Makapuku Forum

Makapuku Forum

46aa8a8cc0c9e5419ce3d2738b1f83bb.jpg
 
MAKABURI YA WASIO NA HATIA (GRAVES OF THE INNOCENTS)- 3
ILIPOISHIA:
Nikamuongoza baba mpaka kwenye kaburi la Alfred ambalo juu yake kulikuwa na msalaba ulioandikwa jina lake kamili, tarehe ya kuzaliwa na tarehe ya kufa kwake. Akaniambia niwe makini kwa kila atakachokuwa anakifanya, nikatingisha kichwa huku hofu kubwa ikiwa imetanda ndani ya moyo wangu kwani kiukweli nilikuwa nikiogopa sana makaburi na maiti.
SASA ENDELEA:

Baba alianza kufukuafukua ule upande wa kichwani kwenye lile kaburim akaingiza mkono mfukoni na kutoa kichupa kilichokuwa na ungaunga mweusi, akaumwaga kuanzia upande wa kichwani mpaka miguuni, kisha akaniambia tuanze kulizunguka lile kaburi kwa kuanzia kushoto kwenda kulia.
Alianza yeye, na mimi nikafuatia, tukawa tunazunguka lakini kwa kutembea kinyumenyume, baada ya kuzunguka raundi sana, nilianza kusikia kizunguzungu kikali, baba akaniambia nikae, yeye akarudi kusimama palepale alipokuwa amesimama.
“Hebu muite jina lake mara tatu kwa sauti kubwa,” alisema baba, nikawa simuelewi anamaanisha nini. Yaani mtu alishakufa siku nyingi zilizopita halafu ananiambia nimuite jina lake, tangu lini maiti ikaitika? Hata hivyo, ilibidi tu nitii kile alichoniambia, nikamuita.
Nililitaja jina lake kwa mara ya kwanza, baba akawa ananionesha ishara kwamba niongeze sauti, nikamuita kwa mara ya pili kisha kwa mara ya tatu. Cha ajabu kabisa, nilisikia akiitikia, tena niliweza kuthibitisha kabisa kwamba ni yeye kwa sababu nilikuwa naijua sauti yake na hata akizungumza neno moja tu, nakuwa nimeshamtambua.
Nilitetemeka kuliko kawaida, nikawa nageuka huku na kule kwa sababu alivyoitikia, ilionesha kwamba hayupo pale kwenye kaburi bali yupo umbali wa mita kadhaa pembeni. Nikiwa bado siamini, baba alinionesha kwa kidole, akaniambia nitazame chini ya mti mkubwa wa mjohoro uliokuwa pembeni kidogo ya makaburi.
Nilitazama lakini sikuona kitu, nikamgeukia baba, akaniambia niendelee kutazama bila kupepesa macho. Katika hali ambayo sikuitegemea, nilimuona Alfred akiwa amesimama chini ya mti, nywele zake zikiwa zimekuwa ndefu na chafu sana, rangi ya ngozi yake ikiwa imebadilika na kuwa utafikiri amejipaka unga wa mkaa usoni. Akiwa ni kama na yeye amegundua kwamba nimemuona, Alfred aligeuka na kuanza kutimua mbio, muda mfupi baadaye akapotelea kwenye msitu mkubwa uliokuwa pemebi ya makaburi hayo.
Nilibaki nimepigwa na butwaa, nikiwa siamini kabisa nilichokiona, baba akanigeukia na kunitazama usoni.
“Unaona sasa? Mambo mengine usiwe unakuwa mbishi tu,” alisema, nikawa bado nimepigwa na butwaa, nikihisi kama nipo kwenye ndoto za kutisha ambazo sikuwa najua mwisho wake utakuwa nini.
Ilibidi baba anishike mkono na kuanza kunivuta, akili zangu zikarudi sawa, nikawa bado nageukageuka kutazama kule Alfred alikokuwa amepotelea. Nitakuja kueleza zaidi juu ya mazingira ya kifo cha Alfrted ambapo sasa na mimi nilianza kuamini kwamba hakikuwa kifo cha kawaida. Baba ni kama alikuwa amenifumbua macho.
Tulirudi mpaka nyumbani, tukakuta bado watu wanazidi kuongezeka pale kwenye msiba wa Mwankuga.
