Shirika la Afya Duniani (WHO) imesema Bara la Afrika lipo katika wimbi la tatu la maambukizi ya ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona na kwamba kuna haja ya kupatikana kwa chanjo zaidi.
Hayo yameelezwa jana Alhamisi Juni 17, 2021 kupitia tovuti pamoja na mitandao ya kijamii ya shirika hilo.
Idadi ya watu walioambukizwa virusi vya corona Afrika ni zaidi ya milioni tano huku nchi saba zikiishiwa na chanjo.
Kwa mujibu wa WHO jumla ya watu 136,030 wamefariki kutokana na ugonjwa wa Covid -19 katika nchi tofauti za Afrika.
Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Matshidiso Moeti amesema Afrika ina uhitaji wa mamilioni ya chanjo hadi sasa kutokana na ugonjwa huo kushika kasi.
Uganda na Namibia zinakabiliwa na wimbi la tatu la maaambukizi huku watu wakiripotiwa kufa kila siku.
Afrika Kusini, Morocco, Tunisia, Ethiopia na Misri zimeripoti ongezeko kubwa la maambukizi ya corona barani humo.
WHO inasema hakuna muda kamili kubaini ni lini chanjo zaidi zitapatikana lakini limesisitiza kwamba kuna haja kushughulikia upatikanaji wake kwa haraka.