This is getting interesting. Luteni Makamba strike back on Maaskofu.
NA JANE MIHANJI
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Yussuf Makamba amesema kauli aliyoitoa Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Arusha Thomas Laizer kumshutumu, inaashiria kuwa ni shabiki wa CHADEMA. Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Makamba alielezea kusikitishwa kwake na habari iliyoandikwa katika gazeti la Mwananchi katika toleo la jana ikimnukuu askofu huyo akisema kuwa Makamba ana uelewa finyu wa Biblia. "Nilikuwa nazungumzia maandamano na ghasia zilizofanywa na CHADEMA kwa kunukuu Biblia, sasa hakunieleza au kunielimisha wapi niliikosea biblia," alisema Makamba. Aliongeza: "Nilihojiwa na TBC One na nikanukuu Warumi 13: 1-7, nilizungumzia CHADEMA, sikuwa nazungumza na askofu... sasa naona anayejibu hili ni shabiki wa CHADEMA," alisema. Katibu Mkuu huyo alisema anaendelea kuamini kwamba viongozi na wanachama wa CHADEMA hawakutii mamlaka halali ambayo ni serikali. Alisema kwa kunukuu kwake mistari ya biblia hakuwa amekosea kama Askofu Laizer anavyodhani. "Kwa kweli nisingependa kulumbana na wakubwa, lakini wanapaswa kuelekeza pale wanapoona mtu amekosea, siyo kumlaumu," alisema.
"Ni kweli nina uelewa mdogo wa Biblia, kwa sababu mimi si askofu, ni muumini wa dini tena Mwislamu. Mazungumzo yangu na waandishi wa TBC One nilinukuu Biblia, Warumi sura ya 13, mstari wa 1-7," alisema Makamba.
Alibainisha kuwa inawezekana uelewa wake katika kifungu hicho ni mdogo, hivyo hapaswi kulaumiwa, bali kuelimishwa kwamba mamlaka iliyotajwa katika mistari hiyo ni ipi?
Makamba alirudia kusoma mistari hiyo isemayo: "Kila mtu na atii mamlaka iliyo kuu, kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu na ile iliyopo imeamriwa na Mungu. Hivyo amwasiye mwenye mamlaka hushindana na agizo la Mungu, nao washindanao watajipatia hukumu.
Kwa maana watawalao hawatishi watu kwa sababu ya matendo mema, bali kwa sababu ya matendo mabaya. Basi wataka usimwogope mwenye mamlaka? Fanya mema nawe utapata sifa kwake, kwa kuwa yeye ni mtumishi wa Mungu kwako kwa ajili ya mema.
Lakini ufanyapo mabaya, ogopa kwa maana hauchukui upanga bure, kwa kuwa ni mtumishi wa Mungu. Amlipizae kisasi mtenda mabaya kwa ajili ya ghadhabu kwa hiyo ni lazima utii si kwa sababu ya ile ghadhabu tu, ila kwa sababu ya dhamiri.
Kwa sababu hiyo na walipa kodi kwa kuwa wao ni wahudumu wa Mungu, wakidumu katika kazi hiyo hiyo. Wapeni wote haki zao, mtu wa kodi, kodi, mtu wa ushuru, ushuru, astahiliye hofu, hofu, astahiliye heshima heshima."
Makamba alisema ni vyema akaelezwa uelewa wake finyu katika mistari hiyo, kuliko askofu kutaka kumnyamazisha na kuingia katika ushabiki wa kisiasa.
Source:
UHURU