Tulienda mpaka nyumbani lakini kwa kuwa bado nilikuwa na maswali mengi kuhusu kifo cha mzee huyo, ilibidi nimtoroke tena baba na kwenda pale msibani. Safari hii watu walikuwa tayariw ameshakaa pale nje kwa kujipanga, kila mmoja akiwa na uso wa huzuni.
Kitendo cha mimi kuonekana tu eneo hilo, nilishangaa watu wakiacha kila walichokuwa wanakifanya na kunikodolea macho. Hata wale waliokuwa wanalia, wote walinyamaza, wakawa wananitazama. Sikuelewa kwa sababu gani hali hiyo imetokea, hofu kubwa ikatanda ndani ya moyo wangu.
Kwa mbali nikaanza kusikia minong’ono huku watu wakiendelea kunitazama. Mzee mmoja ambaye naye siku za nyuma nimewahi kusikia kwamba ana tabia ya kuwaibia watu fedha kwa uchawi wa ‘chuma ulete’, alisimama na kuongea kwa jazba.
“Baba yako alichokifanya ameona hakitoshi ameamua kukutuma na wewe uje kuendeleza uchawi wenu hapa. Mwaka huu mtaisoma namba, kamwambie anajikaanga kwa mafuta yake mwenyewe, mwisho wake umekaribia,” alisema mzee huyo na kusababisha watu karibu wote pale msibani wamuunge mkono, zogo kubwa likatokea huku wengine wakiinuka na kutaka kuja kunishushia kipigo.
Ni hapo ndipo nilipoelewa kwa nini watu walikuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini nilipofika msibani hapo. Kumbe walikuwa wanahisi baba amenituma mwenda kufanya uchawi! Maskini, nilibaki natetemeka kwa hofu kubwa kwa sababu sikuwa najua chochote kuhusu uchawi wala kuroga.
Ili kuokoa maisha yangu, ilibidi nitimue mbio, wakaendelea kunisindikiza kwa maneno makali wakimtuhumu baba na sisi familia nzima kwamba tunahusika na mambo ya kishirikina na kwamba eti sisi ndiyo tumemuua mzee Mwankuga kutokana na ugomvi wetu wa kugombea mpaka wa shamba.
Nilirudi nyumbani nikiwa natweta, mtu wa kwanza kuniona alikuwa ni baba ambaye alikuwa amekaa nje ya nyumba yetu, kwenye gogo kubwa la mti wa mvule akiandaa dawa zake, akashangaa kuniona naingia mbiombio huku nikilia. Alinisimamisha lakini sikusimama kwa hofu kwamba wale watu watakuwa wananifuatilia, nikapitiliza mpaka ndani na kwenda kujifungia chumbani kwetu.
Nilijuta kwa kutosikiliza kile alichokuwa ameniambia, nikawa natetemeka kwa hofu kubwa ndani ya moyo wangu. Niliendelea kujifungia chumbani kutwa nzima, nikijiuliza maswali mengi yasiyo na majibu.
Kwa mujibu wa maelezo ya baba, kama Mwankuga alikuwa amekufa, mwalimu Mwashambwa ambaye naye alikuwa naye kwenye lile tukio la kule porini, naye angekufa, jambo ambalo kidogo lilikuwa gumu kwangu kuliamini.
Kilichotokea siku hiyo, kuanzia kule porini tulikokuwa tumeenda kuchimba dawa na baba, kifo cha Mwankuga, kilichotokea kule makaburini na kelele za watu waliokuwa wakiituhumu familia yetu kuwa ya kichawi, vilinifanya nianze kumtazama baba kwa jicho la tofauti.
Basi siku hiyo ilipita nikiwa na mawazo mengi sana kuhusu yale matukio yaliyotokea, kila nilipokuwa nikifikiria, nilikosa majibu. Gumzo kubwa liliendelea kutawala kijijini kwetu kuhusu uchawi wa baba, kuna ambao walidiriki hadi kuja jirani na nyumba yetu na kuanza kutoa vitisho kwamba dawa yetu inachemka.
Nilifedheheka sana moyoni mwangu. Siku tatu baadaye, Mwankuga alizikwa kwenye makaburi ya kijiji huku msiba wake ukitawaliwa na vituko vya kishirikina vya hapa na pale ambavyo bado watu wengi waliendelea kuamini kwamba familia yetu inahusika.
