


Salehe Mawele

Kuna nyakati ni ngumu sana kuuelewa mpira wa kisasa, unatuvuruga vichwa na unatuchanganya sana akili, mpira unaotazama zaidi roles ( majukumu ) na nafasi ( position ), Meddie, Meddie, Meddie Kagere anaangushwa na soka la kisasa hasa linapokuja swala la kucheza kama single striker, ni ngumu kuelewa.

Meddie, kama anacheza katika ubora wake anawaacha mbali washambuliaji wengi wa Tanzania, bahati nzuri huwezi kumtilia shaka katika consistency ( muendelezo ), ndani ya misimu mitatu ana goli zaidi ya 50 na akichukua golden boot mara mbili mfululizo.

Ukitembelea katika vijiwe vya kahawa au kwenye vibanda umiza kilio kikubwa cha mashabiki wa Simba ni safu yao ya ushambuliaji, ni kweli, ukiwatazama washambuliaji wao wote watatu hakuna hata mmoja aliefikisha goli kumi, mbaya zaidi wawili kati yao bado hawana goli hata moja.

Kitu cha kwanza kilichowaangusha msimu huu ni ingia toka ndani ya kikosi, majeraha ya mara kwa mara yamekuwa yakiwatoa mchezoni, angalau Meddie amekuwa fiti mara nyingi lakini bado hajakuwa mchezaji wa kikosi cha kwanza mbele ya Pablo Franco.

Hoja yangu ipo hapa sasa, kwenye roles, timu nyingi Duniani kama sio zote ambazo zinacheza katika system ya 4-2-3-1 zinakuwa na mshambuliaji ambae hasimami kama wafungaji pekee, anakuwa kama playmaker wa ziada, ndio soka la kisasa na itabidi tuishi nalo tu.

Mugalu vs Meddie, Mugalu ana vitu vingi ingawa hawezi kukwepa lawama za kutokuweka mpira wavuni kwa dakika hizohizo chache alizozipata, ni kweli anaisaidia timu kwenye link up (kutengeneza muunganiko kwenye eneo la mwisho), kushuka between the line (baina ya mabeki na viungo).

Mugalu akicheza kama central striker utategemea kuwaona pia mawinga wakicheza kwenye zile flanks mbili, kwanini? kwa sababu ya ile mikimbio yake ambayo inavunja patterns za ulinzi katika mstari wa mabeki wa timu pinzani kitu ambacho Kagere hawezi.

Meddie ni mfungaji mzuri lakini si mchezaji mzuri katika hiyo system ya mshambuliaji mmoja mbele, kwenye soka la kisasa anafaa zaidi katika system ambayo timu itatumia twin strikers ( 4-4-2, 3-5-2, 4-2-2-2, 3-4-1-2, 4-1-3-2 ), ni ngumu kulielewa hili lakini itabidi tulielewe.
Asante.