Kamanda wa Kamandi ya Afrika ya Jeshi la Marekani (AFRICOM) Jenerali Stephen Townsend, alikuwa na ziara ya siku mbili nchini Tanzania, tarehe 27 na 28 Julai, ambapo alikutana na Maafisa Waandamizi wa Jeshi na kufungua mazoezi ya kwanza ya pamoja ya kijeshi ya Nchi hizi mbili tangu mwaka 2017.
“Tanzania imeendelea kuwa Nchi kiongozi Barani Afrika katika nyanja ya usalama na mbia muhimu sana wa Kamandi ya Afrika ya Jeshi la Marekani, Majeshi yetu ya ulinzi yana historia ndefu ya kufanya kazi bega kwa bega, na ziara hii ni kielelezo cha nia yetu ya kuimarisha zaidi ubia huo”———- Jenerali Townsend.
July 28,2021 Jenerali Townsend aliungana na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo katika hafla ya ufunguzi ya mafunzo ya pamoja ya kijeshi (Joint Combined Exchange Training – JCET) kati ya Askari wa Vikosi Maalumu vya Jeshi la Marekani na Askari wa Jeshi la Wanamaji la Tanzania katika Chuo cha Ulinzi wa Amani kilichopo Kunduchi.
Mazoezi hayo ya kijeshi ya wiki sita ni ya kwanza ya aina yake kwa Majeshi ya Tanzania na Marekani toka mwaka 2017, Askari wa Kimarekani na wa Kitanzania watakuwa bega kwa bega wakishiriki mafunzo haya ili kuimarisha ujuzi wao katika mbinu za medani kwa kikosi kidogo, ulengaji shabaha, utoaji matibabu, mbinu za kimapambano za kikosi kulingana na maeneo tofauti tofauti(unit maneuver), mafunzo kuhusu sheria za kivita au migogoro ya kivita (Law of Armed Conflict) na jinsi ya kulinda haki za binadamu wakati wa mapambano.