Hatimaye Mwankuga alizikwa na kidogo zile kelele tulizokuwa tunapigiwa zikaanza kupungua. Hata hivyo, siku ya kwenda shule ilipofika (kipindi hicho bado nilikuwa nasoma Shule ya Msingi Makongorosi, Chunya) nilikumbana na unyanyapaa mkubwa sana shuleni.
Wanafunzi wenzangu walikuwa wakinitenga na kuniita mchawi, wakawa wanaituhumu familia yetu kwamba inahusika na vifo vya watu wengi waliokuwa wanakufa katika mazingira ya kutatanisha pale kijijini kwetu. Hata hivyo, kama baba alivyotufundisha wanafamilia wote, hatukutakiwa kujibizana na mtu yeyote, nikawa nasikiliza tuhuma zote bila kujibu chochote.
Shauku yangu kubwa ilikuwa ni kutaka kumuona mwalimu Mwashambwa kwa sababu kwa mujibu wa baba, na yeye alikuwa pamoja na marehemu Mwankuga siku waliyokuwa wanapigana kichawi na baba kule porini. Nilikuwa na shauku kubwa ya kumuona mwalimu huyo kwa sababu nilitaka kujifunza kitu juu ya uchawi na wachawi.
Niliamini kwa kumtazama tu, naweza kugundua kitu kilichokuwa kimejificha nyuma ya maisha yake. Hata hivyo, baadaye ulipowadia muda wa kipindi cha hesabu, mwalimu wa darasa alikuja na kutuambia kwamba mwalimu Mwashambwa alikuwa anaumwa sana hivyo asingeweza kuja shuleni wala kuingia darasani mpaka atakapopona.
“Kumbe ni kweli!” nilijikuta nimeropoka kwa sauti kubwa, kauli iliyosababisha wanafunzi wote pamoja na mwalimu wanigeukie pale nilipokuwa nimekaa, nikasikia miguno ya chinichini ikitawala darasa zima.
“Ni kweli nini?” mwalimu wetu wa darasa, Madam Timbuka alihoji huku akinifuata pale nilipokuwa nimekaa. Nilijisikia aibu kubwa iliyochanganyikana na hofu, sikujua nimjibu nini mwalimu huyo kwani ndani ya akili yangu, nilikuwa nimezipokea taarifa hizo za ugonjwa wa mwalimu Mwashambwa na kile alichoniambia baba kwamba mwalimu huyo alikuwa mchawi na walikuwa wakishirikiana na marehemu Mwankuga.
“Naongea na wewe Togolai, ni kweli nini?” alihoji tena Madam Timbuka, safari hii akiwa amenikaribia kabisa pale nilipokuwa nimekaa, nikaanza kubabaika huku hofu kubwa ikishindwa kujificha kwenye uso wangu.
Je, nini kitafuatia?
 
Makaburi ya Wasio na Hatia (The Graves of the Innocents)- 4
ILIPOISHIA:
“Naongea na wewe Togolai, ni kweli nini?” alihoji tena Madam Timbuka, safari hii akiwa amenikaribia kabisa pale nilipokuwa nimekaa, nikaanza kubabaika huku hofu kubwa ikishindwa kujificha kwenye uso wangu.
SASA ENDELEA...

“Kwamba mwalimu wetu anaumwa. Nilisikia asubuhi nikawa siamini,” nilidanganya, nikamuona mwalimu Timbuka akishusha pumzi ndefu, wanafunzi wenzangu waliokuwa wakinitazama kwa shauku, nao walionesha kuridhika na majibu yangu.
Baada ya kutoa taarifa hizo, mwalimu Timbuka alitutaka tusipige kelele bali tuutumie muda huo kujisomea, akatoka na kutuacha wote tukiwa kimya. Moyoni mwangu niliendelea kujiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu.
“Kwa hiyo mwalimu Mwashambwa naye atakufa?” nilijiuliza moyoni wakati nikiendelea kutafakari taarifa za ugonjwa wa mwalimu wetu. Nilijaribu kuunganisha matukio, hofu ikazidi kuongezeka ndani ya moyo wangu. Bado sikutaka kuamini kwamba baba alikuwa mchawi na alikuwa akihusika na kilichokuwa kinaendelea.
