ya shughuli ikiwemo kufungwa kwa vyuo.
āWanafunzi hawa wapo mwaka wa tano wa shahada ya kwanza ya utabibu, ambapo katika mwaka huo, mafunzo hufanyika kwa vitendo zaidi, hivyo madaktari hawa wanafunzi watafanya mzunguko (Rotation) katika idara mbalimbali ikiwemo idara ya upasuaji chini ya usimamizi wa madaktari bingwa ili kuhakikisha wanapata maarifa yanayotakiwaā amesema Profesa Janabi
Profesa Janabi amesema MNH itatoa fursa kwa wataalamu hao kujifunza kama ambavyo inatoa kwa wataalamu wengine wa ndani na nje ya nchi na hata baada ya kumaliza masomo hayo iwapo watapenda kufanya mafunzo tarajali (Intenship) watapatiwa nafasi hiyo.
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa chuo cha UMST, Profesa, Mamoun Homeida ameeleza kufurahishwa baada ya kuona wanafunzi kutoka chuo anachokisimamia wamepokelewa vizuri na kwamba jambo hili limetokana na mahusiano ya kindugu yaliyopo baina na Tanzania na Sudan.
Naye kiongozi wa kundi la wanafunzi hao, Ruba Anwar Salih amesema wamefurahi kupata fursa ya kuendelea na masomo katika hospitali hiyo kubwa na yenye wataalamu wa kutosha nchini huku akisema anaamini watapata fursa nzuri ya kujifunza.