Muda ulizidi kusonga mbele, hatimaye ukawadia muda wa mapumziko. Kwa kawaida, ilikuwa ikifika muda wa mapumziko, kengele inagongwa mara mbili kuashiria wanafunzi wote tutoke madarasani lakini siku hiyo, kengele iligongwa tofauti. Iligongwa mfululizo huku walimu wakiwa wameshatoka na kusimama mstarini, kila mmoja akionekana kuwa ‘siriasi’.
“Kuna nini kwani?” nilijiuliza wakati nikisimama na kutoka pamoja na wanafunzi wenzangu, tukaelekea mstarini huku kila mmoja akiwa na shauku kubwa ya kusikia kilichofanya tukusanyike muda huo, jambo ambalo siyo la kawaida.
Mwalimu mkuu wetu, Nyerema alisimama na kututaka wote kutulia na kumsikiliza alichokuwa anataka kutuambia.
“Ni siku mbaya kwetu, najua wote mnajua kwamba mwalimu wenu, Mwashambwa alikuwa anaumwa sana, taarifa mbaya ni kwamba hatunaye tena, tumepokea taarifa za kifo chake muda huu, nawaomba nyote mtulie na muwe wavumilivu katika kipindi hiki kigumu, taratibu nyingine mtatangaziwa baadaye,” alisema mwalimu Nyerema, vilio vikaanza kusikika kutoka kwa wanafunzi.
Siyo siri nilipatwa na mshtuko mkubwa sana, sikutaka kuamini kwamba mwalimu Mwashambwa ameondoka. Niliunganisha matukio na kile nilichoelezwa na baba, nikawa siamini.
“Ina maana baba ndiye anayehusika na kifo cha mwalimu wetu pia?” nilijiuliza moyoni nikiwa bado nimesimama palepale. Nikiwa katika hali ile, nilihisi kuna mtu ananitazama, nikageukia kule mtu huyo alipokuwepo. Hakuwa mwingine bali mwalimu Timbuka ambaye alikuwa akinitazama kwa makini. Kwa ilivyoonesha, alikuwa akinitazama kwa muda mrefu, nikabaki kubabaika kwa sababu sikuelewa kwa sababu gani ananitazama namna ile.
Ili kuvunga, nilijichanganya na wanafunzi wengine na kuondoka eneo hilo, nikarudi darasani ambako wanafunzi wengi walikuwa wakiendelea kulia kwa uchungu. Baadaye kengele iligongwa tena, tukatoka na kwenda mstarini ambapo tulipewa utaratibu wa namna ya kushiriki msiba wa mwalimu wetu.
Wakati wanafunzi wengine wakifunga safari kuelekea kwa mwalimu Mwashambwa, mimi nilichepuka na kukimbilia nyumbani, moyoni nikiwa na dukuduku kubwa.
“Amekufa kama ulivyosema.”
“Si nilikwambia? Umeamini sasa!”
“Kwa hiyo wewe ndiyo umemuua? Kwani baba wewe ni mchawi?” nilijikuta nikimuuliza baba swali ambalo hata yeye hakulitegemea, akanitazama kwa macho ya ukali.
“Nani aliyekwambia mimi ni mchawi?”
“Nimesikia watu wakisema, hata shuleni kwetu kote watu wananinyooshea vidole wakisema eti mimi na wewe tunashirikiana uchawi,” nilisema huku nikitetemeka, baba akanisogelea kisha akashusha pumzi ndefu.
“Mwanangu Togolai, lazima ujue kwamba hapa kijijini sisi tuna maadui wengi sana kwa sababu ya kazi ninayofanya baba yako. Watu wengi wananionea wivu kwa sababu hakuna mganga mwenye nguvu kama mimi ukanda wote huu. Sasa maadui zangu wameanza kunizushia na kunichafulia sifa nionekane mchawi lakini siyo kweli, mimi ni mganga wala siyo mchawi,” alisema baba kwa sauti iliyojaa busara na upole.
Licha ya maneno yote yaliyokuwa yanazungumzwa na watu, nilikuwa nikiamuamini sana baba. Niliyaamini maelezo yote aliyonipa kwa asilimia mia moja, na mimi nikashusha pumzi ndefu kisha tukawa tunatazamana na baba.
“Ikitokea mtu mwingine yeyote anakutania au anakuzodoa kuhusu uchawi, naomba uje unieleze moja kwa moja, wakati mwingine inabidi tuwe wakali ili kulinda heshima yetu,” alisema baba kisha akainuka na kuniacha nimekaa palepale, nikawa naendelea kuyatafakari maneno aliyoniambia.
Japokuwa nilikuwa nampenda sana mwlimu Mwashambwa, sikuweza kuhudhuria kwenye msiba wake nikihofia macho ya watu kwani tayari maneno yalikuwa yamesambaa sana kwamba baba alikuwa anahusika na vifo vya ghafla vya watu wawili, Mwankuga na Mwashambwa vilivyotokea mfululizo.
Hatimaye mazishi yalifanyika lakini manenomaneno yalizidi kuwa mengi kadiri siku zilivyokuwa zinasonga mbele. Siku moja nikiwa shuleni, nilisikia wanafunzi wenzangu wakinitena kwamba mwisho wa ubabe wa familia yetu ulikuwa umefika kwa sababu wanakijiji walikaa kikao cha pamoja na kufikia maazimio ya kwenda kumleta mganga mashuhuri kutoka Chitipa, Malawi kwa ajili ya kuja ‘kuwanyoa’ uchawi watu wote waliokuwa wakihisiwa kuhusika na ushirkina pale kijijini kwetu, akiwemo baba.
“Baba nimesikia eti kuna mganga amefuatwa Malawi kuja kuwanyoa uchawi watu wote wanaotajwa kuhusika kusababisha viofo vya watu wasio na hatia hapa kijijini, ukiwemo wewe,” nilimwambia baba baada ya kurejea kutoka shuleni.
Tofauti na nilivyotegemea, baba hakuonesha kushtushwa na kitu chochote, akawa anaendelea kukatakata mizizi ya dawa nje ya nyumba yetu huku akisema kwamba wanajisumbua kwa sababu yeye siyo mchawi.
“Watanyoana wenyewe kwa wenyewe, mimi hakuna mtu anayeweza kunigusa,” alisema baba kwa kujiamini, nikakosa cha kuendelea kuzungumza. Maisha yaliendelea kusonga mbele, siku saba baadaye, mkutano wa wanakijiji ulitishwa kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Makongorosi ambapo wanakijiji wengi walikusanyika.
“Baba wewe huendi kwenye mkutano?”
“Siendi, kama unataka nenda kaniwakilishe, nina shughuli zangu muhimu siwezi kuziacha kwenda kusikiliza upumbavu wa watu wa kijiji hiki,” alisema baba kwa kujiamini.
Kwa kuwa siku hiyo sikuwa na kazi, ilibidi nifanye kama baba alivyoniambia, nikaenda kumuwakilisha ingawa nililazimika kukaa nyumanyuma, sikutaka watu wajue kwamba niko pale. Niweke wazi kwamba tuhuma zilizokuwa zinamkabili baba na familia yetu kwa jumla zilitufanya tuikose amani kabisa.
Kila tulipokuwa tukionekana, ilikuwa ni lazima tunyooshewe vidole, jambo ambalo binafsi liliniathiri sana kisaikolojia. Nikapoteza kabisa uwezo wa kujiamini, nikawa naishi kama digidigi, hali kadhalika kwa ndugu zangu wengine ingawa kwa baba yeye alionekana kutojali chochote.
“Tumechoshwa na uchawi hapa kijijini kwetu. Kwa pamoja tumefanikisha ujio wa mganga Mabwanji kutoka Malawi kwa lengo la kusafisha kijiji chetu. Wale wote waliokuwa wanaringia uchawi wao, kiboko yao amewasili, karibu uwasalimie wanakijiji,” alisema mzee wa kimila pale kijijini ambaye tulizoea kumuita Mwene.
Mwanaume mzee mwenye macho mekundu sana na midomo myeusi, akiwa amejifunga shuka refu lenye rangi nyekundu na nyeusi, kichwani akiwa amejifunga kitambaa cheusi, shingoni akiwa na hirizi kadhaa na shanga, alisimama na kunyoosha juu mkia wa mnyama ambaye sikuwa namjua, watu wote wakashangilia kwa nguvu.
“Sina mengi ya kuzungumza, naomba ushirikiano wenu tuwakomeshe wachawi wa kijiji hiki,” alisema mwanaume huyo kwa Kiswahili kibovu, watu wakashangilia tena kwa nguvu kisha Mwene akaendelea na maelezo, akisisitiza kwamba kazi lazima ianze siku hiyohiyo usiku.
Je, nini kitafuatia? Usikose next issue.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom